“Huyo Mwanamke Yezebeli”
“MIMI nina hili dhidi yako, kwamba wewe wavumilia huyo mwanamke Yezebeli, ambaye hujiita nabii wa kike, naye huwafundisha watumwa wangu wafanye uasherati na kula vitu vilivyodhabihiwa kwa sanamu.” (Ufunuo 2:20, NW) Ndivyo Yesu alivyosema kwa wazee Wakristo katika Thiatira. Kundi lilikuwa lenye utendaji sana na lilikuwa limedhihirisha upendo, imani, na uvumilivu. Lakini lilikuwa limevumilia uvutano wenye kufisidi wa Yezebeli. Kwa nini? Na je! jambo hilo lingeweza kutendeka leo?—Ufunuo 2:19.
Yaelekea kwamba hakuna mtu katika Thiatira ambaye kwa kweli aliitwa Yezebeli. Yesu alitumia jina hilo kutukumbusha juu ya Malkia Yezebeli wa kihistoria, mke wa Mfalme Ahabu. Mwanamke huyo mwenye nia ya ushupavu alifisidi watu wa Mungu kabisa alipoingiza katika Israeli ibada ya Baali yenye ukosefu wa adili, akifanya kampeni ya kuazimia kufutilia mbali ibada yenye kutakata.—1 Wafalme 16:31-33; 21:1-7.
Yezebeli katika Thiatira—ama mwanamke mmoja ama kikundi cha wanawake—vivyo hivyo alitia moyo ukosefu wa adili na ibada ya sanamu miongoni mwa watu wa Mungu. Watu fulani katika kundi walimsikiliza, kwa kuwa Yesu hunena juu ya “watoto wake,” yaelekea wafuasi wake. (Ufunuo 2:22, 23) Uvutano wake ulitisha kufanya kundi la Thiatira liwe na ufisadi wa kadiri iliyokuwa katika siku ya Ahabu.
Kwa nini Yezebeli wa Thiatira alikuwa mwenye uvutano mwingi sana? Kwa kutazama ulinganifu pamoja na Yezebeli wa kale, watu fulani wamefikiri yeye alikuwa mke wa mzee mwenye kuongoza katika Thiatira. Hata hivyo, Biblia haisemi hivyo. Yaelekea zaidi kwamba, utu wake wa ushupavu na uhakika wa kwamba alidai kuwa nabii wa kike ulimpa cheo chake katika kundi.
Imedokezwa kwamba mazoea yenye makosa aliyoendeleza yalihusiana na mashirika ya kibiashara. Kulingana na Dakt. W. M. Ramsay, “mashirika ya kibiashara yajulikana kwa wingi zaidi katika Thiatira kuliko katika jiji jingine lolote la Esia.” Kati ya haya, The Interpreter’s Dictionary of the Bible husema: “Kila shirika la jinsi hiyo lilikuwa na mungu walo wa kulitegemeza, karamu zalo, pindi zalo ambazo nyakati fulani zingeweza kuwa sherehe zenye ulaji na unywaji mwingi wa kukosa adili. Huenda ‘Yezebeli’ akawa alibisha kwamba . . . sherehe hizi zenye ulaji na unywaji mwingi hazikuhitaji kushutumiwa kwa kuwa, ili apate riziki, ilikuwa lazima kila mfanya kazi ajiunge na shirika fulani.” The Expositor’s Greek Testament huafikiana na hilo, ikidokeza kwamba wale wenye kufuata Yezebeli “walijivunia uhuru wao usio na mipaka wa kuzinduka.”
Kwa uhakika, fundisho la Yezebeli katika Thiatira lililandana na “fundisho la Balaamu” katika Pergamo. (Ufunuo 2:14, NW) Kundi la Pergamo lilikuwa limevumilia mnyanyaso mwingi, lakini watu fulani huko walikuwa wakiiga Balaamu wa kale katika kuendeleza uasherati na ibada ya sanamu. Imedokezwa kwamba katika Pergamo, uvutano wa Balaamu ulitia moyo kuridhiana msimamo ili kuepuka mnyanyaso mkali, hali katika Thiatira, Yezebeli alitia moyo kuridhiana msimamo kwa sababu za kiuchumi. Vyovyote vile, mafundisho yote mawili yalikuwa uasi-imani wenye kufisha.
Je! uvutano wa Kiyezebeli ungeweza kuwako leo? Ndiyo, hasa. Viongozi wengi wa Jumuiya ya Wakristo huiga Yezebeli katika kuvumilia katika makundi yao ugoni-jinsia-moja wenye kufanywa kwa ukawaida, uasherati, uzinzi, utoaji mimba, na mambo kama hayo yenye kushutumiwa na Mungu. Hata ndani ya kundi la Kikristo, watu wachache mmoja mmoja wamehimiza ‘uhuru usio na mipaka’ wa ibada ya kweli, wakitia moyo wazo la kwamba Wakristo hawapaswi kuambatana mno na viwango na mazoea ya Biblia.
Wote watakao kupendeza Yehova wapaswa kuepuka mawazo hayo, hata ikiwa yatolewa na watu mmoja mmoja—wanaume au wanawake —wenye nyutu za kuvutia au zenye uthabiti mwingi. Fikira hiyo inaweza kuua sawa na ilivyokuwa katika karne ya kwanza.—Ufunuo 2:22, 23.