Finding Happiness—But Where?
YESU alisema: “Wenye furaha ni wale wajuao uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3, NW) Msichana mchanga mwenye moyo mweupe katika Maghariki ya Kati aliona uhitaji wake wa kiroho na alikuwa akitafuta kupendeza Mungu. Hatimaye, alipata furaha—lakini wapi? Tutamwacha aeleze.
“Mimi nililelewa katika jamaa yenye kufuata sana dini ya Umaroni wa Kikatoliki. Sisi watoto tulizoezwa kusali kila jioni mbele ya sanamu, na kutoka utoto mchanga nilikuwa na tamaa ya kutumikia Mungu.
“Nikiwa na umri wa miaka 17, niliingia konventi ili niwe mtawa wa kike, nikifikiri kwamba jambo hili lingetosheleza tamaa yangu. Hata hivyo, niliona mambo mengi miongoni mwa watawa wa kike ambayo yalinisumbua. Walipiga porojo juu ya mmoja na mwenzake. Wanafunzi hawakupewa chakula cha kutosha, hali watawa wa kike waliona shangwe ya kuwa na chakula bora zaidi. Na kulikuwa na mazoea yasiyo ya adili kati ya watawa wa kike na padri. Kwa kutamauka kwa uchungu mwingi, niliondoka konventi baada ya miezi tisa nikarudi nyumbani.
“Bado nilikuwa na maswali mengi yasiyojibiwa, na nilipokuwa siwezi kupata majibu ya kuridhisha, nilifikia hatua ya kutojali dini. Halafu, katika 1982, nilipokuwa na miaka 22, ndugu na dada yangu wa kimnofu walijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Wazazi wangu na mimi waliwapinga. Ndugu yangu alipata mnyanyaso mwingi, mapigo, na kutiwa gerezani kwa sababu ya imani yake mpya. Ingawa hivyo, kilichonivutia ni mabadiliko makubwa aliyofanya maishani mwake. Zaidi ya hilo, alitoa majibu ya Biblia yaliyo ya kiakili kwa maswali niliyokuwa nimekuwa nikiuliza kwa muda mrefu. Kwa hiyo mimi nikaanza kujisomea Biblia kwa siri wakati wa usiku.
“Siku moja niliambatana nikaone kusanyiko la Mashahidi wa Yehova. Nilivutwa na upendo ulioonyeshwa huko. Hakukuwa na tofauti kati ya tajiri na maskini. Mashahidi huishi kwa upatano na mambo wafundishayo. Nilisadikishwa kwamba wao ndio wenye ukweli.
“Mara tu baada ya kusanyiko, niliomba mmoja wao ajifunze nami. Niliambia mwanamke huyo kwamba nilitaka kujifunza tu, si kuhudhuria mikutano wala kwenda kuhubiri. Hata hivyo, upesi nikang’amua kwamba nilikuwa ninajifunza ukweli. Nilisali na kuamua kutumikia Yehova. Siku ya Oktoba 28, 1983, ndugu yangu, dada yangu, na mimi tulibatizwa. Sasa nilikuwa nimeipata njia ya kuridhisha tamaa ya kutumikia Mungu ambayo nilikuwa nimekuwa nayo kutoka utoto mchanga.
“Miezi miwili baada ya ubatizo, nilianza upainia msaidizi, na miezi minane baadaye nikawa painia wa kawaida. Mwaka mmoja na nusu baadaye, nilialikwa kutumikia kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova, ijulikanayo kuwa Betheli, na kwa muda tu nikafanya hivyo kwa miaka miwili. Nilivutwa na unyenyekevu ulioonyeshwa na wote. Ndugu wenye madaraka zaidi hata walishiriki kazi ya kuosha vyombo baada ya chakula cha jioni.
“Siku ya Machi 14, 1988, nikawa mshiriki wa kudumu wa jamaa ya Betheli. Lo, ilikuwa pindi yenye furaha kama nini! Ndiyo, nilipata furaha. Wapi? Miongoni mwa Mashahidi waliojiweka wakfu wa Yehova! Sasa mimi nahisi kama mtunga zaburi aliyesema: ‘Siku moja katika nyua zako ni bora kuliko elfu mahali kwingineko.’”—Zaburi 84:10, NW.