Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 11/1 kur. 4-7
  • Kutokumtegemea Mungu—Sababu Gani Hakufai?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutokumtegemea Mungu—Sababu Gani Hakufai?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tatizo la Tangu Zamani
  • Uhitaji wa Uongozi wa Kimungu
  • Ubora wa Kukubali Mwongozo wa Kimungu
  • Mapenzi ya Mungu Yatakapofanywa Duniani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Tafuta Mwongozo wa Mungu Katika Kila Jambo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Sheria za Mungu Hutufaidi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Mtumikie Yehova Kulingana na Viwango Vyake vya Juu
    Izingatie Siku ya Yehova Maishani
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 11/1 kur. 4-7

Kutokumtegemea Mungu​—Sababu Gani Hakufai?

“Mimi ninatafuta msisimuko.” “Naudhika na kuchoka kuambiwa la kufanya!” “Acha kunifuata-fuata!” Maneno kama hayo huenda yakaonyesha roho ya kujitegemea. Nyakati nyingine maneno hayo yanaweza hata kusikiwa yakisemwa na Wakristo.

Wakristo huenda wakaambukiwaje na roho ya kujitegemea, hata kutokumtegema Mungu? Kwa kawaida inaanza na kutwaa maoni yaliyopotoshwa juu ya matakwa ya Yehova Mungu. (Zaburi 73:2, 13, 14) Wanaziona sheria za Mungu kuwa zinazuia kupata raha, badala ya kuwa ni za kuwalinda wafurahie maisha. Kuangaza na kung’aa kwa ulimwengu usiomwogopa Mungu kumewapumbaza waamini kwamba wanakosa raha. Namna gani wewe? Una maoni gani juu ya kutokumtegemea Mungu?

Tatizo la Tangu Zamani

Tamaa ya kutokumtegemea Mungu si mpya. Ni kama ya umri mmoja na mwanadamu. Roho ya kujitegemea ilianzishwa na Shetani Ibilisi. Alidanganya mwanamke wa kwanza, Hawa, afikiri kwamba angeweza kuwa mwenye furaha zaidi akijiondoa katika mwongozo wa Muumba wake. Hawa aliamini kwamba mwendo huo wa kujitegemea ungemfungua macho ajue mambo na raha nyingi; alizokuwa amenyimwa na Mungu.​—Mwanzo 3:1-5; Ufunuo 12:9.

Kwa kupofushwa macho na tamaa za kichoyo alizokuwa amejifanyia karibuni, hawa alimsihi mume wake ajiunge na uasi huo. Adamu pia alichagua kutokumtegemea Mungu. Matokeo: Huzuni ikawa badala ya furaha. Dhambi, aibu, magonjwa, maumivu na kifo yakafuata, si kwa Adamu na Hawa tu, bali kwa wazao wao wote pia.​—Mwanzo 3:6, 16-19; Warumi 5:12.

Biblia ina kumbukumbu la kwamba malaika pia waliamua kufuata kipito cha kutokumtegemea Mungu kwa kutafuta kuwa na raha haramu pamoja na ‘binti wenye sura nzuri wa watu.’ Je! mwendo huo wa kujitegemea ulileta uradhi wa kweli? Hapana. Bali, ulitokeza ukosefu mbaya sana wa adili na jeuri hata Yehova akaamua kuuharibu ulimwengu huo wa watu wasiomwogopa Mungu. Malaika hao wenye kujitegemea wakawa mashetani, ambao sasa wanaendeleza roho iyo hiyo yenye uharibifu ya uasi kati ya wanadamu.​—Mwanzo 6:1-7, 11; Waefeso 2:2; Yuda 6-12.

Uhitaji wa Uongozi wa Kimungu

Mambo hakika yaliyotangulia yanapasa yatusaidie kuthamini ukweli mmoja wa msingi: Ili awe na maisha yenye mafanikio na yanayofurahisha, ni lazima mwanadamu awe anategemea Mungu apate mwongozo. Hiyo ni sababu moja inayofanya Biblia iseme: “Ee [Yehova], najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Mwanamume wa kale mwenye hekima, Sulemani, aliitambua hatari ya mtu kujiwekea viwango vyake mwenyewe vya maisha bila kutegemea mwongozo wa kimungu. Aliandika hivi: “Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, lakini mwisho wake ni njia za mauti.”​—Mithali 14:12.

Acha tutoe mfano wa jambo hilo kwa njia mbili. Kama marubani wote wa ndege za kibiashara wangepuuza maelekezo wanayopewa na wanja za ndege kisha watushe ndege zao chini wakati wo wote au mahali po pote ambapo wangetaka, usafiri wa angani ungekuwa salama kadiri gani? Au kama kikundi cha wajenzi kingetupilia mbali michoro yenye kuongoza ujenzi kisha kila mmoja ajenge sehemu yake kama apendavyo, kungekuwa na jengo la namna gani? Tunafahamu kwamba ni lazima viwango vifuate ndipo jamii yo yote ya watu iweze kuwa na utaratibu.

Hakuna mtu anayestahili kutoa miongozo hiyo kuliko Yehova, Muumba wa mwanadamu. Kwa sababu ya Uumba wake, Yehova Mungu, wala si mwanadamu kiumbe, ndiye mwenye haki kamili ya kuweka viwango ambavyo viumbe wake wanapaswa kuvifuata maishani mwao. Yeye anajua mipaka yetu; anajua barabara mahali ulipo mpaka ambao kwa kuuruka mtu anapoteza furaha na kuwa na huzuni. (Matendo 17:26, 27) Tena na tena, matukio ya maishani yanathibitisha kwamba njia ya Mungu inafaa kweli kweli. Ndiyo njia bora zaidi kwetu.

Si lazima tukisie viwango vya Yehova ni nini; yeye anatuambia kwa fadhili katika Neno lake, Biblia: “Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawa-sawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana [utatenda kwa hekima, NW]. (Yoshua 1:8) Mtume Paulo anaeleza jinsi viwango vya Mungu vinavyoyahusu mambo yote. Aliandika katika 2 Timotheo 3:16 na 17, NW: “Andiko lote liliongozwa na Mungu na ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa na uwezo wa kutosha, aliye tayari kabisa kwa kila kazi njema.”

Yehova anatualika tuvijaribu viwango vyake, “kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Warumi 12:2, NW) Bila shaka, ili kufanya hivyo ifaavyo, tunahitaji kabisa tujifunze Biblia kweli kweli. Tuwe ndio tumeanza kujifunza Biblia au tumekuwa tukifanya hivyo kwa makumi ya miaka, ni jambo la maana kuwa na mradi wa kupata maarifa sahihi na ufahamu mwingi wa mapenzi ya Mungu. Tusipozoeza fahamu zetu kwa kuzitumia, hatutaendelea kuiona vizuri miongozo ya Yehova.​—Waebrania 5:14.

Kupuuza viwango vya Mungu ni kukaribisha msiba. Vipingamizi ambavyo mtu analazimika kukabiliana navyo ni vingi mno hata asiweze kufaulu kwa kutegemea ufahamu wake mwenyewe. Kwanza, mtu analazimika kushindana na mavutano yenye nguvu zinazozidi za kibinadamu, ya Shetani na mashetani wake. (1 Yohana 5:19; Ufunuo 12:12) Halafu kuna mfumo wa mambo uliofanywa na wanadamu ulimwenguni pote ambao umejaa roho ya kutokutii na uchoyo wa kupita kiasi. (Waefeso 2:2; 1 Yohana 2:15-17) Na, bila shaka, ni lazima tupigane na hali zetu wenyewe za kutokamilika na maelekeo ya moyo wenye udanganyifu. (Zaburi 51:3-5; Yeremia 17:9, 10) Kwa hiyo, kuishi bila mwongozo wa Yehova ni sawa na kusafiri katika motakaa isiyo na usukani.

Yesu Kristo ndiye mfano bora zaidi wa mtu aliyethamini mwongozo wa kimungu. Ingawa alikuwa mkamilifu, alisema hivi juu yake mwenyewe: “Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda.” (Yohana 5:19) Yesu hakuishi ili ajipendeze mwenyewe. Katika pindi nyingine alisema: “Mimi sifanyi lo lote la binafsi: yale ambayo Baba yangu amenifundisha ndiyo mimi nahubiri; yeye aliyenituma yu pamoja nami, naye hajaniacha nikae binafsi, kwa maana mimi sikuzote nafanya yale yampendezayo.” (Yohana 8:28, 29, The Jerusalem Bible) Je! wewe unatamani kuongozwa na kiwango kile kile alichokikubali Yesu Kristo?​—1 Petro 2:21.

Ubora wa Kukubali Mwongozo wa Kimungu

Yehova ndiye yule “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11, NW) Yeye hataki kutunyang’anya raha inayofaa, msisimuko au furaha. Fikiria kidogo maneno yaliyotajwa wazi katika Warumi 1:28-32. Kutokumtegemea Mungu kunaleta matokeo mabaya tu kwa maana masimulizi yanasema hivi kulingana na The New English Bible:

“Hivyo, kwa sababu wao hawajaona inafaa kumkiri Mungu, yeye amewakabidhia kuwaza kwao wenyewe kulikoshuka tabia, Jambo hilo linawaongoza kwenye kuvunja kanuni zote za mwenendo. Wamejawa na kila namna ya udhalimu, ukorofi, pupa, na nia ya madhara; wao ni fungu moja la kijicho, uuaji wa kukusudia, ushindani, hila, na nia mbaya; wanong’onaji na wenye kutokeza kashifa, wenye kujawa na chuki kwa Mungu, wafidhuli, wenye kutakabari, na wenye kujivuna; wanavumbua aina mpya za ukorofi, hawaonyeshi ushikamanifu kwa wazazi, hawana dhamiri, hawana uaminifu kwa neno waliloahidi; wao wako bila shauku ya kiasili na bila huruma. Wanaijua vizuri vya kutosha amri ya Mungu, kwamba wale wanaoenenda kama hivyo wanastahili kufa, hata hivyo wanafanya jambo hilo; si hivyo tu, wao kwa kweli wanapigia makofi mazoea kama hayo.”

Kwa upande mwingine, wale wanaochagua viwango vya Mungu wanatiwa moyo wavue utu wao wa zamani pamoja na roho ya kujitegemea ya utu huo kisha wavae utu mpya ulio kama wa Kristo. Utu mpya ni kutia na kuwa wafadhali, wenye huruma nyororo, wenye kusamehe kwa hiari. (Waefeso 4:20-32) Tena ni utu unaodhihirisha matunda ya roho takatifu ya Mungu: “upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.”​—Wagalatia 5:22, 23, NW.

Baada ya kuzitazama vizuri nyutu zote mbili, wewe ni mtu wa namna gani? Ni upi kati ya hizo mbili ungependa zaidi uone washirika wako wakiwa nao?

Zaidi ya hilo, Biblia inafundisha kwamba hivi karibuni sana watu wote wasiomwogopa Mungu watapatwa na uharibifu mikononi mwa Mungu. (2 Petro 3:7; 2 Wathesalonike 1:7-9) Yesu Kristo alitabiri kwamba muda mfupi tu kabla ya dunia kupata usafishaji huo wa kimungu, watu kwa ujumla wangekuwa wasiojali kufuata viwango vya Mungu kama walivyokuwa watu katika siku za Noa. (Luka 17:26-30) Kwa hiyo ni jambo la haraka kwetu tuthamini kwa ukamili miongozo ambayo Mungu ameweka. Ili tuje tuokolewe, kufanya hivyo ni kwa lazima kwetu leo kama kulivyokuwa kwa lazima kwa Noa katika siku zake.

Basi, kutokumtegemea Mungu hakuleti furaha ya kweli; kufanya mapenzi ya Mungu ndiko kunakoleta. Wale wanaonyenyekea mwongozo wa Yehova watathawabishwa kwa kupewa uzima wa milele juu ya dunia itakayojawa na watu wenye utu ulio kama wa Kristo.​—Zaburi 37:27-29.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Ni jengo la namna gani lingesimamishwa kama kila mfanya kazi angetupilia mbali michoro yenye kuongoza ujenzi kisha ajenge kama apendavyo?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Wewe una uhuru wa kusafiri, lakini ili ufanye hivyo ni lazima uendeshe motakaa yako bila kuruka mipaka iliyowekwa na sheria

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki