‘Tafuta Amani na Uifuatie’
“Atukuzwe BWANA, [Yehova, NW], apendezwaye na amani ya mtumishi wake.”—ZABURI 35:27.
1. Sisi tunaonea shangwe amani gani leo?
NI SHANGWE kama nini kuwa na amani katika ulimwengu huu uliogawanyika! Ni furaha kama nini kumwabudu Yehova, “Mungu wa amani mwenyewe,” na kushiriki katika mibaraka yake ya “agano la amani”! Ni lenye kuburudisha kama nini kati ya mikazo ya maisha, kujua “amani ya Mungu, ipitayo akili zote” na kuona “kifungo cha amani” kinachounganisha watu wa Mungu haidhuru taifa lao, lugha yao, rangi yao, au sehemu ya jamii mtu anakotoka!—1 Wathesalonike 5:23; Ezekieli 37:26; Wafilipi 4:7; Waefeso 4:3.
2, 3. (a) Ingawa watu wa Mungu kwa ujumla watavumilia, ni nini huenda ikatokea kwa Mkristo mmoja mmoja? (b) Biblia yatuhimiza tufanye nini?
2 Sisi Mashahidi wa Yehova, tunalinda amani hii kama hazina. Hata hivyo, hatuwezi kuichukua vivi hivi tu. Amani haidumishwi kwa urahisi tu kwa sababu tunashiriki na kundi la Kikristo au tumepata kuwa sehemu ya familia ya Kikristo. Ingawa mabaki wa wapakwa-mafuta na waandamizi wao wa “kondoo wengine” watavumilia hadi mwisho wakiwa kundi, watu mmoja mmoja wanaweza kupoteza amani yao na kupotea.—Yohana 10:16; Mathayo 24:13; Warumi 11:22; 1 Wakorintho 10:12.
3 Mtume Paulo aliwaonya Wakristo wa siku zake hivi: “Angalieni, ndugu zangu, usiwe katika mmoja wenu moyo mbovu wa kutokuamini, kwa kujitenga na Mungu aliye hai.” (Waebrania 3:12) Onyo hili latumika pia kwa umati mkubwa. Kwa hiyo Biblia inahimiza Wakristo hivi: ‘Tafuteni amani na kuifuatia. Kwa maana macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yanaelekea kuomba kwao; bali uso wa Yehova u kinyume cha wale wanaotenda mambo mabaya.’—1 Petro 3:10-12; Zaburi 34:14, 15.
“Kuweka Akili Juu ya Mnofu”
4. Nini yaweza kusumbua amani yetu na Mungu?
4 Ni nini chaweza kukatiza ufuatiaji wetu wa amani? Paulo ataja kitu kimoja anaposema hivi: “Kuweka akili juu ya mnofu kwamaanisha kifo, lakini kuweka akili juu ya roho kwamaanisha uhai na amani; kwa sababu kuweka akili juu ya mnofu kwamaanisha uadui pamoja na Mungu.” (Warumi 8:6, 7, NW) Kwa kutaja “mnofu” Paulo arejezea hali yetu yenye dhambi tukiwa binadamu wasio wakamilifu ambao wamerithi mielekeo ya kutenda dhambi. Tukijiachilia kwa mielekeo ya mnofu wenye dhambi tutaharibu amani yetu. Mkristo akifanya tendo la ukosefu wa maadili, akisema uwongo, akiiba, akitumia dawa za kulevya, au akivunja sheria ya kimungu kwa njia nyingine yoyote bila kutubu, anavunja amani pamoja na Mungu ambayo alionea shangwe wakati mmoja. (Mithali 15:8, 29; 1 Wakorintho 6:9, 10; Ufunuo 21:8) Tena, akiruhusu vitu vya kimwili viwe vya maana zaidi kwake kuliko mambo ya kiroho, amani yake pamoja na Mungu inatishwa sana.—Mathayo 6:24; 1 Yohana 2:15-17.
5. Nini inatiwa ndani katika ufuatiaji wa amani?
5 Kwa upande mwingine, Paulo alisema hivi: “Kuweka akili juu ya roho kwamaanisha uhai na amani.” Amani ni sehemu ya matunda ya roho, na tukizoeza moyo wetu kuthamini mambo ya kiroho, kusali ili roho ya Mungu itusaidie katika hilo, basi tutaepuka “kuweka akili juu ya mnofu.” ( Wagalatia 5:22-24) Kwenye 1 Petro 3:10-12, amani inaunganishwa na uadilifu. (Warumi 5:1) Petro asema kwamba ufuatiaji wa amani unatia ndani ‘kuepuka yaliyo mabaya na kutenda mema.’ Roho ya Mungu yaweza kutusaidia ‘tufuatie uadilifu’ na hivyo tuhifadhi amani yetu pamoja na Mungu.—1 Timotheo 6:11, 12, NW.
6. Ni nini moja la madaraka ya wazee yanayohusika na amani ya kundi?
6 Ufuatiaji wa amani ni hangaikio kubwa kwa wazee kundini. Kwa mfano, mtu akijaribu kuanza mazoea machafu, wazee wana wajibu kulinda kundi kwa kujaribu kumkaripia mwenye kutenda dhambi. Akikubali karipio hilo, atapata tena amani yake. (Waebrania 12:11) Ikiwa sivyo, huenda ikawa lazima atupwe nje ili uhusiano wenye amani wa kundi pamoja na Yehova uhifadhiwe.—1 Wakorintho 5:1-5.
Amani Pamoja na Ndugu Zetu
7. Paulo aonya Wakristo juu ya onyesho gani la ‘kuweka akili juu ya mnofu’?
7 ‘Kuweka akili juu ya mnofu’ kwaweza kuharibu si amani yetu pamoja na Mungu tu bali pia uhusiano wetu mzuri pamoja na Wakristo wengine. Paulo aliwaandikia Wakorintho hivi: “Kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini. Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina [wivu na ugomvi, NW], je! si watu wa tabia ya mwilini ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu?” (1 Wakorintho 3:3) Wivu na ugomvi ni kinyume kabisa cha amani.
8. (a) Nini huenda ikatokea kwa mtu anayesababisha wivu na ugomvi kundini? (b) Amani yetu pamoja na Mungu yategemea nini?
8 Kusumbua amani ya kundi kwa kusababisha wivu na ugomvi ni jambo la uzito sana. Akiongea juu ya sifa inayolingana na amani ikiwa tunda la roho, mtume Yohana alionya hivi: “Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona.” (1 Yohana 4:20) Kwa njia kama hiyo, mtu akisababisha wivu au ugomvi miongoni mwa ndugu, je! kweli yeye aweza kuwa na amani pamoja na Mungu? Hakika sivyo! Sisi tunahimizwa hivi: “Endeleeni kufurahi, kurekebishwa, kufarijiwa, kufikiri kwa upatano, kuishi kwa amani; na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja na ninyi.” (2 Wakorintho 13:11, NW) Ndiyo, ikiwa tunaendelea kuishi kwa amani pamoja sisi kwa sisi, basi Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nasi.
9. Tunajuaje kwamba pindi nyingine Wakristo watakuwa na kutoelewana na kutopatana?
9 Hilo halimaanishi kwamba hakutakuwa kamwe na mambo ya kutoelewana kati ya Wakristo. Majuma yaliyofuata Pentekoste, kulikuwa na kutopatana katika lile kundi changa la Kikristo juu ya ugawanyaji wa chakula cha kila siku. (Matendo 6:1) Pindi moja kutopatana kati ya Paulo na Barnaba kulitokeza “mfoko mkali wa hasira.” (Matendo 15:39, NW) Paulo alilazimika kushauri Euodia na Sintike, waliokuwa, bila shaka, dada wenye bidii, “wawe na nia moja katika Bwana.” (Wafilipi 4:2) Haishangazi kwamba Yesu alitoa shauri lenye kutia mengi ndani juu ya jinsi ya kukomesha usumbufu wa amani kati ya Wakristo na akakazia uharaka wa kushughulika na matatizo kama hayo mara moja! (Mathayo 5:23-25; 18:15-17) Yeye hangalitoa shauri hilo ikiwa hakutazamia magumu miongoni mwa wafuasi wake.
10. Ni hali gani hutokea nyakati fulani kundini, na hiyo huweka daraka gani kwa wote wanaohusika?
10 Leo, basi, inawezekana sana kwamba mtu aweza kuudhiwa na neno lisilo la busara au jambo linaloonekana kuwa dharau kutoka kwa Mkristo mwenzake. Tabia ya mtu mmoja yaweza kuudhi mwingine sana. Nyutu zaweza kugongana. Huenda mtu akakosa kukubaliana kabisa na uamuzi wa wazee. Kwenye baraza la wazee lenyewe, huenda mzee mmoja akawa mwenye kushikilia maoni yake sana na kujaribu kulemea maoni ya wazee wengine. Ijapokuwa kwa hakika mambo hayo hutokea, sisi bado twapaswa kutafuta amani na kuifuatia. Wito wa ushindani ni kushughulika na matatizo kama hayo katika njia ya Kikristo ili kuhifadhi “kifungo cha amani.”—Waefeso 4:3.
11. Yehova amefanya maandalizi yapi kutusaidia tufuatie amani sisi kwa sisi?
11 Biblia yasema hivi: “Atukuzwe BWANA [Yehova, NW], apendezwaye na amani ya mtumishi wake.” (Zaburi 35:27) Ndiyo, Yehova ataka tuwe na amani. Kwa hiyo, yeye amefanya maandalizi mawili yenye kutokeza ili kutusaidia tuhifadhi amani miongoni mwetu wenyewe na pamoja naye. Moja ni roho takatifu, ambayo amani ni tunda layo, pamoja na sifa zenye amani zinazohusiana nayo, kama ustahimilivu, fadhili, upole, na kujidhibiti. (Wagalatia 5:22, 23) Ile nyingine ni hekima ya kimungu, ambayo tunasoma hivi juu yayo: “Hekima itokayo juu, kwanza ni safi, tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na matunda mema.”—Yakobo 3:17, 18.
12. Tunapaswa kufanya nini ikiwa amani yetu pamoja na ndugu zetu imesumbuliwa?
12 Kwa hiyo, amani yetu pamoja na wengine inaposumbuliwa, tunapaswa kusali kwa ajili ya hekima kutoka juu ili ituonyeshe jinsi ya kutenda, na tunapaswa kuomba ili roho takatifu ituimarishe tufanye yaliyo mema. (Luka 11:13; Yakobo 1:5; 1 Yohana 3:22) Kwa kupatana na sala yetu, tunaweza kutazama chanzo cha hekima ya kimungu, Biblia, ili tupate mwongozo, na pia kuchunguza fasihi za Biblia zinazopatikana kwa ajili ya shauri juu ya jinsi ya kutumia Maandiko. (2 Timotheo 3:16) Huenda pia tutake kutafuta shauri kutoka kwa wazee katika kundi. Hatua ya mwisho ingekuwa kufuata mwongozo unaopokewa. Yasema hivi Isaya 54:13: “Na watoto wako wote watafundishwa na BWANA [Yehova, NW]; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.” Hilo linadokeza kwamba amani yetu inategemea kuzoea kwetu mambo ambayo Yehova hutufundisha.
“Wenye Furaha Ni Wenye Amani”
13, 14. (a) Nini kinadokezwa na usemi wa Yesu, “wenye amani”? (b) Tunawezaje kuwa wafanya amani?
13 Yesu, katika Mahubiri yake ya Mlimani, alisema hivi: “Heri wapatanishi [wenye amani, NW]; maana hao wataitwa wana wa Mungu.” (Mathayo 5:9) Hapa “wenye amani” hairejezei wale ambao asili yao ni kuwa watulivu. Neno la kwanza la Kigiriki lamaanisha “wafanya amani.” Mwenye kufanya amani ana ustadi wa kurudisha amani inaposumbuliwa. Ingawa hivyo, la maana zaidi ni kwamba, mfanya amani anajitahidi kuepuka kusumbua amani pale mwanzoni. ‘Amani inadhibiti moyoni mwake.’ (Wakolosai 3:15, NW) Watumishi wa Mungu wakijitahidi kuwa wafanya amani, basi matatizo kati yao yatakuwa haba.
14 Kuwa mfanya amani kunatia ndani kutambua udhaifu wetu wenyewe. Kwa mfano, huenda Mkristo akawa ana hasira kali au ni mwepesi wa kukasirika na mwepesi wa kuudhika. Akiwa chini ya mikazo, huenda maoni yake ya moyoni yamfanye asahau kanuni za Biblia. Hilo si jambo lisilotazamiwa kwa wanadamu wasiokamilika. (Warumi 7:21-23) Hata hivyo, mambo ya uadui, ugomvi, na kasirani za ghafula ghafula yanatajwa kuwa kazi za mnofu. (Wagalatia 5:19-21) Tukipata mielekeo kama hiyo ndani yetu—au ikiwa wengine wanaileta kwenye uangalifu wetu—tunapaswa kusali kwa bidii na kwa uendelevu ili roho ya Yehova isitawishe ndani yetu kujidhibiti na upole. Kwa kweli kila mtu anapaswa kujitahidi kusitawisha sifa kama hizo kuwa sehemu ya utu wake mpya.—Waefeso 4:23, 24; Wakolosai 3:10, 15.
15. Hekima kutoka juu yatofautianaje na ushupavu usiotaka kusikia maneno ya wengine?
15 Pindi fulani, kundi au baraza la wazee linasumbuliwa na mtu aliye mshupavu, anayesisitiza kwamba njia yake ifuatwe sikuzote. Ni kweli, kwa upande wa sheria ya kimungu, Mkristo apaswa kushikilia mambo sana, hata kuwa asiyeweza kubadili maoni. Na tukiona kwamba tuna wazo zuri linaloweza kufaidi wengine, hakuna kosa lolote kulisema wazi kwa wengine, maadamu tunaeleza sababu zetu. Lakini hatutaki kuwa kama wale katika ulimwengu “wasiotaka kufanya suluhu.” (2 Timotheo 3:1-4) Hekima kutoka juu ni yenye amani, tayari kusikiza maneno ya watu. Wale ambao vitendo vyao hufanyiza kiolezo cha kutoweza kubadili maoni kwa ushupavu wanapaswa kutii shauri la Paulo kwa Wafilipi ‘wasitende neno lolote kwa majivuno.’—Wafilipi 2:3.
16. Shauri la Paulo katika kitabu cha Wafilipi linatusaidiaje tushinde kujivuna?
16 Katika barua iyo hiyo, Paulo ahimiza kwamba tunapaswa “kwa unyenyekevu” na moyo mweupe ‘kuhesabu wenzetu kuwa bora kuliko nafsi zetu.’ Hilo ni kinyume kabisa cha kujivuna. Mkristo aliyekomaa hafikirii kwanza kulazimisha mawazo yake mwenyewe, kujitetea mwenyewe, au kulinda cheo na mamlaka yake mwenyewe. Hilo lingekuwa kinyume cha himizo la Paulo “kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.”—Wafilipi 2:4; 1 Petro 5:2, 3, 6.
Maneno ya Amani
17. Ni utumizi gani mbaya wa ulimi unaoweza kusumbua amani ya kundi?
17 Mwenye kufuatia amani ni mwangalifu hasa katika utumizi wake wa ulimi. Yakobo aonya hivi: “Ulimi nao ni kiungo kidogo, nao hujivuna majivuno makuu. Angalieni jinsi moto mdogo uwashavyo msitu mkubwa sana.” (Yakobo 3:5) Porojo yenye madhara, kuchambua wengine mgongoni pao, maneno yasiyo yenye fadhili na makali, kunung’unika na kulalamika, na pia kusifu mno kwa ajili ya faida ya kibinafsi—haya yote ni kazi za mnofu ambazo husumbua amani ya watu wa Mungu.—1 Wakorintho 10:10; 2 Wakorintho 12:20; 1 Timotheo 5:13; Yuda 16.
18. (a) Iwapo kuna utumizi mbaya wa ulimi usiokusudiwa, ni mwendo gani unaofaa kwa kila anayehusika? (b) Hasira inaposababisha mtu atamke maneno yenye kuumiza, Wakristo wenye kukomaa wanaitikiaje?
18 Ni kweli, Yakobo alisema hivi: “Ulimi hakuna awezaye kuufuga.” (Yakobo 3:8) Hata Wakristo waliokomaa wakati mwingine husema mambo ambayo baadaye wanasikitikia kwa moyo mweupe. Sisi sote hutumaini kwamba wengine watatusamehe makosa kama hayo kama vile sisi huwasamehe. (Mathayo 6:12) Wakati mwingine mfoko mkali wa hasira huenda ukatokeza maneno yenye kuumiza. Wakati huo, mfanya amani atakumbuka kwamba “jawabu la upole hugeuza hasira; bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.” (Mithali 15:1) Mara nyingi, yeye atalazimika tu kuvuta pumzi na kukataa kuitikia maneno ya hasira kwa maneno mengine ya hasira. Baadaye, wakati hasira zimepunguka, mfanya amani mwenye moyo mkubwa ajua jinsi ya kusahau yale yaliyosemwa muda wa hasira. Na Mkristo mnyenyekevu atajua jinsi ya kuomba msamaha na kujaribu kupoza maumivu yoyote aliyosababisha. Ni ishara ya imara ya kimaadili kuweza kusema kwa unyofu, “ninasikitika.”
19. Tunajifunza nini kutoka kwa Paulo na Yesu juu ya jinsi ya kutoa shauri?
19 Ulimi ungehitaji kutumiwa ili kuwashauri wengine. Paulo alimkemea Petro peupe alipotenda kimakosa Antiokia. Na Yesu alitoa shauri kali katika barua zake kwa makundi saba. (Wagalatia 2:11-14; Ufunuo, Sura za 2, 3) Tukichunguza mifano hiyo, tunajifunza kwamba shauri halipaswi kuwa lenye upole sana hata lisitimize lengo lalo. Hata hivyo, Yesu na Paulo hawakuwa wakali au wakatili. Shauri lao halikuwa njia ya kufungulia mafadhaiko yenye kukazana ndani yao wenyewe. Wao walikuwa wanajaribu kihalisi kusaidia ndugu zao. Ikiwa yule anayetoa shauri aona kwamba hawezi kudhibiti ulimi wake kabisa, huenda akachagua kukoma kwa muda mfupi na kupoa kidogo kabla hajasema chochote. Kama sivyo, huenda akasema maneno makali na kusababisha tatizo lililo baya kuliko lile analojaribu kushughulikia.—Mithali 12:18.
20. Nini chapasa kuongoza kila kitu tunachosema kwa au juu ya ndugu na dada zetu?
20 Kama vile imetajwa tayari, amani na upendo yakiwa matunda ya roho yanahusiana kwa ukaribu. Ikiwa yale tunayosema kwa ndugu zetu—au juu yao—sikuzote ni wonyesho wa upendo wetu kwao, basi itachangia amani ya kundi. (Yohana 15:12, 13) Maneno yetu yapaswa “yawe na neema sikuzote, yakikolea munyu.” (Wakolosai 4:6) Yapaswa kuwa matamu, yakivutia moyo. Yesu alishauri hivi: “Mwe na chumvi ndani yenu, mkakae kwa amani ninyi kwa ninyi.”—Marko 9:50.
“Fanyeni Bidii”
21. Ni jambo gani lililo wazi juu ya watu wa Mungu kwenye mikutano yao ya kila juma na pindi za makusanyiko na mikusanyiko?
21 Mtunga zaburi aliandika hivi: “Tazama jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja.” (Zaburi 133:1) Kwa kweli, tunafurahi kuwa na ndugu zetu, hasa katika mikutano yetu ya kila juma na pindi ya makusanyiko na mikusanyiko iliyo mikubwa. Nyakati kama hizo, amani yetu inaonekana wazi hata kwa watu walio nje.
22. (a) Ni amani gani bandia mataifa watafikiri wanafaulu kuipata, ikiongoza kwenye nini? (b) Agano la Mungu la amani litaongoza kwenye amani gani ya kweli?
22 Karibuni mataifa watafikiri kwamba wanafaulu kupata amani bila Yehova. Lakini wanaposema, “kuna amani na salama” ndipo uharibifu utawajia wote ambao hawana amani pamoja na Mungu. (1 Wathesalonike 5:3) Baada ya hayo, Mwana Mfalme wa Amani aliye mkuu ataendelea mbele na kuwaponya ainabinadamu kutoka matokeo yenye kuhuzunisha ya kupoteza kwao mwanzoni amani pamoja na Mungu. (Isaya 9:6, 7; Ufunuo 22:1, 2) Halafu, agano la Mungu la amani litatokeza utulivu wa kotekote ulimwenguni. Hata hayawani wa kondeni wataona pumziko kutoka uadui.—Zaburi 37:10, 11; 72:3-7; Isaya 11:1-9; Ufunuo 21:3, 4.
23. Ikiwa tunalinda kama hazina tumaini la ulimwengu mpya wenye amani, tunapaswa kufanya nini sasa?
23 Huo utakuwa wakati wenye utukufu kama nini! Je! wewe hutazama mbele kwenye wakati huo kwa moyo? Ikiwa ndivyo, ‘tafuta kwa bidii kuwa na amani na watu wote.’ Tafuta amani sasa pamoja na ndugu zako, na hasa pamoja na Yehova. Ndiyo, kwa kuwa “mnatazamia mambo hayo, fanyeni bidii ili mwonekane katika amani kuwa hamna mawaa wala aibu mbele yake.”—Waebrania 12:14; 2 Petro 3:14.
Je! Unakumbuka?
◻ Nini kinaweza kuvunja-vunja amani yetu pamoja na Yehova?
◻ Ni aina gani ya kutoelewana ingehitaji kukomeshwa kundini?
◻ Yehova amefanya maandalizi gani kutusaidia kutafuta amani na kuifuatia?
◻ Ni mielekeo gani ya kimnofu ambayo yaweza kusumbua amani ya kundi, na tunaweza kuikinzaje?
[Picha katika ukurasa wa 22]
Amani ni tele miongoni mwa wale wanaofundishwa na Yehova
[Picha katika ukurasa wa 24]
Amani ya ndugu wanaotumika katika umoja ni yenye kupendeza kama nini!