Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa—United States ya Amerika
“UMATI mkubwa” ni akina nani? Hilo lilikuwa ulizo lenye kusumbua watu wa Yehova kwa miaka mingi. Kwa muda mrefu walikuwa wamedhani “umati mkubwa” (“mkutano mkubwa,” UV) ni jamii ya pili ya kiroho ambayo ingeshirikiana na watiwa mafuta 144,000 mbinguni, kama wanawali wa kumsaidia Bibi-arusi wa Kristo. (Zab. 45:14, 15; Ufu. 7:4-15; 21:2, 9) Tena, mapema mwaka wa 1923 “kondoo” wa mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi walitambulishwa kuwa jamii ya kisasa ya kidunia watakaookoka Har–Magedoni na kuingia katika taratibu mpya ya Mungu iliyoahidiwa. (Mt. 25:31-46; Ufu. 16:14, 16) Volume ya 1931 ya kitabu Vindication (Kitabu cha Kwanza) ilitambulisha watu waliotiwa alama katika vipaji vya nyuso zao wapate kuhifadhiwa (Eze. sura ya 9) kama “kondoo” wa mfano wa Kristo. Mwaka wa 1932 iliazimiwa kwamba jamii hii ya kisasa ya “kondoo” ilikuwa imefananishwa mapema na mshirika wa Yehu Yonadabu. Kwa mara ya kwanza mwaka wa 1934 ilielezwa wazi kwamba “Wayonadabu” hawa walikuwa na matumaini ya kidunia wamepaswa wajiweke wakf kwa Yehova na kubatizwa. Lakini “umati mkubwa” unaotajwa katika Ufunuo sura ya 7 bado ulifahamiwa kuwa kama zamani.
Mashaka juu ya “umati mkubwa” yaliondolewa wakati Ndugu Rutherford alipozungumza habari hiyo wakati wa kusanyiko la Mashahidi wa Yehova Mei 30 mpaka Juni 3, 1935, katika Washington, D.C. Katika hotuba hiyo ilionyeshwa kwa Maandiko kwamba “umati mkubwa” ulikuwa na maana moja na “kondoo wengine” wa wakati wa mwisho. Webster L. Roe akumbuka kwamba J. F. Rutherford alisema hivi akifikia upeo wa hotuba yake: “Nyote walio na tumaini la kuishi milele duniani simameni tafadhalini. Kama asemavyo Ndugu Roe, “zaidi ya nusu ya wasikilizaji wakasimama,” kisha msemaji akasema: “TAZAMA! UMATI MKUBWA!” “Kwanza kukawa na kimya,” akumbuka Mildred H. Cobb, “kisha kukawa na vifijo na vigelegele vilivyochukua muda mrefu.”
Karibuni kusanyiko lilikwisha, lakini lilikuwa limeanza jambo jipya—utafutaji. “Tukiwa na shauku nyingi sana na hali mpya ya kiroho, tukarudi kwenye maeneo yetu tukatafute watu hawa wenye mfano wa kondoo waliopaswa kukusanywa,” asema Sadie Carpenter.
Baada ya kusanyiko la mwaka wa 1935, wengine waliokuwa wakila mkate na kunywa divai mfano katika maadhimisho ya Chakula cha Bwana cha Jioni waliacha. Kwa sababu gani? Si kwa sababu ya kukosa uaminifu, bali kwa sababu sasa walitambua kwamba matumaini yao yalikuwa ya kidunia, si ya kimbinguni. Na ijapokuwa vitabu vya Sosaiti vya miaka iliyotangulia vilikuwa vimekusudiwa viwe hasa kwa ajili ya wafuasi wa Yesu waliotiwa mafuta, tangu mwaka wa 1935 na kuendelea The Watchtower na vitabu vingine vya Kikristo vilitoa chakula cha kiroho kwa faida ya jamii ya watiwa mafuta na wenzi wao pia wenye matumaini ya kidunia.
ACHA KWELI IVUME!
Miaka ya 1930 watangazaji wa Ufalme walitumia mashine za kutangazia habari zilizotiwa katika sahani za santuri ili kutafuta wenye mfano wa kondoo. Henry Cantwell asema hivi juu ya mashine hizo: “Mwaka wa 1933, Sosaiti ilipoanza kupanua kazi ya kuhubiri, mipango ilifanywa kutia katika rekodi hotuba za Ndugu J. F. Rutherford alizotoa katika sehemu zote za nchi. Ili kufanya hivyo Sosaiti ikatengeneza mashine za kutumia umeme za kutangaza habari zilizotiwa katika sahani za santuri. Hivyo vilikuwa vinanda vikubwa vyenye kutiwa ufunguo kwa spring navyo vilikuwa na mkono wa sauti wa kutumia umeme na kikuza sauti kilichotiwa nguvu na beteri. . . . Tulikuwa tumetia mambo mbalimbali katika sahani za santuri. Nyingine zilikuwa kamili; nyingine za hotuba hizo zilitiwa katika sahani mbili au nne ndiyo zimalizike. Kwa hiyo tulikuwa na hotuba kwa dakika 75, dakika 30 na saa moja. Kwa njia hiyo tuliweza kuwa na mikutano ya watu wote katika maeneo mbalimbali tulikofanya kazi.”
“Sosaiti ilitumia mamia ya sahani hizo za kutangazia ujumbe wa Ufalme zenye kuzunguka mara 33 na theluthi moja kwa dakika,” kama asemavyo Ralph H. Leffler, naye aendelea kunena hivi: “Nyingi zilitumiwa na magari na vilori vya utangazaji. . . . Maneno ‘Ujumbe wa Ufalme’ ambayo ndiyo yaliyokuwa kichwa cha utangazaji yalionekana upande wa vyombo vingi vya kupazia sauti. Katika barabara na mashambani ujumbe ulisikiwa. . . . Nyakati nyingine gari la utangazaji likiwa limesimama kilimani kuelekea mji mdogo ulio bondeni sauti ingeweza kusikiwa maili nyingi wakati wa jioni.”
Akikumbuka waliyofanya, Henry A. Cantwell asema: “Tulikuwa tukiingia eneo fulani, tunapiga sahani fulani za muziki ili kuvuta watu, kisha tunatoa tangazo fupi katika kikuza-sauti halafu tunatoa mojawapo ya hotuba. Halafu tulikuwa tukitangaza kwamba watu mmoja mmoja wangefika milangoni kueleza habari zaidi kwa waliozitaka.” Kulikuwa na mashua za utangazaji pia nazo zilifanya kazi kwa njia ile ile.
Kwa miaka mingi kinanda cha kuchukuliwa kwa mikono kilisaidia sana kuhubiri Ufalme. Kusanyiko kubwa la Mashahidi wa Yehova, Septemba 15-20, 1937, katika Columbus, Ohio, lilisaidia sana kuendeleza kazi hii. Elwood Lunstrum atueleza haya juu ya kusanyiko hilo:
“Katika kusanyiko hili kazi ya kutumia kinanda cha kuchukua kwa mikono milangoni pa watu ilisemwa kwamba itaanzwa. Hapo kwanza tulikuwa tumekuwa tukichukua kinanda katika utumishi, lakini tulikuwa tukikifungua tulipokaribishwa ndani tu. . . .
“Mpango wa kuwa na ‘Mapainia wa Pekee’ ulielezwa katika kusanyiko la Columbus ili kuongoza matumizi ya kufika milangoni na kinanda na kufanya kazi ya kurudia wenye kupendezwa (iliyoitwa hapo kwanza ‘marudio’) na pia ya mafunzo ya Biblia pamoja na mpango ulioitwa ‘funzo la kielelezo.’ “
Sasa wazia kwamba wewe u mtangazaji wa Ufalme katika utumishi wa shambani makumi matatu ya miaka iliyopita. “Mwenye nyumba alipofungua mlango, tulikuwa tukisema, ‘Nina Ujumbe wako.’ Pale pale tulikuwa tukiwekelea sindano ya kinanda nayo sauti ya Ndugu Rutherford ilitokea kwa mshindo,” akumbuka L. E. Reusch. “Mwishoni mwa ujumbe huo,” aeleza Angelo C. Manera, Mdogo, “msemaji alikuwa akitaja kitabu tulichokuwa tukitoa na bei yacho. Kisha sisi tulikitoa na kukiangusha, ikiwa mwenye nyumba alipendezwa.” “Hatukuwa kamwe wajeuri kwa watu,” aeleza George L. McKee, “lakini tulikuwa na hakika kwamba kila mtu alipaswa kuzisikia habari njema za Ufalme.”
Ijapokuwa kulikuwa na upinzani, kazi ya kutumia kinanda iliendelea. Kidogo kidogo, chombo hicho kiliacha kutumiwa katika utumishi wa shambani miaka ya 1940. Baada ya 1944 shughuli hiyo ya kuhubiri iliyochukua miaka kumi na ya kutumia kinanda ilianza kubadilishwa kwa kutumia vinywa kutoa ushuhuda milangoni.
Kati ya vyombo vya kutolea ushuhuda viliyotumiwa ilikuwako kadi ya ushuhuda, iliyoanza kutumiwa mwishoni mwa mwaka wa 1933 mpaka miaka ya 1940. John na Helen Groh waeleza hivi: “Wahubiri wa habari njema hawakuwa wengi sana kama leo wala hawakuwa wamezoezwa sana kama leo. Ili kutusaidia katika kazi yetu na kumaliza maeneo kwa njia nzuri zaidi, tulitumia kilichoitwa kadi ya ushuhuda. Hayo yalikuwa mahubiri mafupi yaliyochapwa ambayo watu waliombwa wayasome.”
Je! wewe ungependa kujua vile wazo la kutoa magazeti barabarani lilivyoanza? S. E. Johnston akumbuka kwamba mwaka wa 1935 Sosaiti iliandikia barua watumishi wote wa eneo la dunia (waliokuwako kabla ya waangalizi wa mizunguko wa sasa) ikawaomba wajaribu kutumia njia tofauti za kuangushia watu The Watchtower na Consolation. Ndugu Johnston alifikiria vijana wenye kuuza magazeti yale ya kawaida kwa kuchukua mifuko mabegani pao. “Kwa sababu gani tusijaribu jambo kama hilo?” akawaza. Dave na Emma Reusch walikubali kutengeneza mifuko ya magazeti naye binti yao, Vera Coates, akaiandika “Watchtower” upande mmoja na Consolation upande ule mwingine” kwa kutumia kitambaa cha hariri. Wakati Ndugu Johnston alipotembelea kundi dogo katika Concord, California, kikundi kilijiunga naye kutoa ushuhuda wa barabarani. Yeye aandika hivi: “Juma iliyofuata jama ya Reusch ikatutengenezea mifuko zaidi ya magazeti, na wakati huu tulijaribu kuitumia katika barabara zilizo katika sehemu za biashara za Oakland. Ndugu wengine walikuwa na haya kidogo kwanza, lakini kazi ya barabarani ilipata nguvu nasi tukaanza kupata maagizo kutoka kampuni [makundi] nyingine tuwapelekee mifuko ya magazeti. Wakati huo, nikaandika ripoti kwa Sosaiti kuwajulisha mambo yalivyokuwa, nikawapelekea mfuko mmoja kama mfano . . . Sosaiti ikaniandikia barua, ikatushukuru sisi sote kwa kufanya jaribio hilo, na kusema kwamba wangetangaza jambo hilo karibuni katika Informant (Utumishi wa Ufalme.) Walifanya hivyo.”
—Kutoka 1975 Yearbook of Jehovah’s Witnesses.