Msaada Bora Zaidi wa Kujua Wakati Ujao
Imesimuliwa na Mmoja Aliyeipata Barabara ya Uhai
DINI ilishiriki sehemu y.a maana katika maisha ya jamaa yetu. Baba alikuwa Myahudi, na hata ingawa alikuwa amegeuka afuate Ukatoliki ili aoe mama yangu, bado alistahi sana Biblia. Mama alitoka kwenye jamaa yenye mapokeo ya Kikatoliki yaliyotia sana mizizi—wawili wa dada zake walikuwa watawa wa kike, binamu mmoja akiwa monsinya, na wapwa wawili wakiwa ni watawa wa kiume.
Wakati wa vita ya ulimwengu ya pili, zile hali za wasiwasi, hofu, na tisho la daima la kuhamishwa kupelekwa kwenye kambi ya mateso kwa sababu ya kuwa Myahudi kulifanya baba yangu afe mapema. Kwa kuamini sana lile fundisho la kutokufa kwa nafsi, mama yangu alishiriki katika mikutano ya mafumbo ya kiroho, akijaribu kupashana habari na baba yangu.
Nilipofikia utu mzima, dini ya kimapokeo iliendelea kuwa sehemu ya maisha yangu. Nilibaki nikiwa “Mkatoliki mwema.” Hata hivyo, Ukatoliki haukuweza kueleza wakati ujao ulikuwa na mambo gani kwa ajili yangu. Je! ningeweza kugeukia nani nisaidiwe kujua?
Sawa na vile mama yangu alivyokuwa amefanya wakati mmoja, mimi nilitafuta ushauri kwa watu walio vyombo vya kuwasiliana na roho. Kwa kuwa walianza kila kikao kwa ishara ya msalaba na sala, nilisadiki kwamba matukio ya ajabu niliyoshuhudia yalitoka kwa Mungu. Wakati huu ndipo mimi, kwa kutaka kufanya jambo fulani la kuondoa mateso ya wengine, nilijiunga na shirika la Kikatoliki lililotengeneza visafari vya kwenda kwenye maabadi ya Marian kule Lourdes, ambako wagonjwa walitumainia kupata maponyo ya kimuujiza.
Mimi nilikuwa sijapata kusikia juu ya Mashahidi wa Yehova mpaka siku ambayo mume wangu alikubali magazeti mawili niliyoyaona kuwa ya kupendeza sana. Kilichonivutia zaidi ni kwamba Biblia ilinukuliwa kwa kuunga mkono maelezo yaliyo katika magazeti hayo. Mara hiyo nikang’amua kwamba vichapo hivi vingekuwa na manufaa sana katika kupata maarifa ya Neno la Mungu. Niliandika barua kuomba andikisho kwa magazeti yote mawili. Mashahidi wa Yehova wakanizuru, nami nikaanza kujifunza Biblia.
Nilikuwa mwenye shauku sana kuhusu kweli za Biblia nilizokuwa nikijifunza na nikaanza kuzieleza kwa wazoeani wangu. Nilishtushwa na itikio la rafiki mmoja, yule mwenye kutengeneza zile safari za kuhiji, nilipomwambia kwamba ninajifunza Biblia na Mashahidi. Mwanamke huyo alikasirika sana na kusema mambo mabaya sana kuwahusu mpaka mimi nikaenda zangu. Ndipo nikalazimika kukabiliana na upinzani kutoka kwa mume wangu. (Mathayo 10:36) Kwanza ilikuwa vigumu, lakini kadiri nilivyozidi kuyazoea mambo niliyokuwa nikijifunza, ndivyo maisha yangu ya jamaa yalivyobadilika kuwa mazuri zaidi. Nilibatizwa katika 1977.
Niling’amua kwamba nisingaliipata kamwe barabara iendayo kwenye uhai kama Mashahidi wa Yehova wasingalionyesha upendezi kwa kujaribu kunisaidia nipate kuzijua kweli nzuri sana za Biblia. Nilijua kwamba mimi pia nilikuwa chini ya wajibu wa kufanya yote niwezayo ili kusaidia wengine wajue kuhusu Yehova na kusudi lake zuri sana kwa wakati ujao. Ningefanyaje hivyo? Njia bora zaidi ilikuwa kuanza huduma ya wakati wote. Kwa kuwa niliishi katika nyumba iliyogawanyika kidini, haikuwa rahisi kwangu kufanya hivyo. Lakini nilitumainia tegemezo na mwongozo wa Yehova nami nikafanya kimbilio katika yeye. Sasa, ninaishi miaka ambayo ndiyo yenye furaha kuliko mingine yoyote ya maisha yangu nikiwa painia wa kawaida. Mimi nimesadiki zaidi ya wakati mwingine wowote kwamba “Yehova ni mwema” na kwamba mtu yeyote “afanyaye kimbilio katika yeye” ni mwenye furaha.—Zaburi 34:8, NW.