Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w88 7/15 kur. 26-29
  • Safari Yetu Isiyosahaulika ya Kwenda Vanuatu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Safari Yetu Isiyosahaulika ya Kwenda Vanuatu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Vichwa vidogo
  • Mkusanyiko Katika Port-Vila
  • Kukutana na “Wanamba Wadogo”
  • Kuokoka Kimbunga Kilichoitwa Uma
  • Matokeo ya Baadaye
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
w88 7/15 kur. 26-29

Safari Yetu Isiyosahaulika ya Kwenda Vanuatu

NDEGE yetu ilipoondoka kwenye kituo cha ndege cha Port-Vila ili kuturudisha Noumea, New Caledonia, tulianza kung’amua kwamba mengi ya yale tuliyopata katika safari yetu yalikuwa yasiyotazamiwa. Yaliyokuwa yamepigwa chapa katika kumbukumbu letu hayakuwa tu yale ambayo tungeona kwa macho na sauti za visiwa vyenye kupendeza vya Vanuatu na watu wavyo wenye moyo mchangamfu bali pia ono lenye kuhuzunisha la kuokoka kimbunga chenye kukumba kwenye kisiwa cha kitropiki.

Vanuatu ni kikundi chenye umbo la Y chenye visiwa vinavyokaribia 80 katika Pasifiki ya kusini-magharibi, karibu kilometa 400 kaskazini mashariki mwa New Caledonia. Katika visiwa hivyo kuna mashahidi wa Yehova wenzetu 84 ambao wametawanyika katika makundi mawili. Mke wangu pamoja nami tulisisimuka sana wakati mipango ilipofanywa ili tuwatembelee. Kiasili, maswali mengi yalizuka akilini mwetu. Tungekabiliana na hali gani? Wanavisiwa ni watu wa aina gani? Na ya maana zaidi, wangeitikiaje habari njema za Ufalme?

Mkusanyiko Katika Port-Vila

Tulikuwa na wasiwasi kidogo tulipopata kujua kwamba ingawa wakaaji walio wengi ni wa kabila la Melanesia, kulikuwa na zaidi ya lugha mia moja zilizozungumzwa katika bahari hiyo yenye visiwa vidogo-vidogo. Lakini tulitulizwa kujua kwamba aina fulani ya Kiingereza cha kuvunjia kinachoitwa Bislama ni lugha ya kawaida. Kwa hiyo hakungekuwa na tatizo kubwa kupashana habari na watu hao.

Kituo chetu cha kwanza kilikuwa Port-Vila, jiji kuu la Vanuatu. Tulikuwa tuhudhurie “Amani ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya hapa. Mashahidi wenyeji walifanya kazi kwa bidii ili uwe tayari. Lilikuwa jambo lenye kuchangamsha moyo kukutana na wajumbe kutoka visiwa vya mbali ambao walilazimika kuweka pesa kwa miezi mingi ili wasafiri.

Jumba la mkutano lilijaa kuanzia siku ya kwanza ya mkusanyiko huo. Zaidi ya watu 300 walikuja kuona drama za Biblia zilizoigizwa kupitia kwa kanda za vidyo. Hilo lilikuwa jambo lenye kutokeza, tukikumbuka kwamba kuna wahubiri wa Ufalme 84 tu katika visiwa vyote hivyo. Hakika, Yehova anatayarisha mavuno mazuri katika mahali hapo padogo-padogo kwenye dunia katikati ya Bahari ya Pasifiki.

Kukutana na “Wanamba Wadogo”

Siku iliyofuata, ndugu mmoja mzaliwa wa huko pamoja nami tulichukua ndege ndogo na kuelekea kisiwa cha Malekula. Baada ya safari isiyopendeza na yenye msukosuko, tulitua kwenye Ghuba la Kusini Magharibi. Mwandamani wangu alienda kumtafuta binamu wake ili apate merikebu kwa ajili yetu. Hiyo ndiyo iliyokuwa njia ya pekee kufikia kijiji cha Letokas, kikomo cha safari yetu.

Tulipoondoka katika merikebu yetu na kufuata mpaka wa pwani, niligutushwa na uzuri wa asili wa kisiwa hicho. Miinuko iliyochongoka ya milima yenye kuingia katika bahari ilikuwa yenye kutisha. Mimea mibichi-mibichi ilikuwa kila mahali, ilijaa maua yenye rangi angavu au ilifunikwa kwa mimea yenye kutambaa, dege la watoto, na mimea yenye maua yenye kupendeza. Ndege wenye rangi zenye kupendeza waliruka-ruka kutoka mti mmoja kwenda kwenye mti mwingine, kama ndege anayeitwa kokonati lori.

Kutoka kwenye merikebu yetu tungeweza pia kuona uzuri wa bahari hiyo​—matumbawe, maghala ya kidesturi ya wanavisiwa hao. Watu kutoka sehemu zote za ulimwengu huja kupiga mbizi na kustaajabia uzuri wa matumbawe na samaki wa kitropiki. Kuna shaza na kamba kwa wingi, na wazaliwa wa huko huwavua na kuwanasa kwa ajili ya chakula.

Baada ya muda mfupi tuliona moshi ukivuka kutoka kwenye shamba la minazi kwa mbali. Huo ulionyesha kwamba tumefikia mwisho wa safari yetu, ghuba ndogo lenye kupendeza karibu na Ghuba la Mianzi. Tulipokaribia ukingo wa bahari, pompoo wengi walicheza kutuzunguka sisi. Halafu tuliona wanaume fulani wakiwa na uta na mishale wakifanya ishara nyingi za msisimuko. Miongoni mwao, tuliwaona ndugu zetu, wakishangilia kuja kwetu.

Hawa walikuwa Wanamba Wadogo wa Malekula ya kusini, mojapo ya kabila lililotengwa katika Pasifiki ya Kusini. Wanakaa katika vijiji vidogo katika milima-milima mwendo wa siku chache kutoka pwani. Wanaume walikuwa wakivaa “namba,” vazi lenye kufunika kiuno ambalo limetengenezwa kutoka kwa matawi yakiwa yameunganishwa kwa mshipi wa ganda. Wanawake wanavaa skati fupi za nyasi. Katika kila kijiji, kwa kawaida kuna kituo cha katikati cha sherehe ambapo dansi za kutoa dhabihu na ibada nyingine zinafanyiwa. Ingawa wengi wa wanavijiji hivyo wamechagua kufuata njia ya maisha ya Magharibi, mazoea ya ushirikina na kuwasiliana na ulimwengu wa roho yangali ya kawaida.

Ilifurahisha kukutana na akina ndugu na kuwasalimu. Wanaume walikuwa wenye mwili mdogo lakini wenye nguvu sana. Kuona haya kwao kwa asili na kuonyesha kwao fadhili kuligusa moyo wangu. Watoto fulani fulani waliniogopa mimi kwa kuwa walio wengi wa watu weupe ambao wao walijua walikuwa madaktari, na watoto wangekumbuka vizuri sana zile sindano walizopokea!

Kijiji kiligawanywa katikati mara mbili kwa shamba dogo la minazi. Nusu ya sehemu ya kisiwa iliwekewa wale ambao walikubali ukweli na upesi nilielewa sababu ya jambo hilo. Ili kuchukua msimamo upande wa ukweli na kuendeleza funzo lao la Biblia, inakuwa lazima watu fulani fulani waishi wakiwa wamejitenga kutoka kwa wanakijiji wale wengine.

Vibanda vimejengwa juu ya mafungu ya mianzi. Tulipoingia katika kimojapo, mara moja niliathiriwa na moshi mzito sana kutoka kwa moto uliokuwa katikati ya chumba hicho. Moshi huo ulifanya macho yangu yawashe-washe, lakini angalau ulifukuza umbu na inzi. Katika kibanda kingine kidogo kilichokuwa karibu, mwanamke mmoja alikuwa akishughulikia kipande cha buluk, au nyama, kilichokuwa kimetandazwa kwenye matawi ya laplap, kilikuwa cheusi kwa kufunikwa na inzi.

Tuliwaalika watu hao kwenye onyesho la slaidi jioni ya Jumatano. Ilikuwa programu kuhusu historia ya Mashahidi wa Yehova yenye kichwa “Kusonga Mbele Ulimwenguni Pote Ijapokuwa Mnyanyaso.” Mmoja wa wahubiri alikuwa ametangulia mbele katika safari ya siku moja ili kuwaalika wanavijiji fulani fulani katika milima. Mimi nilitamani sana kuona kama wangalikuja. Kufikia giza la jioni, mwanamume mmoja kijana aliwasili akiwa na uta na mishale yake. Alifuatwa na watu wengine kadhaa. Mimi nilisisimuka sana kuona kwamba mwendo wa safari haukuwazuia wasifike kwenye mkutano huu.

Upesi tulizungukwa na mishale na nyuta. Karibu watu 80 walikuja, na tukaanza kuonyesha slaidi. Ilichekesha kusikiliza kelele ndogo ambazo wangefanya kwa ulimi wao waliposhangazwa na jambo fulani waliloona katika slaidi.

Baada ya programu ya slaidi, mazungumzo yalikuwa juu ya desturi na mazoea ya wazaliwa wa huko hasa. Wanavijiji walisikiliza kwa umakini na kwa mteremo wakakubali onyo la Biblia dhidi ya mashetani kwenye 1 Wakorintho 10:20, 21. Kwa muda fulani, walikuwa wamepinga jitihada za wamisionari wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo za kujaribu kuwafanya wafuate inayoitwa eti njia ya maisha ya Kikristo. Kwa sehemu hii ilikuwa kwa sababu hawakukubaliana na mafundisho fulani ya kidini yaliyofunzwa na wamisionari hao na kwa sehemu ilikuwa kwa sababu waligutushwa na mwenendo wa watu fulani waliojidai kuwa Wakristo. Sasa, wanavijiji walifurahi kujifunza juu ya ahadi ya Mungu kurudisha paradiso ya kidunia na kuwafufua wafu. Sikuwa na budi ila kuyafikiria maneno ya Yesu kwenye Yohana 8:32: “Tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.”

Imani ya watu hao na upendo wao kwa ajili ya Biblia ilimaanisha pia upinzani kwao. Machifu fulani wa kidini waliwalazimisha wenyeji hao kupigilia broshua zetu kwenye milango yao kwa misumari kama ishara inayomaanisha ‘hatuzitaka hapa.’ Lakini mkazo wa aina hii uliwafanya wenye nyumba fulani watake funzo la Biblia ili wapate kujua ukweli. Lilikuwa jambo gumu sana kwangu kuwaacha rafiki wazuri hao ambao wanapenda ukweli. Mimi niliahidi kwamba ningerudi na kutembelea kijiji chao kule juu milimani.

Kuokoka Kimbunga Kilichoitwa Uma

Safari yetu ilitia ndani kituo katika Espiritu Santo, kisiwa kingine upande wa kaskazini katika Vanuatu. Huko tulitembelea Kundi la Luganville. Ingawa kulikuwa na mzee mmoja tu katika kundi hilo, kuna roho nzuri miongoni mwa marafiki. Kwenye hotuba ya Biblia Jumapili, sisi sote tulishangaa kwa kupendezwa kuona watu 150, hesabu iliyokuwa mara tatu ya hesabu ya wahubiri wa Ufalme

Tulihitaji kurudi Port-Vila ili tuchukue ndege ambayo ingetupeleka nyumbani kule Noumea, New Caledonia. Tulipokuwa Port-Vila, tulipata habari alasiri ya Ijumaa kwamba kimbunga kilichoitwa Uma kilikuwa njiani. Watu hawakushangaa sana, kwa kuwa hali ya anga ya aina hii ni ya kawaida sana wakati huo wa mwaka. Kisha ikaripotiwa kwamba kimbunga kingewasili saa 1.00 jioni. Mara moja tulipeleka habari kupitia redio ya mahali hapo kwamba mikutano yetu ingeahirishwa. Nami nilikuwa na wasiwasi kidogo juu ya safari yetu ya kurudi Noumea Jumapili.

Kufikia 11:30 jioni, upepo ulikuwa umekuwa wenye nguvu sana hivi kwamba ukaanza kuvunja-vunja madirisha fulani. Tulig’amua kwamba tulihitaji kukinga madirisha na milango ili upepo usiingie ndani na kuondoa paa. Godoro, vitanda, dawati, na meza zilirundikwa kwenye madirisha na milango. Tungeweza kuhisi kani ya upepo ikipiga nyumba kwa nguvu, lakini kwa furaha kila kitu kilisimama. Baadaye, tulipata kujua kwamba pepo hizo zilivuma kwa mwendo wa kilometa 240 kwa saa usiku huo.

Mara hali ikatulia. Tulitumia nafasi hii nasi tukatoka nje kwa haraka ili tuone wale Mashahidi walioshi mlango uliofuata walikuwaje. Tulishangaa kupata miti kwenye ua lao ilikuwa ikiwa imepasuliwa na ukuta wa chumba kimoja umebomoka. Wale akina dada watatu walikuwa wameketi kwa wasiwasi katika chumba kingine, wakingojea msaada. Tulianza kujiuliza jinsi ndugu zetu wale wengine walivyokuwa. Sisi sote tulisali kwa Yehova ili awahifadhi.

Kufikia usiku wa manane, baada ya karibu saa nane zenye kuchosha, kimbunga hicho kilikuwa kikielekea kusini mwa bahari hiyo yenye visiwa vidogo-vidogo. Lakini umeme na mvua viliendelea. Kwa mimuliko iliyoendelea, tungeweza kuona mabati ya kuezekea ikipeperushwa kila mahali. Na mara mvua ikaanza kunyesha ndani ya nyumba. Sasa ilikuwa saa 8:30 asubuhi, nasi tukaamua kwamba lazima twende kuona ndugu zetu walikuwaje.

Matokeo ya Baadaye

Majani na matawi, vipande vidogo-vidogo vya fanicha, mabati na vyombo vya nyumbani vilikuwa vimetapakaa barabarani. Nguzo za chuma za taa zilikuwa zimekunjwa-kunjwa na kuangushwa chini. Tulihitaji kutafuta-tafuta njia kupitia udongo wa nyumba zilizobomoka-bomoka. Mwono mbaya wa kuachwa ukiwa ulikuwa mbele ya macho yetu. Kisha tukapata mwangalizi msimamizi wa mahali hapo na jamaa yake wakitetemeka-tetemeka kwenye gari lao ndogo. Paa ya nyumba yao ilikuwa imebomolewa na kimbunga hicho na nyumba ilikuwa imeharibiwa. Lilikuwa jambo lenye kutuliza kuwapata wakiwa salama bila madhara.

Kimbunga hicho kilithibitika kuwa chenye kukumba sana ambacho Vanuatu ilikuwa imepata kuona kwa miaka 25. Meli zote zilikwama mwambani kwa sababu ya bahari zenye msukosuko, nasi tulipata kujua kwamba watu 46 walikuwa wameuawa au hawakupatikana, wengi wao wakiwa wale waliokuwa ndani ya meli. Karibu watu 4,000 walipoteza maskani yao, na hasara ya mimea na kuharibika kwa mali ilikadiriwa kuwa dola milioni 200. Tulifurahi kujua kwamba hakuna ndugu zetu ambao waliuawa wala kujeruhiwa.

Mara moja, halmashauri ya kutoa msaada ikaanzishwa. Mashahidi wa Yehova walio katika New Caledonia walipeleka zaidi ya pauni elfu moja za chakula, mavazi, na vifaa vingine vya kusaidia akina ndugu wajenge upya maskani zao. Kikundi cha watu wenye kupendezwa upande ule mwingine wa kisiwa walitukumbatia walipotuona. Mimea yao ilikuwa imeangamizwa, na ni kibanda kimoja kilichojengwa kwa mtindo wa zamani kilichoshinda dhoruba hiyo. Tulihakikisha kwamba wana chakula cha kutosha siku mbili kisha tukarudi Port-Vila.

Mamlaka ya mahali hapo ilikuwa pia inaanza kutoa msaada, na msaada kutoka nchi jirani ukaanza kuingia. Mvundo wa vitu vilivyooza ulipoanza kunuka, serikali ilishauri watu wasafishe mji upesi iwezekanavyo. Tulitoa madokezo fulani kuhusu utumizi wa maji ili kuzuia kuenea kwa ugonjwa kama vile homa ya matumbo na kipindu-pindu.

Alhamisi iliyofuata, tuliweza kuonyesha programu ya slaidi nayo ilifurahisha kila mmoja. Baada ya mkutano, tungeweza kusikia uvumi wa mazungumzo miongoni mwa marafiki. Wengi wao walikuwa wangali wakihisi mgutuko wa kupoteza mali yao yote. Lakini kila mtu alionyesha roho ya ajabu ya nia ya kujitoa kusaidia na kutunza mahitaji ya wengine. Lo! wonyesho ulioje wa umoja wa Kikristo!

Hatimaye, wakati wa kuacha ndugu na dada zetu wapendwa ulifika. Tulitiwa moyo sana na upendo na bidii yao. Magumu ambayo tulikuwa tumepata yalivuta sisi karibu mmoja na mwenzake. Ndege yetu ilipoanza mwendo kutoka Port-Vila, tamaa yetu ya moyoni ilikuwa kwamba huenda tukarudi na kuwaona wote tena wakati mwingine.​—Imechangwa.

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 26]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

VANUATU

ESPÍRITU SANTO

Luganville

MALEKULA

EFATE

Port-Vila

NEW CALEDONIA

Nouméa

[Pictures]

Port-Vila, jiji kuu la Vanuatu

Kuhubiria mkazi wa mahali hapo

Kijiji cha asili

[Picha katika ukurasa wa 29]

Waterema kusikia habari njema

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki