Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb05 kur. 6-30
  • Matukio Muhimu Ya Mwaka Uliopita

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Matukio Muhimu Ya Mwaka Uliopita
  • 2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Makusanyiko ya “Tembea Pamoja na Mungu”
  • Vichapo Vipya Vyatolewa
  • Shule ya Waangalizi Wanaosafiri
  • Mambo ya Kisheria
  • Marufuku Huko Moscow na Matokeo Yake
  • Makusanyiko Huko Moscow Yafanywa kwa Amani
  • Kukabiliana na Majaribu Huko Haiti
  • Kujulikana Kuwa Wakristo Ni Ulinzi
  • Kazi ya Uchapaji Yapiga Hatua Huko Marekani
  • Mabadiliko Huko Brooklyn
  • Tayari kwa Ongezeko Ulimwenguni Pote
  • Waenda Ujerumani Kuzoezwa
  • Wanabetheli Watoa Ushahidi Mzuri
  • Ofisi ya Tawi ya India Yawekwa Wakfu
  • Ofisi ya Tawi ya Ufilipino Yawekwa Wakfu
  • Matukio Muhimu Ya Mwaka Uliopita
    2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
    2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
    2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
    2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb05 kur. 6-30

Matukio Muhimu Ya Mwaka Uliopita

WATU wa Mungu wanafurahia nchi ya kiroho inayozidi kuvutia na kusitawi, huku ulimwengu ukikumbwa na misukosuko. (Mal. 3:12, 18) Maendeleo hayo yanatukumbusha ahadi ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake kabla tu hajapaa mbinguni: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mt. 28:20.

Utendaji wa mwaka jana ni uthibitisho mwingine kwamba ahadi ya Yesu yenye kufariji inatimizwa. Kwanza, tuchunguze karamu ya kiroho ambayo watumishi wa Yehova walifurahia kwenye Makusanyiko ya Wilaya ya “Tembea Pamoja na Mungu.”

Makusanyiko ya “Tembea Pamoja na Mungu”

Nabii Mika alionyesha tofauti kati ya mtu mwadilifu na asiye mwadilifu alipotabiri: “Vikundi vyote vya watu vitatembea kila kimoja katika jina la mungu wake; bali sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.” (Mika 4:5) Kama msemaji alivyoeleza katika hotuba ya msingi, maneno hayo yanaonyesha kifupi mtazamo wa watu wa kale, kama vile Enoko na Noa, ambao walitembea pamoja na Mungu nyakati za misukosuko mikubwa. (Mwa. 5:22-24; 6:9, 22) Tuna pendeleo kubwa kuwaiga.

Je, kusanyiko la wilaya liliimarisha azimio lako la kuendelea ‘kutembea katika jina la Yehova’? Kwa nini usipitie mambo uliyoandika kusanyikoni? Jambo hilo litakusaidia kuyakumbuka na kupata faida za kudumu kutokana na programu hiyo.

Vichapo Vipya Vyatolewa

Je, watu wa eneo la kutaniko lako huongea lugha tofauti-tofauti? Basi huenda tayari umetumia kile kijitabu kipya chenye ujumbe katika lugha mbalimbali (Good News for People of All Nations). Kijitabu hicho kinapatikana katika toleo lenye kurasa 32, 64, na 96, na kila toleo lina lugha mbalimbali ambazo zinazungumzwa katika nchi ambayo toleo hilo limekusudiwa kutumiwa. Hivyo, hakikisha kwamba una kifaa hiki kipya kizuri katika mkoba wako wa kuhubiri. Unapokutana na mtu anayeongea lugha usiyoijua, tafadhali fuata hatua tatu zinazoonyeshwa kwenye ukurasa wa 2 wa kijitabu hicho. Huenda uhai ukaokolewa!

Kupatana na andiko la mwaka wa 2004, “Endeleeni kukesha . . . Iweni tayari,” msemaji wa mwisho katika siku ya pili ya kusanyiko alitangaza broshua Endeleeni Kukesha! (Mt. 24:42, 44) Tunatumaini kwamba broshua hiyo itawasaidia wengi watambue uharaka wa nyakati tunamoishi na kufikiri kwa uzito kuhusu wakati ujao na matukio makubwa yatakayotokea. Na kama msemaji alivyosema, broshua hiyo na itusaidie sote kuvumilia mikazo na mahangaiko mengi ya maisha na kubaki imara kiroho tunapokabili majaribu.

Shule ya Waangalizi Wanaosafiri

Miaka sita iliyopita, waangalizi zaidi ya 600 wa mzunguko na wa wilaya kutoka Kanada na Marekani, kutia ndani Alaska na Hawaii, walihudhuria madarasa 13 ya Shule ya Waangalizi Wanaosafiri yaliyofanywa kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, Marekani. Katika mwaka wa utumishi wa 2004, shule hiyo ilifanywa katika ofisi nyingine 87. Kwenye ofisi 23 kati ya hizo, baadhi ya wanafunzi walitoka nchi nyingine. Kwa mfano, ofisi ya Ujerumani iliwaalika ndugu kutoka Austria, Israel, Makedonia, Uswisi, na Uturuki. Ofisi ya Ureno iliwaalika wanafunzi kutoka Luxembourg na visiwa kadhaa, yaani, Azores, Cape Verde, Madeira, São Tomé na Príncipe. Ofisi ya Kenya iliwakaribisha waangalizi wanaosafiri kutoka Ethiopia, Rwanda, Tanzania, Uganda, na nchi nyingine za Afrika.

Katika shule hiyo waangalizi wa mzunguko na wa wilaya hufunzwa mambo yote yanayohusiana na kazi yao. Lengo ni kuwasaidia ndugu hao wenye bidii wawe na matokeo mazuri zaidi wanapotimiza madaraka yao mengi, kutia ndani kufundisha makutanikoni na makusanyikoni na kuongoza katika kazi ya kueneza Injili. (2 Tim. 2:2; 4:5; 1 Pet. 5:2, 3) Shule hiyo pia huwatia moyo wadumishe hali nzuri ya kiroho na kutumia maandiko kwa utambuzi na ufahamu wanapowasaidia wengine.

Shule hii hufanywa kwenye ofisi za tawi, kwa hiyo waangalizi wanaosafiri na wake zao hujionea jinsi maisha ya Betheli yalivyo. Wanafunzi wa darasa fulani waliandika: “Ratiba ya Betheli ilitunufaisha kiroho. Tulifurahia sana ibada ya asubuhi, inayotia ndani kusoma Biblia na Kitabu cha Mwaka. Ingawa tulikuwa na kazi nyingi baada ya darasa, Jumatatu jioni tulihudhuria Funzo la Mnara wa Mlinzi la familia ya Wanabetheli na kunufaika na ushirika wenye kujenga.”

Kwa muda wa saa moja kila siku, baada ya chakula cha mchana, baadhi ya ndugu hufanya kazi kwenye Idara ya Utumishi. Wao hujifunza jinsi ya kushirikiana kikamili zaidi na ofisi ya tawi, jinsi ya kutumia vizuri zaidi mwongozo wanaopokea, na jinsi ya kuandika ripoti zao kwa njia yenye kueleweka na kwa usahihi.

Kila Ijumaa wanafunzi husikiliza hotuba pamoja na wake zao. Hotuba hiyo hukusudiwa hasa kuwatia moyo kiroho dada hao washikamanifu. Kwa mfano, wao hunufaika na vikumbusho vya kuendelea kuweka kielelezo kizuri cha ujitiisho wakiwa wake, na hujifunza kwamba kuhubiri pamoja na dada makutanikoni ni njia moja ya kuwaunga mkono waume zao. Mwangalizi mmoja anayesafiri alilinganisha hotuba hizo za kila juma na “chakula kitamu cha kumalizia mlo.”

Bila shaka, shule hiyo hukazia sana Biblia, hasa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya yenye marejeo (Kiingereza). Mwanafunzi mmoja nchini Ujerumani alisema: “Nimeamua kutumia Biblia hiyo ninapojifunza kibinafsi na kwenye mikutano ya kutaniko. Sasa ninaelewa kabisa ubora wake.” Ndugu mmoja nchini Uingereza ambaye amekuwa mwangalizi anayesafiri kwa muda mrefu alisema kwamba hali yake ya kiroho na uwezo wake wa kufundisha uliboreshwa na jinsi Neno la Mungu lilivyokaziwa. Aliandika: “Nilijifunza kwamba ingawa kutumia mfano mzuri kunafaa katika hotuba, ni muhimu zaidi kusoma na kueleza maandiko.”

Wanafunzi wengi waliandika barua za kushukuru kwa ajili ya shule hiyo. Ndugu mmoja huko Marekani alisema: “Tunamshukuru Yehova sana na tengenezo lake kwa kututia moyo na kutuandaa kwa ajili ya utumishi wetu. Tunatumaini kwamba tutamtumikia Yehova kwa uaminifu zaidi, ufahamu zaidi, na kuwa wenye upendo zaidi tunapowashughulikia kondoo zake wapendwa.” Mwanafunzi mmoja huko Ufaransa aliandika: “Shule hiyo ilinisaidia kuona uhitaji wa kuwashughulikia kwa upendo ndugu na dada zetu Wakristo na kufanya yote tuwezayo kuwasaidia wamtumikie Yehova kwa furaha.” Mwangalizi mmoja anayesafiri nchini Ureno alieleza kifupi maoni ya wengi aliposema: “Shule hiyo ndiyo pindi yenye kuridhisha zaidi katika utumishi wangu wa Kikristo.”

Naye mwalimu mmoja wa shule hiyo alisema: “Ni pendeleo na daraka zito kuwafundisha wanaume ambao baadaye watatoa mwongozo utakaotumiwa na maelfu ya akina ndugu na dada maishani mwao. Tunatumaini kwamba kwa baraka za Yehova, shule hii itakuwa na faida za kudumu.”—Yak. 3:1.

Mwishoni mwa mwaka wa utumishi wa 2004, waangalizi wanaosafiri 1,700 walikuwa wamehudhuria shule hiyo iliyofanywa katika lugha 14. Shule hiyo itafanywa pia katika mwaka wa utumishi wa 2005 kwenye ofisi za tawi mbalimbali.

Mambo ya Kisheria

Mnamo Mei 19, 2004, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu huko Strasbourg, Ufaransa, ilichapisha uamuzi wake kuhusu kesi ya Lotter v. Bulgaria. Ndugu na dada Lotter ambao ni Mashahidi wa Yehova walikuwa wamishonari nchini Bulgaria. Serikali ilitaka kuwafukuza nchini kwa sababu ya imani yao, kwa hiyo wakapeleka kesi kwenye mahakama hiyo. Serikali ilikubali kuwalipa ridhaa na kubadili uamuzi wa kuwanyima kibali cha kuishi Bulgaria. Pia serikali ilikubali kutangaza waziwazi kwamba Mashahidi wa Yehova wanatambuliwa kisheria nchini Bulgaria, ambako dini yao iliandikishwa rasmi mwaka wa 1998.

Mnamo Desemba 16, 2003, mahakama hiyo ilitoa uamuzi uliomwunga mkono Séraphine Palau-Martínez. Kwa kura 6 kwa 1, iliamua kwamba Ufaransa ilikuwa imevunja haki za Dada Palau-Martínez kuhusiana na familia yake. Alikuwa amepeleka kesi kwenye mahakama hiyo aliponyimwa haki ya kuwalea watoto wake wawili kwa sababu mahakama za rufaa za Ufaransa ziliamua kwamba inafaa ‘kuwaepusha watoto hao na kanuni za Mashahidi wa Yehova za kuwalea watoto ambazo ni kali na zenye kukandamiza.’ Katika uamuzi wake, mahakama hiyo ilisema kwamba zile mahakama za rufaa zilitoa uamuzi bila kuzingatia maisha ya watoto hao wala hali njema yao, na kwamba uamuzi huo ulionyesha ubaguzi wa kidini.

Mashahidi wa Yehova nchini Georgia walihudhuria kwa amani Kusanyiko la Wilaya la “Kutembea Pamoja na Mungu,” baada ya kuvumilia kwa miaka mingi mashambulizi ya watu wenye ghasia waliochochewa na wanadini washupavu, ambao baadhi yao wametiwa gerezani. Akina ndugu walifurahia sana kutangazwa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha ya Georgia. Pia, mnamo Novemba 28, 2003, Wizara ya Haki ya Georgia iliandikisha kisheria ofisi ya tawi ya Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania. Hivyo, ingawa mwaka wa 1998 Mahakama Kuu ya Georgia iliamua kupiga marufuku shirika lililotumiwa na Mashahidi wa Yehova, sasa shirika jipya limeandikishwa kisheria na ndugu wanafurahi sana.

Hata hivyo, kuna kesi kadhaa nchini Georgia zinazongojea kuamuliwa na Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu. Lakini, inafurahisha kuona kwamba hali ya ndugu zetu nchini humo inaendelea kuwa nzuri.

Tangu 1990 ndugu nchini Ujerumani wamejaribu bila mafanikio kuandikisha kisheria shirika letu la kidini kupatana na sheria za mashirika ya umma. Mahakama ya Utawala ilipowawekea Mashahidi wa Yehova matakwa makali zaidi kuliko yale ambayo sheria inadai kuhusu uaminifu wao kwa “Kaisari,” Mahakama ya Katiba ilifutilia mbali uamuzi huo kwa kuwa haukupatana na katiba, kisha ikapeleka kesi hiyo mahakamani tena. (Marko 12:17) Mnamo Machi 25, 2004, ile Mahakama ya Utawala ilianza kusikiza kesi hiyo tena. Mahakama hiyo iliomba ufafanuzi zaidi juu ya msimamo wetu kuhusu damu, kulea watoto, kutenga na ushirika, na kutounga mkono siasa na vita. Hakimu aliyeongoza kesi hiyo alisema kwamba upande wa serikali unapaswa kuwa na ushahidi wenye kutegemeka, yaani, takwimu na hati rasmi, wala si manukuu yasiyoweza kuthibitishwa kutoka vituo vya Intaneti na barua za watu wanaotaka kulipiza kisasi.

Fomu moja inayotumiwa nchini Ugiriki kuhesabu watu wanaoandikishwa jeshini ilikuwa na majina yenye kuwavunjia heshima Mashahidi wa Yehova kwenye sehemu ambapo mtu anapaswa kuonyesha dini yake. Kwa hiyo, ofisi ya tawi nchini Ugiriki ikapeleka malalamiko kwenye Wizara ya Ulinzi. Mnamo Machi 24, 2004, wizara hiyo iliwaandikia Mashahidi wa Yehova na kusema kwamba haikuwa na nia ya kuwaudhi na kwamba “tayari ilikuwa imebadili majina hayo.” Fomu iliyorekebishwa inatumia jina, “Mashahidi Wakristo wa Yehova.”

Peru imeitambua kisheria dini ya Mashahidi wa Yehova kwa miaka mingi. Hata hivyo, mnamo Novemba 1997 Wizara ya Elimu ilianza kukataa maombi yetu ya kusamehewa kodi kuhusiana na vichapo vyetu na badala yake kudai pesa nyingi sana kabla ya kuviachilia kutoka katika ofisi ya forodha. Kesi hiyo ilipelekwa mahakamani. Mnamo Desemba 11, 2003, hakimu alitoa uamuzi uliowaunga mkono Mashahidi wa Yehova. Alisema kwamba hatua ya wizara hiyo ilikuwa ya “kigeu-geu, ya upuuzi, na isiyoeleweka.” Alisema mwenendo wa maofisa wa wizara hiyo ulikuwa “wenye ubaguzi [na] wenye kuudhi.” Matatizo ya kuingiza vichapo nchini yakaisha papo hapo.

Puerto Riko, nchi inayojitawala kwa muungano na Marekani, ina sheria inayoruhusu mitaa inayoishi watu iwe na malango, kuta, na walinzi wa kuzuia watu wasiingie ndani. Vizuizi hivyo hufanya iwe vigumu kuhubiri kwenye mitaa hiyo. Polisi hata wamewafukuza wahubiri katika baadhi ya mitaa hiyo. Jitihada za kusuluhisha jambo hilo nje ya mahakama zimeshindwa. Sasa kesi ya kuomba sheria hiyo itangazwe kuwa kinyume cha katiba na yenye kuwanyima watu uhuru wa kuabudu na wa kusema imepelekwa katika mahakama fulani inayoshughulikia hali kama hizo nchini Puerto Riko. Uamuzi haujatolewa bado.

Mnamo Oktoba 28, 2003, Mahakama ya Rufaa ya Bucharest ilitoa Uamuzi Na. 1756, ulioilazimisha serikali ya Rumania kuorodhesha Mashahidi wa Yehova kati ya dini zinazosamehewa kodi. Mnamo Februari 6, 2004, Gazeti la Serikali Na. 112 lilichapisha orodha ya “dini zinazotambuliwa kisheria nchini Rumania.” Mashahidi wa Yehova walikuwa kwenye orodha hiyo.

Mnamo Machi 21, 2004, Mahakama ya Wilaya ya Seoul katika Jamhuri ya Korea iliwaondolea mashtaka ya uhalifu ndugu watatu waliokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya imani yao. Hii ni mara ya kwanza kwa mahakama ya nchi hiyo kutambua haki ya raia ya kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri zao. Sasa mamia ya ndugu zetu nchini Korea wamefungwa eti kwa sababu ya “uhalifu” wa ‘kufua panga zao ziwe majembe.’ (Isa. 2:4) Kwa kusikitisha, mahakama kuu na mahakama ya katiba zilikataa kuwasaidia ndugu zetu kupatana na katiba ya Korea inayotetea uhuru wa ibada. Hata hivyo, hivi karibuni bunge la Korea liliwasilisha mswada wa kuanzisha utumishi wa kiraia kwa ajili ya wote ambao wamefikia umri wa kujiunga na jeshi.—Met. 21:1.

Uamuzi wa Mahakama Kuu ya Marekani katika kesi ya Watchtower . . . v. Village of Stratton unaendelea kuwanufaisha Mashahidi wa Yehova katika huduma yao ya nyumba kwa nyumba. Kwa mfano, kwenye eneo moja katika jimbo la New York, Marekani, polisi waliendelea kusisitiza Mashahidi wawe na kibali kabla ya kuhubiri kwenye eneo hilo. Hata hivyo, mkuu wa polisi aliandika hivi baada ya kujulishwa jambo hilo na uamuzi huo wa mahakama: “Ninaona aibu kuhusiana na vitendo vya maofisa wangu katika kisa hiki na ninaomba msamaha kwa matatizo yoyote ambayo huenda hali hiyo ilisababisha.”

Watu fulani katika jimbo la Illinois waliagiza idara yao ya polisi wawaeleze polisi wanaoshika doria, maofisa, na wafanyakazi wengine kwamba kupatana na uamuzi wa Mahakama Kuu ya Marekani, “Mashahidi wa Yehova hawahitaji kuwa na kibali wanapohubiri nyumba kwa nyumba.” Waliongeza: “Hawahitaji kutujulisha wanapokuja kuhubiri.”

Mnamo Oktoba 8, 2003, Mahakama Kuu ya Iowa ilitoa uamuzi uliomwunga mkono Lester Campbell katika kesi aliyopeleka mahakamani kwa sababu ya kutiwa damu bila kibali chake. Ndugu Campbell alipeleka kesi hiyo mahakamani ili alipwe ridhaa kwa sababu ya kutiwa damu yake mwenyewe baada ya upasuaji ingawa alikuwa ametoa maagizo kwa kuandika na pia kwa mdomo ya kukataa matibabu hayo. Uamuzi wa mahakama ya kwanza uliunga mkono daktari na hospitali. Hata hivyo, Mahakama Kuu ya Iowa iliubatilisha, na kuamua kwamba Lester Campbell hakuhitaji kusaidiwa na mtaalamu wa kitiba kujua kwamba kutiwa damu bila kibali chake hakufai. Pia iliamua kwamba anaweza kudai ridhaa.

Marufuku Huko Moscow na Matokeo Yake

Mnamo Machi 26, 2004, Mahakama ya Manispaa ya Wilaya ya Golovinsky huko Urusi iliamua kupiga marufuku kazi ya Mashahidi wa Yehova jijini Moscow na kufutilia mbali shirika lao. Rufani ilikatwa, na mnamo Juni 16, 2004, mahakama ya rufaa ya Moscow ikaunga mkono uamuzi wa mahakama ya manispaa, na sheria ya marufuku na kufutiliwa mbali kwa shirika la Mashahidi yakatekelezwa. Akina ndugu wamekata rufani kwenye Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu na wanatumaini kwamba kesi yao itasikizwa mapema kwa sababu marufuku hiyo inasababisha matatizo mengi.

Hata hivyo, marufuku hiyo haikuwavunja moyo akina ndugu. Hata imewachochea ndugu wengi wamtumikie Yehova kwa bidii zaidi. Bidii yao inatukumbusha maneno ya mtume Paulo alipokuwa kifungoni Roma. Aliandika: “Mambo yangu yamegeuka na kuwa yenye kuendeleza mbele habari njema.”—Flp. 1:12.

Kwa mfano, Machi 2004, Urusi ilikuwa na kilele kipya cha wahubiri 136,034 na mafunzo ya Biblia 136,903. Hiyo ni mara ya kwanza katika muda wa miaka saba kwa idadi ya wanafunzi kupita ile ya wahubiri! Na kuanzia Machi hadi Juni, ofisi ya tawi ilipokea maombi 1,000 ya upainia wa kawaida, na katika mwezi wa Aprili kukawa na kilele kipya kabisa cha mapainia wa kawaida 15,489. Ofisi hiyo inasema: “Vivyo hivyo, uamuzi uliotolewa Juni 16 uliwachochea akina ndugu waongeze utendaji wao.” Pia uliwachochea wengine, kutia ndani waume wasioamini, waanze kuhudhuria mikutano ya Kikristo.

Mwanafunzi fulani wa chuo kikuu kutoka Marekani alikuwa Urusi wakati uamuzi huo ulipotolewa mwezi wa Juni. Ofisi ya tawi inaandika: “Alifunga safari ya kwenda kutembelea Betheli, karibu na jiji la St. Petersburg, ili kupata habari zaidi kuhusu hali hiyo. Alivutiwa sana na usafi kwenye majengo hayo na jinsi alivyokaribishwa.” Alishangaa ni kwa nini Mashahidi wa Yehova walipigwa marufuku na akaomba vichapo na video ili aende kuwaonyesha maprofesa kwenye idara yake ya masomo ya kidini huko California.

Makusanyiko Huko Moscow Yafanywa kwa Amani

Kuanzia Juni 11 hadi 13, punde tu kabla ya mahakama ya rufaa kutoa uamuzi wake usiofaa, Makusanyiko ya “Tembea Pamoja na Mungu” yalifanywa jijini Moscow, moja likiwa katika Lugha ya Ishara ya Urusi. Mwanzoni, makusanyiko hayo yalikuwa yafanywe baada ya kusikizwa kwa kesi hiyo, lakini Halmashauri ya Tawi ilifanikiwa kuomba iahirishwe. Ndugu wanasema makusanyiko hayo yalifanywa bila tatizo nao wakuu wa jiji walishirikiana nao. Polisi waliokuwa kwenye malango ya kuingia uwanjani waliambiwa hivi na wakubwa wao: “Mnapowaruhusu watu kuingia uwanjani, msivute sigara wala kutumia lugha chafu.”

Kwenye gari-moshi la chini ya ardhi jijini Moscow, mtu mmoja aliwashutumu dada kadhaa kwa uwongo kwamba waliiba pesa zake. Aliwashurutisha waende naye kwenye kituo cha polisi. Huko aliwashtaki dada hao na pia wafuasi wote wa “madhehebu” ya Mashahidi kwa kusababisha msongamano wa magari kimakusudi ili wawaibie watu. Polisi aliwageukia dada hao na kuwauliza, “Ninyi ni akina nani?”

“Sisi ni Mashahidi wa Yehova na tunaenda kusanyikoni,” wakajibu huku wakionyesha beji za kusanyiko.

Ndipo polisi huyo akamwambia yule mtu: “Mashahidi wa Yehova hawaibi. Lazima uwaombe msamaha kwa kuwatusi.” Halafu akawageukia dada hao na kuwaambia, “Fanyeni haraka mwende kwenye kusanyiko lenu.” Kisha akamwambia mtu huyo, “Lakini wewe kaa hapa. Nataka tuendelee na mazungumzo.”

Watu 21,291 walihudhuria kusanyiko hilo lililofanywa kwenye uwanja wa michezo, na 497 wakabatizwa. Watu 929 walihudhuria kusanyiko la lugha ya ishara kwenye Jumba moja la Ufalme na 19 wakabatizwa.

Kukabiliana na Majaribu Huko Haiti

Mwaka wa 2004 kulikuwa na msukosuko wa kisiasa, jeuri, ukosefu wa bidhaa muhimu, na kupanda kwa bei kisiwani Haiti. Mbali na shida hizo, watu zaidi ya 1,500 walikufa katika mafuriko mabaya mwezi wa Mei na kuwaacha maelfu bila makao. Hakuna Shahidi aliyekufa, lakini baadhi yao walipoteza kila kitu, hata nyumba zao.

Hata hivyo, ndugu waliimarishwa walipotambua waziwazi kwamba Yehova alikuwa akiwasaidia na kuwaongoza, na kwamba Baraza Linaloongoza pamoja na ndugu zao ulimwenguni waliwahangaikia kwa upendo. Upendo huo ulionyeshwa kwa kutoa misaada kwa ajili ya ndugu waliopatwa na msiba. Ndugu wenyeji pia walisaidiana kupata chakula na mahitaji mengine.

Ofisi ya tawi ya Haiti ilifuatilia kwa makini hali hiyo ili iweze kutoa mwongozo kwa makutaniko. Kwa mfano, jeuri ilipoongezeka katika mji mkuu, Port-au-Prince, Halmashauri ya Tawi iliwashauri wazee wafanye mipango ili mikutano iliyokuwa ifanywe Jumapili, Februari 29, ifanywe siku moja mapema. Shauri hilo lilikuwa la hekima kwa sababu siku ya Jumapili, rais wa Haiti aliyekuwa taabani alijiuzulu na kukimbilia uhamishoni. Taarifa moja ya habari ilisema: “Milio ya bunduki iliendelea kusikika kote jijini huku jiji likikumbwa na ghasia nyingi.” Ofisi ya tawi inaandika: “Hakuna aliyetarajia mambo hayo yatukie. Haingewezekana kufika kwenye mikutano siku hiyo ya Jumapili. Tunamshukuru Yehova kwa kuwalinda ndugu zetu.”

Wakati huo wa msukosuko na hatari, polisi na jeshi la waasi na pia wanyang’anyi waliweka vizuizi barabarani, nayo serikali ikatoa amri ya kutotembea usiku. Lakini hata kabla ya amri hiyo kutolewa, makutaniko yalikuwa yamebadili wakati wa mikutano ili wote waweze kurudi nyumbani salama kabla ya giza kuingia. Makutaniko mengi yaliripoti ongezeko la wahudhuriaji kwenye mikutano!

Pia, ndugu waliendelea kuhubiri kwa bidii, jambo lililowavutia majirani. Baadhi yao walisema, “Inatia moyo kuona kwamba ninyi Mashahidi mnaendelea kuhubiri kama kawaida.” Bila shaka, wahubiri hao walikuwa waangalifu sana na walipashana habari kuhusu maeneo yaliyokuwa salama.

Kujulikana Kuwa Wakristo Ni Ulinzi

Ofisi ya tawi ya Haiti inaandika: “Wengi wa ndugu zetu hawakupigwa wala kunyang’anywa vitu kwa sababu majirani wao wanawafahamu vizuri na wanajua hawajiingizi katika siasa.” Kwa mfano, kwenye vizuizi vitatu vya barabara, magenge ya wahuni wenye silaha yaliwasimamisha wenzi wa ndoa wamishonari. Wenzi hao walifanya mambo mawili: Walijitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova na kusali kimyakimya na kwa sauti. Kwenye vizuizi vyote vitatu mtu aliwatetea, akisema kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu wazuri wasiojiingiza katika siasa. Wenzi hao walifika nyumbani salama.

Magenge yenye silaha pia yaliwasimamisha Wanabetheli fulani. Kama wale wamishonari, ndugu hao walijitambulisha kuwa Mashahidi na kusali, na matokeo yakawa yaleyale. Katika kisa kimoja mnyang’anyi aliwaambia: “Nendeni kwa amani na mtuombee!” Kwenye kizuizi kimoja cha barabara, Mwanabetheli mwingine alisimamishwa na polisi waliotaka kutafuta silaha katika gari lake. Ndugu huyo aliwaambia: “Silaha ambazo niko nazo ni Biblia na magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!” Polisi hao walitabasamu na kumpungia mkono apite. Baadaye, walilitambua gari lake kutoka mbali nao wakamruhusu apite bila kumwuliza chochote.

Ofisi ya tawi ilisema kwamba mambo yalitulia kidogo katika miezi iliyofuata. Lakini bado kulikuwa na matatizo na hali ya wasiwasi. Hivyo akina ndugu waliendelea kujihadhari.

Kazi ya Uchapaji Yapiga Hatua Huko Marekani

Katika mwaka wa 2002, Baraza Linaloongoza liliidhinisha mpango mpya wa kuwa na maeneo matano ya uchapaji, yaani, Afrika, Amerika Kaskazini, Amerika Kusini, Asia, na Ulaya, ambayo yatahudumia nchi zilizo katika maeneo hayo. Kwa sababu hiyo, nafasi zilizopo kwenye ofisi mbalimbali za tawi zinatumiwa kwa njia nzuri zaidi, kutia ndani ofisi ya Marekani, ambapo sasa kazi imepungua.

Mwaka wa 2004, idara ya uchapaji, ujalidi, na usafirishaji nchini Marekani zilihamishwa hadi Wallkill, New York. Mnamo Agosti 6, 2002, baraza la ujenzi la mji lilielezwa kuhusu mpango wa ujenzi na kusudi la ujenzi huo. Kisha baada ya mpango huo kusikizwa hadharani mnamo Septemba 3, baraza hilo likatoa kibali. Kwenye mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, Oktoba 5, 2002, ilitangazwa kwamba Baraza Linaloongoza limeidhinisha ujenzi huo. Matbaa mbili mpya (aina ya MAN Roland Lithoman) ziliagizwa, na jengo ambalo matbaa hizo zingewekwa lilitarajiwa kukamilishwa mnamo Februari 2004.

Je, ujenzi huo mkubwa ungeisha kwa miezi 14 tu? Ndugu walimtegemea Yehova awaongoze na awachochee watu wajitoe kwa hiari. Naye akafanya hivyo. Ujenzi huo wa jengo la kuchapia ulianza Februari 2003 na kuisha Septemba. Matbaa ya kwanza kati ya zile tatu huko Wallkill ilipelekwa kwenye jengo jipya mwezi wa Desemba. Matbaa mpya mbili zililetwa Aprili na Mei 2004 na kuanza kufanya kazi Juni na Julai. Mnamo Septemba matbaa zote tano zilikuwa zinafanya kazi.

Awali, mitambo ya kujalidi ilihitaji orofa kumi na moja katika majengo matatu ya Adams Street huko Brooklyn. Sasa mitambo yote iko katika jengo moja huko Wallkill na nafasi inayohitajika imepungua kwa asilimia 58. Vitabu vilianza kujalidiwa kwa kutumia jalada nyepesi mnamo Julai 2004. Baadaye mwezi huo, vitabu vya kwanza vyenye jalada gumu vilijalidiwa kwa kutumia mashine mpya 33 zilizounganishwa kwa kanda 70. Mfumo huo wa kanda na mashine una urefu wa meta 400. Hakuna mtu anayehitajika baada ya visehemu vya vitabu hivyo kuwekwa kwenye mfumo huo. Vitabu 120 vyenye jalada gumu hujalidiwa kwa dakika moja, na kazi hiyo hufanywa na watu 25 tu. Wafanyakazi katika idara hiyo wamepungua kwa asilimia 66. Mashine zote za kujalidi zilianza kufanya kazi Oktoba 2004.

Kuanzia Novemba 2004, Idara mpya ya Upakizi na Usafirishaji huko Wallkill, imekuwa ikipakia vichapo vilivyoagizwa na makutaniko kwa kutumia mfumo mpya wa mashine unaoendeshwa kwa kompyuta. Nafasi inayohitajiwa kuweka mfumo huo imepungua kwa asilimia 45 ikilinganishwa na ile iliyohitajika Brooklyn. Kompyuta hukadiria idadi ya vichapo vilivyoagizwa na kuchagua katoni zinazofaa. Ukanda wa kusafirishia wenye urefu wa meta 800 hupeleka vichapo hivyo kwenye jukwaa maalumu ambapo hupangwa ili viwe tayari kusafirishwa. Makutaniko ya karibu yanaweza kuchukua vichapo hapo bila kuingia ndani.

Tunawashukuru sana ndugu na dada wote waliosaidia katika ujenzi huo. Ndugu waliosaidia ni Wanabetheli na ndugu waliojitolea kufanya kazi kwa muda, ndugu kutoka majimbo matano waliofanya kazi chini ya Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa, na ndugu ambao kwa ukarimu walichanga baadhi ya vifaa vya biashara zao. Tunawashukuru pia ‘watoaji wengi wachangamfu’ waliosaidia kwa kuchanga pesa.—2 Kor. 9:7, 11.

Mabadiliko Huko Brooklyn

Mambo yamebadilika katika Betheli ya Brooklyn baada ya kuhamishwa kwa idara ya uchapaji, ujalidi, na usafirishaji. Aprili 29, 2004 ilikuwa pindi muhimu na yenye kugusa hisia. Jioni hiyo, ndugu walishangilia na kutoa machozi, wakati Max Larson, ambaye amesimamia idara ya uchapaji kwa zaidi ya miaka 60, alipofunga matbaa ya mwisho huko Brooklyn na kukomesha kazi ya uchapaji iliyokuwa imeendelea mfululizo kwa miaka 84. Idara ya ujalidi ilifungwa majuma kadhaa baadaye.

Mnamo Juni 2003, ndugu wa Baraza Linaloongoza walitangaza kwamba huenda jengo namba 360 kwenye Furman Street huko Brooklyn likauzwa kwa kuwa walijua kwamba baada ya mabadiliko hayo jengo hilo halingehitajika tena. Mkataba wa kuliuza ulikamilika Ijumaa, Juni 18, 2004. Hatimaye, dobi, ofisi, na karakana zote zilizokuwa katika jengo hilo lenye ukubwa wa meta 93,000 za mraba zitawekwa katika majengo namba 117 kwenye Adams Street, yaliyoachwa tupu.

Isitoshe, jengo namba 107 kwenye barabara ya Columbia Heights sasa linafanyiwa marekebisho makubwa. Vyumba vya kulala vinatarajiwa kukamilishwa mwishoni mwa mwaka wa 2005, na jengo lote litakuwa limekamilishwa Septemba 2006. Jengo lililorekebishwa litatoshea Wanabetheli 300 na litakuwa na duka, Jumba la Ufalme, maktaba, sebule, ofisi, dobi, na bustani mpya.

Tayari kwa Ongezeko Ulimwenguni Pote

Nchi nyingine ambazo zimepokea matbaa mpya aina ya MAN Roland Lithoman ni Afrika Kusini, Brazili, Japani, Mexico, na Uingereza. Ofisi ya Uingereza ndiyo ya kwanza kuweka matbaa hiyo mpya, ambayo ilifika Julai 2003 na kuanza kufanya kazi Oktoba. Matbaa hiyo huchapa magazeti 750,000 kwa siku, au milioni 1.5, ndugu wakifanya kazi kwa zamu mbili. Idadi hiyo ni mara tatu zaidi ya ile ambayo matbaa ya zamani ilichapa.

Matbaa hiyo mpya inaweza pia kuchapa visehemu vya Biblia na vitabu. Kwa mfano, ofisi ya tawi ya Afrika Kusini tayari imechapa visehemu vya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kisesotho, lugha moja ya Afrika Kusini. Ofisi ya tawi ya Japani inasema kwamba awali ilichukua siku nzima kurekebisha mashine iliyokuwa ikichapa vitabu vidogo ili iweze kuchapa vitabu vikubwa. Sasa inachukua muda wa saa moja tu. Awali ilichukua siku kumi kuchapa trakti milioni moja lakini sasa inachukua muda wa saa tano tu. Katika miezi mitatu ya kwanza, matbaa ya Japani ilichapa trakti milioni 12; magazeti na broshua milioni 12; vitabu 240,000; na Biblia 48,000.

Mashine nyingine mpya zinazotumia kompyuta hukata, huhesabu, hupanga, huweka vibandiko, na kufunga vichapo. Mabamba ya kuchapia yanatengenezwa vizuri zaidi kwa kutumia kompyuta. Mbinu hiyo imerahisisha kazi ya uchapaji kwa kuwa filamu ya kupigia picha haihitajiki. Ofisi ya Uingereza inasema kwamba maendeleo hayo yote yameiwezesha kuchapa vitabu vingi zaidi na pia kupunguza wafanyakazi.

Waenda Ujerumani Kuzoezwa

Ndugu kutoka ofisi za tawi sita walienda kwenye kampuni ya MAN Roland huko Ujerumani ili wazoezwe kutumia matbaa aina ya MAN. Kwa kuwa walimu wao walikuwa wamewazoeza wachapaji wasio Mashahidi, walitazamia ndugu hao wajiendeshe kana kwamba wako likizoni. Kwa hiyo, walimu hao walishangaa na kuvutiwa na bidii ya ndugu zetu. Ndugu hao hata waliomba waanze mazoezi hayo mapema na kuendelea hadi usiku ili wanufaike kikamili.

Baadhi ya ndugu walikuwa na tatizo la lugha kwa sababu mafundisho na vitabu vya maagizo vilikuwa katika lugha ya Kiingereza. Kwa kufikiria kimbele, ndugu wa Japani walijitahidi sana kuboresha Kiingereza chao kabla ya kwenda Ujerumani. Wengi wao hata walijiunga na makutaniko ya Kiingereza kwa muda.

Wanabetheli Watoa Ushahidi Mzuri

Baadaye, matbaa zilipofika kwenye ofisi za tawi, mainjinia kutoka kampuni ya MAN waliziunganisha wakisaidiwa na Wanabetheli. Katika ofisi zote sita, mazingira ya Betheli yenye furaha na yenye kujenga yaliwavutia wafanyakazi hao ambao si Mashahidi. Fundi aliyekuwa akiweka matbaa huko London aliwaambia ndugu hivi: “Nilirudi nyumbani jana jioni na kumwona jirani yangu kwenye bustani yake. Sijawahi kuvutiwa naye, lakini baada ya kuongea naye kwa dakika 20, niligundua kwamba jamaa huyo ni mzuri sana.” Fundi huyo aliongeza kwamba mke wake aliona mabadiliko katika mtazamo na tabia yake, naye akamwambia: “Umekuwa mwenye urafiki, unatabasamu, na kuwasalimu watu.”

“Nimefanya kazi pamoja na Mashahidi kwa majuma sita,” akajibu. “Na katika majuma mawili yaliyopita sikutumia matusi hata kidogo. Ninatumaini sitayatumia tena.”

Baada ya matbaa hizo kuwekwa kwenye ofisi ya London, meneja mmoja wa kampuni ya MAN alipigia ofisi hiyo simu na kuwashukuru akina ndugu kwa kuwatunza wafanyakazi wa kampuni hiyo vizuri. Alisema matbaa hizo ziliwekwa bila matatizo.

Ofisi kadhaa za tawi zilipanga kuwe na chumba cha kulia mahali pa ujenzi kwa ajili ya wale waliokuwa wakiweka matbaa hizo mpya. Wakati wa chakula cha mchana, mafundi wengi, hasa wale ambao si Mashahidi, walifurahia kuhudumiwa na wahudumu waliovalia vizuri. Fundi mmoja nchini Japani hakuwa amewahi kuona jengo la kuchapia safi na lenye utaratibu kama lile la ofisi ya tawi. Alisema, “Hapo ndipo mahali pazuri zaidi pa kufanyia kazi.” Pia alivutiwa na unyoofu wa akina ndugu. Hakuna mahali pengine anapoweza kuacha vifaa vyake bila kuangaliwa na kuwa na uhakika kwamba havitaibwa. Alitaka kujua mengi kuwahusu Mashahidi wa Yehova, hivyo akachukua vichapo kadhaa na akatembezwa kwenye ofisi hiyo.

Ndugu nchini Mexico waliwaalika mafundi wa kampuni ya MAN kwenye Ukumbusho. Wanne walikubali kuhudhuria, lakini hawakuwa na mavazi yanayofaa. Hivyo, Mwanabetheli fulani akawapeleka madukani kwa sababu walitaka kununua suti. Ndugu waliwapa Biblia na wakati wa hotuba ya Ukumbusho wakawasaidia kufungua maandiko. Baada ya mkutano, mafundi hao walipiga picha na kutabasamu sana hivi kwamba wengi kutanikoni walifikiri wao ni Wanabetheli kutoka Ujerumani.

Kwenye ofisi zote za tawi, wenye makampuni ya ujenzi na wale walioleta bidhaa pia walipata ushahidi mzuri. Mtu mmoja mwenye kampuni ya ujenzi huko Marekani aliandika: “Nimevutiwa sana na ubora wa tengenezo lenu na hasa watu wake. Sijawahi kufurahia kazi ya ujenzi kama nilivyoifurahia huko kwenu. Tengenezo lenu linanipa tumaini kwamba wanadamu wanaweza kuwa na wakati ujao mzuri. Kama kuwajali wengine na shauku zingeweza kutiwa ndani ya chupa na kuuzwa, bila shaka watu wenu wangekuwa na bidhaa ambayo kila mtu angetaka kununua.”

Huko Mexico mtu aliyeleta vifereji vya kuwekwa kwenye matbaa mpya alishangazwa na utulivu alioona kwenye ofisi ya tawi. Aliuliza maswali mengi, na sasa yeye na familia yake wanajifunza Biblia na wanafanya maendeleo. Msimamizi wa wajenzi fulani wenyeji aliomba jambo lisilo la kawaida. Alisema: “Kwa kawaida watu hutupa bakshishi ili kutushukuru kwa kazi yetu. Mwaonaje mkitupa sisi sote Biblia badala ya bakshishi? Kutokana na mambo niliyoona hapa, ninafikiri kwamba kuijua Biblia ni muhimu zaidi kuliko pesa.”

Ofisi ya Tawi ya India Yawekwa Wakfu

Ofisi ya tawi ya India inaandika: “Hatimaye siku iliyongojewa kwa muda mrefu ilifika Desemba 7, 2003. Hiyo ilikuwa siku ya kuwekwa wakfu kwa ofisi yetu iliyojengwa karibuni huko Bangalore. Jiji hilo liko kwenye eneo la katikati, kusini mwa India.”

Ofisi hiyo yenye ukubwa wa meta 30,000 za mraba, iliyojengwa kwenye kiwanja chenye ukubwa wa ekari 43, ni kama mji mdogo. Hiyo ni ofisi ya tawi ya kwanza ulimwenguni kujengwa na kampuni ya ujenzi, nayo ina mtambo wa kusafishia maji ya kunywa, mtambo wa kusafishia maji machafu, na wa umeme. Majengo hayo yana ofisi 122, kutia ndani 80 za watafsiri; Jumba zuri la Ufalme; na jengo kubwa la kuchapia. Kuna majengo matatu ya makao yenye vyumba vizuri, dobi, chumba cha kulia, na jiko lenye vifaa vyote vinavyohitajika. Vifaa vingi vilivyotumiwa kujenga ofisi hiyo vilinunuliwa nchini humo, nayo ilijengwa kwa miaka miwili.

Kazi ya Ufalme ilianzishwa India mwaka wa 1905. Sasa vitabu hutafsiriwa na kuchapwa katika lugha 26 za India. Wakati wa kuwekwa wakfu kwa ofisi hiyo, wamishonari wengi waliokuwa wametumika India kwa miaka mingi walisimulia mambo mengi yaliyoonwa yenye kutia moyo. Hotuba ya kuweka wakfu ilitolewa na Stephen Lett wa Baraza Linaloongoza, na watu 2,933 waliisikiliza, wakiwemo wageni 150 kutoka nchi 25.

Ofisi ya Tawi ya Ufilipino Yawekwa Wakfu

“Tunataka kazi yetu ya ujenzi iwe nzuri kama ya Watch Tower!” Hivyo ndivyo wajenzi fulani ambao si Mashahidi walivyosema huko Manila baada ya kuona jinsi ofisi ya tawi ya Ufilipino ilivyojengwa kwa ustadi. Wapiga picha wa televisheni waliokuwa wakitayarisha kipindi fulani kuhusu sheria za ujenzi walimtembelea injinia mmoja wa jiji, naye akawaambia hivi: “Ikiwa mnataka kuwaona watu wanaofuata sheria za ujenzi kwa makini, nendeni kwenye Watch Tower.”

Mbali na jengo jipya la makao lenye orofa kumi, ndugu walijenga nyumba nyingine za ziada na kurekebisha jengo la makao lenye orofa kumi lililojengwa mwaka wa 1991. Kwa nini upanuzi huo ulihitajiwa? Kuanzia mwaka wa 1991 hadi 2003 idadi ya wahubiri iliongezeka kwa wahubiri 34,000 na kukawa na kilele kipya cha wahubiri wa Ufalme zaidi ya 144,000!

Ofisi hiyo iliwekwa wakfu Novemba 1, 2003. Wanabetheli, wamishonari waliokuwa huko zamani, wageni kutoka nchi 13, na ndugu na dada wenyeji zaidi ya 2,000 walihudhuria Jumamosi asubuhi. Wote walikuwa 2,540. Stephen Lett alitoa hotuba yenye kichwa, “Kuthamini Nyumba za Ibada za Yehova za Kale na za Wakati Huu.” Siku iliyofuata, mapainia na wazee wa makutaniko pamoja na wake zao walifurahia programu ya pekee kwenye Jumba la Kusanyiko la Metro Manila. Wote walikuwa 8,151.

Wahudumu waliowekwa rasmi 20,092 hufanya kazi kwenye ofisi za tawi ulimwenguni pote. Wote ni washiriki wa Kikundi cha Ulimwenguni Pote cha Watumishi wa Pekee wa Wakati Wote cha Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 21, 22]

Atekwa Nyara Mchana

Ijumaa saa sita, Machi 19, 2004, Carl, Shahidi mwenye umri wa miaka 20, alikuwa akitembea kwenye barabara yenye watu wengi huko Pétionville, nchini Haiti. Kwa ghafula, wanaume wenye silaha waliovalia mavazi meusi wakamlazimisha kupanda kwenye gari lililokuwa wazi nyuma, wakamfunika kichwa, na kuondoka kwa mwendo wa kasi. Carl anaeleza:

Baada ya kushuka kutoka katika gari hilo, nilipelekwa katika chumba ambapo mateka wengine walikuwa. Yaelekea mateka hao walikuwa wanafunzi wa chuo kikuu walioshutumiwa kwa kushiriki katika maandamano ya kisiasa. Watekaji nyara hao walizidi kuwa wajeuri, wakafyatua risasi kiholela na kumwua mmoja wa mateka. Alipoanguka kichwa chake kilinigusa miguu. Kisha wakaanza kunihoji na kunitisha. Walikasirika na baada ya kunipiga wakanitupa juu ya ile maiti.

“Jibu maswali yetu!” kiongozi wao akaniamuru.

“Mimi sijui chochote kuhusu siasa,” nikajibu.

“Basi, nitakuua sasa hivi!” akasema kwa sauti kubwa.

Ndipo nikamsihi hivi: “Kabla hujaniua, tafadhali niruhusu nimwombe Yehova Mungu wangu awasaidie wazazi na ndugu zangu, kwa kuwa hawataniona tena.”

“Harakisha! Niko na haraka,” akasema kwa ukali.

Nilipokuwa nikisali kwa sauti, mtu huyo aliondoka. Aliporudi, nikawaza, ‘Carl wakati wako umefika. Uwe tayari kufa.’ Hata hivyo, jambo lililotokea lilinishangaza sana.

Mwanamume huyo aliniuliza: “Je, wewe ni Carl . . . ?” kisha akataja majina yangu yote.

“Ndiyo,” nikajibu huku nikishangaa jinsi alivyopata kujua majina yangu.

Alinieleza kwamba nilikuwa nimembeba kwa gari langu mara kadhaa, na kwa kuwa amenitambua, hawezi kuniua. Kwa kuwa kichwa changu kilikuwa kimefunikwa, yaelekea alinitambua kwa sababu ya mambo niliyosema katika sala. Alitoka nje tena na kuzungumza na wenzake. Hatimaye, mmoja wao aliniingiza kwenye gari na baada ya kuliendesha kwa muda fulani akanisukuma nje na kuniacha barabarani. Hilo ni jambo lenye kuogopesha ambalo liliimarisha sana imani yangu katika Yehova na katika nguvu ya sala.

[Chati/Picha katika ukurasa wa 12, 13]

BAADHI YA MATUKIO YA MWAKA WA UTUMISHI WA 2004

Septemba 1, 2003

Septemba: Katika mwaka wa utumishi wa 2004, Shule ya Waangalizi Wanaosafiri ilifanywa katika ofisi za tawi 88.

Oktoba: Ofisi ya tawi ya Uingereza yaanza kutumia matbaa mpya aina ya MAN Roland.

Oktoba 28: Mahakama nchini Rumania yaamua Mashahidi wa Yehova wawekwe kwenye orodha ya dini zinazotambuliwa na serikali ambazo zinasamehewa kodi.

Novemba 1: Ofisi ya tawi ya Ufilipino yawekwa wakfu.

Novemba 28: Wizara ya Haki ya Georgia yaandikisha kisheria ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova.

Desemba 7: Ofisi ya tawi ya India yawekwa wakfu.

Januari 1, 2004

Machi 26: Mahakama ya Golovinsky yawapiga marufuku Mashahidi wa Yehova jijini Moscow. Mashahidi wakata rufani.

Aprili: Urusi yapata kilele cha juu kabisa cha mapainia wa kawaida 15,489.

Aprili 29: Kiwanda cha kuchapia huko Brooklyn chafungwa baada ya kuchapa mfululizo kwa miaka ya 84. Kiwanda kipya kiko Wallkill.

Mei 1, 2004

Mei: Haiti yakumbwa na msukosuko wa kisiasa na mafuriko yenye kuleta maafa. Hakuna ndugu wanaokufa.

Juni 16: Mahakama ya rufaa ya Moscow yaunga mkono uamuzi uliotolewa Machi 26. Sheria ya marufuku na kufutiliwa mbali kwa shirika la Mashahidi yatekelezwa. Rufani yakatwa katika Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu.

Agosti 31, 2004

[Picha katika ukurasa wa 11]

“Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo” katika lugha ya Georgia yatangazwa

[Picha katika ukurasa wa 27]

Ndugu wakiendesha moja kati ya matbaa mbili mpya za MAN huko Wallkill, New York, Marekani

[Picha katika ukurasa wa 29]

Ofisi ya Tawi iliyowekwa wakfu hivi karibuni huko Bangalore, India

[Picha katika ukurasa wa 30]

Ofisi ya tawi ya Ufilipino iliyopanuliwa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki