‘Kuvua Watu’ Katika Belize
BELIZE ni nchi ndogo iliyo kama tropiki inayokaa vizuri katikati ya Meksiko na Guatemala. Kutoka mstari wayo wa pwani, Karibea yenye rangi feruzi-bluu ina matumbawe na miamba ya marijani iliyotapakaa hapa na pale ambayo hufanyiza kizuizi cha miamba-bahari kilicho kirefu kupita vyote katika Kizio cha Magharibi. Sehemu ya bara iliyo kubwa zaidi kuambaa pwani ni kavu na ni tambarare. Lakini ndani-ndani kuelekea kusini, ile Milima Maya hufikia kimo cha meta 1,120. Mkoa huu wa milima-milima ambao wakati mmoja ulikuwa wenye misitu mizito una magenge, mabonde ya mito, na maporomoko ya maji yenye uzuri.
Hapo kwanza wakaaji wa nchi hii walikuwa Maya, kama vile magofu na visalio vingi vinavyoshuhudia. Katika miaka ya 1600, ilianza kukaliwa na waliokuwa hapo zamani maharamia wa bahari walioanza kufanya kazi ya kukata magogo ya miti pamoja na miti ya mkangazi. Baadaye, ikawa koloni ya Hondurasi ya Uingereza. Kujitawala na hali ya kuwa taifa lenye kujitegemea kukaja katika 1981.
Leo, Belize ina idadi ya watu wapatao 175,000. Kweli kweli nchi hiyo ni kundi lenye mchangamano, likifanyizwa na Wabelize-weusi (Wakreole), Wamestizo, Maya, Wagarinagu (Wakaribu), Waesia, Wazungu, na wengineo. Kwa sababu elimu ya Belize ilitoka Uingereza, Kiingereza ndiyo lugha rasmi, Kihispania kikiwa lugha ya pili yenye nguvu. Pia Kikreole kinasemwa sana, na ndivyo Maya, Garifuna, na lugha nyinginezo.
Kile kizuizi mwamba-bahari cha urefu wa kilometa 280, chenye marijani za rangi zenye kumeta, minara iliyo kama ngome, na mapango, huwapa makao viumbe-bahari wa aina tofauti-tofauti ambao hupendeza jicho na kaakaa. Nyanja hizi za kuvulia samaki zilizo kando ya pwani ndizo mojapo mali asilia ya nchi zilizo kubwa zaidi ya zote. Vivyo hivyo, ikiwa na watu na utamaduni wenye utofautiano mkubwa, Belize imethibitika kuwa uwanja wa ‘kuvulia’ kwa wale wanaoitikia mwaliko wa Yesu: “Nifuateni, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa watu.”—Mathayo 4:19.
‘Kuvua’ Kwaanza
Ilikuwa katika 1923 kwamba James Gordon, Shahidi aliyebatizwa katika 1918 katika Jameika, alipohamia Belize. Alianza kana kwamba ni kutupa wavu wake, miongoni mwa jirani zake katika na kuzunguka kijiji cha Bomba katika Wilaya ya Belize. ‘Vifaa vya kuvua’ vyake vilikuja kutia ndani sanduku kubwa sana la mkangazi lenye vitabu, likibebwa kwa mkono mmoja, na fonografu (kinanda) ikibebwa katika ule mwingine.
Yapata 1931 Freida Johnson, mhudumu wa wakati wote kutoka Teksasi, alikuja Belize katika safari ya kueneza habari njema katika nchi za Amerika ya Kati. Wakati wa muda wa miezi sita ya kukaa kwake, alimfikia mwokaji mmoja jina lake Thaddius Hodgeson, ambaye naye aliijulisha kweli kwa mwokaji mwenzake, Arthur Randall. Ndugu Hodgeson aliendeleza kazi mpaka kuwasili katika 1945 kwa Charles Heyen na Elmer Ihring, wamisionari wa kwanza waliozoezwa Gileadi.
Mwaka uliofuata, wakati wa ziara ya N. H. Knorr na F. W. Franz, waliokuwa wakati huo msimamizi na makamu wa msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, ofisi ya tawi ikaanzishwa huko. Tangu hapo “wavu” umetupwa katika sehemu zote za Belize, nayo kazi imezidi kukua. Hesabu ya wale wanaoshiriki ‘kuvua watu’ ilifikia kilele cha 844 katika 1989.
‘Kutupa Wavu’ Mashambani
Leo, Jiji la Belize na miji mingine hufanyiwa kazi kwa ukawaida na wale wanaohubiri habari njema za Ufalme, lakini vingi vya vijiji vilivyotapakaa na visiwa havifanyiwi kazi hivyo. Ndivyo ilivyokuwa kwa San Pedro, katika Kisiwa Ambergris, mpaka miaka michache iliopita.
Kwa miaka mingi, wakazi wa San Pedro walionana na ukweli wakati tu Mashahidi kutoka barakuu walipovuka kwa ziara fupi. Mashahidi waliacha fasihi kwa watu wenye kupendezwa, lakini hawangeweza kufuatia kupendezwa kwa kuwa ilikuwa lazima warudi kwenye barakuu. Baadaye, jamaa moja ya watu wanne ikaja Belize kutumikia palipo na uhitaji mkubwa zaidi. Walijitolea kuhamia kisiwa hicho hata ingawa walilazimika kuishi katika gari la tafrija mpaka wajenge nyumba. Lakini “uvuvi” ulikuwa mzuri. Walianza mafunzo ya Biblia mengi, na leo kuna zaidi ya “wavuvi wa watu” zaidi ya 20 katika kisiwa hicho. Katika Septemba 1986, kwa msaada wa Mashahidi kutoka kote kote nchini, walijenga Jumba la Ufalme lao wenyewe katika mwisho-juma mmoja.
Eneo la tawi latia ndani vijiji kadhaa vya Maya vilivyo peke yavyo katika kusini mwa Wilaya ya Toledo, ambako lugha za Ketchi na Maya Mopan husemwa. Mara moja kwa mwaka, wakati wa majira ya kiangazi wakati mito na milima huvukika, kikundi cha Mashahidi kilizoea kuzuru vijiji hivi. Wakibeba kila kitu walichohitaji kwenye migongo yao, walitembea kwenda vijijini, wakatolea wakaaji ushahidi, na kurudi kutembelea wale walioonyesha kupendezwa.
Katika ‘safari ya mashambani’ moja kama hiyo katika 1968, akina ndugu walitembelea kijiji cha Crique Sarco. Msichana mchanga alipata kuona nakala ya kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, ambacho ndugu mmoja alikuwa ameangusha bila kujua. Msichana huyo anasimulia yaliyofuata.
“Kitabu hicho kilikuwa chenye thamani kubwa kwangu, lakini nilikuwa nikitazama zile picha chache tu, nami sikukisoma kamwe. Zile ziara za kila mwaka ambazo akina ndugu walitembelea baba yangu zilikazia jina Yehova katika akili yangu, nami nikaja kujua kwamba Yeye ana tengenezo. Wakati nilipoanza shule ya sekondari katika mji wa Punta Gorda, swali likaulizwa darasani siku moja: Jina la Mungu ni gani? Nilipojibu, ‘Yehova,’ nilipewa adhabu ya papo hapo (kupunguziwa maksi tano pamoja na mgawo wa kazi ya kinidhamu, kama vile kusafisha choo). Kisha padri akaniita ndani na kuniambia kwamba ni lazima nisitumie jina hilo tena au ningefukuzwa shule. Kwa hiyo nilia-cha shule kwa kupenda mwenyewe nami sikurudi kamwe.
“Nilikutana na ukweli tena miaka mingi baadaye nilipokuwa nimeolewa na nikawa naishi katika Mji wa Corozal kaskazini. Niliona kipande cha karatasi kikipeperushwa na upepo mwanana, nikakiokota, na kupata kwamba kilikuwa jalada la kile kijitabu Mashahidi wa Yehova na Suala la Damu. Nilimtajia rafiki mmoja kwamba hiyo ilikuwa imani moja ya Mashahidi nisingeweza kukubaliana nayo. Akajibu kwamba pengine siku moja ningekubaliana nao. Siku iliyofuata, ndugu mmoja akazuru na kusema alikuwa amesikia kwamba napendezwa katika kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Hata ingawa nilimwambia kwamba kwa kweli sikupendezwa, alieleza kwamba haingechukua wakati mwingi, hivyo nikakubali. Hatimaye, kile kitabu Kweli nilichokuwa nimekithamini na kutunza kwa miaka minane kikatumiwa!
“Upesi, wakwe zangu wakawa wanamhimiza mume wangu akomeshe funzo langu. Halafu tukahamia kijiji kimoja kilicho peke yacho, nami nikawa sionani na Mashahidi. Mwishowe, dada mmoja akanitembelea katika huduma ya nyumba kwa nyumba, nami nikaanza upya funzo langu. Mume wangu alifanya yote awezayo kukatiza funzo. Akawa akiwa mlevi, na kufanya makelele mengi, na kunifukuza nyumbani, au kutisha atakuwa na mwanamke mwingine. Lakini nilisimama imara na kumtegemea Yehova sana kwa sala. Miaka miwili iliyopita Yehova alijibu sala zangu kupita sana matazamio yangu.
“Siku moja mume wangu alikuja nyumbani uso wake wote ukiwa umechubuliwa, naye akaenda moja kwa moja kitandani. Baadaye siku hiyo akasema, ‘Nataka kujifunza Biblia pia!’ Badiliko hilo liliniletea shangwe kubwa lakini pia ghadhabu ya jamaa yake. ‘Kubadili dini ni kama kubadili wazazi,’ wakamwambia, ‘hivyo wewe si mwana wetu tena!’ Kwa kuwa sasa mume wangu nami tulikuwa tumeunganishwa, tulifanya maendeleo ya haraka. Katika Desemba 5, 1987, tulibatizwa kwenye Siku ya Kusanyiko la Pekee letu la kwanza.”
Basi “samaki” wanashikwa hata katika sehemu za mbali za Belize. Ile broshua Furahia Milele Maisha Duniani! imetafsiriwa katika Ketchi kwa matumaini ya kwamba wengi zaidi katika vijiji hivi wangesaidiwa kukubali habari njema. Wale ambao wameokolewa kutoka maji yaliyochafuliwa ya mfumo wa Shetani wanafurahia maji yenye kutakata kama fuwele ya ukweli katika paradiso ya kiroho ya Yehova.
Mathalani, kijana mmoja katika Jiji la Belize alijifunza juu ya viwango safi vya Yehova kutoka Biblia. Akaacha uzoevu wake wa marijuana na dawa nyinginezo za kulevya na kubatizwa. Upesi baada ya hapo, akawa ‘mvuvi wa watu’ wa wakati wote. Pia ana pendeleo la kuwa mtumishi wa huduma katika kundi lake. Mamia ya wengine wamesaidiwa wasafishe maisha zao kwa kuandikisha kisheria ndoa zao kwa wenye mamlaka. Wengine wengi wamefundishwa kusoma na kuandika ili waweze kujifunza Neno la Mungu wao wenyewe. Hivyo kazi ya kielimu ya Mashahidi wa Yehova katika Belize haitoshelezi mahitaji ya kiroho ya watu tu bali pia inaletea jamii matokeo mengine yenye manufaa.
Kuleta Wavu Ndani
Pindi moja wanafunzi wa Yesu walifuata mwelekezo wake wakatupa wavu wao upande ule mwingine wa mashua. Kama tokeo, “hawakuweza kulivuta tena kwa sababu ya wingi wa samaki.” (Yohana 21:6) Vivyo hivyo, itikio la habari njema ni kubwa mno hivi kwamba Mashahidi katika Belize wanalipata kuwa jambo lenye kudai sana kutunza halaiki wanaokuja ndani ya tengenezo.
Kuna uhitaji mkubwa wa ndugu waliokomaa kuongoza katika makundi. Kwa wastani, kuna mzee mmoja au wawili tu katika kila kundi. Kisha, kuna lile jambo lenye kudai la kufikia sehemu zote za nchi kwa habari njema kwa ukawaida. Sehemu nyingi zaweza kufikiwa kwa barabara, lakini kwa sababu ya kukosekana usafiri wa umma, ni vigumu Mashahidi kusitawisha kupendezwa kunakopatikana au watu wenye kupendezwa kufika kwenye mikutano kwa ukawaida. Kutembea au kutumia mitumbwi ingali ndiyo njia yenye kutumika kufikia maeneo fulani yaliyo peke yayo.
Mashahidi katika Belize wanaona pia ugumu wa kupata mahali pa kutosha pa kufanyia mikutano yao ya kundi ya kila juma na makusanyiko ya kila mwaka. Jumla ya hudhurio kwenye 1987 “Tumaini Katika Yehova” Mikusanyiko ya Wilaya lilikuwa zaidi ya 2,200, karibu mara tatu hesabu ya wahubiri katika nchi. Kwa ajili ya mikusanyiko hiyo, akina ndugu walijenga jengo la muda kwenye uwanja karibu Ladyville. Sasa, wanaangalia uwezekano wa kujenga Jumba la Kusanyiko la kudumu mahali hapo.
Ingawa ushindani ni mkubwa, Mashahidi wanauitikia kwa idili. Wameonyesha hilo kwa kuzidisha ushiriki wao katika huduma ya shambani. Katika 1979 wahubiri walitumia, kwa wastani, saa 8.3 kila mwezi katika kazi ya kuhubiri. Sasa wanatumia wastani wa saa 11.3 kila mwezi. Pia kumekuwako ongezeko zuri katika safu ya mapainia. Katika 1979 kulikuwa na wastani wa mapainia wasaidizi 10 na mapainia wa kawaida 12 kila mwezi. Sasa kuna mapainia wasaidizi 51 na mapainia wa kawaida 42 kila mwezi, kuanzia umri wa miaka 14 mpaka 74.
Matazamio ya upanuzi ni makubwa, kwa kuona hudhurio lenye kutokeza la Ukumbusho wa kifo cha Kristo uliofanywa Machi 22, 1989. Akina ndugu walifanya kazi kwa bidii kuwaalika wenye kupendezwa. Matokeo yakawaje? Jumla ya hudhurio la 3,834—zaidi ya mara nne kilele cha wahubiri! Ilisisimua kuona vikundi vingi vya kikabila—Wakreole, Wamestizo, Wamaya, Wazungu, Wachina, Walebanoni, na wengine—wakichangamana pamoja kwa njia hii.
Kwa kuongezea, wale wahubiri 844 nchini wanaongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani zaidi ya elfu moja. Kwa kuendelea kutegemea Kichwa cha kundi, Yesu Kristo, kwa mwelekezo, bila shaka wengi zaidi katika Belize wataitikia mwaliko wa kuwa “wavuvi wa watu.”
[Ramani katika ukurasa wa 22]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
GULF OF MEXICO
MEXICO
BELIZE
Belize City
Punta Gorda
GUATEMALA
GULF OF HONDURAS
[Picha katika ukurasa wa 24, 25]
Ujenzi wa Jumba la Ufalme katika San Pedro, Kisiwa Ambergris