Ongezeko la Ufalme Katika Nchi ya Wamaliki
UKITAZAMA ramani ya Ulaya ya Kati, utaiona imekaa vizuri chini ya milima Alps ile nchi ndogo ya Austria, yenye eneo la kilometa za mraba 83,850. Hiyo ndiyo nchi ya nyumbani kwa Johann Strauss, yule mfalme wa dansi ya farasi walio maridadi sana na stadi wa michezo. Na hapa, wakati mmoja ndipo yalipokuwapo makao ya ile Milki kubwa ya muungano wa Austria na Hangari, iliyotawala Bohemia na Moravia, sehemu za Italia, Polandi, Romania na Yugoslavia.
Milki hiyo haipo leo, lakini bado ilikuwapo mwaka 1911 wakati Charles Taze Russell, msimamizi wa kwanza wa Sosaiti yetu, alipotembelea Vienna nayo magazeti ya nchini yakachapisha hotuba yake kwa njia ya kutokeza. Bado ilikuwapo miaka mitatu baadaye, wakati mtu mwingine alipopeleka habari njema huko.
Maxwell Friend anaandika hivi: ‘Wakati J. F. Rutherford, ambaye angekuwa ndiye msimamizi wa pili wa Sosaiti yetu, alipotutembelea, aliniuliza kama ningependa kutumwa Austria-Hangari nikaeneze habari njema za Ufalme wa Kimasihi kati ya Wayahudi wengi wenye kuishi huko. Nilikubali mwaliko huo kwa furaha nikaenda Prague mwanzoni mwa mwaka 1914 . . . Baadaye nilienda Vienna . . . Walikuwako waandikishaji wanne tu wa Mnara wa Mlinzi katika Vienna. Mimi niliwatembelea-tembelea kuwatia moyo wapendezwe na Neno la Mungu.’
Lakini, baadaye mwaka huo mwana-mfalme mwenye kutawala Austria aliuawa, na Ulaya ikarushwa ndani ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Zile Mamlaka za Kati, kutia ndani Austria-Hangari, zilishindwa vita, nayo Milki kuu ya muungano wa Austria na Hangari ikavunjiliwa mbali. Kutokana na masalio yake, ikatokea Jamhuri ndogo ya Austria yenye kusema Kijeremani.
Lakini, kulingana na unabii wa Biblia, “taifa” jingine lilipasa kuzaliwa wakati huo, taifa la kiroho ambalo lingekuwa na washiriki katika sehemu zote za ulimwengu. (Isaya 66:8) Wakati “taifa” hilo lilipoanza kueneza kati ya mataifa yote habari njema za Ufalme wa Mungu uliokuwa sasa umesimamishwa, mavutano ya taifa hilo yalihisiwa upesi katika Austria.
Joseph Ehm, mwalimu wa muziki katika Deutsch-Wagram, karibu na Vienna, aliusikia ujumbe ule na kutambua huo ulikuwa ni ukweli wa Kibiblia. Baada ya muda mfupi alianza kuzishiriki habari njema pamoja na wengine. Katika mwaka uliofuata, 1921, mtu mwingine mwenye kupendezwa katika Austria, France Ganster, mtunza vitabu katika Klagenfurt, alipokea vitabu kutoka Uswisi. Wakati ule ule, mkulima mmoja katika Austria ya Juu, Simon Riedler, alipata kijitabu kwa rafiki katika Linz. Hivyo, mwanzo mdogo ulifanywa. Afisi ya tawi ya kwanza ya Sosaiti yetu ilianzishwa katika Vienna mwaka 1923. Mbegu ya ukweli ikawa imeanguka katika udongo wenye rutuba na kuanza, kukua. Kufikia mwaka 1937, watu 549 walikuwa wakishiriki katika kazi ya kueneza habari njema.
Tukio Kubwa la Pili Ulimwenguni
Lakini, wakati wa kipindi hiki kani nyingine zilianzishwa ambazo zingeleta msukosuko mkubwa na kuihusisha sana Austria katika matukio ya ulimwengu kwa mara nyingine. Fujo za kitaifa na mashindano ya kisiasa yalimwezesha Adolf Hitler, waziri mkuu wa Ujeremani aliyezaliwa Austria, aingize nchi ya nyumbani kwao katika Reich, au milki, mpya ya Kijeremani. Jambo hilo lilikubaliwa na kura ya taifa na kuungwa mkono na makasisi Wakatoliki wa nchi hiyo. Lakini jambo hilo lilileta matatizo ya mara hiyo kwa Mashahidi wa Yehova katika Austria.
Kwa sababu ya kutokuwamo kwao, mashahidi wengi wa Austria sasa wakatiwa katika kambi za mateso. “Historia ya Kambi ya Mateso ya Mathausen,” ambayo imeandikiwa utangulizi na France Jonas, aliyekuwa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Austria, inasema: “Kulikuwa na kikundi cha watu katika Kambi ya Mateso Mathausen kilichoteswa kwa sababu za kidini tu: washiriki wa madhehebu inayoitwa ‘Wanafunzi wa Biblia Wenye Bidii,’ au ‘Mashahidi wa Yehova’ . . . Kukataa kwao kutoa kiapo cha ushikamanifu kwa Hitler, na kukataa utumishi wa kijeshi wa aina yo yote ambao ungekuwa ni hali ya kisiasa kuhusiana na imani yao, ndiyo sababu iliyofanya wateswe.”
Ongezeko la Hivi Majuzi
Utawala ambao Hitler alikusudia uwe wa “miaka 1,000” ulikuwa wa miaka michache tu, na ulipoanguka kundi hilo jaminifu la watumishi washikamanifu wa Mungu lilipata tena uhuru. Alois Moser mwenye umri wa miaka 84, aliyekaa katika kambi za mateso miaka kadha, anasimulia hivi juu ya siku ya kufunguliwa kwake mwaka wa 1945: “Mashahidi 230 kutoka mataifa kumi walikusanyika mwituni karibu na Schwerin, Mecklenburg. Sisi tulionyesha shukrani za moyo wetu katika azimio: ‘Sisi sote Mashahidi wa Yehova tunapeleka salamu zetu za kutoka moyoni kabisa kwa watu waaminifu wa agano la Yehova na kwa wenzi wao katika ulimwengu mzima . . . Sisi tunafanya azimio zito la kwamba tunataka jambo moja tu, baada ya kujionea mlolongo usio na mwisho wa mambo yenye kututhibitishia ulinzi wa ajabu na ukombozi kutoka katika maelfu ya mizozo na mateso wakati wa kukaa kwetu katika tundu la simba, yaani, kutumikia Yehova na Mfalme Yesu Kristo kwa kuongozwa na shukrani za ndani kabisa kwa moyo wenye nia na shangwe na kwa wakati usiojulikana.”
Mwaka mmoja baadaye watu 730 wenye kusifu Yehova waliripoti utendaji wao. Miaka miwili baada ya hapo kulikuwa na 1,551, na ongezeko limeendelea kuja bila kukoma tangu wakati huo. Kazi ya kuhubiri kati ya maelfu kadha ya wafanya kazi wa kigeni imezaa matokeo pia. Sasa Austria ina vikundi vya Wakristo wenye kusema Kihangari, Kiingereza, Kipolandi, Kiromania, Kispania, Kituruki, na Kiarabu, na pia makundi yenye kusema Kijeremani 229 na 6 ya Kiserbo-Croatia. Kufikia sasa, Mashahidi wa Yehova ni zaidi ya 15,000, lakini watu wengine wengi wanavutwa na uwezo wa habari njema. Hivyo, watu 27,502 walikusanyika mwaka 1985 kwa ajili ya ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Yesu Kristo. Kwa kweli, ‘mdogo amekuwa elfu.’—Isaya 60:22.
Wonyesho wa Umoja wa Kimataifa
Mahali ambapo nchi ya Austria ipo paliwezesha Mashahidi kutoka Ugiriki, Yugoslavia, Polandi, Hangari, na Uturuki waje hapa wakati wa miaka ya majuzi ili kuwa na ushirika wenye furaha. Mwaka 1981, lilikuwa jambo la kusisimua kwenye “Ushikamanifu kwa Ufalme” mkusanyiko wa wilaya kuona Mashahidi wa Austria wakiinuka kutoka kwenye viti vyao pamoja na ndugu zao wa kutoka Yugoslavia, Polandi, na Hangari, wamalize mkusanyiko kwa wimbo wenye shangwe wa kusifu Yehova.
Mwaka 1982, Mashahidi katika Austria wakawa tena ndio wakaribishaji wa ndugu zao kutoka Hangari kwenye mkusanyiko katika Vienna. Mmoja aliyekuwa mwanariadha wa Vienna aliwaambia Mashahidi waliokusanyika jinsi alivyofanya mazoezi kwa ajili ya matukio yake ya kimichezo katika uwanja ule ule ambamo kusanyiko lilikuwa likifanyiwa, na kwamba shindano la mwisho aliloshiriki lilikuwa dhidi ya wanamichezo wa kutoka Hangari. Baadaye Shahidi kutoka Hangari alikuwa kwenye afisi ya mkusanyiko akaeleza kwamba yeye, pia, alikuwa mwanariadha. Shindano lake la mwisho la uanariadha lilikuwa dhidi ya wanamichezo wa kutoka Austria. Sasa, Wakristo hawa wawili hawashindani tena kati ya wao kwa wao. Wao wanakimbia pamoja katika mbio ya Kikristo kwa ajili ya uzima wa milele.—Waebrania 12:1.
Ongezeko la Ufalme Laendelea
Watu wa kutoka vyanzo mbalimbali, na pia wenye maoni tofauti tofauti ya kisiasa na kidini, wamekuja kutambua kwamba wala utawala wenye amri yote wala wa kutumia mabavu wala demokrasi haitaweza kuleta suluhisho la kudumu kwa matatizo ya wanadamu. Utambuzi huo umetokeza ukuzi wenye kuongezeka wakati wote katika hesabu ya wale wanaoutambua Ufalme wa Mungu kuwa kitu halisi na wanaojitiisha kwa moyo wote kwenye Ufalme huo wakiwa raia washikamanifu. Mashahidi wa Yehova katika Austria wanaendelea kwa bidii kujitahidi kuwapelekea habari njema za Ufalme watu wa aina zote. Muda wote huo, katika nchi hii ya waliokuwa wamaliki, wao wenyewe wanatanguliza serikali hiyo ambayo utawala wao wenye kufaidi watu utafika “toka bahari hadi bahari, toka Mto hata miisho ya dunia.”—Zaburi 72:8.
[Ramani katika ukurasa wa 26]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
UJEREMANI MAGHARIBI
CHEKOSLOVAKIA
AUSTRIA
HANGARI
YUGOSLAVIA
ITALIA
THE ALPS
USWISI