Timizo la Ajabu kwa Kosta Rika
“NINYI mnafanya jambo ambalo sisi tumefanya kujifunza tu!” akasema mhandisi wa utaalamu wa ujenzi aliyekuwa amekuja kuliona tawi jipya lililokuwa linasimamishwa kilometa 11 nje ya San Jose, Kosta Rika.
Ni jambo gani lililokuwa la ajabu juu ya majengo hayo? Yalijengwa kwa njia ile ya kuinamisha upande—mara ya kwanza kufanyika hivyo katika Kosta Rika. Msingi na nguzo zilijengewa chini kwanza. Ndipo, pale pale penye uwanja wa ujenzi, visehemu vya zege vya kuta vikatayarishwa kimoja juu ya kingine katika marundo. Ndipo visehemu hivyo vya kuta vilivyotangulia kutayarishwa chini vilipoinamishwa upande na kuinuliwa juu kwa mashine ya kunyanyua kisha vikaunganishwa kwa kutambuzwa katika mahali palipovifaa. Mwishowe, paa iliezekwa, na kazi iliyobaki tu ikawa ni kumalizia-malizia mambo madogo-madogo.
Mradi huo ulikuwa pia ndio jaribio la kwanza la Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi kujenga jengo kwa kutumia nje ya United States njia ile ya kuinamisha upande. Kwa sababu hiyo, wafanya kazi wa kutoka matawi mengine yanayopanga kufanya ujenzi au mpanuko walikuwapo kutazama jinsi utaratibu huo ulivyofanya kazi. Waliokuwapo, pia, walikuwa wahandisi na wataalamu wa ujenzi kutoka mashirika mengine. Wote walivutiwa sana na waliyoona.
Majengo hayo yalifanywa kwa mtindo ule wa kupendeza sana wa siku za ukoloni wa Hispania, yakiwa na paa yenye vigae vyekundu na madirisha yenye matao. Kibarabara chenye kuzunguka bustani ya mviringo kinaongoza kwenye mwingilio mkuu na sebule. Upande wa kuume ndipo lilipo jengo lile la ghorofa mbili lenye makao, lililo na vyumba 24, pamoja na chumba kikubwa cha jamaa kilicho na maktaba, maeneo ya kujifunzia, na mahali panapovutia pa kuotea moto. Chumba cha kulia chenye viti 100, na jiko la kisasa na mahali pa kufulia kimeunganishwa na sehemu hiyo. Upande mwingine wa ua ndipo lilipo jengo lenye afisi likiwa na afisi moja moja 13 na chumba cha mazungumzo ya kibaraza ambacho kimewekwa kuzunguka bustani ya kitropiki iliyo mahali peupe chini ya nuru ya anga. Jengo lile kubwa upande wa kushoto ni bohari la kuwekea vitabu na vifaa vingine.
Kila mtu aliyekuwa amekuja kutembea alistaajabishwa na aliyoona. Maelezo kama haya yalisikiwa tena na tena: “Kazi bora kama nini!” “Mimi sijapata kuona kitu kizuri kama hiki!” “Kwa wazi hii ni kazi ya upendo.”
Kweli kweli, yote haya yaliwezeshwa na “kazi ya upendo.” Ndugu na dada zaidi ya 4,700, kutia na 295 kutoka nchi nyinginezo, walifanya kazi ya jasho kwa miezi 24 kuhusiana na mradi huo. Sehemu kubwa ya vifaa na vitu vya matumizi ilifanyiwa penye uwanja wa ujenzi. Kwa mfano, katika hatua moja ya mwanzoni-mwanzoni chombo cha kuinua mpaka ghorofa mbili, ambacho akina ndugu walikiita Yulio kwa shauku, kilijengwa. Vichanganyio vya saruji vyenye kuitwa Bertha na Martha vilinunuliwa na kutayarishwa-tayarishwa kabisa kwa ajili ya mradi huo. Taa za kuonea, vyombo vya kutolea nuru, kazi ya mapao ya vyuma vya kusubu, vipandio-ngazi vya mari-mari ya Palladia na vituo, na vitu vinginevyo, vilifanyizwa vyote na akina ndugu ambao hawakuwa na ujuzi mahsusi katika kazi hizo. “Shauku iliyoonyeshwa na akina ndugu wa nchi hii kwa mradi huo ilikuwa nzuri ajabu,” akatamka msimamizi wa mradi huo.
Kilele cha shauku kilidhihirishwa Januari 4, 1987, wakati kutano la watu 13,111 lilipokuja kwa ajili ya wakfu. Roshani iliyo upande wa kaskazini wa chumba cha jamaa ilitumiwa kama jukwaa na kutano lile likakusanyika katika nyanja zenye eneo kubwa kule chini. Ndugu M. G. Henschel na L. A. Swingle wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova walikuwa ndio wasemaji wakuu katika programu. Hotuba yenye shauku ya Ndugu Swingle ilihusu kichwa “Yehova Anaendelea Kufanya Ikue,” na katika hotuba ya wakfu, Ndugu Henschel aliwasaidia wote wathamini kwamba jengo lenye sura zuri ni lenye mafaa kwa watu wa Yehova ikiwa tu wao wanaendelea kuzaa tunda la roho yake.
Walioletwa pamoja kwa ajili ya pindi hiyo maalum walikuwa washiriki wa jamii ya kwanza ya wamisionari wa Gileadi katika Kosta Rika. Sasa wakiwa wamezeeka kwa kadiri fulani, waliguswa sana moyoni na muungano huu wa mara nyingine na ushuhuda wenye kuonekana wa baraka nyingi za Yehova juu ya kazi ya kuuhubiri Ufalme katika Kosta Rika muda wa miaka iliyopita. Wakiwa na uandalizi mzuri ajabu wa kao hilo lenye nafasi kubwa, lenye kustarehesha, na lenye kufaa, wahudhuriaji wote walikuwa na uhakika wa kwamba jina la Yehova litatukuzwa zaidi katika nchi hii ya kitropiki.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Ukuta uliotangulia kutayarishiwa chini ukiinamishwa upande . . . na kuwekwa mahali panapoupasa kuwa
Kibarabara cha mviringo kinachoongoza kwenye jengo lililojengwa kwa mtindo wa siku za ukoloni wa Hispania
Sehemu ya umati wenye shauku siku ya wakfu