Kunajisi Jina la Mungu—Kwa Kutolitumia
YEHOVA alishughulika kwa rehema na watu wa Israeli kwa ajili ya jina lake mwenyewe, ili lisije likanajisiwa kati ya mataifa. (Ezekieli 20:9, 13,14, 22) Lakini, baada ya muda fulani Waisraeli waliepuka kutumia jina la Mungu, hivi kwamba mwishowe matamko yalo yalipotea. Kutotumia jina la Mungu kwa njia hiyo kulikuwa sawa na kulinajisi.
Kuhusu hilo, R. Laird Harris alieleza hivi: “Ni jambo la kushangaza sana kwamba matamko ya kale ya jina la Mungu wa Israeli yamepotea kabisa. Imani ya Israeli ilikuwa ndiyo imani pekee yenye kustahili nyakati za kale. Ilikuwa ndiyo ibada ya kwanza ulimwenguni ya kumfuata Mungu mmoja tu na ndiyo imani moja tu ya kale iliyopata kweli kweli kuwa dini ya ulimwengu mzima. Ilitofautiana kabisa na imani zile nyingine kwa kuwa ya kiroho kabisa bila kutumia mfano wenye kuonekana wa mungu. Jambo la kusikitisha ni kwamba ilikuwa tofauti pia kwa kupoteza matamko ya jina la mungu. Hali hiyo ni ya ajabu sana na haingaliweza kutabiriwa na watu hao wenye moyo mweupe waliohisi kwamba hawangethubutu kulitamka jina hilo tukufu wasije wakalinajisi. Kwa kweli matokeo yanaonekana kuwa yalikuwa unajisi wa aina tofauti. Kutolitumia jina la Mungu kunaelekea kulinajisi sawa na vile matumizi machafu ya Jina hilo yangalifanya. Lakini mambo ya hakika ni wazi. Kwa asili, Waebrania wa kale walilitamka na kuliandika jina la Mungu.”— The Law and the Prophets, kilichohaririwa na John H. Skilton, Nutley, New Jersey, 1974, ukurasa 215.
Waisraeli walijua kwamba kama wangelisahau jina la Yehova, Mungu mwenyewe ‘angelichunguza neno hilo.’(Zaburi 44:20, 21) Baadaye, wakati jambo hilo lilipotukia, yeye ‘aligeuza fikira zake kwa mataifa ili achukue katika hao watu kwa ajili ya jina lake.’ (Matendo 15:14, NW ) Ingawa sisi leo hatujui barabara jinsi ya kulitamka jina la Mungu katika Kiebrania, fasiri inayofaa na ya kutosha ya Tetragramatoni (zile herufi bubu nne za Kiebrania zinazowakilisha jina hilo) katika Kiswahili ni Yehova. Leo, watu zaidi ya milioni tatu wanajulikana kama Mashahidi wa Yehova, nao wanafurahia kulichukua jina hilo la Mungu wao na kuhusianishwa nalo.