“Jikusanyeni Pamoja”
YEREMIA alisema juu ya maneno yaliyoandikwa juu, huku msiba ukitisha kupata Yerusalemu na Yuda ya kale. Lilikuwa jambo la haraka kwamba waabudu wa kweli wa Yehova wenye kutubu wakusanywe ili wapate wokovu. Vile vile leo, karibu Jumuiya ya Wakristo yenye kuasi imani iangamie katika “uharibifu mkuu,” pamoja na milki nzima ya ulimwengu ya dini ya uwongo. Ingawa miaka imesonga sana tangu 1914, wakati ambao viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo waliunga mkono kabisa umwagaji mwingi wa damu wa Vita ya Ulimwengu wa Kwanza, “hasira inayowaka ya Yehova haijageuka kurudi nyuma” kama vile haikugeuka wakati wa kipindi cha wakati unaoweza kulinganishwa na huu kilichohusu tawala za wafalme wa Yuda kuanzia Manase mwenye hatia ya damu mpaka Zedekia asiye na imani. Ni lazima wanyenyekevu wa dunia wamtafute Yehova sasa ili waokoke.—Yeremia 4:5-8; 2 Wafalme 24:3,4; Sefania 2:2,3, NW.
Onyo la kisasa limetolewaje? Gazeti unalosoma sasa limekuwa chombo kimoja chenye matokeo mazuri. Tangu 1879 jarida hili limeendelea tu kuvuta fikira za watu, kama mlinzi aliye juu ya mnara wa ulinzi, kwenye anguko linalokaribia la dini ya uwongo, iliyofananishwa na Babuloni, na pia kwenye Utawala wa Kristo wa Mileani wenye amani ambao utafuata. (Isaya 21:6-12; Ufunuo20:2, 3; 21:1-4) Kuanzia toleo la kwanza la nakala 6,000 katika Kiingereza, jarida hili limepanuka mpaka Mnara wa Mlinzi—Unaotangaza Ufalme wa Yehova ukawa leo unafurahia mwenezo wa duniani pote wa nakala 12,315,000 katika lugha 103. Tena, umbo la jarida lenyewe limeongezewa maendeleo katika muda wa miaka iliyopita. Sasa linapigwa chapa kwa rangi nne katika lugha 21, lakini chapa nyingine zinatokea pia kwa namna yenye kuvutia, kama inavyoistahili kazi muhimu ya gazeti lenyewe.
Utokezaji gazeti hili unapoendelea kuongezeka, imehitajiwa kabisa kugawa jukumu la upigaji chapa, hivi kwamba sasa kazi hiyo inashughulikiwa na viwanda vinavyoendeshwa na Sosaiti katika matawi 35 nje ya United States. Zaidi, kuanzia Januari 1987, chapa za gazeti-jenzi letu Amkeni! (kwa Kiingereza) linalopigwa chapa katika United States, Uingereza, Kanada, Ufini, Ujeremani, Italia, na Japani zitatokea zote katika rangi nne. Katika United States jambo hilo limewezeshwa na kusimamishwa kwa mashine tatu za rotari zenye mwendo wa kasi aina ya “MAN-Roland,” za kuchapia magazeti, kwenye kiwanda cha Mashamba ya Mnara wa Mlinzi kule Wallkill, New York.
Tawi la Sosaiti katika Japani linatumia pia mashine tatu zenye kasi kutokeza Biblia, vitabu, na magazeti katika lugha kadha za Esia. Tena, tawi hilo limeunga mkono kwa ukarimu pia matawi ya Australia, Korea, na Afrika Kusini kwa kuyanufaisha na mashine za uchapaji wa rangi nne, hivi kwamba matawi hayo matatu yataanza pia uchapaji wa magazeti kwa rangi nne wakati huo.
Katika muda wa miaka iliyopita, matawi ya Sosaiti yamekuwa yakigawana rasilimali, huku tengenezo la makao makuu likitoa uongozi. Hivyo mengi yamesaidia kulingana na uhitaji, iwe ni katika kujenga au kupanua majengo ya matawi, kuyanufaisha kwa vifaa, au kuitolea pesa ile kazi iliyo ya maana zaidi ya kuhubiri shambani. Utaratibu huo wa “usawazishi,” unaofanywa uwezekane na michango ya ukarimu ya Mashahidi wa Yehova katika sehemu zote za dunia, umebarikiwa sana na Yehova.—2 Wakorintho 8:12-15, NW.
Unaweza kurejea kwenye ukurasa 2 wa gazeti hili upate habari juu ya kufanya andikisho ili uwe ukilipata.