Kuvitazama Visiwa vya Bahamas—Kupitia Macho ya Mhudumu Anayesafiri
VFIKIRIE visiwa vya Bahamas. Kuna wakati ambao maneno hayo yalinifanya niwazie-wazie kwamba mtu akiwa kule analala katika fuo za bahari zenye mchanga wa kupendeza sana chini ya minazi yenye kuwaya-waya kwa uanana au akiwa anaogelea katika maji safi kama kioo, yenye rangi ya samawati kijani. Kwa kweli, kwa maelfu ya walikizaji wanaotembelea visiwa vya Bahamas kila mwezi, maono kama hayo yamekuwa jambo la kweli. Na si ajabu kwamba hali ya hewa katika visiwa hivyo vyenye hali za tropiki inafurahika, ikiwa na joto la wastani ya digrii 70 Farenhaiti (digrii 21 Selsio) Katika majira ya baridi na digrii 85 Farenhaiti (digrii 29 Selsio) katika kiangazi.
Ingawa hivyo, sasa visiwa vya Bahamas vinamaanisha mengi zaidi kwangu kuliko kujilaza tu nipate joto la jua la tropiki nikiwa mlikizaji. Visiwa hivyo vimekuwa mgawo wangu nikiwa mhudumu anayesafiri wa Mashahidi wa Yehova. Njoo uende nami uvione visiwa vya Bahamas kupitia macho yangu.
Vile Visiwa vya Nje-nje
Ni visiwa na vijisiwa karibu 20 tu kati ya vile 700 vinavyokaliwa na watu, walio wengi wa wakaaji wa Bahamas wanaishi katika mji mkuu wa Nassau katika kisiwa cha New Providence. Nassau ni kisiwa kinachojulikana kuwa kibandari kinachotembelewa na meli zinazopita kasi katika bahari kuu nacho kina hoteli kubwa kadha za kutumiwa na walikizaji. Labda wewe umekaa katika moja yazo. Lakini je! umepata kutalii visiwa vile vingine?
Hesabu kubwa ya wakaaji wa Bahamas wanaishi katika vile Visiwa vya Nje nje, ambavyo pia vinaitwa Visiwa Jamaa. Visiwa hivyo vinazunguka Nassau, kile kilicho mbali zaidi kikiwa kilometa zaidi ya 480 kutoka Nassau. Katika vichache vya hivyo Visiwa vya Nje nje unaweza kufurahia makao na vifaa vyote vya kisasa vya Nassau, lakini vingine havijasitawi kwa kadiri hiyo. Kwa mfano, vingine havina nguvu za umeme wala maji ya mabomba. Katika vingine, bado unaweza kuona watu wakipika kwa kuteleka vyungu vyao juu ya mioto ya kuni katika majiko yao yaliyoezekwa kwa nyasi au wakisaga mahindi katika visagio vya kuzungushwa kwa mkono.
Jinsi Mimi Ninasafiri
Vyote vya Visiwa vya Nje nje vinaweza kufikiwa kutoka Nassau kwa mashua au ndege, lakini umbali wavyo unaweza kutatiza watu walio na kazi kama yangu. Kwa kufuata utaratibu unaofanana na ule uliofuatwa na Wakristo wa karne ya kwanza, mhudumu anayesafiri, au mwangalizi wa mzunguko, anatembelea makundi na vikundi vidogo vya Mashahidi wa Yehova ili kuvipa nguvu na kuvitia moyo kiroho.—Matendo 15:36; 16:4, 5.
Mimi nakumbuka kikundi cha Mashahidi watatu tu nilichopaswa kutembelea katika kimoja cha hivyo Visiwa vya Nje nje. Kikundi hicho hakikuwa kimetembelewa na mwangalizi wa mzunguko kwa miaka zaidi ya mitatu. Mimi niliwaandikia nikiwa Nassau, nikawajulisha juu ya tarehe za ziara yangu. Lakini nilipofika kwa mashua, hakuna Shahidi aliyenilaki kwenye kibandari. Kwa hiyo nikauliza kama mtu ye yote angeweza kunisaidia nipate mmoja wa Mashahidi. Nilielekezwa kwa mwanamke fulani, na nilipojijulisha kuwa mwangalizi wa mzunguko, alisisimuka sana hata akapiga mbio akaambia Mashahidi wale wengine kwamba nimefika. Alikuwa ameniacha nikisimama pale nikiwa na mizigo yangu. Kwa kuwa Mashahidi hao hawakuwa kamwe wamepokea barua yangu, walishangazwa na kufurahishwa sana na ziara yangu.
Safari ya kurudi Nassau ilikuwa ya kutumia mashua ndogo ya kusafirisha shehena na barua. Safari hiyo ya majini ilichukua saa zaidi ya 30 kupitia bahari zenye msukosuko, lakini wakati huo ulipita haraka, angalau kwangu mimi. Nilitumia nafasi hiyo kuwahubiri wengine wa abiria. Muda fulani baadaye, mmoja wa wenye kuendesha mashua alianza kujifunza Biblia na sasa anahudhuria mikutano kwenye moja la makundi katika Nassau.
Njia nyingine ya kutembelea Visiwa vya Nje nje ni kwa kutumia ndege. Hata hivyo, ni ndege ndogo ndogo tu zinazoweza kutua katika baadhi ya viwanja vidogo vya visiwani. Kwa kawaida ndege hizo ni salama kiasi cha kutosha, lakini nyakati nyingine kunakuwa na vituko vya kuogopesha sana. Katika pindi moja, mimi niliingiwa na wasiwasi mwingi nilipoona moshi ukijaa katika kile kijumba cha waendeshaji ndege wakati ilipokuwa ikiinuka kutoka chini. Ndege hiyo ilirudi upesi kwenye kiwanja. Sababu ya moshi ule ulikuwa nini? Ilikuwa kiota cha panya wa aina fulani kilichojengwa katika kifereji cha kupashia ndege joto na kupitisha hewa karibu na ingini!
Namna Gani Watu Wale?
Wakati wa kusafiri katika Visiwa vya Nje nje, nimekuta watu wengi wanaotamani vitabu vya Kibiblia. Lakini kwa wengine wao, hata ile bei ya chini ya vitabu inakuwa yenye kupita uwezo wao. Kwa mfano, katika mchana mmoja wenye joto kali sana watatu kati yetu tulikuwa tukihubiri katika kisiwa kimoja cha mbali wakati nilipokutana na mwanamke mmoja aliyeonyesha kupendeza kwingi na kichapo Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Yeye hakuwa na pesa zo zote za kuchangia bei ya kichapo hicho, lakini vitu vile alivyokuwa navyo katika friji yake ndivyo hasa tulivyokuwa tukivihitaji—mikebe mitano ya kinywaji baridi. Tulibadilishana kitabu kile na vinywaji vyake baridi, na kila mtu akafurahi.
Wakaaji wa Bahamas wanaipenda Biblia kweli kweli. Jambo hilo linafanya ifurahishe kuwaletea “habari njema” za Ufalme wa Yehova. (Mathayo 24:14) Mara nyingi unapotembelea nyumba fulani, utamkuta mwenye nyumba akiisoma Biblia. Kwenye nyumba moja niliyotembelea, mama wa hapo aliona fahari kumwagiza binti yake mwenye umri wa miaka mitatu anitajie kwa kukariri majina ya vitabu vyote 66 vya Biblia kwa kufuatisha utaratibu unaofaa wa jinsi vilivyopangwa.
Wakati wa miaka michache iliyopita, Wanavisiwa wa Nje nje wamefurahiwa kuona maonyesho ya slaidi juu ya habari za Biblia yaliyotayarishwa na Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi. Katika kisiwa kimoja, hakuna jumba lililopatikana, kwa hiyo tukafanya mipango ya kuonyesha slaidi nje katika ukuta uliokuwa umepakwa rangi nyeupe hivi majuzi karibu na kiduka cha chakula. Karibu watu 60 walikusanyika kuzunguka mahali hapo—wengine wakiwa wamesimama, wengine wakiwa wameketi.
Katika pindi nyingine, watu 120 walikusanyika. Walithamini programu ya slaidi hivi kwamba wakati taa zilipowashwa tena, hakuna mtu aliyeenda zake. Mimi nikakumbuka kwamba nilikuwa nimekuja na aina nyingine ya slaidi kuhusu habari tofauti ya Biblia. Kwa hiyo taa zikazimwa tena, na aina ya pili ya slaidi ikaonyeshwa na kufurahisha umati huo.
Nyakati nyingine matatizo yanaweza kutokea. Katika kisiwa kimoja kikundi cha watu kilikusanyika katika nyumba ya shule ya hapo ili waone programu yetu ya slaidi. Nilipofungua projekta, kioo cha taa kiliungua. Mimi sikuwa na kioo cha ziada cha projekta, na hakuna cho chote kilichopatikana katika hicho Kisiwa cha Nje nje. Ni wazi kwamba umati huo ulikata tamaa. Hata hivyo, kwa kufanya haraka kufungua fungua projekta hiyo na kufanya marekebisho machache, niliweza kutumia kioo cha taa ya umeme kinachotumiwa kwa kawaida nyumbani kikawa kibadilisho chenye mafaa ya kiasi, lakini chenye kutoa mwangaza mdogo. Watazamaji hawakujai. Hata hivyo, walifurahia programu.
Buibui Wakubwa, Mbu, na “Paka Waliokaangwa”
Kufanya ziara za kawaida kwenye Visiwa vya Nje Nje kunahitaji kujifanyia marekebisho ili kujipatanisha na hali za tropiki. Mimi nakumbuka mara ya kwanza nilipoona buibui mkubwa. Buibui huyo alikuwa akitambaa kupita katikati ya sakafu na alionekana kama kwamba ana ukubwa unaolingana na mkono wangu! Mimi nilisimama nikiwa nimeduwaa kwa wasiwasi —nimehofu sana. Nashukuru kwamba mwenye nyumba alikuja kuniokoa. Kwa pigo moja la haraka sana la kutumia upanga wake, “adui” huyo aliondolewa. Mwenye nyumba huyo alikuwa mwanamume mwenye umri wa miaka 82. Hapo kwanza, yeye alikuwa akipinga vikali jitihada za mke wake za kutumikia Yehova. Lakini baada ya muda akaanza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme na kujifunza Biblia pamoja na mkeye.
Kwa sababu ya hali yenye joto, huenda mbu wakatokeza tatizo. Nyakati nyingine wanaweza kuwa wengi sana hivi kwamba unaposema huenda mmoja akaruka na kuingia moja kwa moja kinywani mwako. Bila shaka, vitu vingine vyenye uhai vinafurahisha kuvitazama, kama vile flamingo wa kupendeza sana wenye rangi nyekundu nyeupe wanaoishi katikati ya mazingira yao asilia ya mimea ya kitropiki yenye kusitawi sana na mitunda.
Kujifunza juu ya vyakula vya mahali hapo kunaweza kufunulia mtu mengi. Katika kisiwa kimoja, nilitupa jicho nikaona ulioonekana kama mchungwa wenye kujaa matunda yenye maji mengi. Nikauliza bibi wa nyumba ile kama ningeweza kuchuma moja au mawili ya machungwa yake. Yeye alinitahadharisha. Hayakuwa machungwa bali matunda makali makali. Lakini akasema ningeweza kujisaidia mwenyewe. Ikawa kwamba, mimi niliwaza kwamba nilijua chungwa lilivyo wakati nilipoona moja. Kwa hiyo nikachagua moja nene lililo zuri nikaliuma. Wee, acha nishangae! Kinywa changu kilikunjamana. Tunda lile lilikuwa kali kweli kweli, kama limau. Mwanamke yule alicheka, lakini nikajifunza kwamba ingawa tunda la ‘mchungwa’ mkali huo linaonekana kama chungwa, hakika ladha yalo si kama ya chungwa!
Nilifikiri nilikuwa nikijirekebisha vya kutosha nijipatanishe na maisha ya kisiwani mpaka nilipofunga safari ya kwenda kwenye kimoja cha visiwa hivi majuzi. Nilikuwa nikikaa na mjane wa kiume aliye mzee-mzee nilipokuwa nikitumikia kundi lake. Nilipoamka asubuhi ya kwanza, yeye alinialika nijiunge naye kula kiamsha kinywa. Mate yalinidondoka kinywani kwa kutazamia mlo mpaka alipotaja vitu alivyokuwa akipika. “Paka waliokaangwa!” Nilipoingia jikoni nikiwa karibu kukataa toleo lile, nikaona akipindua-pindua panikeki. “Wa wapi ‘paka waliokaangwa’?” nikauliza. Nilitweta vikubwa, nikatusha moyo, nasi wawili tukaangua kicheko. Yeye alifikiri kwamba mimi nilijua ya kuwa panikeki huitwa paka wa kukaangwa katika kisiwa hicho.
Thawabu za Kusafiri
Kwa sababu ya vingine vya visiwa hivi kuwa mbali, kuna uhitaji mkubwa wa wahudumu zaidi wasaidie kueneza habari njema za Ufalme wa Mungu. Uhitaji huo si wa kufikia watu wanaosema Kiingereza pekee yao katika Bahamas bali pia wa kufikia wakaaji Wahaiti waliohamia kule, wenye kusema Kifaransa.
Kuwa mhudumu anayesafiri katika Bahamas ni jambo lenye kusisimua linalohitaji marekebisho fulani ili kujipatanisha na njia ya maisha ya kisiwani. Lakini pia kuna thawabu kubwa kubwa. Moja ni ile furaha isiyokadirika ya kuona watu wakiitikia ujumbe wa Biblia. Nyingine ni pendeleo zuri sana la kuyasisimua kiroho makundi yaliyotapakaa na vikundi vilivyo peke yavyo.
Sisi katika Bahamas tunafurahia sana uzuri wa kupendeza wa fuo za bahari zinazometameta michanga yenye rangi nyekundu nyeupe na miamba matumbawe inayopendeza macho, yenye kupambwa samaki. Lakini hasa tunafurahishwa sana na jambo ambalo linatukia sasa hapa na kuzunguka dunia. Sisi tulio Mashahidi wa Yehova, tunaona Zaburi 97:1 ikitimizwa. Inasema: “[Yehova] ametamalaki, [dunia] na ishangilie, visiwa vingi na vifurahi.”—Imechangwa.
[Blabu katika ukurasa wa 27]
Mimi nikawa na wasiwasi sana nilipoona moshi ukijaa katika kijumba cha waendeshaji ndege wakati ilipokuwa ikiinuka juu kutoka chini
[Blabu katika ukurasa wa 28]
Wakaaji wa Bahamas wanapenda Biblia kweli kweli. Jambo hilo linafanya iwe furaha kuwaletea habari njema za Ufalme wa Yehova
[Blabu katika ukurasa wa 28]
Mimi nakumbuka mara ya kwanza nilipoona buibui mkubwa. Alikuwa akitambaa kupita katikati ya sakafu na alionekana kama kwamba ana ukubwa unaolingana na mkono wangu!
[Blabu katika ukurasa wa 29]
Nikamwuliza, “Wa wapi ‘paka waliokaangwa’?”
[Map/Picture katika ukurasa wa 26]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
FLORIDA
BAHAMAS
ATLANTIC OCEAN