Ukristo wa Kweli Unaleta Nafuu ya Maisha Katika Sweden
SWEDEN huandalia idadi ya wakaaji wayo kimoja cha viwango vya maisha vilivyo vya juu kabisa ulimwenguni. Zaidi ya kuwa na chakula tele na nyumba kubwa, magari, mashua za anasa, televisheni, na kompyuta za kibinafsi, wakaaji wa Sweden huonea shangwe matibabu ambayo ni kama ya bure, malipo ya uzeeni na ya wasiojiweza, posho za watoto, na huduma nyingine zenye kuungwa mkono na serikali.
Hivyo huenda ukakata shauri kwamba haiwezekani mtu yeyote aweze kuleta maendeleo juu ya ubora wa maisha katika bara la jinsi hiyo. Hata hivyo, ijapokuwa na faida zote za kimwili, Sweden ina fungu la matatizo pia: talaka, uzoelevu wa kileo, utumizi mbaya wa dawa za kulevya, uhalifu, na kujiua. Dini, ambayo ingeweza kutarajiwa itokeze uvutano thabiti wa kiadili, imekufa katika Sweden. Zaidi ya asilimia 90 ya raia za taifa hilo ni wa Kanisa la Kiserikali la Lutheri, lakini ni asilimia 2.1 tu ambao huenda kwenye ibada zalo kwa ukawaida. Padri mmoja adai hivi: “Kanisa limestaafu. . . . Limepoteza kani-uhai yalo na likaacha kujishirikisha na mahitaji ya watu.”
Hata hivyo, kushindwa kwa kanisa kuleta maendeleo maishani katika Sweden kwa vyovyote si kushindwa kwa Ukristo wa kweli. Mashahidi wa Yehova wapatao 22,000 katika makundi 331 wanapata mafanikio kusaidia watu watumie kanuni za Biblia ili hali yao iwe bora. Kazi hii haikupita bila kuonwa.
“Ni lazima sisi tuvutiwe na Mashahidi wa Yehova kwa bidii yao katika kwenda nje wakiwa na ujumbe wao!” asema mwalimu mmoja wa dini katika gazeti la taifani pote la Kipentekoste Dagen (Siku Hii). Makala hiyo yaongeza hivi: “Mashahidi wa Yehova ndicho kikundi ambacho huvutia hesabu kubwa kabisa ya washiriki wapya kila mwaka na ndicho chenye umati mkubwa kabisa wa vijana . . . Sisi twapaswa kujifunza kutoka kwa Mashahidi wa Yehova!”
Kwa kweli, wale ambao kwa uhalisi wana nia ya kujifunza kutoka kwa Mashahidi wa Yehova watagundua jambo fulani. Nini hilo? Jinsi kweli za Biblia zaweza kuleta maendeleo yenye kutazamisha katika ubora wa maisha zao.
Maarifa ya Biblia Husaidia!
Fikiria barua moja ambayo ofisi ya tawi la huko la Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ilipokea kutoka kwa mama mchanga asiyefunga ndoa. Aliandika hivi: “Mimi nataka kueleza uthamini wangu kwa ajili ya maisha mema ambayo nimekuwa nikiishi tangu nilipoanza kujifunza na Mashahidi wa Yehova. Makao yangu hayana uvutaji sigareti. Nimepata kuthamini uhitaji wa kutumia wakati mwingi zaidi pamoja na binti yangu. Hali yangu ya kifedha imepata nafuu, ingawa mshahara wangu ni ule ule. Nina matatizo machache zaidi ya kuzuia kupata usingizi. Pia nina marafiki wa kweli wa kushirikiana nao. Ndiyo, mimi singebadilishana njia yangu ya maisha ya sasa na ile niliyokuwa nayo hapo kwanza.”
Kielelezo kingine chahusu talaka—jambo la kawaida sana katika Sweden. Hata hivyo, Biblia ilisaidia wenzi wa ndoa ambao majina yao ni Arne na Ketie. Walikuwa wamefunga ndoa kwa miaka 13 wakiwa na watoto wawili wakati tofauti za kibinafsi ziliposababisha wapate talaka. Walichukiana.
Arne, aliyehama ili akaishi peke yake, alifikiwa na Mashahidi wa Yehova na akaanza kujifunza Biblia. Mwanamume huyo alisisimukia sana mambo aliyojifunza hivi kwamba siku moja alimwendea Ketie mbio na kujaribu kumlazimisha yeye na watoto wajifunze pia! Ketie alipokataa, alimtupa dhidi ya ukuta na kusema: “Wewe jifunze, au sivyo nitakuua!” Ketie aliwapigia simu Mashahidi wa Yehova akalalamika, akisema: “Kwani huyo Yehova ni Mungu mkatili kama nini?”
Ketie aliambiwa kwa saburi kwamba Yehova ni Mungu mwenye upendo asiyelazimisha mtu yeyote. Akawa na hamu ya kuulizia-ulizia na kutaka kujifunza mengi zaidi. Kwa kadiri Arne alivyopata maarifa zaidi juu ya kanuni za kimungu, alituliza msisimuko na akarudia hali ya kuweza kunena mambo pamoja na Ketie. Walionana kwa ukawaida kwenye mikutano katika Jumba la Ufalme. Tokeo likawa nini? Baada ya wote wawili kuwa Mashahidi waliobatizwa, walifunga ndoa upya! Wamekuwa katika hali ya kufunga ndoa kwa miaka minane, na Arne hutumikia akiwa mzee wa kundi. “Ndoa yetu haijapata kuwa bora kuliko ilivyo sasa,” wao husema. “Sisi twapaswa sana kumtolea Yehova asante.”
Kweli za Biblia zinasaidia vijana pia wafanyie maendeleo ubora wa maisha zao. Kijana mwanamume jina lake David akumbuka hivi: “Wazazi wangu walitalikiana, na kila jambo lilionekana likienda kombo katika maisha yangu. Mimi sikujali chochote. Mara nyingi nilikosa kwenda shule na sikufanya masomo ya nyumbani wakati wa miaka mitatu ya mwisho. Nyakati fulani hata niliona kwamba haistahili kuishi. Nilivaa suruali-jini zilizo matambara na viatu vikuukuu. Nywele zangu ziliteremka zikafika mgongoni katikati. Nilijaribu mitindo-maisha iliyo tofauti, kama ule wa “panki-roka” na “hadi-roka.” Nilivuta sigareti na kunywa na kuhusika katika uhalifu.
“Katika 1986 mmoja wa Mashahidi wa Yehova alinizuru. ‘Hii ni namna nyingine ya zile dini za kishaka-shaka,’ nikawaza. ‘Acha nimwulize maswali fulani ambayo hataweza kujibu.’ Nilishangaa alipoyajibu. Niliambatana naye kwenye moja la mafunzo yake ya Biblia nikapata kwamba yeye alikuwa na jibu la kiakili kwa karibu kila jambo—kwamba ukweli haukuwa na kasoro yoyote. Nilihudhuria kusanyiko nikastaajabu kuwaona watu hao nadhifu wenye urafiki. Nilianza kwenda kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova nikashangaa wakati wengi sana walipokuja wakanisalimu kwa mkono. Lo, miongoni mwa watu hao mlikuwamo mwungamano ulioje!”
Mwaka mmoja na nusu baadaye, David alibatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Watu wa ukoo wake, marafiki wa zamani, walimu, na wengine hawakuweza kuamini kwamba kijana huyu mwanamume aliyevalia nadhifu na kujipamba vizuri ni David yule waliyekuwa wamemjua.
Matokeo Yenye Kuenea Pote
Kuhubiri mlango kwa mlango katika Sweden kwaweza kuvunja moyo nyakati fulani. Msweden hulinda ufaragha wake kwa bidii nyingi. Kengele ya mlangoni iliapo, huenda akatazama kupitia tundu la mlangoni, na milango mingi hubaki imefungwa kuwazuia Mashahidi wa Yehova. Lakini wao hawaachi kujipa moyo. Mashahidi wajua kwamba malaika waweza kupata mahali walipo watu mmoja mmoja wenye mwelekeo mwadilifu. (Ufunuo 14:6; linganisha Mathayo 13:41.) Ukweli ukiisha kuingia ndani ya maisha ya mtu, mara nyingi huo huenea—kama viwimbi juu ya maji—hadi kwa watu wa ukoo na marafiki.
Mwanamke mmoja katika Stockholm akumbuka akiketi kwenye meza ya jikoni mwake akilia machozi kuhusu mashaka makubwa ya maisha yake. “Nilihitaji sana msaada,” yeye asema. “Kwa ghafula, nikaanza kusali hivi: ‘Mungu, mimi nataka kuongea nawe juu ya maisha.’ Kengele ya mlangoni ililia. Nilipochungulia katika tundu la mlangoni, nikaona mwanamume aliyevalia vizuri, kwa hiyo nikafungua mlango. Alisema alitaka kushiriki mawazo fulani yenye kutia moyo kutokana na Neno la Mungu. Alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nikamwuliza kama alikuwa ametembelea watu wengine katika ghorofa yangu. ‘La,’ yeye akasema, ‘nilikuwa njiani kwenda nyumbani kutoka funzo moja la Biblia nilipoamua kufanya ziara kadhaa. Imetukia kwamba nikaanzia hapa.’ Nilimaka kwa sababu mimi niliishi ghorofa kadhaa juu. Nilipendezwa na aliyonionyesha.”
Muda si muda mwanamke huyu alianza kujifunza Biblia. Kwa shauku, alianza kushiriki mambo aliyojifunza pamoja na watu wa ukoo na marafiki. Aligawanya Biblia 28 na vitabu 96. Tokeo likawa nini? Muda si muda, mume wake, wawili wa dada zake, mpwa wake wa kike na wa kiume, ndugu-mkwe, baba na mama yake, mwana wa mume wake kutokana na ndoa fulani iliyotangulia, mfanya kazi mwenzie, na mfanya kazi mwenzi wa mumeye na mke wake wakawa wakijifunza Biblia na kujitayarisha kwa ubatizo. Kufikia hapa, watu 13 wamekuwa na fursa ya kufanya hali ya maisha yao ipate nafuu kupitia ziara moja iliyofanywa mlangoni na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Mwanamke huyu asema hivi: “Kujipatanisha na mapenzi ya Yehova kumeleta faida nyingi sana katika maisha zetu hivi kwamba twapasa kumtolea asante tukiwa tumepiga magoti kila siku!”
Kutoa Ushahidi Shuleni
Katika shule nyingi katika Sweden mna matatizo mazito ya kinidhamu. Lakini Mashahidi wachanga wanathibitika kuwa uvutano wenye matokeo chanya kwa kushiriki kweli za Biblia pamoja na walimu na wanafunzi wenzao. Kwa kielelezo, Jorgen mchanga aliwaambia wazi walimu wake na wanadarasa kwamba yeye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Alistahiwa kwa uwazi wake na mwenendo mwema. Sikuzote Jorgen alijibu kwa uungwana na kwa marejezeo kwenye Biblia. Hiyo ilikaza maoni mazuri ya kina kirefu katika akili za wanadarasa wenzake. Jorgen aripoti hivi:
“Mwaka mmoja baada ya kumaliza shule, nilikutana na Peter, mwanadarasa wa hapo zamani. Baada ya mazungumzo fulani, nilianza kuongoza naye funzo la Biblia. Kwa kuwa mama yake alikuwa akipinga, tulijifunzia ufuoni. Peter alibatizwa katika Machi 1988. Mama yake aliona kwamba mwanaye alikuwa amebadilika akawa bora, kwa hiyo yeye pia akaanza kujifunza. Baada ya muda fulani, alibatizwa.
“Mwanadarasa mwingine wa zamani, Torbjorn, alianza kujifunza Biblia. Ndivyo na mama yake. Sasa wao pia wamebatizwa.” Kwa ujumla, wanne wa wanadarasa wa Jorgen walianza kujifunza Biblia, na wa tano ameeleza ana upendezi. “Natumaini kwamba ono hili litawatia moyo Mashahidi wachanga shuleni wasisite-site,” amalizia Jorgen. “Mwenendo wao wa Kikristo na msimamo imara kwa ajili ya ukweli huenda ukapanda mbegu ambazo baadaye huenda zikazaa tunda jema.”
Kupigania Uhuru wa Kidini
Pia Mashahidi wa Yehova wameshiriki fungu la maana katika kuanzisha uhuru wa msingi wa kidini katika Sweden. Hiyo imenufaisha kila mtu.
Kwa kielelezo, kama ilivyo katika mabara mengine yote, Mashahidi wa Yehova katika Sweden wameamua mmoja mmoja kudumisha kutokuwamo kwa Kikristo. (Yohana 17:16) Tokeo ni kwamba, wengi walihukumiwa vifungo virefu gerezani. Lakini katika 1966 hatua kubwa ilichukuliwa ya uhuru wa kidini wakati wenye mamlaka walipoamua kwamba ikingojewa kuchunguza watu mmoja mmoja, Mashahidi hawangeitwa kwa ajili ya utumishi wa kijeshi. (Isaya 2:2-4) Uvumilio wa maoni ya watu kuhusu dini katika Sweden umetumika kuwa kigezo kwa serikali nyinginezo.
Jambo jingine lilihusu haki za wagonjwa. Mashahidi wa Yehova huichukua kwa uzito amri ya Biblia ‘kushika mwiko wa damu’ na kwa hiyo hukataa kutiwa damu mishipani. (Matendo 15:28, 29) Ingawa si madaktari wote na wanatiba ambao wamestahi msimamo huu wa Kimaandiko, juzijuzi jarida la kitiba lililo mashuhuri zaidi katika Sweden lilitangaza hivi katika kichwa kimoja kikubwa: “Katao la Kutiwa Damu Mishipani Lapasa Kustahiwa Ikiwa Mgonjwa Ayajua Matokeo.”
Maneno hayo yalikuwa kichwa cha ripoti iliyohusu mkutano mmoja wa Baraza la Kitaifa la Afya na Halinjema na Ujumbe wa Kanuni za Kitiba za Sosaiti ya Tiba Sweden. Baada ya kuzungumza hali ya Mashahidi wa Yehova, wenye mamlaka hawa waliamua kuhimiza madaktari wote wakubali hiari ya mtu wakati mgonjwa mwenye akili timamu kisheria—kuanzia umri wa miaka 15 na zaidi—akataapo kutiwa damu mishipani. Walitambua kwamba sasa kuna kizuizi kikubwa zaidi juu ya kutia damu mishipani kwa sababu ya hatari ya kuambukiza magonjwa. Hata hivyo, la maana zaidi ni kwamba uamuzi wao wa kuzinduka waunga mkono haki ya msingi ya mgonjwa yeyote kukataa namna fulani hususa ya matibabu.
Kwa kweli, wakaaji walio wengi Sweden huonea shangwe maisha mema kimwili. Lakini wengi wahitaji kujengwa kiadili na kiroho. Bila shaka, Wakristo wa kweli katika bara hilo wanasaidia kuletea nafuu maisha za wote walio na nia ya kujifunza na kutumia Neno la Mungu. Watu hao mmoja mmoja huonea shangwe pia tazamio la uhai wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu unaokuja.—Yohana 17:3; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4.
[Ramani katika ukurasa wa 22]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
SWEDEN
NOROWEI
DENMARK
FINLANDI
POLANDI
UJEREMANI MASHARIKI
UJEREMANI MAGHARIBI
URUSI