“Hii ni Nyumba Yako”
“HII ni nyumba yako—tumeiongezea.” Maneno hayo yalieleza kwa ufupi mzuri kama nini hisia za wale ambao ndipo tu walikuwa wamemaliza miaka miwili ya kazi ngumu kwenye ofisi ya tawi la Watch Tower Society Australia! Maneno hayo yalielekezwa kwa Yehova Mungu, na yalikuwa sehemu ya wimbo uliotungwa kwa ajili ya pindi maalumu. Pindi gani? Kuwekwa wakfu kwa mipanuo mipya ya makao na kiwanda cha Betheli.
Mpanuo Upesi Hivyo?
Kwa kushangaza, ni muda mchache kuliko miaka saba uliokuwa umepita tangu kuwe na wakfu kama huo wa jengo-tata la Betheli lililokuwa limejengwa karibuni huko Ingleburn, kwenye viunga vya kusini-magharibi vya Sydney, Australia. Kwa nini mpanuko zaidi ukahitajiwa upesi hivyo?
Kwanza, hesabu ya Mashahidi katika Australia imeongezeka kutoka wachache kuliko 32,000 katika 1981 ikafikia kilele cha 51,152 katika Oktoba 1989, na hiyo ilitokeza uhitaji wa ongezeko la wafanya kazi wa Betheli. Tena, kulikuwako ongezeko la kutazamisha katika kiasi cha fasihi ambazo Australia ilipelekea matawi mengine. Kwa sasa, Australia hutokeza vichapo katika lugha 37 tofauti-tofauti ili kutimiza mahitaji ya Fiji, Indonesia, Papua New Guinea, New Caledonia, New Zealand, Visiwa vya Solomon, Tahiti, Vanuatu, Niue, Samoa ya Magharibi, Tonga, Tuvalu, na Visiwa vya Wallis, na pia Australia. Hivyo, familia ya Betheli imeongezeka haraka sana kufikia washiriki 164.
Ili kuipa nafasi familia hii yenye kukua, mapema katika 1987 mpanuo wa ghorofa tatu za ofisi ulimalizwa, hiyo ikiandaa nafasi ya ziada ya kiofisi iliyohitajiwa sana. Halafu, Baraza Linaloongoza lilikubali ujenzi wa kiwanda chenye ghorofa tatu na mpanuo wa makao ya ghorofa tano. Katika Januari 1988 kazi ilianza ya ziada ya kiwanda kipya, ambacho kingeandaa nafasi zaidi ya sakafu yenye meta za mraba 3,600. Miezi michache baadaye, kazi ilianza ya mpanuo wa makao, ambao ungeandaa vyumba vya kulala 51 zaidi.
Dhabihu na Upaji Wenye Ukarimu
Mialiko ilipelekwa kwenye makundi kotekote nchini ikitoa wito kwa wenye kujitolea ambao wangeweza kuwa sehemu ya “familia ya ujenzi” kwa muda unaofikia miaka miwili. Itikio lilikuwa kubwa mno, na wenye kujitolea kutoka kazi za namna zote waliitikia kwa utayari. Fomu za maombi ya watu mbalimbali 700 zilipokewa, na katika kipindi hicho cha ujenzi, jumla ya wenye kujitolea 270 walikuja wakafanya kazi kwenye mradi huo kwa vipindi vyenye kutofautiana kuanzia majuma mawili hadi karibu miaka miwili.
Shahidi mmoja alikuwa na biashara ya kuhamisha udongo katika mkoa wa kaskazini wa Queensland. Aliuza sehemu ya biashara yake, na yeye na mke wake wakawa sehemu ya familia ya ujenzi tangu mwanzo wayo. Alinunua mashine kubwa ya uchimbaji yenye kuambatana na lori na kufanya sehemu kubwa ya uchimbaji uliohitajiwa kabisa bila kugharimisha Sosaiti. Kadiri kubwa ya uchimbaji ilipomalizwa, aliuza mashine hiyo halafu akabaki pale kazini katika maeneo mengine ya ujenzi. Hiki ni kielelezo kimoja tu cha roho nzuri ya kujinyima iliyoonyeshwa kotekote katika mradi huo.
Mashahidi walitoa msaada wa mabomba ya malori ya kubeba zege ili kumimina meta za kyubiki 3,300 za zege lililohitajiwa kwa zile sakafu nane katika yale majengo mawili. Wengine walitoa vijengeo vilivyohitajiwa kwa yale matangi ya maji ya lita 22,000 yenye kujengwa kwa zege, na Mashahidi wenye kufanya kazi kiwandani wakatoa jitihada yao kujenga matangi hayo.
Bila shaka, si wote hao wenye kujitolea waliokuwa wanakazi wenye ujuzi. Kwa kweli, wanaume wengi vijana walijifunza stadi mpya papo hapo ujenzini. Hesabu fulani wakawa wajenga-matofali walio hodari walipokuwa wakisaidia kujenga yale matofali nusu milioni yaliyohitajiwa kwa mradi huo. Wengine walijifunza kujenga ukuta na kuweka sakafu kwa kutumia vigae, na katika muda wa majuma machache tu, dada mmoja akajua sana kubandika karatasi pambo la ukutani.
Siku ya Wakfu
Siku ya wakfu, Jumamosi, Novemba 25, 1989, ilipambazuka ikiwa nyangavu na yenye jua—siku nzuri ya mwisho-mwisho wa masika. Sakafu ya pili ya ile ziada ya kiwanda kipya ilikuwa imeondolewa vilivyomo ili iwe jumba kuu la programu ya wakfu. Televisheni ya uonyeshaji wa ndani tu ulifungamanisha visehemu vya sakafu zile nyingine za kiwanda na sakafu ya usafirishaji vitabu, jumba la mikutano ya Betheli, na chumba cha maakuli ya Betheli. Hiyo iliruhusu kuwe na nafasi ya watu zaidi ya 3,000 kuketi ndani ya nyumba wakiwa wamestareheka.
Kwa sababu nafasi ilikuwa kidogo, ni wale tu waliobatizwa karibu miaka 40 walioalikwa kuhudhuria, pamoja na wageni wa kibinafsi wa Betheli na familia za wajenzi. Viburudisho vilikuwako asubuhi, na chakula cha mchana chenye ladha kikaandaliwa adhuhuri. Saa 3:00 asubuhi, mkutano wa kila mwaka wa Watchtower Society of Australia ulifanywa, na washiriki wote 21 wa shirika la Australia wakahudhuria. Baada ya mambo ya kisheria yaliyohitajiwa kabisa kutimizwa, wengine walialikwa ndani ya mkutano huo, na wote wakafurahi sana kusikia hotuba ikitolewa na Theodore Jaracz wa Baraza Linaloongoza.
Saa 7:45 alasiri, dakika 15 za muziki wa Ufalme zikawa utangulizi wa programu ya wakfu. Wasikilizaji walifurahi kusikia ripoti mbalimbali, masimulizi ya kufurahisha, maono, na maelezo ya washiriki watatu wa Baraza Linaloongoza waliokuwapo. Kati yao, Carey Barber na Daniel Sydlik walikuwa wakifanya ziara yao ya kwanza kwenye bara hilo la huko chini. Ndugu Barber alihutubu juu ya habari “Mavuno Ni Mwisho wa Enzi,” naye Ndugu Sydlik akashughulikia kichwa “Wenye Furaha ni Watu Ambao Mungu Wao Ni Yehova.” Ndugu Jaracz, aliyekuwa akitumikia tawi la Australia akiwa mwangalizi wa eneo la dunia, alitoa hotuba ya wakfu.
Sehemu yenye upendezi mwingi wa programu ilikuwa kuimbwa kwa wimbo wenye beti nne kabla tu ya hotuba ya wakfu. Kikitegemea maneno ya Isaya kwenye 60:22, kichwa cha wimbo huo kilikuwa “Mdogo Awa Elfu.” Katika maneno ya wimbo huo shukrani zilitolewa kwa Yehova ya kwamba wenye kujitolea wengi wenye nia walikuwa wamepata pendeleo la kuiongezea ‘nyumba yake’ katika sehemu hii ya shamba la ulimwenguni pote.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Nyongeza mpya kwenye sehemu ya uchapaji huko Ingleburn, N.S.W., Australia
C. Barber
T. Jaracz
D. Sydlik