Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w87 8/15 kur. 25-27
  • Kuonyesha Ushikamanifu wa Kikristo Katika New Caledonia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuonyesha Ushikamanifu wa Kikristo Katika New Caledonia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Vichwa vidogo
  • Mianzo ya Ushikamanifu wa Kikristo
  • Ushikamanifu kwa Ufalme wa Mungu Chini ya Jaribu
  • Kupanua Kishikamanifu Kujapokuwa Msukosuko
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
w87 8/15 kur. 25-27

Kuonyesha Ushikamanifu wa Kikristo Katika New Caledonia

MAMBO yote hayakuwa sawa katika paradiso. Kufikia mapema mwa 1985, msukosuko wa kisiasa ulikuwa umetwaa karibu maisha za watu 20 katika kisiwa cha Pasifiki Kusini cha New Caledonia. Jambo hili liliongoza gazeti la Maclean’s kutoa maelezo haya: “Tayari kisiwa kimeanza kufanana na Ailandi ya Kaskazini, kikiwa kimegawanyika katika kambi mbili zenye silaha nyingi na zenye uhasama.”

Hali hiyo ilikuwa imekuwa mbaya sana katika Januari 1985 hivi kwamba Rais wa Ufaransa François Mitterrand alienda upesi sana Jumamosi moja katika ziara isiyoratibiwa kwenda Noumea, mji mkuu wa kisiwa hicho mwendo wa kuzunguka nusu ya ulimwengu. Wakaaji wa kisiwa hicho, wakiwa wamegawanyika katika ushikamanifu wao, walitamani kusema walivyohisi wakati wa ziara hiyo. Wenyeji asilia, wakisukumwa na viongozi wa kidini na hisia yenye nguvu ya ushikamanifu kwa asili yao ya Kimelanesia, walisisitiza sana utawala wa Kifaransa wa miaka zaidi ya 130 ukome. Kwa upande ule mwingine, wazao wengi wa Wazungu na wa Polinesia na wahamiaji Waesia, na hata Wamelanesia, walionyesha ushikaminifu wao kwa serikali ya Kifaransa na wakatetea kwamba utawala wayo uendelee.

Wakati uu huu, Jumamosi ii hii, Mashahidi wa Yehova 1,567 pamoja na marafiki wao walikuwa pia wamekusanyika katika Noumea ili wafanye wonyesho wa waziwazi wa ushakamanifu. Hata hivyo, ushikamanifu wao, haukuwa kwa kikundi cho chote cha kikabili au kwa serikali ya kidunia; ulikuwa ushikamanifu kwa Ufalme wa Mungu uliosimamishwa. Lakini ilitukiaje kwamba walikuwa katika Noumea katika siku yenyewe hiyo? Kwa habari hiyo, ilikuwaje kwamba walikuwa katika New Caledonia hata kidogo?

Mianzo ya Ushikamanifu wa Kikristo

New Caledonia ina kile ambacho huenda ukatazamia kwa habari ya paradiso ya Pasifiki ya Kusini—hali ya hewa yenye kupendeza mwaka mzima, kuna matunda matamu sana yenye kupendeza kaakaa la kinywa, kuna mimea na miti kwa wingi sana yenye kufurahisha jicho, kuna mchanganyiko wa rangi nzuri-nzuri wa Wamelanesia, Wapolinesia, Waesia, na Wazungu zaidi ya 150,000.

New Caledonia ilivumbuliwa katika 1774 na Kapteni James Cook, yule nahodha Mwingereza na mvumbuaji wa nchi anayejulikana sana, lakini ikawa koloni la Ufaransa katika 1853. Wamisionari wa Jumuiya ya Wakristo walikuja muda mfupi tu baada ya wavumbuaji na wafanya biashara wa kwanza kufika. Bila shaka watu waliowakuta walihitaji kuwekwa huru na mazoea fulani mabaya. Kwa mfano, wamisionari hao walifanikiwa katika kuondolea mhali ulaji wa nyama ya wanadamu. Pia wao waliwajulisha watu Biblia na hata wakaitafsiri katika lugha nne za mahali hapo. Jambo lenye kusifika ni kwamba walitia ndani jina la Mungu, linalotafsiriwa Iehova au Jehova katika lugha ya watu wa mahali hapo. Lakini mengi zaidi yalihitajiwa.

Katika muda wa tangu 1930, kikundi cha Mashahidi wa Yehova kilisafiri kwa meli kupitia Visiwa vya Ushikamanifu wakigawanya vichapo vya Biblia. Katika muda wa kati ya 1950 na 1960 Mashahidi wa Australia kadha wa kadha walihamia New Caledonia. Ijapokuwa baadaye walifukuzwa nchini, kazi ilisitawi, na kufikia 1967 hesabu ya Mashahidi wa mahali hapo ilikuwa imeongezeka ikafikia zaidi ya 100. Katika 1976 Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ilianzisha afisi ya tawi katika Noumea nayo ikasimamia kazi ya ujenzi wa Jumba la Ufalme la kwanza katika kisiwa hicho.

Hasa tangu wakati huo hatua ndefu zimefanywa katika kukusanya raia washikamanifu wa Ufalme wa Yehova uliosimamishwa kutoka katika vikundi tofauti-tofauti vya kikabila vya nchi hiyo. Kwa mfano, karibu watu 17,000 kutoka Wallis na Futuna—visiwa vidogo vilivyo kaskazini mwa Fiji—wanaishi katika New Caledonia. Wengi wa Wawalisi hao ni Wakatoliki na wamejitoa sana kwa kanisa lao. Lakini mwelekeo wao umekuwa ukibadilika kadiri wengi zaidi na zaidi wao wameanza kusikiliza ujumbe wa Ufalme. Kasisi mmoja, akiwa amekasirishwa sana na jambo hili, alimtuma mwanamke mmoja aliyesimamia fedha za kanisa ili “akawaokoe kondoo wasipotee.” Lakini mwanamke huyo pia alisikiliza. Kisha binti yake, ambaye alikuwa akisomea Roma awe mmisionari, alirudi nyumbani naye akakubali ukweli wa Biblia waliofundisha Mashahidi wa Yehova. Sasa msichana huyo na mama yake ni Mashahidi washikamanifu waliojiweka wakfu.

Leo Mashahidi wanajulikana sana kila mahali katika visiwa hivi, katika sehemu fulani, kuna Shahidi mmoja kwa kila watu 80. Katika kisiwa cha Lifou, kijana seremala akawa Mpentekoste. Yeye alienda kutoka kijiji kwa kijiji, akitangaza kwamba Kristo angerudi kwa kuonekana katika kisiwa hicho. Ili aonyeshe usadikisho wake kwamba vitu vya kimwili havina thamani, yeye alizichoma nguo na pesa zake hadharani. Lakini alikuja kupendezwa na habari alizosoma katika trakti moja iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Funzo la Biblia la kawaida lilimsaidia apate maarifa sahihi ya Neno la Mungu. Leo yeye ni Mkristo aliyesawazika, mhudumu wa wakati wote.

Ushikamanifu kwa Ufalme wa Mungu Chini ya Jaribu

Msukosuko wa kisiasa na hali zilizochafuka ambazo zilitokea katika 1984 zilitokeza matatizo kwa watu wengi wa New Caledonia, kutia na Mashahidi. Wengine wao washambuliwa na kundi lenye ghasia na kupigwa walipokuwa wakihubiri. Watu watatu waliingia katika nyumba ya Shahidi mmoja, wakidai funguo za gari kwa mtutu wa bunduki, kisha wakaliiba gari lake. Mmisionari mmoja aligundua kwamba gari lake lilikuwa limechomwa moto na kuharibiwa alipokuwa akiongoza funzo la Biblia.

Ingawa wakaaji wa kisiwa hicho wamegawanyika katika ushikamanifu wao mwingi, Mashahidi—bila kujali ni wa kikundi gani cha kikabila—wana umoja katika msimamo wao wa kutokuwamo. Viongozi wa kidini, wao wenyewe wakiwa wamejiingiza katika siasa, wametumia hali ya msukosuko ulioko sasa kuamsha chuki kwa Mashahidi. Kwa mfano, Mashahidi waliokuwa wakiendesha gari ili wakachukue watu wanaopendezwa na kuwapeleka kwenye mkutano walisimamishwa. Mwangalizi wao asafiriye, aliyekuwa akiwatembelea juma hilo, aliburutwa kutoka mojayapo magari hayo mawili na kupigwa, na miwani yake ikavunjwa-vunjwa. Mtu mmoja mwenye kupendezwa alisukumwa kwenye ukuta na kupigwa mpaka kichwa chake kikatoka damu, mke wake aliyekuwa mjamzito akilazimishwa kumtazama.

Hata hivyo, Mashahidi wanajua kwamba ushikamanifu wao haujawekwa mahali pasipofaa. Wao wanayakumbuka maneno ya Paulo: “Kwa kweli, wale wanaotamani kuishi kwa kujitolea Mungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.”—2 Timotheo 3:12, NW; ona pia Mathayo 10:16.

Kupanua Kishikamanifu Kujapokuwa Msukosuko

Katika muda wa kati ya 1984 Mashahidi waliona uhitaji wa kujenga jumba la makusanyiko. Sehemu inayofaa ilipatikana katika kilima ambacho kutoka kwacho ungeweza kuona bandari ya Noumea, nayo kazi ikaanzishwa Septemba. Lakini katika Novemba, kwa sababu ya msukosuko wa kisiasi, mamlaka ilipasisha kafyu, na hali ya dharura ikatangazwa. Yajapokuwa magumu hayo, Mashahidi kutoka kisiwa chote waliitikia uhitaji wa kusaidia penye mahali pa ujenzi. Kufikia watu wenye kujitolea 400 walikuja kwa wakati mmoja, jambo hilo likiwastajabisha sana watazamaji. Kwa kuwa kazi ya ujenzi ilifanywa wakati wa likizo ya shule, vijana wengi walisaidia. Msichana mmoja mchanga alisema hivi: “Hii ndiyo likizo nzuri zaidi ambayo nimewahi kupata.” Na kumwona Shahidi wa kike mwenye umri wa miaka 60 akitupa simenti na changarawe kwa koleo katika mashine yenye kuchanganyia saruji lilikuwa jambo la kutosha kustajabisha stadi wa ujenzi ye yote anayelipwa!

Baada ya miezi minne tu ujenzi ulimalizwa. Mipango ya kuzindua ilifanywa, lakini siku iliyopangwa ikawa mwisho-juma ule ule wa ziara isiyotazamiwa ya Mitterrand! Kwa sababu ya hali ambayo huenda ingetokeza jeuri ya kisiasi, mamlaka iliwaomba Mashahidi waifutilie mbali programu yao. Hata hivyo, mwanamume aliyesimamamia usalama, ambaye alikuwa ameuona mkusanyiko wa Mashahidi hapo mbeleni katika Ufaransa, aliwaambia: “Mimi nawafahamu ninyi watu. Si na ninyi tutakuwa na matatizo. Chukueni tu hatua zinazohitajiwa kabisa za usalama; sisi hatutaingilia mikutano yenu.”

Zaidi ya watu 1,500 walifika kwenye programu nzuri sana ya kuzindua, iliyofikia upeo kwa hotuba ya mzinduo iliyotolewa na Lyman Swingle, mshiriki mwenye kuzuru wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Ijapokuwa msukosuko wa wakaaji wa mji, hudhurio kwenye mkutano huu ulionyesha ushikamanifu wenye kutenda kwa Ufalme wa Yehova, ushikamanifu unaozaa matunda katika New Caledonia. Kilele kipya cha watangazaji Ufalme 889 kimefikiwa, na kuna mataraja mazuri sana kwa ongezeko zaidi. Uthibitisho wa jambo hili unaonekana katika 2,145 waliohudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo katika 1986.

Kipindi cha karibuni cha msukosuko wa kisiasa kinaonyesha waziwazi kwamba wakaaji walio wengi zaidi wa New Caledonia wanatumainia serikali za kibinadamu zitatue matatizo yao. Sivyo ilivyo kwa wale walio washikamanifu kwa Ufalme wa Mungu, ambao wanauweka utumainifu wao kamili katika utawala wa Mungu. Wakati wa magumu haya, ishara moja ilionwa pwani mwa barabara kuu upande wa mashariki yenye kusema hivi: “Yehova Nje!” Lakini Yehova, kama anavyowakilishwa na Ufalme wake uliosimamishwa, yupo na atadumu. Ndivyo walivyo na “washikamanifu wake.” —Zaburi 37:28, NW; ona pia mistari 9-11, 22, 29 na 34.

[Ramani katika ukurasa wa 25]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

AUSTRALIA

[Ramani]

NEW CALEDONIA

Lifou

LOYALTY ISLANDS

Nouméa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki