Guadeloupe “Kisiwa cha Maji Mazuri”
GUADELOUPE nchi iliyo kilometa karibu 480 kusini-mashariki mwa Puerto Rico, ni kikundi cha visiwa kilicho karibu katikati ya ule mlolongo wa visiwa vya Lesser Antilles. Katika ramani, visiwa viwili vilivyo vikubwa vya nchi hiyo vinaonekana kama kipepeo aliyenyosha mabawa yake. Eneo la milima-milima la Basse-Terre, lenye volkeno isiotoa moto ya Soufriere, liko upande wa magharibi, na lile eneo la chini la Grande-Terre liko upande wa mashariki. Visiwa hivyo viwili vimetenganishwa na ule mfereji mwembamba wa Riviere Salee. Visiwa vingine vitano vidogo zaidi na vingine vilivyo vidogo hata zaidi ya hivyo vinajumlika kuwa wilaya ya ng’ambo yenye usimamizi wa Wafaransa.
Kabla ya Christopher Columbus kuivumbua nchi hii mwaka 1493 na kuipa jina la sasa la Guadeloupe, Wakaribu wenyeji waliiita Karukera—Kisiwa cha Maji Mazuri. Waliiita hivyo kwa kufikiria mvua nyingi na mimea ya kitropiki inayositawi sana katika visiwa hivyo. Leo, jina hilo linafaa hata zaidi kwa sababu ya maji mengi ya ukweli yanayowatiririkia wakaaji 328,000. Ingawa watu hao wenye adabu na wakaribishaji-wageni ni Wakatoliki hasa, wengi wao wanayakubali kwa hamu nyingi maji safi ya ukweli unaotoka katika Neno la Mungu, Biblia.
Maji ya Ukweli Yalianza Kutiririka
Mtiririko wa kwanza wa maji ya ukweli ulianza katika Gaudeloupe mwaka 1938, kabla tu ya kutokea Vita ya Ulimwengu ya Pili. Cyril Winston na jamaa yake walitoka kisiwa jirani cha Dominika wakaanza kuwahubiri habari njema wakaaji wa visiwa hivi. Baada ya muda mfupi watu 5 walianza kukutana kwa ukawaida, na kufikia Juni 1940, kundi la kwanza lilitengenezwa, likiwa na watu karibu 15 wenye kuhudhuria funzo la Kifaransa la Mnara wa Mlinzi kila juma.
Lakini, Vita ya Ulimwengu ya Pili ilileta mkazo mwingi kutokana na serikali yenye kuongozwa na Wajeremani katika Ufaransa. Wakati huo, vitabu vilivyosafirishwa kutoka Brooklyn viliteketezwa vyote kwa ujumla vilipofika bandarini, na mawasiliano pamoja na makao makuu katika Brooklyn yakakatizwa. Ndugu Winston akawa mgonjwa sana na kulazimika kurudi Dominika, akafa kule miezi mitatu baadaye. Sasa mtiririko wa maji ya ukweli ulipungua sana; ulikuwa wakati wenye magumu kwa kile kikundi kidogo cha Wakristo.
Baada ya vita, akina ndugu walirudia kazi yao kwa kadiri ambavyo wangeweza. Ili kufikia watu wengi iwezekanavyo, walijaribu kutoa hotuba za Biblia katika sehemu zenye watu wengi nyakati za jioni. Mhutubu alikuwa akitoa hotuba yake akiwa amesimama juu ya kitu kilichoinuka, huku watu wakiwa wamekusanyika kumzunguka katika duara. Ndugu mwingine angemmulikia mwangaza kwa kutumia mshumaa wa kinyumbani. Nyakati za jioni hizo za kitropiki zisizo na joto jingi, wapitaji na majirani walifurahia kusikiliza Neno la Mungu likizungumzwa peupe.
Wakati wa hotuba moja ya namna hiyo, kikundi cha vijana waskauti Wakatoliki kilitokea kwa ghafula. Kwa kumzunguka mhutubu, walianza kupuliza tarumbeta zao na kupiga-piga mabirika makubwa, wakijaribu kuizima sauti ya mhutubu. Kwa kutambua lililokuwa likifanyika, mhutubu alikuwa akiendelea kwa utulivu na hotuba yake lakini akitoa ishara tu na kufungua-fungua midomo bila kusema. Baada ya muda mfupi, maskauti wale walichoka wakaenda zao kwa kuishiwa na pumzi. Kisha ndugu yule aliendelea na hotuba yake kama ilivyopangwa.
Utiririkaji Unaharakishwa
Katika muda wa miaka iliyofuata, wamisionari kadha walipelekwa Guadeloupe wakasaidie kikundi kile kidogo cha wahubiri wenye bidii wa kule. Hapo kwanza, hawakuweza kufanya mengi kwa sababu ya kizuizi cha lugha. Lakini, katika miaka ya katikati ya 1950 wamisionari wenye kusema Kifaransa walianza kufika, na kazi ikasonga mbele.
Lakini, kwa sababu ya upinzani mkali wa kidini, wengi waliokubali ukweli wa Biblia walilazimika kuwa na msimamo wenye azimio lisilo la kawaida. Ndivyo ilivyokuwa kwa mwanamke mmoja aliyelazimika kubatizwa kwa siri baharini wakati wa giza saa kumi na moja alfajiri na mapema. Mwanamke huyo na mumeye walianza kujifunza Biblia pamoja. Lakini majirani walipoanza kuwatesa, mumeye aliacha kujifunza kwa kuogopa kwamba wao hawangeendelea kuwa wanunuzi katika kiduka cha jamaa yake. Mwanamke huyo alizidi kujifunza na kufanya maendeleo mazuri sana. Lakini, baada ya muda mfupi mkazo uliongezeka sana hata mumeye akatisha kumwua.
Jioni moja, alikuta kisu kimefichwa chini ya mto wa mumeye, naye akaona kwamba kwa sababu ya mwelekeo wa mumeye, hakukuwa na shaka juu ya makusudi aliyokuwa nayo. Kwa kuhisi kwamba uhai wake ulikuwa hatarini, alikimbilia nyumba ya jamaa Mashahidi, akitembea karibu kilometa 16 kupitia msitu wa kitropiki na katikati ya migomba. Alipokuwa huko akijificha mumeye, aliomba abatizwe, akisema: “Ikiwa nitalazimika kukabili kifo kwa sababu ya imani yangu, nataka nihesabiwe kuwa mmoja wa watu wa Yehova!” Baadaye dada huyo mwaminifu alianza utumishi wa wakati wote na amekuwa painia wa pekee kwa miaka 24 iliyopita. Ingawa amepoteza jamaa yake ya kimwili kwa sababu ya imani, amepata jamaa kubwa ya kiroho, kama ilivyoahidiwa na Yesu kwenye Mathayo 19:29. Amesaidia watu wapatao 35 wajitoe wakfu na kubatizwa.
Maji ya ukweli yanasambaa kwa njia zisizotazamiwa. Wanaume wawili Wakatoliki katika kijiji cha mbali kaskazini walinunua Biblia. Wakaanza kuisoma kila siku na wakawa wakitafuta mtu wa kuwasaidia waielewe. Jirani mmoja akawaambia kwamba angeweza kumpasha habari binamu yake “Myehova” naye angefurahi kuwasaidia. Hiyo ilikuwa ndiyo mara ya kwanza watu hao kusikia juu ya jina la Mungu.
Binamu huyo aliwapelekea nakala za gazeti Amkeni!, wakafurahia kuzisoma wao wenyewe lakini pia wakagawia wengine kijijini. Walipopata habari kwamba kusanyiko lingefanywa karibu na Pointe-a-Pitre, walilihudhuria wakamwambia mwangalizi wa mzunguko: “Sisi tumekuja kwenye kusanyiko hili, na tungependa kubatizwa.” Bila shaka, walikaribishwa kwa uchangamfu lakini wakasaidiwa pia kufahamu kwamba ni lazima hatua fulani zichukuliwe na mabadiliko yafanywe kabla ya kustahili ubatizo. Kwa hiyo mipango ilifanywa kuwasaidia, nao wakabatizwa kwenye mkusanyiko uliofuata.
Mambo yaliyoonwa kama hayo yaliwaletea akina ndugu furaha kubwa na kitia-moyo kikubwa. Maji ya ukweli yaliendelea kutiririka, na kufikia mwaka 1960, kukawa na jumla ya watangazaji Ufalme 251 katika Guadeloupe.
Tatizo Lakabiliwa
Tatizo kubwa katika kisiwa hiki kidogo limekuwa kupata mahali panapotosha kufanyia makusanyiko. Kwa muda mrefu vilikuwako viwanja viwili tu. Akina ndugu walitamani sana kufanya makusanyiko katika sehemu zote za kisiwa ili maji ya ukweli yaweze kufikia watu wengi zaidi.
Mwishowe, akina ndugu waliamua kujenga mahali pao wenyewe. Walijitayarishia muundo wa jengo lenye kubebeka la chuma cha pua na mabati, lenye nafasi ya watu 700, na wakachanga pesa za kutosha kulijenga. Walipotumia “jumba la makusanyiko” hilo lao lenyewe kwa mara ya kwanza katika Basse Terre katika Januari 1966, mkutano wenye shauku wa watu 907 ulikuja. Jumba hilo lilikuwa dogo mno tangu mwanzoni!
Kwa kuwa na uandalizi mpya huo, imewezekana kufanya makusanyiko hata katika visiwa fulani vya kando-kando. Jambo hilo limeongeza sana utoaji wa maji ya ukweli katika maeneo mengi. Wazia jinsi walivyosisimuka wenyeji wa Grand-Bourg, mji mdogo wenye watu karibu 6,000 katika kisiwa cha Marie Galante, ‘walipovamiwa’ na mashua tatu zenye wakusanyikaji elfu moja wakiwa na mizigo yao na vifaa vingine. Lilikuwa jambo lisilopata kuonekana tena—mlolongo mrefu wa watu wakipiga miguu kutoka gatini kupitia mjini wakielekea kusanyikoni. Huo ukawa ni ushuhuda mzuri sana kwa wenyeji, na leo kuna makundi matatu yenye bidii katika kisiwa hicho.
Katika muda wa miaka mingi, “jumba” hilo lilikuwa limepanuliwa mara nyingi. Mwishowe, likawa jengo la tani 30 lenye kuchukua meta za mraba 3,000, likiwa na nafasi ya kukaa watu 5,000. Kwa wazi, ilikuwa kazi kubwa sana kusafirisha, kusimamisha, na kuviondoa tena vifaa vyote kila wakati kusanyiko lilipofanywa. Jambo lililoongeza tatizo ni kwamba, ilizidi kuwa vigumu kupata mahali panapofaa pa kuliweka jumba hilo lenye kubebeka kwa sababu majengo yalichukua upesi nafasi ya ardhi iliyokuwa wazi. Ilionekana kwamba utatuzi peke yake ulikuwa kupata mahali pa kudumu pa kuliweka “jumba” hilo.
Kwa mara nyingine Yehova akatoa uandalizi kwa mahitaji ya akina ndugu. Kilipatikana mahali panapofaa kiwanja cha meta za mraba 50,000. Kilinunuliwa mwaka 1979 kwa michango ya ukarimu kutoka makundi yote visiwani. Pakawa mahali pakuu pa kudumu pa ibada ya kweli Guadeloupe.
Mtiririko Wenye Kuongezeka Daima wa Maji ya Ukweli
Kule nyuma mwaka 1954 wakati tawi lilipoanzishwa mara ya kwanza katika Guadeloupe, walikuwako wahubiri wa Ufalme 128. Sasa hesabu hiyo imeongezeka kufikia zaidi ya 4,500. Hiyo ni kuonyesha kwamba karibu moja kati ya kila watu 72 katika Guadeloupe ni shahidi wa Yehova. Na katika Pointe-a-Pitre, ambao ndio mji mkuu, kuna shahidi mmoja kati ya kila watu 29—bila shaka hesabu hiyo ikiwa ni moja wa uwiano ulio mzuri zaidi ulimwenguni!
Waaminifu hao wamekuwa na shughuli nyingi wakitoa maji ya ukweli, wakiongoza mafunzo ya nyumbani ya Biblia zaidi ya 7,300 kwa watu wenye kupendezwa katika sehemu zote za eneo. Jitihada zao zilibarikiwa wakati watu 12,553 walipokusanyika mwaka 1986 kukumbuka kifo cha Bwana Yesu Kristo. Kwa kweli, akina ndugu katika Guadeloupe wanahisi kwamba Yehova Mungu ‘anatikisa’ visiwa vyao ili kukusanya pamoja ‘vitu vinavyotamanika’.—Hagai 2:7, NW.
Kile “kisiwa cha maji mazuri” kinaendelea kuwa kizuri zaidi ya wakati mwingineo wote kwa njia ya kiroho. Watu wengi wanauitikia mwito huu: “Njoo!” na wanayatwaa “maji ya uzima bure.”—Ufunuo 22:17.
[Ramani katika ukurasa wa 27]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
GUADELOUPE
GRANDE TERRE
Pointe-à-Pitre
Soufrière
Rivière Salée
BASSE-TERRE
MARIE GALANTE
Grand Bourg