Wavenezuela Wajifunza Kumtegemea Yehova
“MIAKA ya Utele”—hivyo ndivyo Wavenezuela wengi zaidi wanavyokikumbuka kipindi kilichofuata 1976. Mwaka huo, serikali ilitaifisha mashirika yote ya kigeni yenye kushughulika na mafuta katika Venezuela, na uchumi wa nchi ukasitawi sana. Ushuhuda wa ufanisi mkubwa wa mali uliokuwa umepatikana karibuni ni miradi ya majengo mengi sana yaliyoanza kuinuka katika sehemu zote za taifa. Majengo yaliyo marefu zaidi nchini, yale ya Parque Central Towers, yalijengwa katika Caracas, mji mkuu. Watu walionekana kuwa na kila sababu ya kutegemea ufanisi huo wenye kuendelea sana.
Hata hivyo, leo matazamio ya mbele hayaonekani yakiwa mazuri hivyo. Ingawa Venezuela lingali ni taifa lenye ufanisi, hilo pia limepatwa na matatizo ya kiuchumi. Watu wote hapa wanaikumbuka ‘Ijumaa Nyeusi,’ ambao ndio mtajo wa watu wengi kwa Februari 28, 1983, wakati ambapo pesa iliyo msingi wa matumizi, bolivari, ilishushiwa thamani. Tokeo ni kwamba, pesa za taifa zilipoteza nguvu, na madeni ya nchi za kigeni yakaanza kuongezeka. Kwa ghafula, “Miaka ya Utele” iligeuka ikawa “Miaka ya Kukosa Starehe.” Wengi wamekatishwa tamaa sana kwa kuweka uhakika na tegemeo lao mahali pasipofaa. Kinyume cha hivyo, Mashahidi wa Yehova katika Venezuela wamejifunza kutegemea Mungu wa kweli, Yehova. Wao wameona shangwe juu ya ukuzi na mpanuko wenye kuendelea muda wa miaka yote hiyo.
Ukuzi wa Mbegu za Mapema za Ufalme
Katika 1936 ndipo mbegu za habari njema za Ufalme zilipoletwa kwanza Venezuela na mapainia wawili, au wahudumu wa wakati wote, kutoka Texas, U.S.A. (Mathayo 24:14) Miaka kumi baadaye, wamisionari wawili—wahitimu wa darasa la tano la Shule ya Biblia ya Mnara wa Mlinzi ya Gileadi—walifika. Na katika Septemba mwaka huo, ofisi ya tawi la Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ikafunguliwa katika Venezuela. Ripoti ya mwaka huo ilionyesha jumla ya wapiga mbiu 19 wa Ufalme katika Venezuela.
Katika Novemba 1953, N. H. Knorr, aliyekuwa msimamizi wa Sosaiti wakati huo, na mwandishi wake, M. G. Henschel, walitua Venezuela wakiwa katika utalii wao wa Amerika ya Kusini. Watu mia tisa na arobaini na wawili walikuja kwenye kusanyiko lililofanywa katika Caracas. Kufikia 1977 hesabu ya wahubiri wa Ufalme katika Venezuela ikawa imekua kufikia kilele cha zaidi ya 13,800. Hiyo ilifanya ihitajiwe kabisa kujenga ofisi mpya ya tawi katika La Victoria, kilometa 85 nje ya mji mkuu. Sehemu mpya iliongezwa na kuwekwa wakfu katika 1985. Leo, kuna wahubiri zaidi ya 42,900 katika makundi na vikundi kama 500 katika Venezuela. Na watu wengi zaidi katika Venezuela wanajifunza kutegemea Yehova, kama ilivyoonyeshwa na hudhurio bora la 154,881 kwenye Ukumbusho wa 1988 wa kifo cha Kristo.
Shamba Lenye Utofauti-tofauti Lakini Lenye Rutuba
Venezuela ni bara lenye matofautiano, na hii inaonekana katika wale ambao wamejifunza kutegemea Yehova. Kwanza, nchi hii inajulikana sana kwa wengi walioihamia. Hivyo, hata miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, mna wengi kutoka Italia, Ureno, Ujeremani, Hispania, Ufaransa, Haiti, Trinidadi, Kyuba, Jamhuri ya Dominika, Ekwedori, na mahali penginepo. Hata hivyo wao wana umoja na Wavenezuela wenzao katika kumtegemea na kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova.
Pia kuna tofauti nyingi za kijimbo. Mvuvi wa nchi za Mashariki mwenye kutoka majimbo ya mashariki huonekana wazi kuwa tofauti na mllanero mfuga ng’ombe wa kutoka nyanda za kusini. Mcaraqueño mtembea haraka wa kutoka jiji kuu, au mfanya kazi mwenye urafiki katika shirika la mafuta aliyetoka Maracaibo, jiji la pili kwa ukubwa katika taifa, wanatofautiana sana na mkulima mtembea pole kidogo aliye Mwandino wa kutoka kusini-magharibi, inakoanzia Milima Andes. Kila mmoja ana desturi na njia yake mwenyewe ya kutamka lugha. Kwa hiyo, pamoja na ule mchanganyiko wa kupendeza unaoongezewa na wahamiaji wa kigeni, miongoni mwa watu wenyewe mna unamna-namna wa kuvutia.
Wajapokuwa na malezi yenye kutofautiana hivyo, watu wa namna zote za maisha wamepata kujifunza juu ya Yehova. Maria Luisa alikuwa mmoja wao. Yeye alikuwa akihusika katika kuwasiliana na roho waovu tangu alipokuwa na miaka saba. Alipoendelea kukua, akazoelea utumizi wa kileo na dawa za kulevya, akaendesha maisha ya kukosa adili, na kuingilia sana ibada ya Maria Lionza mungu-mke wa Venezuela.a Alipochukizwa sana na njia yake ya maisha, alianza kazi katika misheni ya Kikatoliki miongoni mwa Wahindi katika sehemu ya magharibi ya nchi. Karibuni akakata shauri kwamba kazi yake haikuwa ikisaidia Wahindi wala yeye. Ndipo akaanza kujiingiza katika falsafa ya kufumbua mafumbo ya maisha na ya kuzaliwa katika umbo jipya baada ya kifo, lakini wapi. Hapo, ndipo Maria Luisa alipofanyiwa ziara na Mashahidi wa Yehova. Maarifa ya Biblia aliyopata yalimpa imara aliyohitaji ili kupigana dhidi ya roho waovu. Sasa yeye anategemea Yehova na ni mpiga mbiu mtendaji wa habari njema za Ufalme.
Hata watu wenye vizuizi vya kimwili wanajifunza kutegemea Yehova, kama ilivyo kwa habari ya Juan na Carlos, ndugu wawili wa kimnofu. Carlos alipokuwa na miaka tisa aligonjweka utando wenye kufunika ubongo wake akawa hawezi kuona. Baadaye, ingawa alihusika na harakati ya kikarisma ya Wakatoliki, alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Alibatizwa katika 1982, na tangu Desemba 1983 amekuwa mhudumu wa wakati wote. Yeye hutembea kila pembe ya eneo lake akiwa painia kipofu, akiwa peke yake inapohitajika kabisa. Hata hivyo, Juan ndugu yake ni tofauti kabisa.
Juan ana urefu wa meta 1.8 na alikuwa akipigana na watu kweli kweli katika mashindano ya barabarani. Siku moja alipigwa risasi mgongoni mara mbili. Ingawa aliponyoka kifo, alipooza kuanzia kifuani kwenda chini na akawa mtu wa kukaa kitandani wakati wote. Mashahidi walipomfanyia ziara, alikubali toleo lao la kujifunza naye Biblia ingawa hakutaka. Mafunzo aliyopata yalimfanya aanze tena kuistahi Biblia. Tumaini la kupata uhai mkamilifu katika Paradiso lilimgusa. Baada ya kuacha kuvuta sigareti, kunywa, na kutumia usemi mchafu, wote waliokuwa rafiki zake hapo kwanza walimwacha kwa sababu, kulingana na maelezo yao, Juan alikuwa amekuwa “mtakatifu.” Hata hivyo, yeye aliendelea kutegemea Yehova, na mwishowe akabatizwa.
“Kuwa mtu wa kukaa kitandani wakati wote hakujanizuia nisifanye penzi la Yehova,” anasema Juan, “kwa sababu angalau mikono na ubongo wangu ungali ukifanya kazi vema.” Anatumikiaje Yehova katika hali yake? “Mimi hutumia mashine ya kanda za kunakili sauti ili kutimiza madaraka yangu, kama hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, sehemu katika Mkutano wa Utumishi, na kusoma kwenye Funzo la kila juma la Mnara wa Mlinzi. Nina pendeleo la kuongoza moja la Mafunzo ya Kitabu ya Kundi, linalofanywa nyumbani kwangu. Pia nimeweza kutumikia nikiwa painia wa kawaida.” Yeye anahisije juu ya yote haya? “Nawashukuru sana watu wa ukoo wangu na ndugu na dada zangu wa kiroho, ambao wananisaidia sana. Natumaini na kusali kwamba sisi sote tutavumilia katika kumtegemea Yehova ili tuweze kuiona siku ambapo “mtu aliye kilema ataruka-ruka [atapanda juu, NW] kama kulungu.”—Isaya 35:6.
Makusanyiko Yamletea Yehova Sifa
Hivi majuzi Mashahidi katika Venezuela wamejenga Majumba ya Kusanyiko mawili ili kuendeleza kazi inayosaidia wengi sana wamtegemee Yehova. Moja limo Campo Elias, Mkoa wa Yaracuy, sehemu ya magharibi ya katikati ya nchi. Lile jingine, lililoko kilometa 60 kusini mwa Caracas, lina vifaa kamili vya kidimbwi cha ubatizo, vipepeaji-hewa na vipasha-joto, jiko, na vifaa vya chumba cha kulia chakula.
Majumba haya yamewavutia sana watu wa nje na wenye kupendezwa ambao wamekuja kuyaona. Dreva mmoja wa basi alikodiwa na kikundi cha Mashahidi awapeleke kwenye kusanyiko la mzunguko lao. Alipofika na kuuona uwanja mkubwa wa kuwekea magari na mazingira yale ya kupendeza, dreva huyo aliona ni lazima pia aingie ndani kupaona mahali hapo. “Kile nilichokiona ndani ya Jumba la Kusanyiko kilikuwa ulimwengu tofauti kabisa, mazingira ya namna nyingine,” akasema baadaye. Alivutiwa sana na utaratibu na umoja uliokuwapo hata akaisikiliza kwa makini programu nzima. Baadaye aliomba funzo la Biblia na sasa ni ndugu aliyebatizwa.
Wakati mmoja kusanyiko la mzunguko lingefanywa katika El Tigre, jiji lililo katika sehemu ya kusini-mashariki mwa nchi. Kwa kuwa eneo hilo halikuwa na Jumba la Kusanyiko, uwanja wa huko ulikodiwa. Hata hivyo, ndugu hawakujua kwamba sherehe fulani ya kujifurahisha ingefanywa katika jiji hilo tarehe zile zile. Wenye mamlaka wa hapo walipokuja kujenga kibanda cha wapiga muziki karibu na uwanja wa kusanyiko, Mashahidi waliwasihi sana wapanga-sherehe waweke kibanda cha wapiga muziki mahali pengine, lakini wapi. Ikiwa ndiyo hatua ya mwisho, Shahidi mmoja akawaambia hivi wasimamizi: “Tafadhali jueni kwamba mnatafuta matata na Yehova.” Kusikia hivi, mwanamume mmoja mwenye kusimamia akajibu: “He, mimi sitaki matata na Yehova!” Sherehe zilihamishwa zikapelekwa kwenye uwanja ulio mbali na mahali ambapo kusanyiko la mzunguko lingefanywa.
Kwenye kusanyiko jingine, mume wa dada mmoja, ambaye ni mwanamume mwenye kazi ya kisiasa, alikuja kuona kama dada huyo alikuwa akifanya mapenzi na mtu fulani huko. Alishangazwa na ubora wa hotuba zilizotolewa. “Kama mimi ningeweza kuongea kama mwanamume yule, ningesonga mbele kweli kweli katika kazi yangu ya kisiasa,” akamwambia mke wake. Baada ya programu, alifikia mmoja wa wazee akaomba aonyeshwe jinsi angeweza kufanya maendeleo katika kuhutubu peupe—hilo tu. “Msinitazamie niende mlango kwa mlango nikiwa na mkoba,” yeye akatahadharisha. Funzo la Biblia lilianzwa, na upesi mwanamume huyo akabadili nia—alitaka kwenda mlango kwa mlango akiwa na mkoba na kuzihubiri habari njema! Alijiuzulu siasa akabatizwa, na sasa yeye na jamaa yake wanamtegemea Yehova.
Kutengeneza Njia ya Mpanuko Zaidi
Wakati wa ziara moja iliyofanywa na L. A. Swingle, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, umati wa watu 63,580 walikusanyika katika uwanja wa Plaza Monumental, wa maonyesho ya kupambana na ng’ombe wakali, katika Valencia. Wengi wao walikuwa wamesafiri kwa basi usiku wote. Wote waliokuwapo walitiwa moyo sana kumsikia Ndugu Swingle akiwaambia: “Nyinyi si tawi dogo tena. Sasa nyinyi ni tawi lenye ukubwa wa kadiri. Na inaonekana kwamba, siku moja hivi karibuni mtaingia katika ile ‘klabu ya wahubiri 100,000’!”
Mipango inafanywa kupanua ofisi ya tawi katika La Victoria ili kutunza ukuzi mkubwa ajabu uliopo. Ndiyo, maelfu ya watu katika Venezuela wanajifunza kumtegemea Yehova.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Amkeni! ya Juni 22, 1967 (Kiingereza), kurasa 21-3.
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 21]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
CARIBBEAN SEA
VENEZUELA
Maracaibo
ANDES MOUNTAINS
Campo Elias
Valencia
La Victoria
Caracas
El Tigre
COLOMBIA
BRAZIL
GUYANA
600 Km
400 mi
[Picha katika ukurasa wa 24]
Jinsi Jumba la Kusanyiko la Cua linavyoonekana kwa nje na ndani