Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 7/1 kur. 301-310
  • “Umtazame Mtu Mnyofu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Umtazame Mtu Mnyofu”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUZOEA ADILI KATIKA MAMBO YA NGONO NA UAMINIFU
  • UPENDO WA KIKRISTO HUVUTA
  • MATOKEO MEMA​—BAADA YA MIAKA MITANO
  • ZAIDI YA WAIGAJI WA MUNGU MILIONI MBILI
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Sehemu ya 4—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kitabu-mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1990
    1990 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 7/1 kur. 301-310

“Umtazame Mtu Mnyofu”

1. (a) Mtunga Zaburi Daudi alisema tuangalie watu wa aina gani? (b) Je! wako watu wa aina hiyo wanaoishi leo?

MTUNGA zaburi Daudi aliona ubora wa kupendezwa sana na wale wanaojaribu kuwa kama Mungu, kwa maana aliandika hivi: “Umwangalie sana mtu mkamilifu, umtazame mtu mnyofu, maana mwisho wake mtu huyo ni amani.” (Zab. 37:37) Wako watu wengi wa aina hiyo, na wote wana shughuli nyingi katika utumishi wa Mungu. Imekuwa furaha sana miaka yote hiyo kupata habari za wale wanaotembea katika nyayo za Kristo Yesu, wakijitoa wazihubiri habari njema, na kujaribu sana kuwa kama Yesu Kristo, ambaye alikuwa kama Baba yake. Kuhubiri kwao na kushikamana kwao na mwendo unaofaa huleta watu wengi kwa Mungu, kama mifano inayofuata ionyeshavyo.

KUZOEA ADILI KATIKA MAMBO YA NGONO NA UAMINIFU

2. Baada ya hotuba ya watu wote iliyokuwa juu ya adili ya mambo ya ngono, msemaji alizungumza mambo gani na watu wawili waliokuwako?

2 Ndugu aliyekuwa na pendeleo la kutoa hotuba ya watu wote katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova alikuwa akitetea kanuni bora ambazo Mungu ameweka mwanadamu azifuate; alikazia pia upendo wa Mungu. Katika hotuba yake alizungumza sana juu ya ufisadi wa wanadamu, akikazia wazo la kwamba malazi ya ndoa hayapaswi kuchafuliwa kwa kufanya uasherati. (Ebr. 13:4) Baada ya hotuba hiyo ya kupendeza sana, mwanamume mmoja na mkewe walimwendea msemaji wakamwuliza maulizo kadha, na ulizo moja lilikuwa hili: ‘Ikiwa mwanamume hawezi kufanya uasherati, anaweza kufanya nini?’ Ulizo lake halikuwa tofauti sana na mawazo ya kawaida ya wanaume katika ulimwengu. Hata huko nyuma siku za Paulo, yeye alisema kwamba kwa sababu ya kuwako kwa uasherati kila mwanamume awe na mke wake mwenyewe. (1 Kor. 7:2) Kwa hiyo msemaji akaeleza watu hao wawili kwamba ngono si jambo la kuchezea; ndoa ni kitu kizito sana, ilianzishwa na Yehova Mungu huko katika Bustani ya Edeni wakati Adamu na Hawa walipofanywa “mwili mmoja.” Msemaji akaendelea kueleza kwamba Kristo Yesu aliitaja ndoa ya kwanza, na kwamba huo ni mpango wa Mungu nao wapaswa kuendelea kuwa safi na kwamba malazi ya ndoa yasichafuliwe. (Mt. 19:4-6) Ikiwa kweli mwanamume ampenda mkewe, naye mke ampenda mumewe, na ikiwa watafuata kanuni bora zilizoandikwa katika Neno la Mungu, dhamiri zao zitakuwa safi. Hivyo watakuwa na ndoa yenye furaha, nao hawatapatwa na aina ya ugonjwa ulioenea sana ulimwenguni leo kwa sababu ya uasherati na ngono za namna nyingi. Watu hao watatu walikuwa na mazungumzo ya kupendeza sana, na mwishowe msemaji alipendekeza wawe na funzo la nyumbani la Biblia.

3. (a) Juma tano baadaye, mwanamume huyo kijana aliuliza ulizo gani? (b) Aliamua kufanya nini juu ya ugumu huo, na kwa sababu gani?

3 Juma tano baadaye, mwanamume huyo kijana alikuwa akijifunza Biblia kwa makini sana, akamwuliza mwenye kumfundisha ulizo zito. Alisema: “Mwezi wa Juni rafiki yangu alipatwa na tukio lisilotazamiwa na gari lake likapondeka. Akaniomba niseme ndimi dereva wa gari hilo ili alipwe pesa za bima. Wakati huo sikuona ubaya wo wote, nikasema nitafanya hivyo. Lakini, kampuni ya bima imepeleka jambo hilo mahakmani na mashahidi wote wamepaswa kwenda. Nikienda nikasimulie hadithi yangu ya kwanza nitasema uongo, na hiyo haipatani na Neno la Mungu. Baada ya kujifunza Neno la Mungu dhamiri yangu hainiruhusu kusema uongo.” Ulizo la mtu huyo lilikuwa, “Sasa nifanyeje?” Baada ya kuzungumza juu ya kanuni za Biblia zinazohusu uaminifu na unyofu, mwanamume huyo kijana aliamua kulipa hasara za gari hilo na kumwagiza mwanamume mwenye gari hilo afute dai lake kwa kampuni ya bima. (Yohana 8:44; Ebr. 13:18) Kwa hiyo shtaka mahakmani likafutwa. Sasa mwanamume huyo kijana ana dhamiri safi naye anajaribu kuzidi kuwa kama Mungu, ambaye ni mwenye haki. (1 Pet. 3:12) Kupenda unyofu kwa mtu huyo kulifanyiza mabadiliko makubwa katika maisha yake na sasa anakwenda nyumba kwa nyumba akizihubiri habari njema za ufalme wa Mungu.

4. Hivyo, watu hao wawili walikuwa wakifanya nini ili wazidi kuwa kama Mungu?

4 Jambo hilo lililoonwa latueleza nini? Kwa kujifunza Biblia, ingawa walikuwa wamekuwa wakifanya hivyo kwa juma tano tu, mume na mke huyo walikuwa wakijaribu kubadili maisha zao, wakijaribu kuzidi kuwa kama Mungu, aliyewaumba Adamu na Hawa. Wanajitahidi kuishi maisha zenye unyofu. Wanataka kujipatanisha na kanuni za Mungu. Hawafanyi tena uasherati wala hawana pupa katika maisha zao.​—Rum. 12:2; Efe. 5:5.

UPENDO WA KIKRISTO HUVUTA

5. (a) Yakobo 2:8 yatutia moyo tuonyeshe sifa gani? (b) Kama ilivyosimuliwa katika kusanyiko Uingereza, Shahidi alionyeshaje upendo huo?

5 Ili kuwa kama Mungu, lazima tupende sana watu wengine. Ziko njia nyingi ambazo watu wanaweza kuonyesha wanapenda jirani zao. (Yak. 2:8) Jambo lililoonwa lilisimuliwa katika kusanyiko Sheffield, Uingereza, katika kiangazi cha mwaka wa 1975. Bibi mwenye kusimulia jambo hilo alisema hivi: “Nilijisikia sifai kabisa miaka miwili iliyopita wakati mume wangu aliponiacha mimi na mwanangu wa miaka sita. Sikuwa na jamaa ya kutegemea. Nilikuwa mgonjwa; sikuwa na pesa. Sikuwa na moto wa kuota nyumbani. Ndipo jirani (mwanamke) alipoingia kupiga simu. Alipoona hali yangu, akarudi ameniletea chupa ya kahawa na keki kadha. Akakusanya dawa akanipa kisha akarudi na ndoo ya kuni na kunisaidia kwa mambo mengi, nalo jambo hilo likanichangamsha.

6. Ni hatua gani zaidi zilizosaidia mwanamke huyo afanye maendeleo ya kiroho?

6 “Nilishangaa sana, kwa sababu nilijua jirani yangu huyu alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Sikuzote nilikuwa nimejitenga naye kwa sababu nilidhani Mashahidi ni tofauti kwa njia fulani. Lakini tendo hilo la kijirani sana lilinionyesha wao ni watu wenye kufikiria wengine sana. Urafiki wetu ukaongezeka na juma chache baadaye akanikaribisha kwenye Jumba la Ufalme kuhudhuria mwadhimisho wa kifo cha Bwana Yesu wakati wa Ukumbusho. Tukaenda pamoja na mwanangu mdogo. Nilifurahi sana. Sikuona haya ingawa nilikuwa kati ya watu tusiojuana. Jioni hiyo jirani yangu mwema akanipa zawadi ndogo. Kilikuwa kitabu kiitwacho ‘Kweli Iongozayo kwenye Uzima wa Milele.’ Kwanza sikukisoma, lakini mwishowe nikaona kwamba kichwa cha sura mojawapo kilikuwa ‘Kujenga Maisha ya Furaha ya Jamaa.’ Hiyo ilinipendeza. Nikachunguza katika Biblia yangu mwenyewe nikaona kwamba kila jambo lililosemwa lilikuwa kweli. Karibuni nikawa na funzo la Biblia. Nilipojifunza Biblia husema nini juu ya talaka na ndoa katika Bwana, nikavunja uhusiano na mwanamume Mkatoliki niliyekuwa nikimfikiria anioe, kwa maana kufika wakati huo nilikuwa nimejifunza kwamba mtu hapaswi kutiwa katika nira isiyofaa, na kwamba Mkristo akioa au kuolewa, aoe au aolewe ‘katika Bwana.’​—1 Kor. 7:39; 2 Kor. 6:14.

7. Imeonekanaje katika utendaji wake mwenyewe kwamba anapenda watu wengine?

7 “Mimi namshukuru sana Yehova kwamba karibuni nilijiweka wakf nikabatizwa. Mwaka huu nimefanya upainia wa muda katika miezi mbalimbali ya mwaka, nami natumaini nitakuwa nimeufanya miezi mitano kabla ya mwaka kwisha. Ingawa nina nyumba ndogo tu, furaha yangu kuu imekuwa kuonyesha upendo wa kidugu kwa kuwapa ndugu na dada 20 mahali pa kulala katika kusanyiko letu la wilaya, na watano kati yao walilala katika hema uwanjani pangu. Sasa maisha yangu yanatosheleza, asante Yehova.”​—Rum. 12:13; 3 Yohana 5-8.

8. Kama inavyoonyeshwa katika Waefeso 5:1, 2, ni nini kitakachotusaidia tumpendeze Mungu?

8 Kwa hiyo, kujaribu kuwa kama Mungu na ‘kuishi katika upendo kama Kristo alivyotupenda’ bila shaka kwampendeza Mungu. (Efe. 5:1, 2, NE) Mtu akijifunza Neno la Mungu, akiliamini kwa unyofu na kujinyenyekeza mbele za Mungu aweza kufanya mabadiliko makubwa katika maisha yake.

9. Mwanamume mmoja Canada alionaje wakati mkewe na watoto walipoanza kwenda kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova, naye mke alifanya nini kwa hekima?

9 Ushirika na upendo wa kidugu unaweza kubadili sana maisha ya mtu. Kwa mfano, habari hii yatoka Ottawa, Canada: Mwanamke mshika dini aliye Mkatoliki katika Ottawa alianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova katika kundi lao. Alikwenda pamoja na watoto wake wote. Mmoja wao alikuwa amekuwa mtumishi katika altare (madhabahu) ya kanisa. Walipokuwa wakirudi kutoka Jumba la Ufalme, watoto walikuwa wakimwambia baba yao kwa furaha nyingi baadhi ya mambo waliyojifunza katika Biblia. Baba alifadhaika sana. Alitenda kama waume wengi. Kwa kukata tamaa kabisa, akamwambia mkewe na watoto kwamba lazima waache kujifunza na Mashahidi wa Yehova na wasihudhurie mikutano tena. Alifadhaika sana hata akasema atapiga wote risasi, pamoja na dada painia aliyekuwa akijifunza Biblia nao nyumbani kwao. Mke aliamini kwamba mumewe hakuwa akicheza kwa kusema hivyo. Kwa hiyo akampigia simu mzee katika kundi la Mashahidi wa Yehova akamwomba awatembelee na kujaribu kumweleza mumewe mambo yalivyokuwa. Pengine angeweza kuondoa maoni mabaya na chuki isiyo na msingi ya mumewe juu ya Mashahidi wa Yehova.

10. Wakati mzee alipomtembelea mwanamume huyo, alifanya nini juu ya hali hiyo?

10 Kwanza mwenye nyumba alikuwa baridi sana asitake kuzungumza. Lakini mzee alikuwa mwenye urafiki, mwenye fadhili na mwenye mafaa hata akasema anaelewa vile mwanamume angeona mkewe na watoto wakienda mahali pamoja pa ibada na yeye mahali pengine. (2 Tim. 2:24, 25) Mzee akaeleza kwamba yeye mwenyewe asingetaka mkewe awe na uhusiano na tengenezo ambalo yeye (mzee) hajui habari zake. Kwa hiyo akapendekeza mwenye nyumba ahudhurie angaa mkutano mmoja akaone ni watu wa aina gani wanaohudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Kwa kuwatazama wenye kuhudhuria, kusikiliza mambo wanayofundishwa, kwa kuona nia ya watu hawa, ndipo angekuwa katika hali bora ya kufanya uamuzi wa hekima juu ya faida za kiroho za jamaa yake.

11. Ni nini kilichomvuta mwanamume huyo alipokuja kwenye Jumba la Ufalme, na matokeo yalikuwa nini?

11 Mume huyo mwenye kupinga alikaribishwa kwa uchangamfu ahudhurie mmojawapo wa mikutano akaone tu mkewe hupendezwa na nini hasa. Wakaachana na mzee kwa urafiki na kila mtu alitaka sana kujua litakalotokea. Jumapili iliyofuata ikafika naye mume mwenye kupinga akaenda asubuhi peke yake kwenye kanisa lake, halafu akamshangaza sana mkewe na watoto alipokuja kwenye Jumba la Ufalme alasiri hiyo. Alivutwa sana na upendo mchangamfu na urafiki alioonyeshwa na akina ndugu hata akarudi Jumapili iliyofuata, lakini wakati huu hakwenda kwanza kwenye kanisa lake. Karibu na wakati huo funzo la Biblia lilianzwa pamoja naye, na mzee aliyekuwa amemtembelea nyumbani mara ya kwanza kulipokuwa kumechacha sana ndiye aliyeendelea kujifunza na mtu huyo kwa miezi mitatu. Sasa kusanyiko la wilaya likatangazwa, nao mji ambamo kusanyiko lingefanyiwa ulikuwa maili mia sita kutoka kwao. Mtu huyo alitaka kuona na kujua mengi zaidi. Kwa hiyo akaenda na jamaa yake kwenye kusanyiko lao la kwanza la wilaya. Upendo wa jirani, upendo wa Mungu, ambao ndio amri iliyo kuu zaidi ya zote, ulimvuta sana mume huyu. (Yohana 13:35; Mt. 22:35-39) Mwaka mmoja baadaye mwanamume huyo na mkewe wakabatizwa, naye amekuwa mwenye bidii sana kundini tena anafanya maendeleo mazuri ya kiroho.

12. Wale wanaojaribu kuwa kama Mungu wanafanya kazi gani kwa ajili ya watu wengine?

12 Onyo la upole la Paulo kwa Waefeso lafaa sana hapa. “Katika neno, kama watoto wa Mungu wapendwa, jaribuni kuwa kama yeye, na kuishi katika upendo kama Kristo alivyowapenda ninyi.” Zile sifa njema zilizotiwa ndani ya mwanadamu hapo kwanza wakati ule ule wa kuumbwa kwake, yaani, upendo haki ya hukumu, hekima na uwezo, zinasitawishwa leo na watu wengi. Zinaweza kusitawishwa. Tusidhani kwamba mfano ambao tumesoma ni jambo lisilowezekana kwa wengine. Sasa hivi wako watu zaidi ya milioni mbili wanaohudhuria kwa kawaida mikutano ya Mashahidi wa Yehova; na si hilo tu​—⁠wao wanazihubiri habari njema za Ufalme ulimwenguni pote, wakiletea watu wengi aina ile ile ya amani na furaha na uradhi. Mzee aliyetajwa sasa hivi alikuwa na shauku ya kulichunga kundi la Mungu, si kwa sababu ya kupenda faida ya udhalimu, wala si kwa sababu ya kulazimishwa, bali kwa hiari.​—1 Pet. 5:1, 2.

MATOKEO MEMA​—BAADA YA MIAKA MITANO

13. (a) Saburi ya Yehova imefaidije wanadamu? (b) Kulikuwa na matokeo gani wakati msichana mwenye kwenda shuleni alipoonana kwa ufupi na Shahidi mmoja?

13 Yehova amesubiri sana wanadamu. (2 Pet. 3:9) Hilo limekuwa jambo la faida sana, kwa sababu mara nyingi huchukua muda kabla moyo wa mtu haujapatana kabisa na makusudi ya Mungu. Inasisimua kuona jinsi vijana wanavyofahamu kweli ya Neno la Mungu kwa kipindi fulani, ijapokuwa wanapingwa sana na wazazi na kushawishwa na “masomo ya juu zaidi.” Kulingana na ripoti zinazotoka Ureno, karibu miaka mitano iliyopita msichana mmoja alikutana na mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliyekuwa akihubiri nyumba kwa nyumba. Habari kuu ya mazungumzo yao ilikuwa mageuzi. Baba ya msichana huyo alikubali kuchukua kitabu Evolution akakisoma, lakini alitetea bado fundisho la mageuzi, akajaribu sana kuvuta binti yake asiamini yanayosemwa na Biblia juu ya kuumbwa kwa mwanadamu. Wakati huo msichana huyo alikuwa akihudhuria masomo ya katekisimu katika Kanisa Katoliki, naye alimwuliza padre wake awaonaje Mashahidi. Akamwambia msichana kwamba Mashahidi wa Yehova hata hawamwamini Yesu Kristo. Miaka kadha ikapita bila ya kuonana tena na Mashahidi. Wakati wa miaka ya mwisho ya kuwako kwa msichana huyo katika masomo ya juu fundisho la mageuzi lilitokea likawa la kuzungumzwa. Msichana huyo alifaulu sana alipoanza kumbisha mwalimu juu ya hoja zake, akitumia mambo aliyopata katika kitabu Did Man Get Here by Evolution or by Creation?, ingawa hakueleza alipata habari hizo wapi. Mwishowe mwalimu akalazimika kukubali kwamba fundisho la mageuzi halina uthibitisho. (Ebr. 3:4) Hiyo ikamfanya msichana huyo afikirie kwa uzito habari nyingine za Biblia zilizoelezwa katika kitabu icho hicho.

14, 15. Mwishowe, ni nini kilichomwongoza msichana huyo aonane na Mashahidi, nayo matokeo yalikuwa nini?

14 Alipokwenda chuo kikuu, kukawa na maasi makuu ya mapinduzi Ureno. Kama watu wengine wengi yeye akajitia sana katika mazungumzo ya siasa na kuhudhuria mikutano yote ya kisiasa. Alivutwa sana na msemo “Usawa, Udugu na Uhuru.” Akawa mpiganiaji mwenye bidii wa chama alichochagua hatimaye. Lakini juhudi yake iliharibiwa na ugomvi wa kisiasa, akajua kwamba haiwezekani vyama vyo vyote vya kisiasa viunganishe wanadamu. Alipokuwa akiyafikiria mambo hayo, mwezi wa Desemba 1974, alichukua gazeti lake la Lisbon akaona ukurasa mzima wenye kusimulia kwamba Mashahidi wa Yehova wameandikwa kisheria. Alifurahi sana kusoma masharti yote ya tengenezo, akayaelewa makusudi ya Mashahidi wa Yehova. Sasa alisadiki kwamba Mashahidi wa Yehova ndio watu wa pekee wanaofundisha kweli ya Neno la Mungu.

15 Akachukua mara moja hatua za kuonana tena na Mashahidi, akatazama anwani iliyoandikwa katika gazeti, nayo ilikuwa anwani ya muda tu ya makao makuu ya shirika hilo. Kabla ya hapo Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepigwa marufuku Ureno. Funzo la Biblia likaanzwa pamoja na msichana huyo, na ingawa aliendelea kupingwa na wazazi wake, yeye aliendelea tu kujifunza hata akaelewa kabisa kusudi la Yehova ni nini. (Mt. 10:36, 37) Yeye pamoja na wenye kushirikiana naye walifurahi sana alipoonyesha wakf wake kwa Yehova Mungu katika “Enzi Kuu ya Kimungu” Kusanyiko la Wilaya katika kiangazi cha 1975 huko Lisbon. Ilimchukua miaka mingi kuamua, lakini alipata nafasi ya kuwaangalia sana wakamilifu na kuwatazama wanyofu. (Zab. 37:37) Kwa kuwa sasa amepata kumjua Yehova na anajitahidi kweli kweli kuwa kama yeye, wakati wake ujao utakuwa wenye amani. Atakuwa na uradhi wa akili na moyo.

ZAIDI YA WAIGAJI WA MUNGU MILIONI MBILI

16. (a) Kuna Mashahidi wa Yehova wangapi ulimwenguni pote? (b) Mwaka jana, ni wangapi waliobatizwa, na iliwapasa kufanya mabadiliko gani?

16 Hayo ni machache tu ya mambo yaliyoonwa na wahubiri 2,179,256 wa Mashahidi wa Yehova wakati wa mwaka wa utumishi wa 1975. Je! waweza kuwazia watu 295,073 wakiweka maisha zao wakf kwa Yehova mwaka jana na kupanga mambo yao ili wazihubiri habari njema za Ufalme kwa kwenda nyumba kwa nyumba na kuongoza mafunzo ya Biblia na watu ambao hawajapata kuonana nao hapo kwanza? Neno la Mungu lilibadili maisha zao. Waliuvua “utu wa kale.” Mtume Paulo aliusimuliaje? “Utu wa kale unaofanana na namna ya mwenendo wenu wa zamani na unaoharibika kulingana na tamaa zake za udanganyifu; bali mpate kufanywa wapya katika nguvu yenye kuendesha akili zenu, na kuuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika haki ya kweli na uaminifu.” (Efe. 4:22-24, NW) Kwa hiyo watu hao waliobatizwa wanajaribu kuwa kama yeye, yaani, kama Mungu. Wanaruhusu nguvu mpya iendeshe akili zao, nao utu mpya, kama unavyoitwa katika Maandiko, unaumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika haki ya kweli na uaminifu. Kwa hiyo watu hao waliobatizwa walitaka kufanya badiliko hilo, wakifanya hivyo kwa kushirikiana na tengenezo linalojulikana kama Mashahidi wa Yehova. Wao ni Wakristo.

17. (a) Ni wakati kiasi gani uliotumiwa katika utumishi wa shambani mwaka jana? (b) Ni watu wa aina gani waliofanya kazi hii?

17 Inapendeza kuona kutokana na ripoti yao ya kila mwaka kwamba watumishi wa Mungu hawa walitumia saa 382,296,208 kuhubiri. Huo ni wakati mwingi. Ni nani waliotumia saa zote hizo? Walikuwako wale wanaotumia saa nyingi kama wanavyoweza katika kawaida ya maisha ya kila siku wakijaribu kusaidia watu wapate ujuzi wa Biblia. Wengi wao wameoa au kuolewa na wana jamaa, nao hutoka nje siku za Jumamosi na Jumapili au jioni, pengine saa kumi au kumi na mbili kwa mwezi. Wako wengine ambao hupanga mambo yao watumie karibu saa mia moja kwa mwezi wakihubiri shambani, nao Mashahidi hao twawaita mapainia. Halafu wako mapainia wa pekee, wanaotumia saa 150 katika utumishi wa shambani na mara nyingi wao hufanya kazi katika maeneo mapya.

18. (a) Ni wangapi wanaofanya kazi ya upainia? (b) Kazi ya kuhubiri inafanywa katika nchi ngapi? (c) Magazeti yanasaidiaje katika kazi hii?

18 Ripoti ya mwaka yaonyesha kwamba walikuwako mapainia 114,491 na mapainia wa pekee 15,734 waliokuwa wakihubiri kwa kawaida kila mwezi mahali fulani ulimwenguni. Wako 2,456 wanaotumikia kama wamisionari. Kwa kawaida wao huwa mbali sana na makwao. Kwa kweli, habari njema hizi za Ufalme sasa zinahubiriwa katika nchi mbalimbali 210. Habari za Kristo Yesu hazihubiriwi katika Jumuiya ya Wakristo tu, wala hazihubiriwi kwa lugha moja tu. Kwa mfano, gazeti hili unalosoma huchapwa katika lugha mbalimbali 78 nalo lina mwenezo wa zaidi ya nakala milioni kumi za kila toleo. Mwaka wa 1975, nakala 513,705,582 za Mnara wa Mlinzi pamoja na gazeti mwenzi wake Awake! zilichapwa. Mashahidi wa Yehova ndio wenye kuyagawa magazeti hayo na kuyapeleka nyumbani kwa watu ili waweze kujifunza mengi zaidi juu ya Mungu Mwenye Nguvu Zote na kujaribu kuwa kama yeye.

19. (a) Kwa sababu gani sisi hugawa vitabu? (b) Kazi ya kurudia watu ilifanywa kwa kadiri gani mwaka jana?

19 Mashahidi wa Yehova hawagawi magazeti peke yake. Wana vitabu vizuri sana ambavyo wangependa kutumia kujifunza na watu wanaopendezwa katika nyumba zao wenyewe. Kwa kweli, mwaka jana watumishi hawa wa Mungu wa Kikristo walitoa vitabu 28,410,783 wakafanya ziara za kurudia 155,336,481 kwa wale waliovipokea vitabu hivyo. Wazia hili: Waliketi katika nyumba za watu mbalimbali wasiopungua 1,411,256 kila juma mwaka wa 1975 wakajifunza nao Biblia. Huko ni kujitoa. Huko ni kuonyesha unapenda jirani, nasi twakaribisha mtu ye yote ambaye angependa kufanya kazi kama Yesu Kristo na mitume walivyofanya miaka mia kumi na tisa iliyopita ashirikiane na Mashahidi wa Yehova na kuendesha utendaji wa aina ii hii.

20. Ulimwenguni pote, ni watu wangapi walioonyesha kwamba wanapendezwa kadiri fulani kwa kuhudhuria Ukumbusho?

20 Bila shaka yako mamilioni ya watu wanaopendezwa na kazi yetu. Lakini, si kila mtu anayeipenda na katika sehemu nyingi za ulimwengu kuna mateso. Serikali hazipendi tuhubiri juu ya ufalme ulio tofauti na wao​—yaani, ufalme wa Mungu kama tumaini la pekee la wanadamu. Mashahidi wa Yehova huhesabu kila mwaka wale wanaohudhuria Ukumbusho wa kufa kwa Kristo Yesu, na Machi 27, 1975, watu 4,925,643 walifika kwenye Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova kusikia mazungumzo yenye kuonyesha kifo cha Kristo Yesu kilimaanisha nini kwao na kwa wanadamu wote. Kama ulivyoona katika ripoti hii, watu 295,073 waliamua kujaribu kuzidi kuwa kama Yehova Mungu kwa kumtumikia kwa bidii na kuzihubiri habari njema za Ufalme, na kuvaa utu mpya, unaopatana na ule ambao Kristo Yesu alituwekea kama kielelezo tuufuate.

21. Kwa sababu gani ziara za kurudia na mafunzo ya Biblia zimeonyeshwa katika ramani ya utumishi iliyochapwa pamoja na makala hii?

21 Pengine wewe ungependa kupata habari zaidi juu ya mambo yanayofanywa na Mashahidi wa Yehova katika zile nchi na visiwa vya bahari mbalimbali 210 wanakofanya kazi kwa bidii. Ili kusaidia Mashahidi wa Yehova wote tumechapa ramani yenye kuonyesha hesabu ya watu waliobatizwa kila nchi, na pia hesabu ya makundi waliyo nayo. Kwa kuwa tumechapa saa zilizotumiwa katika utumishi wa shambani na Mashahidi wa Yehova wote katika nchi yako unaweza kuona ni ushuhuda wa aina gani uliotolewa katika eneo hilo. Ziara za kurudia na mafunzo ya Biblia ndiyo ya maana zaidi kwa Mashahidi wa Yehova, kwa maana tunaweza kuketi na watu nyumbani mwao na kujibu maulizo yao yanayohusu Biblia, tukielekeza akili zao kwenye Biblia tupate majibu ya maulizo wanayoweza kuwa nayo juu ya hali zilizomo ulimwenguni leo na kujua sababu ya Mungu kuruhusu uovu wa namna hiyo uwepo. Je! kutakuwa na mwisho wa ulimwengu? Je! yuko mtu kama Shetani Ibilisi mwenye kuleta madhara? Pengine wewe una maulizo elfu na moja. Kwa hiyo, ukitaka kujaribu kuwa kama yeye, yaani, kama Yehova Mungu, sisi twapendekeza sana utembelee mojawapo la makundi 38,256 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Fika kwenye Majumba yao ya Ufalme ufurahie ushirika nao wala usione haya kusema na ye yote na kumwomba ajifunze Biblia nawe. Tutapendezwa kujifunza nawe.

22. Kupatana na Zaburi 37:1-4, twasihi watu wote wanyofu wafanye nini?

22 Je! una magumu katika maisha yako? Je! una dhiki? Je! una wasiwasi wa kupata usalama? Je! unahangaishwa na hali zilizomo ulimwenguni? Basi sikiliza yaliyosemwa na Mfalme Daudi: “Usikasirike kwa sababu ya watenda mabaya, usiwahusudu wafanyao ubatili. Maana kama majani watakatika mara, kama miche mibichi watanyauka. Umtumaini [Yehova] ukatende mema, ukae katika nchi, upendezwe na uaminifu. Nawe utajifurahisha kwa [Yehova], naye atakupa haja za moyo wako.” (Zab. 37:1-4) Je! wewe waamini hilo? Sababu gani usijaribu kuona kama ni kweli. Ushirikiane na Mashahidi wa Yehova nao watakusaidia kwa furaha.

​—Kutoka The Watchtower, Jan. 1, 1976.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki