Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w89 3/15 kur. 26-29
  • Kupiga Mbiu ya Ufalme Katika Malesia Yenye Unamna-namna

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kupiga Mbiu ya Ufalme Katika Malesia Yenye Unamna-namna
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Vichwa vidogo
  • Kushinda Lile Tatizo la Dini
  • Kukabiliana na Lugha na Desturi
  • Katika “Bara la Wawinda-vichwa”
  • ‘Mdogo Anakuwa Elfu’
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
w89 3/15 kur. 26-29

Kupiga Mbiu ya Ufalme Katika Malesia Yenye Unamna-namna

MISIKITI yenye kuba zilizopakwa dhahabu, sehemu takatifu zenye matao, makanisa yenye minara iliyochongoka, na zigurati za mahekalu zilizorembwa kwa sanamu. Hiyo ni Malesia, bara lenye dini zote zile kubwa-kubwa nne za ulimwengu. Wakaaji walo 16,000,000 ni Wamalei, Wachina, Wahindi, Wazungu-waesia, Waibani, Wakadazani, na makabila kadhaa ya kienyeji. Labda hakuna mahali penginepo penye unamna-namna mkubwa jinsi hiyo katika dini, utamaduni, desturi, mapokeo, na lugha.

Malesia iko pale juu kidogo tu kaskazini mwa ikweta katika Bahari ya China Kusini, nayo ina visehemu viwili vya kijiografia: ile peninsula iliyokuwa ikiitwa Malaya upande wa magharibi na ile mikoa ya Sabah na Sarawak katika kisiwa cha Borneo upande wa mashariki. Kuanzia nyanda za chini katika pwani yenye mabwawa ya matope-matope, kupita kwenye misitu iliyosongamana miti, ambayo mara nyingi huwa haipenyeki, hadi kwenye vilele vya milima mirefu​—kutia na Mlima Kinabalu wa meta 4,101 katika Sabah​—bara lenyewe lina unamna-namna ulio sawa na ule wa watu na utamaduni walo.

Ni katika hali ya namna hiyo kwamba Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kuhubiri “habari njema hizi za ufalme.” (Mathayo 24:14, NW) Wanaweza kufikiaje watu, zikiwako zile lugha zote, desturi, na mawazo tofauti-tofauti ya kidini? Mtu anahisije kuhubiri ujumbe wa Ufalme katika bara hili? Juu ya yote, Mashahidi wameweza kutimiza nini?

Kushinda Lile Tatizo la Dini

Ili kufikia watu wa malezi tofauti ya kidini, ni lazima wahubiri wa habari njema wajifunze kutofautisha nyumba ya Mwislamu na nyumba ya Mhindu, kutofautisha jamaa ya Kibuddha au ya Kitao na ya Kiprotestanti au ya Kikatoliki. Hilo laweza kufanywaje?

Kuna vionyeshi vilivyo wazi. Kwa kielelezo, madhabahu nyangavu nyekundu ni ishara ya nyumba ya Mtao au Mbuddha kama vile sanamu ya Maria au Yesu ilivyo ishara ya kao la Mkatoliki. Ishara nyingine za jinsi hiyo hiyo ni majani ya miembe kwenye nyumba za Wahindu au maandiko ya Kiarabu yaliyotolewa katika Korani na kuandikwa juu ya nyumba za Kiislamu.

Kutambua malezi ya kidini ya mwenye nyumba ni jambo moja; kumfanya apendezwe na habari njema ni jambo tofauti kabisa. Itikio la kawaida, ambalo huwa kwa mchanganyiko wa Kichina, Kimalei, na Kiingereza, ni: “Semua agama sama lah.” Maneno hayo hufuatwa na, “Samahani, mimi sipendezi.” Kwa tabasamu pana, hapo hapo mwenye nyumba amekuambia kwamba anafikiri dini zote ni hali moja tu na kwamba hapendezwi.

Wamalesia wengi waliozaliwa wakiwa Wabuddha, Watao, au Wahindu wamevutiwa na ule uongofu wa dakika moja unaotolewa na misheni za Jumuiya ya Wakristo na wakajiunga na mafarakano mbalimbali ya Kiprotestanti. Kwa kushawishwa na makasisi wao, wengi wao wamefunga masikio wasisikie habari njema. Na bado, jina kuu na kusudi la Yehova linazidi kupigiwa mbiu kwa uthibitifu katika bara hili lenye unamna-namna.

Kwa sababu ya saburi na uelewevu wa Mashahidi wa Yehova, watu wengi wenye mioyo ya kufuata haki wanaitikia vizuri ujumbe wa Ufalme. Mathalani, fikiria Patrick, aliyekuwa mvuta-sigareti mwenye nywele ndefu zisizochanuliwa. Alizoezwa mbinu za Kichina za kupigana na watu naye akawa akifanya jeuri alipochokozwa. Ingawa hakuwa na kusudi maishani, alivutiwa sana na maneno “mauti haitakuwapo tena,” aliyosomewa na mhubiri wa Ufalme kutoka Ufunuo 21:4. Kwa hiyo Patrick akakubali funzo la Biblia. Kwa kusisimuliwa na ukweli wa Kimaandiko aliokuwa akijifunza, upesi alianza kuusimulia kwa mama yake, kwa barua na yeye binafsi aliporudi nyumbani. Lakini mama yake alipinga sana.

Siku moja, Patrick na mama yake walikuwa wakimtia nidhamu ndugu yake mchanga, ambaye pia alikuwa stadi wa kupigana karate. Ndugu huyo alipoanza kurusha mapigo na mateke, mama huyo alistaajabu kuona kwamba Patrick hakulipa kisasi bali alibaki mtulivu. Akapendezwa sana na hicho ambacho mwana wake alikuwa akijifunza hata kikawa na nguvu za kumgeuza sana. Mama yake alifanya maendeleo ya haraka sana na kubatizwa katika muda wa miezi sita. Yeye, naye, alimpa ushuhuda mama yake wa miaka 73, aliye Mbuddha imara. Bibi huyo pia alithamini tazamio la kuishi milele. Ingawa hakujua kusoma, alianza kujifunza kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, akikariri herufi nyingi za Kichina kwa kadiri alivyoweza. Sasa yeye pia ni mhubiri wa habari njema.

Kukabiliana na Lugha na Desturi

Ili kushughulika na hali hiyo ya kuwako na lugha nyingi, inahitajiwa kuwa na mkoba uliojazwa fasihi wakati wa kuhubiri nyumba kwa nyumba. Lakini hiyo haitatui tatizo sikuzote.

Mathalani, mtu kuwa Mchina na kuwa na fasihi ya Kichina hakumaanishi moja kwa moja kwamba Shahidi anaweza kuwasiliana na mwenye nyumba Mchina. Kwani je! wao huongea lugha moja? Ikiwa Shahidi ni Mhokkien na mwenye nyumba ni Mkantoni, hilo lingeweza kuwa tatizo. Kwa kuwa lahaja ya Kichina hutamka maneno kwa kutegemea hali ya sauti, utofauti mdogo sana wa matamko unaweza kutoa ujumbe tofauti kabisa. Kielezi ni hiki: Ilichekesha sana wakati dada mmoja painia msema Kihokkien alipotembeatembea katika eneo la Kikantoni akiambia watu kwamba yeye ni “mwanafunzi mwenye kichaa” na hali alikusudia kusema ni “mwanafunzi wa Biblia.”

Hata wakati neno lifaalo linapotumiwa, huenda lisimaanishe jambo lile lile kwa kila mtu. Kwa kuwa wanaishi kati ya watu wa rangi nyingi, kwa ujumla Wamalesia wana hisani na hujiangalia wasiudhi mtu yeyote. Hasa ni vigumu sana wao kusema hapana kwa watu wasiowajua. Hivyo, mtu hujifunza kutosisimuka sana wakati mwenye nyumba anaposema ndiyo amekubali mwaliko wa kujifunza Biblia au kwenda kwenye mikutano ya Kikristo. Kwa nini? Kwa sababu hiyo haimaanishi kwa lazima kwamba amekubali jambo lolote. Wakati na ujuzi huhitajiwa ili kuwajua wanaopendezwa kikweli.

Malesia ni miongoni mwa nchi zenye sikukuu na sherehe nyingi zaidi za kidini. Nyakati hizo watu hushughulika sana wakizuru marafiki na watu wa ukoo. Mashahidi Wamalesia huongeza pia utendaji wao na kutumia sikukuu hizo ili kutangaza habari njema. Lakini lazima wafanye hivyo kwa busara na uelewevu ili wawe na matokeo mema.

Mwaka Mpya wa Kichina ni siku ya namna hiyo hasa. Watao huitikadi kwamba wanapaswa kuanzisha mwaka mpya kwa maneno ya fadhili na matendo mema ili kuhakikisha kutakuwa na ufanisi mwaka wote. Siku hiyo, Shahidi ataepuka kutumia maneno kama “kifo,” “ugonjwa,” na “maumivu.” Badala ya hivyo, atataja-taja habari za kufurahisha, kama “kuishi milele katika afya njema pamoja na amani na ufanisi wa kudumu katika ulimwengu mpya.” Sikukuu hiyo sio wakati wa kukumbusha watu ole zao.

Katika “Bara la Wawinda-vichwa”

Kwa kuwa “umati mkubwa” ni wa watu mmoja mmoja “kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na ndimi,” ni sharti tuyafikirie makabila mengi ya uenyeji wa Malesia Mashariki. (Ufunuo 7:9) Inatia moyo kuona kwamba hesabu inayoongezeka ya wakaaji wa Sarawak​—ambalo hapo kwanza lilijulikana kuwa Bara la Wawinda-vichwa​—wanaitikia ujumbe wa Ufalme.

Kwa kielelezo, katika mji wenye mafuta wa Miri, katika Sarawak, miaka minne iliyopita walikuwako wahubiri watatu tu wa Ufalme. Leo, wengi wanaonyesha wanapendezwa kujifunza juu ya Biblia. Dada mmoja painia anaripoti mafunzo 17 ya Biblia, na baadhi ya wanafunzi wake wanaongoza mafunzo wao wenyewe pamoja na watu wanaopendezwa. Sasa kuna kundi lenye kusitawi katika mji huo mdogo wa Miri.

Jambo la namna ya pekee kuhusu Waiban wa Sarawak ni ile nyumba-ndefu. Jengo hilo refu lenye kushikiliwa na miguu mirefu ya miti hujengwa kwa magogo ya miti mikavu na makuti. Kwa kawaida hujengwa kwenye ukingo wa mto karibu-karibu na msitu, nalo huwa na safu ya makao 30 hadi 40 au zaidi yaliyo upande huu na huu wa kijia kimoja kinachopita hapo katikati. Sehemu kubwa ya kazi yetu ya kuhubiri hufanywa katika eneo la namna hiyo.

Pindi moja, hotuba ya Biblia juu ya “Kuna Tumaini Gani kwa Wafu?” ilipasa kutolewa kwenye moja ya hizo nyumba-ndefu. Jumbe wa mtaa (au, tuai rumah) alikusanya watu wote ndani ya ruai, au jumba la watu wote. Kila mtu alisikiliza kwa uungwana na kwa unyamavu kabisa mpaka hotuba ikamalizika. Halafu, mwanamume mmoja akauliza hivi: “Yawezaje kuwa wafu hawajui kitu?” Mwingine akasisitiza kwamba tayari watu wema wamo mbinguni na wabaya wamo katika moto wa mateso. Lakini baadhi yao walivutiwa na tazamio la kuishi milele katika dunia-paradiso wakataka kujua mengi zaidi. Ilikuwa sawa na wakati Paulo aliponena kwa Waathene juu ya Areopago.​—Matendo 17:32-34.

Katika nyumba-ndefu nyingine ndimo alimoishi Juing Insoll, Mwiban wa miaka 72 aliyekuwa wa Kanisa Anglikana. Akiwa kijana, alitatanishwa na maswali kama haya: Mungu mwenye upendo awezaje kutesa-tesa wafu milele katika moto wa mateso? Ikiwa kuna Mungu, mbona ukosefu wa haki ni mwingi sana? Hakuna mtu aliyeweza kumpa majibu ya kuridhisha. Siku moja, rafiki yake mmoja mwenye kutoka jijini alijipatia nakala ya kitabu Kweli Iongozayo kwenye Uzima wa Milele. Kwa kuona kwamba kingeweza kujibu maswali ya Juing, rafiki huyo alimwazima kitabu hicho. Ulikuwa upendezo kama nini kwa Juing! Hatimaye, baada ya miaka 60 ya kutafuta, akawa ameupata ukweli juu ya Mungu!

Juing alipiga moyo konde apate nakala yake mwenyewe ya kitabu hicho. Alisafiri kilometa 240 kwenda Kuching, mji mkuu wa Sarawak, na kukitafuta-tafuta katika maduka ya vitabu. Hakuona hata dalili ya kitabu hicho. Usiku huo, akiwa katika nyumba ya mtu wa ukoo, akasikia kwamba mtu mwingine wa ukoo alikuwa na nakala. Alielekezwa kwenye Jumba la Ufalme la huko akajipatia vichapo 15 tofauti arudi navyo kwenye nyumba-ndefu yake.

Baada ya kusoma habari zote hizo, Juing alirudi jijini, akiomba kubatizwa. Wazee walitabasamu na kutikisa vichwa. Hata hivyo, upesi wakashangaa kugundua kwamba alistahili kabisa. Kwa hiyo, yeye kabatizwa! Aliporudi katika ile nyumba-ndefu, akiwa na furushi kubwa la fasihi zaidi ya Biblia, Juing alianza kuhubiria jirani zake. Kwanza, alishangaa ni kwa nini rafiki zake hawakukubali ukweli mara baada ya kuvisoma vitabu. Lakini upesi akang’amua kwamba alipaswa kujifunza Biblia pamoja nao. Sikuzote Juing alipotoa ripoti ya utumishi wa shambani aliijaza sana tarakimu na tarehe nyingi ikawa kama kijitabu cha kuhesabia tarehe!

Kutoka mji ulio pekee wa Lahad Datu katika mkoa wa Sabah ilikuja ripoti hii: Mwanamke kijana aliyeolewa mwenye watoto watatu alijifunza ukweli kupitia funzo la Biblia lililoongozwa kwa barua na dada mmoja katika Kota Kinabalu, mji mkuu wa mkoa huo. Mwishowe, mwanamke huyo aliamua kubatizwa kwenye kusanyiko la mzunguko. Hata hivyo, hotuba ya ubatizo ilipokuwa katikati, mume wake aliingia ndani kwa kishindo na kudai mke wake arudi naye nyumbani.

Waliporudi nyumbani, mume akajaribu kumwomba radhi lakini wapi. Mwishowe, akapaaza sauti hivi: “Sasa, wataka nini?” “Mimi nataka kubatizwa,” mke wake akajibu. “Kwani ni jambo la maana sana kwako?” mume akauliza. “Ndiyo, hiyo ndiyo pindi ya maana kuliko zote maishani mwangu.” “Haya!” mume akaitikia mwishowe. “Mwite mzee wenu. Nitakujengea kidimbwi cha kuogelea ili ubatizwe hapa.”

Mwanamume huyo alifanya sawasawa na maneno yake. Na mke wake akabatizwa wakati wa ziara iliyofuata ya mwangalizi wa mzunguko​—katika kidimbwi cha kuogelea alichojengewa na mume wake! Lakini ni nini kilichompa dada huyo hali hiyo ya kupiga moyo konde? Basi, ingawa yeye alikuwa mahali pa upekee, alitayarisha kwa ukawaida habari zote za mikutano ile tofauti-tofauti. Ikiwa wakati wowote alikosa “mkutano” mmoja, alihisi kama kwamba alikuwa amekosa mlo mmoja. Sasa dada huyu anafundisha watoto wake na kuongoza mafunzo matatu ya nyumbani ya Biblia.

‘Mdogo Anakuwa Elfu’

Kazi ya Ufalme katika Malesia ilifunguliwa na Alfred na Thelma Wicke, walioenda huko kutoka Australia katika 1939. Utumishi wao mwaminifu wa kimisionari umerefuka ukawa karibu miaka 50, na Yehova amebariki sana jitihada zao! Tangu kuanzishwa kwa ofisi ya tawi katika Penang katika 1972, huku Ndugu Wicke akiwa mwangalizi wa tawi, kazi ya kuhubiri katika Malesia imeongezeka mwendo. Wakati huo, walikuwako wahubiri wa Ufalme 207. Miaka kumi baadaye, hesabu hiyo imekuwa maradufu. Kwa hiyo, katika Julai 1983, tawi lilihamishwa likapelekwa Klang, jiji lenye kibandari karibu na mji mkuu wa serikali, Kuala Lumpur. Uwanja mpya wa tawi una safu moja ya majengo matatu yenye ghorofa mbili, inayofaa sana mahitaji ya sasa. (Ona ukurasa 26.)

Miaka michache iliyopita, jitihada zaidi zilifanywa kuwapelekea ujumbe wa Ufalme wakaaji wengi zaidi wenye kusema Kichina na Kitamil. Sasa, zaidi ya kuwako makundi mawili ya Kichina, kuna vikundi vya Kichina na Kitamil katika makundi mengine kadhaa na pia kikundi cha Kijapani kinachositawi cha karibu watu 20.

Katika eneo lote, sasa kuna makundi 20, yakiwa na wahubiri karibu 900 wa Ufalme. Hiyo inafanya uwiano uwe ni mhubiri 1 kwa watu 18,500. Kwa hiyo kungali kuna kazi nyingi ya kufanywa. Kuonyesha ni ukuzi gani unaoweza kuwako, watu 2,633 walikuja kwenye mwadhimisho wa Ukumbusho wa 1988. Hiyo iliwafurahisha sana Mashahidi Wamalesia, na wengi zaidi wanajitahidi kuifikia huduma ya wakati wote. Ndiyo, tena Mashahidi wa Yehova katika Malesia wana hamu nyingi wakitazamia kuifikia alama ya kuwa wahubiri 1,000. Wanaikumbuka vizuri ahadi ya Yehova: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, Bwana [Yehova, NW], nitayahimiza hayo wakati wake.”​—Isaya 60:22.

[Ramani katika ukurasa wa 26]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

THAILAND

MALAYSIA

Penang

Kuala Lumpur

Klang

Singapore

MALAY PENINSULA

SUMATRA

EQUATOR

South China Sea

PHILIPPINES

SABAH

Kota Kinabalu

Mt. Kinabalu

Lahad Datu

BRUNEI

Miri

MALAYSIA

SARAWAK

Kuching

BORNEO

600 Km

400 MI

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki