Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Mimba ya rafiki yangu ilitoka yenyewe. Nikiwa mwanamke namsikitikia, lakini je, ingefaa kumtia moyo atumainie ufufuo?
Hakika unaweza kufanya mengi kwa kumfariji na kumpa msaada wa upendo wa Kikristo. Lakini Biblia haitoi msingi wa kutazamia ufufuo wa kiini cha mtoto. Fikiria ni kwa sababu gani haitoi:
Mwanamke anapopata mimba, kunakuwa chembe moja tu, yai moja la mwanamke lililoungana na mbegu ya mwanamume. Kwa kawaida, kwa kipindi cha zaidi ya miezi tisa chembe hiyo inajigawanya na kujipenyeza kwenye mji wa mimba wa mwanamke, kiini cha mtoto kinasitawi, na mwishowe mtoto anazaliwa. Kutoka kwa mimba kunakatiza mwendo huo wa asili, na kumaliza uhai ambao umeanza na ambao unapasa kukua na kuwa binadamu tofauti. Ikiwa mimba inaharibiwa makusudi, inapingana na utakatifu wa uhai na amri ya Mungu ya kutokuua makusudi.—Kutoka 20:13; 21:22,23; Hesabu 35:16-18; 1 Petro 4:15.
Mpaji-Uzima wetu anajua uhai unaokua katika mji wa mimba, kama tuonavyo kutokana na yale ambayo Biblia inasema juu ya mke wa Yese akiwa anabeba kiini cha mtoto kilichositawi na kuzaliwa na akaitwa Daudi. (Zaburi 139:13-16; linganisha Ayubu 31:15.) Lakini, namna gani uwezekano wa kufufuliwa kwa visa vya mimba inayotoka yenyewe au mtoto kuzaliwa amekufa?
Biblia inakubali kwamba kitoto mimbani au kiini cha mtoto kinaweza kufa. Matokeo yanakuwa mimba inayotoka yenyewe, au mtoto kuzaliwa amekufa.—Mwanzo 31:38; Kutoka 23:26; 2 Wafalme 2:19-21; Ayubu 21:10; Zaburi 58:8; 144:14.
Ayubu alitaja njia mbalimbali ambazo mimba inaweza kutoka yenyewe. Aliona kila ya njia hizo ingalikuwa ni afadhali kwake kuliko taabu aliyokuwa akipata. Alisema angaliweza kuwa “mimba [iliyofichika] iliyoharibika,” mtu ambaye ‘hangekuwako, kama wachanga wasiouona mwanga kabisa.’ (Ayubu 3:16) Huenda hiyo ikawa inahusu mwanamke anayetokwa na mimba hata kabla hajajua kwamba alikuwa na mimba na wakati kiini cha mtoto kilikuwa kingali hakijajulikana kipo. Kichapo The Body Machine kinasema: “Mayai mengi ya mwanamke [yaliyokwisha kuungana na mbegu ya mwanamume] kwa kawaida hayasitawi, kwa kweli ni hesabu kubwa [isiyositawi] zaidi ya ile [inayositawi]. Karibu asilimia kumi ya mayai yanashindwa kupenya mji wa mimba na kati ya yale yanayopenya karibu nusu yanajitoa yenyewe, kwa kawaida bila ya mama kujua.”
Pia Ayubu alisema kwamba kama ‘milango ya tumbo la mamake ingalifungwa, angekuwa amefichwa asione taabu.’ Kwa hiyo angaliepuka kutaabika kama ‘angalikufa tokea mimbani’ au “mji wa mimba.” (Ayubu 3:10, 11, Union Version; New World Translation) Kasoro kubwa katika kiini cha mtoto au kitoto mimbani nyakati nyingine zinasababisha jambo hilo. Au huenda ikatokezwa na kasoro katika viungo vya uzazi vya mama; upungufu wa vitamini, hormoni au oksijeni; au maradhi ya mama.
Akiwa katika maumivu yake makali Ayubu alikuwa na maoni kwamba uwezekano huo mbali-mbali ungalikuwa ni afadhali kwake. Hata hivyo mamaye angalisikitika, sawa na wanawake leo wanavyosikitika, wakati kutokamilika kulikorithiwa kunapofanya mimba itoke yenyewe au mtoto kuzaliwa amekufa. Kwa kutaja uwezekano huo mbalimbali, Ayubu hakusema kwamba yajapokuwa hayo angalifufuliwa. Kwa maoni yake, faida ingalikuwa kufichwa asione taabu na kuteseka.
Ayubu aliongeza uwezekano mwingine: “Mbona [nisife] hapo nilipotoka tumboni?” (Ayubu 3:11) Kama inavyotokea nyakati nyingine, kama Ayubu angalizaliwa halafu upesi baada ya hapo afe, pengine hata kabla ya kunyonyeshwa, mataraja yake ya wakati ujao yangalikuwa nini? Katika habari hiyo hakuzungumza juu ya jambo hilo. Lakini baadaye alionyesha kwamba kama, angekufa na kwenda Sheoli baada ya kuishi akiwa binadamu, inawezekana Mungu ‘angeweka kipimo cha wakati na kumkumbuka.’ Mpaji-Uzima wetu ‘angeita na Ayubu mwenyewe angejibu.’ Ndiyo, Yehova Mungu angeweza kumrudisha Ayubu kwenye uzima, amfufue—Ayubu 14:13-15, NW.
Hilo linalingana na maarifa yetu ya ufufuo katika mifano ya Biblia. Wale waliofufuliwa kwa wazi walirudishwa kwenye uzima wakiwa watu wale wale kama wakati wa kufa kwao. Yaani, watoto waliokufa walifufuliwa wakiwa watoto, watu wazima wakiwa watu wazima. (2 Wafalme 4:17-20, 32-37; Luka 7:12-15; 8:40-42, 49-55; Yohana 11:38-44) Je! lingekuwa jambo la akili kuwaza kwamba kama ‘mimba iliyofichika, iliyoharibika’ ingalikuwa ndicho kisa cha Ayubu, kiini cha mtoto hicho kilicho kidogo sana kingerudishwa katika mji wa mimba wa mama katika Utaratibu Mpya ili kiendelee kuwa mimba ambayo pengine mama hakuijua? Hiyo haipatani na yale ambayo Biblia inaonyesha juu ya ufufuo, ambao sikuzote ulihusu watu ambao walikuwa wamezaliwa na wakawapo wakiwa watu binafsi walio tofauti mbele za Mungu.—Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15.
Lakini namna gani ikiwa kiini cha mtoto kilikuwa kimesitawi sana, kikawa kitoto mimbani au hata kukaribia kuzaliwa kama mtoto? Kuna hali nyingi zinazowezekana. Hata hivyo, hakuna haja ya kudhania-dhania, kwa maana kuna matokeo mengi sana ya huzuni yanayowapata watu leo. Katika Paradiso iliyorudishwa Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo ataondoa hali ya dhambi ya mwanadamu na kuleta baraka nzuri ajabu. Watu wengi watafufuliwa. Uamuzi wa jinsi ufufuo utakavyofanywa, na utafanywa kufikia kadiri gani, ni wa Yehova na Yesu. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba uamuzi huo utaonyesha hekima na haki kamilifu ya Yehova.
Elihu alimhakikishia Ayubu hivi: “Mungu asidhaniwe kutenda udhalimu; wala Mwenyezi kufanya uovu. Kwani atamlipa binadamu kwa kazi yake . . . Naam, hakika, Mungu hatatenda mabaya.” (Ayubu 34:10-12) Sisi sote, kutia wenzi ambao wamehuzunika sana kwa mimba kutoka yenyewe au mtoto kuzaliwa amekufa, tunaweza kufarijika kwa kujua kwamba “[Yehova] yu mwema, mwenye adili.”—Zaburi 25:8.