Furaha ya Kutimiziwa Mahitaji ya Kiroho
UMEPATA kuona kwamba ni watu wachache sana wenye furaha ya kweli siku hizi? Wanaona sana kwamba kuna kitu wanachokosa maishani mwao, lakini hawajui ni kitu gani hasa. Je! ndivyo wewe umeona? Ikiwa ndivyo, je! huenda ikawa ni kwa sababu mahitaji yako ya kiroho hayatimizwi?
Bila shaka kuna kitu zaidi tunachohitaji ili tuwe wenye furaha, zaidi ya chakula, mavazi na mahali pa kulala. Kama kitu hicho kisingehitajiwa watu wenye mali wasingekuwa na huzuni. Lakini twajua wana huzuni. Kwa upande mwingine, watu wengine walio maskini wana furaha nyingi. Kwa sababu gani? Wameona kwamba Biblia yataja kweli nyepesi inaposema hivi: “Wenye furaha ni wale wauonao uhitaji wao wa kiroho.” (Mt. 5:3, NW) Mtu anapojua kwamba ana uhitaji wa kiroho, anafanya haraka kuutimiza. Uradhi wa kiroho anaopata kwa njia hiyo unaweza kumfurahisha kweli kweli.
Lakini mtu aweza kupata wapi chakula cha kiroho? Je! ni katika mojawapo matengenezo mashuhuri ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo? Au labda ni kati ya kikundi kidogo zaidi cha Wakristo waliojitoa?
Ili tupate jibu la maulizo hayo, na tuangalie yaliyotukia karibuni Italia. Maneno kama yanayofuata husikika huko: “Tumeanza karibuni tu kujifunza Biblia na twataka kuchunguza sana kweli ya pekee iliyo ulimwenguni.” “Nataka kukujulisha kwamba nilizidi kutopendezwa na dini lakini nina tumaini la siri juu ya kupata nuru ya imani ya kweli.” “Hii ndiyo mara yangu ya tatu kuongea na wafanya kazi wenzenu. Ingawa mimi Mkatoliki, nathamini sana mnayofanya tena yananifaidi sana kiroho. Nilikubali kujifunza Biblia kama mlivyojitolea kunisaidia nami nawashukuru sana kwa ajili ya kazi mnayofanya ya kulieneza Neno la Bwana.” Hiyo ni mifano michache tu inayopokewa kila siku katika afisi ya tawi ya Watch Tower Bible and Tract Society katika Rome.
Huenda wengine wakaona ni ajabu kwamba, katika nchi ya Italia inayodhaniwa na wengi kuwa ndiyo makao ya Ukristo, wako watu ambao wameshindwa kutimiziwa mahitaji yao ya kiroho katika kanisa lao wenyewe na wanataka kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, jambo lenye kushangaza ni kwamba, Cardinal Poletti aliuita Rome hivi majuzi “mahali panapohitaji wamisionari,” kwa sababu watu wanaendelea kutopendezwa na Kanisa. Hali hiyo yahusu Italia yote.
Naam, hesabu zaidi na zaidi ya Waitalia inauona uhitaji wao wa kiroho. Hasa miaka 30 iliyopita mkazo mwingi zaidi umetiwa juu ya kupata masomo ya juu zaidi. Kwa hiyo Waitalia wanasoma zaidi, na tokeo moja la kufanya hivyo ni kwamba, wengi wao wameona hawakufundishwa masomo ya Biblia na viongozi wao wa dini. Kanisa lao lilianza kuwatia moyo wasome Maandiko Matakatifu hivi majuzi tu.
WATU WENYE VIZUIZI VYA KIMWILI WAITIKIA
Ujumbe wa Biblia wavuta watu wa namna zote. Kwa mfano, watu wenye vizuizi vibaya sana vya kimwili wameitikia. Wao pia wanaweza kupata furaha nyingi wakimaliziwa njaa yao ya kiroho.
Chukua mfano wa kijana mwanamume mmoja katika Italia aliyepooza mikono na miguu akiwa kijana tu kwa kupatwa na msiba-barabara. Baada ya hapo rafiki alimweleza habari za Biblia na kumwachia nakala moja, pamoja na kitabu cha kumsaidia kujifunza Biblia, Kweli Iongozayo kwenye Uzima wa Milele. Baada ya miezi miwili kijana huyo alikuwa amevisoma vyote viwili kutoka jalada mpaka jalada, akaanza kujifunza Maandiko Matakatifu na Mashahidi wa Yehova. Baada ya muda mfupi akaona ubora wa kueleza wengine mambo aliyokuwa amejifunza. Shemeji yake, ambaye hakuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova wakati huo, akawa akimchukua garini ili akaeleze wengine habari za Maandiko. Kwa kuwa kijana huyo aliyepooza alilazimika kubaki kitandani au katika kiti chake cha kutembelea, alitumia kila nafasi aongee na waliomtembelea. Vilevile, alijaribu kuandika barua kwa kufunga kalamu katika kiganja chake. Lakini hakufaulu sana, kwa maana mwandiko wake ulikuwa mbaya sana. Kwa hiyo alinunua mashine ya chapa (typewriter) akaja na chombo fulani ambacho angeweza kufunga katika kiganja chake, kumwezesha kugonga zile chapa za mashine.
Miezi sita baada ya kubatizwa, kijana huyo alianza kutumia karibu saa 100 kila mwezi akisaidia wengine wajifunze habari za Biblia. Aliongoza hata mafunzo sita ya Biblia, naye alifurahi sana kuona watatu kati ya watu ambao alijifunza nao wakifanya maendeleo hata wakabatizwa katika kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova.
Ijapokuwa hali ya mwili wake si nzuri, anapata furaha akisaidia wengine kiroho. Katika mojawapo barua zake, aandika hivi: “Namshukuru Yehova kwa sababu amenipa uwezo wa kusitawisha moyoni kupendezwa na Biblia Takatifu na kutaka nimtumikie.”
Vivyo hivyo, mume na mke mabubu walisaidiwa na funzo la Biblia wakapata uradhi wa kweli na furaha katika maisha. Licha ya kuwa na vizuizi vya kimwili, walikuwa na matatizo mengine makubwa. Walikuwa wenye huzuni sana katika ndoa yao.
Kila usiku mume alikuja nyumbani akiwa amelewa na nyakati nyingine alimpiga mkewe. Walikuwa na ukosefu mwingi wa pesa, na walikuwa na watoto wanne wa kupatia riziki, wa miaka sita mpaka kumi na mitatu. Kwa sababu ya afya mbaya, mke aliogopa asichukue mimba nyingine. Alipoichukua nyingine, alijaribu kujiua. Lakini aliharakishwa hospitali na hivyo hakufa. Wakati huo rafiki yake bubu, aliyekuwa akijifunza na Mashahidi wa Yehova, alimweleza habari za ufalme wa Mungu, Mwanamke huyu alikubali kwa furaha wajifunze Biblia. Karibuni mumewe alijiunga nao katika mazungumzo.
Kwa sababu ya kutimiziwa mahitaji yao ya kiroho, maisha yao yakawa bora. Mume hakuvuta sigareti tena, hakumpiga tena mkewe wala hakulewa. Kwa kuwekwa huru na tabia zenye gharama nyingi, jamaa ilianza kuwa na pesa. Baadaye, mke alibatizwa katika kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova mwaka 1974, naye mume akazamishwa katika kiangazi cha mwaka 1975 wakati wa “Enzi Kuu ya Kimungu” Kusanyiko la Wilaya. Sasa wote wawili wana shughuli nyingi za kusaidia mababu wengine Italia maarifa sahihi ya kweli.
NJIA MPYA YA MAISHA YENYE FURAHA ZAIDI
Wevi, wenye kuzoea kutumia dawa za kulevya, malaya, na vilevile watu ambao maisha zao zimejawa sana na mambo kama michezo, wamekuja kuthamini ubora wa mambo ya kiroho. Ndiyo sababu sasa wanafuatia njia ya maisha yenye furaha zaidi.
Bila ya yeye kujua, mama mmoja Shahidi alisaidia mwivi aanze kuangalia mahitaji yake ya kiroho. Mama huyo alikuwa na kawaida ya kusomea kitoto chake kidogo yaliyomo katika Biblia. Jioni moja alimaliza usomaji wake kwa kusoma Waefeso 4:28: “Mwibaji asiibe tena; bali afadhali afanye juhudi, akitenda kazi iliyo nzuri kwa mikono yake mwenyewe.” Kisha aliifunga Biblia, akaiweka juu ya kimeza kilichokuwa karibu na kitanda, akazima taa alale. Alipoamka asubuhi yake, Biblia haikuwapo. Nyumba yote hakuna aliyejua ilikokwenda. Biblia ilikwenda wapi?
Miezi kadha baadaye, wakati wa kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova katika Cagliari, Sardinia, mwanamume mmoja alimfikia akamwuliza: “Wajua nilipojulia kweli?” “Hapana,” yule mama akajibu. Mwanamume huyo akaendelea kusema: “Niliijulia uvunguni mwa kitanda chako.” Shahidi alishangaa sana. Mwanamume alipomwonyesha Biblia aliyokuwa nayo, Shahidi aliitambua mara kuwa ndiyo ile iliyopotea katika kimeza karibu na kitanda chake. Mwanamume akamweleza aliingia nyumbani mwake aibe. Lakini, aliposikia kelele, akajificha uvunguni mwa kitanda akakaa humo mpaka Shahidi akamaliza kusoma Biblia yake, akazima taa na kulala. Mwanamume huyo aliendelea kusema, “Mara nilipohakikisha umelala, niliichukua Biblia ambamo ulisoma ‘Mwibaji asiibe tena,’ nikaondoka nyumbani nikaenda kwangu. Biblia hiyo ndicho kitu changu cha mwisho kuiba.” Wakati huo alitafuta Mashahidi wa Yehova akaanza kujifunza nao Biblia.
Halafu alikuwako mwanamke kijana Mwitalia aliyejaribu kujifunza na kueleza wengine Injili, lakini alifanya hivyo akiongozwa na dawa za kulevya. Baadaye alionana na Mashahidi wa Yehova, akaanza pamoja na mumewe kujifunza nao. Waliacha kuishi maisha ya ufisadi na kutumia dawa za kulevya kwa sababu ya mambo waliyojifunza. Wote wawili sasa wanajaribu kusaidia vijana wengine wafahamu kwamba Mungu aweza kufikiwa, si kwa kutumia dawa za kulevya, bali kwa kufanya mapenzi yake kama yanavyoelezwa katika Biblia Takatifu.
Ziko nyakati ambapo wanaotwaa chakula cha kiroho cha Neno la Mungu hupata maoni tofauti kabisa juu ya mambo. Huanza kuchukua mambo ya kiroho kuwa ya maana zaidi katika maisha yao na kuwa na nia ya kuacha mambo waliyokuwa wakiyapenda sana.
Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya msichana aliyekuwa amekuwa bingwa wa kutupa sahani michezoni. Asimulia hivi: “Kila siku nikawa nikienda uwanjani kujizoeza. Sikuzuiwa kwenda na mvua wala upepo. Mradi wangu ulikuwa kushinda rekodi ya Italia ya mchezo wangu.” Lakini, alipoendelea kujifunza Biblia, msichana huyo alitambua kwamba kuhusika katika michezo ya kushindana kungeweza kumzuia asisitawishe roho ifaayo ya Kikristo. Kwa hiyo aliamua kuacha michezo, kisha mwishowe, kama alivyoandika mwenyewe, “nikabatizwa Rome katika uwanja ule ule ambako nilikuwa nikiheshimiwa kwa ajili ya michezo yangu.”
Mwingine aliyepata maoni tofauti juu ya maisha yake alikuwa mwenye jumba ambamo watu walifundishwa michezo ya kupigana, judo na karate. Baada ya kujifunza Biblia, dhamiri yake ilimwongoza akawa na maoni tofauti juu ya kuzoeza watu jeuri. Aliamua kuvunja uhusiano na “ufundi wa kupigana.” Kwa kuwa alitenda kupatana na dhamiri yake, yeye hufurahia kufahamisha wengine ujumbe wa Kikristo wa amani.
UKOMBOZI WA AJABU
Chakula cha kiroho kutoka Neno la Mungu kimesaidia watu kweli kweli wakaacha njia walizofahamu hazipatani na maisha ya Kikristo. Wengine Italia wamekombolewa wasisumbuliwe na majeshi ya malaika wabaya.
Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya kisichana cha miaka tisa, Siku moja kilikwenda kutembelea shangazi wake kikaletwa katika njozi mbele ya mjuzi wa kusoma akili na kujua mambo yaliyopita. Kwa sababu hiyo, kisichana huyo alipooza, macho yake yakafunguka sana yakawa namna ya kioo, rangi ya uso wake ikawa sana ya kijivu. Tangu wakati huo kisichana huyo aliona njozi na kusikia sauti; ilielekea kama kwamba aliweza kuponya watu pia na kutabiri vifo. Aliudhika sana akalia mara nyingi kwa hofu, kwa sababu ya kukosa usingizi mara kwa mara. Alitoa jasho kweli kweli, kama kwamba alikuwa akipigana na mtu. Mchoro wa msalaba ulitokea kifuani pake. Ilionekana kama kwamba alikuwa amepasuliwa kifuani.
Wazazi wa kisichana huyo walihuzunishwa sana na yaliyokuwa yakimpata. Viongozi wa dini hawakuweza kumsaidia. Mmoja wao hata alisema pengine kisichana huyo alikuwa akikaribia kuwa na “utakatifu.” Lakini mtoto alitaabika sana akahuzunika sana. Alitaka sana awe kama visichana vingine vyote na kucheza, kupiga mbio na kuruka.
Wakati ambao baba yake alikuwa amekuwa hoi, alionana na Mashahidi wa Yehova. Aliwaeleza hali ya binti yake. Alionyeshwa katika Biblia kwamba hakupatwa na mambo hayo kwa mapenzi ya Mungu. Jamaa yote ilianza kufunzwa Biblia. Walipotambua kwamba Neno la Yehova hukataza kuwa na sanamu za ibada, waliondolea mbali kila kitu walichokuwa nacho nyumbani cha ibada ya uongo. Kisichana yule alipofanya maendeleo katika funzo la Biblia, alianza kupata faraja nyingi. Baada ya muda mfupi hakusikia tena “sauti,” hakuona tena njozi, na msalaba uliokuwa kifuani pake ulitoweka. Alirudiwa na furaha ya maisha, jamaa yote ikafurahia fadhili zisizostahilika za Yehova Mungu. Baada ya muda mfupi walionyesha shukrani zao kwa kubatizwa, kuonyesha walijiweka wakf kwa Mungu mwenye rehema, Yehova.
WATU WENYE KAZI ZA KIDINI
Twastahili kuangalia pia kwamba watu wenye kazi za kidini wanaonyesha hawatimiziwi mahitaji yao ya kiroho. Magazeti ya Italia yaendelea kusema kwamba vyuo vingi zaidi vya uanadini vinafungwa au vinaelekea kuwa vitupu kwa sababu ni vijana wachache zaidi wenye nia ya kuwa mapadre. Vilevile, hesabu inaongezeka ya mapadre, watawa wa kike na wa kiume wenye kuacha uanadini waanze kazi nyingine. Na linaloshangaza ni kwamba, hesabu inaongezeka kati ya Mashahidi wa Yehova waliokuwa watawa wa kike, wa kiume na mapadre. Watu hao walionaje uhitaji wa kiroho?
Mtawa mmoja wa kiume alikuwa ameketi katika mlango wa makao yao wakati mwanamke alipomjia akamwambia kwamba Mashahidi wa Yehova walimtembelea nyumbani wakamwachia magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Mtawa huyo alipendekeza mwanamke amwachie magazeti hayo, ili mwanamke asichafuke kwa kuyasoma. Lakini mtawa huyo baadaye aliyasoma magazeti akashangaa sana kujua kwamba masimulizi ya Injili yataja kwamba Yesu alikuwa na ndugu waliozaliwa na mama yule yule aliyemzaa. Alipopata nafasi, alikwenda maktabani na mwishowe akapata Biblia. Baada ya kuangalia maandiko ya Biblia yaliyoonyeshwa katika magazeti, alisadiki kwamba yalikuwa na kweli.
Alijitahidi alivyoweza akaanza kueleza watawa wenzake wa kiume mambo aliyojifunza. Alikaripiwa, akapelekwa makao mengine ya watawa na mwishowe akapelekwa hospitalini kwa kusingizia kwamba alikuwa na wazimu. Alipotolewa hospitalini, alikwenda nyumbani akaeleza jamaa zake sababu yake ya kuondoka katika makao ya watawa. Walimkasirikia sana, lakini hakuogopa. Alitafuta Mashahidi wa Yehova akawapata, kisha akaanza kujifunza nao Biblia.
Miaka kadha mtu huyu aliyekuwa mtawa amekuwa akitangazia wengine kweli ya Biblia na anafurahia sana kufanya hivyo.
Mfano mwingine ni mwanamume aliyekuwa amekuwa padre miaka kumi na saba. Alifuata kanuni za Kanisa kwa uaminifu mwingi. Lakini alianza kusumbuliwa na mafundisho fulani. Hakuweza kufahamu jinsi Mungu mwenye upendo angeweza kutesatesa milele viumbe Wake mwenyewe wa kibinadamu katika moto. Baadaye alipata nafasi ya kusoma kitabu chenye kusaidia watu wajifunze Biblia, Kweli Iongozayo kwenye Uzima wa Milele, pamoja na vitabu vingine vya Watch Tower.
Baada ya kutafakari miezi kadha aliamua kujiuzulu cheo chake cha upadre atafute kazi ya kimwili. Alianza kushirikiana kwa kawaida na kundi la mtaa wake la Mashahidi wa Yehova. Mwishowe alionyesha wakf wake kwa Yehova Mungu kwa kubatizwa majini. Sasa anafurahia sana kuongoza mafunzo ya Biblia kwa watu wengine waliokuwa wa kanisa la mtaa aliosimamia.
MIANZO MIDOGO
Elimu ya Biblia inayoendeshwa na Mashahidi wa Yehova nyakati za kisasa ilikuwa na mwanzo mdogo sana. Ulikuwa mdogo katika Italia vilevile. Huko nyuma mwaka 1946 ni watu 120 peke yao waliokuwa wakipelekea jirani zao ujumbe wa Biblia. Kufika mwaka 1950 hesabu hiyo ilikuwa imeongezeka ikawa 1,211. Miaka 25 baadaye, katika mwaka 1975, watu 56,264 walikuwa wakishughulika kutia wengine moyo wajifunze Biblia.
Watu wengi zaidi wanahudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova katika Majumba ya Ufalme yao. Mara nyingi hudhurio linakuwa mara mbili ya Mashahidi wanaoshirikiana katika makundi. Kwa mfano, Aprili 7, 1975, watu 120,031 walihudhuria katika makundi mbalimbali ya Italia yote waadhimishe Chakula cha Bwana cha Jioni.
Kama katika Italia, watu wa maisha ya namna zote wamefaidika sana kwingineko kutokana na kujifunza Biblia na Mashahidi Wakristo wa Yehova. Wakiisha kutimiziwa mahitaji yao wenyewe ya kiroho, wanakuwa na shauku ya kueleza wengine mambo ambayo wamejifunza. Kufanya hivyo kwawaongezea furaha, kwa maana Maandiko yatuambia, “Ni heri kutoa kuliko kupokea.”—Matendo 20:35.
Ikiwa wewe wataka uwe na furaha ya kutimiziwa mahitaji ya kiroho, wakaribishe Mashahidi wa Yehova wakuongoze katika funzo la Biblia nyumbani mwako au mahali penginepo panapokufaa, bila malipo. Ujionee mwenyewe jinsi mpango wa kawaida wa kula chakula cha kiroho unavyoweza kukupa mambo bora maishani na kukuongezea furaha nyingi ajabu.