“Wote Wale Walio Katika Maziara ya Ukumbusho”
JE! WAWEZA kuwa na uhakika kwamba walio wengi kati ya wafu wataishi tena? Ndiyo, kwa kuwa Yesu alisema: “Msione hili kuwa ajabu, kwa sababu ile saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale walio katika maziara ya ukumbusho watasikia sauti yake na kutoka nje.” (Yohana 5:28, 29, NW) Angalia usemi “maziara ya ukumbusho,” ambao ni wa aina yake katika New World Translation. Hutukumbusha umaana wa kumbukumbu la Mungu katika ufufuo.
Kwa nini ule ufasiri wa kawaida, ‘makaburi,’ hautumiwi? Kwa sababu Yesu hakutumia wingi wa neno la Kigiriki taʹphos, ambalo humaanisha “kaburi” au “ardhi ya kuzikia.” Kwa kweli, si wote waliopata kufa ambao walizikwa katika makaburi halisi, au taʹphoi. Hata hivyo, wale ambao Mungu atarudisha katika ufufuo wamo katika kumbukumbu lake. Hiyo yaonyeshwa na utumizi wa Yesu wa namna ya wingi ya mne·meiʹon, ambayo yahusiana karibu-karibu na maneno ya Kigiriki ambayo kwa msingi humaanisha “kukumbuka.” (Mathayo 16:9; Marko 8:18) Greek-English Lexicon ya H. G. Liddell na R. Scott hutafsiri mne·meiʹon kuwa “ukumbusho,” ukumbuko, rekodi ya mtu au kitu, . . . ziara, . . . kwa ujumla, nguzo ya ukumbusho.”
Hivyo, New World Translation hutofautisha kati ya maneno taʹphos na mne·meiʹon. Pia yastahiki kuangalia kwamba tafsiri nyingi za Biblia hutumia vivyo hivyo semi mbili tofauti kwenye Mathayo 23:29 ambapo mitajo yote miwili ya Kigiriki huonekana. Revised Standard Version huifasiri ifuatavyo: “Nyinyi hujenga maziara [namna ya taʹphos] ya manabii na kuremba nguzo za ukumbusho [namna ya mne·meiʹon] za waadilifu.”
Muumba mwanadamu hasahau vigezo vya maisha vya maelfu ya mamilioni ya wanadamu ambao wameishi. (Zaburi 139:16; 147:4; Mathayo 10:30) Katika wakati wake ufaao, yeye atakumbuka wale walio katika “maziara ya ukumbusho” na kuwarudisha kwenye uhai katika dunia iliyosafishwa. Sisi twatiwa moyo na kufarijiwa kama nini kwa kujua kwamba kumbukumbu kamilifu la Mungu haliwezi kuwa la bure!—Ufunuo 20:11-13.