Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb04 kur. 6-30
  • Matukio Muhimu Ya Mwaka Uliopita

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Matukio Muhimu Ya Mwaka Uliopita
  • 2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Makusanyiko ya “Mtukuzeni Mungu”
  • Vitabu Vipya Vyatolewa
  • Viziwi Wafurahia Video
  • Msaada kwa Watafsiri
  • Kuzoezwa Kuwa Walimu Bora
  • Mambo ya Kisheria
  • Kuvumilia Majaribu
  • Maeneo ya Uchapaji
  • Mabadiliko Mengine Huko Brooklyn na Wallkill
  • Ujenzi wa Majumba ya Ufalme
  • Majumba Mapya ya Makusanyiko
  • Kuweka Wakfu Ofisi za Tawi
  • Matukio Muhimu Ya Mwaka Uliopita
    2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Mashahidi wa Yehova—Ripoti ya Kitabu-Mwaka 1994
    1994 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Kitabu-mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1990
    1990 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
yb04 kur. 6-30

Matukio Muhimu Ya Mwaka Uliopita

YEHOVA alitabiri kwamba “katika siku za mwisho,” watu wangemiminika kwenye mlima wake wa mfano ili wafundishwe naye. (Mika 4:1, 2) Unabii huo uliendelea kutimizwa mwaka uliopita watu wengi walipotenda kupatana na maneno ya andiko la mwaka wa 2003, “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yak. 4:8) Makusanyiko ya Wilaya na ya Kimataifa ya “Mtukuzeni Mungu,” yaliwasaidia wengi kujenga uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Yehova.

Makusanyiko ya “Mtukuzeni Mungu”

Msemaji fulani katika mojawapo ya makusanyiko hayo yaliyotajwa, alisema hivi kwa shauku: “Kwa kuwa uumbaji wa Yehova usio na uhai unaweza kumtukuza, hakika sisi tulio na akili na tunaoweza kusema, tunaweza kumtukuza hata zaidi Muumba wetu Mkuu!” Kisha akanukuu andiko la Ufunuo 4:11 linalosema hivi: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.”

Makusanyiko 32 ya kimataifa ya “Mtukuzeni Mungu” yalimletea Yehova sifa kwa njia ya pekee. Makusanyiko hayo yalifanywa katika nchi ya Afrika Kusini, Australia, Chile, Denmark, Ghana, Hawaii, Hispania, Hungaria, Japani, Kanada, Marekani, Mexico, Ukrainia, na Uswisi. Mishonari na wengine wanaotumikia katika nchi za kigeni waliweza kutembelea nchi za kwao, ambako walihojiwa kuhusu kazi ya Ufalme katika maeneo ya mbali wanakotumikia. Maelfu ya ndugu na dada kutoka nchi nyingine walihudhuria pia makusanyiko hayo.

Ndugu kutoka nchi nyingine walifurahia hasa kuzuru ofisi za tawi katika nchi walizotembelea. Ofisi ya tawi ya Marekani ilikuwa na pendeleo la kuwakaribisha zaidi ya wageni 6,750 kutoka nchi 36 na kuwaandalia milo 15,000 hivi! Siku moja baada ya chakula cha mchana, ndugu na dada kutoka Afrika Kusini waliwaimbia Wanabetheli kwa ulinganifu wa sauti nne katika lugha sita: Kiafrikana, Kiingereza, Kisepedi, Kisesotho, Kixhosa, na Kizulu. Nyimbo hizo tamu ziliwagusa sana wasikilizaji hivi kwamba wengi walibubujikwa na machozi.

Ndugu mmoja ambaye alikuwa amesafiri kutoka nchi ya mbali sana, alisema hivi: “Sijawahi kuwa pamoja na ndugu na dada zangu wa kiroho kwa muda mrefu hivi. Sitasahau kamwe pindi hii ya pekee. Hivi ndivyo tutakavyoishi katika ulimwengu mpya.” Ndugu mmoja kutoka Uingereza, aliyekuwa ameacha ukweli alipokuwa na umri wa miaka 17, lakini aliyerudi miaka michache iliyopita, aliguswa moyo alipoona mchoro wa mwana mpotevu. Baadaye, alipokuwa akifurahia chakula cha mchana pamoja na familia ya Betheli huko Brooklyn, alitafakari rehema ya Yehova, kisha akaanza kutokwa na machozi. Ndugu kutoka Hispania alisema kwamba mke wake hajawahi kumwona akilia tangu wafunge ndoa miaka 29 iliyopita. Lakini alilia wakati yeye na wasafiri wenzake walipokaribishwa na umati wa Mashahidi wenye shangwe kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa huko Houston, Texas.

Nyakati nyingine ni vigumu kukodi kwa bei nafuu uwanja unaofaa kwa ajili ya makusanyiko makubwa. Hata hivyo, jina zuri ambalo Mashahidi wa Yehova wamejijengea tangu zamani husaidia mara nyingi. Ofisi moja ya tawi iliripoti hivi kuhusiana na jambo hilo: “Baada ya kutafuta uwanja kwa bidii, tulipata uwanja mmoja unaofaa ambao ungeweza kutoshea watu wote 50,000 waliotarajiwa kuhudhuria kusanyiko. Hata hivyo, baada ya kuzungumza na maafisa wa uwanja huo, ndugu waliona kwamba gharama ilikuwa ya juu sana. Siku chache baada ya ndugu kutoka ofisi ya tawi kuzungumza na maafisa wa uwanja huo, maafisa hao waliwasiliana na ofisi ya tawi na walitaka kuzungumza na ndugu hao tena. Baadaye, mkurugenzi mmoja mkuu alisema hivi: ‘Mwanzoni hatukuelewa vizuri ni kusanyiko la aina gani mnalotaka kufanya. Lakini tulipoona kwamba mna uzoefu na ujuzi mwingi wa kupanga na kuandaa huduma mbalimbali, tulisisimuka sana kuhusu kusanyiko hilo. Tunavutiwa na ustadi na uzoefu wenu wa kupanga mambo na utaratibu wenu mzuri.’” Hivyo, Mashahidi wa Yehova waliweza kukodi kwa bei nafuu uwanja huo kwa ajili ya kusanyiko lao.

Vitabu Vipya Vyatolewa

Je, wewe ni mwanafunzi mwenye bidii wa Neno la Mungu? Ikiwa ndivyo, bila shaka ulifurahia kupokea broshua ‘Ona Nchi Nzuri’ yenye kurasa 36, iliyo na picha zenye rangi. Pasipo shaka, ramani, picha, michoro ya kompyuta, na mambo mengineyo mengi, yataboresha funzo lako la kibinafsi. Kwa hiyo, iweke broshua ‘Ona Nchi Nzuri’ pamoja na Biblia yako na vitabu unavyotumia kwa ukawaida unapojifunza. Na usisahau kwenda nayo mikutanoni wakati nchi za Biblia zitakapozungumziwa.

Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu chenye kurasa 256 na picha maridadi kilitolewa na msemaji aliyetoa hotuba, “Watoto Wetu Ni Urithi Wenye Thamani.” Wazazi wanaowapenda watoto wao watafurahia kujifunza kitabu hicho kizuri pamoja nao. Kitabu hicho kinasema hivi: “Watoto . . . wanahitaji mwongozo bora wa maadili, na kanuni za kuwaongoza maishani. Wanahitaji mwongozo huo tangu utoto. Mambo yenye kuvunja moyo hutokea watoto wasipopata msaada wakiwa wangali wachanga.”

Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu kina zaidi ya picha 230, karibu maradufu ya idadi ya picha zilizo katika kitabu Hadithi za Biblia. Kila picha, au picha kadhaa zikiwa pamoja, inaambatana na maelezo au swali. Majibu yanapatikana kwenye ukurasa uleule. Maswali hayo na maswali mengine mengi katika kitabu hicho yanaweza kuchochea mazungumzo kwa kuwa yanawapatia watoto nafasi ya kujieleza kutoka moyoni. Kwa mfano, swali “Kwa nini ni jambo la maana kukumbuka kusema asante?” linaambatana na picha zilizo kwenye ukurasa wa 101. Wazazi, msikose kusoma utangulizi, “Watoto Wanahitaji Nini Kutoka kwa Wazazi?” Ukifuata mapendekezo yanayotajwa hapo, watoto wako watafaidika sana na kitabu hicho kizuri cha funzo.

Viziwi Wafurahia Video

Katika mwaka wa 1915 huko Marekani, mwangalizi anayesafiri, John A. Gillespie, alitafsiri nyimbo katika lugha ya ishara kwa viziwi wachache waliohudhuria kusanyiko la Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo. Sasa kuna zaidi ya makutaniko na vikundi 1,200 vya wahubiri viziwi na watu viziwi wanaopendezwa ulimwenguni pote. Wanalishwa kiroho kwa njia gani?

Kwa sasa, magazeti na vitabu vya kujifunzia Biblia vinapatikana katika lugha 18 za ishara, na idadi hiyo inaendelea kuongezeka. Wale wanaotumia Lugha ya Ishara ya Marekani walipata zawadi ya pekee mnamo Septemba 2002. Kuanzia mwezi huo, makala za funzo la Mnara wa Mlinzi zinapatikana kwenye video inayotolewa kila mwezi. Video hiyo inawasaidia viziwi kwa njia ambazo watu wengine hawajawahi kufikiria.

Kwa mfano: Mashahidi wengi wasio viziwi wanaweza kukariri maandiko mengi. Wanaweza kukumbuka maandiko kwa sababu kila wanaposoma au kusomewa maandiko hayo, wao husoma au kusikia maneno yaleyale. Sivyo ilivyo na viziwi. Kwa nini? Kwa sababu Biblia haipatikani katika Lugha ya Ishara ya Marekani, na wale wanaoongoza mikutano hawatumii ishara zilezile wanapozungumzia andiko fulani. Lakini, hali hiyo ilianza kubadilika wakati video za magazeti na vitabu zilipotolewa katika Lugha ya Ishara ya Marekani. Na sasa, kwa kuwa makala za funzo la Mnara wa Mlinzi pia zinapatikana kwenye video, viziwi wanaohudhuria funzo la Mnara wa Mlinzi wanaona ishara zilezile zikitumiwa kutafsiri maandiko yaleyale ya Biblia.

Isitoshe, makutaniko na vikundi vya Lugha ya Ishara ya Marekani havihitaji tena kuwa na “wasomaji” wanaotafsiri mafungu ya Funzo la Mnara wa Mlinzi katika lugha ya ishara. Katika makutaniko ya watu wasio viziwi, huenda ndugu atakayesoma mafungu wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi akatumia saa moja hivi ya ziada anapotayarisha makala ili kufanya mazoezi ya kusoma vizuri. Lakini katika kutaniko la wahubiri viziwi, mara nyingi ndugu waliotafsiri mafungu katika lugha ya ishara walikuwa wakitumia saa nyingi kufanya mazoezi. Sasa, muda huo unaweza kutumiwa katika utendaji mwingine wa kiroho. Ndugu na dada wanaonaje mpango huo mpya?

Kikundi cha wahubiri viziwi katika jimbo la Rhode Island, Marekani, waliandika hivi: “Tulifurahi sana tulipotangaziwa kwamba tungepata makala za Mnara wa Mlinzi kwenye video. Baadhi ya wahubiri waliguswa hivi kwamba walibubujikwa na machozi.” Kiongozi mmoja wa Funzo la Mnara wa Mlinzi huko Florida alisema kwamba sasa watu wengi sana huinua mikono ili watoe maelezo hivi kwamba yeye “hutatizika kuchagua atakayejibu!” Aliongeza kwamba “akina ndugu wanatoa maelezo bora.” Mzee mwingine aliandika hivi: “Matokeo yamekuwa mazuri sana! Ndugu na dada huelewa vizuri zaidi mambo magumu pia.” Naam, kwa sababu ya baraka ya Yehova, umati unaoongezeka wa viziwi hufurahia pendeleo la kumjua na kumtukuza Mungu.—Rom. 10:10.

Msaada kwa Watafsiri

Chakula cha kiroho kinachoandaliwa na jamii ya msimamizi-nyumba mwaminifu kinapatikana sasa katika angalau lugha 390. (Luka 12:42) Kwa hiyo, kazi ya kutafsiri ni mojawapo ya kazi muhimu ya tengenezo la Yehova, nayo inaongezeka daima.

Tafsiri sahihi si tafsiri ya neno kwa neno. Bali inamaanisha kutafsiri kwa usahihi maana ya habari. Kwa hiyo ni lazima watafsiri waelewe habari vizuri kabla ya kuanza kutafsiri. Nyakati nyingine, hilo linaweza kuwa jambo gumu.

Ili kutatua tatizo hilo, Baraza Linaloongoza lilielekeza kwamba ndugu kadhaa walioteuliwa wazoezwe kufundisha Mtaala wa Kuongeza Ujuzi wa Lugha ya Kiingereza. Baada ya kuhudhuria mtaala kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, ndugu hao waliwafundisha watafsiri kotekote duniani katika mwaka wa utumishi wa 2002 na 2003. Walitumia miezi mitatu hivi kufundisha kila kikundi cha watafsiri mtaala huo na kuwapa mawaidha kuhusiana na kazi yao. Mtaala huo umewasaidia watafsiri kuelewa vizuri zaidi habari za Kiingereza wanazotafsiri.

Kikundi kimoja cha watafsiri kilisema hivi: “Kwa fadhili, Yehova alitusaidia kufanya kazi yetu kwa ustadi zaidi. Sasa tuna uhakika zaidi. Tunatarajia kuona matokeo mazuri, Yehova akiendelea kutubariki.” Msimamizi mmoja wa Idara ya Kutafsiri alisema hivi: “Zamani, wengi wetu tuling’ang’ana kwa saa nyingi kuelewa maneno au sentensi fulani za Kiingereza. Jambo hilo lilichelewesha kazi yetu. Kwa hiyo, tunathamini sana mtaala huo. Tulionyeshwa jinsi ya kuchanganua maana ya habari za Kiingereza hatua kwa hatua, na tulifundishwa njia nzuri sana za kushughulikia habari tata. Kwa hiyo, sasa hatuna wasiwasi mwingi, na tunaweza kutafsiri kwa usahihi na haraka zaidi.”

Watafsiri wengine waliandika hivi: “Mtaala huo ulikuwa mzuri kuliko mtaala unaotolewa chuoni, kwa kuwa ulilenga hasa matatizo tunayokabili katika kazi yetu. Tunaamini kwamba masomo hayo yatawasaidia watafsiri ulimwenguni pote, na kuwawezesha watu wenye mfano wa kondoo ‘kuelewa maana’ ya kweli za Biblia kwa urahisi zaidi.”—Mt. 13:23.

Kufikia leo, watafsiri 1,660 hivi ambao wanatafsiri katika zaidi ya lugha 150 wamefaidika na mtaala huo. Isitoshe, mpango huo umewasaidia pia watafsiri wa lugha ya ishara na wale wanaotafsiri kutoka Kihispania hadi lugha mbalimbali za kienyeji za Amerika ya Kati na Kusini.

Kuzoezwa Kuwa Walimu Bora

Yehova na Mwana wake wa pekee, anayeitwa “Neno,” huyaona mawasiliano kuwa jambo muhimu sana. (Yoh. 1:1, 14; 3:16; Ufu. 19:13) Jamii ya mtumwa mwaminifu inaendelea kufanya kazi kwa bidii ili kuwasaidia watu wa Mungu kuboresha ustadi wao wa kuhubiri na kufundisha. Kwa kusudi hilo, tengenezo la Yehova lilichapisha kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Wahubiri wengi wamelishukuru tengenezo la Yehova kwa kitabu hicho tangu kilipoanza kutumiwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi mnamo Januari 2003.

Mzee mmoja huko Filipino aliandika hivi: “Hakuna dini nyingine inayowasaidia sana washiriki wake, vijana kwa wazee, kuboresha ustadi wao wa kuwasiliana.” Mzee fulani nchini Brazili alisema hivi: “Kwa maoni yangu, mpango ulioanzishwa Januari 2003 ulikuwa hatua muhimu sana kuhusiana na kazi ya kufundisha ya Mashahidi wa Yehova.” Mzee mwingine alisema hivi: “Nimeona kwamba vijana kutanikoni wana hamu zaidi ya kujiunga na shule. Wengine wao wamekwisha soma kitabu chote na wamefanya mazoezi yote hata kabla hatujazungumzia habari hizo kwenye shule!” Mwangalizi mmoja anayesafiri ametumia kitabu Shule ya Huduma mara kwa mara katika ziara zake za uchungaji. Anaandika hivi: “Sura kama vile ‘Jitahidi Uwe Msomaji Mzuri,’ ‘Funzo Lina Faida,’ na ‘Jua Jinsi Unavyopaswa Kujibu’ zinatoa mawaidha mazuri ya jinsi ya kujitayarisha kwa ajili ya huduma na mikutano.”

Dada mmoja huko Uingereza alisema kwamba “mazoezi yaliyo katika kitabu hicho ni mazuri sana. Tukitaka kukuza stadi zinazofundishwa katika shule, tunahitaji kuzifanyia mazoezi kwa ukawaida. Mazoezi yaliyo katika kitabu hicho hutuwezesha kutimiza lengo hilo.” Ndugu kutoka Japani, aliye na kigugumizi, anaandika hivi: “Kila ninapopata mgawo wa kusoma, mimi huwa na wasiwasi sana kwa sababu sijui ikiwa nitasoma vizuri nikiwa jukwaani. Nimetambua kwamba wasiwasi huo umeathiri usomaji wangu. Kwa hiyo, hivi majuzi nilipopata mgawo wa kusoma, niliandika mashauri yanayopatikana katika kitabu Shule ya Huduma, chini ya kichwa kidogo ‘Jinsi ya Kusema kwa Njia Inayoeleweka Wazi’ (ukurasa wa 87 na 88) na katika sanduku lenye kichwa ‘Kukabiliana na Kigugumizi’ (ukurasa wa 95). Sitarajii kushinda tatizo langu la kigugumizi mara moja, lakini sitakata tamaa!”

Ndugu kwenye ofisi ya tawi ya Kenya wanaandika hivi: “Ndugu huko Burundi wanathamini kitabu hicho kipya ambacho sasa kinapatikana katika Kirundi. Watu wengi katika nchi hiyo hawajasoma sana, lakini sasa wanafunzi wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi wanaweza kuelewa mashauri ya usemi vizuri zaidi. Kwa hiyo, wao hutoa hotuba zao kwa shauku zaidi.”

Kitabu hicho pia kimewasaidia watu kadhaa kuboresha ustadi wao wa kuandika barua. Dada mzee mgonjwa huko Mexico, anasema hivi: “Katika kitabu Shule ya Huduma, ukurasa wa 71 hadi 73, nilipata mapendekezo mazuri sana kuhusu jinsi ya kuandika barua. Kwa kawaida mimi huhubiri kwa njia ya barua kwa sababu ya ugonjwa wangu, hata hivyo, sikuwaandikia watu wangu wa ukoo. Lakini sasa, kwa kufuata mwelekezo wa kitabu hicho kipya, ninaweza kuwahubiria kwa njia nzuri zaidi.” Mwangalizi wa wilaya huko Afrika Kusini alisema hivi: “Kitabu hicho kinatoa mwongozo mzuri sana. Mbali na kuzifafanua sifa za usemi, kinaonyesha kwamba sifa hizo hutokana na upendo wa Kikristo na kuwajali wengine.”

Mambo ya Kisheria

Juni 17, 2002, Mahakama Kuu ya Marekani ilitoa uamuzi muhimu katika Kesi Kati ya Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc. na Kijiji cha Stratton. Mahakimu 8 kati ya 9 wa Mahakama ya juu zaidi nchini humo walihisi kwamba takwa la sheria la kuwa na kibali ili kwenda nyumba hadi nyumba kuombaomba au kuuza bidhaa, halihusu kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova, na ni kinyume cha katiba kuwalazimisha kuwa na kibali.

Baada ya ushindi huo, Idara ya Sheria katika ofisi ya tawi ya Marekani iliwasiliana na manispaa mbalimbali nchini humo. Kwa hiyo, matatizo yaliyohusu kazi yetu ya kuhubiri yalitatuliwa katika manispaa 238, ambazo zilikuwa zimejaribu kuwekea kazi yetu ya kuhubiri vizuizi kupatana na sheria inayohusu kuombaomba au kuuza bidhaa nyumba kwa nyumba. Isitoshe, kwa sababu ya uamuzi wa kesi ya Stratton, wahubiri wa Ufalme katika manispaa nyingine 216 hawahitaji tena kuwaarifu polisi au maafisa wengine kabla ya kuhubiri katika maeneo fulani. Yehova na aendelee kuondoa vizuizi vya aina hiyo.—Isa. 40:4; Mt. 24:14.

Ndugu wangali wanakamatwa na kufungwa nchini Armenia kwa sababu wanakataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri zao. Mwendesha-mashtaka katika jiji kuu la Yerevan, amekata rufani ya kesi kadhaa za ndugu kusudi wahukumiwe vifungo virefu zaidi. Mahakimu wamekubali rufani hiyo, na kuwahukumia adhabu kali zaidi.

Mnamo Februari 2003, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu ilikubali kusikiliza kesi ya Mashahidi wa Yehova wawili waliokuwa mishonari. Wenzi hao wa ndoa walifukuzwa Bulgaria mwaka wa 1995, na walihisi kwamba huo ulikuwa ubaguzi na haki yao ya kuabudu ilikuwa imeingiliwa. Mahakama hiyo ilipata kwamba malalamiko hayo “yalikuwa na msingi.”

Mara baada ya ndugu kumaliza kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana jijini Asmara, Eritrea, polisi walizingira mahali ambapo walikutanika na kuwakamata watu wote 164 waliohudhuria—wanaume, wanawake, na watoto. Walifungwa na kuhojiwa usiku kucha. Siku iliyofuata, wenye mamlaka waliwaachilia watoto wote, dada wengi na watu waliopendezwa. Wengine walipelekwa kwenye gereza kubwa zaidi huko Asmara, ambamo baadhi yao walifungiwa kwa mwezi mmoja hivi kabla ya kuachiliwa. Mbali na kisa hicho, ndugu kumi ambao walikataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri zao, wangali katika kambi ya wafungwa. Watatu kati yao wamekuwa gerezani kwa miaka tisa.

Ndugu huko Georgia wanaendelea kushambuliwa kikatili. Makusanyiko ya wilaya yalisimamishwa kwa nguvu na maafisa na polisi wenye silaha waliovamia makusanyiko yaliyokuwa yakiendelea. Walipanda jukwaani na kuwaamuru wasikilizaji waondoke. Katika sehemu moja, waliweka vizuizi barabarani ili kuwazuia akina ndugu wasifike kusanyikoni. Mtesaji mkuu wa Mashahidi wa Yehova ana kesi ya kujibu lakini hajafungwa bado. Kesi yake imeahirishwa angalau mara 19. Wafuasi wake wamevamia mahakama mara kadhaa, na kuwapiga na kuwatukana akina ndugu. Idara ya Kodi ilifuta namba ya usajili ya kodi ya Mashahidi ambayo wanahitaji ili kuingiza vitabu nchini na kufanya shughuli nyingine.

Kuna habari njema kutoka Kosovo na Rumania. Wale wahubiri 90 wa Ufalme nchini Kosovo waliandikishwa kisheria Mei 20, 2003, na shirika lao likahalalishwa. Vivyo hivyo, Mei 22, 2003, serikali ya Rumania ilitoa amri ya kusajili dini ya Mashahidi wa Yehova nchini humo. Kifungu cha 3 cha amri hiyo kinasema hivi: “Dini hiyo ya Kikristo, yaani, ‘Shirika la Kidini la Mashahidi wa Yehova,’ ina wajibu na haki zote kama dini nyingine zinazokubaliwa na Serikali ya Rumania.” Amri hiyo inapatana na uamuzi fulani uliotolewa na Mahakama Kuu ya Rumania mwaka wa 2000.

Kesi iliyofunguliwa Mei 22, 2003, ili kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova jijini Moscow, Urusi, iliahirishwa hadi wakati usiojulikana. Hakimu aliwaamuru “wataalamu” wachunguze tena jinsi ambavyo vitabu vya Mashahidi wa Yehova vimewaathiri watu kiakili katika miaka kumi iliyopita. Hakimu huyo hakuweka wakati hususa wa kukamilisha uchunguzi huo. Kuna shaka kama uchunguzi huo utaweza kuthibitisha jambo lolote kisayansi. Wakati uo huo, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu imeanza kushughulikia malalamiko ambayo ndugu wamepeleka kwenye mahakama hiyo. Malalamiko hayo yanahusu ubaguzi na mnyanyaso ambao Mashahidi jijini Moscow wamevumilia kwa muda wa miaka saba iliyopita.

Kupatana na Kifungu Na. E-1516-2002 cha Agosti 8, 2002, Baraza la Mawaziri la sehemu ya kaskazini ya Cyprus, liliondoa marufuku iliyowakataza Mashahidi wa Yehova wasiingie sehemu ya kaskazini ya kisiwa hicho. Mapainia walifukuzwa kutoka sehemu hiyo marufuku ilipowekwa mwaka wa 1997. Ndugu walirudishiwa Majumba mawili ya Ufalme yaliyokuwa yamechukuliwa.

Nchini Uzbekistan, Marat Mudarisov, alipatikana na hatia ya “kuchochea chuki ya kidini na kuwadanganya watoto” wawe wafuasi wa dini yake. Alipewa kifungo cha nje. Hakufanya “kosa” lingine ila kuwahubiria majirani wake habari njema na kuongoza mazungumzo ya Biblia kila juma katika mikutano ya kutaniko. Hivi majuzi, ndugu walikata rufani katika Mahakama Kuu ya Uzbekistan na hukumu isiyo ya haki ya Ndugu Mudarisov ilibatilishwa.

Kuvumilia Majaribu

Mwisho wa ulimwengu huu unapokaribia, jeuri na vurugu za kisiasa zinazidi kuongezeka na mara nyingi husababisha magumu. Katika mwaka uliopita, vita vya wenyewe kwa wenyewe vilikumba nchi ya Liberia na jiji lake kuu, Monrovia. Ripoti moja ya shirika la habari la Reuters inasema hivi: “Vita viliendelea mitaani kwa juma zima na jiji lote lilikumbwa na machafuko na fujo. Baada ya waasi kuondoka kulikuwa na utulivu, lakini Juni 24, shambulio lingine baya zaidi liliharibu sana jiji hilo, na watu wengi waliuawa.” Ndugu kwenye ofisi ya tawi walieleza kwamba katika sehemu moja, ndugu walilazimika kulala chini kwenye sakafu yenye maji katika Jumba la Ufalme, makombora na risasi zilipokuwa zikifyatuliwa. Ndugu hao waliandika hivi: “Jiji liliharibiwa vibaya sana. Kulikuwa na uvundo wa maiti.” Watu walikufa pia kutokana na kipindupindu.

Watu wenye silaha walipora nyumba na Majumba ya Ufalme mara kwa mara. Wenzi wa ndoa ambao ni mishonari huko Monrovia, walieleza kwamba ndugu walijua wangeporwa vitu vyote vyenye thamani, kwa hiyo, wengi wao waliamua kuridhika na vitu vya lazima vya maisha. Baadhi ya familia hata hawakununua vitanda vipya, vile walivyokuwa navyo vilipoibiwa, bali walilala kwenye mikeka sakafuni. Wale ambao hawakuweza kurudi nyumbani walikimbilia sehemu nyingine, au nchi jirani.

Ofisi ya tawi inaandika hivi: “Watu hawajui kile kitakachowapata kesho. Hata hivyo, inatia moyo sana kuona kwamba akina ndugu wana hamu ya kuhudhuria mikutano na kushiriki katika kazi ya kuhubiri inapowezekana.” Mishonari waliotajwa hapo juu walisema kwamba msaada unapoletwa, “ndugu kwanza huomba vitabu vya Biblia, na nyakati nyingine, mkoba wa mahubiri.”

Maeneo ya Uchapaji

Septemba 1, 2001, ndugu saba kutoka sehemu mbalimbali za dunia waliwekwa kuchunguza uchapaji katika nchi mbalimbali. Baraza Linaloongoza liliwaomba ndugu hao kuchunguza ofisi zote za tawi zilizo na matbaa za kuchapa na kupendekeza jinsi ya kutumia vifaa hivyo kwa kiwango kikubwa zaidi. Kwa kutegemea mapendekezo ya kikundi hicho, Oktoba 17, 2001, Baraza Linaloongoza liliidhinisha mpango mpya wa maeneo ya uchapaji. Maeneo hayo ni Afrika, Amerika Kaskazini, Amerika Kusini, Asia, na Ulaya. Uchapaji wa magazeti na vitabu vyote kwa ajili ya nchi zilizo katika maeneo hayo utashughulikiwa na ofisi fulani za tawi katika maeneo hayohayo.

Mpango huo mpya ulianzishwa mapema mwaka wa 2002. Matokeo yamekuwa mazuri. Kwa mfano, fikiria uchapaji wa vitabu. Katika mwaka wa 2000, ofisi ya tawi ya Marekani ilichapa karibu nusu ya vitabu kwa ajili ya Mashahidi ulimwenguni. Lakini sasa chini ya mpango mpya, ni asilimia 26 tu ya vitabu ambayo huchapwa Marekani. Tokeo ni kwamba gharama ya kusafirisha vitabu imepungua, na vilevile idadi ya majengo ya kuchapia, mashine, na wafanyakazi imepunguzwa huko Marekani. Pia, matbaa za kuchapa katika nchi nyingine hutumiwa kwa kiwango kikubwa zaidi.

Walipoidhinisha mpango huo mpya wa uchapaji, Baraza Linaloongoza pia liliidhinisha ununuzi wa matbaa saba kubwa sana za kuchapa aina ya MAN Roland Lithoman. Matbaa hizo mpya zina uwezo mkubwa kuliko zile za zamani, hivyo, zitatosheleza mahitaji ya wakati ujao. Tano kati ya matbaa hizo ni za ofisi ya tawi ya Afrika Kusini, Brazili, Japani, Mexico, na Uingereza, na tayari baadhi yake zimewekwa. Zile nyingine mbili ni za kiwanda cha Wallkill, New York, na imepangwa ziwekwe Aprili na Mei 2004. Kila matbaa ina urefu wa meta 40, inaweza kuchapa visehemu vya vitabu vyenye ukubwa wa gazeti, au magazeti, 90,000 kwa saa (25 kwa sekunde), na inaweza kuchapa kwa rangi pande zote mbili za karatasi kwa wakati mmoja.

Mabadiliko Mengine Huko Brooklyn na Wallkill

Mbali na matbaa hizo mpya, kiwanda cha Wallkill kitapata pia mashine mpya zinazoweza kujalidi vitabu na Biblia aina ya deluxe 120 kwa dakika. Idara ya Upakizi na Usafirishaji, itahamishwa kutoka Brooklyn hadi Wallkill, ambako jengo refu jipya la kuhifadhia vitabu limejengwa. Katika jengo hilo, eneo linalohitajiwa kuhifadhia vitabu ni nusu ya eneo linalotumiwa kuhifadhia idadi ileile ya vitabu huko Brooklyn.

Majengo yaliyohamwa huko Brooklyn yatatumiwa kwa kazi nyingine. Isitoshe, mnamo Juni 2003, Baraza Linaloongoza lilitangaza kwamba huenda jengo lililo kwenye barabara ya 360 Furman Street, lenye ukubwa wa meta 95,000 za mraba, likauzwa. Idara ya Upakizi na Usafirishaji na idara nyingine zimekuwa katika jengo hilo. Baadhi ya idara hizo tayari zimehamishwa hadi majengo mengine huko Brooklyn na nyingine zitahamishwa hivi karibuni.

Ujenzi wa Majumba ya Ufalme

Majumba ya Ufalme 2,340 yalijengwa kotekote duniani mwaka wa utumishi wa 2003. Huo ni wastani wa majumba 195 kila mwezi, au zaidi ya 6 kila siku! Majumba ya Ufalme 7,730 yamejengwa tangu Novemba 1999, mpango huo ulipoanzishwa katika nchi maskini. Katika maeneo mengi, muda mfupi tu baada ya ujenzi kumalizika, hudhurio la mikutano huongezeka sana na majumba hujaa kabisa.

Mpango huo wa kujenga Majumba ya Ufalme ulipoanzishwa Afrika, kulikuwa na majumba mazuri ya ibada 550 katika nchi 38 barani humo. Miaka minne hivi baadaye, kulikuwa na Majumba ya Ufalme 5,060 katika nchi hizo 38, yaani, jumba 1 kwa kila makutaniko 3 au 4. Ili kuonyesha jinsi ambavyo watu wamevutiwa na ujenzi wa Majumba ya Ufalme, ofisi ya tawi ya Malawi ilitaja kamusi mpya iliyochapishwa na Shirika la Vitabu vya Kikristo la Malawi. Ofisi hiyo ya tawi inasema hivi: “Kamusi hiyo inaorodhesha jina Mashahidi wa Yehova na inaonyesha tafsiri sahihi ya jina hilo katika Kichichewa. Kisha, ili kuonyesha jinsi ya kutumia jina hilo katika sentensi, kamusi hiyo inasema hivi: ‘Mashahidi wa Yehova wamejenga makanisa mengi.’”

Ofisi ya tawi ya nchi fulani ya Afrika iliandika hivi: “Ndugu walipompelekea afisa mmoja ombi lao la kujenga Jumba la Ufalme, mara moja afisa huyo alirarua ombi letu na kulitupa. Baada ya kumwendea mara tatu, ndugu waliacha jambo hilo mikononi mwa Yehova. Punde baadaye, wenye mamlaka walimpa mmoja wa ndugu hao anayejulikana kwa unyofu wake, kazi ya kuwagawia maafisa wa serikali mikopo fulani.

“Yule afisa aliyerarua maombi yetu alikuwa miongoni mwa wale walioenda kupata mkopo. Lakini, alipomwona huyo ndugu katika ofisi ya mkopo, aliondoka mara moja na akarudi juma moja baadaye akitumaini kumpata afisa mwingine wa mkopo. Lakini wakati huu, ndugu yetu alimkaribia, akamwomba ampe fomu yake, na akaidhinisha mkopo. Afisa huyo aliaibika na kuwaomba ndugu wapeleke ombi lingine. Yeye mwenyewe alimwendea mkubwa wake ili aidhinishe ombi hilo, na akapata kiwanja kwa ajili ya Jumba la Ufalme. Sasa, afisa huyo anawaheshimu Mashahidi, naye alisema hivi: ‘Wao hawalipi ovu kwa ovu.’”

Ofisi ya tawi nchini Ukrainia inasimulia hivi: “Walipokuwa wakitafuta kiwanja, ndugu katika jiji la Artsyz walimwendea msanifu fulani wa ujenzi wa eneo hilo. Walimwonyesha picha za Majumba ya Ufalme ambayo tayari yalikuwa yamejengwa. Alivutiwa na kusema: ‘Jumba la Ufalme kama hilo linapaswa kujengwa karibu na majengo ya usimamizi wa mkoa, kwa kuwa litarembesha sehemu hiyo ya katikati ya jiji.’ Kisha akapendekeza kiwanja fulani. Baadaye mchora-ramani mkuu wa majengo wa eneo hilo aliongeza: ‘Ni mara yangu ya kwanza kuona wafuasi wa kanisa wakikubaliana kuhusu ramani ya ujenzi kabla ya kuanza kujenga. Kwa kawaida wao huanza kujenga kisha wanakubaliana kuhusu ramani.’”

Ujenzi wa Jumba la Ufalme ulipokuwa ukiendelea jijini Lysychans’k, mwanamke mmoja mfanyabiashara kutoka jiji jirani alisema hivi: “Nimekuwa nikiwatazama. Ninataka mjenge Jumba la Ufalme kama hili katika jiji langu. Hata nitawasaidia kupata kiwanja kinachofaa.” Ndugu walimwambia kwamba kuna Mashahidi watano tu katika eneo hilo, na watu hao wachache hawawezi kuanzisha kutaniko wala kujenga jumba. “Basi, mnahitaji Mashahidi wangapi?” aliuliza, kisha akaongeza: “Niandikishe mimi kuwa Shahidi wa sita.” Huenda alikuwa akifanya mzaha. Hata hivyo, alikubali kujifunza Biblia.

Majumba Mapya ya Makusanyiko

Mwaka wa utumishi uliopita, Majumba ya Makusanyiko yamejengwa na kuwekwa wakfu huko Nhandeara na Goiânia, Brazili; El Trébol, Santiago, Chile; Morne Daniel, Dominika; Machala, Ekuado; Syracuse, Sicily, Italia; Newburgh, New York, na West Palm Beach, Florida, Marekani; Gerehu, Papua New Guinea; Lomé, Togo. Mfanyabiashara mmoja alisema hivi kuhusu ujenzi uliokuwa ukiendelea huko Newburgh: “Shirika lenu ni la ajabu! Wafanyakazi wenu wanaojitolea wana malezi tofauti-tofauti, vipawa na stadi mbalimbali, lakini wote wanafanya kazi pamoja kwa amani. Sijawahi kuona jambo kama hilo!” Mkaguzi mmoja wa ujenzi aliyevutiwa na ujenzi na vilevile na ndugu na dada, alisema hivi: “Ninafurahia kuja hapa, ninastarehe nikiwa pamoja nanyi.”

Ujenzi huko Newburgh ulipokaribia kumalizika, karibu asilimia 20 ya jengo hilo iliteketezwa kwa moto. Ndugu hawakukata tamaa bali walilirekebisha jengo hilo kwa bidii sana. Kazi hiyo ilimalizika kwa mwezi mmoja hivi, na jumba hilo liliwekwa wakfu Oktoba 19, 2002, siku iliyopangwa awali. Gazeti moja lilisema hivi kuwahusu wale waliojitolea kujenga: “Wana imani yenye nguvu sana hivi kwamba wameushinda moto ulioteketeza asilimia 20 ya jengo hilo la meta 5,600 za mraba.” Kwa sababu wenye mamlaka walitambua umoja kati ya watu wa Mungu, waliwapa ndugu ruhusa ya kuiita barabara inayoelekea kwenye Jumba la Kusanyiko, Mtaa wa Umoja.

Kuweka Wakfu Ofisi za Tawi

Licha ya vita vya wenyewe kwa wenyewe na msukosuko wa kisiasa uliokuwa ukiendelea nchini Côte d’Ivoire, ndugu walikutanika kwa amani huko Abidjan Machi 29, 2003, ili kuweka wakfu majengo mapya ya ofisi ya tawi. Baadhi ya majengo hayo ni Jumba la Ufalme jipya, majengo mawili ya makao, jengo moja lenye chumba cha kulia, jikoni, dobi, vyumba vya kuhifadhia vitu, na karakana mbalimbali. Majengo hayo mapya yako karibu na ofisi ya tawi ambayo ilijengwa ng’ambo ya barabara mwaka wa 1982. Ndugu waliojitolea kutoka nchi 15, ambao wengi wao waligharimia safari yao, waliwasaidia wajenzi wenyeji 110. Sébastien Johnson, mwangalizi wa eneo la dunia aliyetembelea ofisi hiyo ya tawi, alitoa hotuba ya kuweka wakfu yenye kichwa, “Zingatia Ibada Safi.”

Watu 332 walikuwapo ofisi ya tawi mpya ya Guyana ilipowekwa wakfu siku ya Jumamosi, Februari 15, 2003. Richard Kelsey, kutoka ofisi ya tawi ya Ujerumani alitoa hotuba ya kuweka wakfu. Alikazia kwamba Yehova ndiye Mjenzi Stadi wa ulimwengu wote. Hata hivyo, Ndugu Kelsey alionyesha kwamba uumbaji wa Yehova ulio muhimu zaidi ni uumbaji wake wa kwanza, kiumbe mtukufu wa kiroho, yaani, Mwana wake mzaliwa pekee. Mishonari wengi waliotumikia nchini humo zamani walirudi ili kuhudhuria programu ya kuweka wakfu. Baadhi yao walirudi kwa mara ya kwanza tangu waondoke miaka mingi iliyopita! Kuna wahubiri 2,000 hivi tu nchini Guyana, kwa hiyo, wote walifurahi sana kuona kwamba watu 4,752 kutoka nchi 12 walihudhuria programu ya pekee Jumapili.

Katika programu ya kuzindua sehemu mpya ya Betheli huko Haiti, ndugu wa zamani, George Corwin, alisimulia kwa sauti iliyotetema kwa hisia juu ya ziara yake ya hivi majuzi huko St. Marc, mji wenye bandari ulio umbali wa kilometa 60 kaskazini ya Port-au-Prince. Zaidi ya miaka 40 iliyopita, alipokuwa mishonari, alisaidia kuanzisha kutaniko la kwanza mjini humo. Sasa kuna makutaniko manne makubwa katika mji huo. Wanafunzi wake wa Biblia, ambao sasa ni Mashahidi waaminifu wa siku nyingi, walifurahi sana kumkaribisha. Ndugu Corwin alipowasili Haiti, kulikuwa na wahubiri 900 tu nchini humo, na watu wawili tu walifanya kazi katika ofisi ya tawi iliyokuwa nyumba ndogo ya kukodisha.

Ofisi mpya ya tawi ilijengwa nchini Haiti mwaka wa 1986, lakini hiyo pia ikawa ndogo. Ofisi ya tawi iliyopanuliwa na kuwekwa wakfu hivi majuzi ina nafasi ya Wanabetheli 40, wanaowahudumia zaidi ya wahubiri 12,000. Ndugu waliojitolea kutoka Australia, Denmark, Kanada, Marekani, Uingereza, na Ujerumani, walishiriki katika ujenzi huo, nao waliwafundisha ndugu waliojitolea kutoka Haiti kazi ya ujenzi.

Kwa sababu ya upungufu wa vifaa nchini humo, karibu mashine na vifaa vyote vya ujenzi vililetwa kutoka nchi nyingine. Jambo hilo lilichelewesha kazi nyakati nyingine lakini ujenzi haukusimama. Siku ya kuweka wakfu ilikuwa Jumamosi, Novemba 23, 2002. Watu 3,122 walihudhuria, kutia ndani wageni 240 kutoka nchi 13. Ndugu David Splane wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya kuweka wakfu. Siku iliyofuata, zaidi ya watu 20,000 walihudhuria programu ya pekee kwenye Uwanja wa Sylvio Cator huko Port-au-Prince.

“Na twende, tukajenge.” (Neh. 2:18) Maneno hayo yenye kutia moyo ya Wayahudi waaminifu katika siku za Nehemia, yalitajwa katika nyongeza ya Huduma Yetu ya Ufalme ya Juni 2000 huko Hungaria. Watu wa Yehova kutoka sehemu zote za nchi walialikwa kusaidia katika ujenzi wa ofisi ya tawi jijini Budapest. Ndugu 13,741 waliojitolea kutoka makutaniko yote 251 nchini humo, walishiriki katika mradi huo wa miaka miwili uliohusisha kurekebisha jengo ambalo lilikuwa kituo cha jeshi hapo awali. Ofisi hiyo ya tawi iliwekwa wakfu Mei 10, 2003, na wageni 554 kutoka nchi 22 walihudhuria. Ndugu Guy Pierce wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya kuweka wakfu yenye kichwa, “Yehova Anaendelea Kukuza.”

Ofisi ya tawi nchini Mexico imepanuliwa mara kwa mara. Majengo 14 mapya yaliwekwa wakfu Machi 15, 2003, majengo yale mengine yalikuwa yamewekwa wakfu mwaka wa 1974, 1985, na 1989. Kuweka msingi wa meta 80,000 za mraba wa majengo hayo ilikuwa kazi ngumu kwa sababu mbili. Kwanza, uwanja huo una udongo tepetepe kwa sababu sehemu hiyo ilikuwa ziwa zamani. Pili, eneo hilo hukumbwa na matetemeko ya ardhi mara kwa mara. Kwa hiyo, ili majengo yawe na msingi imara, mihimili 3,261 ilipigiliwa ardhini hadi kina cha meta 24! Ilichukua miaka 12 kupanga ujenzi na kujenga, na ndugu 28,600 kutoka Mexico na ndugu 734 kutoka nchi nyingine walijitolea kufanya kazi.

Ndugu watatu wa Baraza Linaloongoza walitoa hotuba wakati majengo hayo yalipowekwa wakfu. Ndugu Guy Pierce alitoa hotuba kuhusu furaha kubwa inayotokana na kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Ndugu Theodore Jaracz alieleza kwamba baraka ambazo Wakristo hupata wanapomtumikia Mungu kwa uaminifu ni nyingi sana kuliko magumu wanayokabili katika siku hizi za mwisho. Ndugu Gerrit Lösch alitoa hotuba ya kuweka wakfu yenye kichwa, “Mwabudu Mungu wa Kweli!” katika Kihispania.

Novemba 23, 2002, ofisi ya tawi nchini Peru iliweka wakfu majengo kadhaa, kama vile jengo jipya maridadi la ofisi na la makao lenye ghorofa tano. Ndugu Gerrit Lösch alitoa hotuba ya kuweka wakfu yenye kichwa, “Upanuzi Humletea Yehova Sifa.” Siku ya Jumapili, watu 59,940 walikusanyika kwenye Uwanja wa San Marcos huko Lima, ambako programu ya pekee ilikazia jinsi ambavyo Yehova amebariki sana kazi ya Ufalme nchini Peru. Baraka hizo zinaonekana wazi sana! Wakati mishonari wa kwanza walipowasili mwaka wa 1946, kulikuwa na wahubiri na watu wanaopendezwa wachache tu nchini humo. Sasa kuna wahubiri 87,318 na makutaniko 916 nchini Peru.

Mei 17, 2003, Wanabetheli 350 na wageni 600 kutoka nchi 30, walikusanyika kwenye ofisi ya tawi ya Urusi, ili kushuhudia kuwekwa wakfu kwa majengo mapya ya makao na ofisi, na mabohari. Ofisi hiyo ya tawi iliwekwa wakfu miaka sita tu iliyopita, kwa nini basi walihitaji kuipanua baada ya muda mfupi tu?

Ofisi ya tawi ya Urusi huko Solnechnoye, karibu tu na St. Petersburg, inasimamia kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme katika nchi kumi. Zaidi ya lugha 100 hutumiwa katika eneo hilo kubwa. Kwa hiyo, kazi ya kutafsiri ni mojawapo ya kazi muhimu katika ofisi hiyo ya tawi, na inazidi kuongezeka. Kwa sasa, magazeti na vitabu vya Biblia hutafsiriwa katika lugha 34 katika ofisi hiyo. Isitoshe, tangu ofisi ya tawi iwekwe wakfu kwa mara ya kwanza, idadi ya wahubiri katika eneo hilo imeongezeka kwa zaidi ya 40,000, ongezeko la wahubiri 7,000 hivi kila mwaka! Ofisi ya tawi inaandika hivi: “Ongezeko hilo linaendelea bila kupungua.” Kwa hiyo, walipoona baraka za Yehova, ndugu huko Urusi walifurahi ‘kurefusha kamba za hema lao.’—Isa. 54:2.

Siku ya Jumamosi, ndugu wengi waaminifu ambao wamevumilia mateso mengi chini ya utawala wa Kikomunisti walihudhuria programu ya kuweka wakfu. Wote walimsikiliza kwa makini Ndugu David Splane alipozungumzia Hagai 2:7 katika hotuba ya kuweka wakfu yenye kichwa, “Nitaijaza Nyumba Hii Utukufu.” Alieleza kwamba ijapokuwa majengo mapya mazuri husifiwa, ni mwenendo na sifa za kimungu za Mkristo mmoja-mmoja ndizo hasa ambazo humletea Yehova utukufu na kurembesha ibada ya kweli. Ijapokuwa kulikuwa na manyunyu na baridi siku ya Jumapili, watu 9,800 walihudhuria programu ya kipekee kwenye Uwanja wa Kirov huko St. Petersburg.

Jumla ya wahudumu 19,848 hutumikia kwenye ofisi za tawi ulimwenguni pote. Wote ni watumishi wa pekee wa Mashahidi wa Yehova wa wakati wote.

[Chati/Picha katika ukurasa wa 12, 13]

BAADHI YA MATUKIO YA MWAKA WA UTUMISHI WA 2003

Septemba 1, 2002

Septemba 1: Makala za Mnara wa Mlinzi zapatikana kwenye video katika Lugha ya Ishara ya Marekani.

Novemba 23: Ofisi ya tawi ya Haiti na Peru zawekwa wakfu.

Januari 1, 2003

Januari 1: Makutaniko yaanza kutumia kitabu kipya cha shule Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.

Februari 15: Ofisi ya tawi ya Guyana yawekwa wakfu.

Machi 15 na 29: Ofisi ya tawi ya Mexico na Côte d’Ivoire zawekwa wakfu.

Aprili 16: Polisi huko Asmara, Eritrea, wawafunga watu 164 wanaohudhuria Ukumbusho.

Mei 1, 2003

Mei 10 na 17: Ofisi ya tawi ya Hungaria na Urusi zawekwa wakfu.

Mei 20: Mashahidi wa Yehova waandikishwa kisheria nchini Kosovo.

Mei 22: Dini ya Mashahidi wa Yehova yaandikishwa kisheria na serikali ya Rumania. Kesi iliyofunguliwa ili kuwapiga marufuku Mashahidi jijini Moscow yaahirishwa hadi wakati usiojulikana.

Agosti: Matbaa mpya aina ya MAN Roland Lithoman yawekwa kwenye ofisi ya tawi ya Uingereza.

Agosti 31, 2003

Agosti 31: Majumba ya Ufalme 7,730 yamejengwa tangu Novemba 1999 katika nchi zinazoendelea. Wahubiri watendaji wafikia 6,429,351 katika nchi 235.

[Picha]

Haiti

Peru

[Grafu katika ukurasa wa 11]

(Ona nakala iliyochapishwa)

Ongezeko la idadi ya lugha:

Vitabu vyote

“Mnara wa Mlinzi”

“Amkeni!”

400

300

200

100

1880 1920 1960 2000

[Picha katika ukurasa wa 14]

Walimu wa Mtaala wa Kuongeza Ujuzi wa Lugha ya Kiingereza, na wake zao

[Picha katika ukurasa wa 22, 23]

Matbaa ya kuchapa ikilinganishwa na basi

Ukubwa wa matbaa ya kuchapa:

Urefu: meta 41

Kimo: meta 5.5

Uzani: tani 201

[Picha katika ukurasa wa 28]

◼ Majengo ya ofisi za tawi yaliyowekwa wakfu hivi karibuni (1) Guyana, (2) Hungaria, na (3) Côte d’Ivoire

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki