Ufufuo wa Yesu Kristo—Si Hadithi tu ya Uwongo
JE! MASIMULIZI ya Biblia juu ya ufufuo wa Yesu yangeweza kuwa ni jambo la kutungwa tu? Hivi majuzi kichapo International Herald Tribune kiliarifu juu ya uchunguzi uliofanywa na Pinchas Lapide mwandikaji Myahudi. Yeye alikataje maneno? Kwamba ufufuo si hadithi ya uwongo tu.
Mambo kadha yalimwongoza Lapide kukata maneno hivyo. Kwanza, masimulizi ya Injili yanasimulia kwamba wanawake watatu walienda kwenye kaburi la Yesu wakakuta likiwa tupu. Lakini katika nyakati za kale, wanawake ‘walionwa kuwa wasioweza kutoa ushahidi halali,’ inasema ripoti ya Tribune. Kwa kweli, wanafunzi wa Yesu mwenyewe hawakuwaamini wanawake hao! Hivyo inaelekea kuwa vigumu sana kwamba hadithi ya namna hiyo ingalitungwa tu kwa makusudi.
Lapide anataja pia matokeo yenye kusisimua juu ya wanafunzi wa Yesu. Ingawa wanaume hao walikuwa wameogopa sana hata wakamwacha Yesu alipokamatwa, wao ‘walibadilika upesi sana wakawa jamii ya watume wenye uhakika, wenye kuusadiki wokovu.’ Kichapo Tribune kinaarifu hivi juu ya sababu anayotoa Lapide, “Hakuna njozi au ndoto inayotosha kueleza badiliko hilo la kimapinduzi.”
Mwisho, kuna shtaka la kwamba wanafunzi wa Yesu waliuiba mwili wake tu. Kuhusu hilo, Bw. Lapide anajibu: “Je! walaghai wanaweza kujiacha waumizwe-umizwe na kuteswa kwa sababu ya maono ya kuwaziwa tu, mpaka wafurahie kufia imani?” Ingawa Bw. Lapide bado hadai kuwa anaamini Yesu kuwa Masihi, yeye hana shaka kubwa kwamba lililotangazwa na malaika miaka elfu mbili iliyopita ni kweli: ‘Kristo alifufuliwa.’—Mathayo 28:6.