Je! Unakumbuka?
Je! wewe umeona kwamba matoleo ya hivi majuzi ya Mnara wa Mlinzi ni yenye mafaa? Basi ona kama unaweza kukumbuka mambo yafuatayo:
◻ kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba Biblia ni kitabu kwa ajili ya wanadamu wote?
Tangu mwanzo wayo, Biblia inatoa maoni yanayohusu ulimwengu wote inapotaja wakati ujao wa wanadamu. (Mwanzo 1:28) Kiwango chayo kinainuka juu ya mipaka yote ya ubaguzi wa rangi, utukuzo wa taifa, na kani nyingine zenye kuleta mgawanyiko zinazowakumba wanadamu. Inasema na watu wa mataifa yote na kuisema dunia kuwa kao moja kubwa la jamii nzima ya kibinadamu. (Matendo 17:26)—4/15, ukurasa 5.
◻ Yesu alimaanisha nini aliposema: “Ikiwa, basi, jicho lako ni rahisi, mwili mzima wako utakuwa mwangavu”? (Mathayo 6:22, NW)
Neno “rahisi” limetokana na neno la Kigiriki ambalo kwa msingi linamaanisha umoja wa akili au kujitoa kwa ajili ya kusudi moja. Kwa kufanya mradi wetu maishani uwe ni kutenda mapenzi ya Mungu, tutatafuta kuzitangaza habari njema tukufu juu ya Ufalme katika kila upande wa maisha zetu—5/1, kurasa 12, 13.
◻ Maana yake nini kwamba Yehova ni mweza yote na mjuzi wa yote?
Yehova alimwambia Abrahamu: “Mimi ni Mungu mwenye Nguvu Zote.” (Mwanzo 17:1, NW) Kwa kuwa ni mwenye nguvu zote—mweza-yote—Yehova anaweza kutumia uwezo wake ashinde kipingamizi cho chote kinachozuia kutimizwa kwa ahadi na makusudi yake. Pia Yehova anajua yote, ni mwenye hekima yote. Hivyo yeye anaweza kutangulia kuona jambo lo lote analotaka kutangulia kuona. Sifa hizo mbili zinafanya isiwezekane Yehova ashindwe. (Isaya 14:24)—5/15, ukurasa 4.
◻ Tunaweza kuonyeshaje unyenyekevu tunaposali hadharani kwa ajili ya wengine?
Tunaweza kuonyesha unyenyekevu kwa namna ya sauti yetu—tusisikike kamwe kana kwamba tunatumia maneno makubwa ya kujionyesha au kujifanya. Haitupasi kamwe tudai kwamba Yehova afanye mambo fulani. Bali, inatupasa tumwombe Yehova kwa bidii kupatana na mapenzi yake, na maneno yetu ni lazima sikuzote yawe yenye heshima na staha, tukitambua kwamba sisi wenyewe ni watu nduni. (Mathayo 6:5: Isaya 66:2) 5/15, kurasa 21,22.
◻ Mkristo anaweza kuendelezaje mwelekeo wa kutazamia mazuri akiwa chini ya mateso?
Haimpasi kamwe aruhusu akili yake ziendelee kufikiria mambo yasiofaa. Bali, anahitaji kutafakari juu ya mambo waliyotenda watumishi wengine waaminifu wa Yehova katika nyakati za majaribu. Wao walikuwa na imani kamili na uhakika katika Yehova, wakautumaini uwezo wake wa kuwafufua na kuwathawabisha. (Ufunuo 2:10) Vivyo hivyo, leo Mkristo mwenye kuteswa anaweza kulikumbuka wazi-wazi tumaini lake katika mfumo mpya wa Yehova wenye uadilifu. (Linganisha Waebrania 12:2.)—6/1, ukurasa 30.
◻ Ni katika jambo gani moja Hus na Wycliffe, na Lutheri walikubaliana?
Wote walikubali kwamba Neno la Mungu lilipasa kutangulizwa, hata kama wanadamu walikuwa na maoni gani. Wakristo wa kwanza walishiriki maoni ayo hayo yenye kutiwa nuru kwa sababu walikuwa wamefundishwa na Yesu Kristo mwenyewe. (Matendo 5:29; Yohana 17:17)—6/15, ukurasa 31.
◻ Je! rangi ya ngozi nyeusi ni matokeo ya laana ya kimungu iliyowekwa juu ya Kanaani na wazao wake?
Hapana. Jamii ya watu weusi haikutokana na Kanaani bali na Kushi na labda Putu. Hakuna laana iliyowekwa juu ya ye yote wa wajukuu hao wawili wa Noa. (Mwanzo 9:24,25; 10:1, 6)—7/1, ukurasa 4.
◻ Yesu alimaanisha nini aliponena juu ya kuchukia washiriki wa jamaa ya mtu mwenyewe na hata kujichukia mwenyewe? (Luka 14:26)
Yesu alimaanisha kwamba kwa kulinganishwa na upendo wa mtu kwa Mungu na kujitoa kwake kwa Kristo, uhusiano alio nao na watu wa ukoo wake ungeweza kuonekana kana kwamba ni uchukivu. (Linganisha Mathayo 12:46-50)—7/1, ukurasa 27.
◻ Ni kwa njia gani Yesu alikuwa “Bwana wa sabato,” kama inavyotajwa kwenye Mathayo 12:8?
Yesu alikuwa akimaanisha utawala wa Ufalme wake wenye amani wa miaka elfu moja. Utawala huo mkuu wa Sabato ya Kristo utakuwa wakati wa pumziko la kutokuwa na taabu na uonevu wote,—7/15, ukurasa 9.
◻ Kwa sababu gani si jambo la hekima mtoto kujiwekea miradi yake mwenyewe maishani?
Ujuzi wa watoto maishani ni mdogo mno isifae kujiwekea miradi yao wenyewe katika maisha. Wazazi wasipowasaidia kuweka miradi hiyo, mtu fulani atafanya hivyo—labda watoto shuleni au mshauri wa shule. Wazazi Wakristo wanaweza kuwasaidia kwa kuwaonyesha miradi inayopatana na uthamini wao wa mambo ya kiroho.—8/1, ukurasa 28.