Kushinda Tatizo la Eneo Lililo la Zamani Zaidi Duniani
“UFALME wa mbinguni umekaribia.” Kwa wale wapiga mbiu 370 wa “habari njema” walio katika Serikali ya Israeli ya ki-siku-hizi, kuutangaza ujumbe huo kuna umaana wa pekee. Kwa nini? Kwa sababu hapa ndipo ujumbe wa Ufalme ulipotangazwa kwanza na Yesu Kristo kama miaka 2,000 iliyopita. (Mathayo 4:17; 24:14) Hiyo yafanya Israeli liwe ndilo eneo la zamani zaidi duniani ambamo habari njema zinahubiriwa.
Hata hivyo, tangu pale mwanzo hili limekuwa eneo lenye tatizo. Ingawa wengi walionyesha upendezi katika ujumbe wa Yesu, ni wachache waliochukua hatua zaidi. (Yohana 6:2, 66) Leo, tatizo lenyewe limo katika ule wingi wa dini mbalimbali, utamaduni, na maoni ya kisiasa.
Kwa upande mmoja, kuna Waarabu milioni 2.2. Miongoni mwao wamo Wakristo wa jina tu, Waislamu walio au wasio wazoeaji wa dini yao, washiriki wa imani ya Druze, na watu wenye kudai kwamba wao hawaamini kuna Mungu. Wamejipanga katika njia tofauti za kisiasa pia, baadhi yao wakipendelea kwamba kusimamishwe imara serikali ya Kipalestina yenye kujitegemea katika Ukingo wa Magharibi na Ukanda wa Gaza.
Kwa upande ule mwingine, kuna Waisraeli Wayahudi milioni 3.5, wao pia wakiwa wamegawanyika kwa njia nyingi. Baadhi yao wamehama kutoka Morocco, Yemen, Iraki, na Siria. Wengine wametoka Ulaya na Urusi. Na bado wengine wametoka India, kontinenti za Amerika, Ethiopia, Afrika Kusini, na kwingineko. Wao huishi katika mitaa yenye utamaduni na mapokeo yayo yenyewe na pia fasiri yao isiyolingana na nyinginezo kuhusu dini ya Kiyahudi na jinsi ya kuizoea.
Kwa kielelezo, kuna rabi mkuu mmoja wa Wayahudi Waashkenazi (Wazungu) na mmoja wa Wayahudi Wasefardi (wa Mashariki ya Kati). Ingawa walio wengi wanaonyesha upendezi mwingi sana katika masuala ya kisiasa, kuna Wayahudi wanaofuata dini kwa kina kirefu, ambao hata hawatambui kuwako kwa Serikali ya Israeli na hukataa kulipa kodi. Halafu kuna wale waokokaji wa yale Maangamizi Makuu ya Wayahudi, wengi wao wakiwa bado wanateseka wanapofikiria mabaya makubwa waliyotendwa wakati uliopita, kila mmoja akiwa na mambo ya kusimulia kuhusu mabaya ya kukata moyo yaliyompata. Wengi pia wanazidi kudai kuwa hawaamini kuna Mungu, wakishikilia falsafa mbalimbali za kibinafsi. Jambo moja tu linalounganisha Wayahudi ni kuokoka kwao wakiwa jamii ya watu na muungano wa kisiasa.
Kulishinda Tatizo
Baada ya pumziko la miaka zaidi ya 1,800, kazi ya kuuhubiri Ufalme ilianza tena hapa kwa kadiri ndogo katika 1913. Wakati huo, kijana mwanamume mwenye kupendezwa na Biblia alianza kupanda mbegu ya Ufalme katika Ramallah, karibu kilometa 16 kaskazini ya Yerusalemu. Kutoka hapo habari njema zilienea kwa wakaaji Waarabu wa Beit-Jala na Haifa. Muda mfupi baada ya Vita ya Ulimwengu 2, dada wawili Mashahidi wenye malezi ya Kiyahudi walianzisha kazi upya katika eneo la Tel Aviv/Jaffa. Leo, kuna makundi sita na vikundi viwili vya Mashahidi wa Yehova wenye kutumikia katika Haifa, Tel Aviv, Bethlehemu, Ramallah, Lod, na katika eneo la Beer-Sheba.
Kama ilivyokuwa karne 19 zilizopita, huduma ya nyumba kwa nyumba ingali ndiyo njia yenye matokeo makubwa zaidi ya kupata wenye kupendezwa na habari njema. (Luka 8:1; linganisha Matendo 5:42.) Kwa uhakika, kwa kulinganishwa na mabara mengineyo, ni raha kutoa ushuhuda hapa kwa njia hiyo. Kwa ujumla, watu huwa wadadisi kuhusu ujumbe wetu na hualika wahubiri wa Ufalme ili kuzungumza. Mara nyingi udadisi huu huongoza kwenye angusho la magazeti yetu na fasihi nyingine za Biblia. Mara kwa mara, vichapo hivyo hupokezanwa kutoka kwa jirani hadi kwa jirani, tokeo likiwa kwamba watu fulani mmoja mmoja hujifunza ukweli wa Biblia.
Hata hivyo, udadisi uu huu huwa tisho mara nyingi kwa mbegu ya ukweli iliyo changa sana katika mioyo ya wapya. (Mathayo 13:20, 21) Majirani, marafiki, na hasa viongozi wa kidini hufanya yote wawezayo kuwabana, kuwadhihaki, kuwatisha-tisha, na katika visa fulani kuwatenda mabaya ya kimwili wale wenye kuonyesha upendezi katika ujumbe wa Ufalme. Tokeo ni kwamba, baadhi yao wamepoteza kazi ya kuajiriwa, huku wengine wakiwa wamekatiliwa mbali na marafiki na jamaa wasiwe na uhusiano nao. Wale wenye kusimama imara na kuwa Mashahidi wa Yehova huwa ni lazima wavumilie mioto ya upinzani,—Linganisha Yohana 9:22.
Upinzani huja kwa njia nyinginezo pia. Mashahidi wenye malezi ya Kiyahudi wameshambuliwa na wanaghasia. Ofisi ya tawi na Jumba la Ufalme katika Tel Aviv na Jumba la Ufalme katika Haifa zimekuwa shabaha za wateketezaji. Sasa Mashahidi Waarabu na Wayahudi pia wanabanwa sana wajiunge katika ugomvi wa kisiasa kwamba kusimamishwe imara serikali ya Kipalestina. Kwa kudumisha msimamo wa kutokuwamo katika mambo hayo, akina ndugu hueleza kwa busara kwamba hakuna shirika lolote la kibinadamu liwezalo kutatua matatizo ya aina ya binadamu wenye kuugua. Badala ya hivyo, kwa kuiga Kiongozi wao, Yesu Kristo, Mashahidi huonyesha kwamba Ufalme wa Mungu ndio utatuzi mmoja tu.—Yohana 17:16; 18:36.
Tunda la Ufalme Lazaliwa
Kujapokuwa na matatizo mbalimbali katika eneo hili la kutolea ushuhuda lililo la zamani zaidi, ‘wanaolisikia neno na kuelewa nalo’ huzaa tunda la Ufalme katika shamba hili. (Mathayo 13:23) “Kuna watu walio na kiu kwa ajili ya ukweli, wapenda uadilifu, ambao wanautafuta kihalisi,” akasema mhudumu wa wakati wote aliye na ujuzi. “Wao hawavutwi na maoni wala mibano inayotoka kwa wengine. Fursa ya kujifunza ukweli itokeapo, wao huishika haraka.” Mambo mengi yaliyoonwa yanashuhudia jambo hili.
Akiwa amelelewa katika makao ya wanadini katika Ugiriki, Benvenida alivutwa sana na yale inayosema Biblia juu ya “dini iliyo safi na isiyo na hitilafu,” yaani, “kuwasaidia yatima na wajane katika shida zao, na kujilinda mwenyewe usichafuliwe na ulimwengu huu.” (Yakobo 1:27, HNWW) Akiwa msichana mchanga wa Kiyahudi, yeye alisema kwamba yaliyompata yalikuwa “msiba baada ya msiba” tu. Alivumilia ugumu wa kukaliwa kwa nchi na Wanazi na vita ya wenyewe kwa wenyewe, ambamo alipoteza mume wake. Lakini tumaini lake la kupata watu walio wafuataji haki na wasio wanafiki halikufifia.
Baada ya kuhamia Israeli katika 1949, Benvenida alifuatia kazi-maisha ya kuwa mkunga mpaka alipostaafu katika 1974. “Wakati wote huo,” yeye akasema, “niliendelea kujiuliza: ‘Wako wapi wale watu wema walio wafuataji haki ambao Biblia hueleza juu yao? Iko wapi haki katika ulimwengu huu?’” Yeye alianza kufuata dini ya Kiyahudi, akihudhuria sinagogi na kuishika Sabato na sikukuu. Lakini masengenyo na mzozano uliokuwa miongoni mwa washiriki wa kundi la kwao yalifanya azidiwe na njaa ya kuitaka “dini iliyo safi na isiyo na hitilafu.”
Mwishowe, katika 1985, wakati wa moja ya ziara za Benvenida za kila mwaka za kwenda kwenye chemchemi yenye maponyo kwa afya katika Ugiriki, mwanamke Shahidi mwenye kupokea matibabu huko alianza maongezi naye. Zungumzo refu likafuata. Usiku uo huo, Benvenida alihudhuria mkutano wake wa kwanza kwenye Jumba la Ufalme la huko akavutwa kwa kina kirefu na uchangamshi na weupe wa moyo wa akina ndugu na dada.
Benvenida aliendelea kujifunza aliporudi Israeli, na karibu mwaka mmoja na nusu baadaye, akabatizwa kwa kuonyesha wakfu wake kwa Mungu wa ukweli, Yehova. Yeye alisema, “Baada ya miaka yote hii na kwenye umri wa miaka 70, mwishowe niliwapata watu wenye kiasi na wanyenyekevu ambao Biblia hunena juu yao, wale wenye kunitendea mimi kama mtu. Sasa, kila siku niishiyo ni siku yenye shangwe na kusudi!”
Moshe alikuwa mtafutaji mwingine wa ukweli aliyekuwa akingojea tu ‘kuisikia sauti ya mchungaji mwema.’ (Linganisha Yohana 10:14-16.) Ingawa sikuzote Moshe aliyapenda Maandiko, alijua habari za Yesu Kristo kutokana na nakala moja ya “Agano Jipya” ambayo ndugu yake alikuwa karibu kuitupilia mbali, naye akavutwa kwa kina kirefu. Muda fulani baadaye, Moshe alijiunga na mwanamke mmoja aliye mfanya kazi mwenzake katika funzo lake la Biblia pamoja na Shahidi, na akahudhuria hotuba iliyotolewa na mnenaji anayezuru. “Haya ndiyo nimekuwa sikuzote nikitaka kuyasikia!” akapaaza sauti baada ya mkutano huo wa kwanza.
Baada ya kupatwa na kipingamizi hapo mwanzoni, maendeleo ya Moshe yalikuwa ya haraka sana. Alibatizwa katika muda wa miezi sita. Hata hivyo, maendeleo yake yalileta upinzani kutokana na jamaa yake, hasa mke wake. Mambo yakachacha wakati yeye, akiwa ndiye mwana wa umri mkubwa zaidi katika jamaa, alipokataa kushiriki sala za kisherehe kwenye maziko ya baba yake. Kuongezea hilo, marafiki na watu wa ukoo waliambia mke wake kwamba ingekuwa afadhali ‘achukue hatua ya haraka’ kabla mume wake hajatia sahihi kwamba kila kitu kiwe mali ya kundi. “Mimi nikatuliza hofu zake kwa kujitolea kuiandikisha nyumba kwa jina lake,” Moshe akaeleza. Na kwa kuratibu wakati wake ifaavyo, akaweza kudumisha usawaziko wenye kufurahisha kati ya jamaa yake na madaraka ya kundi.
Hata hivyo, si watu wote wa ukoo ambao hupinga ukweli. Nehai alishiriki na mume wake, Hanna, mambo aliyokuwa amejifunza kutokana na Biblia, wakati huo mume wake akiwa ni mtendaji sana katika siasa. Muda si muda, wote wawili wakang’amua kwamba Ufalme wa Mungu ndilo tumaini moja tu kwa aina ya binadamu wenye kuonewa. Kwa hiyo wakawa watumishi waliojiweka wakfu wa Yehova na kuanza kutoa ushuhuda miongoni mwa jamaa za Waarabu katika Haifa na vijiji vyenye kuizunguka. Hasa walitoa ushuhuda miongoni mwa jamaa za ukoo wao, karibu watu 252 kwa ujumla.
Je! jambo hili limekuwa tatizo? Ndiyo, kwa maana mbali na kulazimika kuendesha gari kwa saa moja na nusu mwendo wa kwenda na wa kurudi pia ili kufanya ziara kwenye vijiji vya Kiarabu, saburi na uvumilivu mwingi ulihitajiwa. “Nyakati fulani watu tofauti-tofauti hukuambia kwamba hawataki kusikia tena. Iwapo hivyo, utalazimika kuacha kuongea. Baadaye, labda waweza kuingia polepole katika habari hiyo tena. Ni kama kupigwa teke utoke kwenye mlango wa mbele na kupandia dirishani tena ili urudi ndani,” Hanna akaeleza. Yote haya yameleta malipo. Kufikia sasa, 24 kati ya watu 36 wa ukoo wake wameonyesha upendezi wa makini katika Maandiko, na 13 kati yao wanajifunza pamoja na Hanna au Mashahidi wengine. Kufikia tarehe hii, watano kati ya watu wa ukoo wake wa karibu na pia watoto wake mwenyewe wameweka wakfu maisha zao kwa Yehova, na wengine watatu wanafanya maendeleo kuelekea hatua hiyo.
Vilele Vipya Katika Eneo Lililo la Zamani Zaidi
Maono ya kuchangamsha moyo kama haya yanaongezeka hapa katika Israeli, na kuna matazamio ya kutia moyo sana kuhusu ukuzi. Katika 1988 hesabu ya wapiga mbiu wa Ufalme ilifikia kilele cha 370. Hesabu ya wastani wa mafunzo ya Biblia yenye kuongozwa kila mwezi katika nyumba za watu wenye kupendezwa imeruka kutoka 89 katika 1979 kuwa 301 katika 1988—ongezeko la asilimia 240!
Yote haya huwaletea shangwe kubwa Mashahidi wa Yehova katika bara hili la kale. Sisi tunatazama mbele kwenye mibaraka mikubwa hata zaidi kutoka kwa Mungu wetu, Yehova, huku sisi tukisonga mbele pamoja na kazi ya kufanya wanafunzi katika eneo lililo la zamani zaidi duniani.
[Picha katika ukurasa za 26 na 27]
Juu: Kaburi la bustanini, Yerusalemu
Upande mwingine: Tamasha za sokoni na barabarani katika Israeli
Chini: Ofisi ya tawi katika Tel Aviv