Mambo Makubwa Yanatukia Katika Bara Dogo
WEWE unaweza kupata Grand Duchy ya Luxembourg katika ramani yako? Nchi hii ndogo sana imekaa kama kioto pale pale penye makutano ya mipaka ya Ubelgiji, Ufaransa, na Ujeremani. Ingawa ni ndogo, si nchi isiyo na maana hata kidogo. Mji mkuu, Jiji la Luxembourg, ni moja ya sehemu kuu za Jumuiya za Ulaya. Pia ni kitovu mashuhuri kifedha, kukiwa na benki 125 zenye kuwakilishwa huko. Hata hivyo, ile Grand Duchy ya Luxembourg ina eneo la kilometa za mraba 2,586 tu na ina idadi ya wakaaji 372,000 tu!
Basi, inaeleweka ni kwa nini uchangiaji wa Mashahidi wa Yehova katika Luxembourg kwenye kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri Ufalme ni mdogo unapolinganishwa na ule wa Mashahidi katika mataifa makubwa zaidi yanayotuzunguka. Na bado, ukuzi wa kazi ya kuhubiri Ufalme huko unaleta akilini Zekaria 4:10: “Ni nani aliyeidharau siku ya mambo madogo?” Kama vile malaika alivyoambia mnabii huyo Mwebrania, “si kwa uwezo, wala si kwa nguvu, bali ni kwa roho yangu, asema BWANA [Yehova, NW] wa majeshi.” (Zekaria 4:6) Kwa hiyo kazi yetu, hata iwe ya kiasi kidogo kadiri gani, hakika si ya kudharauliwa. Kwa kuongozwa na roho ya Mungu, inamletea yeye sifa.
‘Siku za Mambo Madogo’
Kazi ya kutolea Ufalme ushuhuda ilianza katika Luxembourg wakati Wakristo wachache sana wa kutoka Strasbourg, Ufaransa, walipokuja hapa kati ya 1922 na 1925 ili kugawanya trakti. Wangawa wachache, jumbe zao zilizochapwa zilikuwa na nguvu nyingi. Fikiria vichwa vya trakti hizo: Sai kwa Viongozi wa Ulimwengu, Onyo kwa Wakristo Wote, na Viongozi wa Kanisa Washtakiwa. Ushujaa mwingi ulihitajiwa ili kueneza jumbe hizo, kwa kuwa Grand Duchy ya Luxembourg ilikuwa ya Wakatoliki Waroma kwa asilimia zaidi ya 96 na ilishikwa sana na dini na mapokeo yao.
Wakati wa 1930 na 1931, Photo-Drama of Creation ilionyeshwa katika Luxembourg. Kwa njia fulani, maonyesho na matokeo yayo yanakumbusha mtu huduma ya Yesu. Umati mkubwa wa watu ulisongamana kumzunguka Yesu ili wamsikie akinena na kuona au kupata wenyewe maponyo aliyoyafanya, lakini ni wachache tu waliokuja kuwa wanafunzi wake. (Mathayo 4:23-25; 23:37) Kwenye maonyesho ya Photo-Drama katika Jiji la Luxembourg, jumba lililokuwa limekodiwa lilijaa mpaka nje kila jioni likiwa na umati wa watu 300. Lakini ni wachache waliorudi kwa ajili ya hotuba ya mfuatilio na vile vipindi vya maswali na majibu majuma yaliyofuata. Hapo kwanza, walikuwako watu 20 au 30, baadaye 10, na hatimaye 4. Wachache hao tu ndio waliokuwa na uthamini wa kudumu kwa chakula cha kiroho walichotolewa.
Uvumilio Wavuna Thawabu
Katika 1931 wenyeji wa kwanza wa Luxembourg walianza kazi ya kuhubiri. Hilo halikuwa jambo rahisi. Kanisa Katoliki la Kiroma lilikuwa limetokeza kampeni ya kueneza propaganda za chuki nyingi dhidi ya watu wa Mungu, na likawa na uvutano kwa polisi ili wavuruge huduma yetu ya mlango kwa mlango kwa kadiri ilivyowezekana. Polisi walitunyang’anya fasihi, au wakakamata-kamata akina ndugu kila wakati walipoenda nje katika utumishi wa shambani. Je! sasa mpanuko wa ibada ya kweli katika Grand Duchy ungesimama kabisa? Kinyume kabisa! Mara tu baada ya kufukuzwa nchini kwa August Riedmueller, mhudumu wa kwanza wa wakati wote kufanya kazi nchini, wenyeji kumi wa Luxembourg walibatizwa siku ya Septemba 25, 1932. Walijihusisha katika kazi ya kuhubiri kwa ukawaida, wajapopatwa na magumu ya polisi.
Katika ule mwaka uliotangulia vita wa 1934, wahubiri 15 hapa waligawanya vipande 3,164 vya fasihi ya Biblia. Mara nyingi walikuwa wakisafiri kwa baiskeli mwendo wa kuanzia kilometa 80 hadi 100 kwa siku! Dada mmoja aliripoti hivi: “Baiskeli yangu ilikuwa ‘mwandamani’ wangu wa daima. Kufanya kazi kijiji kimoja baada ya kingine kukaja kuwa ndio utendaji niupendao zaidi, hasa siku za Jumapili.”
Majeshi ya Ujeremani yalivamia Grand Duchy ya Luxembourg katika 1940, yakitumbukiza ndugu zetu katika kipindi cha kufanya kazi ya kisirisiri kwa miaka mitano. Hesabu fulani kati yao walikamatwa. Baada ya kukaa miezi kadhaa gerezani, waliachiliwa kwa kuamrishwa vikali wasiendelee kuhubiri peupe wakiwa Mashahidi wa Yehova. (Ona Matendo 4:17, 18.) Ndugu wawili walipelekwa kwenye kambi za mateso. Hata hivyo, ndugu waliobaki walifanya waliyoweza, na hesabu ya mafunzo ya Biblia ya nyumbani yenye kuongozwa pamoja na watu wenye kupendezwa ikapanda kutoka 6 katika 1942 na kuwa 20 katika 1944. Na ijapokuwa watu 23 waliripoti utumishi wa shambani katika mwaka 1939, mwaka 1946 ulileta kilele kipya cha 30.
Baraka ya Yehova Yaonwa
Katika miongo ya tangu wakati huo, Yehova Mungu ameibariki kwa wingi kazi ya kuhubiri Ufalme katika Luxembourg kwa kuipa ongezeko. Hesabu ya Mashahidi ilikua ikawa kilele cha 1,336 katika 1988. Sasa kuna wastani wa shahidi 1 wa Yehova kwa kila wakaaji 327 wa eneo la tawi letu. Watu zaidi ya 2,900 walihudhuria mwadhimisho wa Mlo wa Jioni wa Bwana siku ya Aprili 1, 1988, hiyo ikiwa ni mtu 1 kwa kila wakaaji 148! Upendezi mwingi unaonyeshwa katika huduma ya wakati wote pia. Kufikia juzijuzi tu 1955, walikuwako wafanya kazi 5 tu wa wakati wote, au mapainia, lakini Mei 1988 iliona jumla ya mapainia 190 shambani!
Ukuzi huo umefanya ihitajiwe kabisa kupanua vifaa vya tawi letu. Ofisi ya tawi ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Biblia na Trakti ilianzishwa hapa katika Septemba 1955 ikiwa na vyumba katika maskani ya faragha. Siku ya Septemba 12, 1987, ofisi ya tawi iliyo mpya na nzuri, yenye vyumba 20 na jengo kubwa ambalo ni Kao la Betheli, ilizinduliwa. Wakati ule ule, maskani nzuri mpya ya kimisionari yenye nyumba tatu na Majumba ya Ufalme mawili iliwekwa wakfu.
Kuhubiri Penye Fursa Zote
Luxembourg ni nchi ya kimataifa kweli kweli. Wenyeji wenyewe wa Luxembourg husema lugha tatu. Hata hivyo, kwa kuwa 1 kati ya kila wakaaji 4 ni wa kutoka nchi fulani ya kigeni, lugha nyingi hunenwa kwa kawaida.
Wageni huja kuzifanyia kazi Jumuiya za Ulaya, zile benki nyingi zilizopo, au katika vibiashara vya kazi za mikono. Kwa hiyo sisi tuna makundi ya Kifaransa, Kiitalia, na Kireno ili kutumikia vikundi hivyo vya lugha za kigeni.
Mmoja wa dada zetu Wareno anaeleza lililotukia katika mruko mmoja wa ndege hivi majuzi: “Nilienda nikiwa na magazeti machache ili nitoe ushuhuda wa hivi hivi ikiwezekana. Kwenye kituo chetu cha kwanza, ndege ilihitaji kutengenezwa mahali fulani. Hakuna aliyeruhusiwa kwenda nje ya ndege. Kwanza sikuwa na ushujaa wa kufanya lile ambalo moyo wangu uliniambia napaswa kufanya. Nilisali tena na tena kwa Yehova ili anipe imara ya kutumia fursa hiyo kwa njia nzuri.
“Baada ya kufikiria mambo kwa muda, niliwaendea watumishi wa ndege nikawauliza kama ningeruhusika niwatolee watu waliomo magazeti fulani ya kutia moyo na kunufaisha. Wakaniruhusu, nami nikapata upendezo mwingi kwa kuweza kuwafikia abiria kwa uhuru, nikitoka safu moja ya viti hadi ile nyingine, sawasawa na kama nilikuwa nikifanya kazi nyumba kwa nyumba. Niliweza kuangushia watu mbalimbali magazeti 12 na kijitabu kimoja na nikawa na maongezi mazuri sana.
“Mtu wa mwisho niliyemfikia alijibu kwa unyenyekevu wa kujionyesha ni mtu wa maana sana akisema kwamba hakuhitaji msaada kwa kuwa yeye ni kasisi Mwevanjeliko. Pia, yeye hakufikiri ilikuwa sawa mimi kuwafikia abiria jinsi hiyo. Kwa busara, mimi nikaendeleza maongezi kwa kutaja mambo yale ya kikawaida tu kuhusu imani katika Mungu na uthamini kwa baraka zote ambazo yeye angeleta juu ya wenye kumwitikadi. Baada ya zungumzo hilo, pasta huyo alinipongeza kwa kuwa na imani na pia kwa ujasiri wangu katika kunena na abiria wote.
“Sasa mtu yule aliyekuwa kando yangu akaanza kuuliza maswali, nasi tukaongea kwa muda wa karibu saa tatu!”
Pia ndugu zetu wameonyesha bidii isiyo ya kawaida katika utumishi wao wa nyumba kwa nyumba. Mwangalizi wa mzunguko mmoja anaripoti juu ya hudhurio katika kundi moja: “Upeo mkubwa ulikuja wakati tulipokusanyika kwa ajili ya utumishi wa shambani asubuhi ya Jumapili. Kati ya wahubiri 109 wanaoshiriki na kundi, 102 walikuwapo ili kushiriki kazi ya kuhubiri! Walitia jitihada bora kabisa kualika watu wenye kupendezwa waje kwenye hotuba ya watu wote alasiri ile, na tokeo ni kwamba jumba lilijaa pomoni likiwa na watu 198! Ilikuwa ndiyo mara ya kwanza kwa wengi wao kuhudhuria mkutano, ingawa kuna Shahidi 1 kwa kila wakaaji 50 katika eneo la kundi hilo!”
Vijana pia wanaonyesha mwelekeo mzuri sana kuelekea fursa zao za kuupigia mbiu ujumbe wa Ufalme. Walipopata habari katika Mnara wa Mlinzi wa Aprili 1, 1985 (Kiingereza) juu ya kutiwa gerezani kwa baadhi ya ndugu zetu katika Uturuki, vijana-matineja wawili waliamua kumtembelea balozi wa Uturuki. Wanaripoti hivi:
“Hatua yetu ya kwanza ilikuwa kupewa mwadi wa kumfikia. Kwanza, mwandishi wake hakutuchukua kwa uzito. Ili tusadikishe bibi huyo kwamba madhumuni yetu yaliongozwa na moyo wa bidii, tulimwonyesha nakala fulani-fulani za gazeti hilo, katika lugha kadhaa, zenye ripoti ile. Kwa kuvutiwa, bibi huyo akayachukua magazeti na kuingia ofisi ya balozi. Baada ya dakika kumi, alirudi akatuambia tungeweza kurudi katika muda wa majuma mawili lakini balozi angebaki na magazeti hayo achunguze yale mashtaka makali yaliyofanywa humo. Sisi tukachukua hiyo kuwa ishara njema.
“Tuliporudi kwenye ubalozi huo kwa ajili ya mwadi wetu, tulimpata balozi akiwa mwenye fadhili na urafiki sana. Alituonyesha ujumbe wa teleksi aliokuwa amepelekea serikali ya Uturuki kuchunguza maelezo kadhaa katika ripoti ya gazeti letu. Yalikuwa yamehakikishwa kuwa kweli na kulipa lalamiko letu uzito mwingi.
“Yeye alivutwa na jambo la kwamba makala hiyo ilikuwa imeandikwa kwa lengo zuri sana, bila kutiwa chumvi wala kuwachambua isivyofaa viongozi wa kisiasa. Sisi tuliweza kuongea naye kwa saa moja na nusu kuhusu enzi kuu ya Mungu, kutokuwamo kwa Kikristo, na kutoweza kwa mwanadamu kutawala mwanadamu mwenzake kwa mafanikio. Yeye akasema ameelewa msimamo wetu na kuuliza angeweza kusaidiaje. Tukadokeza kwamba ajulishe serikali yake kwamba tulikutana naye na kuwaambia fikira yake juu ya shauri lote. Akakubali kufanya hivyo, na akaomba nakala kadhaa za gazeti hilo apelekee wawakilishi mbalimbali wa serikali. Akasema angefanyiza faili ya habari zinazohusika na kujaribu kusaidia vyovyote vile.”
Miezi michache baadaye, Mnara wa Mlinzi uliripoti kwamba Mashahidi katika Uturuki walikuwa wameachiliwa gerezani kwa amri ya Mahakama Kuu Zaidi ya Uturuki. Walipopata habari, wale vijana wanaume walirudi na kupokewa na balozi kwa uchangamfu.
Kutokana na historia ya kazi ya kuupigia mbiu Ufalme hapa katika Grand Duchy ya Luxembourg, tunaona hekima ya kutodharau “siku ya mambo madogo” bali kuitibari katika roho ya Yehova ili impe kila mmoja wetu imara tunayohitaji kufanya penzi lake hadi ukamilisho walo mtukufu. Kwa msaada wa Yehova Mungu, mambo makubwa yamekuwa yakitukia hapa katika eneo letu dogo la tawi la Luxembourg. Sisi tunakuita wewe ambaye hujaanza kufanya hivyo ili ‘umtukuze Yehova’ pamoja nasi na hivyo ‘uonje uone ya kuwa Yehova yu mwema.’—Zaburi 34:3, 8, NW.
[Ramani katika ukurasa wa 25]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
North Sea
Netherlands
Federal Republic of Germany
Belgium
France
Luxembourg
150 km
100 mi
Belgium
Luxembourg
Luxembourg
Federal Republic of Germany
Trier
France
Metz
[Picha katika ukurasa wa 27]
Ingawa amezidi miaka 80, Victor Bruch, ambaye wakati wa Vita ya Ulimwengu 2 alikuwa katika kambi ya mateso, anatumikia akiwa mzee Mkristo