Kujithibitisha Kuwa “Wenye Bidii kwa Ajili ya Kazi Nzuri” Katika Kenya
“HILI ndilo jambo ambalo nimekuwa nikitafuta kwa maisha yangu yote!” akasema kwa kupaaza sauti mwanamume mmoja wa asili ya Kihindu akiisha kuhudhuria kusanyiko la karibuni la Mashahidi wa Yehova katika Kenya, Afrika. “Hili ni jambo la pekee.”
Ni jambo gani lililomsukuma aseme hivyo? “Watu wa rangi nyingi sana, malezi mengi, na nchi nyingi—wote wakichangamana kwa uhuru wakiwa na shauku ionekanayo wazi kwa mmoja na mwenzake,” yeye akasema. Lakini jambo hilo liliwezekanaje katika ulimwengu uliojaa sana ukosefu wa umoja na ubaguzi wa rangi? Ni kitu gani kilichoongoza kwenye umoja na upatani huo wa kiroho katika Kenya?
Mapainia wa Kwanza-kwanza Watayarisha Njia
Huko nyuma katika 1931, Frank na Gray Smith walisafiri kwa meli kutoka Afrika Kusini kuja Mombasa wakiwa na vibweta 40 vya vitabu. Kutoka hapo, walifanya safari yenye kuchosha na yenye hatari kuja Nairobi, ambako waligawanya akiba yao yote ya vitabu katika mwezi mmoja. Wote wawili waliugua maleria, na Frank akafa,—mwaminifu mpaka mwisho. Baadaye mwaka uo huo, Robert Nisbet na David Norman walifuata safari kama hiyo, wakigawanya vibweta 200 vya vichapo katika Afrika Mashariki. Hivyo ndivyo zile mbegu za kwanza za ukweli zilivyopandwa katika Kenya.
Ndipo katika 1935, Gray Smith na mkeye, wakiwa pamoja na Robert Nisbet na ndugu yake George, waliondoka wakafuatie kupendezwa kulikopatikana. Wakati huu Robert alishikwa na ugonjwa wa homa ya matumbo. Wale wengine walitaabishwa na maleria na namna nyingine ya maleria inayomfanya mtu akojoe mkojo mweusi. Kuongezea shida hizo ni upinzani na amri za kurudishwa makwao za serikali ya kikoloni. Hata hivyo yajapokuwa yote hayo, mapainia hao wa kwanza wenye bidii waligawanya kiasi kikubwa mno cha vitabu, wakaweka msingi kwa ukuzi. Kwa mfano, kama miaka 30 baadaye, Shahidi mmoja akifanya kazi katika eneo la mbali la mashambani katika Kenya alishangaa kumpata mwanamume aliyekuwa na nakala ya kitabu Reconciliation. Ndugu yake alikuwa amekipata katika 1935. Mtu huyo alifanya maendeleo na sasa ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Ukuzi Zaidi
Haikuwa mpaka 1949 kwamba Shahidi wa kwanza, Mary Whittington, akaja kukaa Nairobi, mji mkuu wa Kenya. Yeye alikuwa amebatizwa huko Uingereza mwaka mmoja tu uliotangulia. Yeye hakujua sana juu ya hali ya kukaa pekee, vipingamizi, na upinzani ambao alikuwa karibu kupatwa nao. Hata hivyo, yeye alikuwa na furaha ya kuona ‘mdogo akiwa elfu.’ (Isaya 60:22) Leo, akiwa na umri wa miaka 73, angali anatumika akiwa painia wa kawaida.
Bill na Muriel Nisbet, wahitimu wa kwanza wa Shule ya Biblia ya Gileadi ya Mnara wa Mlinzi kupewa mgawo Kenya, walifika katika 1956. Wakati huo, ubaguzi wa rangi ulienea pote, na utawala wa kikoloni ulikuwa na sheria zilizozuia utendaji wa kuhubiri na kuwekea mipaka ukubwa wa mikutano isiwe na watu wanaozidi tisa. Kwa hiyo kazi ya akina Nisbet ilifanywa miongoni mwa shamba la Wazungu tu na mazungumzo ya vivi hivi pamoja na Waafrika. Ingawa hivyo, ukuzi ulikuja.
Katika 1962, kazi ya Mashahidi wa Yehova ilitambuliwa kisheria. Muda mfupi baada ya hapo, katika 1963, utawala wa kikoloni ukakoma, hivyo ukafungulia mlango upanuzi zaidi kwa kazi yetu ya Kikristo. Sasa vichapo vingeweza kuchapwa katika lugha ya Kiswahili, na wazee wa Mashahidi wa Yehova waliruhusiwa na serikali kuandikisha ndoa. Tangu wakati huo, Mashahidi wa Yehova wamesaidia karibu watu waume na wake 2,000 waandikishe ndoa zao kisheria.
Kufika 1972, jengo zuri jipya la afisi ya tawi, lililo katika sehemu inayofaa sana katika Nairobi, liliwekwa wakfu. Tangu hapo limepanuliwa. Kenya sasa ilikuwa imepewa vifaa kwa njia nzuri zaidi isimamie kazi ya Ufalme katika zile nchi kumi za Afrika Mashariki zilizo chini ya uangalizi wayo na kutoa vichapo vilivyohitajiwa katika lugha mbalimbali za wenyeji.
Mifano Mizuri Sana ya Bidii
Watangazaji wa habari njema katika Kenya wanadhihirisha ‘bidii kwa ajili ya kazi nzuri’ ile ile iliyoonekana miongoni mwa Wakristo wa karne ya kwanza. (Tito 2:14) Wao hawaruhusu magumu yawazuie kuwasaidia wengine wapate maarifa sahihi ya Biblia.
Katika kisa kimoja, Shahidi mmoja alipokea ombi kutoka afisi ya tawi amtembelee mtu kipofu mwenye kupendezwa, aliyeishi umbali wa kilometa 26. Shahidi huyo kwa ukawaida alifanya safari kwa baiskeli akaongoze funzo la Biblia pamoja naye. Ijapokuwa mtu huyo alikuwa amepatwa na vipindi kadha vya fikira zisizofaa na mshuko wa moyo, sasa yeye mwenyewe ni Shahidi, kwa bidii akiwaambia wengine juu ya ahadi ya Mungu ya Paradiso itakayorudishwa wakati hata macho ya vipofu yatafunguliwa.—Isaya 35:5.
Katika maeneo mengine, jitihada kubwa lazima zifanywe ili kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Mwanamke mmoja wa miaka 70 kwa ukawaida hutembea karibu kilometa kumi kufika kwenye mikutano ya kila juma. Akiwa njiani, yeye hupitia katikati ya mmoja wa mito iliyo mikubwa zaidi ya Kenya, ingawa mamba wanaotea karibu karibu. Nyakati nyingine mkondo unakuwa wenye nguvu sana hivi kwamba karibu unamfagilia mbali. Hata hivyo, yeye anaona karamu ya kiroho inastahili jitihada hiyo. Lo! ni mfano wenye kutokeza jinsi gani wa bidii!
Mfano mwingine mwema wa bidii na uthamini ulionyeshwa na Shahidi mmoja ambaye alitembea kwa saa tisa akahudhurie kusanyiko la mzunguko. Ni kwa sababu gani alifanya hivyo, hata ingawa yeye alikuwa na fedha za kutosha za nauli ya basi? Kwa kusukumwa na upendo, yeye alitoa fedha zake akampa mwanafunzi wa Biblia wake ili yeye pia aweze kufurahia programu ya kusanyiko! Ndiyo, upendo na ‘bidii kwa ajili ya kazi nzuri,’ msingi wake ukiwa ni maarifa sahihi ya Biblia, vinaonekana wazi katika Kenya.
“Roho ya Painia”
Bidii hii imeonyeshwa katika huduma ya wakati wote ya painia kwa njia yenye kutokeza sana. Wengi wamepata furaha katika utumishi huu ijapokuwa hali ngumu. Painia mmoja wa kawaida kijana anatumikia katika mji wa bandarini wenye joto na unyevunyevu wa Mombasa. Miguu yake yote miwili ilikuwa imekatwa kwa sababu ya aksidenti ya lori miaka kadha iliyopita. Alipokuwa hospitalini, alifikiria kujiua na alikuwa amemsihi mwuguzi amdunge sindano ya kumwua, jambo ambalo mwuguzi huyo alikataa kufanya. Baada ya kufunguliwa kwake, yeye aliwapata Mashahidi na akaanza kujifunza Biblia pamoja nao. Hilo liliongoza kwenye ubatizo wake na njia mpya ya maisha katika utumishi wa wakati wote. Yeye anafurika kwa bidii na shukrani.
Hesabu kubwa ya akina mama wenye madaraka ya jamaa pia wamekuwa pia mapainia wa kawaida. Kati yao ni mmoja mwenye watoto watatu. Yeye ana ugonjwa wa mpigo wa damu wa juu sana na kigugumizi. Yeye analazimika kufanya kazi wakati wote, na mume wake si Shahidi. Hata hivyo, yeye ni painia mwenye furaha. Bila shaka, si akina mama peke yao wanaoshiriki katika utumishi wa painia wa kawaida. Hivi karibuni, baba aliye na watoto wanane wa kutunza na kazi inayohusu kufanya kazi kwa zamu pia alichukua pendeleo hilo la utumishi.
Wengi wasioweza kuwa mapaina wa kawaida wanawakwa na “roho ya painia.” Wao wanatafuta nafasi za kushiriki katika utumishi wa wakati wote wakiwa mapainia wasaidizi, wakitumia saa 60 katika kazi ya kuhubiri kila mwezi.
Katika Aprili 1984, na pia katika 1985, zaidi ya theluthi moja ya wahubiri wote katika Kenya walishiriki katika namna fulani ya utumishi wa wakati wote. Kundi moja lilikuwa na wahubiri 73 waliojiandikisha kuwa mapainia wasaidizi mwezi huo, wakifanya kazi pamoja na wale mapainia wa kawaida watano. Wale washiriki wengine 28 wa kundi walikuwa na wastani wa saa 64.6, ingawa wengi wao hawakuwa wamebatizwa. Kama matokeo, jumla ya mafunzo ya Biblia 233 yaliongozwa!
Hata umri hauthibitiki kuwa kizuizi. Nyanya mmoja wa umri wa miaka 99 alichukua huduma ya painia msaidizi. Ijapokuwa vizuizi vyake vya kimwili, yeye anaacha nuru yake ing’ae kwa ushujaa kuelekea vijana na wazee. (Mathayo 5:16) Kupitia jitihada zake, hesabu fulani ya wengine wamesaidiwa kuwa watangazaji wa Ufalme, nao wanapenda sana kukumbuka kujitoa na roho ya painia ya huyo “nyanya.” Ndiyo, ‘bidii kwa ajili ya kazi nzuri’ kama hiyo imeongoza wengi wasitawishe roho ya painia.
Sifa—Kutoka Vinywani mwa “Watoto Wachanga”
Wachanga, pia, ingawa hawajabatizwa bado, kwa furaha na kwa shauku wanaambatana na wazazi wao katika kupelekea watu wengine habari njema kutoka kwa Mungu wa kweli. (Mathayo 21:16) Wakati wa kampeni ya pekee, kisichana cha miaka minne na nusu kilifanya kazi pamoja na wazazi wacho katika eneo lililo pekee yalo. Kilitumia saa 160 katika huduma ya shambani mwezi huo, kikaangusha vitabu 27, vijitabu 66, na magazeti 47 kwa watu waliokuwa wakipendezwa katika Biblia!
‘Bidii hii kwa ajili ya kazi nzuri’ inadhihirishwa shuleni pia. Katika sehemu ya mashambani nje ya Nairobi, mvulana wa shule ya msingi, ambaye mama yake alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, aliweza kusaidia mwalimu wake aingie kwenye barabara iendayo kwenye uzima wa milele. Darasani, wakati mwalimu alipoanzisha mazungumzo juu ya habari ya uzima baada ya kifo, mvulana huyo kwa heshima alitaja kwamba mama yake alikuwa amemfundisha jambo tofauti, ambalo msingi wake ni Biblia. Jambo hilo liliamsha utafiti wa mwalimu huyo. Mwalimu huyo wa kike alionana na mama wa mvulana huyo, ambaye alimwelekeza kwa Shahidi mwenye ujuzi zaidi. Sasa, mwalimu mwenyewe anaeneza ukweli wa Biblia kwa wengine, shukrani kwa ushujaa wa kijana huyo. Lo! ni mfano mwema wa bidii kama nini miongoni mwa watoto Wakristo leo!
Ukuzi Zaidi Watazamiwa
Zaidi ya nusu ya idadi ya watu wa Kenya wangali wanahitaji kusikia habari njema za Ufalme. Kwa sababu ya umbali, maeneo fulani yaliyo peke yayo yanaweza kuenezwa mara moja tu kwa mwaka. Wafikapo katika maeneo haya, ni jambo la kawaida Mashahidi kusalimiwa kwa maneno haya: “Mmekuwa wapi? Tumekuwa tukiwakosa.” Ndipo, baada ya kutoa ushuhuda hapo kwa siku chache au majuma, na wakati unafika wa kuondoka, mtu anaguswa sana moyo kusikia semi kama hizi: “Sasa mtatuacha tena? Tutafanyaje maendeleo?” Kwa furaha, mipango imefanywa kuwarudia walio wengi wa watu hawa mmoja mmoja “wenye njaa” kiroho.
Leo, kuna wahudumu wa Ufalme 3,686 katika Kenya. Kwenye mwadhimisho wa Ukumbusho wa kifo cha Kristo katika 1986, 13,067 walihudhuria. Karibu hesabu hiyo ilikuwa mara nne ya hesabu ya Mashahidi. Waliokuwa hapo kwanza wazoelevu wa kileo, wapiga watu, viongozi wa magenge, wanyang’anyi, wawasilianaji na ulimwengu wa roho, na wengineo wamefanya mabadiliko makubwa katika maisha zao na sasa wanatembea katika vijia vya ukweli. Hilo linatuambia nini juu ya wakati ujao?
Kwa wazi, ukuzi zaidi unatazamiwa. Ndiyo, watu wanaitikia kwa uelekevu “habari njema hizi za Ufalme” katika Kenya leo. Wengi wamejiunga na safu za Mashahidi wa Yehova—watu ‘wenye bidii kwa ajili ya kazi nzuri.’ Kwa sababu ya kazi hizo, wanasimama peke yao wakiwa watu wa pekee sana, bila vizuizi vya kikabila pamoja na vizuizi vingine vya umoja wa kweli. Kweli kweli, hilo ni “jambo la pekee.”
[Ramani katika ukurasa wa 22]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
KENYA
Nairobi
Mombasa
[Picha katika ukurasa wa 23]
Maelfu ya wajumbe wenye kusema Kiswahili walihudhuria “Washika-Ukamilifu” Mkusanyiko katika Desemba 1985
[Picha katika ukurasa wa 24]
Michezo ya kuigiza ya Kibiblia ikitolewa katika Kiswahili na Kiingereza iliwajenga wasilikizaji
[Picha katika ukurasa wa 25]
Ubatizo uliofanywa hadharani ulitoa ushuhuda wa baraka ya Yehova