Je! Wewe Unathamini Yale Ambayo Mungu Amekufanyia Wewe?
MWANAMKE mmoja alijaribu kushiriki habari njema kutoka Biblia pamoja na jirani yake, mke wa nyumbani Mchina pamoja na watoto wawili. Lakini zijapokuwa jitihada hizo alipewa jibu hili: “Siwezi kamwe kuwa Mkristo kama wewe!”
Badala ya kuvunjwa moyo na jibu hilo, hata hivyo, mwanamke huyo Mkristo aliendelea kuonyesha jirani yake fadhili, akaenda kumsaidia tena na tena alipohitaji msaada. Polepole, jirani huyo aliguswa moyo na fadhili hizo na hatimaye akakubali funzo la Biblia ili ajifunze zaidi juu ya Mungu ambaye waabudu wake wanaonyesha upendo huo usio na choyo. Muda si muda mwanamke huyo Mchina yeye mwenyewe akawa mwabudu wa Yehova, Mungu wa Biblia, na alifanya hivyo ujapokuwa upinzani mkali sana wa mume wake.
Jambo hilo lililoonwa linaonyesha kwamba kila mtu wa kawaida anathamini kutendewa kwa fadhili na huruma. Na ni jambo la asili na linalofaa kwamba tuonyeshe kuthamini kwetu mtu anayetuonyesha fadhili hizo. Ebu tuseme rafiki angekualika kwenye chakula kinono-kinono ambacho wakati mwingi, jitihada na pesa zilitumiwa kukitayarisha. Baada ya kufurahia karamu hiyo, je, ungewaza kutoka mezani bila hata kusema neno moja la kuonyesha kuthamini ukaribishaji wake? Basi, namna gani Muumba? Je! wewe unathamini yale ambayo ametufanyia sisi sote?