Mambo Makuu ya Biblia Zaburi 1 hadi 41
Mtunga Zaburi Aimba Sifa ya Yehova
“Sifa.” Hii ndiyo maana ya jina la Kiebrania la kitabu cha Zaburi, na linafaa kama nini! Kwa kweli kitabu chote ni sauti moja ndefu ya sifa kwa Yehova Mungu. Zaburi zinaeleza sifa za kazi zake za nguvu. Zina mambo mengi ya unabii na pia zinatueleza jinsi walivyojisikia waandishi wenye roho ya Mungu walipokuwa wakivumilia kuteswa, kusalitiwa, kuvunjika moyo, hata pia kuwa na dhamiri mbaya. Wakristo wengi wenye kupatwa na majaribu kama hayo wamepata nguvu kutokana na maneno hayo ya Zaburi.
Kitabu cha Zaburi kimegawanywa katika sehemu tano. Hapa tutazungumza mojapo ya hizi Zaburi 1 hadi 41.
Kunyenyekea Makusudi ya Yehova
Tafadhali Soma Zaburi 1 hadi 14. Fungu hili la Zaburi linaingiza vingine vya vichwa vikuu vya kitabu cha Zaburi: Maana ya Sheria, unabii kuhusu kuja kwa Mfalme wa Kimasihi, na sala za kusaidiwa wakati wa kukabiliana na mikazo mikali. Kuongezea, tunajifunza kwamba, hata waovu wakipanda daraja kwa muda, waadilifu watabarikiwa.
◆ 2:1—Ni “ubatili” gani mataifa waliendelea ‘kutafakari’?
Mataifa waliendelea ‘kutafakari’ juu ya kuendeleza milele mamlaka zao wenyewe, badala ya kukubali Mpakwa Mafuta wa Yehova. Maneno hayo yalikuwa na matumizi katika karne ya kwanza W.K., wakati Waroma na wakuu Wayahudi walipoungana pamoja ili wamwue kwa kuua Mfalme mpakwa-mafuta wa Yehova, Yesu Kristo. (Matendo 4:26-28) Lakini, utimizo ulio mkubwa umekuwako tangu mwaka 1914, wakati mataifa yote yalipomkataa Mfalme aliyetawazwa wa Yehova, na kujaribu kuendeleza enzi yao wenyewe.
◆ 2:12—Kwa nini amri inatolewa ya kwamba, [“Mbusuni Mwana”?]
Nyakati za Biblia, kubusu kulikuwa wonyesho wa urafiki na kulitumiwa kwa kukaribisha wageni katika ukarimu wa nyumba ya mtu. Katika mstari huu, Yehova anaamuru mataifa wabusu, au wakaribishe, Mwanaye akiwa Mfalme mpakwa-mafuta wake.—Zaburi 2:2, 6-8.
◆ 9:12—Kwa nini Yehova huenda ‘akilipiza kisasi cha damu’?
Kama hakimu aketiye katika hukumu, Yehova anatafuta wale ambao wana hatia ya kuua kwa sababu ya kumwaga damu ya watu wake wasio na hatia. (Mwanzo 9:5, 6; Luka 11:49, 50) Pia anaadhibu wenye hatia. Lakini maadhibisho yake hayapati kila mtu tu bila kuchagua. Mtunga Zaburi Daudi anatuthibitishia hivi: “Hakukisahau kilio cha wanyonge.”—Linganisha 2 Petro 2:9.
◆ 11:3—Ni nini “misingi” ambayo inaharibika?
Misingi hiyo ni haki, sheria, na utaratibu—misingi ambayo jamii ya watu inategemea. Wakati utaratibu wa kijamii unapoharibika, bila uwezekano wa kufanywa haki, watu wanaoogopa Mungu wanapaswa kufanya nini? Kumtumaini Yehova. Yeye yuko katika kiti chake cha enzi cha mbinguni, anaona kila jambo linaloendelea, na hatatukatisha tamaa.
Somo Kwetu Sisi: Zaburi 4:5 inasihi wanaoogopa Mungu ‘watoe dhabihu za haki.’ Katika siku za Daudi, Waisraeli walipaswa watoe dhabihu zao juu ya madhabahu ya Yehova. Lakini pia walipaswa wawe na nia nzuri na wenye toba ya kweli. (Isaya 1:11-17) Wakati Wakristo wanapotoa dhabihu zao za kiroho, wao pia, wanahitajiwa wawe na makusudio yanayofaa na ni lazima waishi kulingana na kanuni bora za Yehova.—Waebrania 13:4,5, 15, 16; 1 Petro2:1,5.
Mungu asiyelinganika
Soma Zaburi 15 hadi 24. Fungu hili la zaburi lina semi nyingi za sifa kwa Yehova. Yeye ni Mhifadhi wa watu wake (18), Muumba na Mtoa-sheria (19), Mwokozi (20), Mhifadhi wa Mfalme wake mteule (21), Mchungaji Mkuu (23), na Mfalme Mtukufu (24).
◆ 16:10—Ni nani “Mtakatifu” (“Mshikamanifu” NW) ambaye ametajwa hapa?
Wanachuo wengine wa Biblia wanatumia mstari huu kwa waaminifu wote, kwa kutaja kama tegemezo lao kwamba katika hati fulani za maandishi ya Kiebrania neno “Mtakatifu” (“Mshikamanifu,” NW) limetumia kwa namna ya wingi. Lakini maneno ya mstari huo yanapotumiwa katika Maandiko ya Kigiriki ya, Kikristo, neno hilo linahusu umoja, kuonyesha mtu mmoja tu “Mtakatifu” (“Mshikamanifu” NW). Yeye ni nani? Mwanzoni, pengine ni Daudi mwenyewe. Lakini kwa unabii, Petro na Paulo pamoja wanautumia mstari huu kuhusu Yesu.—Matendo 2:25-32; 13:35-37.
◆ 21:3—Ni nini iliyokuwa “taji ya dhahabu safi”?
Pengine hilo lilikuwa taji halisi, kama lile lililoondolewa kutoka sanamu Malkamu. (Linganisha 2 Samweli 12:29, 30.) Au pengine taji lilikuwa la mfano tu, mfano wa kwamba ushindi wa Daudi uliuletea mapambo zaidi utawala wake mtukufu. Hata hivyo, zaburi hii inayoonyesha kwa unabii vile Yehova alivyompa Yesu taji ya utawala mwaka 1914. “Taji ya dhahabu safi” inayoonyesha kwamba utawala wake ni wa sifa kuu sana.
◆ 22:1—Je! Mungu alikuwa amemwacha Daudi?
La, lakini wakati Daudi alipokuwa katika mkazo mkubwa kutoka kwa adui zake, ilionekana kuwa hivyo. Lakini, hali ya kibinadamu iliyomwingia Daudi kwa sababu ya shida nyingi haikuonyesha hakuwa na imani, kwa vile yeye anaendelea kusali kwa ujasiri akombolewe. (Mistari 16-19) Jambo linalofaa kuangaliwa ni kwamba Yesu alitumia maneno ya zaburi hiyo kabla hajafa juu ya mti wa mateso. Kwa kuuliza “mbona?” Yesu aliuonyesha mkazo mwingi sana sana aliokuwa nao, hali wakati ule ule akitangaza hakuwa na hatia ya mashtaka ya uwongo yaliyofanya auawe.
Somo Kwetu Sisi: Mtume Paulo anataja juu ya maneno ya zaburi 22:22 na kuyatumia kuhusu njia ambayo Yesu Kristo anaongoza katikati ya ndugu zake wapakwa-mafuta kwa kutangaza jina la Yehova. (Waebrania 2:11, 12) Zaburi 22:27 inaelekeza kwenye wakati ambao “jamaa zote za mataifa” zitaungana na watu wa Yehova kwa kumsifu yeye. Leo, kundi kubwa sana la watu wa kimataifa wanaabudu Mungu pamoja na ndugu za Yesu. (Ufunuo 7:9) Tunapaswa kukaa karibu na mpango huu uliotengenezwa kimungu.
Uwezo Mkuu wa Yehova
Soma Zaburi 25 hadi 34. Katika Zaburi 25 na 26, Daudi anajulisha kwamba ana tamaa ya kutembea katika ukamilifu wake. Halafu zinafuata semi za kumtumaini Yehova kwa ushujaa na katika Zaburi 33 maelezo bora, kuhusu uwezo wa Yehova.
◆ 28:8—Ni nani “masihi” [“mtiwa mafuta”] wa Yehova?
Katika mstari huu “masihi” [“mtiwa mafuta”] ni watu wa Yehova wateule, kama inavyoonekana katika mstari-sambamba, wenye kusema “[Yehova] ni nguvu za watu wake.” Maneno hayo yana maana ya unabii inayofanana na ile ya maneno katika Habakuki 3:13. Yanaelekeza kwenye wokozi ambao Yehova atawapa mabaki watiwa mafuta wake katika pigano la Har–Magedoni.
◆ 29:5, 6 (NW)—Sauti ya Yehova inavunja-vunjaje mierezi?
Katika zaburi hii uwezo wa Yehova unakaziwa waziwazi sana kwa kufananisha sauti yake na radi. Radi inasafiri kutoka Lebanoni upande wa kaskazini mpaka kwenye majimbo yenye jangwa upande wa kusini, ikitia watu hofu inapoenda. (Mstari 9b) Upepo wayo unatikisa-tikisa mierezi ya Lebanoni na “Kuirusha-rusha kama ndama wa ng’ombe,” na umeme wayo unakata miti mingine, na ‘kuivunja-vunja.’ Vivyo hivyo, pepo za dhoruba ‘zinafanya jangwa lijinyonge-nyonge kwa maumivu makali’ (mstari 8), zikikusanya michanga ya jangwa hivi kwamba inaonekana ni kama inajinyonga-nyonga kwa maumivu makali.
◆ 33:6 (NW)—Ni nini ‘roho ya kinywa cha Yehova’?
Roho au pumzi, inayomaanishwa hapa ni roho takatifu ya Yehova, au kani ya utendaji. Kama vile maneno yetu na pumzi zinavyotoka katika vinywa vyetu wakati ule ule mmoja, ndivyo neno, au amri ya Yehova vinavyoambatanishwa hapa na pumzi yake, au roho. Mungu alitumia roho takatifu yake kwa kuumba jua, mwezi, na nyota, yaani, jeshi lote la mfano la mbingu zinazoonekana.—Linganisha Mwanzo 1:1,2.
Somo Kwetu Sisi: Katika Zaburi 26:5, Daudi alisema alikuwa amechukia kusanyiko la watenda mabaya, Mashahidi wa Yehova leo vivyo hivyo wanaepuka mashirika ya watenda maovu. (1 Wakorintho 15:33) Kama vile Daudi alivyoonyesha kupendezwa sana na makao ya nyumba ya Yehova, Wakristo hawa wa kweli wanafurahia kushirikiana katika tengenezo la Yehova.—Zaburi 26:6-8; 122:1.
“Na Atukuzwe [Yehova]”
Soma Zaburi 35 hadi 41. Ya kutokeza katika fungu hili ni Zaburi 36, inayotambulisha Yehova kuwa Chanzo cha uhai, na Zaburi 37, inayotuhakikishia kwamba wale wanaofundishika watapata thawabu baadaye. Ya kuangaliwa hasa ni Zaburi 40 ambayo ina semi za kiunabii. kuhusu Yesu Kristo.
◆ 35:19 (NW)—Kwa nini adui za Daudi ‘wangemkonyezea jicho’?
Maneno ya Kiebrania yanawaita kwa uhalisi “adui zangu [katika] uwongo.” Yaani, uchukivu wao ulitokana na makusudio machafu. Daudi hakuwa amefanya jambo lo lote la kumstahilisha uadui huo, na alisali kwamba isiwezekane wapate nafasi yo yote ya kufurahi au kushangilia kwa sababu yake. (Mstari 19b) Kwa hiyo aliomba kwamba adui zake wenye kijicho wasipate sababu yo yote ya ‘kumkonyezea jicho,’ kwa maana kukonyeza kwa aina hiyo kungemaanisha wangekuwa wakimsimanga kwa sababu ya hila zao kufanikiwa. (Mithali 10:10; 16:29, 30) Yesu alitaja maneno ya mstari huo na kuutumia kuhusu wale waliomchukia.—Yohana 15:24, 25.
◆ 36:3—Je! kuna wakati waovu hao walipokuwa na akili?
Dokezo hasa ni kwamba kulikuwa na badiliko katika mwenendo wa mtu huyo na kwa hiyo ameacha kuwa kama alivyokuwa akidai kuwa. Pengine wakati mmoja alikuwa akionyesha hekima na kufanya mambo ambayo yalikuwa mema. Lakini sasa alikuwa ameacha hayo yote nyuma, na kuwa mwasi-imani. MfaIme Sauli ni mmoja aliyeacha mwendo wa hekima, na akamwonyesha Daudi uchukivu. (1 Samweli, sura 18) Wanafunzi wengine wa Biblia hata wanafikiria kwamba Daudi alitumia Zaburi 36 kwa kurejea mambo yaliyohusu Sauli.
◆ 40:6—Ni nini maana ya maneno, ‘Masikio yangu uliyazibua’?
Hii ingeweza kuwa na maana ya kwamba Yehova alifanya masikio ya Daudi yaelekezwe kwenye mielekezo ya Mungu, au hata kwamba Yehova aliumba masikio ambayo Daudi angetumia asikie amri Zake. Jambo linalofaa kuangaliwa ni kwamba, katika Septuagint maneno hayo yametafsiriwa hivi: “Ulinitayarishia mwili.” Hata tafsiri hiyo iwe imetokana na chanzo gani, ina wazo lile lile la msingi kama lile la Kiebrania. Yaani, inakazia uhitaji wa kutii. (Linganisha 1 Samweli 15:22; Hosea 6:6) Paulo alitumia mstari huo kuhusu Yesu Kristo. (Waebrania 10:5-10) Kwa vile Paulo aliitumia fasiri iliyo katika Septuagint, sasa kifungu kile cha maneno kinachosema “ulinitayarishia mwili” ni kati ya “kila andiko, lenye pumzi ya Mungu.”—2 Timotheo 3:16.
Somo Kwetu Sisi: Zaburi 37 ina masomo mengi kwetu sisi tunaoishi katikati ya kizazi kiovu. Hata watenda mabaya wakisitawi, hatupaswi kuwaonea kijicho, na kujaribu kuwafuatisha. Bali, tunapaswa ‘tukae kimya mbele za Yehova,’ bila kutafuta makosa, lakini, tuwe watulivu tukimtumainia yeye achukue hatua kwa ajili yetu katika wakati wake mwenyewe.—Zaburi 37:5, 7.
Ndiyo, Zaburi zinatoa maneno mengi yenye kufariji na kutia nguvu. Zaburi hizo 41 za kwanza zimeonyesha-onyesha kwamba, hata hali zetu ziwe ngumu namna gani, Yehova hatatuacha kamwe. Kwa kweli, baada ya kuzisoma, tunapaswa kusukumwa kuitikia maneno yale yanayoimalizia Zaburi ya 41: “Na atukuzwe [Yehova], Mungu wa Israeli, tangu milele na hata milele. Amina na Amina.”