Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb92 kur. 3-32
  • Mashahidi wa Yehova—Ripoti ya Kitabu-mwaka 1992

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mashahidi wa Yehova—Ripoti ya Kitabu-mwaka 1992
  • 1992 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mlango Ulio Wazi Leo
  • ‘Wakarimu Katika Mchango Wenu’
  • Kuruka Ukuta wa Uonevu
  • ‘Kutandaza Mapazia ya Hema’
  • Shule ya Mazoezi ya Kihuduma—Mlango wa Kimataifa Wafunguka
  • Kesi za Kisheria Zafungua Milango ya Kuhubiri
  • Kurudishwa kwa Mali Katika Afrika
  • Uchapishaji Katika Ulaya
  • Huduma za Kutafsiri—Chombo cha Kuenezea Habari Njema
  • Mikusanyiko Inayofungua Milango Yenye Kuongoza Kwenye Uhuru wa Kimungu
  • Kuwekwa Wakfu kwa Matawi: Mlango Mwingine wa Fursa Ulio Wazi
  • Fiji
  • Ugiriki
  • Hong Kong
  • New Caledonia
  • Ufilipino
  • Mashahidi wa Yehova—Ripoti ya Kitabu-Mwaka 1994
    1994 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Kitabu-mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1990
    1990 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Matukio Muhimu Ya Mwaka Uliopita
    2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
Pata Habari Zaidi
1992 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb92 kur. 3-32

Mashahidi wa Yehova—Ripoti ya Kitabu-mwaka 1992

KUSINI mwa Mto Kogamis kulikuwako Lidia jiji la Filadelfia. Likiwa juu ya uwanda wa juu wenye vilima katika sehemu yenye rutuba na hali nzuri, liliinuka juu ya bonde pana lililoelekea magharibi kupitia Sardisi hadi Smirna kwenye pwani ya Mediterranea. Filadelfia, linaloitwa sasa Alasehir, katika magharibi mwa Uturuki, lilikuwa kitovu chenye utajiri cha kufanyiza divai. Basi haishangazi kwamba mungu walo mkuu alikuwa Dioniso, mungu wa divai! Lakini kwa utofautiano mkubwa na furaha na macheko yanayotokana na kulewa divai, jiji hilo lilikuwa pia mahali ambapo Yesu alipaita “sinagogi la Shetani.” (Ufu. 3:9) Kundi la wafanyakazi Wakristo wa kweli lilisitawi katika mazingira hayo yasiyopendeza, ambapo matendo matakatifu ya mwenendo yangeonwa kuwa yasiyofaa. Lilikuwa moja la yale saba ambayo Yesu Kristo binafsi alisema nayo moja kwa moja katika kitabu cha Ufunuo. Mlango wa utendaji wa kitheokrasi ulikuwa umefunguka mbele ya waabudu hao washikamanifu wa Yehova.

“Nayajua matendo yako. Tazama,” akasema Yesu, mwenye ufunguo wa Daudi na Mtawala wa wafalme wa dunia. “Nimekupa mlango uliofunguliwa mbele yako, ambao hapana awezaye kuufunga, kwa kuwa unazo nguvu kidogo, nawe umelitunza neno langu, wala hukulikana jina langu.”—Ufu. 1:5; 3:7, 8.

Ebu wazia kwamba kikundi kidogo cha wafuasi wa Kristo wasiohofu, wenye umoja sana, walioshindana sana na wanyanyasi, ndio waliobarikiwa kuwa na mlango uliofunguliwa wazi kabisa wa utumishi mtakatifu! Viongozi wa kidini au watawala wa jiji hawakupata pendeleo kama hilo. Walikuwa hawajapata upendeleo wa Yesu walipotumia uwezo wao wa kutawala katika Filadelfia—sehemu yenye kufaa kwa maana ilikuwa katika mipaka ya utamaduni na ilikuwa ndiyo kilango cha kupitiwa kuingia Esia Ndogo ya kati. Kwa upande mwingine, Yesu alitia moyo kundi la Filadelfia litumie kikamili fursa yalo ya kuhubiri Ufalme wa Mungu. Walikuwa wamevumilia na kuonyesha kwamba walikuwa na uwezo wa kutosha, kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu, wa kuendelea na utendaji zaidi katika utumishi wa Yehova. Upinzani wa Wasio Wayahudi pamoja na ule wa Wayahudi haukusimamisha, wala hautaweza kamwe kusimamisha kazi ya kuupigia mbiu Ufalme.

Mlango Ulio Wazi Leo

Leo, kwa sababu ya mahubiri yanayoongozwa na ndugu wapakwa-mafuta wa Kristo, idadi kubwa za watu zimeingia katika utumishi wa Ufalme kupitia mlango uliofunguliwa. Unapofikiria juu ya ripoti ya utumishi ya ulimwenguni pote, bila shaka utakubali kwamba katika mwaka wa utumishi uliopita, Mashahidi wa Yehova kwa kweli wamepiga miguu kupitia mlango wa utendaji.

Kilele cha wahubiri: 4,278,820, ongezeko la asilimia 6.5 kupita mwaka wa utumishi wa 1990. Kiwango cha juu kipya katika wastani wa idadi ya wahubiri mapainia: 558,514. Jumla ya saa zilizotumiwa kuhubiri habari njema: 951,870,021.

Ni matokeo gani mazuri ambayo yametokana na utendaji huu wa kitheokrasi wakati wa mwaka wa utumishi wa 1991? Kwanza, watumishi wapya 300,945 waliojiweka wakfu kwa Yehova wamebatizwa. Pia, kulikuwa na makundi 3,191 zaidi ya yaliyokuwa katika 1990—ongezeko la wastani wa 8.7 kila siku—hiyo ikiwa jumla ya makundi 66,207 katika mabara 211. Pia, jumla ya hesabu ya ofisi za matawi imeongezeka kutoka 93 hadi 97, kutia na matawi 2 katika nchi zilizokuwa ng’ambo ya Pazia la Chuma la zamani. Na mabara ambayo sasa yamekuja kutambua Mashahidi wa Yehova kisheria ni Msumbiji katika Afrika, Cape Verde katika Bahari ya Atlantiki magharibi mwa Afrika, Nikaragua katika Amerika ya Kati, Paraguay katika Amerika ya Kusini, na Bulgaria, Urusi, na Ukrainia katika Ulaya ya Mashariki.

Inasisimua sana kama nini kuona uwezekano wa ukuzi wa wakati ujao kama inavyoonyeshwa na idadi ya wale waliokuwa kwenye Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Hudhurio lilikuwa 10,650,158 Jumamosi, Machi 30, usiku wa uadhimisho huo mtakatifu!

Katika Meksiko, hudhurio la Ukumbusho lilikuwa 1,230,099, ongezeko la asilimia 8 zaidi ya mwaka uliopita. Hilo lamaanisha kwamba mkaaji 1 kati ya kila 67 katika Meksiko alikuwako kwenye mwadhimisho huo. Na Brazili yenye wahubiri 302,367, ilikuwa na hudhurio la watu 897,739, wakiwa ni 106,813 zaidi ya mwaka uliopita. Basi haishangazi kwamba, kwa wastani, kundi jipya lilikuwa lazima lifanyizwe kila siku wakati wa mwaka wa utumishi katika Brazili, na mizunguko mipya 21 na wilaya mbili zilianzishwa katika Septemba 1, 1991. Mwadhimisho wa Ukumbusho katika Ufilipino mwaka huu ulileta shangwe kwa akina ndugu walipokaribisha 332,830 mahali pao pa mikutano. Hiyo ni mara tatu zaidi ya kilele chao cha wahubiri. Ulaya ya Mashariki pia ilikuwa na ongezeko zuri katika wahudhuriaji wa Ukumbusho. Urusi yaripoti 108,633 waliohudhuria, asilimia 43 zaidi ya mwaka jana! Polandi ilikuwa na watu 200,422 waliojaa Majumba ya Ufalme na sehemu nyinginezo katika usiku huo mtakatifu.

Kulikuwako jeuri katika usiku wa Ukumbusho katika miji mingi ya Afrika Kusini, ikifanya watu wengi wenye kupendezwa wakae nyumbani kwa sababu ya hofu ya kutaabishwa wakiwa wanasafiri kuelekea au kutoka sehemu ya Ukumbusho. Kutoa mfano wa magumu yaliyopatwa na watu fulani mmoja mmoja, fikiria hali ya Kundi la Montebello katika sehemu za mashambani za Natal. Hili ni kundi dogo la wahubiri kumi ambao juzi tu wamejenga na kuweka wakfu Jumba la Ufalme lao wenyewe. Jumamosi asubuhi, vita vya mafarakano vilizuka katika eneo hilo. Mzee mmoja katika kundi la jirani alipewa mgawo wa kuitoa hotuba. Yeye na mke wake walipokaribia kijiji cha Montebello, mtu wa mahali hapo aliyemjua ndugu huyu alimwuliza: “Unaenda wapi?” Akaeleza kwamba walikuwa wanaenda kwenye Jumba la Ufalme, ambapo angetoa hotuba ya Ukumbusho. Ndipo mtu huyo akaonya: “La, msiende huko kwa sababu huko ndiko watu wanauana.”

Na kweli kabisa, ndugu huyo alipokaribia Jumba, alihesabu miili kumi ya watu waliokufa, matokeo ya vita vya mafarakano. Kujapokuwa hatari hizo, watu 16 walihudhuria Ukumbusho. Jumba hilo ndilo pekee katika eneo hilo lililokuwa na mwangaza. Nyumba zote zilikuwa katika giza kwa kuhofu kuvutia wafanya matata. Baada ya Ukumbusho akina ndugu wote na watu waliopendezwa walilala katika nyumba ya ndugu mmoja karibu na hilo jumba. Asubuhi iliyofuata, baada ya kurudi nyumbani, vita vya mafarakano vilizuka tena.

‘Wakarimu Katika Mchango Wenu’

Ukuzi wa ajabu wa watu wa Yehova ulimwenguni pote umefanya kuwe na ongezeko katika hesabu ya wahudumu wa wakati wote wanaotumikia katika makao ya wamisionari, pamoja na hesabu ya mapainia wa pekee na waangalizi wasafirio. Ingawa wote ni wenye kujitolea wanaopokea rudishio dogo tu la kifedha kununua vitu vya kibinafsi vilivyo vya lazima, hata hivyo nyumba, ulishaji, na utunzaji wa ujumla wa wafanyakazi hawa walio wakfu katika migawo yao ya utumishi wa shambani ulihitaji dola 40,219,589.01 mwaka jana. Nyinyi mnastahili pongezi kwa ukarimu wenu, kama vile mtume Paulo alivyolishukuru kundi la Korintho kwa utayari wao wa kushiriki vitu na wengine. Yeye aliandika kuhusu utukufu unaomwendea Mungu “kwa ajili ya utii wenu katika kuikiri Injili ya Kristo, na kwa ajili ya ukarimu [katika mchango, NW] wenu.”—2 Kor. 9:13.

Watu wanyofu kwa moyo wanapoona jitihada zenye kudhamiriwa ambazo Mashahidi wa Yehova wamefanya ili kuendeleza habari njema, hata kwa njia ambayo wao hufanya kazi pamoja kujenga jengo jipya la tawi, wengi hutaka kufanya yote wawezayo kusaidia kuendeleza kazi ya Ufalme. Ruth ambaye ni msichana wa shule katika Naijeria, ni mfano mmoja. Baada ya kutembelea Betheli na jengo-tata la kiwanda katika Igieduma, ambalo lilimalizwa rasmi katika Aprili, aliandika:

“Nilihisi kuwa mwenye furaha sana kuona majengo hayo mazuri pamoja na maandalizi mengine ya kupendeza katika Betheli ya Igieduma. Yote hayo bila shaka yalifanywa yawezekane kwa michango ya hiari ya akina ndugu na dada. Nilipokuwa nikimshukuru Yehova kwa kazi hiyo kubwa katika Igieduma, swali moja likaja akilini mwangu. Ni nini uliokuwa mchango wangu kuelekea kusimamishwa kwa majengo haya? Nikiwa msichana wa shule wa miaka 16, nilikuwa bila kitu cha kuchanga kifedha. Hata hivyo, nilipokuwa nikizuru, nilikuwa na kuku aliyekuwa akitaga mayai. Baadaye akayaangua. Siku ambayo kuku huyo alitoka na vifaranga wake, nilichagua kimoja nikakiita Kuku wa Igieduma. Kwa kusikitisha, majuma kadhaa baadaye vifaranga walikumbwa na ugonjwa. Kimoja baada ya kingine kilikufa, kutia na mama yao. Lakini Kuku wa Igieduma alikataa kufa! Hivi karibuni nilimwuza kuku huyo na sasa ninapeleka pesa hizo zikiwa ‘mchango wangu mdogo kama ule wa mjane’ kuwezesha usambazaji wa habari njema.”

Mfano mwingine unatoka Ekwedori, mahali ambako painia mmoja anajifunza Biblia na mume na mke walio vipofu ambao wameanza kuhudhuria mikutano. Upesi walitaka kujua jinsi ya kujitayarishia mikutano. Hivyo painia huyo akaanza kurekodi somo la Mnara wa Mlinzi na sehemu ya funzo la kitabu kwenye utepe. Je! wanathamini msaada huo? Siku moja wakati mume huyo alipokuwa akiuza bidhaa kwenye kibanda chake sokoni, mteja mmoja mwanamke alimwambia kwamba yeye alikuwa anamlipa kiasi cha fedha kilicho sawa na dola tano hivi kwa bidhaa alizokuwa amenunua. Kwa uhalisi, mwanamke huyo alimlipa kiasi kinachopungua senti 50 [za U.S.]. Pesa alizopoteza zilikuwa sawa na kodi ya mwezi mmoja kwa mume huyo na mke wake ambao ni vipofu. Hata hivyo, jambo hilo la kuhuzunisha halikuwazuia kuwapo kwenye mkutano usiku huo. Na kabla ya kuondoka, aliuliza mahali sanduku la michango lilipo ili aweze kutia kitu fulani kwa ajili ya kazi ya Ufalme. Kwa kuona hilo, painia huyo alisema: “Uthamini wao hunistaajabisha kikweli.”

Kuruka Ukuta wa Uonevu

Mashahidi wa Yehova wanathamini sana uhai, nao hutafuta utibabu ulio mzuri. Lakini wao hawakubali mitio ya damu mishipani; huo ni msimamo wa kidini usioweza kubadilishwa. (Mdo. 15:29) Inawezekanaje kushinda ukuta wa uonevu na mkatao ambao Mashahidi hupata mara nyingi katika suala la damu? HIS (Hospital Information Services, yaani, Huduma za Kihospitali za Upashaji Habari) katika Brooklyn huzoeza na kuelekeza wazee wasaidie Mashahidi wenzao wakati wa uhitaji wa kitiba. Mfunzi mmoja kutoka idara hii alisema: “Mashahidi wa Yehova hawazuiliwi na ‘ukuta’ huu bali hujaribu kuupanda. Tunakumbushwa Zaburi 18:29: ‘Kwa msaada wa Mungu wangu naruka ukuta.’”

Tangu 1988, kwa msaada wa semina 32, shirika hili HIS limezoeza na kuanzisha Halmashauri za Kupatanisha na Hospitali kufikia 811 katika matawi makubwa 62 katika Amerika ya Kaskazini na Kusini, Karibea, Ulaya, na eneo la Pasifiki. Halmashauri hizi, za wazee 3,846, hushughulikia mahitaji fulani ya kipekee ya Mashahidi milioni 3.4 ambao huenda wakalazwa hospitalini katika mabara hayo. Je! semina hizo zimewawezesha wazee hao kufanya hivyo kwa matokeo?

Mzee mmoja wa kundi alisema: “Tuliwezeshwa kufanya maoni yetu yawe wazi, tukiwa thabiti na wenye heshima istahiliyo lakini bila kuzuiwa na hofu.” Mjumbe mwingine alisema: “Tulijifunza jinsi tunavyoweza kuelezea utibabu mwingine usiohusu damu, kurejezea vyanzo vya habari za kitiba, au kudokeza kupangia kupata utibabu mahali pengine ili kushikilia kanuni ya kujiepusha na damu.” Mwenyekiti mmoja katika idara ya upasuaji katika hospitali moja kubwa alisema: “Nyinyi watu kama nionavyo, mna maarifa mengi sana ya habari za kitiba na kisheria kuhusu utumizi wa damu.”

Bila shaka, maarifa stadi ya kitiba hayakuwa ndilo jambo kuu. Mjumbe mmoja alisema: “Maarifa ya kibinadamu siyo yaliyokuwa ya kuelekezewa fikira, kwa sababu ilikuwa imeonyeshwa mara nyingi kwamba Yehova na roho takatifu yake ndio wanaounga mkono mpango huo.” Ndugu mmoja aliyekuja kutoka ile iliyokuwa Ujerumani Mashariki alisema: “Semina hiyo ilikuwa pia kichocheo kwetu kuonyesha upendezi hata zaidi kwa ndugu wagonjwa.” Naam, Wakristo wa kweli wako chini ya wajibu wa kutunza waamini wenzao wanaougua. (Linganisha Mathayo 25:36.) Kutoa msaada pamoja na kitia moyo kwa akina ndugu walio katika hali za dharura, kutia ndani wale wanaokabiliwa na swala la damu, ni wonyesho wa upendo wa Kikristo.—Mhu. 4:12.

‘Kutandaza Mapazia ya Hema’

“Panua mahali pa hema yako, na wayatandaze mapazia ya maskani yako.” (Isa. 54:2) Aliyoandika Isaya kuhusu kuzaliwa kwa taifa jipya kwaweza kutumika kwa ujumla kuhusu ukuzi wa Mashahidi wa Yehova. Kwa sasa, zaidi ya matawi 20 kuzunguka ulimwengu yanajihusisha katika miradi mikubwa ya ujenzi, kutia ndani hesabu ya Majumba ya Mikusanyiko na Majumba ya Ufalme yanayojengwa.

Katika United States, kumekuwa na maendeleo makubwa mwaka jana katika ujenzi wa Kitovu cha Uelimishaji cha Watchtower katika Patterson, N.Y. Sehemu hiyo ya hektari 270 iko katika eneo lifaalo katika sehemu ya mashambani yenye mandhari nzuri kilometa kama 110 kaskazini mwa Brooklyn na kilometa 70 mashariki mwa Watchtower Farms, Wallkill, N.Y. Ujenzi unaendelea katika majengo kadhaa. Mawili ya hayo ni majengo ya makao yenye orofa tano, na jingine ni jengo la orofa tatu lenye sehemu ya jiko na chumba cha kulia kitakachotumiwa na watu zaidi ya 1,600. Kuna ndugu na dada zaidi ya 650 wanaofanya kazi katika mradi huo kila siku. Zaidi ya watu 80,000 wamezuru sehemu hiyo ya ujenzi tangu kitovu cha wageni kifunguliwe katika Septemba 1990.

Katika Japani, wakati ujenzi wa Jumba la Kusanyiko la Tokai ulipoanza, jirani mmoja alipinga vikali mradi huo akajaribu kupanga kampeni ya kusimamisha ujenzi. Alikuja kila siku kuchunguza kile kilichokuwa kinaendelea kwenye ujenzi huo, wakati wote akinung’unika. Lakini siku moja alipokuja kwenye sehemu ya ujenzi, akiwa na msumeno mkononi, ndugu mwenye uangalizi wa ujenzi alimsimamisha. Kwa mshangao wa ndugu huyo, mtu huyo akasema: “Nimekuwa nikitazama kile ambacho mmekuwa mkifanya kufikia sasa. Na inaonekana kwamba mianzi inawazuia. Acha nishiriki katika utumishi wa kujitolea leo.”

Si majumba na majengo ya tawi tu yanayohitaji kujengwa au kupanuliwa bali pia hesabu ya lugha ambazo tunachapisha vichapo yahitaji ‘kutandazwa.’ Kwa mfano, Idara ya Kompyuta kwenye Watchtower Farms hutegemeza mfumo wa kompyuta wa ulimwenguni pote wa Sosaiti uitwao MEPS. Mfumo huo sasa husaidia katika kupanga maandishi, kutafsiri, na kuchapisha maandishi yaliyoandikwa katika lugha 205.

Shule ya Mazoezi ya Kihuduma—Mlango wa Kimataifa Wafunguka

Wakati wa mwaka wa utumishi wa 1991, Shule ya Mazoezi ya Kihuduma kwa mara ya kwanza iliongozwa katika lugha nyinginezo zaidi ya Kiingereza. Hizo zilikuwa Kifaransa, Kijerumani, Kiitalia, na Kihispania. Darasa la saba la United States lilifanywa katika Belleville, Michigan, na darasa la nane katika Coraopolis, Pennsylvania. Madarasa ya pili na tatu katika Uingereza yaliongozwa katika Surrey na Manchester. Madarasa katika lugha za kigeni yalifanywa katika Creil, Ufaransa; Möllbergen, Ujerumani; Roseto degli Abruzzi, Italia; na Barcelona, Uhispania.

Kila asubuhi wanafunzi hukusanyika katika chumba cha chakula kwenye shule, mara nyingi katika Jumba la Kusanyiko au Jumba la Ufalme lenye vyumba vingine vya ziada, ili kufikiria andiko la siku kama inavyofanywa katika matawi yote ya Sosaiti. Ikiwa sehemu ya mazoezi yao, wanafunzi hupewa mgawo kutoa maelezo kwa andiko la siku au kutoa sala nyakati za milo. Baada ya kiamshakinywa, shule huanza saa 2:30 asubuhi. Kuna saa moja ya mapumziko kwa ajili ya chakula cha mchana, halafu kuanzia saa saba hadi saa nane alasiri, wanafunzi hushughulika na migawo yao ya kazi, ambayo yaweza kutia ndani usafi, kuosha vyombo vilivyotumiwa katika chakula cha mchana, kushughulikia kazi za kurekebisha na kutengeneza katika vifaa hivyo, au kutunza uwanja nje. Saa 8:00 alasiri huanza tena utendaji wao wa darasani. Baada ya masomo, wao hufurahia mlo wa jioni kwenye makao yao na humalizia jioni kwa saa tatu za masomo ya nyumbani.

Kupatana na kusudi la shule hiyo, wahitimu hawa wanatiwa moyo kupatikana wakiwa waaminifu wakifanya mapenzi ya Mungu kwa nafsi yote wanapotunza madaraka mbalimbali ya kundi kwa utii pamoja na migawo mingine.—1 Kor. 4:2; Efe. 6:6.

Kesi za Kisheria Zafungua Milango ya Kuhubiri

“Najua ya kuwa BWANA [Yehova, NW] atamfanyia mnyonge hukumu, na wahitaji haki yao,” Daudi akasema alipodhulumiwa. (Zab. 140:12) Yehova atalinda waabudu wake waaminifu kwa wakati wake na kwa njia yake mwenyewe. Yeye yuko upande wa wanaodhulumiwa, wanaoonewa, na wanaotendwa vibaya. Katika nchi fulani yeye hata aweza kutumia mfumo wa kisheria ili kufungua, au kuweka wazi mlango wa kazi ya kuhubiri.

Ili kusaidia katika kuuweka mlango ukiwa wazi, Idara ya Kisheria katika Brooklyn, yenye ndugu na dada wapatao 40, hufanya kazi chini ya mwongozo wa Baraza Linaloongoza kushughulikia mambo ya kisheria yaliyo ya lazima. Ingawa mifumo ya kisheria hutofautiana nchi na nchi, mingi yayo hutokana na kanuni za kawaida za “haki ya kiasili” na ‘inayokubaliwa na wote,’ au sheria ya kikatiba. Matukio ya ulimwengu ya hivi karibuni kama ule muungano wa kiuchumi wa sehemu kubwa ya Ulaya Magharibi unaotazamiwa karibuni na pia mabadiliko ya kisiasa yenye kutazamisha katika Ulaya ya Mashariki yanaonyesha waziwazi utegemeano ambao umeongezeka miongoni mwa mifumo ya kisheria. Kama tokeo, Idara ya Kisheria inahusika zaidi na zaidi katika kusaidia matawi ya Sosaiti wakati yanapokabiliwa na mambo ya kisheria, kama vile haki zetu zinazohusu kukataa utumizi wa damu kitiba, na huduma ya peupe.

Kurudishwa kwa Mali Katika Afrika

Wakati marufuku ya miaka 14 katika Benini ilipoondolewa mwaka jana, serikali ilirudisha Majumba ya Ufalme kadhaa yaliyokuwa yametwaliwa hapo kwanza, pamoja na makao yaliyokuwa ya wamisionari katika Porto-Novo na jengo lililokuwa ofisi ya tawi katika mji mkuu wa kifedha, Kotonou. Majengo hayo yanarekebishwa, na serikali imeruhusu wamisionari wanane waingie nchini.

Marufuku ilipoanza ghafula katika 1976, wamisionari wetu walikuwa na wakati unaopungua siku moja kufunga virago vyao waondoke Benini. Ni nini kilichotukia kwa vichapo na vifaa vya tawi kwenye ofisi ya tawi ambayo serikali ilitwaa? Jibu lilijulikana hatimaye katika Novemba 1990, wakati mtu mmoja alipopiga simu akisema kwamba vitu fulani vya Mashahidi vilikuwa vimewekwa kwenye nyumba moja katika mji mkuu huo. Je! akina ndugu wangeenda na kuvichukua? Kwa mshangao wao, akina ndugu walivikuta vitabu na vijitabu zaidi ya 5,000, kutia ndani maktaba za kibinafsi za wamisionari. Vifaa vingine vya Sosaiti vilikuwa mashine mbili za kufulia, jiko la gesi, mitungi ya gesi (mingine ikiwa bado imejaa gesi), kifaa cha kuchemshia maji, birika la kuogea, na mashine ya kukatia majani. Ingawa vitabu fulani vilikuwa vimegeuka rangi vikawa manjano, vingi vya vitu vilivyopatikana vilikuwa katika hali nzuri ijapokuwa miaka 14 ya kuwekwa akiba. Vitabu hivyo viliwekwa tayari akina ndugu wavipate, nao wakavichukua upesi ili kukamilisha maktaba zao za kibinafsi.

Uchapishaji Katika Ulaya

Ripoti moja kutoka Ufaransa yasema kwamba baada ya kufanya jitihada nyingi kwa zaidi ya mwaka mmoja, hatimaye Mei 16, 1991, tawi la Ufaransa lilipata ruhusa ya serikali ya kutumia mtambo wao mpya wa kupiga chapa kwa rangi nne. Matoleo ya kwanza ya magazeti yetu yenye rangi kamili kupelekwa kwenye makundi yalikuwa Mnara wa Mlinzi la Julai 15 na Amkeni! la Julai 22.

Ingawa Yugoslavia imetikiswa na misukosuko, kazi ya Ufalme inaendelea, na kwa kutofautiana na miaka iliyopita, hakukuwa na faini hata moja iliyotozwa na wenye mamlaka kwa sababu ya kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Vichapo na magazeti yenye rangi kamili, yanayochapishwa katika Ujerumani, vimeinua utendaji wa kuhubiri katika lugha za Kikroasha, Kimakedonia, Kiserbia, na Kislovania, na vile vile katika Kialbania. Hivyo, ingawa vizuizi vya kisheria, kazi ya kuhubiri Ufalme yasonga mbele. Kazi ya Yehova yapata nguvu.—Yer. 15:20.

Huduma za Kutafsiri—Chombo cha Kuenezea Habari Njema

Mvurugo wa lugha ya mwanadamu wakati wa ujenzi wa Mnara wa Babeli ulifanya familia ya kibinadamu kuwa na lugha za aina nyingi mara ile ile. Hilo lilifanya kuwe na uhitaji wa kazi mpya—ile ya mfasiri au mtafsiri. Kwa kutofautiana, katika Pentekoste 33 W.K., roho takatifu iliwawezesha wanaume na wanawake wazungumze kimuujiza lugha za watu kutoka wilaya 16 tofautitofauti za Milki ya Roma, bila kupoteza lugha yao wenyewe. Ingawa leo hakuna tafsiri ipitayo uwezo wa kibinadamu, bado chakula cha kiroho kinatolewa kwa ukawaida katika lugha zaidi ya 175, kingi chacho kikiwa sawia.

Vichapo vyote vya Watch Tower hutayarishwa kwanza katika Kiingereza, lugha inayozungumzwa na karibu asilimia 9 ya watu wote duniani. Ili kutoa vichapo hivi katika lugha za ulimwengu, Sosaiti ina watafsiri zaidi ya 900 wenye ustadi katika matawi 65 ulimwenguni pote. Halmashauri ya Uandikaji ya Baraza Linaloongoza huelekeza jitihada ya kutafsiri ulimwenguni pote kutoka makao makuu katika Brooklyn. Hiyo yatia ndani kuanzisha idara mpya za kutafsiri, kupangia kuzoezwa kwa watafsiri, kujibu maswali kutoka matawi, na kuandaa vyombo vifaavyo vya utafiti. Ili kusaidia jitihada hii ya kutafsiri, katika Aprili 1989 idara mpya iitwayo Huduma za Kutafsiri ilianzishwa.

Kwa sababu mara nyingi maneno huwa na maana nyingi, kutafsiri si kazi kama ya mashine ya kubadilisha neno kwa neno kutoka kamusi bila kutumia akili. Nahau huwa ni tatizo la aina ya pekee kwa watafsiri kwa sababu haziwezi kutafsiriwa kwa njia halisi. Kwa mfano, usemi wa Kiingereza “bite your tongue” katika Amkeni! la Juni 8, 1991, Kiingereza, haumaanishi ‘kujiumiza mwenyewe’; bali wamaanisha ‘kunyamaza.’ Pia, maana kamili ya usemi wa kwanza lazima ielezwe kwa usahihi katika lugha inayotafsiriwa. Zaidi ya hayo, neno lililonenwa na kuandikwa li hai kwa sababu hukua, hupanuka, na hubadilika kwa kadiri utumizi walo unapobadilika baada ya muda. Miaka michache iliyopita, ni nani aliyekuwa amesikia juu ya “glasnost,” “perestroika,” “right to life,” “pro-choice,” na “computer hacker”? Semi kama hizo hutokeza ugumu usioisha kamwe kwa watafsiri.

Wakiwa wanafanya kazi kwa ukaribu pamoja na wafanyakazi wa uandikaji wa Sosaiti, watafsiri hujaribu kudumisha nguvu ileile na ladha ya maandishi ya Kiingereza. Ili kuhakikisha kuwa na upatano, watafsiri huandaliwa mafafanuzi ambayo hueleza nahau na mambo mengine yanayohusiana na sarufi ya maandishi ya Kiingereza. Matawi yameitikiaje huduma hii?

Ujerumani yaandika: “Watafsiri wetu walipokea kwa msisimuko mkuu jambo hilo lililongojewa kwa muda mrefu.” Ghana yaandika: “Utaratibu wa kutia ndani maana za semi fulani umetuondolea mzigo wa kufanya utafiti mwingi wenye kuchukua wakati pamoja na ufikirio wa habari ya Kiingereza itakayotafsiriwa.” Na Italia yasema: “Wakati majina ya Kilatini ya mimea na wanyama yanapotolewa, huwa tunaona hilo kuwa lenye mafaa pia. Hilo huokoa wakati mwingi ambao sasa mtafsiri aweza kutumia katika kutafsiri kwenyewe.”

Tafsiri ya Biblia ni shughuli nyingine kubwa ya Sosaiti. Biblia ya New World Translation of the Holy Scriptures sasa yapatikana ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 13 na kuitafsiri katika lugha 20 zaidi kumeidhinishwa. Kufikia sasa, watafsiri wamemenyeka sana kwa wastani wa miaka 15 ili kuitafsiri. Ili kupunguza wakati unaohitajiwa kwa kutafsiri Biblia, Halmashauri ya Uandikaji ilielekeza uchunguzi ili kuona kufaa kwa kompyuta. Akili za kibinadamu kwa kutokuwa na kikomo zazipita kompyuta kwa sababu zinaweza kupata maana ya semi na zaweza kuchagua “maneno ya kweli [sahihi, NW].” (Mhu. 12:10) Hata hivyo, ilionekana kwamba kompyuta zaweza kuwa vyombo vya maana sana. Hivyo watafsiri wa Biblia wanatumia kwa faida mfumo wa kompyuta wenye kufaa matumizi yote ili kuhifadhi na kupata tena habari za maana sana za maneno na semi za Biblia. Mfumo huo una uwezo kamili wa kufanya utafiti wa maelezo ya Sosaiti juu ya Maandiko. Inatumainiwa kwamba hilo litaharakisha tafsiri ya Biblia huku ubora wa juu zaidi ukidumishwa.

Sosaiti imejitoa kufanya habari njema zijulikane kwa kiwango kikubwa iwezekanavyo. Kuanzia toleo la Januari 1, 1992, gazeti la Mnara wa Mlinzi linatafsiriwa katika lugha 111, kati ya hizi 66 zikiwa sawia na Kiingereza. Kwa maneno mengine, asilimia 95 ya Mashahidi wa Yehova hupokea chakula cha kiroho kilekile kwa wakati uleule. Vichapo vipya vinapatikana katika lugha nyinginezo zaidi, kutia ndani Kialbania, Kikambodia, Kiestonia, Kijojia, Kimakedonia, Kindonga, na Kinepali. Baraza Linaloongoza litaendelea kuelekeza jitihada za kuimarisha vikundi vya kutafsiri kwa ajili ya kazi kubwa iliyoko mbele. Kwa tabasamu ya kibali cha Yehova, hilo lapasa kutokeza Biblia nyingi hata zaidi na vichapo vya Kibiblia vinavyofanywa vipatikane kwa jamii zote za watu, mataifa, na lugha.

Mikusanyiko Inayofungua Milango Yenye Kuongoza Kwenye Uhuru wa Kimungu

“Nitakushukuru katika kusanyiko kubwa; nitakusifu kati ya watu wengi.” (Zab. 35:18) Mashahidi wa Yehova hutumia fursa za kutukuza Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima, nao hufanya hivyo kwa umoja katika mikusanyiko ya wilaya ya kila mwaka. Wakati wa mwaka wa utumishi wa mwaka uliopita, mikusanyiko iliyobaki ya 1990 ya “Lugha Iliyo Safi” ilipokuwa inakamilishwa katika sehemu moja ya tufe, mikusanyiko ya 1991 yenye kichwa “Wapendao Uhuru” ilianza katika sehemu nyingine ya dunia.

Jambo la kutokeza zaidi kwa Mashahidi wa Yehova katika Brazili lilitukia wakati wa miezi ya Agosti, Septemba, na Oktoba 1990. Lilikuwa mfululizo wa mikusanyiko ya siku nne ya “Lugha Iliyo Safi.” Baadhi ya mikusanyiko 110 iliyofanywa katika majiji 68 iliyotawanyika kotekote katika eneo kubwa la Brazili ilikuwa ya kimataifa na ilitumikia wajumbe kutoka nchi nyingine mbalimbali. Kulikuwako jumla ya watu 548,517 waliohudhuria, na 13,448 waliobatizwa walifurahisha watu wote.

Mikusanyiko hii ya kimataifa ilitangazwa vyema na waandishi habari na televisheni. Gazeti Jornal da Tarde, katika ripoti yalo ya ukurasa mzima, lilisema: “Tofauti na sherehe nyingine za kidini, mkusanyiko huo hautoi ithibati yoyote ya ushupavu wa kidini—hakuna yeyote anayepiga kelele, nyimbo za kidini ni nyororo, hakuna majionyesho ya maponyo wala watu wenye magunia wakitafuta pesa za waamini. Kwa upande mwingine, kuna hali ya usikivu kamili.”

Mwaka huu uliopita Mikusanyiko ya Wilaya ya “Wapendao Uhuru” iliyofanywa katika Brazili katika Julai na Agosti 1991 ilifanikiwa sana pia, na hotuba zilisaidia ndugu zetu watunze hata zaidi uhuru waliopewa na Mungu. Hali ya kujifurahisha ilikuwamo kwenye karamu hizi za kiroho za siku tatu. Jumla ya hudhurio la mikusanyiko yote 98 ikiwa pamoja ilikuwa 482,034, kukiwa na watu 8,991 wenye kubatizwa.

Katika Italia kasisi wa Katoliki alikuwa mmoja wa watu 245,161 waliohudhuria “Wapendao Uhuru” Mikusanyiko ya Wilaya. Alichangamana na umati kwenye mkusanyiko uliokuwa Brescia siku za Julai 19 hadi 21. Alivutiwa sana hivi kwamba aliweka kikaratasi chenye maandishi katika sanduku la michango. Aliandika hivi: “Mimi ni kasisi Mkatoliki, niliyevalia nguo za kawaida, niliyetaka kujionea wanalofanya na kusema watu hawa, ambao kanisa wakati wote limewafikiria kuwa wachache tu. Basi, robo saa ambayo mimi nilikuwa katika stediamu hii ilinitosha kuweza kung’amua jinsi nilivyokuwa nimepoteza wakati mwingi kufikia sasa. Nyinyi ni mfano wa kufuatwa kweli kweli. Mmenifanya nifikiri, na mmetumia kile ambacho napaswa kutumia mara nyingi zaidi—Biblia. Nani ajuaye, huenda siku moja nikawa pamoja nanyi, nikiwa nimevalia tai na koti.”

Ulaya ya Mashariki ilikuwa ndiyo kikao cha mikusanyiko mitatu ya kimataifa mwaka huu uliopita wa utumishi. Budapest, Hangari, ilikuwa na wajumbe 40,601; Prague, Chekoslovakia, ilikuwa na wahudhuriaji 74,587; wakusanyikaji 14,684 walikaribishwa Zagreb, Yugoslavia. Kwa kuwapo kwao kwenye uchangamshi, wajumbe kutoka sehemu zote za dunia walipamba barabara zilizosongamana watu zilizokuwa karibu na maeneo ya mikusanyiko. Shangwe tele ilikuwapo miongoni mwa wajumbe walipokuwa wanapokea maagizo mazuri ya Biblia na kuanzisha upya urafiki wa zamani na kufanya rafiki wapya.

Mkusanyiko wa kimataifa uliofanywa katika Nepstadion katika Budapest, Julai 26 hadi 28, ulikuwa na wajumbe waliozuru kutoka nchi 35. Ni miaka miwili tu iliyokuwa imepita, tangu Juni 1989, Mashahidi wa Yehova walipotambuliwa kisheria. Kwa kutofautiana, miaka michache iliyopita, wakati ambao stediamu hiyo ilikuwa inajengwa, wengine wa akina ndugu walikuwa gerezani kwa sababu ya itikadi zao za kidini. Walinzi wa jela walijigamba wakiwaambia: “Hamtaona stediamu hii kamwe.” Mmoja wa ndugu zetu akajibu: “Ni nani ajuaye? Labda siku moja Mashahidi wa Yehova watakuwako huko.” Kwa sababu ya maneno hayo, alipigwa. Lakini ndugu huyo alikuwa mwenye furaha jinsi gani kuwako kwenye mkusanyiko huu na kuona stediamu ikiwa imejaa wahudhuriaji zaidi ya 40 elfu!

Mikusanyiko ilifanywa waziwazi kwa mara ya kwanza katika Urusi. Tallinn, jiji la pwani lililo katika taifa huru la Estonia, liliandalia baadhi ya waliohudhuria mkusanyiko kikao kisichotarajiwa. Kutoka sehemu hiyo ambapo watu 447 walibatizwa, akina ndugu na dada wangeweza kuona boma la zamani ambalo katika 1950 na 1951 lilitumiwa kuwa gereza la muda kwa wengine wao walipokuwa wakingoja zamu yao ili wapelekwe kwenye kambi za magereza katika Siberia ya mbali. Hivyo, kumbukumbu zenye kuleta fikira nzito ziliamshwa mara kwa mara katika wakati huu wa kushangilia sana.

Kuwekwa Wakfu kwa Matawi: Mlango Mwingine wa Fursa Ulio Wazi

“Heri wakaao nyumbani mwako, wanakuhimidi daima,” wakaimba wana waaminifu wa Kora. (Zab. 84:4) Leo, majengo ya tawi hufungua milango ya fursa kuendeleza ibada ya Yehova. Na wakati jengo jipya linapowekwa wakfu, ni fursa ya pekee ya kuimba sifa kwa Yehova.

Fiji

Jumanne, Desemba 25, 1990, ilikuwa siku yenye hali ya kitropiki yenye uzuri na joto katika Suva, mji mkuu wa Fiji. Maelfu walikusanyika kwenye programu ya kuwekwa wakfu kwa ofisi ya tawi iliyomalizwa karibuni pamoja na mpanuo wa makao. Fiji ina visiwa zaidi ya 800, ambavyo kati yavyo, mia moja hivi vinakaliwa. Fiji ni makao ya watu zaidi ya 736,000, wanaojulikana kwa tabasamu zenye kuambukiza na ukaribishaji wenye fadhili. Haikuwa mpaka mwaka 1913 ndipo Shahidi wa Yehova wa kwanza alipowasili Fiji. Kufikia miaka ya 1930, kulikuwa na kikundi kidogo tu cha familia tatu kilichofanya mikutano katika Suva. Katika 1940 kazi ilipigwa marufuku kisheria. Baada ya Vita ya Ulimwengu ya 2, marufuku iliondolewa. Hivyo, njia ilifunguliwa kwa wamisionari wa kwanza wa Gileadi kuingia Fiji mnamo Aprili 5, 1947, ili kufanya kazi pamoja na wahubiri 12 waliokuwa watendaji katika utumishi.

Katika 1957, Len Helberg, anayeishi sasa katika Australia, pamoja na Len Heatley, painia wa sehemu hiyo, walipelekwa kwenye Shule ya Gileadi. Baada ya kurudi Fiji mwaka mmoja baadaye, ofisi ya tawi ilifunguliwa katika Suva. “Sisi hatukufikiri lilikuwa tawi siku hizo,” akumbuka Ndugu Heatley. “Tuliliita ‘kitawi.’” Ndugu Helberg akaongeza: “Lakini Yehova alijua alichokuwa anafanya.” Kulikuwa na kundi moja katika Suva miaka ya mwisho-mwisho ya 1940, lakini sasa habari njema zimeenea kotekote katika Pasifiki ya Kusini, hivi kwamba leo kuna ofisi za tawi katika New Caledonia, Tahiti, na Samoa ya Magharibi pia.

Lyman Swingle wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya wakfu kwa watu 434 waliohudhuria mahali penyewe pa tawi na kwa wengine zaidi 3,489 kwenye stediamu iliyokuwa karibu ikiwa imeunganishwa kwa kamba za simu ili kusikia programu ya siku hiyo. Kwa kufikiria kwamba kuna wahubiri wasiozidi 1,600 katika Fiji, hilo lilikuwa hudhurio zuri sana! Jioni hiyo, akina ndugu Wafiji walitumbuiza wajumbe wengi kwa tamasha za kuimba na kucheza dansi kwa saa mbili.

Ugiriki

Aprili 13, 1991, tarehe iliyokuwa imewekwa kwa ajili ya kuwekwa wakfu kwa majengo mapya ya tawi yaliyokuwa katika Eleona, sehemu ya mashambani kilometa 64 kaskazini mwa mji mkuu Athene, ilikuwa siku ya maana sana kwa makundi 334 ya Mashahidi wa Yehova katika Ugiriki.

Siku ya kuweka wakfu ilipambazuka ikiwa na mawingu yaliyotanda. Ilionekana kuwa mvua ingenyesha. Lakini mawingu yaliyokuwa yakishuka hayangeweza kuondosha uzuri na utulivu wa zulia la kijani kibichi la mashamba ya shayiri yaliyozunguka sehemu ya hekta 22 yenye madoadoa ya maua ya popi yaliyo mekundu kama damu na maua ya deizi manjano. Wawakilishi wa makundi mbalimbali walipoanza kuwasili, mvua pia iliwasili, lakini hilo halikuzima roho ya shangwe ya watu 3,815 waliokuwapo. Programu ya wakfu ilipitishwa pia kwa simu kwenye viwanja vya mikusanyiko karibu na Athene na Thesalonike na katika kisiwa cha Krete. Muunganisho huu wa simu ulipatanisha jumla ya watu 13,484.

Mkusanyiko wa kwanza katika Ugiriki ulifanywa miaka 66 iliyopita, katika 1925. Hata hivyo, kanisa la Orthodoksi la Ugiriki bado linapinga Mashahidi kwa bidii, kama kwamba ni dini mpya. Makasisi hata walipanga maandamano nje ya makao katika Eleona wakati wa ujenzi wa tawi. Polisi wa kupambana na ghasia walikuwako ili kuweka utengamano na kulinda mali hiyo. Upinzani huo ukawaendea kinyume wapinzani wenyewe—mradi huo ulimalizwa miezi sita kabla ya wakati ulioratibiwa.

Washiriki wawili wa Baraza Linaloongoza, Milton Henschel na Albert Schroeder, walikuwako kwenye programu ya kuweka wakfu. Siku hiyo iliisha kwa mlo wa familia ya Betheli na ya ujenzi, pamoja na wajumbe waliokuja Ugiriki kwa ajili ya tukio hilo. Wageni walifurahia dansi za kienyeji za Kigiriki zilizochezwa na ndugu na dada.

Hong Kong

Januari 1, 1980, ofisi ya tawi ilihama kutoka kwenye jengo dogo kwenda kwenye jingine kubwa zaidi lisilo na kelele kwenye 4 Kent Road nje ya Kowloon Tong. Makao hayo yangetumikia mahitaji ya tawi vema sana kwa muda wa miaka minane. Ndipo wakati ukafika wa upanuzi zaidi. Kwa wakati ufaao kabisa jengo zuri linalofaa kwa ofisi ndogo ya tawi pamoja na Makao ya Betheli lilipatikana kwenye 12 Kent Road, nalo likanunuliwa. Hata hivyo, baada ya miaka mitatu tu, ikawa wazi kwamba mahali pengine pangehitajiwa upesi. Yehova akaandaa tena.

Alasiri moja, padri Mkatoliki aliyeishi kwenye 16 Kent Road aliambia mratibu wa Halmashauri ya Tawi hivi, “Rafiki zetu wameenda.” Alikuwa anarejezea familia moja ya Wachina ambao 14 Kent Road ilikuwa mali yao. Familia hiyo ilikuwa imehama mwisho-juma huo, na nyumba yao ilikuwa iuzwe. Ilifaa sana. Makao yetu ya tatu kwenye 14 Kent Road ni nyongeza nzuri sana kwa makao yetu mengine kwenye nambari 4 na 12. Hilo ni jengo jeupe la orofa mbili, lililoimarishwa kwa saruji. Familia ya Betheli sasa ni 19, na kuna nafasi ya 30.

Januari 15, 1991, ndiyo jioni iliyowekwa kando kwa kuwekwa wakfu kwa jengo hilo la nyongeza. Lloyd Barry, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya wakfu, “Yehova Hufanya Iendelee Kukua.” Yeye anafahamu Hong Kong, akiwa amezuru huko katika 1956 pamoja na Nathan H. Knorr, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo. Ndugu Barry amezuru tawi hilo mara nyingi tangu wakati huo, akitumika akiwa mwangalizi wa eneo la dunia. Hotuba yake ilifuatia historia ya kazi kutoka mianzo ya mapema hadi leo, wakati kuna wahubiri 2,320 katika makundi 23 katika Hong Kong.

New Caledonia

Katika upande wa kusini-magharibi mwa Bahari ya Pasifiki kuna New Caledonia—“Kisiwa cha Nuru.” Kisiwa hicho kina sehemu za asili zenye uzuri wa ajabu ambazo nyakati zote zimekuwa makao yapendwayo na wasanii na ambazo ni kichocheo kwao. Katika miaka ya karibuni, watu wengi zaidi na zaidi wametafuta nuru iletayo uzima wa milele.—1 Yn. 1:5.

Tangu 1977 ofisi ya tawi imekuwa kwenye makao ya wamisionari. Vyumba viwili vya kulala vilibadilishwa kuwa ofisi kwa utumizi wakati wa mchana. Kutafsiri, kupanga maandishi, na kuchapa, pamoja na kushughulikia na kusafirisha vichapo, vyote vilifanywa katika sehemu yenye eneo la meta karibu 100 za mraba! Hilo laeleza sababu ya Baraza Linaloongoza kukubali ujenzi wa jengo jipya la Betheli lenye eneo la zaidi ya meta 1,200 za mraba. Lina vyumba sita vya kulala na liko katika Nouméa, mji mkuu wa New Caledonia. Uchimbuzi wenyewe ulianza Januari 1989.

Kikundi kidogo cha wahubiri 9 kilichokuwako huko nyuma katika 1956 kimekua kikawa 1,265. Kutia ndani Mashahidi wanaoishi katika New Caledonia, Vanuatu, na Visiwa vya Wallis na Futuna, ofisi ya tawi sasa inashughulikia mahitaji ya wahubiri zaidi ya 1,400. Katika Desemba 15, 1990, wasikilizaji zaidi ya 2,700 walifurahi kusikia hotuba ya wakfu ya mwakilishi kutoka makao makuu ya Sosaiti katika Brooklyn, ambaye alikuwa akitumikia akiwa mwangalizi wa eneo la dunia. Baada ya programu, akina ndugu kutoka visiwa mbalimbali walianza programu ya muziki kwa nyimbo za Ufalme na dansi za kienyeji.

Ufilipino

Katika 1972, wakati tawi lilipopanuliwa kwa mara ya mwisho, kulikuwako wahubiri 54,212 katika Ufilipino. Kufikia wakati ujenzi wa tawi jipya ulipoanza katika Mei 1988, idadi ya wahubiri ilikuwa imeongezeka kuwa zaidi ya 97,000.

Mavuno ya kiroho yalianza wakati ujumbe wa habari njema uliposikiwa kwa mara ya kwanza katika Januari 14, 1912, katika Jumba Kuu la Muziki la Manila. Charles T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Sosaiti, alitoa hotuba “Wafu Wako Wapi?” akihutubia watu karibu elfu moja. Mbegu hizi za kweli za mapema zilizaa matunda pole kwa pole, na kufikia 1930 darasa la kawaida la Biblia kila juma lilikuwa linaongozwa, watu kumi hivi wakihudhuria. Betheli ya kwanza ya Ufilipino ilikuwa kwenye jumba lililokodishwa, lililoanza kutumiwa katika Juni 1934. Kiwanja cha kwanza ambapo sasa pana ofisi ya tawi katika Jiji la Quezon kilinunuliwa Desemba 1947, na jengo lililokuwa hapo likaanza kutumiwa likiwa ofisi ya tawi katika Februari 1948. Majengo zaidi yalijengwa kwenye kiwanja cha kwanza cha hektari moja katika 1953, 1962, na 1972.

Kukiwa na ukuzi wa wahubiri wakati wa miaka ya 1970, kulikuwa na uhitaji halisi wa ‘kutandaza mapazia ya hema’ la tawi. (Isa. 54:2) Hapo mbeleni, majirani waliulizwa kama wangependa kuuza sehemu yoyote. Hakuna aliyetaka wakati huo. Kwa kweli, jirani mmoja alisema: “Wachina hawauzi mali yao. Wao hununua tu.” Kwa kustaajabisha, majirani waliokuwa wamekataa hapo mbeleni kuuza mali zao baada ya kuulizwa na Sosaiti, walianza kuuza mali na nyumba zao mmoja baada ya mwingine. Kwa muda wa miaka sita, viwanja kumi vilinunuliwa, hivyo mali ya Sosaiti ikawa mara tatu zaidi.

Ujenzi wa kiwanda cha orofa 2 na Makao ya Betheli ya orofa 11 ulianza Mei 1988. Watumishi wa kimataifa na wenyeji wenye kujitolea waliungana kwa uchangamfu katika ujenzi wa tawi hilo jipya. Tawi la Japani lilisaidia kwa michoro kutoka kwa idara yao ya uhandisi na pia kwa michango ya kifedha kuongezea ile michango ya ndugu Wafilipino.

Mwongozo wa Yehova ulionwa mara nyingi. Kwa mfano, wakati akina ndugu walipokuwa wakitaka kununua vifaa vya kufanyizia paa na sakafu, waligundua kwamba ni kampuni moja tu katika Ufilipino iliyoshughulika na aina ya muundo wa vifaa walivyotaka. Hata hivyo, ujenzi huo wa tawi ulikuwa mteja namba 301 kwenye orodha ya kungojea ya kampuni hiyo. Mwadi ulifanywa ili kusema moja kwa moja na makamu wa msimamizi wa kampuni hiyo, na ikaelezwa kwamba kazi yetu ni ya kujitolea. Halmashauri ya wakurugenzi ya kampuni hiyo ilikubali ombi letu, na agizo la tawi lilisogezwa hadi namba 1 kwenye orodha. Hilo lilikuwa uongozi wa kimungu kwani, muda tu baada ya kutukabidhi vifaa hivyo, wafanyakazi wa kampuni hiyo waligoma.

Aprili 13, 1991, ilipambazuka ikiwa yenye kuangaza na kutakata. Wasikilizaji zaidi ya 1,718 walikuwa na furaha ya kumkaribisha John E. Barr wa Baraza Linaloongoza kwa hotuba ya wakfu. Kichwa cha hotuba yake kilikuwa nini? “Wimbo wa Ongezeko la Kitheokrasi.” Kilikuwa kichwa chenye kufaa kama nini, si kwa kuwekwa wakfu kwa tawi hilo tu bali pia mengine yote.

[Chati katika ukurasa wa 22]

Mikusanyiko Iliyofanywa Katika Urusi na Estonia

Tarehe Jiji Hudhurio Waliobatizwa

Julai 13, 14 Tallinn, Estonia 4,808 447

Julai 20, 21 Usolye-Sibirskoye, Siberia 4,205 543

Agos. 2, 3 Kiev, Ukrainia 14,654 1,843

Agos. 3, 4 Lvov, Ukrainia 17,531 1,316

Agos. 24, 25 Odessa, Ukrainia 12,115 1,943

Agos. 31–Sep. 1 Chernovtsy, Ukrainia 14,137 1,126

Sep. 7, 8 Alma-Ata, Kazakhstan 6,802 602

Jumla Kuu: 74,252 7,820

(Kwa kustaajabisha jumla ya waliobatizwa ni asilimia 10.5 ya jumla ya kilele cha hudhurio.)

[Grafu katika ukurasa wa 18]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Mwendeleo wa Uchapishaji Sawia

Mnara wa Mlinzi Lugha Zinazochapishwa Lugha Zinazochapishwa Sawia

Mwaka

1980 106 0

1985 103 24

1991 110 65

Hesabu ya Lugha

140 120 100 80 60 40 20 0

Amkeni! Lugha Zinazochapishwa Lugha Zinazochapishwa Sawia

Mwaka

1980 34 0

1985 54 14

1991 64 30

Hesabu ya Lugha

70 60 50 40 30 20 10 0

Uchapishaji Sawia Hunufaisha Asilimia 95 ya Mashahidi wa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 5]

Mwaka jana, watu 10,650,158 ulimwenguni pote walihudhuria mwadhimisho wa kila mwaka wa Chakula cha Bwana cha Jioni

[Picha katika ukurasa wa 12]

Wengi wa wahitimu wa madarasa manane yaliyofanywa mwaka huu sasa wanatumika katika zile nchi sita ambamo shule hiyo imefanyiwa, lakini wengine wameanza migawo katika nchi zifuatazo: Austria, Benini, Kanada, Chekoslovakia, Chadi, Côte d’Ivoire, Hondurasi, Hangari, Ailandi, Uholanzi, New Caledonia, Ureno, na Romania. Linaloonyeshwa juu ni darasa la kwanza katika Ufaransa na katika Ujerumani

[Picha katika ukurasa wa 13]

Watumishi wa huduma na wazee wote waliohitimu shule hiyo mwaka huu wamepewa migawo ya mapendeleo mbalimbali ya utumishi. Ikitegemea ujuzi wao wa hapo kwanza na ustahili wao wa sasa, huo watia ndani migawo ya upainia wa pekee, utumishi wa misionari, kazi ya mzunguko, na kazi katika ofisi ya tawi. Linaloonyeshwa juu ni darasa la kwanza katika Italia na la kwanza katika Uhispania

[Picha katika ukurasa wa 20]

Mjumbe huyu mchanga wa Polandi alikuwa miongoni mwa 74,587 waliohudhuria kusanyiko katika Prague, Chekoslovakia

[Picha katika ukurasa wa 21]

Wakusanyikaji wa Prague walitokwa na machozi wakati Biblia ya New World Translation ilipotolewa na A. D. Schroeder katika lugha za Kicheko na Kislovakia

Kulikuwa na mikusanyiko ya kimataifa katika Budapest, Prague, na Zagreb. Wajumbe katika Zagreb, Yugoslavia, walishangilia kuimba nyimbo za Ufalme wakati wa mapumziko ya mchana

[Picha katika ukurasa wa 22]

Tallinn, Estonia, ambayo sasa ni huru, ndiyo mahali palipofanyiwa mkusanyiko wa kwanza kabisa usiopata kufanywa kamwe katika Urusi

Kitabu “Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi” kilitolewa katika lugha ya Kirusi na katika lugha nyinginezo za Ulaya ya Mashariki

[Picha katika ukurasa wa 27]

Fiji

Tawi la Fiji katika Suva, iliyo jiji kuu, liliwekwa wakfu Desemba 25, 1990. Sehemu ya kupokelea wageni imepambwa ifaavyo

[Picha katika ukurasa wa 27]

Ugiriki

Majengo mapya ya tawi ya Ugiriki yaliyo katika Eleona yaliwekwa wakfu Aprili 13, 1991

[Picha katika ukurasa wa 28]

Ua wa upande wa kuingilia wa tawi jipya la Ugiriki

[Picha katika ukurasa wa 28]

Sehemu ya kupokelea wageni katika tawi la Ugiriki iko tayari kupokea wageni

[Picha katika ukurasa wa 28]

Hong Kong

Sehemu mpya iliyoongezwa kwenye jengo la tawi katika Hong Kong iliwekwa wakfu Januari 15, 1991

[Picha katika ukurasa wa 29]

New Caledonia

Jengo la tawi kule New Caledonia katika Nouméa, jiji kuu la New Caledonia, liliwekwa wakfu Desemba 15, 1990

[Picha katika ukurasa wa 29]

Ufilipino

Aprili 13, 1991, ndiyo iliyokuwa tarehe ya kuwekwa wakfu kwa Majengo-tata mapya ya tawi katika Manila, yenye jengo la ofisi na jengo la makao lenye orofa 11. Sehemu ya kupigia chapa iko upande wa mbali kulia

[Picha katika ukurasa wa 30]

Jumba la Ufalme lenye viti 500 katika ofisi ya tawi ya Ufilipino

[Picha katika ukurasa wa 30]

Chumba cha kulia chenye nafasi ya watu 400 kwenye Makao ya Betheli katika Ufilipino

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki