Jinsi Wewe Unaweza Kuona Amani ya Kimungu kwa Ukamili Zaidi
“Laiti ungalisikiliza amri zangu! ndipo amani yako ingalikuwa kama mto wa maji, na haki yako kama mawimbi ya bahari.”—ISAYA 48:18.
1. Ni nini linalohitajiwa ili tuone amani kwa ukamili kama ambavyo tungeweza?
WALE wanaoshiriki kwa ukawaida katika funzo la kundi la Biblia kwa msaada wa gazeti hili wanajifunza ubora wa amani ambayo Mungu anatoa, nao wanataka amani hiyo. Walio wengi bila shaka wanaifurahia. Lakini si wote wanaoiona kwa ukamili kama ambavyo wangeweza. Kwa sababu gani? Kuhusu wale ambao wangeweza kuwa na amani ya kimungu, Yehova anasema: “Mimi ni [Yehova], Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata. Laiti ungalisikiliza amri zangu! ndipo amani yako ingalikuwa kama mto wa maji, na haki yako kama mawimbi ya bahari. —Isaya 48:17, 18.
2. (a) Ni wazo gani linalodokezwa na neno ‘kusikiliza’? (b) Ni amri ngapi za Mungu ambazo lazima tusikilize? (1 Yohana 5:3)
2 Kwa wazi, mtu ye yote anaweza kupata manufaa kutokana na kuhudhuria mikutano ambako tunazungumzia Biblia. Lakini ni wale tu ambao wanasikiliza amri za Yehova, wakizitumia kibinafsi na kuishi kulingana nazo, wanaofurahia amani ya kimungu kweli kweli. Je! kuna maeneo ambamo wewe unahitaji kufanya hivyo kwa ukamili zaidi? (2 Petro 1:2) Haitoshi kusikiliza matakwa machache ya Mungu na kuyaacha mengine ambayo tunaona kwamba yanasumbua au ni magumu zaidi. Shetani alipojaribu kumshawishi Yesu Kristo afuate njia yake ya ubinafsi ya kufikiri, Yesu alimjibu hivi kwa uthabiti: “Imeandikwa, mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha [Yehova].”—Mathayo 4:4.
3. Ni pande gani za maisha zetu ambazo ni lazima zipatanishwe na njia za Yehova ikiwa tunataka tuwe na amani tele kweli kweli?
3 Amri za Mungu zinahusu kila upande wa maisha zetu. Kwanza kabisa, zinahusu uhusiano wetu pamoja na Yehova. Halafu zinagusa maoni yetu kuelekea tengenezo lake linaloonekana na huduma ya Kikristo, jinsi tunatendea washiriki wa jamaa, na shughuli zetu pamoja na watu wa ulimwengu. Wale wanaosikiliza kwa bidii amri za Yehova katika mambo yote hayo ndio wanaobarikiwa kwa amani tele. Acheni tufikirie mambo kadha yanayoweza kutusaidia tubarikiwe hivyo sisi binafsi.
Je! Yo Yote ya Mambo Haya Yanahitaji Uangalifu Wako?
4. (a) Kwa sababu gani kuwa na funzo la nyumbani la Biblia au kwenda kwenye Jumba la Ufalme si’ uthibitisho kwamba sisi tuna amani pamoja na Mungu? (b) Ni jambo gani linalotiwa ndani ya kujizoeza imani katika Yesu Kristo? (Yohana 3:36)
4 Je! wewe umeanza hivi majuzi kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova? Au je! labda wewe umekuwa ukishirikiana na kundi la kwenu kwa miezi kadha au hata miaka? Ikiwa ndivyo, bila shaka umepata furaha ya kuwa na maarifa ya kujua makusudi ya Mungu yaliyofunguka mbele yako. Lakini jambo la kwamba mtu anafurahia funzo la nyumbani la Biblia au anapata raha katika kwenda kwenye Jumba la Ufalme halithibitishi kwamba yeye ana amani pamoja na Mungu. Sisi sote tulizaliwa katika dhambi, na amani pamoja na Mungu inawezekana kwetu kupitia Yesu Kristo peke yake. (Isaya 53:5; Matendo 10:36) Kumwamini Yesu tu bila tendo hakuleti amani hiyo. Inahitajiwa kabisa tuthamini uhitaji wetu kibinafsi wa ukombozi, kujizoeza imani katika ubora wa dhabihu ya Yesu, ndipo tutoe ushuhuda wa kuonyesha kwamba tuna imani hiyo kwa kutii amri zake. (Yakobo 2:26) Moja ya amri ambazo Yesu alitoa alipokuwa duniani ilikuwa ile ya kwamba wale ambao wangekuwa wanafunzi wake wamepaswa wabatizwe katika maji. (Mathayo 28:19, 20) Je! wewe umezamishwa kwa kuonyesha wakfu wako kwa Yehova kupitia Yesu Kristo?
5. Kwa sababu gani wakfu na ubatizo ni mambo ya maana ili sisi tuwe na amani pamoja na Mungu?
5 Je! kuna jambo lo lote katika maisha yako linalokufanya usistahili ubatizo? Ikiwa unajua kwamba lipo, au ikiwa unapoendelea kujifunza unapata kujua kwamba kuna jambo kama hilo, usikawie kunyoosha mambo. Utambue kwamba mwelekeo wo wote au mwenendo ambao ungefanya mtu asistahili ubatizo ni kipingamizi pia cha kuwa na amani pamoja na Mungu. Chukua hatua ya haraka maadamu nafasi ingali ipo. Kama inavyoonyeshwa kwenye 1 Petro 3:21, wale wanaopewa na Mungu dhamiri njema kwanza wanajiweka wakfu kwa Yehova kwa kutegemea msingi wa imani katika dhabihu ya Kristo, wanabatizwa kuonyesha wamejiweka wakfu hivyo, na ndipo wanafanya mapenzi ya Mungu. Ndipo amani inayoambatana na dhamiri njema kwa sababu ya kuwa na msimamo unaokubaliwa mbele za Mungu inakuwa yao; haiwezekani kwa njia nyingineyo yote. Bila shaka, huo ni mwanzo tu.
6. Kwa sababu gani mwelekeo wetu juu ya mikutano ya kundi unahusu kwa njia fulani kufurahia kwetu amani?
6 Halafu fikiria ukawaida wako katika kuhudhuria mikutano ya kundi na ushiriki wako katika mikutano hiyo kwa kadiri ambayo unaweza. Je! mikutano hiyo ina mahali fulani katika maisha yako hivi kwamba huruhusu ivurugwe na ulimwengu au shughuli nyingine za kibinafsi? Je! wewe unajitayarisha kwa ajili ya mikutano na kulihesabu kuwa pendeleo kuishiriki? Mambo hayo, pia, yanahusu wazi kufurahia kwa mtu amani. Kwa sababu gani? Kwa sababu roho ya Mungu iko pamoja na watu wake waliokutana wakiwa kundi, na amani ni tunda la roho hiyo. (Wagalatia 5:22) Ni kwenye mikutano hiyo kwamba sisi tumesaidiwa tufahamu matakwa ya Yehova, na tunahitaji ufahamu huo ili tufanye yanayopendeza machoni pake. Hapa, pia, tumejifunza na kukumbushwa jinsi ya kuendeleza amani katika uhusiano wetu pamoja na wanadamu wenzetu—katika kundi, nyumbani, shuleni, na kwenye kazi yetu ya kimwili. Mikutano yetu ni moja ya njia zile kubwa kubwa ambazo katika hizo sisi tunafundishwa na Yehova, na kama vile Maandiko yanavyoonyesha wazi, ni wale wanaofundishwa na Yehova wanaofurahia amani tele.—Isaya 54:13.
7. Ni mwendelezo gani unaohitajiwa juu ya mambo yanayozungumzwa katika mikutano yetu?
7 Jambo linalohusiana kwa ukaribu na hilo ambalo linastahili kuangaliwa ni kutumia tunayojifunza hatua kwa hatua katika maisha yetu binafsi. Hatutaki kuwa kama Waisraeli wale ambao Yehova alisema ‘wangesikia tena na tena lakini hawangefahamu.’ (Isaya 6:9, NW) Wala hatutaki kuwa kama wale ambao Yehova alimweleza Ezekieli habari zao—watu ambao wangesikiliza nabii wa Yehova lakini wasifanye aliyosema kwa sababu walichagua kutimiza tamaa zisizo safi au za kufuatia vitu vya kimwili. (Ezekieli 33:31, 32) Tofauti na hilo, wale ambao wangekusanyika kwenye nyumba ya Yehova katika siku zetu na kupata kibali chake wanaelezwa kuwa wakisema: “Twende juu mlimani kwa [Yehova], na nyumbani kwa Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.” (Mika 4:2) Tukizingatia kikweli katika moyo maagizo tunayopokea kwenye mikutano, ikiwa katika kila mkutano tunatenga angalau jambo moja ambalo sisi binafsi tunahitaji kisha tulitengeneze, tutavuna tunda la amani. Kama vile Yesu alivyosema kwenye Luka 11:28, NW: “Wenye furaha ni wale wanaosikia neno la Mungu na kulishika!”
8. Ni kwa njia gani sisi binafsi tunaweza kupata manufaa kwa kushiriki katika huduma ya shambani kwa ukamili ambao hali zetu zinaruhusu?
8 Moja la mambo yanayokaziwa kwenye mikutano yetu ni umaana wa kushiriki kikamilifu kuutangaza Ufalme wa Mungu na kuwasaidia wengine wawe wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19) Utendaji huo mbalimbali unapewa nafasi kubwa kadiri gani katika maisha yako? Ikiwa sisi tumesikiliza kwa makini yale ambayo Yehova anatuambia kupitia Neno na tengenezo lake, tunajua kwamba hii ndiyo kazi ya maana zaidi inayofanywa duniani leo. (Ufunuo 14:6, 7) Na ni jambo linalojulikana sana kwamba wale walio katika utumishi wa wakati wote—na wale ambao, ingawa hawawezi kuwa mapainia, wana bidii kweli kweli katika huduma —ndio wale ambao miongoni mwetu kwa kutokeza sana ni wenye furaha. Amani wanayofurahia si kama tone la maji tu, bali, kama alivyosema Yehova, inakuwa kama “mto wa maji.” (Isaya 48:18) Je! hilo ndilo unaloona wewe? Sisi sote tunaweza kuliona.
9. Ni nini linaloweza kutusaidia tuendeleze amani yetu tuliyopewa na Mungu hata tunapopatwa na magumu makali sana?
9 Ijapokuwa hivyo, kutii kwetu mashauri yote hayo hakutufanyi tuwe watu wasioweza kamwe kupatwa na mikazo ya maisha katika mfumo wa mambo uliopo. Lakini hata hali ziwe ngumu namna gani, Mungu anatuhakikishia juu ya msaada wake wenye upendo ikiwa tutamgeukia yeye. (1 Petro 5:6, 7) Je! sisi tumejifunza kutafuta msaada wa Yehova na mwelekezo katika kila jambo tunalofanya, kumwendea kwa uhuru katika sala na, baada ya kufanya yote tuwezayo katika hali zenye magumu, kumtupia Yehova mizigo yetu na kuiacha kwake tukiwa na uhakika? (Mithali 3:5, 6; Zaburi 55:22) Kwa uchangamfu tunatiwa moyo kwenye Wafilipi 4:6, 7: “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.” Lo! uandalizi wa ajabu jinsi gani! Je! wewe umejifunza kupata manufaa kamili kutokana na amani ya Mungu ambayo inafanywa iwezekane kwa njia hiyo?
Endelea Kufuatia Amani
10. Baada ya kutafuta amani, ni jambo gani zaidi linalohitajiwa kwa upande wetu?
10 Mara tukiisha kuwa na amani hiyo, hatutatenda bila kuijali. Jitihada yenye bidii inahitajiwa ili kuidumisha. Hivyo 1 Petro 3:10, 11 husema hivi: “Atakaye kupenda maisha, na kuona siku njema, . . . atafute amani, aifuate sana.” Mtu akiisha kutafuta mradi fulani na kuupata, angekuwa mpumbavu kuuchukua kimchezo. Baada ya kutafuta na kupata amani, tunahitaji kujilinda dhidi ya mambo ambayo yangeweza kuivuruga. Zaidi ya hilo, imetupasa tufuatie kwa bidii mambo yanayochangia amani.
11. (a) Ni mwelekeo gani ambao unaweza kuhatirisha uhusiano wetu pamoja na Yehova? (b) Ni wakati gani kwa kweli tunapopaswa tuwe tukiomba msaada wa Mungu kwa habari ya vishawishi? (Mathayo 6:13)
11 Ikiwa tumefikia amani pamoja na Mungu kupitia njia ambayo yeye ameandaa, tunahitaji tuwe waangalifu tusivuruge uhusiano huo kwa kurudia zoea la dhambi. Bila shaka, kwa kuwa sisi sote ni watu wasiokamilika, sisi sote tunatenda dhambi. Lakini kuna hatari wakati mtu anapotetea ndani yake mwenyewe mielekeo na vitendo ambavyo Mungu analaani. Hatuwezi tu kuinua mabega yetu na kusema, “Hivyo ndivyo nilivyo mimi.” (Warumi 6:16, 17) Tunahitaji kutubia kosa badala ya kulitetea, na ndipo tunapopaswa kuomba sana Mungu atusamehe kwa msingi wa imani yetu katika dhabihu ya Yesu. Tunahitaji pia kujifunza kumwendea Mungu tupate msaada kabla ya kufanya kosa, badala ya kujaribu kupiga vita tukiwa peke yetu, huku tukijiachilia tushindwe mwishowe, na ndipo tuombe msamaha. Kwa msaada wa Mungu, tunaweza kufanikiwa katika kuvaa “utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.”—Waefeso 4:20-24, NW.
12. (a) Ili kufurahia amani, ni mahusiano gani mengine yanayohitaji kuangaliwa? (b) Ni jambo gani linalotakwa kwetu katika habari hii?
12 Bila shaka kufurahia amani kunatia ndani pia uhusiano pamoja na watu wengine. Wakristo wa kweli wanatumikia Mungu wakiwa sehemu ya tengenezo fulani; wao ni ‘ushirika wa ndugu.’ (1 Petro 2:17, NW) Kama vile Yesu alivyosema ingekuwa kweli juu ya wafuasi wake, wao ni wenye kutokeza katika upendo wao kwa mtu na mwenzake. (Yohana 13:35) Lakini hakuna ye yote wao aliye mkamilifu. Kwa sababu ya makosa yetu wenyewe ya kutokamilika na yale ya wengine, huenda tukahitaji kusali kwa kujikaza sana juu ya hali fulani na kujitahidi kutatua matatizo. Waebrania 12:14 linatuhimiza hivi: “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote.” Na katika uhusiano wetu pamoja na ndugu na dada zetu Wakristo, kuna wajibu wa pekee wa kuendelea kufuatia amani. Likisema wazi kabisa, 1 Wathesalonike 5:13, NW linasema hivi: “Mwe wenye kuamanika mtu na mwenzake.” Hiyo haimaanishi kuepuka kulipiza kisasi, bali pia kuwa waendelezaji wa amani walio watendaji, kuchukua hatua ya kwanza kurudisha amani na kuwa na nia ya kukubalia ili kuwe na amani,—Waefeso 4:1-3.
13. (a) Katika kuendeleza amani pamoja na wasioamini, sisi tungeweza kufanya nini, lakini tunaonyeshaje kwamba amani pamoja na Mungu ndiyo inayokuja kwanza? (b) Inawezekanaje sisi tuwe na amani hali kuna msukosuko kutuzunguka?
13 Hata hivyo, nje ya kundi, si kila mtu aliye na nia ya kuwa mwenye kuamanika. Kwa hiyo, kihalisi, Warumi 12:18, NW hushauri hivi: “Ikiwa inawezekana, kwa kadiri ambavyo inategemea ninyi, iweni wenye kutamanika pamoja na watu wote.” Lakini jitihada zetu za kuendeleza amani hazitii ndani kuacha msimamo wetu kuhusiana na matakwa ya uadilifu ya Yehova. Huenda tukarekebisha nyakati ambazo tunafanya mambo fulani, lakini tunajua kwamba halingekuwa jambo la hekima kuacha kuhudhuria mikutano ya kundi au kujiepusha tusishiriki katika huduma ya shambani ili kuendeleza amani pamoja na wenzi wa ndoa au watu wa ukoo. Na tunajua kwamba Yehova hangekubali tukijiunge katika mazoea ya kutokutii Mungu tukiwa pamoja na wafanya kazi au wanashule wenzetu ili tupate kibali chao. Sisi tunatambua kwamba amani ni ya wale tu ambao kwanza kabisa wanafurahia amani pamoja na Mungu, wale wanaoipenda sheria ya Yehova na kutembea katika njia zake. Ni amani hiyo tunayothamini zaidi ya kitu kinginecho chote. (Zaburi 119:165) Ni kweli kwamba huenda kukawa na msukosuko kutuzunguka. Wasioamini huenda wakabishana na kupigana; huenda hata wakarundika juu yetu matukano kwa sababu ya imani yetu. Lakini sisi tunajua jinsi Neno la Mungu limetufundisha kujiendesha wenyewe. Kwa kuendelea kufuatia mwendo unaopatana na njia za uadilifu za Yehova, sisi hatunyimwi amani iliyo ya maana zaidi.—Linganisha Zaburi 46:1, 2.
14. Ingawa sisi binafsi tunapata dhiki, ni nini linalotuwezesha tuendelee kudumisha utulivu wa kindani na tarajio zuri sana?
14 Katika usiku wa mwisho kabla ya kifo chake, Yesu aliambia mitume wake waaminifu hivi: “Hayo nimewaambieni mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33) Ndiyo, tunapata dhiki. Tukiwa Wakristo, tunapatwa na mateso ya namna mbalimbali. Huenda tukatendwa isivyo haki, na wengi wanapatwa na ugonjwa mbaya sana. Lakini amani ya kimungu inatutegemeza kupitia yote hayo. Kwa sababu tumefundishwa na Yehova, twajua kwa nini Wakristo wanateswa. Hatuna mashaka kwa nini kuna udhalimu na kwa nini sisi binafsi tunapatwa na ugonjwa. Tunajua pia ya wakati ujao. Tunajua kwamba matokeo ya mwendo wa maisha ya Yesu yenye uaminifu na kifo chake cha dhabihu, ukombozi ni hakika. Zaidi ya hilo, twajua kwamba hata yawe ni matatizo gani yanayotukabili sasa, tunaweza kumwendea Mungu katika sala tukiwa na uhakikisho wa kwamba anatujali kwa upendo na atatutegemeza kupitia roho yake.—Warumi 8:38, 39.
15. Ni jinsi gani ilivyo kweli kwamba amani ambayo Kristo anafanya iwezekane si kama ile inayotolewa na ulimwengu?
15 Kwa kufaa, Yesu alisema kwenye Yohana 14:27: “Amani nawaachieni; amani yangu nawapa; niwapavyo mimi sivyo kama ulimwengu utoavyo. Msifadhaike mioyoni mwenu, wala msiwe na woga.” Hakika ni kweli—ulimwengu hauna cho chote kinachofanana na amani anayotoa Mungu kupitia Yesu Kristo. Inatuwezesha tuwe wenye nguvu tunapokabili hali ambazo zingefanya wengine wakate tumaini kabisa.
16. (a) Ni tazamio gani lililo mbele kwa ajili ya wale ambao sasa wanathamini kikweli amani ambayo Mungu anatoa? (b) Tunaweza kuonyeshaje kwamba sisi tunaipenda sana amani hiyo?
16 Ni wakati ujao mzuri jinsi gani ulio mbele ya wale wanaokubali amani anayoitoa Mungu na kuifanya iwe sehemu kubwa ya maisha yao! Karibuni ulimwengu ambao una uadui pamoja na Mungu utatoweka. Uumbaji wote utaunganishwa kikamili katika amani kupitia matakwa ya uadilifu ya Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima. Shukrani zetu kwa tarajio hilo kuu na zitusukume tutende kwa upatani kamili nalo sasa. Sisi sote na tusikilize kwa uangalifu maagizo ya Yehova, tuache sheria zake zipandwe katika mioyo yetu ili tuweze kupenda njia zake kikweli, na kufanya anayotaka. Kama Mithali 3:1, 2 inavyosema: “Mwanangu, usisahau sheria yangu, bali moyo wako uzishike amri zangu. Maana zitakuongezea wingi wa siku, na miaka ya uzima, na amani.”
Maulizo ya Kurudia
◻ Kulingananalsaya48:18, ni nini linalohitajiwa ili tuwe na amani tele?
◻ Ni kwa kufanya mambo gani tunaweza kuwa na amani ya kimungu kwa ukamili zaidi?
◻ Ni nini yanayotazamiwa kwetu kwa habari ya kuendeleza amani pamoja na ndugu na dada zetu?
◻ Tunaweza kuendelezaje amani hata tunapozungukwa na wasioamini?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Ubatizo
[Picha katika ukurasa wa 17]
Kuhudhuria mikutano kwa ukawaida
Kutumia tunayojifunza
[Picha katika ukurasa wa 18]
Kushiriki kwa ukamili katika huduma ya shambani
Kumtupia Yehova mizigo yetu