Kuifungua Njia ya Ongezeko Katika Gibraltar
UWANJA wa michezo huo upo mahali ambapo unaweza kuonwa kabisa mtu akiwa Gibraltar—umbali wa karibu kilometa 10,6. Hata hivyo, kwa miaka zaidi ya 13, wakaaji 4a Gibraltar walilazimika kufanya safari ya angalau muda wa saa kumi ili kufika kule. Hiyo ilihusu kusafiri baharini kwanza kwenda Afrika ya Kaskazini, kisha kurudi nyuma kwenda Hispania, na hatimaye kusafiri kwa basi. Kwa sababu gani iwe safari ndefu hivyo kufika mahali pa karibu sana?
Katika 1969 utawala wa Franco wa Hispania ulifunga mpaka kwenye ile shingo nyembamba ya nchi inayounganisha Hispania na Gibraltar. Hilo lilikuwa tokeo la ugomvi kati ya Hispania na Uingereza juu ya kuwa na enzi kuu ya kutawala eneo lililohusu ule Mwamba, kama vile Gibraltar inavyoitwa mara nyingi. Hata hivyo, sumbuo hilo halikuwa jipya kwa wakaaji wa Gibraltar. Kwa sababu ya kuwa mahali pa pekee pa kuongozea jeshi hasa la manowari, Gibraltar imekuwa boma lenye nguvu ambalo mara nyingi limejitenga kutoka nchi zilizo jirani.
Mapema katika karne ya nane, wavamia-nchi Wamoori wakiwa chini ya Tarik waliteka kipande hicho cha nchi na kukiita “Jabal Tariq” (mlima wa Tarik), jina ambalo tangu wakati huo limebadilika-badilika likaja kuwa “Gibraltar.” Wamoori waliutilia boma lenye nguvu ule Mwamba, ambao unainuka karibu meta 430 juu ya usawa wa bahari. Katika muda wa karne zilizopita, ulikuwa mahali palipofanyiwa mazingiwa mengi na Wamoori na Wahispania. Wahispania hatimaye waliteka Gibraltar katika 1462, wakaendelea kuitawala mpaka 1704, wakati ambapo Uingereza iliiteka na kujenga huko kituo cha meli za kivita.
Kwa kuongezea makao hayo ya kijeshi, watu kutoka nchi nyingi walilowea katika mji ambao uko katika sehemu ya chini ya ule Mwamba, na hivyo ikatokea idadi ya watu mchanganyiko ambao walitokana sana-sana na Walowezi Wamoori, Wahispania, Waingereza, Waebrania, na Wagenoe. Walio wengi zaidi kati ya idadi hiyo sasa wanasema Kihispania na Kiingereza.
Ukweli wa Biblia Wafika Gibraltar
Katika nyakati za kisasa, mbegu za ukweli wa Biblia zilipandwa mara ya kwanza katika Gibraltar katika kiangazi cha 1958. Mashahidi wa Yehova waliokuwa wakisafiri kuhudhuria mkusanyiko mmoja katika London, Uingereza, walitumia vizuri kituo chao cha muda katika Gibraltar ili wahubiri habari njema za ufalme. Wakaaji fulani walikubali kufanya maandikisho ya Mnara wa Mlinzi.
Mume na mke wamisionari walifika katika Gibraltar mwaka uliofuata ili kutilia “mbegu” hizo maji. Lakini wenye mamlaka walijiacha waongozwe na mkazo uliotokana na viongozi wa kidini na wakafukuza mume na mke huyo baada ya miaka miwili. Hata hivyo, kikundi kidogo cha Mashahidi kama 25 kilikuwa kimefanyizwa, na kazi yao ya uaminifu kwa muda wa miaka yote hiyo imethawabishwa kwa kuendelea-endelea tu kupata ongezeko, wakifikia watangazaji wa Ufalme 132 katika Machi 1987. Kwa uhakika, ukuzi huo umeshuhudia kwamba kundi hilo lina uvumilivu katika kuelekeana na matatizo ya namna ambayo inapatikana Gibraltar tu.
Kuwa Mbali na Watu Wengine —Tatizo Lisilo na Kifani
Zaidi ya kuwa na matatizo ya kiuchumi na kijamii ambayo yalitokea baada ya mpaka kufungwa, Mashahidi wa Yehova walipata kizuizi kibaya sana cha kutoshirikiana pamoja na wengine wa imani yao katika makundi ya ujirani katika Hispania. Hata hivyo, wakati wa ile miaka 13 ya nchi kuwekewa vizuizi ili watu wasiende bara, wao hawakukosa chakula kinono cha kiroho kilichotolewa kwenye makusanyiko ya mizunguko na mikusanyiko ya Wilaya. Sikuzote programu ilirudiwa baadaye kwenye Jumba la Ufalme la kwao katika Gibraltar.
Hali hiyo ya kulazimishwa kuwa mbali na wengine ilitokeza jaribu la pekee kwa wenye umri mdogo zaidi kundini. Kwa sababu ya kuwa wamezuiliwa wasitoke lile eneo la Gibraltar la kilometa za mraba 5.8, wao walilazimika kutenda kwa hekima ili kuelekeana na maswali ya utukuzo wa taifa, ufuatiaji wa vitu vya kimwili, na ndoa.
Ati ndoa? Ndiyo, kwa maana kuzuiliwa wawe pale tu penye kundi lao dogo kulipunguza nafasi yao ya kupata mwenzi wa ndoa anayefaa. Washiriki wa kike wa kundi waliletewa mialiko mingi sana na vijana walimwengu ambao walitaka kufanya matembezi nao. Mashahidi vijana hao katika Gibraltar walipaswa kuthamini mioyoni shauri lenye hekima la Biblia “kufunga ndoa katika Bwana tu.”—1 Wakorintho 7:39, NW; linganisha Mwanzo 24:1-4.
Katika kisa kimoja Shahidi kijana, kwa kupuuza shauri kutoka kwa Mtungaji wa ndoa, alianza kufanya matembezi na msichana wa eneo la kwao ambaye hakuwa mshiriki wa kundi. Lakini msaada wa wazee wenye subira katika kundi ulifanya yeye afikiri kwa uzito zaidi juu ya hatari zilizohusika. Hatimaye, yeye alifikia rafiki-msichana wake na kumwambia kwamba ingawa yeye alihisi akiwa na shauku nyingi sana kwa ajili yake, maarifa yake juu ya Biblia yalimpa wajibu wa kukomesha uhusiano wao. ‘Mimi nataka kuoa msichana ambaye naweza kuishi pamoja naye milele, si kwa miaka michache tu,’ yeye akaeleza.
Ingawa msichana yule alishangaa na kuudhika, yeye alivutwa sana akataka kujua ni nini hasa kingeweza kupendeza mvulana huyo zaidi ya uandamani wake. Mwishowe msichana huyo alianza kujifunza Biblia. Jambo ambalo lilianza kama udadisi lilichipuka likawa kupendezwa halisi, na yeye alifanya maendeleo ya haraka sana katika ukweli na kubatizwa. Baada ya wonyesho huo wa wazi wa tamaa yake kutumikia Yehova, ndugu yule alifanya upya uchumba. Muda fulani baadaye wao walifunga ndoa kwa furaha, wakivuna baraka ya kufuata mashauri ya Yehova yenye hekima juu ya ndoa.
Kufunguliwa kwa Mpaka Kwaongoza Kwenye Ongezeko la Kitheokrasi
Desemba 14, 1982, iliona lango likifunguliwa liwe likitumiwa na watembea-kwa-miguu mpakani. Halafu katika Februari 6, 1985, ruhusa kamili ya kupita mpakani ilirudishwa. Halaiki ya watu iliingia katika mazingira ya kutulia zaidi. Kwa kutumia kwa faida tukio hilo, kundi la mahali hapo liliongeza kazi yao ya kutoa ushuhuda na kutumia zile pindi kukutana pamoja katika makusanyiko makubwa zaidi. Sasa watu wenye nia nzuri walipata nafasi kubwa zaidi za kuja kuujua upendo na upatani ambao umo miongoni mwa makutano yaliyokusanyika pamoja ya watu wa Yehova.
Mathalani, mwanamume mmoja ambaye mke wake alikuwa amekuwa Shahidi kwa miaka kama 20 aliamua kukubali mwaliko wa kuandamana na mke wake na watoto walipokuwa wakihudhuria kusanyiko la mzunguko katika Hispania. Yeye alifurahia sana programu na ushirika hivi kwamba akaamua kubaki kwa ajili ya siku ya pili. Wakati kusanyiko lilipomalizika, yeye alitokezewa toleo la funzo la nyumbani la Biblia. “Kwa sababu gani nisijifunze?” Yeye akajibu, akiongeza, “Namna gani tukianza juma hili?” Mke wake, baada ya miaka mingi ya kusali kwa tokeo kama hilo, alifurahi sana sana.
Ili kufanya utumizi kamili wa nafasi za ziada za kuhubiri, hesabu ya Mashahidi wenye kutumikia wakiwa mapainia wasaidizi (wale wanaotoa saa 60 kwa mwezi kwenye huduma ya peupe) iliongezeka. Utendaji huo wa juhudi umetokeza ongezeko la asilimia 35 katika kundi tangu 1982.
Kutoa ushuhuda wa vivi hivi kumeshiriki sehemu kubwa pia katika ukuzi wa kundi. Mashahidi wawili wenye kufanya ukaguzi kwenye bandari wakati wa kazi yao ya kimwili waliona Biblia ya New World Translation ambayo ilikuwa ikionekana kidogo tu Kupitia shimo dogo la mashua inayotumiwa kwa mwendo wa kasi. Bila kukawia, wao walitafuta mwenyewe. Kumbe alikuwa ndiye mkubwa wa kibandari hicho cha kuegeshea mashua, ambaye alikuwa amejifunza pamoja na Mashahidi wa Yehova katika Uingereza kabla ya kuja hivi majuzi kukaa katika Gibraltar. Kwa utayari yeye alifanya upya funzo lake na akafanya maendeleo ya haraka sana pamoja na mwandamani wake wa kike. Baada ya muda mfupi wao walihalalisha hali yao ya ndoa na wakabatizwa. Mume na mke huyo Waingereza sasa wanatoa mwingi wa wakati wanaotumia katika huduma wakifanya kazi miongoni mwa jumuiya ya watu wanaosema Kiingereza na wametumika kama vyombo vya kufanyiza kikundi cha funzo humo.
Funzo moja la Biblia ambalo wao walianza lilikuwa pamoja na Tim na Tracy, vijana waliofunga ndoa wenye kuishi katika majengo ya kijeshi. Ingawa Tim alikuwa mpuliza-tromboni katika kikundi cha waimbaji wanajeshi, yeye alipiga moyo konde kujitolea kabisa masilahi za amani za Ufalme wa Yehova. Watu wa ukoo walileta mkazo juu ya vijana wawili hao, wakiwahimiza waache kushirikiana pamoja na Mashahidi. Hata hivyo, wao waliendelea na funzo lao la Biblia na wakawa imara zaidi katika imani yao.
Tim alifanya ombi kwamba afutwe kazi yake, ingawa yeye hapo kwanza alikuwa amejiandikisha atumikie kwa muhula wa miaka sita. Wakati kuangaliwa kwa kisa chake kulipoonekana kunakawia bila sababu, Tim alichukua hatua ya kwanza kusema na daktari wa kijeshi, akimweleza kwamba wasiwasi wa kukosa uhakika juu ya wakati ujao wao ulikuwa na matokeo mabaya juu ya mke wake. Daktari alikubaliana naye na akatumia mavutano ya cheo chake kuharakisha kuangaliwa kwa kisa hicho. Baada ya muda mfupi Tim alihamishwa kurudi Uingereza pamoja na kikundi chake, ambako yeye hatimaye alifaulu kufutwa kazi hiyo. Sasa wote wawili wanatumikia wakiwa Mashahidi walio wakfu.
Mataraja ya Wakati Ujao
Kwa kuwa mpaka umefunguliwa, Mashahidi katika Gibraltar wameweza pia kuyapa msaada makundi ya Kihispania yaliyo karibu. Wao wanahubiri kando kando ya ile Costa del Sol (Pwani ya Jua) yenye sifa kubwa, ambako watu wengi wanaosema Kiingereza wanapatikana.
Ingawa lile “swali la Gibraltar” lingali linabaki bila kutatuliwa kulingana na maoni ya kisiasa, Mashahidi wa Yehova katika Gibraltar na Hispania wana umoja kamili kiroho, kama ilivyo duniani pote. Wao wanatia itibari yao katika ule “Mwamba” ambao nguvu zao ni za milele, wakirudia kuyasema maneno ya mtunga zaburi “Enyi njoni na mwache sisi tulie kwa kupaaza sauti ya furaha kwa Yehova! Acheni sisi tupige kelele kwa shangwe ya ushindi kwa Mwamba wetu wa wokovu.”—Zaburi 95:1, NW.