“Wapole” au “Watoto Wachanga”—Jambo Jipi?
KWENYE 1 Wathesalonike 2:7 mtume Paulo anaeleza kwamba yeye mwenyewe na wenzi wake walikuwa “wapole katikati yenu, kama vile mlezi awatunzavyo watoto wake mwenyewe.” Tafsiri nyingine (The Bible in Basic English; Today’s English Version) hapa zinasema “wapole,” lakini tafsiri nyingine (Westminster Version; American Translation) zinatumia neno “watoto wachanga” au “watoto.” Kwa sababu gani pana tofauti hiyo?
Watafsiri hao wanafuata moja ya namna mbili tofauti-tofauti zinazopatikana katika maandishi ya awali na hati za Kigiriki. Maandishi fulani ya Kigiriki (Textus Receptus, Tischendorf, Merk) na hati zinasema eʹpi·oi, maana yake “wapole,” lakini maandishi mengine ya Kigiriki (Westcott na Hort, Nestle-Aland) na hati zinasema neʹpi·oi, maana yake “watoto wachanga.”
Kuhusu jambo hilo, kichapo The New International Dictionary of New Testament Theology (Buku la 1, 1975, ukurasa 282) kilieleza hivi: “Kuna njia mbili za kusoma 1 The. 2:7: (a) ēpioi (sisi tulikuwa wapole katika ushirika wenu); (b) nēpioi (watoto wachanga). Neno IililotanguIia [katika mstari huu] linaisha na herufi n, na inaelekea kuwa n hiyo imeandikwa mara mbili kupitia kosa la kunakili. Tena kufasiriwa kwa ile njia ya pili ya kusoma maneno hayo kunatokeza matatizo. Kwa maana katika mstari 7b Paulo hajifananishi mwenyewe na ‘watoto’ bali anawafananisha Wathesalonike; yeye na wenzi wake walikuwa kama mlezi (trophos).” Basi, kwa kufaa tafsiri nyingi hapa zinasema “wapole” badala ya “watoto wachanga.”
Lakini mbona Paulo akatumia neno “wapole” hapa? Ni kwa sababu ya upendo wa kweli kweli na kwa kujali asidhuru ukuzi wa kiroho wa wale ambao yeye na wamisionari wenzake waliwafundisha. (1 Wathesalonike 2:8) W. E. Vine (An Expository Dictionary of New Testament Words, chapa ya 1962, Buku la 2, ukurasa 145) anasema kwamba neno eʹpi·os “lilitumiwa mara nyingi na waandikaji Wagiriki kuonyesha mlezi mwenye watoto wenye kuujaribu uvumilivu wake au mwalimu mwenye wanachuo wakaidi, au juu ya wazazi kuelekea watoto wao. Katika 1 The. 2:7, Mtume anatumia neno hilo juu ya mwenendo wake mwenyewe na wa wamisionari wenzake kuelekea waongofu wa Thesalonike.” Tunapofundisha watu Neno la Mungu, sikuzote na tuukumbuke upole ulioonyeshwa na Paulo na wenzi wake kisha tuige mfano wao.