Nani Ataongoza Ainabinadamu Kwenye Amani?
JE! UHAKIKA wa kwamba wanadamu hawawezi kuleta amani wamaanisha kwamba hatutaona amani kamwe? Sivyo. Kama vile Shetani, ambaye ni mwenye nguvu kuliko sisi, ndiye kipingamizi kikubwa zaidi cha amani duniani, kuna Mmoja mwenye nguvu kuliko hata Shetani ambaye mwishowe ataongoza ainabinadamu kwenye amani. Biblia, ambayo yaeleza juu ya Shetani, hueleza pia juu ya Mmoja huyu. Husema hivi: “Utawala wa kimwana-mfalme utakuja kuwa juu ya bega lake. Na jina lake ataitwa Mshauri wa Ajabu, Mungu Mwenye Uweza, Baba wa Milele, Mwana-Mfalme wa Amani.” (Isaya 9:6, 7, NW) Ni nani huyu Mwana-Mfalme wa Amani? Si mwingine ila Yesu Kristo, naye aweza kuleta amani kwa sababu ni mwenye ustahili mwingi kuliko sisi. Kwa njia zipi?
Zaidi ya Sifa za Kibinadamu
Kwanza, Yesu hana hali ya kufa, hayuko chini ya wajibu wa kufa. Ni kweli, yeye aliishi akiwa binadamu na akafa kifo cha dhabihu. Lakini ndipo alipofufuliwa kwenye uhai wa kimbingu usiokufa, na ni katika hali hii kwamba yeye huwa Mwana-Mfalme wa Amani. Ndiyo sababu unabii mmoja husema hivi: “Ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:32, 33) Tofauti na maliki Asoka wa Mashariki, Yesu ataishi bila mwisho ili ahakikishe kwamba kazi yake njema haiharibiwi na warithi walio duni.
Tena, dhambi hatiwi doa na dhambi. Utawala wake uko juu ya msingi wa hekima ya kimungu na kanuni zifaazo. Nabii Isaya alitabiri hivi: “Juu yake roho ya Yehova ni lazima itulie, roho ya hekima na ya uelewevu, roho ya shauri na ya uweza, roho ya maarifa na ya kuhofu Yehova . . . Yeye hatahukumu kwa mwonekano wowote tu kwenye macho yake, wala kukaripia kulingana na jambo lenye kusikiwa tu na masikio yake. Na kwa uadilifu ni lazima yeye ahukumu walio dhalili.” (Isaya 11:2-4, NW) Tofauti na Wanaulaya wa kipindi cha mapema kidogo, Yesu hatahifadhi amani nyumbani na kumbe afanye vita katika mabara ya kigeni. Chini yake, amani itakuwa ya ulimwengu wote mzima.
Zaidi ya hilo, Yesu ana uwezo wa kuleta amani. Unabii wasema hivi: “Roho ya Yehova . . . , roho ya shauri na ya uweza,” iko juu yake. Roho hiyo ilitumika katika uumbaji wa ulimwengu wote mzima na pia miujiza yote ya uadilifu iliyoripotiwa katika Biblia. Hata yule mpinzani mkubwa, Shetani, hana silaha zitakazokinza kwa mafanikio roho ya Mungu.
Hatua za Kwenye Amani
Yesu ataongozaje ainabinadamu kwenye amani? Huenda ukashangaa kujua kwamba tayari ameanza. Katika kitabu cha kinabii cha Ufunuo, Yesu aonwa akipokea kutoka kwa Mungu umaliki katika Ufalme wa kimbingu. (Ufunuo 11:15) Tukichunguza kwa ukaribu unabii wa Biblia na kuulinganisha na matukio katika karne yetu, twaona kwamba kupewa kwa Yesu kiti cha Mfalme kulitukia mbinguni kule nyuma katika 1914. (Mathayo 24:3-42) Hiyo ilikuwa hatua kubwa katika kuleta amani kwenye dunia.
Ingawa hivyo, ikiwa ndivyo ilivyo, kwa nini Vita ya Ulimwengu 1 ilifoka katika 1914? Na kwa nini karne yetu imeona vita vibaya kuliko nyingine yoyote katika historia? Kwa sababu kitendo cha kwanza cha Mfalme wa kimbingu kilikuwa kufukuzia mbali Shetani atoke katika mbingu kwa muda wote na kumtupa chini kwenye ujirani wa dunia. Tokeo? Unabii wasema: “Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” (Ufunuo 12:7-12) Vile vita vikubwa vya karne yetu vyahusiana na kasirani ya Shetani. Lakini angalia: Kasirani ya Shetani ni kwa “wakati mchache tu.” Karibuni hali mbaya iliyopo itamalizika!
Ingawa hivyo, kabla haijamalizika, Mwana-Mfalme wa Amani afanya matayarisho zaidi yaliyo muhimu kwa amani. Kwanza, ni lazima ainabinadamu ijue juu ya kusudi la Mungu kuleta amani kupitia Kristo. Kulingana na hilo, Yesu alitoa unabii kwamba katika wakati wetu “habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia nzima yote inayokaliwa kwa ajili ya ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14, NW) Katika utimizo wa jambo hili, habari njema zinahubiriwa leo na Mashahidi wa Yehova katika kila pembe ya tufe.
Halafu, wenye mioyo ifaayo ni lazima waelimishwe katika njia za amani. Biblia huahidi hivi: “Watoto wako wote watafundishwa na BWANA [Yehova, NW]; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.” (Isaya 54:13) Mamilioni ya wenye mioyo ifaayo wanapokea elimu hii hata sasa.
Hatua Ifuatayo
Sasa ni karibu wakati wa hatua nyingine ya kukata maneno katika ule utaratibu wa kufanyiza amani. Ni nini hiyo? Ni moja ambayo wengi waijua kwa jina lakini ni wachache wajuao kusudi halisi. Biblia yaiita “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi,” au Har-Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Wengi hufikiria Har-Magedoni ni vita ya nyukilia itakayoharibu utamaduni. Kinyume cha hivyo, ni kitendo cha moja kwa moja chenye kufanywa na Yesu, Mwana-Mfalme wa Amani, ili kutimiza mambo yaliyo muhimu kwa amani.
Kwanza, Har-Magedoni itaondoa vipingamizi vyote vya kibinadamu vyenye kuzuia amani. Unabii kwenye Zaburi 37:10 husema: “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo.” Ndiyo, Yesu ataondoa kutoka kwenye mandhari ya kidunia “asiye haki”—wafanyiza vita, wahalifu, wavamizi-haramu, na pia wale ambao hukataa kumpokea Mwana-Mfalme wa Amani aliye mkubwa. Hawatakuwa tena na haki ya kuendelea kuishi katika sayari hii.—Ufunuo 19:19-21.
Pili, kwenye Har-Magedoni unabii huu wa Danieli utatimizwa: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharihu, nao utasimama milele na milele.” (Danieli 2:44) Migawanyiko ya kitaifa ambayo mara nyingi imeongoza kwenye vita itakomeshwa. Mwishowe, kutakuwako serikali ya ulimwengu chini ya mtawala ambaye sisi twaweza kutegemea!
Har-Magedoni itakuja lini? Biblia haisemi. Lakini matukio ya ulimwengu yenye kutimiza unabii wa Biblia yaonyesha ni karibuni sana. Biblia hutabiri wazi tukio moja ambalo litakuwa utangulizi kabla tu ya jambo hilo. Mtume Paulo husema: “Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula.” (1 Wathesalonike 5:3) Halafu, mara tu baada ya uharibifu wa ghafula wenye kufikia upeo kwenye Har-Magedoni, kipingamizi kilicho kikubwa zaidi kwa amani kitaondolewa. “Wakati mchache” wa Shetani utakuwa umeisha, naye atatiwa katika hali ambamo hawezi tena kusababisha matata hapa duniani. (Ufunuo 20:1-3) Lo, ni kitulizo kilichoje!
Ulimwengu Wenye Kukaa kwa Amani
Piga picha ya hali wakati huo. Mtunga zaburi alitoa unabii hivi: “Wenye upole [wasikivu, NW] watairithi nchi [dunia, NW], watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:11) Wasikivu hawa wataendelea kutimiza unabii mzuri wa Isaya: “Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isaya 2:4.
Hatimaye, kwa mara ya kwanza tangu Edeni, wanadamu wote walio hai wataona shangwe ya baraka ya Yehova Mungu, naye atatimiza ahadi yake: “Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:3, 4.
Tumaini Thabiti
Basi, nani ataongoza ainabinadamu kwenye amani? Yesu Kristo, Mwana-Mfalme wa Amani aliyewekwa. Je! hili ni tumaini lenye kutumika kwetu leo? Basi, kama ahadi za Biblia zingekuwa hazitegemeki, hakungekuwa na tumaini halisi la amani. Wanadamu wangeendelea kupigana na kuuana bila tazamio la kukoma. Lakini Biblia ni yenye kutegemeka, na Ufalme wa Mungu chini ya Kristo utaleta amani. Sisi twakutia moyo usikilize habari njema za Ufalme ambazo Mashahidi wa Yehova huleta nyumbani kwako na ujionee mwenyewe jambo hilo. Halafu wakati huo ujapo, wewe na uwe miongoni mwa wasikivu ambao watarithi dunia na kujifurahisha katika wingi wa amani.
Tumaini la amani lililozungumzwa katika makala hii ni kutoka katika Biblia. Leo, wakati ambapo wengi hawaiamini tena Biblia, huenda wewe ukatia shaka kama tumaini hili laweza kutumika. Mashahidi wa Yehova huamini kwa imara kwamba ndivyo lilivyo. Wao huipokea Biblia kuwa Neno la Mungu lililovuviwa, na hivyo yenye kutumainika kabisa. Katika 1989 walitangaza chapa ya kitabu chenye kichwa The Bible—God’s Word or Man’s? kikitoa ithibati nyingi za uhakika huo. Baadhi ya habari zilizo katika kitabu hicho zimezungumzwa katika makala mbili zinazofuata, ambazo sisi twakualika wewe kusoma.
Habari zaidi juu ya ahadi ya Biblia ya amani itatokea katika makala “Amani ya Ulimwengu—Itamaanisha Nini Hasa?” ambayo itatangazwa katika toleo la Aprili 15, 1990 la Mnara wa Mlinzi.
[Blabu katika ukurasa wa 8]
Yesu peke yake ndiye mwenye sifa za kuongoza ainabinadamu kwenye amani
[Blabu katika ukurasa wa 9]
Leo, habari njema za Ufalme zinahubiriwa katika kila kona ya tufe