Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb06 kur. 6-30
  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
  • 2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kampeni ya Broshua Endeleeni Kukesha!
  • Kutafsiri Biblia
  • Masuala ya Kisheria
  • Mwaka wa Misiba ya Asili
  • Tsunami Mbaya Sana Kuwahi Kurekodiwa
  • Kuweka Wakfu Ofisi za Tawi
  • Matukio Muhimu Ya Mwaka Uliopita
    2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Matukio Muhimu Ya Mwaka Uliopita
    2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Kitabu-mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1990
    1990 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb06 kur. 6-30

Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita

NCHI nyingi zimekumbwa na misiba mingi ya asili katika miaka ya hivi karibuni, kutia ndani mwaka wa utumishi wa 2005. Bila shaka, misiba hiyo huwaathiri ndugu zetu. Lakini masimulizi haya yanaonyesha kwamba majaribu huwafanya ndugu waonyeshe upendo wa Kikristo ambao huimarisha umoja wao ulimwenguni pote, na kuwavuta watu wenye mioyo minyoofu wajifunze kweli.—Mal. 3:18; Yoh. 13:35.

Pia kuongezeka kwa misiba ya asili kumewafanya wengi wazingatie zaidi wakati ujao na mambo yaliyo muhimu zaidi maishani. Hivyo, wakati wa ile kampeni ya kugawa broshua Endeleeni Kukesha! tulipata pendeleo kubwa la kuwasaidia watu kama hao waelewe umuhimu wa nyakati tunamoishi. Katika nchi nyingi, kampeni hiyo ilianza Oktoba 18, 2004, nayo ilikuwa na matokeo mazuri.

Kampeni ya Broshua Endeleeni Kukesha!

Argentina: “Ni nani ambaye angeokoka kama msiba ungetokea? Je, ni mtu mbaya, mtu mzuri, au yule anayetii onyo?” Hivyo ndivyo dada mmoja alivyoanzisha mazungumzo alipokuwa akitoa broshua Kukesha! katika eneo lenye watu wengi wasiopendezwa.

Ndugu anayeitwa Juan alimwachia kijana mwenye miaka 16 broshua hiyo. Kijana huyo aliisoma na kumweleza baba yake kwa msisimko mambo aliyojifunza. Baba ya kijana huyo aliisoma broshua hiyo na maandiko yaliyokuwamo kwa kuwa alitaka kujua mengi. Alivutiwa sana na mambo aliyojifunza hivi kwamba alianza kujifunza broshua hiyo pamoja na familia yake. Juan aliporudi alimweleza baba huyo kuhusu mpango wa kujifunza Biblia bila malipo. “Hicho ndicho tunachohitaji hasa, yaani, funzo la Biblia la familia,” akasema baba huyo. Funzo la Biblia lilianzishwa.

Ufaransa: Jocelyne alimpa Alicia broshua Endeleeni Kukesha! Alicia ni msichana ambaye hapo awali alikuwa akijifunza. Alipokea broshua hiyo kwa furaha na akakubali kujifunza pamoja na Jocelyne. Pia, aliazimia kuisoma Biblia kwa ukawaida. Jocelyne anasema, “Baada ya majuma mawili tu, Alicia alisema kwamba alitokwa na machozi aliposoma masimulizi kumhusu Yesu.”

Alicia alimwambia mwanamume rafikiye kwamba anataka wahalalishe ndoa ili wampendeze Mungu na kwamba anatamani kuwa Shahidi wa Yehova. Alishangaa mwanamume huyo aliposema: “Ni sawa. Sitaki kukuzuia usifanye mambo ambayo Mungu anataka ufanye.” Tayari Alicia amehudhuria kusanyiko lake la kwanza la mzunguko.

Madagaska: Nana ni mama aliye na binti wawili wachanga. Alipokuwa kijana, alikuwa akihudhuria mikutano ya Kikristo pamoja na wazazi wake lakini akaacha wazazi wake walipoacha kumtumikia Yehova. Wakati wa kampeni hiyo ya pekee, dada mmishonari alimpa Nana broshua Kukesha! naye akakubali kujifunza Biblia. Sasa yeye huhudhuria mikutano yote pamoja na binti zake na anafanya maendeleo ili awe mhubiri. Isitoshe, wazazi wake walikubali kujifunza broshua hiyo. Hata ndugu yake anayeitwa Josia, ambaye ana miaka 14, anamfundisha kijana fulani rafikiye Biblia. Kijana huyo huhudhuria mikutano.

Nigeria: “Mama yangu alikufa wakati wa kampeni hiyo nami nikapata nafasi ya kuhubiri kijijini mwetu,” anasema ndugu mmoja painia. “Kabla ya mazishi, watu wa ukoo walilia na kujiangusha chini. ‘Mbona mnafanya hivyo?’ nikawauliza. ‘Kifo cha Mama kinatuhuzunisha sisi sote, lakini yeye amelala usingizi katika kifo. Atafufuka wakati wa ufufuo.’ Ijapokuwa mimi pia nilikuwa nikilia, nilifungua ukurasa wa 8 wa broshua Kukesha! na kufafanua picha za ufufuo katika ukurasa huo. Niligawa broshua 195, kutia ndani nakala 45 za broshua Kukesha! Wakati wa mazishi, mimi pamoja na ndugu wengine tuligawa nakala 100 za toleo la Mnara wa Mlinzi, la Mei 1, 2005, lenye kichwa, ‘Je, Wafu Wataishi Tena?’”

Urusi: Irina, ambaye ni painia wa pekee huko Zelenogradsk, anaandika: “Mimi na dada mwingine tulimpa mwanamke anayeitwa Alla, broshua Kukesha! Machoni pake maisha hayakuwa na kusudi lolote kwa kuwa watu wamekuwa na mioyo migumu sana. Tulipanga kumrudia. Siku kadhaa baadaye, mimi na dada mwingine tulipokuwa tukitembea, mwanamke fulani alituita. Mwanamke huyo alikuwa Alla. Alitushukuru kwa broshua tuliyokuwa tumempa, naye akaitoa mkobani mwake na kutuonyesha mambo aliyokuwa ametia alama. Sasa anajifunza broshua Anataka.”

Kwingineko huko Urusi, Vera na mume wake anayeitwa Vitaliy, walienda kwenye duka dogo kando ya barabara. Vera alimfahamu Lyuda, mwanamke aliyefanya kazi hapo. Lyuda alikuwa amesema kwamba hataki kuizungumzia Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, hivyo Vera akasita kumpa broshua Kukesha! Lakini baada ya Vitaliy kumtia moyo, Vera alimtolea Lyuda broshua hiyo naye akashangaa sana alipoikubali. Siku mbili baadaye, Lyuda akapiga simu na kusema: “Ikiwa nimejua mambo mengi hivi kwa kusoma broshua moja tu, bila shaka nitajua mambo mengi sana nikijifunza Biblia kwa ukawaida!” Licha ya upinzani wa watu wa ukoo, Lyuda alianza mara moja kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano. Mwana na binti yake wanajifunza pia. Vera alisema, “Inashangaza kwamba miaka kadhaa iliyopita, Lyuda alipewa kitabu Ujuzi lakini hakupendezwa hata kidogo. Ingawa hivyo, broshua Kukesha!, iliamsha hamu yake ya kujifunza.”

Venezuela: Mke wa mwangalizi mmoja wa mzunguko alizungumza na mume na mke fulani pamoja na watoto wao wanne wakiwa mlangoni. Dada huyo aliwaonyesha picha ya Paradiso iliyo kwenye ukurasa wa 16 na 17 wa broshua Kukesha!, na akakazia umuhimu wa familia nzima kujifunza kumhusu Mungu. Kisha, akawaalika wote sita kwenye mkutano Alhamisi jioni na kupanga wakutane kwenye kituo cha basi hapo karibu. Dada huyo na mume wake walifika kwenye kituo cha basi kwa wakati, lakini familia hiyo haikuwepo. Hawakujua kwamba yule mume, mke, na watoto wao walikuwa wamepanda basi lingine na kufika kwenye Jumba la Ufalme! Watu watano wa familia hiyo wanajifunza Biblia na kuhudhuria mikutano, licha ya safari ndefu na gharama kubwa ya usafiri.

Dada fulani painia alipiga hodi kwenye nyumba moja lakini hakuna mtu aliyeitikia. Alirudi hapo baadaye na kumpata mwanamume fulani mzee aliyekuwa tu ametoka katika nyumba hiyo. Mzee huyo alisema kwamba ana tatizo kubwa la kusikia na nyakati nyingine hasikii mlango unapobishwa au watu huondoka kabla hajafika mlangoni kwa kuwa anatembea polepole sana. Dada huyo alimpa broshua Kukesha! na kumwalika mikutanoni.

Kwenye mkutano, dada huyo alisimulia kisa hicho bila kujua kwamba yule mzee alikuwapo! Sasa mzee huyo anajifunza Biblia na ndugu fulani, anahudhuria mikutano yote, naye anataka kuwa mhubiri. Alipoulizwa kwa nini alihudhuria mkutano ule wa kwanza, aliinua broshua Endeleeni Kukesha! na kusema, “Ni kwa sababu ya broshua hii!”

Kutafsiri Biblia

Kuanzia mwisho-mwisho wa miaka ya 1800, Mashahidi wa Yehova walikuwa wakinunua na kugawa Biblia nyingi. Nyakati nyingine waliwaachia watu waliopendezwa Biblia kwa bei iliyopunguzwa kwa asilimia 65. Kuanzia 1926, ndugu walianza kuchapa na kujalidi Biblia mbalimbali katika kiwanda chao wenyewe cha uchapaji. Baadhi ya Biblia hizo ni The Emphatic Diaglott, King James Version, na American Standard Version. Kisha, katika 1961, Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ikatolewa katika Kiingereza.

Namna gani lugha zile nyingine? Mapema katika karne ya 20, ofisi za tawi zilianza kununua tafsiri mbalimbali za Biblia kutoka kwa mashirika mbalimbali ya uchapaji na kuzigawa kwa bei ileile ambayo zilinunuliwa. Baadhi ya Biblia hizo zilitafsiriwa na watu wanyoofu ambao hata walitumia jina la Mungu, yaani, Yehova, katika lugha za kienyeji. Hata hivyo, baada ya muda, watafsiri wengi waliliondoa jina la Mungu katika tafsiri zao. Leo watafsiri kadhaa wameliondoa jina la Mungu na badala yake wametumia jina la mungu anayeabudiwa na wenyeji! Kwa mfano, tafsiri ya Biblia ya Kichichewa iitwayo Buku Loyera, inayotumiwa nchini Malawi, Msumbiji, na Zambia, ina jina “Chauta” badala ya Yehova. Hilo ni jina la mungu wa kabila fulani linalomaanisha “Mkuu wa Uta.”

Kuna visa vingine chungu nzima. Kwa mfano, tafsiri moja ya Biblia katika lugha fulani ya Afrika inamtaja Luka kuwa mchawi. Katika Biblia ya Tuvalu, Yuda mstari wa 23 umetafsiriwa kwa njia hii iliyopotoka: “Wapendeni sana walawiti; lakini iweni waangalifu msiathiriwe na ulawiti wao.” Lakini, maandishi ya awali hayawataji walawiti wala ulawiti!

Zamani, mashirika ya Biblia ndiyo hasa yaliyochapa na kugawa Biblia. Hata hivyo, hivi karibuni, mashirika fulani ya Biblia yaliyo na haki za kisheria za kuchapa na kugawa Biblia yamezipa dini zinazojidai kuwa za Kikristo haki hizo. Mbali na kupandisha bei za Biblia, dini katika nchi fulani zinakataa kuwauzia Mashahidi wa Yehova Biblia. Kwa mfano, nchini Kyrgyzstan, dini fulani ya Kiprotestanti inamiliki haki za tafsiri moja ya karibuni ya lugha ya Kirghiz ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Ndugu wanapotaka kununua Biblia hiyo, wao huulizwa, “Je, wewe ni Shahidi wa Yehova?” au “Je, unajua jina la Mungu?” Wakisema ndiyo, wananyimwa Biblia.

Kwa sababu hizo na nyinginezo, Baraza Linaloongoza limeagiza kazi ya kutafsiri Biblia izingatiwe zaidi. Sasa, Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inapatikana katika lugha 35, na Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo inapatikana katika lugha 20. Ulimwenguni pote kuna vikundi 33 vya watafsiri wa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Vikundi 19 kati ya hivyo, vinatafsiri Maandiko ya Kiebrania, 11 vinatafsiri Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na 3 vinatafsiri chapa ya marejeo (Reference Bible). Biblia hutafsiriwa na kikundi cha kati ya watu watatu hadi sita. Kwa kutumia mifumo ya kompyuta na mbinu zilizoboreshwa, vikundi fulani vya watafsiri vimefaulu kutafsiri Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kwa muda usiozidi miaka miwili.

Ndugu wanahisije wanapopokea Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha zao? Wengi wanahisi kama painia fulani nchini Albania aliyesema: “Nilitokwa na machozi. Sijawahi kuhisi hivyo ninaposoma Neno la Mungu. Nataka kuelewa vizuri kila mstari!”

Masuala ya Kisheria

Armenia: Mnamo Oktoba 8, 2004, Mashahidi wa Yehova waliandikishwa kisheria. Kabla ya hapo walikuwa wamewasilisha maombi rasmi mara 15. Hata hivyo, bado ndugu vijana wanatiwa gerezani kwa sababu ya kufuata dhamiri zao na kukataa kujiunga na jeshi. (Isa. 2:4) Tunatumaini kwamba ndugu zetu wataendelea kuwa na uhuru wa kidini utakaowawezesha kuingiza vichapo nchini humo na kufanya makusanyiko. Ama kweli, mnamo Juni 2005, idara ya forodha iliwapa akina ndugu kibali rasmi cha kuingiza nchini Armenia shehena ya kwanza ya vichapo.

Austria: Kwa zaidi ya miaka 30, Mashahidi wa Yehova wamepambana kisheria ili waandikishwe rasmi. Hivyo, kesi tano zimewasilishwa kwenye Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu. Mnamo Februari 1, 2005, Mahakama hiyo ilikubali kusikiliza kesi mbili. Kesi hizo zinawahusu ndugu walionyimwa haki ya kutojiunga na jeshi ijapokuwa wao ni wahudumu wa kidini. Walinyimwa haki hiyo kwa sababu Mashahidi wa Yehova hawajaandikishwa kisheria. Mnamo Julai 5, Mahakama hiyo ilikubali kusikiliza kesi hizo lakini haijafanya uamuzi bado.

Eritrea: Mnamo Januari 24, 2004, washiriki 38 wa kutaniko la Saba, wakiwemo wanaume, wanawake, na watoto, walitiwa nguvuni na wenye mamlaka mjini Asmara. Wale waliokamatwa walikuwa na umri wa kati ya miaka 6 na 94. Baadhi yao hawakuwa wamebatizwa. Baada ya kukaa siku tatu korokoroni, wale wachanga zaidi waliachiliwa. Wale wengine 28 walipelekwa kwenye gereza fulani nje ya Asmara na kufungiwa ndani ya makontena ya chuma ya kusafirishia mizigo ambayo yana joto kali mchana na baridi usiku. Baada ya muda wa zaidi ya miezi saba, ndugu wawili wenye umri mkubwa zaidi, yaani, miaka 94 na 87, waliachiliwa mnamo Septemba 2, 2004. Wengine waliachiliwa baadaye. Hata hivyo, ndugu 6 bado wamefungwa pamoja na ndugu wengine 16, ambao 3 kati yao wamekuwa gerezani kwa miaka 11. Tafadhali endeleeni kusali kwa ajili ya ndugu hao wapendwa.—Mdo. 12:5.

Ufaransa: Kitabu cha Mwaka cha 2001 kiliripoti kwamba serikali ilianza kuwatoza akina ndugu kodi kwa ajili ya michango, kutia ndani michango iliyokuwa imetolewa miaka minne mapema (1993-1996). Ndugu walipaswa kulipa kodi kwa kiwango cha asilimia 60 na pia kulipa faini! Ndugu walikata rufani kwenye mahakama ya chini, mahakama ya rufaa, na mahakama kuu, lakini hawakufanikiwa. Mnamo Februari 25, 2005, walikata rufani kwenye Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu kwa msingi wa ubaguzi wa kidini uliokuwa wazi.

Jamhuri ya Georgia: Wakati huu ndugu zetu hawateswi sana. Wanaweza sasa kuingiza vichapo nchini humo nao wanaweza kukusanyika bila kusumbuliwa. Hata hivyo, kesi nyingi kuhusu kuwatenda ndugu kijeuri hazijaamuliwa bado. Ndugu wamewasilisha kesi nne dhidi ya serikali ya Georgia kwenye Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu. Kesi hizo zinahusu shtaka la kuwatesa ndugu zetu kijeuri, kupigwa marufuku kwa mashirika yetu ya kisheria, na kushindwa kwa mahakama kutatua matatizo hayo. Mnamo Julai 6, 2004, Mahakama ya Ulaya ilikubali kusikiliza kesi iliyowasilishwa na Kutaniko la Mashahidi wa Yehova la Gldani dhidi ya serikali ya Georgia.

Ujerumani: Ujerumani ilipoungana, ndugu walitaka kuhakikisha kwamba shirika la kidini la Mashahidi wa Yehova limeandikishwa kisheria. Hivyo mapambano ya kisheria ya miaka 12 yakaanza. Katika 2000, Mahakama Kuu ya Ujerumani ilitoa uamuzi mzuri uliopinga kauli ya kwamba Serikali ina haki ya kudai utii wa Mashahidi wa Yehova kinyume cha dhamiri yao inayoongozwa na Biblia. Katika vikao vilivyofuata, tatizo hilo lilitatuliwa. Mnamo Machi 24, 2005, Mahakama fulani ya Berlin iliagiza Jimbo la Berlin lilipe shirika la Mashahidi wa Yehova haki za kisheria. Jimbo hilo linataka kukata rufani dhidi ya uamuzi huo.

Urusi: Kitabu cha Mwaka cha 2005 kiliripoti kwamba mnamo Machi 26, 2004, Mahakama ya Manispaa ya Wilaya ya Golovinsky ilipiga marufuku kazi yetu jijini Moscow. Tangu hapo imekuwa vigumu kukodi majumba kwa ajili ya mikutano au makusanyiko. Hata hivyo, ndugu wana jengo kubwa lenye Majumba ya Ufalme matano yanayotumiwa na makutaniko 44 na vikundi 2. Ndugu wa makutaniko 17 ya Moscow hufanya mikutano nje ya jiji hilo. Kufanya hivyo huwagharimu na kuwatatiza sana. Makutaniko mengine 31 hufanya mikutano kadhaa au yote nyumbani kwa akina ndugu. Ndugu wamesumbuliwa na polisi mara kwa mara, lakini hakuna aliyekamatwa. Akina ndugu wamekata rufani dhidi ya uamuzi huo wa Machi 26.

Mnamo Septemba 9, 2004, kesi ya Kuznetsov na wengine iliwasilishwa dhidi ya serikali ya Urusi kwenye Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu. Mnamo Oktoba 4, Mahakama hiyo ilikubali kuisikiliza. Kesi hiyo inamhusu ofisa fulani aliyewaamuru polisi wavunje mkutano wa kutaniko fulani la lugha ya ishara huko Chelyabinsk mnamo Aprili 2000. Awali kesi hiyo iliposikilizwa makosa mengi ya kisheria yalifanywa, na hilo limeifanya iwe ngumu sana. Tunasubiri uamuzi wa Mahakama.

Turkmenistan: Ndugu watatu—Mansur Masharipov, Atamurat Suvkhanov, na Vepa Tuvakov—walihukumiwa kifungo cha miezi 18 kila mmoja, kwa sababu ya kufuata dhamiri yao na kukataa kujiunga na jeshi. Ndugu mwingine, Begench Shakhmuradov, alihukumiwa kifungo cha mwaka mmoja. Katika Februari 16, 2005, ofisi ya Mashahidi wa Yehova inayoshughulikia mambo ya kisheria iliandikia ubalozi wa Turkmenistan jijini Washington, D.C., na kuomba ndugu hao wanne waachiliwe bila masharti. Mnamo Aprili 16, ndugu hao waliachiliwa kufuatia msamaha wa pekee wa rais wa Turkmenistan. Katika mwaka huo, ndugu na dada wengi walitiwa korokoroni na kuhojiwa na polisi ili waikane imani yao. Lakini jitihada za polisi hao zikaambulia patupu.

Mwaka wa Misiba ya Asili

Katika 2004, nchi mbalimbali zilikumbwa na misiba mikubwa ya asili. Misiba hiyo iliwaathirije ndugu zetu?

Visiwa vya Carriacou, Grenada, na Petite Martinique: Mnamo Septemba 7, 2004, Kimbunga Ivan kilikumba visiwa hivyo na kuharibu zaidi ya asilimia 90 ya nyumba. Inashangaza kwamba hasara iliyosababishwa na waporaji huenda ikawa sawa na ile iliyosababishwa na kimbunga! Ndugu walipoteza mali nyingi, na Majumba ya Ufalme mawili kati ya majumba sita katika kisiwa cha Grenada yakaharibiwa vibaya. Hakuna ndugu aliyejeruhiwa sana.

Muda fulani mapema, ofisi ya tawi ya Barbados, ambayo inasimamia kazi katika visiwa hivyo, ilipendekeza kwamba katika Mkutano wa Utumishi, makutaniko yazungumzie jinsi ya kujitayarisha kwa ajili kimbunga. Pendekezo hilo lilitolewa licha ya kwamba eneo hilo halikuwa limekumbwa na kimbunga tangu 1955. Dada fulani kisiwani Grenada aliuliza: “Mbona tunapoteza wakati kuzungumzia vimbunga hali kuna mambo mengine yaliyo muhimu zaidi?” Kimbunga Ivan kilipokumba eneo hilo, dada huyo aliazimia kutochambua kamwe mwelekezo wa tengenezo! Upesi, ofisi ya tawi iliunda halmashauri ya kutoa misaada, na ofisi za tawi za Guyana na Trinidad zikatuma misaada. Mamia ya ndugu kutoka Karibiani na Marekani walisaidia katika ujenzi.

Jamaika na Visiwa vya Cayman: Ingawa hakuna ndugu aliyeumizwa na Kimbunga Ivan, wengi walipoteza mali zao. Mara tu hali ya hewa ilipokuwa afadhali, wazee waliwatafuta wahubiri katika visiwa hivyo vyenye makutaniko 199. Watu walioona hayo walisema: “Ninyi watu mnawajali sana wenzenu.”

Haiti: Katikati ya Septemba, sehemu ya kaskazini ya Haiti ilikumbwa na Kimbunga Jeanne, ambacho kilisababisha mafuriko makubwa katika mji wa Gonaïves na maeneo ambayo yanauzunguka. Maji yalifika kwenye magoti ya watu waliokuwa wamepanda kwenye paa za nyumba ili kujisalimisha! Ndugu mmoja anasema: “Usiku kucha tulisikia nyumba zikibomoka na watu wakipiga mayowe.” Watu 2,900, kutia ndani dada mwenye umri wa miaka 83, walikufa katika kimbunga hicho.

Ndugu fulani anasema, “Namshukuru Yehova kwa kuwa familia yetu iliacha mali na kukimbia na hivyo ikanusurika.” Siku kadhaa baadaye, Mashahidi wa miji jirani walituletea chakula na maji safi, na ofisi ya tawi ikatuletea misaada mingine. Licha ya kazi nyingi ya usafi, kufikia mwishoni mwa juma, sote tulifaulu kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kuhubiri. “Watu 40 waliojitolea walirekebisha nyumba yangu kwa muda wa siku nne,” anasema dada fulani. “Hata waliipaka rangi! Hilo liliwavutia sana watu wa familia yetu ambao si Mashahidi. Tayari mmoja wao ameanza kujifunza.”

Marekani: Katika Agosti na Septemba 2004, jimbo la Florida lilikumbwa na vimbunga vinne: Charley, Frances, Ivan, na Jeanne.a Zaidi ya nyumba 4,300 za akina ndugu na angalau Majumba ya Ufalme kumi yaliharibiwa. Hatimaye, mwenyekiti wa Kamati ya Kushughulikia Hali za Dharura huko Florida alifanya uchunguzi ili kuhakikisha kwamba misaada iliyotolewa inatumiwa vizuri. Alisema kwamba hakuna kikundi kingine chenye utaratibu kama Mashahidi wa Yehova. Aliiambia halmashauri ya kutoa misaada kwamba ingepewa chochote ilichohitaji.

Kutaniko fulani lilikuwa likifanyia mikutano kwenye jengo lililokodiwa kwa dola 50 kwa kila mkutano. Jengo hilo liliharibiwa wakati kimbunga cha kwanza kilipokumba eneo hilo. Mafundi walipewa kazi ya kulirekebisha, lakini hawakukamilisha kazi hiyo. Ndugu waliwaomba wenye jengo hilo wawaruhusu walirekebishe nao wakakubali. Akina ndugu waliifanya kazi hiyo haraka sana. Kwa hiyo, wenye jengo hilo wakaamua kutowatoza kodi kwa miezi mitatu.

Japani: “Japani imekumbwa na vimbunga vingi zaidi [katika 2004] kuliko katika mwaka mwingine tangu ilipoanza kurekodi matukio hayo mnamo 1551,” inasema ripoti fulani. Katika wilaya za Niigata na Fukui, hali mbaya ya hewa katika mwezi wa Julai iliharibu nyumba na majengo mengine zaidi ya 34,000, kutia ndani Jumba la Ufalme na nyumba 60 za akina ndugu. Mamia ya ndugu wa makutaniko jirani walitoa msaada bila kukawia. Majuma mawili baadaye, hilo Jumba la Ufalme lilikuwa limerekebishwa kabisa.

Akina ndugu walisaidia pia kusafisha nyumba za watu ambao si Mashahidi wa Yehova wanaoishi karibu na Jumba la Ufalme, na pia kuzipiga dawa za kuua viini. Mtu fulani aliyekuwa akipinga ujumbe wa Ufalme alitokwa na machozi ya furaha. Wenye mamlaka waliiandikia halmashauri ya kutoa misaada ili kuwashukuru akina ndugu kwa kazi yao.

Mnamo Septemba na Oktoba, vimbunga viwili viliikumba Japani, na ndugu mmoja na dada mmoja wakafa katika mafuriko na maporomoko ya udongo. Mashahidi wengine 100 waliathiriwa pia. Jiji la Toyooka, katika Wilaya ya Hyogo lilikumbwa na mafuriko. Mwangalizi wa mzunguko alisaidia kufanya mipango ya kutoa misaada ijapokuwa nyumba yake ilikuwa imejaa maji.

Baada ya maji yenye matope kupungua katika nyumba ambayo dada fulani painia alikuwa amekodi, akina ndugu waliisafisha hadi ikatakata. Mwenye nyumba hiyo si Shahidi, lakini alivutiwa sana. Dada huyo alisema: “Nimekuwa tu nikisikia kuhusu misaada inayotolewa na tengenezo la Yehova, lakini wakati huu mimi binafsi nimesaidiwa. Najivunia pendeleo la kumtumikia Mungu wetu, Yehova, na la kuwa sehemu ya tengenezo lake.”

Pia, mwezi wa Oktoba, watu 40 walikufa na wengine zaidi ya 100,000 wakalazimika kuhama makwao kwa sababu ya tetemeko kubwa la ardhi lililokumba eneo la kaskazini la Japani. Hakuna ndugu aliyejeruhiwa wala kufa, hata hivyo familia 200 ziliathiriwa na Jumba la Ufalme moja likaharibiwa kabisa. Tetemeko hilo lilipoanza wazee wa mzunguko wa eneo hilo walikuwa wamekusanyika ili kutayarisha kusanyiko la mzunguko. Wazee hao walifanyaje? Walifuata mwelekezo wa ofisi ya tawi na wa Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa ya eneo hilo, nao wakaanza mara moja kufanya mipango ya kutoa misaada. “Tulitiwa moyo tuwe na maoni ya kiroho kuhusu msiba huo,” anasema mzee fulani. Kusanyiko la mzunguko lilifanywa, na hata wale walioathiriwa na tetemeko hilo walihudhuria.

“Tetemeko hilo lilimtetemesha mume wangu,” anasema dada fulani ambaye mume wake si mwamini. Nyumba yao ilikuwa imeharibiwa. Alipoona jinsi ndugu walivyoonyesha upendo wakati wa kutoa misaada, mume huyo alihudhuria mkutano kwa mara ya kwanza. Alisema: “Naweza kulitegemea kabisa tengenezo lenu. Haliwezi kamwe kutukatisha tamaa.”

Filipino: Vimbunga vilipokumba wilaya za Quezon na Aurora mwishoni-mwishoni mwa 2004, mume na mke fulani ambao ni Mashahidi, na watoto wao wanne, walikufa wakati nyumba yao ilipojaa maji na matope. Felimon Maristela, ambaye ni mwangalizi wa mazunguko, alikuwa kwenye wilaya ya Quezon mafuriko yalipoanza. Anaandika: “Jumba la Ufalme lilijaa maji haraka sana na gari langu likabebwa na maji. Mimi, mke wangu, na ndugu wengine wawili, tulikaa kwenye paa la Jumba la Ufalme usiku kucha huku maji yakiipiga-piga paa hilo. Nilishuka chini mwendo wa saa 9:00 alasiri siku iliyofuata na bado maji yalifika kwenye kifua changu.”

Licha ya hatari, Ndugu Maristela aliwatafuta wahubiri ili ahakikishe kwamba walikuwa salama. Huko Dingalan, Aurora, mzee fulani wa kutaniko alipata nafasi ya kuhamishwa kwa ndege lakini akaamua kubaki katika eneo hilo ili awasaidie Wakristo wenzake.

Tsunami Mbaya Sana Kuwahi Kurekodiwa

Mnamo Desemba 26, 2004, tetemeko la ardhi la kiwango cha 9.0 lilikumba eneo lililo karibu na pwani ya magharibi ya Sumatra kaskazini, huko Indonesia, na kusababisha mawimbi ya tsunami yaliyoleta uharibifu mkubwa zaidi kuwahi kurekodiwa. Inakadiriwa kwamba idadi ya watu waliokufa na ya wale waliopotea ni zaidi ya 280,000! Hata katika nchi ya Somalia iliyo mbali sana barani Afrika, mawimbi hayo yaliwaua watu 290.

Indonesia: Ijapokuwa watu wengi sana walikufa nchini Indonesia, hakuna ndugu hata mmoja wala mtu anayependezwa aliyekufa. Kwa sababu ya visa vya jeuri vya hapo awali, ndugu wengi walikimbia Aceh, sehemu iliyoathiriwa vibaya sana na tsunami hiyo, na kuhamia maeneo yaliyo mbali na pwani. Kisiwa cha Nias pia kiliathiriwa vibaya sana, lakini ndugu walifaulu kukimbilia usalama.

India: Hakuna ndugu aliyekufa, hata hivyo, wengi walipoteza nyumba na mali zao. Dada Lakshmi alikuwa akihubiri jijini Pondicherry aliposikia kuhusu tsunami hiyo. Alirudi kwake na kupata nyumba yake ya udongo iliyokuwa umbali wa kilometa tatu kutoka kwenye ufuo wa bahari, ikiwa imeharibiwa vibaya sana. Ndugu walimsaidia kuisafisha na kuirekebisha.

Huko Madras, Naveen aliye na umri wa miaka 13 alikuwa akicheza kriketi alipoona mawimbi makubwa. Alimjulisha dada yake na mama yake, na wote wakakimbilia usalama. Hata hivyo, iliwabidi kupita kwenye maji yaliyobeba vyombo vya nyumbani na maiti nyingi.

Lini, aliye na umri wa miaka saba, alikuwa ufuoni huko Kanniyākumāri pamoja na baba mdogo na binamu yake. Lini alibebwa na mawimbi na hatimaye akakwama kwenye ua fulani wa mbao. Maji yaliendelea kumpiga. Baba yake mdogo na binamu yake waliokoka, lakini baba yake mdogo akapoteza miwani na hakuweza kuona vizuri. Hata hivyo, aliendelea kumtafuta Lini. Punde si punde, alimsikia Lini akimlilia Yehova naye akamwokoa. Sasa Lini anawaeleza watu wote kwamba Yehova alisikiliza sala yake.

Visiwa vya Andaman na Nicobar: Mary na mwanawe mwenye umri wa miaka minane anayeitwa Alwyn, walikuwa wameenda kuwatembelea watu wa ukoo tetemeko lilipotikisa nyumba walimokuwa. Wote walikimbia nje. Mary aliona wimbi kubwa la maji likielekea kasi ufuoni. Kufumba na kufumbua, basi fulani likafika. Mary na mwanawe wakalipanda na kukimbilia usalama. Hata hivyo, wengine walirudi makwao ili wakusanye mali zao nao wakabebwa na maji. Muda si muda, wale waliokuwamo basini wakasikia tetemeko lingine. Wote walishuka na kukimbilia eneo fulani lililoinuka ambapo watu wengine 500 hivi walikuwa wamekusanyika. Waliona basi hilo likibebwa na maji yaliyoongezeka na kufikia nusu meta hivi kutoka mahali walipokuwa wamesimama.

Maji yalipopungua, Mary alirudi kwake kwa muda mfupi. Alipata Biblia na kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku, na vitabu hivyo vikamwimarisha katika siku zilizofuata. Watu kisiwani humo walipopashwa habari kwamba meli zingetumiwa kuwahamisha, mamia ya watu walipiga mbio kwenda ufuoni na hata kuingia baharini wakitazamia kupata nafasi ya kuingia melini. Kwa saa kadhaa kila siku, Mary na mwanawe walisubiri wakiwa kwenye maji yaliyofika viunoni mwao na walizungukwa na maiti zilizoelea. Hatimaye, siku sita baada ya tsunami kutokea, walihamishwa kwa meli. Wengi walimlaumu Mungu kwa sababu ya msiba huo, hivyo Mary akapata nafasi ya kuwahubiria. Sasa dada-mkwe wake anajifunza Biblia na kuhudhuria mikutano.

Prasanthi na Jehoash, mwana wake mwenye umri wa miaka mitano, walikuwa wameenda Hut Bay ili kumtembelea baba yake mzee anayeitwa Ndugu Prasad Rao. Wakiwa hapo, walisikia tetemeko, wakaona mawimbi, na kukimbilia eneo lililoinuka. Maji yaliongezeka na kufikia meta tano juu ya barabara nayo yakaifunika nyumba ya Prasad. Maji hayo yalibeba kitanda, friji, na televisheni yake, na pia akiba ya kutaniko ya vitabu Mtu Mkuu. Baadaye, waokokaji walipata baadhi ya vitabu hivyo na kuvisoma. Kwa siku tano, Prasad, Prasanthi, na Jehoash walikula chakula walichookota, wakasumbuliwa na mbu na nzi. Hatimaye meli ziliwasili. Ili waokolewe iliwabidi Prasanthi, Jehoash, na watu wengine wengi kupita ndani ya maji yaliyofika vifuani mwao. Maji hayo yalikuwa na mamba! Wakati huo Prasanthi, alikuwa na mimba ya miezi sita. Baba yake alijiunga nao baadaye.

Nyumba zote katika Kisiwa cha Teressa zilibebwa na maji. Ndugu na dada 13 walikaa siku sita msituni ambako, mbali na kukosa chakula walishambuliwa na wadudu. Hatimaye walipelekwa kwenye Kisiwa cha Camorta. Walikaribishwa na Mark Paul, ndugu anayeishi katika eneo fulani lililoinuka. Mikutano inafanywa katika nyumba ya ndugu huyo. Kwa kawaida, watu 10 hadi 12 ndio waliokuwa wakihudhuria mikutano. Lakini siku ambayo tsunami ilitukia, watu 300 walihudhuria mkutano! Tangu hapo, wanafunzi wapya 18 huhudhuria mikutano kwa ukawaida, baada ya kujionea wenyewe jinsi watu wa Yehova wanavyotegemezana kwa upendo.

Sri Lanka: Mawimbi yalikumba thuluthi mbili za pwani ya kisiwa hicho na kusababisha uharibifu mkubwa. Mawimbi hayo ya tsunami yalitokea Jumapili asubuhi wakati ndugu wengi walipokuwa mikutanoni katika eneo ambalo halikuathiriwa. Makutaniko kumi yaliathiriwa na dada mmoja akafa pale nyumba yake ilipobebwa na maji hadi baharini. Akina ndugu wanaomboleza sana kifo cha dada huyo mzuri. Watu fulani wanaopendezwa walikufa na ndugu wengi walifiwa na watu wa ukoo. Mzee mmoja wa kutaniko alifiwa na watu 27 wa jamaa yake! Licha ya hayo, “akina ndugu wameokoka msiba huo bila kupatwa na dhara lolote la kiroho,” ofisi ya tawi inaandika.

Misaada mingi sana ilimiminika Betheli nao Wanabetheli wengi wakasaidia kuigawa. Magari ya akina ndugu yalitumiwa kusafirisha misaada hiyo kwenye maeneo yaliyoathiriwa. Ilichukua siku nne tu kuwapata ndugu wote na kuwapa chakula na mavazi. Walipoulizwa wanataka nini kingine, walijibu: “Biblia na vitabu! Vitabu vyetu vilibebwa na maji.” Walipewa vitu hivyo mara moja.

Mwangalizi wa mzunguko Gerrad Cooke, alikuwa Colombo wakati huo. Gerrad alisafiri kwa gari lake kwa muda wa saa saba kwenye barabara ambayo ni hatari usiku kwa sababu ya tembo. Alipowasili mwendo wa saa 4:30 usiku, yeye pamoja na ndugu mwingine wa eneo hilo, ambaye nyumba yake ilikuwa imejaa maji, walianza kutembelea familia za akina ndugu na kuwapa misaada. Walifanya kazi hiyo mpaka che.

Thailand: Ndugu wenyeji hawakujeruhiwa, hawakufa, wala hawakuachwa bila njia za kujiruzuku. Hata hivyo, watalii kadhaa waliokuwa likizoni nchini humo hawajapatikana na yaaminiwa kwamba wamekufa. Watalii hao wanatia ndani ndugu mmoja Mfini, mume na mke Waswedi, ndugu mmoja kutoka Austria, na mume asiyemwamini wa dada fulani. Ndugu wawili Waswedi na wake zao walikuwa wameenda kuhubiri pamoja na akina ndugu katika eneo lililokuwa mbali na ufuo. Waliporejea kwenye hoteli yao, waliona tu maiti na uharibifu.

Jumatatu asubuhi, baada ya tetemeko, mwangalizi msimamizi wa Kutaniko la Phuket alipigiwa simu na ofisi ya tawi ya Thailand na kujulishwa kwamba dada Mfini anayeitwa Kristina, alikuwa amelazwa katika hospitali fulani. Safari ya kutoka Phuket hadi kwenye hospitali hiyo huchukua muda wa saa moja na nusu. Mwangalizi huyo na ndugu mwingine walifunga safari mara moja kwenda huko. Mwangalizi huyo anaandika hivi: “Sijawahi kuona maafa makubwa kama haya. Tuliwaona watu waliopoteza waume au wake, wazazi waliopoteza watoto, watoto waliopoteza wazazi. Baadhi yao walikuwa wakililia msaada, huku wengine wakitazama tu dari au sakafu. Hali hiyo ilikuwa yenye kusononesha sana hivi kwamba mara kwa mara tulilazimika kutoka nje ili kudhibiti hisia zetu na kusali tupate nguvu.”

Ndugu hao walimpata Kristina alipokuwa akitayarishwa ili afanyiwe upasuaji kwenye mguu wake uliokuwa umevunjika. Alikuwa amepoteza hati zake zote. Baada ya upasuaji, ndugu hao wawili walisali pamoja naye na wakakaa naye hadi usiku wa manane. Siku kadhaa baadaye, Kristina alirudi Finland kwa ndege. Ndugu hao wanaripoti kwamba “Kristina alikuwa mjasiri na imara,” licha ya hali ngumu alizokabili. Inasikitisha kwamba mume wake alikufa katika tsunami hiyo.

Kuweka Wakfu Ofisi za Tawi

Angola, Januari 8, 2005: Hiyo ilikuwa siku muhimu sana katika kazi ya kuhubiri nchini Angola, nchi ambayo imekumbwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe kwa miaka 40 hivi. Stephen Lett alikuwa na pendeleo la kutoa hotuba ya kuweka wakfu ofisi ya tawi nchini Angola, naye ni wa kwanza kati ya ndugu wa Baraza Linaloongoza kutembelea nchi hiyo. Watu 730 kutoka nchi 11 walikuwapo wakati makao hayo yalipowekwa wakfu. Kwa nini ofisi mpya ya tawi ilihitajiwa? Katika 1975, ofisi ya tawi iliripoti kilele cha wahubiri 3,055. Kufikia mwisho wa 2004, idadi ya wahubiri ilikuwa imeongezeka mara 18 na kufikia 54,000!

Bulgaria, Oktoba 9, 2004: Katika kipindi cha miaka mitatu, wafanyakazi 150 wa kujitolea wa kimataifa, na ndugu wenyeji 300 hivi, walisaidia kujenga ofisi mpya ya tawi huko Sofia. Gerrit Lösch wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya kuweka wakfu iliyosikilizwa na watu 364 kutoka nchi 24.

Ethiopia, Novemba 20, 2004: Kufikia mwanzoni mwa 2004, Wanabetheli 60 walikuwa wakiishi katika nyumba tisa mbalimbali. Hilo halikupendeza hata kidogo! Betheli mpya ya Ethiopia iko kwenye mteremko fulani ulio mashariki mwa jiji kuu, Addis Ababa. Eneo hilo liko mita 2,400 juu ya usawa wa bahari. Usiku unaweza kusikia vicheko vya fisi. Gerrit Lösch alitoa hotuba iliyosikilizwa na watu 2,230, kutia ndani wageni 200 kutoka nchi 29. Baadhi ya waliohojiwa walikuwa wameteswa na hata kufungwa kwa sababu ya imani yao. Binti ya ndugu fulani aliyeuawa alisema, “Wakati wa ufufuo, Baba atafurahi kujua kwamba niliiga mfano wake wa kumcha Mungu na kwamba nilitumika Betheli.”

Ghana, Machi 5, 2005: Malcolm J. Vigo wa ofisi ya tawi ya Nigeria alitoa hotuba ya kuweka wakfu iliyosikilizwa na watu 3,243. Majengo mapya kwenye ofisi ya tawi yanatia ndani nyumba tatu za makao, ofisi 50, jengo la udumishaji, Jumba la Ufalme, jumba la kulia, jikoni, na mahali pa kufulia nguo.

Guam, Juni 25, 2005: Hii ndiyo iliyokuwa programu ya tatu ya kuweka wakfu nchini Guam tangu 1980. Katika mwaka huo 1980, kulikuwa na kutaniko moja tu nchini humo. Sasa kuna makutaniko kumi. Mradi wa ujenzi ulihusisha kurekebisha majengo fulani na pia kujenga Jumba la Ufalme jipya na jengo la makao lenye orofa mbili. Wafanyakazi 100 wa kujitolea wa kimataifa walitoka Australia na Marekani, nao waligharimia safari yao. Ofisi ya tawi inaandika kwamba mkaguzi mmoja wa ujenzi aliposikia kuhusu ujenzi huo na kuona ubora wake, “alipigwa na butwaa na kutikisa kichwa.” Lorence Shepp wa ofisi ya tawi ya Peru alitoa hotuba ya kuweka wakfu majengo hayo.

Mauritius, Novemba 6, 2004: Gerrit Lösch alitoa hotuba ya kuweka wakfu majengo mapya kwenye ofisi ya tawi. Majengo hayo mapya yana ofisi 12 za Idara ya Tafsiri na jengo jipya la udumishaji. Wageni walitoka Afrika Kusini, Madagaska, Mayotte, Réunion, Shelisheli, na Ulaya.

Nicaragua, Desemba 4, 2004: Zaidi ya wafanyakazi 330 wa kujitolea wa kimataifa na ndugu wenyeji walijenga ofisi mpya ya tawi na majengo ya makao. Pia walijenga Jumba la Kusanyiko lisilo na kuta linalotoshea watu 2,400. Samuel Herd, wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya kuweka wakfu majengo hayo. Wageni walitia ndani wamishonari waliokuwa wametumika nchini Nicaragua. Wazia jinsi walivyofurahi kuwaona wanafunzi wao wa Biblia na pia watoto na hata wajukuu wa wanafunzi hao!

Panama, Mnamo Machi 19, 2005: Samuel Herd, alitoa hotuba iliyosikilizwa na watu 2,967. Wengi kati yao walikuwa wamemtumikia Yehova kwa zaidi ya miaka 20. Ujenzi ulipoanza, ndugu walikodi kreni na mwendesha-kreni ili kuhamisha mabehewa fulani ya kuhifadhia vitu. Mtu huyo alipofika kwenye uwanja wa ujenzi alikataa kufanya kazi kwa sababu uwanja haukuwa umetayarishwa vizuri. Ndugu walimsihi lakini wakagonga mwamba. Kabla tu hajaondoka, aliuliza, “Samahani, ninyi ni wa dini gani?”

“Sisi ni Mashahidi wa Yehova,” ndugu wakajibu.

Aliwaza, kisha akasema, “Sawa, nitafanya kazi hiyo.” Kwa nini alibadili mawazo ghafula? Dada fulani wawili walikuwa wakijifunza Biblia na watoto wake, naye alithamini kazi yao.

Slovakia, Aprili 16, 2005: Theodore Jaracz, wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya kuweka wakfu iliyosikilizwa na watu 448 kutoka nchi 21. Siku iliyofuata, mkutano wa pekee ulifanywa katika uwanja wa michezo, na watu wengi waliwasili kwa mabasi. Dereva mmoja alisema, “Ninyi ni watu wazuri na wenye furaha na kila mmoja wenu ananisalimu! Ninajua ni kwa sababu ya imani yenu. Mimi huwabeba wanafunzi na walimu. Watoto hunisalimu tu baada ya mimi kuwasalimu, lakini walimu hawajishughulishi hata kidogo kunisalimu!”

Wallkill, New York, Marekani, Mnamo Mei 16, 2005, John Barr, wa Baraza Linaloongoza alisema hivi katika hotuba yake ya kuweka wakfu: “Sote tumeazimia kuweka wakfu kwa Mungu wa pekee wa kweli, Yehova, kiwanda hiki kipya maridadi cha uchapaji, na pia majengo ya makao ya A-, C-, na D-.” Kazi ya kuweka msingi wa kiwanda hicho kipya ilianza mnamo Mei 1, 2003. Miezi minane hivi baadaye, moja kati ya zile mashine tatu za kuchapa zilizokuwa zikitumiwa huko Wallkill zilihamishiwa kwenye kiwanda hicho.

Halmashauri za Ujenzi za Mkoa za Marekani, na hasa zile za majimbo jirani, zilituma mafundi. Baadhi ya kazi zilifanywa na wanakandarasi ambao si Mashahidi. Mwanakandarasi mmoja alisema: “Watu wangu hawawezi kufanya kazi kama ninyi hata nikiwapa pesa nyingi kadiri gani. Mnafanya kazi kwa moyo.” Naye msimamizi fulani wa mradi wa ujenzi, akasema, “Nimeelewa na kujifunza mambo mengi kuhusu kazi yangu katika miezi michache ambayo nimefanya kazi mahali hapa kuliko yale niliyojifunza kwa miaka mitano shuleni!” Wawakilishi wa shirika lililowauzia akina ndugu mashine yenye ukanda wa kusafirishia mizigo alisema: “Asanteni enyi watu, hii ndiyo mara yetu ya kwanza kuunganisha mashine haraka hivi. Kila mtu hapa ana furaha, na jambo hilo lanifurahisha! Mahali hapa panapendeza.”

Miaka michache iliyopita, ofisi ya tawi ya Marekani ilikuwa na mashine 15 za uchapaji zenye mabamba duara zinazoendeshwa kwa kompyuta. Mashine 11 zilikuwa Brooklyn na 4 huko Wallkill. Sasa ofisi hiyo ina mashine tano tu. Idadi ya mashine hizo imepunguzwa kwa sababu ya teknolojia bora na vilevile kwa sababu ofisi nyingine za tawi zilizo katika mpango wa uchapaji wa mkoa zinasaidia kuchapa. Kiwanda hicho kipya cha uchapaji kina mfumo wa kuondoa mabaki ya karatasi. Mfumo huo hupitisha karatasi hizo kwenye mabomba ya hewa yaliyo juu ya kiwanda na kuziingiza kwenye mashine ambazo huzifunga mabunda-mabunda. Karatasi hizo hununuliwa na kampuni fulani na hivyo ofisi ya tawi huokoa dola 200,000 hivi za Marekani kwa mwaka!

Zambia, Desemba 25, 2004: Watu 700 hivi walikuwapo kwa ajili ya programu ya kuweka wakfu majengo yaliyopanuliwa. Ndugu 374 kati yao wamemtumikia Yehova kwa zaidi ya miaka 40! Alipotoa hotuba ya kuweka wakfu, Stephen Lett aliwaambia wale waliosaidia kujenga majengo hayo kwamba sawa tu na wale watumwa katika mifano ya Yesu, wao pia wanastahili kupongezwa kwa moyo.—Mat. 25:23.

Akina ndugu walitoa ushahidi mzuri walipokuwa wakijenga. “Ninyi mnaishi paradisoni,” mwanakandarasi fulani alisema.

“Unazungumzia paradiso halisi au ya kiroho?” ndugu wakauliza.

“Zote mbili!” mwanakandarasi huyo akajibu.

[Maelezo ya Chini]

a Habari kuhusu Kimbunga Katrina zitatolewa baadaye.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 29]

Makusanyiko ya Wilaya ya “Utii wa Kimungu”

Kama ilivyoelezwa kwenye Kusanyiko la Wilaya la “Utii wa Kimungu,” wale tu ‘wanaomjua Mungu’ na ‘wanaotii habari njema’ ndio watakaookoka siku ya kisasi ya Yehova. (2 The. 1:6-9) Hivyo, tunataka kufanya yote tunayoweza ili kuwasaidia watu ambao wamemkasirikia Mungu au wana maoni yaliyopotoka kumhusu kwa sababu ya kuteseka ambako wanaona ulimwenguni. Trakti Kuteseka Kote Kutaisha Karibuni! na kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? ni vifaa vipya bora vitakavyotusaidia kufanya hivyo.

Bila shaka trakti hiyo mpya itawafariji watu wengi walioathiriwa na vita, umaskini, majanga, ukosefu wa haki, na magonjwa kwa kuwa itawasaidia kuelewa kwamba Mungu hasababishi mambo hayo. Hali kadhalika, kitabu hicho kipya kitawavutia wale wanaotamani sana kujua mafundisho ya kweli ya Biblia. Kitabu hicho kimeandikwa kwa njia yenye kuvutia na yenye kueleweka. Kuna picha na mifano mingi inayofafanua vizuri mambo makuu. Kabla hujaanza kukitumia kuongoza mafunzo ya Biblia, tafadhali soma vichwa 14 vya ziada vilivyozungumziwa kwenye nyongeza ya kitabu hicho.

[Chati/Picha katika ukurasa wa 12, 13]

BAADHI YA MATUKIO YA MWAKA WA UTUMISHI WA 2005

Septemba 1, 2004

Oktoba 8: Mashahidi wa Yehova waandikishwa kisheria nchini Armenia.

Oktoba 9: Ofisi ya tawi ya Bulgaria yawekwa wakfu.

Oktoba 18: Kampeni ya broshua Kukesha! yaanza.

Novemba 6: Ofisi ya tawi ya Mauritius yawekwa wakfu.

Novemba 20: Ofisi ya tawi ya Ethiopia yawekwa wakfu.

Desemba 4: Ofisi ya tawi ya Nicaragua yawekwa wakfu.

Desemba 25: Ofisi ya tawi ya Zambia yawekwa wakfu.

Desemba 26: Tetemeko la ardhi la kiwango cha 9.0 latokea karibu na Sumatra, Indonesia, na kusababisha mawimbi ya tsunami yaliyotokeza uharibifu mkubwa zaidi kuwahi kurekodiwa.

Januari 1, 2005

Januari 8: Ofisi ya tawi ya Angola yawekwa wakfu.

Machi 5: Ofisi ya tawi ya Ghana yawekwa wakfu.

Machi 19: Ofisi ya tawi ya Panama yawekwa wakfu.

Machi 24: Mahakama fulani ya Berlin yaamuru shirika la Mashahidi wa Yehova huko Berlin lipewe haki za kisheria.

Aprili 16: Ofisi ya tawi ya Slovakia yawekwa wakfu.

Mei 1, 2005

Mei 16: Kiwanda cha uchapaji na majengo ya makao huko Wallkill, New York, yawekwa wakfu.

Juni 25: Ofisi ya tawi ya Guam yawekwa wakfu.

Agosti 31, 2005

[Picha katika ukurasa wa 20]

Ndugu wakisafisha Jumba la Ufalme lililoharibiwa na mafuriko katika Wilaya ya Niigata, Japani

[Picha katika ukurasa wa 24]

Misaada yashughulikiwa nchini Sri Lanka

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki