Roho ya Upainia Inaharakisha Mavuno ya Ufilipino
KAMA ungalikuwa katika Manila kule nyuma mwaka 1935 na ukataka kuonana na Mashahidi wa Yehova, ingalikupasa kutafuta kijumba kimoja kwenye barabara iliyoitwa 1134 Rizal Avenue. Kule, karibu watu 20 walikutana kwa ukawaida kujifunza Biblia. Kijumba hicho kilikuwa ndicho afisi ya tawi ya kwanza ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi katika Ufilipino.
Leo, katika eneo la mji wa Manila, kuna makundi 103 ya Mashahidi wa Yehova yakiwa na watangazaji wa Ufalme zaidi ya 9,000! Vivyo hivyo, miaka 50 iliyopita hakukuwa na Mashahidi katika Mji wa Davao, katika kusini ya mbali ya Ufilipino. Sasa wako zaidi ya 2,800 katika makundi 41 ya mji huo.
Ongezeko katika miji hiyo miwili mikubwa ni sehemu ya ushuhuda wa kwamba Mashahidi hao wa kwanza waliishi kulingana na jina lao. (Isaya 43:10-12) Wao wamepanua kazi yao ya kuhubiri na kufundisha kwenye sehemu zote za Ufilipino. Kwa kuchunguza orodha iliyoambatanishwa na makala hii, unaweza kuona matunda ya kazi ya Kikristo ya kufanya wanafunzi wakati wa nusu-karne iliyopita. Ni jambo gani linaloharakisha ukuzi katika shamba la Ufilipino.
Roho ya Upainia Inasaidia Ukuzi
Kama isingalikuwa ni kwa sababu ya roho ya kuwa na bidii katika upainia kwa upande wa Mashahidi Wafilipino wa kwanza, isingaliwezekana kufika na habari njema kwenye mamia ya visiwa vinavyokaliwa na watu. Roho hiyo ingali hai kabisa. Kwa mfano, ripoti ya Februari 1986 ilionyesha kwamba, zaidi ya mapainia wa pekee 758, kulikuwa na wahudumu mapainia wa kawaida 9,090 wenye kutumikia katika sehemu zote za Ufilipino. Kiasi hicho kilikuwa zaidi ya mara mbili ya hesabu ya wenye kuripoti miaka miwili tu kabla ya hapo! Katika Aprili 1985, ambao ulikuwa ndio mwezi wenye hesabu ya juu zaidi ya mapainia kufikia wakati ambao makala hii ilikuwa ikitayarishwa, watu 26,630 —theluthi moja ya Mashahidi wote walio nchini—walikuwa katika namna fulani ya kazi ya kuhubiri wakati wote.
Ndiyo, watu wa Yehova katika Ufilipino wanauona uharaka wa wakati. Jambo hilo linawaharakisha watumie wakati mwingi kama wawezavyo wakihubiri na kufundisha jirani zao Neno la Mungu. Bila shaka, wewe ungependezwa kujua ni jinsi gani wengine wanaweza kupanga mambo yao ili waingie katika utumishi wa wakati wote na ungependa kujua mambo mazuri wanayofurahia.
Kufanya Marekebisho Ili Kupainia
Felipe Ventura wa Binalonan, Pangasinan, alitumia miaka ya ujana wake katika utumishi wa wakati wote kabla ya kuwa na jamaa. Jamaa yake ilipokua, yeye alitamani kurudia kazi ya upainia. Lakini ugonjwa kisukari ukamfanya awe kipofu katika jicho moja. Halafu miaka minne hivi iliyopita akawa kipofu kabisa. Ingawaje, Felipe aliweza kuendesha biashara ndogo ili ategemeze jamaa yake na, Aprili 1, 1985, kwa msaada wa mke na watoto wake, aliweza kurekebisha wakati wake ili aweze kuwa painia tena. Ijapokuwa kizuizi chake mwilini, anashiriki katika huduma ya nyumba-kwa-nyumba kwa msaada wa kijana wake, ambaye humsomea maandiko ya Biblia. Ndugu Ventura anaongoza mafunzo kadha ya Biblia na ni mzee aliyewekwa wa kundi. Moja wa vijana wake anatumikia kama painia wa kawaida pamoja naye, na binti yake hufanya upainia msaidizi mara kwa mara.
Clodualdo Quiohilag, mzee katika Binan, Laguna, alikuwa painia na mwangalizi mwenye kusafiri katika miaka ya 1960 mpaka yeye na mke wake walipopata mtoto. Lakini, kama anavyosema yeye, “Ukiisha kuonja furaha ya utumishi wa wakati wote, sikuzote unakuwa na tamaa ya kuufanya.” Kwa hiyo ingawa yeye alikuwa amepata mafanikio katika biashara na kufurahia maisha ya starehe pamoja na mke na binti yake, hakulifikiria hilo kuwa ndilo kusudi lake kubwa maishani. Anaeleza hivi: “Vitu vyote nilivyo navyo vingekuwa havina maana kama ndoto yangu ya muda mrefu ya kurudia utumishi wa wakati wote haingetimizwa.” Ili kuwa painia, alipunguza utendaji wake wa kibiashara akawa akiufanya nusu-siku, akitumia nyakati za asubuhi katika huduma ya shambani. “Ndoto” yake ilitimia Oktoba 1, 1984, alipoanza kutumikia akiwa painia wa kawaida. Ingawa mapato yake ni karibu nusu ya vile yalivyokuwa, gharama zake ziko chini pia. Sasa mke wake amejiunga naye katika kazi ya painia wa kawaida, na binti yake anatumikia akiwa painia msaidizi mara kwa mara.
Kutumikia Wakati Wote Ingawa Kipofu
Kwa sababu ya kupatwa na ukambi wa Kijeremani, Pantaleon Tatoy amekuwa kipofu tangu alipokuwa na umri wa miaka mitatu. Katika mwaka 1972 yeye aliusikia ukweli kwa mara ya kwanza na akaanza kujifunza kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Baada ya muda mfupi kilimsaidia akashinda uzoelevu wake wa kutumia tumbako na vileo, naye akaonyesha wakfu wake kwa Yehova kwa kubatizwa Julai 29, 1973.
Wakati Pantaleon alipoanza mara ya kwanza kuhubiria jirani zake, dada yake mkubwa alimgombeza hivi: “Unawezaje kuwa mhudumu na hali wewe ni kipofu na suruali una moja tu? ” Lakini jambo hilo halikumvunja moyo. Kwa kuwa yeye alilijua vizuri eneo la karibu na nyumbani kwao, alienda nje pekee yake na kuwahubiria jirani zake ukweli. Mwaka 1984 alifurahi sana kuweza kusaidia binamu yake na mpwa wa kiume waujue ukweli, nao wakabatizwa katika Septemba wa mwaka huo.
Pantaleon ameweza pia kuongoza funzo la Biblia pamoja na wapwa zake wa kike walio mapacha, Lorna na Luz, wote wawili wakiwa ni mabubu na viziwi. Painia kipofu anajifunzaje na watu kama hao? Akiwa na msaada wa msaidiaji, yeye anatumia picha katika vichapo kwa wingi sana. Anapoeleza ukweli, Roquina binamu yake anamtafsiria kwa lugha ya ishara mambo anayosema kwa ajili ya mapacha wale. Lorna na Luz walibatizwa Aprili 20, 1985, wajapokuwa na kizuizi chao kikubwa. Habari ya Pantaleon, yeye aliwekwa kuwa painia wa kawaida Machi 1, 1985 baada ya kutumikia akiwa painia msaidizi kwa mwaka mmoja.
Utumishi wa Wakati Wote Ukiwa Kazi ya Maisha Yote
Kwenye sherehe ya kuhitimu masomo ya shule ya pili, mwanafunzi fulani alimwambia mwanadarasa mwenzake aliye Shahidi hivi: “Wakati wo wote ninapouliza watu wenu ni taaluma gani watakayochukua baada ya kuhitimu masomo, wote wanasema, ‘upainia.’ Hiyo ni taaluma ya aina gani? ” Yule Shahidi kijana akaeleza maana ya upainia. Mwanafunzi mwenzake akapendezwa na kukubali funzo la Biblia, na msichana huyo, pia, baada ya muda mfupi akawa na mradi wa kuwa painia.
Wengine wameona kwamba taaluma za chuoni hazitoshelezi mahitaji ya mtu ya kiroho. Katika Bohol, dada kijana aliyekuwa katika mwaka wa mwisho wa chuo alikuta kwamba alikuwa na wakati wa kupainia huku akimalizia masomo yake. Baadaye, yeye alihudhuria Shule ya Utumishi wa Painia na akaeleza kwamba mambo aliyojifunza chuoni hayangeweza kulinganishwa na shule hiyo na furaha ile aliiona katika kumtumikia Yehova wakati wote. Sasa yeye anatumika akiwa painia mahali ambako uhitaji ni mkubwa wa wahubiri.
Vijana na Wazee Wanashiriki kwa Nia
Kitabu cha Zaburi kilitabiri kwamba katika siku za mamlaka ya Ufalme watu wa Mungu ‘wangejitoa kwa hiari.’ Kilisema pia kwamba ‘vijana waume, wanawali, wazee na watoto’ wangesifu jina la Yehova. (Zaburi 110:3; 148:12, 13) Hakika hivyo ndivyo imekuwa kati ya watu wa Mungu katika Ufilipino
Kulingana na hesabu ya mwisho, watu 1,159 au asimilia 13, ya mapainia wa kawaida walioandikwa orodhani katika Ufilipino walikuwa chini ya umri wa miaka 20. Ni furaha kama nini kuona vijana kama hao ‘wakimkumbuka bila choyo Muumba wao katika siku za ujana wao’ badala ya kutapanya ujana huo kwa kufuatia mambo ya kichoyo au ya kilimwengu!—Mhubiri 12:1.
Wengine walioanza utumishi wa wakati wote katika ujana wanaendelea sasa kuzeeka lakini bado wanatumikia kwa uaminifu. Ndugu Leodegario Barlaan na Natividad mke wake walianza kupainia Aprili 1, 1938. Wao walipita katika ile miaka yenye magumu ya vita na wametumikia katika nafasi mbalimbali, kutia na kazi ya kusafiri. Sasa ndugu Barlaan ana umri wa miaka 72 na bado anatumikia kwa bidii akiwa painia wa pekee katika Mji San Carlos, Pangasinan, pamoja na mke wake.
Wengine walianza utumishi wa wakati wote baadaye katika maisha na wakaendelea mpaka uzee wao. Kwa mfano, Leoncio Sabandal alianza kupainia akiwa na umri wa miaka 52 na bado yeye ni painia wa pekee akiwa na miaka 92. Yeye na mke wake wamesaidia watu 118 waweke wakfu maisha zao kwa Yehova. Vivyo hivyo, Cipriano Sepulveda, Mkubwa, alianza kupaina alipokuwa na umri wa miaka 72 na alikuwa painia wa kawaida mpaka kufa kwake akiwa na umri wa miaka 88 mwaka 1985. Paula Mariano alianza kupaina akiwa na umri wa miaka 71 na bado yumo katika utumishi wa wakati wote ajapokuwa na hali za udhaifu wa kimwili akiwa na umri wa miaka 88. Wazee hao na wengine ni mifano inayostahili kama nini ya imani na kujitoa!
Kufurahi Sana Katika Maendeleo Yaliyofanywa
Tunapotazama nyuma kwenye nusu-karne iliyopita, baraka ya Yehova juu ya jitihada nyingi za Mashahidi wake inaonekana wazi. Kutoka makumi machache yaliyokuwako mwaka 1935, ni furaha kama nini kuona watu 88,113 wakishiriki katika huduma ya shambani mwezi Februari 1986. Lile kundi lililokuwa dogo katika Rizal Avenue katika Manila sasa limeongezeka yakawa makundi 2,454 nchini pote, yaliyopangwa kuwa mizunguko 120.
Na kuna mataraja gani kwa wakati ujao? Jambo lenye kuonyesha kwamba kuna mataraja ya kutia moyo ni hudhurio la kutokeza la watu 268,526—zaidi ya mara tatu za hesabu ya Mashahidi walio nchini—kwenye mwadhimisho wa Ukumbusho siku ya Aprili 4, 1985. Tena, katika Februari 1986, jumla ya mafunzo ya nyumbani ya Biblia 63,248 yalikuwa yakiongozwa kwa watu wanaopendezwa. Na bila shaka ukuzi wenye kuendelea utaonekana kwa baraka na kibali ya Yehova.
Tunafurahi kwamba Yehova ameifanya izae matunda mengi kazi iliyoanzishwa na mashahidi wake wa kwanza wapakwa-mafuta katika visiwa hivi miaka zaidi ya 50 iliyopita. Kwa baraka na uongozi wake, mradi wa watu wake katika Ufilipino ni kuendelea kuipanua kazi ya kuhubiri na kufundisha katika siku zitakazokuja.
[Chati katika ukurasa wa 29]
Miaka hamsini ya ukuzi wa Mashahidi Wafilipino
1935 20
1940 222
1950 10,055
1960 31,608
1970 54,789
1980 61,164
1986 88,113
[Ramani katika ukurasa wa 28]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Ufilipino
San Carlos
Manila
Biñan
Zamboanga
Davao