Tafuta Sana Amani ya Kweli na Kuifuatia!
“Yeye ambaye angependa uhai na kuona siku zilizo njema, . . . acheni ageuke mbali kutoka lililo baya na kufanya lililo jema; acheni atafute sana amani na kuifuatia.”—1 PETRO 3:10, 11.
1. Ni maneno gani ya Isaya yajulikanayo sana ambayo yatafanikiwa kwa hakika?
“WATAFUA panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena.” (Isaya 2:4) Hata ingawa andiko hili lijulikanalo sana linaonyeshwa karibu na makao makuu ya Umoja wa Mataifa katika Jiji la New York, shirika hilo la ulimwengu halitimizi maneno hayo hata kidogo. Hata hivyo, likiwa sehemu ya neno la Yehova Mungu lisiloshindwa kufaulu, tangazo hilo halitakuwa bila matokeo.—Isaya 55:10, 11.
2. Ni jambo gani lazima litukie “katika siku za mwisho,” kulingana na Isaya 2:2, 3?
2 Maneno yanayopatikana kwenye Isaya 2:4 kwa kweli ni sehemu ya unabii mzuri ajabu, unabii juu ya amani ya kweli—nao unatimizwa katika wakati wetu wenyewe. Kabla ya kupiga mbiu ya matumaini juu ya kutokuwa na vita tena wala silaha za vita, unabii huo wasema: “Itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya BWANA utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa BWANA nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la BWANA katika Yerusalemu.”—Isaya 2:2, 3.
Watu Waweza Kupata Kuwa Wenye Kufanya Amani
3. Mtu aweza kubadilikaje kutoka kuwa mtaka-vita hadi kuwa mwenye amani?
3 Angalia kwamba kabla ya watu kuweza kufuatia mwendo wenye amani, lazima waagizwe kwa njia za Yehova. Itikio la kutii ufundishaji wa Yehova laweza kubadili njia ambayo mtu anafikiri na kutenda, hivi kwamba mtu ambaye amekuwa mtaka-vita apata kuwa mwenye kufanya amani. Mgeuzo umbo huo unatimizwaje? Waroma 12:2 lasema hivi: “Komeni kufanyizwa kulingana na mtindo wa mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe umbo kwa kufanya upya akili yenu, ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” Tunafanya upya akili yetu, au tunaihamasisha kuelekea njia tofauti, kwa kuijaza na kanuni na amri kutoka Neno la Mungu. Funzo la ukawaida la Biblia latusaidia kufanya badiliko hilo na latuwezesha kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Yehova kwetu, ili tuweze kuona kwa wazi njia ambayo ni lazima twende.—Zaburi 119:105.
4. Mtu anavaaje ule utu mpya wa kuwa mwenye kufanya amani?
4 Kweli ya Biblia hugeuza umbo kigezo chetu cha kufikiri na pia matendo yetu na utu wetu. Hiyo yatusaidia kufanya vile mtume Paulo alivyosihi sana: “Mweke mbali utu wa hapo zamani unaofuatana na njia yenu ya kwanza ya mwenendo na ambao unafisidiwa kulingana na tamaa zake za udanganyifu; bali . . . mfanywe upya katika kani inayotendesha akili yenu, na mvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.” (Waefeso 4:22-24) Kani inayotendesha akili ni ya ndani. Inageuzwa umbo na inapata kuwa yenye nguvu huku kumpenda kwetu Yehova na amri zake kunapoongezeka, na inatufanya tuwe watu wa kiroho na wenye kufanya amani.
5. “Amri mpya” ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake inachangiaje amani miongoni mwao?
5 Uhitaji wa mgeuzo umbo huo unaonwa kutokana na agizo ambalo Yesu aliwapa wanafunzi wake katika saa zake za mwisho pamoja nao: “Mimi ninawapa nyinyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile nimewapenda nyinyi, kwamba nyinyi pia mpendane. Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yohana 13:34, 35) Upendo huo ulio kama wa Kristo, usio na ubinafsi huwaunganisha wanafunzi pamoja katika muungano mkamilifu. (Wakolosai 3:14) Ni wale tu walio tayari kukubali na kuishi kulingana na “amri [hiyo] mpya” watakaofurahia amani ambayo Mungu aahidi. Je, kuna watu wowote wafanyao hivyo leo?
6. Kwa nini Mashahidi wa Yehova hufurahia amani, tofauti na watu wa ulimwengu?
6 Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuonyesha upendo katika udugu wao wa ulimwenguni pote. Ingawa wametolewa katika mataifa yote ya ulimwengu, hawashiriki katika ubishi mbalimbali wa ulimwengu, hata wanaposongwa sana kisiasa na kidini. Wakiwa watu wenye muungano, wanafundishwa na Yehova, na wanafurahia amani. (Isaya 54:13) Wanabaki wakiwa na hali ya kutokuwamo katika mapambano ya kisiasa, hawashiriki katika vita. Watu fulani waliokuwa wajeuri hapo zamani wameacha mtindo-maisha huo. Wamepata kuwa Wakristo wapendao amani, wakiiga kielelezo cha Kristo Yesu. Nao hufuata kwa moyo wote shauri hili la Petro: “Yeye ambaye angependa uhai na kuona siku zilizo njema, acheni azuie ulimi wake kutokana na lililo baya na midomo yake isiseme udanganyo, lakini acheni ageuke mbali kutoka lililo baya na kufanya lililo jema; acheni atafute sana amani na kuifuatia.”—1 Petro 3:10, 11; Waefeso 4:3.
Wale Wanaoifuatia Amani
7, 8. Toa vielelezo vya watu walioacha vita wakawa wenye kutafuta sana amani ya kweli. (Simulia vingine ambavyo huenda ukavijua.)
7 Kwa kielelezo, kuna Rami Oved, aliyekuwa ofisa katika kikundi kilichobuniwa kimahususi kupambana na magaidi. Yeye alizoezwa kuua adui zake. Aliuamini sana utukuzo wa taifa lake la Israeli hadi siku aliyogundua kwamba marabi hawakutaka aoe mwanamke aliyempenda kwa sababu tu huyo alikuwa Mwasia, Mtu wa Mataifa. Yeye alianza kuitafuta-tafuta kweli katika Biblia. Kisha akakutana na Mashahidi wa Yehova. Kujifunza kwake Biblia pamoja na Mashahidi kulimsadikisha kwamba hangeweza tena kuwa mfuatia-utukuzo-wa-taifa shupavu. Upendo wa Kikristo ulimaanisha kuacha vita na silaha na kujifunza kupenda watu wa kila jamii. Alishangaa kama nini alipopata barua yenye fadhili yenye maneno haya ya kufungua, “Ndugu Yangu Rami”! Ni nini kilichokuwa kigeni sana kuhusu hilo? Mwandikaji alikuwa Shahidi Mpalestina. “Niliona haiaminiki,” asema Rami, “kwa kuwa Wapalestina walikuwa adui zangu, na hapa mmoja wao alikuwa akiniita mimi ‘Ndugu Yangu.’” Sasa Rami na mkeye hufuatia amani ya kweli katika njia ya Mungu.
8 Kielelezo kingine ni kile cha Georg Reuter, aliyetumikia katika jeshi la Ujerumani lililovamia Urusi wakati wa Vita ya Ulimwengu 2. Hatimaye akapata kuzindushwa na ule mpango mkuu wa Hilter wa kutawala ulimwengu. Aliporudi kutoka vitani, alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Yeye aliandika hivi: “Hatimaye, mambo yalianza kuwa wazi kwangu. Nilitambua kwamba si Mungu aliyekuwa wa kulaumiwa kwa huo umwagikaji damu wote . . . Nilijifunza kwamba kusudi lake lilikuwa kuimarisha paradiso ya duniani pote yenye baraka zidumuzo milele kwa wanadamu watiifu. . . . Hitler alikuwa amejivunia ‘Utawala wake wa Miaka Elfu’ lakini alikuwa ametawala kwa [miaka] 12 tu—na kwa matokeo yenye kuogopesha kama nini! Ni Kristo wala si Hitler . . . awezaye na atakayeimarisha utawala wa miaka elfu juu ya dunia.” Kwa miaka 50 hivi sasa, Georg amekuwa akitumikia akiwa mjumbe wa amani ya kweli katika huduma ya wakati wote.
9. Mambo yaliyoonwa na Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani ya Nazi yanathibitishaje kwamba wao ni wenye moyo mkuu na bado wenye kufanya amani?
9 Uaminifu-maadili na kutokuwamo kwa Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani wakati wa utawala wa Nazi huendelea kuwa ushuhuda wa kumpenda kwao Mungu na kupenda kwao amani hata sasa, miaka zaidi ya 50 baadaye. Kijitabu kilichochapishwa hivi majuzi na United States Holocaust Memorial Museum katika Washington, D.C., hutaarifu hivi: “Mashahidi wa Yehova walivumilia mnyanyaso mkali chini ya utawala wa Nazi. . . . Moyo mkuu ulioonyeshwa na wengi sana katika kukataa [kukana dini yao], walipokabiliwa na mateso makali, kutendewa kwa ukatili katika kambi za mateso, na nyakati fulani kuuawa, uliwapatia heshima ya watu wengi wa wakati wao.” Kisha chaongeza hivi: “Wakati wa kuwekwa huru kwa kambi hizo, Mashahidi wa Yehova waliendelea na kazi yao, wakitembea miongoni mwa waliosalimika, wakifanyiza waumini.”
Badiliko Kubwa Zaidi Sana
10. (a) Ni badiliko gani kubwa linalohitajiwa ili amani ya kweli ije? (b) Hilo lilionyeshwaje katika kitabu cha Danieli?
10 Je, hilo lamaanisha kwamba Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba wanaweza kuleta amani katika ulimwengu mzima kwa njia ya kugeuza watu wengi waamini kutokuwamo kwa Kikristo? La! Ili amani irudishwe duniani, badiliko kubwa zaidi sana linahitajiwa. Hilo ni jipi? Lazima utawala wa Ufalme wa Mungu, ambao Yesu alifundisha wanafunzi wake wasali uje, uchukue mahali pa utawala wa kibinadamu wenye migawanyiko, wenye uonevu, na ulio jeuri. (Mathayo 6:9, 10) Lakini hilo litatukiaje? Katika ndoto iliyopuliziwa kimungu, nabii Danieli alipata kujua kwamba katika siku za mwisho, Ufalme wa Mungu, kama vile jiwe kubwa ‘lisilokatwa kwa mikono ya binadamu,’ ungevunjavunja mfano mkubwa mno unaowakilisha tawala za kisiasa za wanadamu juu ya dunia. Kisha akapiga mbiu hivi: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:31-44.
11. Yehova ataleta kwa njia gani badiliko linalohitajiwa ili amani ipatikane?
11 Kwa nini kutatukia badiliko hili kubwa mno katika hali ya ulimwengu? Kwa sababu Yehova ameahidi kwamba atasafisha dunia na kuondoa wote wale wanaoichafua na kuiharibu. (Ufunuo 11:18) Mgeuzo umbo huo utatukia kwenye vita adilifu ya Yehova dhidi ya Shetani na ulimwengu wake mwovu. Twasoma hivi kwenye Ufunuo 16:14, 16: “Kwa kweli, hizo [yaani, semi zisizo safi zilizopuliziwa] ndizo semi zilizopuliziwa na roho waovu na zafanya ishara, nazo zatoka kwenda kwa wafalme [yaani, watawala wa kisiasa] wa dunia nzima inayokaliwa, kuwakusanya pamoja kwa vita ya siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote. Nazo zikawakusanya pamoja mahali paitwapo katika Kiebrania Har–Magedoni.”
12. Har–Magedoni itakuwaje?
12 Har–Magedoni itakuwaje? Haitakuwa apokalipsi ya kinyuklia wala msiba wenye kuchochewa na wanadamu. La, hii ni vita ya Mungu ya kumaliza vita vyote vya kibinadamu na kuangamiza wote wale waendelezao vita hivyo. Hii ni vita ya Mungu ya kuleta amani ya kweli kwa wale wapendao amani. Ndiyo, Har–Magedoni inakuja kama vile ambavyo Yehova amekusudia. Haitachelewa. Nabii wake Habakuki alipuliziwa kuandika, hivi: “Maana njozi hii bado ni kwa wakati ulioamriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake, wala haitasema uongo; ijapokawia, ingojee; kwa kuwa haina budi kuja, haitakawia.” (Habakuki 2:3) Kwa sababu ya hisia zetu za kibinadamu, huenda ikaonekana kuwa imekawia, lakini Yehova hufuata ratiba yake. Har–Magedoni itafyatuka kwa saa ambayo Yehova ameamua kimbele.
13. Mungu atashughulikaje na yule mkosaji halisi, Shetani Ibilisi?
13 Hatua hiyo ya kukata maneno itaondoa mambo yote yanayozuia amani ya kweli! Lakini ili amani iimarishwe kwa uthabiti, ni lazima jambo jingine lifanywe—kuondolewa kwa mmoja anayesababisha migawanyiko, chuki, na zogo. Na hilo hasa ndilo jambo ambalo Biblia hutoa unabii kwamba litafuata—kutiwa kwa Shetani, mchochezi wa vita na baba wa uwongo, katika abiso. Mtume Yohana aliona tukio hili katika ono la kiunabii, kama ilivyorekodiwa kwenye Ufunuo 20:1-3: “Nikaona malaika akiteremka kutoka mbinguni mwenye ufunguo wa abiso na mnyororo mkubwa mkononi mwake. Naye akalikamata joka kubwa, nyoka wa awali, aliye Ibilisi na Shetani, na kumfunga kwa miaka elfu. Naye akamvurumisha ndani ya abiso na kuifunga na kuitia muhuri juu yake, ili asipate kuongoza mataifa vibaya tena kamwe mpaka miaka elfu ilipokuwa imekwisha.”
14. Tendo la Yehova lenye shangwe ya ushindi dhidi ya Shetani laweza kufafanuliwaje?
14 Hii si ndoto; ni ahadi ya Mungu—na Biblia husema hivi: “Haiwezekani Mungu kusema uwongo.” (Waebrania 6:18) Kwa njia hiyo Yehova aliweza kusema kupitia nabii wake Yeremia hivi: “‘Mimi ni Yehova, Yule ambaye hudhihirisha fadhili-upendo, haki na uadilifu katika dunia; kwa kuwa mimi hupendezwa na mambo haya,’ ni usemi wa Yehova.” (Yeremia 9:24, NW) Yehova hutenda kwa haki na uadilifu, naye hupendezwa na amani ambayo ataleta duniani.
Utawala wa Mkuu wa Amani
15, 16. (a) Ni nani anayechaguliwa na Yehova kutawala akiwa Mfalme? (b) Utawala huo unafafanuliwaje, na ni nani watakaoshiriki katika utawala huo?
15 Ili kuhakikisha kwamba amani ya kweli itakuja kwa wote wale wanaoishi chini ya mpango wake wa Ufalme, Yehova amempa utawala yule Mkuu wa Amani wa kweli, Yesu Kristo, kama ilivyotabiriwa kwenye Isaya 9:6, 7: “Kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, tumepewa mtoto mwanamume; na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme [“Mkuu,” NW] wa amani. Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe. . . . Wivu wa BWANA wa majeshi ndio utakaotenda hayo.” Mtunga-zaburi pia aliandika kiunabii juu ya utawala wenye amani wa Mesiya: “Siku zake yeye, mtu mwenye haki atasitawi, na wingi wa amani hata mwezi utakapokoma.”—Zaburi 72:7.
16 Kwa kuongezea, ndugu za Kristo 144,000 waliotiwa mafuta kwa roho watakuwa wakitawala pamoja naye mbinguni. Hawa ndio warithi-washirika pamoja na Kristo ambao Paulo aliandika hivi juu yao: “Kwa upande wake, Mungu apaye amani atamponda-ponda Shetani chini ya miguu yenu upesi. Fadhili isiyostahiliwa ya Bwana wetu Yesu iwe pamoja nanyi.” (Waroma 16:20) Ndiyo, hawa watashiriki kutoka mbinguni katika ushindi wa Kristo juu ya mchochea-vita, Shetani Ibilisi!
17. Ni lazima tufanye nini ili kuirithi amani ya kweli?
17 Kwa hiyo basi swali ni, Ni lazima ufanye nini ili urithi amani ya kweli? Amani ya kweli yaweza kuja tu kwa njia ya Mungu, na ili uipate lazima uchukue hatua chanya. Ni lazima umkubali Mkuu wa Amani na kumwendea. Hilo lamaanisha kwamba ni lazima umkubali Kristo katika fungu lake akiwa Mkombozi na Mfidi wa jamii ya kibinadamu yenye dhambi. Yesu mwenyewe alisema maneno haya yajulikanayo sana: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” (Yohana 3:16) Je, uko tayari kudhihirisha imani katika Kristo Yesu akiwa Wakili wa Mungu wa kuleta amani ya kweli na wokovu? Hakuna jina jingine lolote chini ya mbingu ambalo laweza kuimarisha amani na kuihakikisha. (Wafilipi 2:8-11) Kwa nini? Kwa sababu Yesu ni Mchaguliwa wa Mungu. Yeye ndiye mjumbe wa amani aliye mkubwa kupita wote waliopata kutembea duniani. Je, utamsikiliza Yesu na kufuata kielelezo chake?
18. Twapaswa kufanya nini katika kuitikia maneno ya Yesu yaliyorekodiwa kwenye Yohana 17:3?
18 ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele,’ Yesu akasema, “wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Sasa ndio wakati wa kuendelea kutwaa ujuzi sahihi kwa kuhudhuria kwa ukawaida mikutano ya Mashahidi wa Yehova kwenye Jumba la Ufalme. Mikutano hiyo yenye kuelimisha itakuhamasisha ushiriki ujuzi wako na tumaini lako na wengine. Wewe pia waweza kupata kuwa mjumbe wa amani ya Mungu. Waweza kufurahia amani sasa kwa kumtumaini Yehova Mungu, kama ilivyotaarifiwa kwenye Isaya 26:3 kulingana na tafsiri ya New International Version: “Utamweka katika amani kamilifu yule ambaye akili yake ni thabiti, kwa sababu yeye hukutumaini wewe.” Wapaswa umtumaini nani? “Mtumainini Yehova, nyinyi watu, nyakati zote, kwa kuwa katika Yah Yehova mna Mwamba wa nyakati zisizo dhahiri.”—Isaya 26:4, NW.
19, 20. Ni jambo gani linalowangojea wale leo wanaotafuta sana amani na kuifuatia?
19 Chukua msimamo wako sasa kwa ajili ya uhai udumuo milele katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye amani. Kwenye Ufunuo 21:3, 4, Neno la Mungu hutuhakikishia: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa vikundi vya watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” Je, huo sio wakati ujao wenye amani unaotamani sana?
20 Basi kumbuka kile ambacho Mungu ameahidi. “Wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani. Umwangalie sana mtu mkamilifu, umtazame mtu mnyofu, maana mwisho wake mtu huyo ni amani.” (Zaburi 37:11, 37) Siku hiyo yenye furaha itakapofika, na tuseme kwa shukrani, “Hatimaye amani ya kweli! Shukrani kwa Yehova Mungu, chanzo cha amani ya kweli!”
Je, Waweza Kueleza?
◻ Ni nini kiwezacho kumsaidia mtu afanye mabadiliko katika fikira na tendo?
◻ Mashahidi wa Yehova, mmoja-mmoja na wote kwa ujumla, wameonyeshaje kupenda kwao amani ya kweli?
◻ Yehova atashughulikaje na wote waendelezao chuki na vita?
◻ Utawala wa Mkuu wa Amani utawafanyia wanadamu nini?
[Picha katika ukurasa wa 14]
Maneno ya Isaya hayatimizwi na UM, bali yanatimizwa na wale waitikiao ufundishaji wa Yehova
[Picha katika ukurasa wa 15]
Wanaume hawa wawili walifanya mabadiliko ili kufuatia amani
Rami Oved
Georg Reuter
[Picha katika ukurasa wa 16]
Amani ya kweli itaenea chini ya utawala wa Mkuu wa Amani