Visiwa Marquesas na Tuamotus Vyakaribishwa “Kuishi Milele Katika Paradiso”
BAADA ya kuruka kwa ndege karibu kilometa 1,450 kuelekea kaskazini-mashariki kutoka Tahiti, mke wangu na mimi tulifika Nuku Hiva, kisiwa kilicho kikubwa zaidi kati ya Visiwa. Marquesas. Katika ramani, visiwa hivyo vinaonekana kama vidoa vidogo katika Bahari Kuu ya Pasifiki Kusini. Lakini tulistaajabishwa na uzuri ulio katika visiwa hivyo vyenye mawe-mawe.
Vingi vya visiwa hivyo ambavyo kwa ujumla vinaitwa Marquesas vina vilele vilivyoinuka mpaka mawinguni na vina miamba iliyochongoka sana inayoning’inia juu kama marinda yaliyokusanywa pamoja. Yale mabonde yenye kina kirefu ambayo yana rutuba, yenye kufunikwa na minazi na majani-majani mengine yaliyositawi sana, yanapanuka yanapofika kwenye bahari huku na kuonekana kuwa ghuba zenye kustarehesha sana. Lakini, yale mawimbi na mikondo ya maji yenye nguvu inayovizunguka visiwa, na ukosefu wa miamba-tumbawe, inafanya iwe vigumu kurudisha mashua kwenye nchi kavu. Yale matumbawe, yaliyozunguka visehemu-sehemu vya maji katika visiwa Tuamotus hayaonekani vizuri yanapokuwa mbali, na jambo hilo lilitusaidia tufahamu sababu iliyowafanya mabaharia wa zamani waviite Visiwa vya Chini au Kikundi cha Visiwa Vidogo Hatari.
Sisi tukaja kuwatolea wanavisiwa hao mwaliko unaofanana na kile kichwa cha msaada wa kujifunzia Biblia wenye rangi ya kupendeza, Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Katika kisiwa Nuku Hiva, tulipanda meli ya shehena inayoitwa Araroa ili tufunge safari ya siku 21 yenye umbali wa kilometa 4,000 kwa kupitia visiwa Marquesas na Tuamotus. Meli ilipokuwa ikisimama sehemu mbalimbali ili kupakia na kupakua shehena, sisi tukawa tukitolea watu ujumbe wetu.
Njia Rahisi ya Maisha ya Wanavisiwa
Ingawa hivyo, huenda wewe ukataka kujua watu tuliokuta walikuwa namna gani. Wakaaji wengi wa Marquesas wanaishi katika vijiji vidogo kuzunguka zile ghuba ndogo-ndogo au kando-kando ya mto. Vijiji vyao vinakuwa vya watu ambao hesabu yao ni kuanzia jamaa mbili au tatu hivi kufikia kama wakaaji mia kadha. Jamaa zilizo nyingi ni kubwa, zikiwa na watoto 8 kufikia 10, na nyingine zina watoto wanaofika 18 au 20. Maisha zao ni rahisi lakini si za ustaarabu. Wao wanakula vitu wanavyopata katika ile bahari kuu, kuongezea pindi kwa pindi, nguruwe na kuku wanaowafuga nyumbani. Wanaingia mwituni pia kuwinda mbuzi-mwitu wa milimani au kuzingira farasi-mwitu, kisha wanawafuga na kuwatumia kama wanyama wa kukokotea mizigo. Minazi ambayo ni tele inawapa mbata (nyama kavu ya nazi yanakokamuliwa mafuta ya kutengeneza sabuni na vitu vingine vya matumizi). Mbata ndiyo zao kubwa la uchumi wa visiwa hivyo, lakini wanakuwa na mapato fulani kutokana na vitu wanavyochonga kwa kutumia miti, tapa (vitambaa vyenye mapambo vinavyotengenezwa kutokana na maganda ya miti), na piere (ndizi zilizokaushwa).
Wakaaji wa Marquesas walikuwa wakila wanadamu wenzao wakati mmoja na kutolea miungu yao ya tiki dhabihu za kibinadamu. Leo, walio wengi kati ya watu hao ni Wakatoliki. Wanapamba nyumba zao kwa mifano na taswira za Mariamu na za Yesu. Inafaa kuangaliwa kwamba njia ya kuingilia makao ya askofu Mkatoliki katika kisiwa Nuku Hiva imepangwa mstari wa taswira za tiki. Katika visiwa Tuamotus, maisha ya kidini yanaongozwa na Wamormoni, Wakatoliki, na Reformed Church la Latter-day Saints, kanisa linaloitwa huko Sanitos.
Wanavisiwa wanasema lugha ya Marquesas, lakini wanafahamu Kifaransa na Kitahiti pia. Njia ya maisha yao inafanana sana na ya Wapolinesia wote—wanaoishi siku moja-moja kulingana na mwendo wa polepole wa maisha ya visiwani. Kwa sababu meli hazitembelei visiwa hivyo kwa ukawaida sana, watu wa kule wamejifunza ustadi wa kungoja kwa subira. Nguvu za umeme zililetwa Januari 1979, na kwa sababu sasa televisheni zimefika, wanavisiwa wamezidi kujua mambo yanayotukia katika ulimwengu mzima.
Katika Kisiwa Nuku Hiva
Kisiwa Nuku Hiva, chenye wakaaji 1,800, ndicho kituo cha usimamizi wa mambo ya Visiwa Marquesas. Ikulu (nyumba ya serikali), bandari kuu, na makao ya askofu yamo katika ghuba ndogo ya Taiohae, mahali ambapo sisi tulianzia.
Hakukuwa na kengele za milangoni, sisi tulikuwa tukiita kwa kupaaza sauti tu na kusema hou-hou. Kama mtu angejibu, tungesema, Kao-ha! (“Jambo!”) Tukiwa na tabasamu ya urafiki kisha tunaeleza sababu ya ziara yetu. Wengi wa wanavisiwa walikikubali kitabu kwa hamu nyingi na kusema: “Asanteni sana kwa kuja. Sisi hatukuwa kamwe na kitu kama hiki cha kutusaidia tufahamu Neno la Mungu.” Wao wana Biblia ya Kikatoliki katika lugha ya Tahiti na vitatu kati ya vile vitabu vya Injili katika lugha ya Marquesas.
Watu fulani waliokubali toleo letu walituomba kwa moyo mweupe tutembelee wengine. Kwa mfano, kijana mmoja mwanamume alimhimiza mke wangu amfuate akisema, “Nenda kule nyuma! Nenda kule nyuma!” Kama asingalinyosha kidole kuonyesha ni wapi, mke wangu angalikosa kuiendea nyumba ya mchonga sanamu za mawe na miti, aliyekuja kukithamini sana kitabu hicho chenye mafundisho.
Katika Hakaui, zilikuwako jamaa mbili tu, zenye kuishi ng’ambo hii na ng’ambo ile nyingine ya mlango mwembamba wa mto. Tulipofika, jamaa ya kwanza ilionekana kuwa yenye shughuli sana. Kwa hiyo, kwa kusaidiwa na mabaharia wenye fadhili, tukavuka mto kwa motaboti ili tuiendee jamaa ile nyingine. Tulipokuwa tukikaribia, tukaona wanawake wawili wameketi katikati ya nguruwe waliokuwa wakitanga-tanga kwa kuizunguka-zunguka ile nyumba—tuliona maisha ya hali ya chini kweli kweli. Hata hivyo, tulipowaonyesha kitabu, wao walitoa kwa furaha kiasi kidogo walichokuwa nacho ili wapate kitabu kimoja. Tukalazimika kumfikiria yule mjane maskini aliyetajwa katika Luka 21:2-4 aliyetoa hekaluni kiasi chote alichokuwa nacho.
Mahali pengine tulipotua ni Taipivai, katika pwani ya mashariki kisiwa Nuku Hiva, chenye kutajwa sana na kitabu kilichoandikwa na Herman Melville kinachoitwa Typee. Hilo ni bonde la kupendeza lenye kina kirefu, lililosongamana minazi. Saa kumi na mbili ya asubuhi, tulisafiri upesi mtoni tukiwa katika motaboti yetu, huku yale maji yenye kung’aa kama kioo yakionyesha vivuli vya majani ya minazi na mwangaza wa kwanza wa mapambazuko. Tukaweza kuona nyumba kadha kati ya miti hiyo.
“Tutakaa hapa muda gani?” Nikaambiwa kwamba lori lililosafirisha magunia ya mbata lilikuwa limeharibika. Kwa hiyo, tukifanya haraka, tungepata wakati wa kusafiri kwa kupanda farasi katika eneo lote hilo mpaka kwenye ncha ya mbali zaidi ya bonde, ambako poromoko la maji lenye kuvutia sana lilianguka mpaka kwenye madole matano. Karibu jamaa kumi na mbili ziliitikia vizuri “ushambulizi wetu wa haraka.”
Kuviendea Visiwa Vile Vingine
Kisiwa Ua Huka kiko kilometa karibu 40 mashariki mwa Nuku Hiva. Kisiwa hicho ni kidogo zaidi ya kile kingine, hakina rutuba nyingi kama kile kingine, na ni chenye milima-milima sana. Saa kumi na mbili tulianza tena safari ya kuelekea ufuoni. Tulipofika kwenye ule ufuo wenye mawe-mawe tukajikaza-kaza kupanda barabara yenye miamba, na baada ya kutembea kwa miguu mwendo mrefu wa saa moja, tukafikia Hane, kile kijiji kikuu. Kama kawaida, kanisa la huko ndilo lililoonekana zaidi katika mazingira ya kisiwa hicho. Nguvu zalo za kuvuta watu zilikuwa zimeongezeka hivi majuzi kwa sababu ya kikundi cha kidini chenye shughuli ya ukarisma (imani ya kupokea vipawa vya roho). Lakini kijana mmoja mwanamume mwenye kuishi kule alihangaishwa na badiliko hatari la matukio ya ulimwengu naye akakubali kwa hamu nyingi “mwaliko” wetu, ule ujumbe unaohusu kuishi katika dunia-paradiso.
Mahali pale pengine tulipotua palikuwa kisiwa cha Ua Pu. Mara tu tulipofika tulivutiwa na vilele vya meta 1,200 vya miamba myeusi, iliyoinuka mawinguni kwa kuchongoka sana kama misumari. Kwa kweli hiyo ilikuwa matope ya volkano yaliyofanywa yakawa magumu. Katika kisiwa hicho kulikuwa na vijiji vitano vya kutembelea. “Mwaliko” wetu ulipokewa na watu wenye tabasamu pana na macho yenye kung’aa. Tuliyasikia mara kwa mara maneno, “Mea kana hau!” (“Ni kizuri sana!”) Kitabu hicho kiliwavutia sana wengi wa wanavijiji hata wakatoa shukrani wakisisitiza kwamba wangeshindilia katika mifuko yetu ya kubeba mgongoni makombe na matunda—malimau, maembe, machungwa, na mabalungi. Katika Haakuti, ambacho ni kijiji kilichojengwa juu katika ukingo wa mwamba mrefu, tulikuta mwanamke mmoja na binti yake nao wakawa na shauku nyingi sana juu ya mambo waliyosikia hata wakateremka umbali wote ule mpaka mahali pa kuwekea mashua ili waambie kila mtu kule asikilize ujumbe wetu na kukichukua kitabu kile kizuri sana.
Tulipofika kwenye kijiji kile kikuu, Hakahau, tulihangaikia jinsi ya kuwafikia wakaaji wale zaidi ya elfu moja katika muda mfupi wa namna hiyo. Mioyo yetu ilitulia sana wakati, mwanamume mmoja, alifurahishwa sana na ujumbe wetu, alipotutolea gari lake tuweze kulitumia: “Mimi naweza kuwapeleka ko kote mnakotaka kwenda.” Miaka michache kabla ya hapo, padri wa mahali pale alikusanya vitabu vyote ambavyo Mashahidi wa Yehova walikuwa wameacha akaviteketeza kwa moto. Watu walikuwa wameogopeshwa na jambo hilo. Lakini ujumbe wetu ukawa wa kuwavutia sana hata jamaa kumi na mbili zikaondolea mbali hali yao ya kuogopa wanadamu na kukubali kitabu tulicholeta.
Hiva Oa, kisiwa kilichofuata katika safari yetu, ndicho kilicho na rutuba na majani-majani yenye kusitawi zaidi kati ya visiwa vyote vya Marquesas. Hicho kilipata kujulikana sana kwa sababu ya michoro ya kupendeza na kuvutia iliyofanywa na Paul Gauguin. Yeye alitumia miaka yake ya mwisho katika Atuona, ambako sisi tulisimamisha mashua yetu. Ulizo la kawaida analoulizwa mgeni ni: “Je! wewe umepata kwenda kuona tiki?” Lile jiwe tiki la meta 2.4 lililoko mwisho mwingine wa ghuba hiyo ndogo ndilo lililo kubwa zaidi katika Polinesia ya Wafaransa. Sisi tukajibu hivi kwa fadhili: “Jiwe hilo lina macho lakini haliwezi kuona, lina kinywa lakini haliwezi kusema. Kwa kuwa sisi tupo hapa kwa muda mfupi tu, tunataka kusema na watu walio hai na kuwaonyesha kitu cha kupendeza.” Bibi mmoja aliona shauku sana juu ya toleo hata akamtia moyo rafiki yake akichukue kitabu. Hata alimkopesha rafiki yake huyo pesa za kukinunua. Bibi mwingine alitangaza hivi: “Sasa nimeanza kufahama kwamba kusoma Biblia ni jambo la maana kuliko kwenda kanisani kusali kila jioni.”
Giza lilipoanza kuingia tulikuwa katika gati ya Hanaiapa tukiongea na wengine wa watu wa kule kwa kutumia taa ya karabai. Maongezi yetu yakaingilia ile habari ya moto wa mateso. “Tuseme kama ungekuwa na mtoto mbaya sana. Je! ungewasha moto umtupe ndani?” sisi tukawauliza. “Hapana” wao wakajibu. “Basi, je! Mungu angefanya watoto wake wateseke milele katika moto.” Wanawake wanne na mwanamume mmoja walipendezwa sana na “mwaliko” wenye upendo wa Mungu wa kuishi katika dunia ambapo “asiye haki hatakuwapo” kwa sababu atakuwa ameharibiwa milele, wala si kuteswa milele.—Zaburi 37:10.
Kutoka Hiva Oa, ilichukua hatua chache tu halafu tukafikia kisiwa kidogo cha Tahuata. Baharia mmoja akifanya mchezo kidogo alituambia kwamba muda usiopita miaka mia moja kule nyuma weupe fulani waliliwa na wenyeji wa hapa. Ingawa hivyo, sisi tuliwatolea tu maongezi yenye kupendeza. Mwanamume mwenye kuongoza kile kikundi cha ukarisma (imani ya kuingiwa na vipawa vya roho) katika kijiji kile hakutaka kuchukua kitabu lakini akasisitiza tukubali bilauri ya maji kutoka kwake. “Maji haya niliyowapa ninyi,” yeye akasema, akitumia vibaya maneno ya Yesu kwenye Yohana 4:14, “ninyi hamtaona kiu tena kamwe, bali haya yatakuwa chemchemi ya maji yenye kububujika ndani yenu.” Kwa kumshukuru, sisi tukamjibu: “maji haya ni maji tu, nasi tunayakubali kwa shukrani. Lakini je! wewe unayakataa maji yenye kutoa uzima na chakula cha kiroho ambacho tunakualika ukile?” Kwa kuguswa moyo na maneno hayo, akachukua vitabu kadha. Baadaye, tulipokuwa pale mahali pa kuwekea mashua, watu fulani walianza kudhihaki wakisema: “Hata kuna mtu aliyekubali toleo lenu?” Hata hivyo mkuu wa wafanya kazi pale akaomba akione kitabu kile na, pale pale mbele ya kila mtu akaamua kukichukua. Lo, wote walishangaa kama nini kujua kwamba wengine, pia, walikuwa wamekubali toleo letu!
Kituo chetu cha mwisho katika visiwa vya Marquesas kilikuwa kisiwa cha kusini kabisa, Fatu Hiva. Kilikuwa kati ya vile vya kwanza kuvumbuliwa mwaka 1595, na Mhispania Alvaro de Mendana de Neyra, ambaye aliviita visiwa hivyo jina la kuheshimu mke wa makamu wa mfalme wa Peru—Las Marquesa de Mendoza. Fatu Hiva ni kisiwa cha kupendeza sana. Katika kile kijiji kikuu, Omoa, tulikuta jamaa moja iliyoonyesha kupendeza kwingi. Tuliposonga mbele kwenye bonde, mama yule alitoka nje akakusanye rafiki zake pamoja, hivi kwamba tuliporudi wote walikuwa wakitungoja kwa kutabasamu. Walitaka vitabu tulivyokuwa navyo ili wajifunze angalau jambo fulani kuhusu Neno la Mungu katika mikutano ya jioni ya kujifunza Biblia. Kufikia wakati tuliporudi kwenye ile sehemu ya kuwekea mashua, mmoja wa mifuko yetu ya kubeba mgongoni ulikuwa mtupu, na ule mwingine ulijawa na machungwa na malimau.
Kwenda Kwenye Visiwa Tuamotus
Baada ya kutwa moja na mausiku mawili ya kusafiri baharini kuelekea kusini-magharibi, tulifikia kisiwa-tumbawe cha Pukapuka katika visiwa vya Tuamotus. Mipango ya pekee ilifanywa ili ile mashua Araroa isimame kwenye visiwa-tumbawe viwili kila siku. Kufanya hivyo kulitutolea nafasi ya kufikia vingine vya visiwa-tumbawe ambavyo tusingaliweza kuvifikia kama tusingalitumia njia hiyo.
Kati ya Wapomotu elfu moja walio katika visiwa hivyo, jamaa 30 ziliukubali kwa furaha “mwaliko” wetu. Katika nyumba moja ya hali ya chini iliyo katikati ya minazi, mwanamke mmoja alifanya haraka ya kuuza madafu yake ili anunue nakala kadha kabla hatujaondoka. Ni shida kwetu kuisahau jamaa hiyo, ambayo ilisisitiza pia kututolea samaki wakubwa waliokaushwa wenye kuning’inia chini ya paa iliyoezekwa kwa madebe ya nyumba yao.
Mambo ya Kupendeza Sana Tunayokumbuka
Kulikuwa na nyuso nyingine nyingi sana zenye furaha zitakazobaki katika kumbukumbu zetu, nasi tunamtumaini Yehova awatunze watu hao. Sisi tunafurahi sana kwamba tulifunga safari hiyo kwenda kwenye visiwa vya Marquesas na vya Tuamotus, tukajionea kwa macho yetu wenyewe matokeo yenye nguvu nyingi ya ule “mwaliko” unaosema: “Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani”!—Imechangwa.
[Ramani katika ukurasa wa 25]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Visiwa Marquesas
Nuku Hiva
Taiohae
Ua Huka
Ua Pu
Hiva Oa
Atuona
Tahuata
Fatu Hiva
Omoa