Kitabu-mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1990
Uthibitisho upo kila mahali. Unauona katika Afrika, Esia, Ulaya, Bara za Amerika, na visiwa vya bahari vilivyotapakaa. Huenda ukauliza, ‘uthibitisho wa nini?’ Kwamba umati wenye kuongezeka unamtukuza Mungu na kujithibitisha kuwa wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo.
Wanafanyaje hivyo? Kwa kuzaa matunda mengi mazuri. Hili ndilo jambo tunalopaswa kutazamia kwa kuwa Yesu mwenyewe alisema: “Hivyo hutukuzwa Baba yangu, kwa vile mzaavyo sana; nanyi mtakuwa wanafunzi wangu.” (Yohana 15:8) Wakati mtu anapochagua matunda halisi ili ayaweke mezani, yeye hutafuta yaliyo bora. Je! tunapaswa kuangalia jambo lisilo bora katika maisha na kazi ya wale wanaodai kuwa wanafunzi wa Kristo? Kwa kuwa ubora ni jambo la maana, wapaswa kuonekana wazi katika utendaji na njia ya maisha ya kila mmoja anayemtumikia Mungu.
Katika kumtukuza Mungu, Wakristo wanatumikia pia masilahi muhimu ya wanadamu wenzao. Kwa sababu hiyo, kazi yao inatofautiana sana na kazi za kawaida za wanadamu. Kazi yao kubwa ni ipi hasa? Kwenye Mathayo 13:18-23, Yesu alitoa kielezi cha jambo hili kwetu sisi. Kwenye mstari wa 23 wa fungu hilo, aliwatambulisha wale watu wanaopata maana ya neno la Ufalme kuwa wale ambao kwa kweli wanazaa matunda, wakizaa 100 au 60 au 30. Basi, kazi ya Wakristo wa kweli ni kuzaa tunda—kupiga mbiu kwamba Ufalme ndicho chombo cha Mungu cha kuletea wakaaji wa dunia baraka za uhai usio na kikomo. Hiyo ndiyo kazi ambayo Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakifanya muda wote wa karne hii. Katika 1989 walizaa tunda jingi zaidi ya wakati uliopita kwa kuwahubiria watu katika mabara 212 habari njema za Ufalme.
Ni nini kinachofanya Mashahidi wa Yehova wawe tofauti sana hivyo? Ni ujumbe wetu wenye kutegemea Biblia na sifa za kimungu zinazohusiana na kazi yetu muhimu. Yesu alikazia sifa fulani za maana sana ambazo wafuasi wake wangekuza na kuonyesha. Kwenye Yohana 13:35 yeye aliwaambia hivi: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” Hata wawe wanatumikia wapi katika shamba la ulimwenguni pote, upendo huu wenye kujidhabihu kama wa Kristo, ungewatambulisha.
Pia wangekuwa na shangwe ambayo bwana-mkubwa wao alikuwa nayo. (Yohana 15:11) Si kwamba wangekuwa na matazamio yenye kuleta shangwe tu bali kutoa ushahidi kwao kungewaletea shangwe. Zaidi ya hilo, ingawa wanaishi katika ulimwengu wenye kutaabika, wangekuwa na amani. (Yohana 14:27; 16:33) Wangedumisha amani hii isiyo na kifani hata ingawa watu wengi wangekataa ujumbe wao.—Mt. 10:12, 13.
Upendo, shangwe, amani—sifa hizi ni miongoni mwa zile za kwanza zinazoorodheshwa kwenye Wagalatia 5:22, 23, NW kuwa matunda ya roho. Kutokeza sifa hizi na nyingine za kimungu tunaposhiriki katika huduma ya Kikristo na katika pande zote za maisha yetu ya kila siku kunamtukuza Mungu na hutuletea upendeleo wake. (Mt. 7:17-20) Kwa kuzaa matunda mengi mazuri, sisi, tulio ushirika wa ulimwenguni pote wa Mashahidi wa Yehova, tunatoa uthibisho wenye nguvu nyingi kwamba, sisi, tunatembea inavyolistahili jina tukufu ambalo tunabeba, na kwamba, tu wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo.—Kol. 1:10.
Kuchachawa Katika Paradiso Yetu ya Kiroho
Muda mrefu uliopita Yehova alitabiri juu ya hali ya kiroho yenye kusitawi ambayo taifa la watu wake linaonea shangwe sasa. (Isa. 51:3) Kupanuka kwa paradiso yetu ya kiroho kunatokeza ongezeko la hesabu ya watu wanaoikaa. (Isa. 26:15; 60:22) Hivyo, ni shangwe iliyoje kuona vilele vingi vya wahubiri katika mwaka wa utumishi uliopita! Ingawa wastani wa hesabu ya Mashahidi kila mwezi ilikuwa 3,624,773, kulikuwa na kilele cha 3,787,188 ambao walishiriki kuzaa tunda. Huo ndio uliokuwa mwaka mkubwa kuliko yote kwa kiasi cha wakati uliotumiwa katika kuhubiri Ufalme, jumla ya saa 835,426,538 zikitolewa kwa kazi kubwa ambayo inamtukuza Yehova.
Ili wathibitishe kwamba kwa kweli wao ni wanafunzi wa Kristo, Mashahidi wa Yehova wanahakikisha kwamba wanafunza wengine mambo yote ambayo Yesu Kristo amewaamuru wao. Hii ndiyo sababu waliongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani 3,419,745 kila mwezi kwa wastani, hii ikatokeza ubatizo wa wanafunzi wapya 263,855 wakati wa mwaka. Uwezekano wa umati mkubwa wa watu wengine wakishirikiana na watu wa Yehova kwa kutenda unaweza kuonekana pia katika uhakika wa kwamba 9,479,064 walihudhuria Ukumbusho. Fikiria sasa maono mengine yenye kuvuta fikira na yenye kusisimua na ripoti za mwaka wa utumishi uliopita.
Kupanda na Kuvuna kwa Wingi
Ijapokuwa msukosuko wa kisiasa mkubwa wa nchi yenyewe katika Panama, tawi laripoti mwaka mwingine wenye matunda mengi kwa Mashahidi wa Yehova. Jumla ya 731 waliobatizwa mwaka wa utumishi uliopita ni mara tatu zaidi ya hesabu ya watu waliobatizwa mwaka wa utumishi uliotangulia na ilikuwa karibu asilimia 13 ya wahubiri wote katika nchi hiyo. Hesabu ya wahubiri waliojiandikisha kuwa mapainia wa kawaida yaendelea kuongezeka, na sasa kuna karibu mara tatu zaidi ya waliokuwako katika mwaka wa utumishi wa 1984.
Ndugu zetu walioko kwenye kisiwa cha Karibea cha Guadeloupe wamekuwa na vilele saba katika wahubiri. Kilele cha hivi karibuni cha Mei, 5,980 wakiripoti, chafanya kuwe na uwiano wa mhubiri 1 kwa wakazi 55. Je! akina ndugu wamevunjika moyo kwa sababu ya kutembelea watu wale wale katika eneo? Tawi lajibu hivi: “La, sivyo kabisa!” Kama tokeo la ziara zao za mara nyingi, hesabu ya mafunzo ya Biblia ya nyumbani ilifikia kilele cha 8,438.
Katika Jameika upendo ulioonyeshwa na akina ndugu umetokeza ushahidi mzuri. Wakati Kimbunga Gilbert kilipopiga kisiwa hicho, Majumba ya Ufalme 35 yaliharibiwa kidogo, pia mengine 11 pamoja na makao 238 ya akina ndugu yaliharibiwa kabisa. Jambo hili lilitokeza upendo mwingi sana wa udugu wa ulimwenguni pote. Wenye kujitolea kutoka United States, Kanada, na Netherlands Antilles pamoja na akina ndugu wenyeji walitengeneza upya na kujenga tena majengo yaliyoharibiwa. Tawi laandika hivi: “Mwanamke mmoja ambaye alikuwa akijifunza na kuhudhuria mikutano alitengenezewa nyumba yake na akina ndugu. Jambo hilo lilikuwa na matokeo mazuri sana kwake, na tangu wakati huo amekuwa mhubiri. Kwa kuona upendo ulioonyeshwa, dada yake aliomba funzo la Biblia. Mwezi mmoja baadaye, aliandikia kanisa lake barua ya kujiuzulu naye amekuwa akihudhuria mikutano ya kundi ijapokuwa dhihaka na upinzani.”
Ongezeko laendelea katika Kosta Rika. “Ilikuwa shangwe iliyoje kwetu kufikia kilele cha wahubiri 12,001 katika mwaka huu wa utumishi!” tawi laripoti. “Pia, katika Januari 1989 tulikuwa na shangwe nyingi kwa kuwa na hesabu ya mapainia wasaidizi, 2,007 wakilinganishwa na kilele chetu kilichopita cha 785.” Na Malesia yaandika: “Mwaka wa utumishi wa 1989 umethibitika kuwa wenye kuleta shangwe sana.” Februari uliopita akina ndugu walipita alama ya 1,000 katika wahubiri. Vilele vipya vilivyofuata vilifanya jumla iwe 1,102. Hudhurio la Ukumbusho lilikuwa kilele kipya, 2,790.
Mwenendo mzuri wa ndugu zetu unatia ndani kuwa “wenye kuamanika pamoja na watu wote.” (Rum. 12:18, NW) Hii inavuta watu wenye mioyo yenye ufuataji haki. Katika Kenya mwanamke mmoja alipinga ukweli na akawakataza watoto wake wasicheze na watoto Mashahidi. Hata hivyo, baada ya muda fulani, alimwendea jirani yake ambaye ni Shahidi akamuuliza ni kitu gani kilichofanya Mashahidi wawe tofauti sana hivyo. “Nyinyi hampigani kamwe. Jamaa yenu ni yenye amani sana,” akasema mwanamke huyo. Funzo la Biblia lilianzishwa pamoja naye, na leo mwanamke huyu yumo katika ukweli.
Katika New Zealand barua ya Kanisa la Uingereza ilionya kwa hofu kuhusu “hatari kwa imani.” Ilitaja kwamba makanisa fulani ya nchini yanafungwa na kwamba haiwezekani tena kutegemeza wahudumu wenye kulipwa katika sehemu zote za nchi. Tofauti na hilo, ripoti ya tawi kutoka nchi hiyo yatoa maelezo haya: “Kama uthibitisho wa imani iliyo hai, kilele cha wapiga mbiu ya Ufalme 11,007—ongezeko la asilimia 9.6 zaidi ya wastani wa mwaka uliopita—walishiriki katika kufanya ‘julisho la peupe la wokovu.’”—Rum. 10:10, NW.
Katika Lebanoni yenye kusumbuliwa na vita, kama ilivyo katika sehemu nyingine za dunia zenye msukosuko, inataka imani kubwa kuhudhuria mikutano na kushiriki katika kuhubiri habari njema. Akina ndugu walipokuwa wanahudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme lao, makombora yalianza kulipuka karibu na hapo. Wakati makombora yalipoendelea kupiga kwa nguvu na kuzidi kukaribia jumba hilo, walio wengi wa akina rafiki waliokuwa wakihudhuria Funzo la Mnara wa Mlinzi walianza kuhangaika na kuwa na wasiwasi. Kwa kuhisi hivyo, waangalizi walianza kuwatia moyo wote kwa uchangamfu na utulivu waweke tumaini lao kwa Yehova na kumtegemea, kwa kuwa yeye hulinda nafsi za waaminifu wake. (Zab. 97:10) Baada ya kuokoka hatari hiyo, walimshukuru Yehova kwa ajili ya usalama wao.
Mavuno mengi yanavunwa katika Ureno. Miaka mitano iliyopita tawi liliangalia jumla ya wahuburi 34,091 katika maeneo sita. Sasa kuna wahubiri 48,044. Hili ni ongezeko la asilimia 41. Kilele cha hesabu ya mafunzo ya Biblia ya nyumbani kinachoripotiwa katika maeneo yote kilikuwa 61,657, ongezeko zuri sana la asilimia 64 katika wakati wa miaka hiyo mitano. Miezi fulani, makundi kadhaa katika nchi moja yalikuwa na wengi wakitoa ripoti wakiwa mapainia zaidi ya wahubiri. Kwa kielelezo, kundi moja liliripoti mapainia wa kawaida 10, mapainia wasaidizi 83, na wahubiri 58. Wangali wanaliona eneo lao kuwa lenye kutoa mazao, kwa kuwa wanaripoti mafunzo ya Biblia ya nyumbani 99, na hili ni jiji ambalo uwiano wa wahubiri kwa idadi ya watu ni 1 kwa 160.
Kitendo cha kuonyesha fadhili kinaweza kuwa njia ya kuwasaidia wengine wajifunze ukweli. Walipokuwa wakitembea kwenda nyumbani wakitoka katika utumishi wa shambani, wahubiri wawili Wareno walimwona mwanamke mzee-mzee akishuka kutoka ndani ya basi, ambaye alionekana kuwa mgonjwa. Wao walisimama wakamwuliza mwanamke huyo kama anahitaji msaada. Alishangaa sana kwamba watu wawili asiowajua kabisa wangeonyesha kupendezwa naye, akasisitiza anataka kujua ni jambo gani lililotokeza wonyesho huo wenye fadhili. Jambo hili lilifungua mlango wa kutoa ushahidi kifupi. Mwanamke huyo akawapa dada hao anwani yake mara hiyo na kuwaalika kwa uchangamfu wamtembelee. Ziara ya kurudia ilifanywa, na funzo la Biblia la nyumbani likaanzishwa. Upesi mwanamke huyo akaharibu sanamu zake, akaanza kuhudhuria mikutano, na sasa anashiriki kweli za Biblia pamoja na rafiki na jamaa pia.
Ushahidi wa Vivi-Hivi Wazaa Tunda
Yesu aliwashauri wanafunzi wake waache nuru yao iangaze. Kwa kufanya hivyo katika kila fursa leo, Mashahidi wa Yehova wanawafikia watu wengi kwa habari njema. Ndugu mmoja katika Brazili anaripoti: “Sikuzote mimi huweka Biblia na fasihi yangu katika kabati yangu kwenye mahali pa kazi ili niweze kutoa ushahidi wakati wa chakula cha mchana. Nilimwangushia mwuguzi wa kiume kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani kwenye kiwanda. Karibu na wakati ule ule, ndugu mwingine alimwangushia mwuguzi wa kike nakala ya kitabu icho hicho, naye akakiweka tu ndani ya kitoto cha dawati. Mwuguzi wa tatu alikipata kitabu hicho na kukisoma chote katika muda wa saa saba, akikionea shangwe sana. Mwanamke huyo aliongea juu ya kitabu hicho pamoja na mwuguzi wa kiume ambaye nilikuwa nimemwangushia kitabu kimoja, naye mwanamume huyo akamjulisha kwangu. Nilikaribisha mwanamke huyo kwenye mkutano, naye akaja pamoja na watoto wake watatu. Funzo la Biblia lilianzishwa pamoja na jamaa hiyo. Sasa mmoja wa binti hao anajitayarishia ubatizo. Mama na yule binti mwingine wanashiriki utumishi wa shambani, naye mume anajifunza na kuhudhuria mikutano pamoja nao.”
Katika nchi moja ya Amerika ya Kati ambako kazi yetu imezuiwa, ndugu mmoja aliyekuwa anangojea katika kituo cha basi alimtolea trakti mbili mwanamume kijana ambaye pia alikuwa anangojea hapo. Mazungumzo mazuri juu ya Ufalme wa Mungu yakafuata. Mwishowe ikawa lazima wote wawili waondoke. Miezi kadhaa baadaye mnenaji mwenye kuzuru alikuja kwenye kundi la yule ndugu, mwanamume mmoja kijana akiwa anaambatana naye. Wakati mwanamume huyu kijana alipomwona yule ndugu, alimwendea na kumuuliza: “Je! wanikumbuka? Mimi ni yule mtu uliyeongea naye kwenye kituo cha basi miezi fulani huko nyuma. Majuma machache baada ya wewe kunipa zile trakti mbili, nilikubali funzo la Biblia. Leo mimi ni mhubiri na ninapanga kubatizwa karibuni.”
Kujenga Majumba ya Ufalme Zaidi
Kazi ya kukusanya inapoendelea wakati wa majira haya ya mavuno, kuna uhitaji wa Majumba ya Ufalme zaidi. Ujapokuwa upinzani fulani kutoka kwa jamii ya kidini katika Italia, tawi la huko laandika kwamba Mashahidi wa Yehova “wanatoka kwenye majumba badala, kama vile magaraji, maghala, nyumba za orofa ya chini, na maduka, na sasa wanakusanyika pamoja katika Majumba ya Ufalme au Majumba ya Makusanyiko yaliyo mazuri wakionekana waziwazi na watu wote.” Sasa kuna Majumba ya Makusanyiko 12 katika Italia. Moja lilizinduliwa kiangazi kilichopita, na mengine matatu yanajengwa.
Katika Chile mafunzo ya Biblia ya nyumbani zaidi ya 50,000 yanaongozwa, na hudhurio la Ukumbusho lilikuwa mara tatu ya hesabu ya wahubiri. Tawi lasema hivi: “Limekuwa jambo lenye uharaka sana kujenga Majumba ya Ufalme zaidi ambayo yanatukuza ibada ya Yehova, na hili limekuwa ukuzi wenye kutokeza wakati wa mwaka wa utumishi.” Majumba ya Ufalme 12 makubwa yakiwa yamejengwa katika Bolivia, matazamio ya ukuzi wa wakati ujao huko yanaonekana kuwa maangavu zaidi.
Ailandi yaripoti kwamba hata makundi ambayo yana wahubiri walio chini ya 30 yameweza kujenga Majumba ya Ufalme mazuri. Kazi nyingi imefanywa pia katika Taiwani. Kati ya makundi 22 ambayo sasa yanatenda katika kisiwa hicho, 12 yamejenga au kununua Majumba ya Ufalme yao wenyewe au wanajitayarisha kufanya hivyo.
Ujenzi wa Majumba ya Ufalme waendelea kwa kasi katika Australia. Zaidi ya Majumba ya Ufalme mapya 170 yalijengwa wakati wa miaka mitano iliyopita. Majengo matano yalimalizika mwaka huu uliopita katika Trinidadi. Makundi mengine mawili yalijenga upya majengo ili kuwe na nafasi ya ongezeko. Katika Jameika ile njia ya “kujenga upesi” Majumba ya Ufalme mapya ilitumiwa kwa mara ya kwanza. Katika mahali pamoja meya wa mji alikuja kuona jengo lililokamilishwa. Mwanzoni yeye alikuwa na mashaka kuhusu jengo hilo, na yeye alihisi kwamba mtu yeyote aliyesema kwamba lingemalizika katika siku mbili alikuwa mwenye kichaa. Lakini baada ya kuona na macho yake mwenyewe, alistaajabia sana uwezo wa akina ndugu.
Mambo ya Kisheria
Katika Aprili 1, badiliko lilitokea katika hali na njia ya kitengenezo ya Mashahidi wa Yehova katika Meksiko. Sasa sala inaweza kutolewa kwa uhuru kwenye mikutano yote ya kundi, na Biblia yaweza kutumiwa kwenye utumishi wa shambani. Mwanamke mmoja, aliye mtendaji katika programu ya funzo la Biblia ya Kikatoliki, alisema hivi kuhusu uhuru mpya wa kidini wa Mashahidi: “Ikiwa mwanzoni walituacha tukiwa hatuna la kusema, sasa kwa vile wanafungua Biblia kwenye milango, sisi tumepotelea mbali!”
Katika miaka ya majuzi mlango ulifunguliwa katika Ulaya ya Mashariki kwa Wakristo waliojiweka wakfu wazae tunda kwa kadiri kubwa zaidi. Katika Polandi, mazungumzo yaliyochukua muda mrefu yalifanywa kati ya ndugu wenye madaraka na maofisa wa serikali kuhusu kuwapa ndugu hali inayotambuliwa kisheria. Katika Mei 18, ombi la shirika la kidini la Mashahidi wa Yehova lilikubaliwa na likaandikishwa rasmi—kwa wakati unaofaa kabisa kwa ajili ya mikusanyiko mikubwa ambayo ilikuwa inapangwa ifanyiwe Chorzów (karibu na Katowice), Poznan, na Warsaw.
Zaidi ya mwezi mmoja tu baadaye, Juni 27, akina ndugu katika Hangari waliona shangwe wakati Mashahidi wa Yehova walipotambuliwa kisheria katika nchi hiyo. Kwa mara ya kwanza, wenye mamlaka waliwaruhusu watumie mahali pa kufanyiwa mikutano ya watu wote kwa ajili ya mikusanyiko ya wilaya yao katika majiji mbalimbali.
Mashahidi wa Yehova kila mahali wanashangilia pamoja na wafanya kazi wenzao katika Meksiko, Hangari, na Polandi. Yehova na abariki utendaji wao sana wanapozidi kuzaa tunda la Kikristo na kutimiza penzi lake kikamili.—1 The. 4:1, 9, 10.
Kukabili Swali la Damu
Kuenea kwa haraka kwa UKIMWI kunahangaisha ulimwengu, kutia na kisiwa kidogo cha Pasifiki ya Kusini cha Tonga. Mapema katika Novemba mwaka uliopita, mkutano wa siku moja ulifanywa kuhusu visababishi na njia za kuzuia UKIMWI katika Tonga. Mwakilishi aliyetoka katika WHO (Tengenezo la Afya Ulimwenguni) alikuwapo pia. Miongoni mwa maswali yaliyoulizwa ni kama viongeza-kiasi cha umajimaji katika damu visivyo na damu vinapatikana katika nchi hiyo. Wale waliokuwapo walijulishwa msimamo ambao Mashahidi wa Yehova wanachukua kuhusu matumizi ya damu. Na kijitabu Mashahidi wa Yehova na Suala la Damu kiligawanywa pamoja na toleo la Amkeni! ya Oktoba 8, 1988, (Kiingereza) iliyokuwa ikishughulika na habari inayohusu UKIMWI. Isipokuwa mtu mmoja tu, wote walikubali mara hiyo vichapo hivyo.
Katika visiwa vilivyo karibu vya Samoa ya Magharibi, daktari wa baraza la kitiba la hospitali ya taifa alionyesha kwamba madaktari wanapaswa kuwatibu wagonjwa kulingana na kupenda kwao na wasiharibu dhamiri ya mgonjwa. Alieleza kwamba Mashahidi wa Yehova wana nia ya kupata aina nyingine ya matibabu, kwa hiyo hata kwa kuangalia mambo kwa maoni ya kitiba, madaktari wapasuaji wana sababu nzuri ya kuheshimu mapenzi yao.
Mikusanyiko Ambako Msongamano wa Watu Wambariki Mungu
Mtunga zaburi Daudi alipata furaha nyingi kuwa miongoni mwa msongamano wa watu waliokusanyika kumbariki Yehova. (Zab. 26:12) Na kwa kweli ndivyo watu wa Yehova wamehisi ulimwenguni pote wakati wa mwaka wa utumishi uliopita. Kulikuwako 6,273,804 waliohudhuria “Haki ya Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya wakati wa sehemu ya mwisho ya 1988 na mapema 1989.
Baadhi ya akina ndugu walihitaji jitihada ya pekee ili wahudhurie. Kwa kielelezo, katika Mianmari (iliyokuwa Burma hapo kwanza) haikuwa salama kusafiri katika sehemu fulani-fulani kwa sababu ya hali zenye hatari. Ijapokuwa hatari, wahubiri fulani walitembea kwa siku kadhaa na kupanda magarimoshi yaliyokuwa yamesongamana watu ili wasikose karamu yao ya kiroho. Na katika Kenya wahubiri walipanda baiskeli au wakatembea kilometa nyingi ili wahudhurie.
Kuhusu hali ya kutokuwa na ubaguzi wa rangi iliyoonekana wazi kwenye mikusanyiko yetu, ndugu mmoja kutoka Zambia aliyeenda Afrika Kusini aliandika hivi: “Lilikuwa jambo zuri ajabu kuwapo hapa kwenye mkusanyiko katika Johannesburg. Nilionea shangwe sana ushirika wa akina ndugu wa rangi mbalimbali—wote wakiwa pamoja kama jamaa moja.” Mwanamume kijana Mwislamu katika Senegali ambaye alikuwa hajawahi kuhudhuria yoyote ya mikutano yetu alipendezwa sana na roho yenye upendo ya wenye kuhudhuria mikusanyiko na msimamo ulio wazi unaochukuliwa na Mashahidi wa Yehova dhidi ya mazoea mabaya. Baada ya programu Jumamosi, hakuhisi vizuri kuendelea kuweka talasimu na hirizi za bahati nzuri ambazo alikuwa amefunga kuzunguka kiuno chake ili apate ulinzi. “Sioni tena uhitaji wa kuzitumaini,” akakiri. “Mimi najua kwamba Mashahidi wa Yehova ndio wana ukweli, na hakuna mmoja wao anayevaa talasimu ili apate ulinzi. Yehova ndiye anayewalinda.”
Usafi na utaratibu mzuri ambao ni sifa njema ya kawaida ya mikusanyiko yetu hutoa ushahidi mwema. Msimamizi mmoja kwenye stediamu moja katika Brazili alisema: “Ilikuwa furaha kuwa nanyi hapa, kwa kuwa inamaanisha kwamba stediamu itakuwa safi na itaachwa katika hali yenye utaratibu. Mnapaswa kupongezwa kwa usafi wenu. Njoni tena!”
Mikusanyiko ya wilaya ya 1989 ilikuwa na kichwa, “Ujitoaji Kimungu.” Hudhurio zuri limeripotiwa kutoka sehemu nyingi za dunia, pamoja na kubatizwa kwa mamiriadi. Kwa kielelezo, hudhurio la eneo la tawi la United States lilifikia 1,366,700, na watu 18,011 walibatizwa. Mfululizo huu wa mikusanyiko utaendelea kuingia sehemu ya kwanza ya mwaka wa utumishi wa 1990 katika Kizio cha Kusini.
Hata hivyo, wakati wa mwezi wa Agosti 1989, Polandi ilikaziwa fikira. Mambo ambayo watu wa Yehova walipata kuona huko yalikuwa hayasahauliki.
Mikusanyiko ya Polandi Yenye Kufanyiza Historia
Katika Oktoba 1987, kwenye mkutano wa kila mwaka wa Shirika la Pennsylvania la Sosaiti, ilitangazwa kwamba katika 1989 mikusanyiko ya kimataifa ingefanyiwa Polandi. Wakati huo si watu wengi walitambua jinsi vikusanyiko hivi vingethibitika kuwa vyenye maana kubwa. Katika Agosti 4-6 mikusanyiko ilifanyiwa wakati ule ule mmoja katika majiji yote mawili Chorzów na Poznan; halafu katika Agosti 11-13 mkusanyiko ukafanyiwa Warsaw.
Ilikadiriwa kwamba watu 140,000 kutoka nchi 22 wangevutwa kwenye karamu hizi za kiroho. Hata hivyo, jumla ya hudhurio ikawa 166,518, na hesabu ya nchi ilizidi ile iliyokadiriwa mwanzoni.
Kwa majuma mawili mfululizo, kuanzia Julai 28, uwanja wa ndege katika Warsaw ulikuwa na shughuli nyingi sana huku ndugu Wapolandi wakiwakaribisha wajumbe waliokuwa wakiwasili siku baada ya siku kutoka sehemu zote za Ulaya na pia Japani na Amerika Kaskazini. Wajumbe fulani walisafiri zapata kilometa 11,000, hasa kwa garimoshi, kwa siku sita mchana na usiku. Wageni walitoka Siberia, Kazakhstan, Caucasus, Majimbo ya Baltiki, na pia Jamhuri ya Ukrainia. Ijapokuwa ukawizi uliokuwako kwa sababu ilikuwa pindi ambayo watu wengi huenda likizoni pamoja na matatizo mengine, akina ndugu hawakuvunjwa moyo. Walikuwa na furaha kuja pamoja kwenye karamu hii ya kiroho.
Kwa habari ya wajumbe kutoka Ulaya ya Magharibi, Japani, na Amerika Kaskani, Orbis Congress Bureau, shirika rasmi la usafiri la Polandi, lilikubali kwamba hicho ndicho kikundi kimoja kilichopata kuwa kikubwa zaidi cha wageni wa kimataifa kuzuru Polandi na kuhudhuria mikusanyiko. Maofisa hawa walivutiwa sana na mwenendo mzuri wa akina ndugu na pia mpango wa kitengenezo wenye kufanikiwa.
Ushirikiano wa wenye mamlaka ulithaminiwa sana. Kwenye vituo vya ndege, basi, na garimoshi, wafanya kazi wa mkusanyiko Wapolandi walipata msaada wenye fadhili kutoka kwa maofisa na wafanya kazi wao.
Ingawa 12,000 hivi walilala kwenye mahoteli katika majiji mengi ya mkusanyiko, kulikuwa na wajumbe zaidi ya 60,000 ambao ndugu zetu waliweza kuwapa mahali pa kulala katika nyumba zao za faragha, Majumba ya Ufalme, mabweni ya shule, na mahema. Kundi moja lenye wahubiri 86 liliwapa mahali pa kulala wageni zaidi ya 500. Kundi jingine lenye wahubiri 146 kwenye kiunga cha magharibi mwa jiji la Warsaw waliwakaribisha nyumbani mwao wajumbe 1,276.
Ijumaa asubuhi kwenye kila mkusanyiko, barabara zote kuu zinazoelekea kwenye stediamu zilisongamana wajumbe waliokuwa wakienda kwenye mkusanyiko. Magari ya abiria yaliwasili yakiwa yamejaa Mashahidi wenye furaha na wenye kujaa mazungumzo ya kirafiki. Mabasi ya kukodishwa yaliyojaa ndugu zetu kutoka majiji na miji iliyo karibu yaliegeshwa mahali palipopangwa kimbele. Mashahidi wengine walikuja kwa magarimoshi ya pekee. Kadi za shavu la koti za mkusanyiko zilikuwa kila mahali.
Kwenye hiyo mikusanyiko mitatu, sehemu zilizoonyeshwa kipekee ziliwekwa kando kwa ajili ya wajumbe wa kutoka nchi za kigeni. Vikundi vikubwa vilitoka katika nchi mbalimbali, hasa Chekoslovakia. Wengi kutoka Urusi waliokuwa wakizuru marafiki na watu wa ukoo walikuwapo pia.
Sehemu za Pekee za Programu
Kwa kuwa mikusanyiko ilikuwa ya kimataifa, ripoti zilisikiwa kutoka nchi 25 tofauti-tofauti. Sehemu za programu zilitafsiriwa wakati ule ule mmoja katika lugha nyingi tofauti-tofauti kufikia 16, na kila kikundi cha lugha kingeweza kusikia programu kwa uwazi bila kutatizwa na sehemu nyingine za lugha kutoka kwenye stediamu hiyo. Mtu mmoja anayefanya kazi ya kurekodi ambaye aliulizwa jinsi ya kutekeleza mpango huu alisema hivi: “Ni jambo lisilowezekana kukuza sauti ya stediamu katika njia ya kwamba washiriki wanaweza kusikiliza programu katika lugha 16 wakati ule ule mmoja.” Hata hivyo, ndugu zetu walifanya jambo ilo hilo, na wote waliweza kuwasikiliza kwa umakini washiriki wa Halmashauri ya Nchi ya Polandi na washiriki wa Baraza Linaloongoza.
Kutolewa kwa trakti mbili katika lugha ya Kipolandi Jumamosi alasiri kulitokeza mshangao mkubwa. Ilikuwa ndiyo mara ya kwanza akina ndugu katika Polandi kupokea kitolewaji kwenye mkusanyiko. Kutolewa kwa Broshua Should You Believe in the Trinity? Jumapili asubuhi kulitokeza mshangao mkubwa hata zaidi. Kwa Polandi, kichapo hiki kitakuwa chombo chenye matokeo sana katika kufunua fundisho hili bandia na kusaidia watu wenye mioyo yenye ufuataji haki wajue ukweli kuhusu Mungu mmoja wa kweli anayeishi na Mwana wake, Kristo Yesu.
Ubatizo uliofanywa Jumamosi ulivutia sana. Katika kila jiji la mkusanyiko wakati wenye kutaka kubatizwa waliponyanyuka ili wajibu maswali mawili yaliyoulizwa na msemaji, makofi mengi ajabu yalitikisa stediamu. Hakuna wakati mwingine wowote uliotangulia ambapo watu wengi kadiri hiyo walikuwa wamebatizwa kwenye mikusanyiko katika Polandi. Machozi ya shangwe yalijaa katika macho ya wote!
Hali iliyokuwapo kwenye mikusanyiko hii mitatu ilivutia sana kwa sababu kadhaa zisizoweza kusahaulika. Kwanza, ilikuwa shangwe na pendeleo kuwa kwenye stediamu hizo kubwa kushiriki chakula kizuri cha kiroho kutoka kwenye meza ya Yehova kama kilivyopangwa na “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mt. 24:45-47) Na lilikuwa jambo lenye kuchochea moyo kama nini kuketi pamoja na ndugu wa kutoka Chekoslovakia, Hangari, Ujeremani Mashariki, Urusi, Yugoslavia, na sehemu nyingine, ambao wakati uliopita hawakuwa na fursa ya kukutana na vikundi vikubwa vya waamini wenzi!
Mgeni mmoja wa kutoka Urusi alisema hivi: “Kwa miaka mingi tumekuwa tukingojea siku hii, na sasa tupo hapa kwenye mkusanyiko huu wa kimataifa. Tunaliona kuwa jambo gumu kuelewa yote haya na kuyafahamu yote. Ni kama ndoto. Ni vigumu kueleza kwa maneno kila jambo ambalo tumeona na kusikia. Tulipoona ile stediamu kubwa, yenye kuonekana kama bakuli ikiwa imejaa watu na kusikia muziki, macho yetu yalijaa machozi. Na sala—huku sisi sote tukiwa tumeunganika kwa ukimya—ilifanya tuteteme kana kwamba tunahisi baridi kwenye migongo yetu. Ilikuwa yenye uzito sana na yenye umoja. Mkusanyiko huu katika Warsaw ni tukio bora sana na tukufu hivi kwamba ulimwengu mpya tu ndio utakaouzidi. Sikuzote sisi tutakumbuka siku hizi zenye kustaajabisha. Ni jambo ambalo mtu hawezi kusahau. Shukrani za pekee na utukufu na ziwe kwa Muumba wetu, Yehova Mungu!”
Toleo moja la nyusipepa Życie Warszawy ya Kipolandi ya Agosti 16, 1989, ilisema hivi kuhusu mkusanyiko uliofanyiwa kwenye stediamu ya Dziesieciolecia katika Warsaw: “Wale wanaomwabudu Yehova Mungu—kama wao wenyewe wanavyosema—wanathamini sana vikusanyiko vyao, ambavyo kwa kweli ni udhihirisho wa umoja ulio miongoni mwao. . . . Na jambo jingine—kwa habari ya utaratibu, kuamanika, na usafi, washiriki wa mkusanyiko ni vielelezo vya kuigwa.”
Kwa kweli hisia ya udugu, upendo, na shangwe ya kuwa pamoja ni gumu sana kueleza. Basi, inaeleweka kwa nini kwenye kila jiji la mkusanyiko akina ndugu walikawia-kawia baada ya hotuba ya kumalizia—wasitake kuondoka, wasitake kusahau pindi hiyo. Uhakika wao na imani ni kwamba katika wakati ujao usio mbali sana, dunia nzima itajawa na wale wanaompenda na kumtumikia kwa umoja Muumba Mtukufu wetu, Yehova.
Kwa wale waliokuwa na pendeleo la kuhudhuria mikusanyiko ya Polandi katika kiangazi cha 1989, maneno ya Zaburi 70:4 yanafaa kweli kweli: “Washangilie, wakufurahie, wote wakutafutao. Waupendao wokovu wako waseme daima, atukuzwe Mungu.”
Shule ya Mazoezi ya Kihuduma Yazaa Tunda
Wakati wa mwaka wa utumishi wa 1989, madarasa mawili zaidi ya shule hii yalifanyiwa United States. Majumba ya Kusanyiko katika St. Louis, Missouri, na Coraopolis, Pennsylvania, yalitumiwa kwa darasa la tatu na la nne. Darasa la tano lilifundishwa katika Vienna, Austria, wakati wa masika ya 1989.
Kati ya wale wanafunzi 25 wa darasa la tatu, 6 walipewa migawo katika nchi za kigeni. Wale wengine walipewa migawo ya kutumikia katika United States na Kanada, wengine wao wakiingia katika kazi ya mzunguko. Katika darasa la nne, 16 kati ya wanafunzi 24 walipewa migawo katika nchi za kigeni. Kwa sasa, wale wengine wanaendelea katika utumishi wa wakati wote katika United States na Kanada.
Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ikawa ya kimataifa zaidi kuanzia mwishoni mwa Aprili 1989. Wakufunzi wawili wenye ujuzi wanaotumikia wakiwa waangalizi wasafirio katika United States walipelekwa Vienna. Wale wanafunzi 23 waliofanyiza darasa la kwanza la Ulaya walitoka Austria, Ubelgiji, Ufaransa, Ujeremani, Uholanzi, Uswisi, na Yugoslavia. Pia, wanane waliotazamiwa kuwa wakufunzi kwa madarasa ya wakati ujao katika Ujeremani, Ufaransa, Italia, na Hispania walihudhuria mtaala huo. Darasa zuri lilipatikana na pia vifaa vya maktaba na ofisi ya shule. Mahali pa kulala paliandaliwa katika Makao ya Betheli.
Wakufunzi walifurahia sana maendeleo mazuri ya wanafunzi. Kwao lilikuwa ono la mara moja maishani, jambo ambalo hawatasahau wala kujutia kamwe. Wahitimu wanne wamepewa mgawo wa kwenda katika nchi zilizo nje ya Ulaya, hali kwa sasa wale wengine wanashughulikia migawo papo hapo katika kontinenti ya Ulaya.
Baada ya kumaliza kusoma kwao, barua moja kutoka darasa la Vienna ilisema hivi kwa sehemu: “Kabla hatujaja, wengi wetu tulikuwa tukitumikia katika kazi ya uchungaji. Lakini sasa twaelewa vizuri zaidi kiwango cha wachungaji wa watu wa Mungu ni kipi hasa. Tuna uhakika kwamba tumezoezwa vizuri na tumeandaliwa kumtumikia Yehova, ndugu zetu, na wanadamu wenzetu vizuri zaidi kuliko tulivyoweza kufanya bila elimu hii nzuri.”
Kufikia sasa, wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma wamepewa migawo ya kutumikia katika nchi 25 nje ya nchi ambako walizaliwa. Wakati wa mwaka wa utumishi wa 1990, inatumainiwa kwamba manufaa za shule hii zitaenezwa hata mbali zaidi.
Wakfu wa Matawi Umtukuzao Mungu
Jambo kuu katika maisha ya mtu ni wakati anapojiweka wakfu kwa Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. Vivyo hivyo, jambo kuu la maisha ya kitheokrasi ya ofisi ya tawi ya nchi ni kuwekwa wakfu kwa vifaa vyayo kwa Bwana Mwenye Enzi Kuu yule yule, ambaye ‘ndiye aliyefanya mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo.’ (Mdo. 4:24) Wakati wa mwaka huu wa utumishi uliopita, matawi matano yaliwekwa wakfu, kutia na moja katika Meksiko.
Peru
Novemba 6, 1988, ilipambazuka ikiwa na mawingu yenye baridi. Lakini upesi, kana kwamba limetiwa moyo na nyuso zenye furaha zilizokuwa zikienda kuelekea mahali pa pekee katika Monterrico Chico, Lima, anga likatokeza jua lenye kuangaza. Watu wa Yehova walikuwa wakitazamia tukio la pekee—umalizio wenye kuleta shangwe wa mradi “Upanuzi—Betheli ya Peru.” Wakiwa na mioyo iliyojaa uthamini, watu 694 walikusanyika katika Jumba la Ufalme jipya kwenye tawi, na wakiwa wameunganishwa kwa simu, wasikilizaji 48,150 kwenye mahali pa kusanyiko katika Campoy, katika viunga vya Lima, walisikiliza kwa umakini programu ya kuwekwa wakfu. Lilikuwa hudhurio lenye kushangaza, kwa kuwa Mashahidi 31,000 tu ndio wanaokaa katika nchi nzima! Theodore Jaracz wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya wakfu.
Mipango ilipofanywa katika 1980 ili sehemu ya kwanza ya tawi ijengwe, kadiri ya ongezeko la wahubiri haikutazamiwa hata kidogo. Kwa sababu hiyo, kufikia wakati ambao mradi huo ulimalizika katika Desemba 1984, ilikuwa wazi kwamba tawi lingehitaji kupanuliwa tena.
Mradi huo “Upanuzi—Betheli ya Peru” ulikuwa mpango wa kufanya maradufu jengo-tata lililokuwako kwa ubuni na namna ya ujenzi unaoweza kustahimili tetemeko ya dunia. Mfumo wa kujengea chini mabapa na kuyainua ulitokeza udadisi mwingi. Watazamaji walikuwa wengi sana zile siku ambazo mtambo wa kuinulia vitu vizito wa tani 60 ulipoinua mabapa mazito ya saruji yaliyotangulia kutayarishwa, na kuyaweka mahali payo, kila moja likiwa na uzito wa tani kadhaa. Yote pamoja mabapa 120 yalitumiwa. Mabapa hayo yalikamilishwa yakiwa na tyubu zilizotiwa ndani na kukazwa imara kwa ajili ya mfumo wa umeme, na pia fremu za madirisha na za milango zikiwa zimewekwa mahali pazo. Utayarishaji huu ulipokuwa ukiendelea, akina ndugu waliokuwa katika kiwanda cha useremala walifanya kazi pia kama nyuki wenye shughuli nyingi wakitengeneza namna ya mti mzuri mwekundu uitwao mahogane utokao kwenye msitu wa Peru wenye mvua nyingi uwe vifaa vyote vya mbao vilivyohitajiwa.
Wakitoa kwa upendo michango yao ya wakati na gharama za usafiri, WKKUK 55 (Wafanya Kazi wa Kujitolea wa Ujenzi wa Kimataifa) walikuja kutoka nchi nyingine ili wasaidie. Wakiwa na uwezekano mkubwa zaidi wa kupatwa na matatizo fulani ya afya, kama vile inavyokuwa mara nyingi kwa wageni wa kutoka nchi nyingine, walitoa shukrani zao kwa madaktari wawili, wote wawili wakiwa Mashahidi, ambao bila kuchoka walishughulikia mahitaji yao ya kitiba. Utumishi mwingine uliohitajiwa kabisa uliotolewa wakati wa kipindi chote cha ujenzi. Vinyozi wawili, ndugu zetu, waliobadilishana zamu kila juma kufanya kazi kwenye mahali pa ujenzi, walinyoa kila mtu kwa uchangamfu.
Washiriki 60 wa jamaa ya Betheli wanaweza kushuhudia kwamba mradi “Upanuzi—Betheli ya Peru” ulitokea kwa sababu ya uhitaji wa haraka nao umekamilishwa ili kumletea Yehova sifa.
El Salvadori
“Theokrasi yazidi, shangilia! Kuna mupanuko wa ajabu.” Jumamosi, Novemba 12, 1988, sauti 22,091 ziliungana pamoja kuimba maneno hayo yenye kuchochea kwa kuadhimisha—kuwekwa wakfu ofisi mpya ya tawi na Makao ya Betheli katika nchi ya Amerika ya Kati ya El Salvadori.
Jengo-tata la Ofisi na makao, likitazama kutoka mahali palo pafaapo kwenye kiunga chenye milima-milima, latazama chini kwenye mji mkuu, San Salvadori, na linaweza kuona volkano kadhaa ambazo hufanya nchi hiyo kuwa mashuhuri.
Ndugu John Barr, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alisema kwa uchangamfu juu ya kichwa: “Wimbo wa Ongezeko la Theokrasi.” Pia programu hiyo ilitia ndani dansi za kale zenye kupendeza zilizochezwa na ndugu na dada wenyeji mia moja.
Zaidi ya ndugu 300 wenye kuzuru, wakiwakilisha nchi tisa tofauti-tofauti za Amerika ya Kaskazini na ya Kati na pia Ulaya, waliweza kushiriki katika programu ya uwekaji wakfu. Hii ilitia ndani watu kadhaa miongoni mwa wale 326 wa Wafanya Kazi wa Kujitolea wa Ujenzi wa Kimataifa waliokuwa wameshiriki sehemu kubwa katika ujenzi huo.
Sauti za kwanza za wimbo wa ongezeko la theokrasi zilisikika katika 1945, wakati wamisionari wawili wa kwanza, Roscoe na Hilda Stone, walikabili kazi kubwa sana ya kuwapelekea ukweli wakazi milioni moja na nusu waliokuwa wakiishi huko wakati ule. Tangu wakati huo, wimbo huu umeimbwa kwa sauti inayozidi kuongezeka daima. Mwaka huu uliona kilele cha wahubiri 17,647, ikiwakilisha uwiano wa mhubiri 1 kwa wakazi 322. Wakati wa pindi ambayo tawi lilikuwa likijengwa—kuanzia wakati wa kununuliwa kwa viwanja vya kwanza kwanza katika Aprili 1983 kupitia miaka miwili na nusu ya ujenzi mpaka tawi lilipomalizika katika Julai 1988—nchi hiyo iliona ongezeko lenye kustaajabisha sana la asilimia 50, ijapokuwa mapainia wengi wa kawaida na wa pekee walikuwa hawako kwenye migawo yao shambani walipokuwa wakisaidia katika ujenzi. Uwezekano wa kuwa na ongezeko kubwa hata zaidi unaweza kuonwa kutokana na hesabu kubwa ya wapya wanaopendezwa waliokuja kwenye Ukumbusho wa 1989, ambao ulihudhuriwa na 58,503.
Ile hali ya ujenzi huo mpya inayoweza kustahimili matetemeko ya dunia ilitahiniwa pia mapema katika Oktoba 10, 1986, wakati jiji la San Salvadori lilipotikiswa na tetemeko kubwa la dunia. Ijapokuwa majengo yaliyo mengi yaliyo katika kitovu cha jiji hilo yaliharibiwa—mamia ya watu wakipoteza uhai wao na maelfu wakiachwa bila makao—hakuna ndugu hata mmoja aliyekuwa akifanya kazi kwenye tawi jipya aliyeumia, na majengo hayakuharibiwa. Vifaa hivi vya ki-siku-hizi vikiwa vimekamilishwa, roho ya Yehova inaendelea kuwa juu ya akina ndugu wa El Salvadori wanapojiunga pamoja na ndugu zao kuzunguka ulimwengu katika kuimba wimbo usiokoma wa ongezeko la theokrasi.
Maurishasi
Kama vile kito chenye thamani kinachozungukwa na bahari yenye rangi feruzi ya buluu, miamba ya marijani, na fuo nyeupe-nyeupe, taifa hili la kisiwa cha kitropiki katika Bahari Hindi ni makao ya wazao zaidi ya milioni moja wa wahamiaji wa kipindi cha miaka ya majuzi. Ukulima wa miwa uliwaleta Maurishasi walio wengi wao, ambako walipata mandhari yenye rangi ya emeraldi ya kijani-kibichi yenye vilele vya volkano hapa na pale vilivyo kama jino. Leo, walio wengi wa idadi ya watu ni Wahindi Wahindu, wanaoshiriki kisiwa hicho pamoja na Wakreole Wakatoliki, Wahindi Waislamu, Wazungu, na Wachina. Ingawa Kiingereza ndiyo lugha rasmi, wakazi walio wengi wanasema Kikreole, ambacho ni lahaja (lugha mchanganyiko wa maneno ya kienyeji na Kifaransa).
Katika 1933 tawi la Afrika Kusini lilipeleka mapainia wawili, Bert McLuckie na Robert Nisbet, kwenye kisiwa hiki. Walipanda mbegu za kwanza za Ufalme. Hata hivyo, haikuwa mpaka baada ya miaka 18, wakati George ndugu ya Robert Nisbet alipojiunga naye kwamba mbegu zilitia mizizi na kuanza kuchipuka.
Wakati ule ule, habari za Ufalme zilifika visiwa jirani vya Réunioni na Rodrigues. Leo, utendaji wa kuhubiri Ufalme katika visiwa vya Réunioni, Rodrigues, Mayotte pamoja na Komoro umepangwa kitengenezo pia chini ya mwongozo wa tawi la Maurishasi. Kwa kweli, kuna Mashahidi wa Yehova wengi katika Réunioni kuliko Maurishasi.
Baada ya miongo ya kutumia makao yaliyokodishwa, ofisi mpya ya tawi pamoja na Makao ya Betheli na Jumba la Ufalme ilijengwa katika mji wa Vacoas ulio sehemu za ndani zaidi za kisiwa. Katika Desemba 10, 1988, hili jengo-tata liliwekwa wakfu. Lo, jinsi walivyofurahi wale watu 701 waliosikiliza mhadhara wa uwekaji wakfu uliotolewa na Carey Barber, mshiriki wa Baraza Linaloongoza!
Mradi huo uliamsha kupendezwa kwa majirani wengi wenye urafiki. Mara nyingi wanataja kuhusu mwenendo mzuri wa ndugu vijana ambao waliishi na kufanya kazi hapo. Mmoja wa jirani hao, Amrita, anaishi pamoja na mama na nyanya yake katika kao dogo lenye kujengwa kwa mabati linalopakana na upande mmoja wa uwanja wa jengo hilo. Alipofikiwa kwenye huduma ya nyumba kwa nyumba mapema wakati wa mradi huo, alikubali funzo la Biblia. Kwa kuchochewa sana na yale aliyoyasikia, Amrita alijitolea kila siku kusaidia kuwapikia wafanya kazi hao wenye njaa. Kama tokeo la ushirika huo wenye kujenga, alifanya maendeleo mazuri ya kiroho na leo ni Shahidi aliyejiweka wakfu na kubatizwa akiwa katika kazi ya kuhubiri wakati wote.
Lo, ni shangwe iliyoje ambayo ukuzi wa watu wa Yehova katika sehemu hii ya ulimwengu umewaletea watumishi wa kale! Katika 1951 kundi la kwanza lilianzishwa, likiwa na wahubiri wanane wa Ufalme. Sasa kuna wahubiri 2,564 wanaoshirikiana na makundi 30 katika visiwa hivi vya Bahari Hindi. Hisia za wafanya kazi wanne wa wakati wote wa kutoka nchi za kigeni ambao wametumikia hapa kwa jumla ya miaka 132, zilielezwa vizuri na Dada Eunice Price wakati aliposema hivi: “Sisi tulipanda, tulieneza mbegu, na Yehova ametoa ukuzi. Lo, tumepata pendeleo lililoje kuona jambo hilo kwa macho yetu wenyewe!”
Japani
Baada ya kazi ya miaka mitano iliyofanywa na akina ndugu zaidi ya 500, programu ya kuweka wakfu tawi la Japani katika Ebina ilifanywa katika Mei 13, 1989, Carey Barber, John Barr, na Lloyd Barry wa kutoka Baraza Linaloongoza wakiwa wasemaji wakuu.a Umati wa watu 3,213 waliohudhuria pindi hii ya pekee yenye kufurahisha sana ulitia ndani wamisionari wote na waangalizi wasafirio katika Japani, wahubiri walioshiriki kazi ya ujenzi pamoja na jamaa zao, na wahubiri wengi waaminifu kwa muda mrefu. Waliotiwa ndani pia walikuwa wageni karibu 60 kutoka ng’ambo, wakiwakilisha matawi 13.
Siku iliyofuata uwekaji wakfu, Jumapili, Mei 14, mkutano wa pekee ulipangwa, mahali 46 pakiwa pameunganishwa kwa simu. Hivyo, 233,780 waliweza kusikiliza hotuba zilizotolewa na wajumbe waliotoka katika nchi mbalimbali na kutoka Baraza Linaloongoza. Hakika matukio yaliyotukia katika siku hizo mbili yamekuwa tukio kuu katika historia ya kitheokrasi ya Japani.
Kwa sasa, matawi yapatayo 38 yanahusika katika kuchora ramani au wanajenga majengo mapya au wanapanua vifaa walivyo navyo sasa. Na Programu ya Wafanya Kazi wa Kujitolea wa Ujenzi wa Kimataifa imepeleka wafanya kazi kwenye matawi 30 ili wasaidie wafanya kazi wa ujenzi wenyeji. Kwa kweli, katika njia mbalimbali, Yehova amewapa watu wake uwezo mwingi ili ‘wakatoe ushuhuda’ kwa utukufu wake na wa Mwana wake.—Mdo. 4:33.
Afrika
Penzi la Mungu ni kwamba “watu wote waokolewe.” Na mwaka wa utumishi wa 1989 umekuwa wenye maendeleo thabiti kuelekea kutimiza hilo katika kontinenti la Afrika.—1 Tim. 2:4.
Katika Senegali profesa mmoja wa shule ya sekondari amekuwa mwandikishi wa kawaida wa magazeti yetu kwa miaka mingi. Mara nyingi yeye hutumia makala kutoka Amkeni! ili afundishe wanafunzi wa darasa lake. Ili awasaidie wanafunzi wake wafuate masomo yao vizuri, yeye huwaazima nakala zake za kibinafsi. Hata hivyo, kwa kuwa amekuwa na matatizo fulani kuwafanya wanafunzi warudishe magazeti yale, yeye hununua mabuku yaliyojalidiwa mwishoni mwa mwaka na kuyatumia darasani!
Ijapokuwa Mashahidi wa Yehova ni wachache katika Jamhuri ya Gini, kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi inafanywa kwa bidii nyingi. Akina ndugu wamekuwa na shughuli nyingi wakijenga Jumba la Kusanyiko dogo, ambalo liko umbali fulani kutoka kwenye barabara na liko juu ya kilima. Akina ndugu walikuwa wakifikiri jinsi watakavyosafirisha mchanga mwingi kwenye mahali hapo. Walienda kwa kampuni moja yenye kujenga barabara ili wakodi lori la kubeba mchanga. Meneja wa kampuni hiyo alifanya mpango ili akina ndugu wapewe lori moja pamoja na mtambo wa kupakia. Ilikuwa lazima kufanya Safari sita ili mchanga uweze kupelekwa kwenye mahali pa ujenzi. Akina ndugu walipokwenda kulipia lori hiyo na ule mtambo wa kupakia, meneja aliwaambia kwamba kazi hiyo ilifanywa bila malipo. Yeye alisema: “Jambo moja tu ambalo mnaweza kutufanyia ni kusali kwa Yehova kwa ajili yetu ili sisi pia tuweze kukuza upendezi katika ibada yake.”
Mwangalizi wa mzunguko aliyepewa mgawo wa kwenda Côte d’Ivoire alikuwa anatafuta jumba kubwa kutosha kwa ajili ya utoaji wa pekee wa slaidi katika jiji la Bondoukou. Alimwendea mkurugenzi wa kitovu cha mambo ya kitamaduni jijini. Kwanza mkurugenzi huyo alipinga Mashahidi wasikitumie, kwa kuwa, wakati uliopita, vikundi vingine vya kidini vilikuwa vimesumbua sana. Hata hivyo, yeye alimdokezea mwangalizi wa mzunguko kwamba barua iandikwe ikieleza sababu ya ombi hilo. Siku hiyo hiyo, mwangalizi wa mzunguko alikutana na polisi mmoja, mwanamume ambaye yeye alikuwa amejifunza Biblia pamoja naye wakati uliopita katika Abidjan. Ilitukia kwamba polisi yule alikuwa rafiki wa kibinafsi wa yule mkurugenzi. Alimwendea mkurugenzi yule na kumweleza kwamba Mashahidi wangeweza kutumainiwa. Kisha mkurugenzi yule akakubali kwamba jumba litumiwe, akimpa yule polisi ufunguo. Kundi hilo dogo la wahubiri 21 lilifurahi sana kuwa na hudhurio la 124, kutia na mkurugenzi na yule polisi rafiki. Mkurugenzi yule alivutiwa sana na usafi wa jumba na programu ya kiroho yenye kujenga hivi kwamba akakubali jumba lile litumiwe wakati mwingine wowote wakati ujao. Kwa kuongezea tangu wakati huo amekubali funzo la Biblia.
Mary, msichana mwenye umri wa miaka 11 anayeishi katika Sierra Leone, ana ugonjwa wenye maumivu sana unaoitwa Sickle-cell anemia (ugonjwa wa kurithi wa ukosefu wa chembe nyekundu). Kwa sababu ya ugonjwa huo, ametumia miaka miwili iliyopita ya maisha yake akiingia na kutoka hospitalini kuhusiana na upasuaji ili kuondoa mfupa ulioambukizwa kutoka kwenye mguu wake. Mary amebaki akiwa amepiga moyo konde asivunje sheria ya Mungu iliyotaarifiwa wazi kwenye Matendo 15:29, yaani, ‘mjiepushe na damu,’ ijapokuwa imetokeza pambano lenye kuendelea na madaktari kuhusu kutiwa damu mishipani. Ijapokuwa mama yake anamuunga mkono katika uamuzi wake, Mary hujisemea mwenyewe wakati kukataa damu kunapohusika. Miaka miwili iliyopita, Mary alipokuwa na miaka tisa, alikaa hospitalini kwa miezi mitatu huku madaktari, wauguzi, na wagonjwa wengine wakimkaza akubali kupasuliwa na kutiwa damu. Wapasuaji walimwambia kwamba upasuaji huo haungefanywa bila kutiwa damu mishipani, wakimwonya kwamba asipopasuliwa, hangeweza kutembea tena kamwe. Na pengine angekufa. Hata hivyo Mary alikuwa akijibu hivi: “Ningependelea kufa badala ya kupata damu. Kutiwa damu mishipani si jambo ambalo Yehova anakubali. . . . Nikitiwa damu, nitajihisi nikiwa mchafu mbele za Yehova.”
Madaktari walimkaza mama ya Mary, wakidai kwamba alitaka Mary afe na kwamba ndiye angekuwa na daraka la kifo cha binti yake. Walidai kwamba ni yeye alitia maoni hayo akilini mwa Mary.
Mary na mama yake walisimama imara katika uamuzi wao wa kutii sheria ya Mungu. Hatimaye wapasuaji wawili wakakubali kufanya upasuaji huo kwa kushirikiana. Kwa njia hiyo ungefanywa kwa haraka na bila kutumia damu. Hata hivyo, hawakutoa tumaini kubwa la kupata mafanikio. Mary alipopata fahamu zake baada ya upasuaji huo, maneno yake ya kwanza yalikuwa: “O Yehova, mwokoe mtumishi wako!” Mary alipata nafuu kwa haraka zaidi kuliko wale wagonjwa wengine wawili waliokuwa wamefanyiwa upasuaji huo huo siku hiyo lakini wakatiwa damu.
Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, ugonjwa wa sickle-cell anemia hauponi, na kwa habari ya Mary, ataendelea kupata maumivu na kuhitaji upasuaji zaidi. Yeye hawezi kufika kwenye mikutano mingi, kwa kuwa ana tatizo la kutembea. Akina ndugu hawana magari, na usafiri wa umma haupatikani. Kwa jitihada nyingi aliweza kuhudhuria Ukumbusho mwaka uliopita lakini alianguka mara kadhaa akienda nyumbani.
Ijapokuwa Mary ni mdogo, aonekana kuwa dhaifu na anatembea kwa kutumia mkongojo, hakuna udhaifu wowote kuhusu imani yake. Kitu kimoja kinachoonyesha hivi ni jina alilompa mbwa ambaye mama yake alimpa awe mnyama rafiki alipokuwa karibu kupasuliwa mara ya kwanza. Alimwita Holdfast (Shika-imara). Mjomba wake alipomtembelea, alimwuliza hivi: “Je! ulimpa jina hilo kwa kuwa unapaswa kumshika imara ili asiume mtu yeyote?”
“La, Mjomba,” Mary akajibu, “Nilimwita hivyo kwa kuwa Biblia inatuambia yatupasa tushike imara ukamilifu wetu. Tukishika imara ukamilifu wetu, tutakuwa sawa.”
Katika Burkina Faso misionari mmoja aliongoza funzo la Biblia pamoja na mwanamke ambaye mume wake alipinga sana. Kwa kuwa kazi yake yamtaka asafiri mara nyingi, misionari alimtia moyo mkuu yule mwanamke aweke magazeti fulani katika sanduku la mavazi la mume wake asafiripo. Pole kwa pole yule mwanamume akaanza kusoma yale magazeti. Upesi upinzani wake ukakoma. Alialikwa kwenye Ukumbusho katika 1988, na kwa mshangao wa wengi, alikuja. Tangu wakati huo funzo la Biblia limeanzishwa, na mwanamume huyo amefanya mabadiliko mengi maishani mwake hivi kwamba jamaa na marafiki wake wanasema kwamba lazima Mashahidi wa Yehova wawe na dini ya kweli kwa sababu waliweza kumfanya mwanamume huyo awe mtu bora.
Katika nchi nyingine ya Afrika, ndugu zetu walikuwa wanahudhuria mkutano na kwa ghafula polisi wakaingia ndani. Painia wa pekee alikamatwa, akaburutwa kwenye gereza, akapekuliwa-pekuliwa, na kuhojiwa. Polisi walichukua karatasi ambayo painia alikuwa akiandika maandiko ya Biblia wakati wa mkutano. Polisi waliona majina Yohana, Petro, na Yeremia, yakiwa yameandikwa yakifuatwa na tarakimu nao wakakata maneno kwamba ni orodha ya watu waliokuwa na deni la pesa nyingi sana za yule painia. Polisi walimwuliza painia: “Watu hawa watakulipaje ukiwa gerezani?” Hata katika hali ngumu kama hiyo painia huyo alilazimika kutabasamu.
Esia
Ndugu zetu katika Esia wanatoa maandikisho ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa idili. Kwa kutafuta kwa bidii upendezi katika ujumbe wa Biblia, wanawasaidia watu ‘wasikilize’ Neno la Mungu ili nafsi zao ‘ziishi.’—Isa. 55:3.
Katika India painia wa kawaida mmoja, akifuata madokezo yaliyotolewa katika Huduma ya Ufalme Yetu, alitayarisha kwa umakini orodha ya watu aliofahamiana nao, watu wa ukoo, na wanafunzi wa Biblia akiwa na maoni ya kuwatolea maandikisho ya magazeti yetu wakati wa kampeni ya uandikishaji. Jitihada zake za moyo mweupe zilikuwa na matokeo mazuri sana. Alipata maandikisho 30 wakati wa mwezi huo.
Ndugu mwingine aliyekuwa akifanya kazi katika shirika moja kubwa la usafiri wa basi alipeleka madokezo yake kumi kuhusu uendeshaji gari ulio salama kwenye mashindano yaliyokuwa wazi kwa wafanya kazi walo 36,000. Alitegemeza habari yake kwenye Amkeni! ya Januari 8, 1988 (Kiingereza). Madokezo yake kumi yalikuwa ndiyo bora zaidi. Alipewa hati, na magazeti ya kila siku yanayoongoza katika jimbo hilo yalitangaza pia habari hiyo. Hata hivyo ndugu huyo anakubali hivi kwa unyenyekevu: “Najua kwamba mimi sistahili kupokea sifa kwa jambo hili. Ni ya Yehova na tengenezo lake, ambalo liliandaa habari hii yenye thamani.”
Mwangalizi wa mzunguko mmoja katika Japani alitia moyo mkuu kila kundi ambalo alizuru wakati wa kampeni ya uandikishaji wajitahidi kwa njia ya pekee ili wapate maandikisho. Anaripoti kwamba kama tokeo, kundi la kwanza liliweza kupata maandikisho 181 wakati wa juma, la pili 153, na la tatu 145. Ijapokuwa siku moja tu ndiyo iliyobaki kwa kampeni kwa kundi alilotembelea kuanzia Mei 30, alitia akina ndugu moyo mkuu wajaribu sana siku iliyofuata. Katika siku moja, walipata maandikisho 84, 56 yayo yakipatikana nyumba kwa nyumba.
Dada mmoja huko aliweka mradi wa kupata maandikisho 30 kila mwezi wa kampeni ya uandikishaji, Aprili na Mei. Anasema kwamba alifuata madokeza yaliyotolewa katika nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya 1983 na Yehova alibariki jitihada zake. Mtu fulani alipokuja kwenye nyumba yake, kama vile wakusanya pesa, wauzaji, na watu wa kuleta vitu, aliwapendekezea magazeti hayo. Alitoa maandikisho pia kwa watu aliofahamiana nao kwa kuwatembelea au kuwapigia simu, na, alipokuwa akinunua vitu, alitolea maandikisho wale watu wanaosaidia kwenye maduka ambao walionekana kuwa hawana kazi ya kufanya wakati huo. Alipata maandikisho 40 katika Aprili na 32 katika Mei. Maandikisho arobaini na sita kati ya hayo yalipatikana kwa njia ya kutoa ushahidi vivi hivi.
Ndugu mmoja katika Pusan, Jamhuri ya Korea, alionelea kwamba majengo ya biashara hayakufanyiwa kazi mara nyingi katika huduma. Akiwa mwanasheria, yeye angeweza kuingia ofisi hizo kwa urahisi na kuongea na wasimamizi au mameneja wa makampuni hayo. Alitumia njia gani? Kutoa ushahidi mfupi ulio rahisi. Ni wakati tu itikio lenye kutia moyo mkuu lilipopatikana ndipo alikuwa akiendelea. Kwa njia hii aliweza kupata maandikisho 26 wakati wa mwezi wa kampeni ya uandikishaji. Alipiga moyo konde kufikia mradi wake na hangezuiwa, ijapokuwa alilazimika kupanda ngazi nyingi isivyo kawaida katika eneo la namna hii. Jambo hili lilikuwa gumu kwake, kwa kuwa yeye ni jeruhi wa ugonjwa wa kupooza ambao ulipoozesha upande mmoja wa mwili wake.
Taiwani ni mojapo majimbo ambayo yamesongamana sana watu ulimwenguni, ikiwa na idadi ya watu zaidi ya 20,000,000. Asilimia 95 ya wakazi ni Wachina, wengi wao wakiwa waamini wa dini ya Budha na ya Tao. Je! watu hawa wangeweza kuitikia ujumbe wa Ufalme? Ndiyo. Sasa Wabudha na Watao hali kadhalika, pamoja na wengi wanaoitwa eti Wakristo wanaitikia habari njema nao wanajifunza juu ya Muumba wao. Ni nini hasa kinachowavutia watu wenye utamaduni wa fikira za Kichina wajifunze Biblia?
Mmoja aliyekuwa Mbudha hapo awali, sasa ni ndugu yetu, anatuambia kitu kilichomvutia: “Mimi nililelewa katika makao ya Wabudha wenye kutenda, karibu na hekalu la Kibudha. Hii ilimaanisha kwamba maisha yangu ya mapema yaliongozwa sana na dini ya Budha. Wakati wa miaka yangu ya kwenda shule, jamaa yetu ilihamia kwenye jiji kubwa zaidi, na huko nikajulishwa Biblia na Kanisa Presbeteri. Kwa kweli, sikuelewa Biblia kamwe lakini nikawa mshiriki wa kanisa, kwa kuwa mambo waliyofuatia yalipatana na mradi wangu maishani wakati huo. Nilitamani kuwa tajiri na mwenye kujitegemea. Kanisa lilikazia sana mambo ya fedha na utegemezo wa vitu vya kimwili kutoka kwa wanaparishi walo, au maoni ya kufuatia vitu vya kimwili. Kwa hiyo nikalikubali kanisa.
“Baada ya wakati fulani nikawa salama kwa habari ya vitu vya kimwili na nikawa nimeoa na kuwa na jamaa, lakini bado katika moyo wangu sikuhisi nimeridhika. Siku moja mmoja wa Mashahidi wa Yehova alimtembelea mke wangu na kumwuliza kama alijua jina la Mungu. Hakujua na kwa hiyo akaonyeshwa jina la Mungu ni Yehova. (Zab. 83:18) Niliporudi nyumbani kutoka kazini, mke wangu aliniuliza swali hilo hilo, nami nilihisi nikiwa nimezinduka kweli kweli kufikiri kwamba kufikia wakati huo nilikuwa nimekuwa mshiriki wa Kanisa Presbeteri na hata sikujua kwamba jina la Mungu ni Yehova! Funzo la Biblia likaanzishwa pamoja nasi na yule dada painia.
“Baada ya miezi mitatu hivi ya kujifunza, nikaweza kuona jambo lililotakwa na kwa hiyo nikaanza kufanya marekebisho katika maisha na mtazamo wa jamaa yetu. Nilikuja kutambua kwamba Yehova ni halisi na kwamba kwa kweli Biblia ni Neno lake lililoandikwa lenye kuvuviwa. Kwa muda wa miaka sita iliyopita, jamaa yetu imesonga mbele kiroho. Sasa nina pendeleo la kutumikia nikiwa mzee katika kundi la mahali petu. Mke wangu nami tunaweka wakati kando kila mwaka ili kushiriki huduma ya painia msaidizi. Wavulana wetu wawili ni wahubiri, na mradi wetu ni kwamba jamaa yetu iwe mapainia wa kawaida. Tunamshukuru Yehova kwamba kupitia mafundisho ya tengenezo lake, sasa tuna jamaa iliyoungana ikiwa na mradi wa kweli, jambo ambalo halikuwezekana kupitia dini ya Budha au zile zinazoitwa eti dini za Kikristo.”
Wamisionari wapya wanapowasili Taiwani, ile miezi mitatu ya kwanza, wanakazia fikira kujifunza lugha ya Kichina. Hii inatia ndani saa kadhaa za siku za kujifunza darasani. Kisha wanatumia saa nne katika kazi ya nyumba kwa nyumba, wakitumia yale ambayo wamejifunza, hiyo ikifuatwa na saa nyingi za kufanya mgawo wa masomo ya nyumbani. Wao wanaelewa kiasi gani wanapoanza huduma ya nyumba kwa nyumba? Si mengi sana mwanzoni. Misionari mmoja mpya aliweza kumweleza mwenye nyumba kifupi kwa nini alikuwa anazuru lakini alishindwa jinsi ya kumalizia na kutoa uandikishaji wa Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kwa fadhili mwenye nyumba alipigia ofisi ya tawi simu ili aulize umalizio wa utoaji ulikuwa nini kisha akaandikisha Mnara wa Mlinzi na Amkeni!
Ulaya
“Vijana waume, na wanawali, wazee na watoto; na walisifu jina la BWANA [Yehova, NW],” yataarifu Zaburi 148:12, 13. Ndugu zetu katika Ulaya wanafanya vivyo hivyo.
Frankie mwenye umri wa miaka tisa anaisha katika Luxembourg. Alipolazwa hospitali kwa muda fulani, alichukua kaseti pleya yake na kaseti za Kumsikiliza Mwalimu Mkuu. Kasisi wa Roma Katoliki huzuru vyumba vya hospitali kila jioni ili aseme kwaheri ya usiku. Alipoingia chumba cha Frankie, aliona kaseti hizo lakini hakusema lolote. Kesho yake wakati wa mchana, alikuja tena, lakini Frankie alikuwa analala. Alichukua kaseti moja, akaiingiza katika kaseti pleya, akaketi kwenye kitanda cha Frankie, na kusikiliza pande zote mbili. Frankie alipoamka, kasisi yule alianza kumwuliza maswali fulani. Alimwambia Frankie kwamba lilikuwa jambo zuri kwamba yeye anaamini Mungu.
“Kisha,” Frankie asema, “akaniuliza kama angeweza kupata kitabu kilichoambatana na zile kaseti. Kwa hiyo nikamwangushia kitabu Mwalimu Mkuu na pia kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani.”
Katika jimbo la Paris la Ufaransa, matineja wawili kutoka Laosi walijifunza ukweli wa Biblia kutoka kwa Mashahidi wa Yehova lakini wakawa majeruhi wa jeuri ya baba yao kwa sababu hawakuweza tena kushiriki ibada ya mababu waliokufa. Baada ya kupata kujua kwamba walikuwa wakiendelea kujifunza Biblia kisiri, akiwa na hasira kali yule baba alijaribu kukata koo la mwana mmoja. Yeye hakusita-sita kuandika kwa herufi kubwa kwenye gari lake na kwenye kuta za jengo lake hivi: “Kifo kwa Mashahidi wa Yehova”!
Wale wavulana wawili walifanya uamuzi wao wa kuanza utumishi wa shambani katika hali hizi zenye kutazamisha. Ijapokuwa baba yao alieneza habari hizi mbaya, walishangazwa na ukaribishaji mzuri waliopewa na watu katika eneo hilo. Leo wote wawili wamebatizwa, na mmoja amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka kadhaa. Kwa habari ya baba yao, sasa yeye amekubali uhakika wa kwamba watoto wake ni Mashahidi.
Viziwi wanajifunza pia kusifu jina la Yehova. Mtu mmoja kiziwi katika Italia aliishi maisha yaliyowekwa wakfu kwa michezo, hasa kupiga risasi kwa kulenga shabaha. Alihudhuria mashirika ya viziwi ambako utendaji wa michezo ulipangwa. Tamaa yake ilikuwa kushiriki katika Olimpiki ya viziwi.
Wakati wake wa ziada, alikuwa akisoma zile Gospeli, naye alipata wazo la kwamba mwisho wa ulimwengu ulikuwa unakuja. Siku moja Mashahidi wa Yehova walizuru kwenye nyumba yake na kusema na mke wake, ambaye, wakati huo hakuonyesha kupendezwa. Hata hivyo, alimnunulia mume wake kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani kisha akaalika Mashahidi warudi. Mume angeitikiaje kitabu hicho?
“Nilisoma kitabu hicho chote kwa usiku mmoja, nami nilikionea shangwe sana,” anasema. “Sasa mimi nilielewa kwamba dini niliyokuwamo haikuwa ile ambayo Kristo alifunza.” Hivyo akakubali toleo lao la funzo la Biblia. “Baada ya mwezi mmoja,” anaendelea kusema, “niliacha utendaji wangu wa michezo, nikarudisha silaha zangu za kulenga shabaha kwa bunduki, nami nikaacha kuwa na tumaini langu la kushiriki katika Olimpiki ya viziwi. Nilianza kuhudhuria mikutano yote. Lakini nilikuwa na tatizo. Kwa sababu ya kuwa kiziwi, sikuweza kuelewa chochote! Kwa upendo ndugu kadhaa waliandika habari zilizozungumzwa, na jambo hilo lilinivutia sana. Lakini baada ya mwezi mmoja, nilihisi nikiwa nimevunjika moyo—ilikuwa kana kwamba ninalazimika kuwategemea kabisa, nami nikawaza: ‘Kuna faida gani?’ Lakini hotuba moja ya Biblia iliyotolewa katika pindi hiyo ilinifanya nifikiri.
“Msemaji alisema kwamba maarifa sahihi yanahitajiwa ili kubadili utu wa mtu. Lakini ningepata wapi maarifa hayo ikiwa ningeacha kuja kwenye mikutano? Suluhisho la tatizo langu lilikuwa kwamba mtu fulani katika kundi ajifunze kuongea kwa kutumia ishara. Niliamua kumtahini Yehova kulingana na mwaliko wake mwenyewe kwenye Malaki 3:10. Yehova alinipa ombi langu. Tengenezo lake lilialika washiriki fulani katika kundi langu wahudhurie shule ya kujifunza kuongea kwa kutumia ishara. Maonyesho hayo ya upendo wa Yehova na akina ndugu yalinifanya nikate maneno, nami nikajiweka wakfu kwake na nikabatizwa. Nimetumikia nikiwa painia msaidizi mara mbili. Nashukuru kwa vile niliweza kufanya hivyo kwa msaada wa akina ndugu na dada waliotafsiria wenye nyumba ishara zangu kwa maneno. Pia nina shangwe ya kuongoza funzo na mwana wangu, ambaye si kiziwi na ninaweza kuwasiliana naye vizuri sana.”
Baraka zilizoko Italia zinaonekana wazi zaidi wakati mtu anapofikiria kwamba mapadri Wakatoliki wamewaonyesha Mashahidi uhasama mwingi kwa kujaribu kuzuia utendaji wao. Kwa kielelezo, kasisi wa mtaa wa mji mmoja wa jimbo la kati la Abruzzi alipanga asubuhi 12 za sala mfululizo. Kwa nini? Ili kazi ya Mashahidi wa Yehova isiwe na uvutano juu ya Wakatoliki. Lakini sala zake hazikufanikiwa, sawa na ilivyokuwa kwa laana za Balaamu wakati wa Mfalme Balaki Mungu alipobadili laana ziwe baraka. (Hesabu sura ya 23) Vilele mfululizo vya wahubiri katika Italia, vikifikia 172,382 katika Agosti, ni uthibitisho wa jambo hilo.
Katika Hispania, Charo alikuwa amemaliza kutoa ushahidi Jumamosi moja. Yeye na mume wake walipokuwa njiani kwenda kununua vitu fulani, alisukumwa na moyo amwendee mtu mmoja zaidi, tineja aitwaye Susana. Susana alipoona trakti Mashahidi wa Yehova Wanaamini Nini? alionyesha kupendezwa mara hiyo, kwa kuwa alikuwa amepata trakti hiyo hiyo mwezi mmoja uliopita, na tangu wakati huo yeye alikuwa akijaribu kuwatafuta Mashahidi. Alimpa Charo anwani yake, na mipango ikafanywa ya kuanzisha funzo la Biblia. Charo alishangaa kama nini wakati alipopata kwamba anwani hiyo ilikuwa ya kao la watawa! Susana alilelewa na watawa wa kike baada ya wazazi wake kupata talaka. Funzo la kwanza liliongozwa katika ua wa kao hilo la watawa, lakini ilikuwa lazima kuficha Biblia na kitabu kila wakati watawa fulani wa kike wenye shuku walipokuwa wakipita. Siku iliyofuata Susana alihudhuria kusanyiko la mzunguko, kisha baadaye akahudhuria mikutano kwa ukawaida. Baada ya kujifunza sura tatu tu za kitabu Kuishi Milele, Susana alifukuzwa kutoka kao hilo la watawa, na sasa anafanya maendeleo katika ukweli bila kizuizi.
Pia katika Hispania, vitabu zaidi ya 1,500 na magazeti 1,500 vimeangushwa kwa muda wa mwaka mmoja katika taksi ya Ndugu Félix! Yeye anafanyaje hivyo? Yeye hujaribu kujiendesha kwa ungwana kuhusiana na abiria wake wote na ni mfuataji haki kwa kulipiza bei ile inayolingana na urefu wa safari. Hivyo, wateja wake wana maelekeo ya kusikiliza anapowatolea ushahidi kuhusu Neno la Mungu.
Kutoka Uholanzi, msichana mwenye umri wa miaka 13 anaandika hivi: “Ilidokezwa kwamba tushiriki utumishi wa shambani wakati wa saa moja kabla ya funzo la kitabu. Kwenye mlango wa kwanza, nilikutana na kijana msichana wa miaka 13. Alisikiliza kwa umakini na kuchukua fasihi. Kesho yake nikiwa shuleni nilimwona msichana huyo huyo katika darasa langu. Tangu mwanzo tukawa marafiki. Katika muda wa majuma mawili nilimtolea kitabu Kuishi Milele nami nikajitolea kujifunza pamoja naye. Yeye akasema ndiyo, na funzo linaendelea vizuri sana.”
Amerika ya Kilatini
Kwa habari ya siku za mapema za Ukristo, mwanafunzi Luka aliandika hivi: “Walioamini wakazidi kuongezeka kwa Bwana, wengi, wanaume na wanawake.” Leo, Amerika ya Kilatini imeona mmiminiko wenye kuendelea wa watu wenye mioyo yenye ufuataji haki wakiingia katika tengenezo la ki-siku-hizi la Mungu.—Mdo. 5:14.
Ile hotuba ya slaidi “Halaiki za Watu Zafundishwa na Yehova,” iliyotolewa na waangalizi wa mzunguko katika Guatemala, imesaidia wengi wathamini tengenezo la Yehova. Hii inatia ndani wale wanaoishi katika sehemu yenye milima-milima ya nchi hiyo ambako matokeo ya utendaji wa maharamia umehisiwa kwa nguvu sana na ambako kutokuwamo kwa ndugu zetu Wakristo kumetahiniwa mara nyingi. Katika eneo moja ambako vikundi vidogo vya akina ndugu vinaishi—wote wakiwa wahubiri 65—1,426 walihudhuria hotuba hiyo ya slaidi.
Mwangalizi wa mzunguko mmoja anasimulia hivi: “Tulipokuwa tukifanya kazi karibu na kituo kimoja cha kijeshi, tuliomba turuhusiwe tuwaonyeshe askari slaidi. Tulipewa ruhusa na ofisa mkuu. Jioni hiyo tuliwasili tukiwa ndani ya lori-pikapu pamoja na vifaa. Baada ya kuweka projekta na kaseti pleya katika Jumba la Kulia, ofisa mkuu aliwaamuru askari wote waingie ndani. Wapatao 90 kati yao waliharakisha kuingia wakiwa wamebeba bundi zao, nao wakasimama kimya wakiwa wanakaza fikira wakitazama na kusikiliza hotuba hiyo kuanzia mwanzo mpaka mwisho. Baada ya kutoa shukrani kwa ukazaji fikira wao na kutoa maelezo fulani ya kumalizia, tuligeuza sehemu ya nyuma ya pikapu iwe idara ya magazeti na fasihi ambapo dada mmoja aliwagawanyia magazeti, vijitabu, na vitabu askari wengi ambao walikuwa na hamu nyingi ya kujifunza mengi zaidi.”
Februari 21, 1989, jamaa 35 za Mashahidi wa Yehova zilirudi kutoka kambi ya wakimbizi katika Meksiko ambako walikuwa wameishi kwa zaidi ya miaka sita. Walikuwa wamelazimishwa kukimbia kutoka Guatemala katika 1983 kwa sababu ya machinjo mengi yaliyotukia wakati huo. Hesabu fulani ya watu waliokuwa wakijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, na wengine wenye kupendezwa ambao walikuwa wamehudhuria mikutano katika kambi, walirudi pamoja na akina ndugu. Jumla ya mabasi sita kutoka Umoja wa Mataifa yaliwarudisha wakimbizi Guatemala. Halmashauri ya ukaribishaji ya Mashahidi ilikaribisha jamaa zilipowasili katika Huehuetenango katika Guatemala. CEAR, tengenezo ambalo limeanzishwa na serikali ili kuwezesha kurudishwa kwa wakimbizi, lilikuwa limetayarisha kuku wenye kukaangwa, mchele, na tortilla (namna fulani ya chapati). Kwa kuwa hawakuwa na chochote cha kula wakati wa safari ya basi ya mwendo wa saa tisa kutoka Meksiko, akina ndugu walikuwa na hamu nyingi na walithamini sana mlo huo.
Akina ndugu walirudi wakiwa na afya nzuri ya kiroho. Halmashauri ya Tawi iliona uhitaji wa kufanyiza halmashauri ya dharura, ambayo ilipanga kujenga nyumba kwa jamaa 17 na kusaidia jamaa nyingine 9 wamalize makao yao. Pia ndugu zetu wamepelekewa chakula. Baraza Linaloongoza limeandaa kwa upendo fedha zilizohitajiwa.
Idadi kubwa ya watu wa Venezuela wanaishi upande wa kaskazini wa nchi karibu na Karibea. Katika majimbo ya kusini, sehemu kubwa za misitu yenye kupata mvua nyingi inakaliwa na hesabu fulani ya makabila ya Wahindi. Tangu 1987, wenzi wawili waliooana ambao ni mapainia wa pekee wamekuwa wakiishi katika mji wa Santa Elena de Uairén, karibu na mpaka wa Brazili. Walikuwa na maono mapya yenye kupendeza katika eneo hili la Wahindi. Tayari yale makabila tofauti tofauti wanajua kuhusu kitabu Revelation Climax, na Maricures (machifu) wanaviomba kwa ajili ya jamii zao. Masanduku matatu ya vitabu hivyo yalisafirishwa, lakini ugavi huo haukutosha hata kidogo. Siku mbili baada ya katoni moja ya kitabu Revelation Climax kuwasili, inakuwa tupu. Mwalimu mmoja Mhindi wa shule ya jamii ya Sampai, ambayo ni safari ya mwendo wa saa mbili kwa gari kutoka Santa Elena, amekuwa akiwauliza hao wenzi wawili waliooana mapainia wa pekee katoni moja ya kitabu Ujana akigawanye miongoni mwa watoto wa shule. Anataka kutumia kitabu hiki katika darasa lake badala ya maagizo ya kidini ya kawaida.
Alipokuwa akifanya kazi mlango kwa mlango katika Ajentina, Susana, painia wa pekee, alikutana na mwanamke mmoja ambaye alikuwa amehamia kwenye eneo hilo hivi karibuni. Mume wa mwanamke huyo ni meneja wa benki na, kabla hajahamishwa, alikuwa amepokea zawadi ya uandikishaji wa Amkeni! kutoka kwa mfanya kazi mwenzi. Mwanamke huyo alitaarifu kwamba mojapo gazeti hilo lilikuwa limeokoa uhai. Jinsi gani?
Mwanamke huyo anaeleza kwamba bila kujua kwamba alikuwa na mimba, alikuwa amepigwa picha za Eksirei mfululizo. Kwa kuwa Eksirei zinaweza kusababisha ulemavu, madaktari tofauti-tofauti 20 walimshauri atoe mimba. Walimwambia kwamba mtoto wake alikuwa na uwezekano wa asilimia 95 wa kuwa kilema. Madaktari na jamaa yake walimkaza sana atoe kijusi hicho. Lakini kabla hajafanya uamuzi wa mwisho, yeye alitaka kupata ushauri wa kasisi wa jamaa. Alizungumza na makasisi wawili, wote wawili walimwambia kwamba Mungu hangemwadhibu kwa sababu ya kutoa mimba ya mtoto huyo. Akiwa ameudhika sana kwa sababu ya jibu hilo, alimwomba Mungu mwongozo. Wakati huo huo akapokea kupitia kwa posta Amkeni! yenye jalada lenye kichwa: “Kuzaa? Au Utoaji-Mimba?” Mwanamke huyo alipaaza sauti hivi: “Hili ni jibu la Mungu kwa sala yangu!” Hakutoa mimba. Tokeo lilikuwa nini? “Shukrani kwa Amkeni! leo mimi nina kisichana kizuri, na chenye afya nzuri,” akasema. “Amkeni! iliokoa uhai wa kisichana changu!”
Amerika Kaskazini na Visiwa vya Karibea
Mtunga zaburi aliandika hivi: “Umeuvika mwaka taji ya wema wako.” (Zab. 65:11) Kweli kweli, tumekuwa na mwaka wa utendaji wenye kufurahisha na uliobarikiwa, kama maono yafuatayo yanavyoonyesha.
Kuna ono moja kutoka Kanada linaloonyesha umuhimu wa wazazi kuwaelimisha watoto wao kanuni za Biblia, si sheria tu, na pia matumizi yenye ufahamivu ya kanuni hizo. Wakati Terra alipokuwa mwenye umri wa miaka 11 na akiwa hajabatizwa, alitahiniwa na mwalimu wake bila kutazamia. Wakati huo, Terra alikuwa ndiye mwanafunzi Shahidi pekee katika shule nzima.
Asubuhi moja wakati wa masomo, Terra aliona kwamba mwalimu pamoja na mwanafunzi mwenzake walitoka darasani wakaenda nje kwa dakika chache. Muda mfupi baada ya hapo mwalimu alimwomba Terra kwa upole aandamane naye kwenye ofisi ya mkuu wa shule. Hakupewa sababu yoyote wakati huo. Hata hivyo, alipowasili kwenye ofisi ya mkuu wa shule, Terra aliona kwamba bendera ya Kanada ilikuwa imewekwa juu ya dawati ya mkuu wa shule. Ni wao watatu tu waliokuwa katika ofisi: Terra, mwalimu wake, na mkuu wa shule yake.
Ndipo mwalimu akamwagiza Terra ateme mate kwenye bendera ya Kanada. Yeye alidokeza kwamba kwa kuwa Terra haimbi wimbo wa taifa wala kusalimu bendera, hakukuwa na sababu kwa nini asiteme mate kwenye bendera alipoagizwa kufanya hivyo. Akiwa ameshangazwa sana na agizo hilo, Terra alikataa kutendea kwa dharau kifananishi hicho cha nchi. Alieleza kwamba Mashahidi wa Yehova wanastahi bendera, ijapokuwa hawaiabudu. Mwalimu alipoona kwamba Terra alikuwa thabiti kwa msimamo wake, wao wawili wakarudi darasani.
Mle darasani mwalimu alitangaza kwamba alikuwa sasa hivi amefanya jaribio. Alikuwa amechukua wanafunzi wawili kila mwanafunzi kwa zamu yake kwenye ofisi ya mkuu wa shule, akiwaagiza wateme mate kwenye bendera. Ijapokuwa mwanafunzi wa kwanza alishiriki sherehe za kizalendo, alitema mate kwenye bendera alipoagizwa afanye hivyo. Tofauti na hilo, kama mwalimu alivyoeleza, Terra alikuwa na kanuni za juu sana. Ijapokuwa haimbi wimbo wa taifa wala hasalimu bendera, alikataa kuidharau bendera katika njia hii. Mwalimu alisema kwamba Terra ndiye aliyeonyesha staha inayofaa. Lo, ni heshima iliyoje ambayo mwenendo wenye kustahi wa Terra ulimletea Yehova na tengenezo lake!
Katika Jamhuri ya Dominika mke wa mwangalizi mmoja asafiriye alipata andikisho la gazeti kwa mwanamke kijana ambaye alikubali pia toleo la funzo la Biblia. Funzo lilianzishwa wakati wa juma la ziara, na dada mmoja mwenye kutegemeka katika kundi la mahali hapo aliachiwa utunzaji wa funzo hilo. Kwenye kusanyiko la mzunguko lililofuata, mhubiri alimleta yule mwanafunzi wa Biblia ili asalimu mke wa mwangalizi wa mzunguko. Kufikia wakati huo, tayari mwanafunzi huyo alikuwa mhubiri wa habari njema. Walipokutana tena miezi sita baadaye, tayari mwanamke huyo kijana alikuwa amejiweka wakfu na alikuwa amebatizwa kwa miezi kadhaa. Alimwalika mwangalizi wa mzunguko na mke wake kwenye kao lake kwa mlo na ili wapate kumjua mume wake, daktari mpasuaji, ambaye alikuwa ameanza kujifunza. Muda mfupi baada ya hapo, walipokutana tena kwenye mkusanyiko wa wilaya, mwangalizi wa mzunguko na mke wake walifurahi kupata kujua kwamba mume yule alikuwa amebatizwa pia. Haya yote yalitukia katika muda wa mwaka mmoja na nusu tu kwa sababu ya bidii ya mke wa mwangalizi wa mzunguko, kufuatia kulikofanywa na mhubiri wa kundi aliyechukua kwa uzito uhitaji wa kuendelea kutunza kwa ukawaida upendezi wa kiroho wa huyo mtu wa aina ya kondoo, na baraka ya Yehova.
Katika United States huu umekuwa ni mwaka wenye kutokeza wa kutimiza mambo ya kitheokrasi miongoni mwa watu wenye tatizo la kusikia na idadi ya watu wasiojua Kiingereza ambamo habari njema zinapigiwa mbiu katika lugha 20, kutia na lugha ya kutumia ishara. Shamba la wenye kusema Kihispania limepata mpanuko mkubwa. Wakati wa mwaka huu wa utumishi uliopita, makundi mapya 90 ya wenye kusema Kihispania yalianzishwa. Wahubiri zaidi ya 101,000 katika nchi hii wanashirikiana na makundi zaidi ya 1,150 ya Kihispania.
Sehemu nyingine yenye kutokeza imekuwa ni uchapaji wa vitabu na Biblia wa tawi, ambao ulifikia tarakimu ya 35,811,861. Hii ilirudufisha uchapaji wa Biblia na vitabu vya mwaka uliopita na kwa mara ya kwanza uchapaji umekuwa maradufu ya ule wa mwaka uliotangulia tangu 1938! Kaseti zimetakwa sana. Wakati wa 1989, kaseti 3,500,000 zilitengenezwa, ambalo ni ongezeko la asilimia 71 zaidi ya mwaka uliotangulia. Hii inafanya jumla yote iwe kaseti 36,715,613 ambazo zimetengenezwa tangu utengenezaji ulipoanza katika Aprili 1978. Miongoni mwa zile zilizotengenezwa ni kaseti za Mnara wa Mlinzi. Mwaka wa utumishi ulianza kwa maandikisho 29,559 katika chapa ya kaseti, lakini mwaka ulimalizika kwa 38,896—ongezeko la asilimia 31.
Ili kutegemeza uchapaji sawia huu wa magazeti yetu katika lugha nyingi, habari zinazohusu maneno, miandiko, na picha huwekwa kwenye disketi za kompyuta na filamu. Hivyo, inakuwa lazima tawi lisafirishe disketi 50 na vipande vya filamu kati ya 3,000 na 3,500 kila juma kwa ajili ya magazeti peke yake. Kwa njia hii inawezekana mashine za kupiga chapa zichape Mnara wa Mlinzi kwa usawia katika lugha 45 katika matawi kuzunguka ulimwengu.
Visiwa vya Pasifiki
Mtume Paulo aliwahubiri wafalme, na leo, njia ziko wazi pia kwa wale wenye mamlaka kuu wajue ile “Njia” ya Ukristo wa kweli.—Mdo. 24:22; Rum. 13:1.
Painia wa pekee katika Fiji anajifunza Biblia na chifu mmoja mwenye cheo cha juu, ambaye baba yake ni waziri wa habari wa kisiwa hicho and ndugu yake ni gavana wa Benki ya Kuweka Akiba ya Fiji. Chifu huyo alikuwa mjumbe kwenye baraza la mkoa la hivi majuzi, mkutano wa machifu wa vyeo vya juu ukiongozwa na rais wa Fiji. Kwenye ajenda lilikuwako suala la amri ya Sabato ambayo, miongoni mwa mambo mengine, inazuia shughuli za umma siku ya Jumapili na imekuwa suala zito kwa Wamethodisti.
Wakati wa mkutano huo, mjumbe mmoja alitaka kuzungumza juu ya shauri la kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova. Huyo chifu anayejifunza akakatiza, akisema kwamba kwa ukawaida Shahidi huenda kwenye nyumba yake kumfundisha Biblia. “Sasa ninaanza kujua Mashahidi wa Yehova ni akina nani na kwa nini mafundisho yao yanawasukuma wazuru makao yetu,” akasema yule chifu. “Pia nimeona kwamba Mashahidi wanabeba Biblia zao kuanzia Jumatatu mpaka Jumapili, jambo ambalo ni tofauti sana na sisi Wamethodisti, ambao tunabeba zetu Jumapili peke yake. Mashahidi wa Yehova wanaeleza unabii wa Biblia waziwazi na kwa njia dhahiri.” Kisha akamwuliza hivi yule mjumbe aliyetokeza shauri la kuwapiga marufuku Mashahidi: “Je! wewe umepata kufungua mlango wako ili uwasikilize Mashahidi?”
“La,” akajibu yule mjumbe. “Basi ni kuwaza kipumbavu kupiga marufuku dini ambayo hujawahi kusikiliza,” akajibu yule chifu. Kisha, akatokeza shauri la kupinga lile la mjumbe: “Wale ambao miongoni mwenu wamesikiliza fundisho la Mashahidi wa Yehova na wanataka waendelee kuhubiri katika mkoa huu, inueni mikono yenu.” Wajumbe ishirini kati ya wale 30 wakainua mikono.
Papua New Guinea ni bara lenye kupita kiasi katika viwango vya maisha na desturi. Ijapokuwa kutoa ushahidi katika majiji makubwa ni sawasawa na kutoa ushahidi katika nchi nyingi za Magharibi, ni tofauti sana katika vijiji ambamo desturi za zamani zingali zinaongoza. Walipokuwa wakifanya kazi katika eneo lisilogawiwa mtu katika sehemu ambamo Ukatoliki wa Roma umezidi, akina ndugu walishauriwa wapate ruhusu ya kwenda mlango kwa mlango kutoka kwa chifu wa kijiji, kwa kuwa ana mamlaka kamili katika kijiji kile. Ni nini kilichotukia Mashahidi walipomwendea chifu mmoja wa kijiji?
Ndugu aliyekuwa akiongoza kile kikundi anasimulia hivi: “Tuliegesha magari yetu nje ya kizingo cha kijiji, kisha watatu wetu tukaingia kwenye kijiji kile tukitafuta nyumba ya chifu. Wanakijiji walitupeleka kwenye nyumba moja iliyokuwa karibu na kitovu cha kijiji kile, ambako tulijulishwa kwa chifu na jamaa yake. Alikuwa mtu mwenye kuvutia, mwenye mvi nyingi na umbo kubwa, linalomfaa chifu. Alikuwa mwenye elimu ya juu na alisema Kiingereza kwa ufasaha. Alituambia tulete ndugu na dada wote wa kikundi chetu kwenye kijiji. Kisha akatuambia sisi sote tuketi chini huku akituma wanaume vijana kwenye nyumba zote ili wawaambie wanavijiji watusikilize. Kwa hiyo tukiwa wawili wawili kikundi chetu kilitumia saa mbili na nusu zilizofuata tukizuru kila nyumba. Wanavijiji walio wengi walitualika ndani ya nyumba, na wengi walikubali fasihi. Tulipomaliza kuzuru zile nyumba, yule chifu alituambia tuketi chini tena mbele yake. Yeye alieleza kwamba haamini tena mafundisho ya Wakatoliki, akihisi kwamba makanisa ya Jumuiya ya Wakristo ‘wamepotosha mawazo’ ya wanavijiji. Kwa wema yeye alitualika tuzuru kile kijiji tena, akisema kwamba huenda atashambuliwa na kasisi Mkatoliki wa mahali hapo, lakini kwamba jambo hilo halingemhangaisha kamwe.”
Mastermind ni programu kichemsha-bongo ya televisheni inayoenda hewani katika taifa lote la New Zealand. Kwenye programu hiyo kila mmoja wa wale wanne wanaoshindana anaulizwa swali kuhusu habari fulani maalumu anayochagua mwenyewe, kisha kuhusu habari za kawaida. Kwa kuwa mshindani mmoja, mwanasheria, alichagua kiwe kichwa chake cha pekee, “Historia na Mafundisho ya Mashahidi wa Yehova,” stesheni ya televisheni iliomba ofisi ya tawi itayarishe na kupeleka maswali 30 kwenye programu hiyo.
Programu hiyo ilitangazwa kwa juma moja kabla ya kwenda hewani, na bila shaka, kila wakati programu hiyo ilipotangazwa, jina Yehova lilionekana kwenye kiwambo cha Televisheni, likionwa na makumi ya maelfu ya watazamaji. Programu hiyo ilipopelekwa hewani, watazamaji walisikia majibu kwa maswali kama haya:
Toa rangi na maelezo kuhusu alama iliyotumiwa kuwatambulisha Mashahidi wa Yehova katika kambi za mateso za Nazi.
Katika Agosti 1985, Mashahidi 94,000 walihudhuria mikusanyiko katika nchi gani ya kikomunisti?
Maswali mengine yalihusiana na Shule ya Biblia ya Gileadi ya Mnara wa Mlinzi, wasimamizi wa Sosaiti, mti wa mteso ukitofautishwa na msalaba, Har–Magedoni, na sababu za Kimaandiko za talaka.
Tawi laandika hivi: “Tunaterema kuripoti kwamba ushahidi umetolewa si kwa wasikilizaji wa televisheni tu bali pia kwa wafanya kazi wa televisheni walioombwa wafanye utafiti kuhusu maswali hayo na watu waliohusika kufanyiza programu.”
Nchi Zilizo Chini ya Marufuku
“Ikiwa wameninyanyasa mimi, watawanyanyasa nyinyi pia,” akasema Bwana Yesu. Katika siku zetu, mnyanyaso huu unatia ndani kupigwa marufuku wanafunzi wake katika nchi 36.—Yoh. 15:20, NW.
Hatua kadhaa dhidi ya utendaji wa kitheokrasi zilichukuliwa mwaka huu uliopita katika nchi kadhaa katika Afrika. Tawi katika mojapo nchi hizo laandika hivi: “Kikundi cha askari wakiwa na bunduki mimina-risasi, kilipanda juu ya ua penye mahali petu pa ujenzi, kikamshinda nguvu askari mlinzi, kikafungua malango, na kuingia ndani. Tangu wakati huo kimekuwa humo, majengo hayo yetu yanatumiwa sasa kama kituo cha kuzoezea askari wapya. Ijapokuwa barua nyingi zilizopelekewa wenye mamlaka na ujumbe wa kibalozi kuingilia jambo hilo, jitihada zote za kupata mali hiyo na vichapo vilivyowekwa humo zimekuwa bure mpaka sasa. Halafu miezi minne baada ya majengo hayo kuchukuliwa, Msimamizi wa Baraza la Hukumu ambaye pia ni Waziri wa Haki alitia moyo kwamba vitovu vyovyote vya utendaji vifungwe na pia watu wowote ambao wanashikwa wakihubiri dini hii isiyo halali washtakiwe. Miezi mitano baadaye, Msimamizi huyo huyo wa Baraza la Hukumu aliitisha mkutano wa wawakilishi wa madhehebu ya dini zote. Kwenye mkutano huo alilaumu hasa Mashahidi wa Yehova, akisema kwamba sisi ni roho waovu halisi.”
Hata hivyo akina ndugu wa huko waliendelea kutoa ushahidi kwa ujasiri. Kwa kielelezo, taarifa rasmi ilipelekwa kwa wenye mamlaka wote katika eneo la mwangalizi wa mzunguko mmoja, likilalamika kwa sababu ya utendaji ulioongezeka wa Mashahidi na kuwakumbusha wenye mamlaka kuhusu hali ya kupigwa marufuku. Ijapokuwa hivyo, mwangalizi wa mzunguko akiwa ameandamana na ndugu mwenyeji aliamua kwamba atamtembelea meya wa sehemu moja. Kabla ya kwenda, walimtolea Yehova sala kwa moyo wa bidii. Walipomkosa meya nyumbani, walienda kwenye ofisi yake, ambako walieleza wao ni akina nani. Kwa mshangao wao, alifunga ofisi yake akawakaribisha nyumbani kwake. Wakiwa wanajua kwamba mke wake alikuwa amekufa karibuni, ndugu hao walimpa faraja kutoka kwa Maandiko. Kisha meya akawauliza kwa nini walikuwa wanaendelea kuhubiri na wanajua kwamba wamepigwa marufuku. Walisababu pamoja naye kutoka kwa Maandiko, alikubali kitabu na vijitabu vitano.
Nchi moja katika Esia imekuwa chini ya marufuku kwa miaka 13. Wakati wa mwaka wa utumishi uliopita, wamekuwa wakipata upinzani zaidi. Hata hivyo, wamekuwa na ongezeko la asilimia 10 katika wahubiri na kilele kipya katika mafunzo ya Biblia ya nyumbani.
Katika nchi hii funzo la Biblia lilianzishwa na mke wa ofisa wa kijeshi. Mwanamke huyo pamoja na watoto wake watano walianza kuhudhuria mikutano. Upinzani mkali kutoka kwa mume wake ukaanza; hata akampiga kwa mshipi wake wa kijeshi. Upinzani huo mkali ulipoendelea, mwanamke huyo alijitahidi kuzoea kanuni za Kikristo ambazo alikuwa amejifunza. Hatimaye, kuendelea kwake kuwa na mwenendo mwema wa Kikristo kulimvutia sana mume wake. Tangu wakati huo mume amejiuzulu na sasa anajifunza Biblia na mmoja wa ndugu zetu.
Ijapokuwa marufuku katika nchi kadhaa na vizuizi vinavyotokana nayo, Yehova amebariki jitihada za watu wake sana. Kupitia yote haya, Yehova amethibitisha kwamba mkono wake si mfupi. Kondoo wanalishwa, na wapya wengi wanakuja kutambua chanzo cha tumaini la kweli.—Zab. 18:2.
[Maelezo ya chini
a Ili upate habari zaidi ona Mnara wa Mlinzi, Novemba 1, 1989.
[Chati katika ukurasa wa 18]
Mikusanyiko ya Wilaya ya Polandi ya 1989
JIJI TAREHE HUDHURIO UBATIZO
Poznan Agosti 4-6 40,442 1,525
Katowice Agosti 4-6 65,710 2,663
Warsaw Agosti 11-13 60,366 1,905
JUMLA 166,518 6,093
[Chati katika ukurasa wa 34-41]
RIPOTI YA MWAKA WA UTUMISHI WA 1989 YA MASHAHIDI WA YEHOVA ULIMWENGUNI POTE
(Ona nakala iliyochapishwa)
[Ramani katika ukurasa wa 18]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
POLANDI
Poznan
Warsaw
Katowice
[Picha katika ukurasa wa 6]
Mwaka wa utumishi uliopita, wanafunzi wapya 263,855 walibatizwa
[Picha katika ukurasa wa 13]
Katika Italia kwenye “Ujitoaji Kimungu” mikusanyiko, kile kitabu kipya “Questions Young People Ask—Answers That Work” chatolewa, na vijana waonyesha kwa fahari vitabu vyao vipya
Kwenye mkusanyiko mmoja katika United States, kile kitabu “The Bible—God’s Word or Man’s?” chatolewa
[Picha katika ukurasa wa 19]
Stediamu Slaski katika Chorzów, karibu na Katowice, ilisongamana wakusanyikaji; na umati mkubwa wa watu walibatizwa
[Picha katika ukurasa wa 20]
Wajumbe kutoka Ulaya ya Mashariki walisisimuka kuwa miongoni mwa makutano mengi ya waliohudhuria mkusanyiko wa Poznan, ambapo ile broshua mpya, “Should You Believe in the Trinity?”, ilitolewa katika lugha ya Kipolandi
[Picha katika ukurasa wa 21]
Stediamu ya Warsaw ilijazana wajumbe waliotoka nchi 28. Hapa visehemu ya programu vilitafsiriwa kwa wakati ule ule mmoja katika lugha 16. Anayesimama ni mtafsiri Mfaransa pamoja na wasemaji Wapolandi
[Picha katika ukurasa wa 22]
Darasa la kwanza katika Ulaya la Shule ya Mazoezi ya Kihuduma lilihitimu katika Juni 18, 1989, Vienna, Austria
[Picha katika ukurasa wa 23]
Katika United States darasa la tatu la Shule ya Mazoezi ya Kihuduma lilihitimu katika Novemba 13, 1988, na darasa la nne katika Juni 11, 1989
[Picha katika ukurasa wa 27]
Tawi la Maurishasi lina ofisi na makao ya kuishi. Kuna Jumba la Ufalme upande mmoja wa uwanja
[Picha katika ukurasa wa 28]
Majengo manne mbalimbali yakiwa yamezungukwa na bustani za kitropiki zenye majani mabichi-mabichi yafanyiza majengo-tata ya Betheli yenye meta za mraba 8,900 katika El Salvadori. Hayo majengo-tata yana sebule mpya, na chumba cha kulia chenye kukaa watu 200, pia vyumba vya kulala Wanabetheli wakujitolea 72
[Picha katika ukurasa wa 29]
Jengo-tata la tawi katika Peru lina bohari mpya na Jumba la Ufalme pia vyumba zilizoongezwa 36, zikifanyiza jumla ya vyumba 58. Sebule inaonekana upande wa kulia.
[Picha katika ukurasa wa 30]
Katika Japani jengo jipya la tawi la makao lenye orofa nane lina nafasi ya sakafu ya meta 8,980 za mraba na linatia ndani vyumba 128 kwa ajili ya Wanabetheli wa kujitolea. Kiwanda kipya kina nafasi ya sakafu ya meta za mraba 22,600. Sebule inaonekana upande wa kulia.