Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 11/1 kur. 29-30
  • Aliisikiliza Sauti Isiyofaa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Aliisikiliza Sauti Isiyofaa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Atii Washauri Wasio na Ujuzi
  • Aiacha Ibada ya Kweli
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 11/1 kur. 29-30

Aliisikiliza Sauti Isiyofaa

“MWENYE hekima asikie na kuongezewa elimu, na mwenye ufahamu ayafikie mashauri yenye njia.” (Mithali 1:5) Mithali hii ya Biblia inaonyesha wazi kwamba watu walio na hekima wanasonga mbele katika kujifunza. Wanatambua mashauri yenye utimamu na wana nia ya kuyafuata. Hivyo wanapata “njia” [“mwongozo wenye ustadi,” NW], au uongozi timamu, ili kushughulikia mambo ya maana maishani.

Mithali yenyewe inasemwa kuwa ilinenwa na Sulemani, mtawala aliyekuwa mwenye hekima zaidi nyakati za kale. (Mithali 1:1) Ikiwa Rehoboamu mwana wa Sulemani angalitenda kupatana na mithali hiyo, angalizuia uasi mzito katika milki yake. Lakini yeye alipendelea kusikiliza sauti isiyofaa​—sauti ya wasio na ujuzi. Kwa kuyafikiria matokeo ya mwendo wake, tutasaidiwa tuthamini uhitaji wa kufuata mashauri timamu.

Atii Washauri Wasio na Ujuzi

Wakati wa utawala wa Sulemani, watu waliendelea sana kuona uchungu kwa sababu ya Waisraeli huru kulazimishwa kisheria wafanye kazi katika shughuli za mfalme. Basi, wakati Rehoboamu alipomwandamia babaye katika ufalme, tume ya raia zake ilimtolea ombi hili: “Baba yako alilifanya zito kongwa letu; basi sasa utupunguzie utumwa mzito tuliotumikishwa na baba yako, na lile kongwa zito alilotutwika, nasi tutakutumikia.”​—1 Wafalme 12:4.

Mfalme alikubali kufikiria jambo hilo na baada ya hapo akaenda kushauriana na washauri wenye umri mkubwa na ujuzi. Wakapendekeza kwamba apunguze mizigo ya watu na hivyo aweze kuwafanya wamuunge mkono na kumpenda. (1 Wafalme 12:6, 7) Lakini ndipo Rehoboamu alipoomba maoni ya wanaume waliokuwa wamekua pamoja naye. Shauri lao lilikuwa: “Uwaambie hivi, Kidole changu cha mwisho ni kinene kuliko kiuno cha baba yangu. Basi kama vile baba yangu alivyowatwika kongwa zito, mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, bali mimi nitawapigeni kwa nge.”​—1 Wafalme 12:10, 11.

Shauri la vijana hao wa kiume lilimpendeza Rehoboamu. Kwa hiyo, wakati tume ya Waisraeli ilipofika katika wakati uliowekwa isikie uamuzi wa mfalme, yeye aliwaambia maneno yaliyopendekezwa na wale vijana wa kiume. Jambo hilo likachochea uasi wa makabila kumi, yakatimia maneno aliyonena Yehova kupitia nabii Ahiya kwamba makabila kumi yangeondolewa mbali kwa mwana huyo wa Mfalme Sulemani. (1 Wafalme 12:14-16) Yote hayo yalifanyika kwa sababu Rehoboamu alifuata shauri lisilo la utimamu! Aliisikiliza sauti isiyofaa.

Akitaka kuyarudisha makabila yaliyoasi yawe chini ya uongozi wake, Rehoboamu, pamoja na Adoramu (Hadoramu), mwanamume yule mwenye kuwasimamia watu waliolazimishwa kujiandikisha wafanye kazi ngumu muda wa utawala wote wa Sulemani, aliingia katika eneo la makabila hayo. Kwa wazi kuonekana tu kwa sura ya Adoramu mzee kuliwajaza hasira Waisraeli, kwa maana yeye alikuwa kiwakilishi cha kongwa zito la uonevu walilokuwa wamelazimishwa kuchukua. Waisraeli hao walimpiga kwa mawe akafa, naye Rehoboamu akamudu kuokoa uhai wake kwa kukimbia akiwa katika gari la kukokotwa na farasi.​—1 Wafalme 12:18; 2 Mambo ya Nyakati 10:18.

Ndipo sasa Rehoboamu akaita jeshi likusanyike ili liyalazimishe makabila yaliyoasi yanyenyekee. Lakini, wakati huo vita kati ya wananchi wenyewe kwa wenyewe ilizuiwa. Hiyo ni kwa sababu watu walitii vile Yehova alivyosema kupitia nabii Shemaya kwamba wasipigane na ndugu zao.​—1 Wafalme 12:21-24.

Aiacha Ibada ya Kweli

Kwa muda fulani, Mfalme Rehoboamu alijaribu kujipatanisha na amri za Mungu. Halafu ‘akaiacha torati ya Yehova,’ labda kwa sababu ya uvutano wa Kiamoni uliokuwa katika jamaa yao kupitia mama yake. (2 Mambo ya Nyakati 12:1; 1 Wafalme 14:21) Watu walifuata uongozi wake kuacha ibada ya kweli. Ikieleza yaliyotukia, Biblia inaripoti hivi: “Basi Yuda wakafanya maovu machoni pa [Yehova]; wakamtia wivu, kwa makosa yao waliyoyakosa, kuliko yote waliyoyafanya baba zao. Maana hao pia wakajijengea mahali pa juu, na nguzo, na maashera, juu ya kila kilima kirefu, na chini ya kila mti wenye majani mabichi. Na mahanithi walikuwako katika nchi, wakafanya sawasawa na machukizo yote ya mataifa [Yehova] aliowafukuza mbele ya wana wa Israeli.”​—1 Wafalme 14:22-24.

Kwa sababu ya ukosefu wa uaminifu wa Rehoboamu na raia zake,Yehova aliondoa ulinzi Wake. Katika mwaka wa tano wa utawala wa Rehoboamu, Shishaki (Sheshonki wa Kwanza) mfalme Mmisri alivamia Yuda, akateka miji yenye ngome, mmoja baada ya mwingine. Hata mji mkuu, Yerusalemu, ulitishwa. Akieleza sababu ya msiba huo, nabii Shemaya alimwambia Rehoboamu na wana-wafalme wake hivi: “[Yehova] asema hivi, Ninyi mmeniacha mimi, kwa hiyo nami nimewaacha ninyi mkononi mwa Shishaki.” Maneno hayo yaliwasukuma kutubu.

Kwa hiyo, Yehova Mungu hakumruhusu Shishaki aharibu Yerusalemu. Hata hivyo, Aliye Juu Zaidi aliruhusu Rehoboamu na raia zake wauhisi uzito wa mkono wa Wamisri katika maana ya kwamba walilazimishwa kuacha hazina za Yerusalemu zichukuliwe.​—2 Mambo ya Nyakati 12:1-12; 1 Wafalme 14:25, 26.

Kwa sababu Rehoboamu aliisikiliza sauti ya wasiokuwa na ujuzi, hakuendelea vizuri akiwa mfalme. Utawala wake ulikuwa na hali za uadui kati ya ufalme wake na ule wa makabila kumi yenye uasi yaliyokuwa chini ya Mfalme Yeroboamu. (1 Wafalme 14:30) Lakini, jambo zito zaidi ya hilo ni kwamba Rehoboamu alijiacha akengeushwe kutoka ibada ya kweli, kwa maana yeye alikufa akiwa mfalme ambaye ‘alitenda yaliyo maovu, kwa kuwa hakuukaza moyo wake amtafute Yehova.’​—2 Mambo ya Nyakati 12:14.

Hakika kisa cha Rehoboamu kinapasa kitukazie umaana wa kutoisikiliza sauti ya wasio na ujuzi. Inahitajiwa sana tutii mashauri yenye utimamu, hasa yale yanayotegemea Neno la Mungu!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki