Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 1/1 kur. 25-29
  • Uvumilivu Wenye Shangwe Katika Mashariki Ya Kati

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uvumilivu Wenye Shangwe Katika Mashariki Ya Kati
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • ‘Upande Wenye Matokeo Mazuri’
  • “Jina la Yehova Liliokoa Uhai Wangu”
  • “Utunzaji wa Yehova Ulituzunguka”
  • Msaada Usiotazamiwa Katika Kitendo!
  • “Nyinyi Ni Watu wa Aina Gani?”
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 1/1 kur. 25-29

Uvumilivu Wenye Shangwe Katika Mashariki Ya Kati

Ripoti hii inayosisimua inakuja kutoka kwa Mashahidi wa Yehova Katika Lebanoni

MWAKA wetu wa utumishi wa 1990 ulianza kwa vipindi vya jeuri ya kufyatua risasi katika Beirut. Halafu kukawa na utulivu ulioendelea kuanzia mwisho wa Septemba 1989 mpaka Januari 1990.

Wakati wa miezi hiyo kilele kipya cha wahubiri 2,659 kiliripotiwa (katika Novemba), kikilinganishwa na 2,467 katika mwaka wa utumishi wa 1989. Watu 44 walibatizwa, na kila mwezi wastani wa 65 walishiriki katika utumishi wa painia msaidizi. Kwa mara ya kwanza, mafunzo ya Biblia zaidi ya 2,000 yaliripotiwa, nasi tukaanza kutazamia mambo ambayo yangeweza kutimizwa katika wakati ujao.

Lakini vita ikalipuka tena katika Beirut ya Mashariki, ambako ndiko kwenye makundi mengi zaidi, na wengi wa ndugu zetu wakalazimika kukimbilia sehemu nyingine za nchi. Kwa siku nyingi hatukupashana habari na makundi katika maeneo yaliyopatwa na mambo hayo, na ripoti za utumishi wa shambani hazikuwa kamili. Hata hivyo, akina ndugu waliokuwa wametawanyika walijiunga na makundi katika maeneo waliyokimbilia, na kazi ya nyumba kwa nyumba ikaendelea kwa matokeo mazuri kotekote nchini. Kwa sasa, nyingi za nyumba za ndugu zetu ziliteketezwa au zikaharibiwa na mitupo ya makombora. Dada mmoja alipoteza uhai wake.

Tukiwa na uhakika tulitegemea Yehova kwa msaada na mwongozo. Mapainia wenye moyo mkuu walijitolea kwa moyo wa kupenda wakapeleka misaada ya kiroho, pamoja na chakula na maji, kwa ndugu zetu katika majimbo yenye kuzingirwa. Kwa kusukumwa na upendo kwa ajili ya Yehova na akina ndugu, hata kwa kujihatarisha wakavuka barabara zilizokuwa zimetegewa baruti. Ushahidi mzuri ulitolewa watu walipokuwa wakiona msaada wenye kuzijia familia za ndugu zetu. Waliona yale ambayo upendo wa kweli unaweza kufanya wakati wote wanapokuwa wameunganika katika ibada ya yule Mungu mmoja wa kweli, Yehova.—Yohana 13:34, 35; 15:13.

Wakati wa mwaka wa utumishi, akina ndugu hawakukosa hata toleo moja la magazeti yetu. Kama vile ilivyokuwa tayari kuhusu Mnara wa Mlinzi, gazeti Amkeni! katika Kiarabu lilianza kuchapishwa wakati mmoja na Kiingereza, kuanza na toleo la Januari 8, 1990. Mashahidi na watu wenye kupendezwa waliona shangwe sana. Pia ilisisimua kuona vitolewa vipya katika Kiarabu, kama ile broshua Should You Believe in the Trinity? na vitabu The Bible—God’s Word or Man’s? na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia.

Zawadi hizi za kiroho zilitolewa ijapokuwa kufungwa kwa viwanda vingi na mashirika mengine katika Beirut. Hali ya kiuchumi ni mbaya kote nchini. Mahali pengi hapana nguvu za umeme, wala maji, wala huduma ya simu. Sasa, acheni wengine wa ndugu zetu waeleze jinsi wamepata shangwe hata wakati wa kushindana na uharibifu wa vita ambayo imekuwa ikiendelea kwa miaka 15.

‘Upande Wenye Matokeo Mazuri’

Ndugu mmoja katika Beirut anaandika hivi: “Kwanza kabisa, mimi nampa Yehova shukrani za moyoni kwa sababu ametuweka salama ndani ya tengenezo lake la ibada safi zijapokuwa hali zote ngumu ambazo tumekabili. Wakati wa matukio ya hivi majuzi, mimi nilipata maono yaliyoniletea shangwe, nami nayaona kuwa upande wa vita ulio na matokeo mazuri.

“Wakati wa lile mimino la makombora, tuliketi pamoja na majirani katika ngazi za nyumba, kwa maana hapa ndipo mahali salama zaidi wakati wa kumiminwa kwa risasi. Tuliongea nao daima juu ya Ufalme wa Mungu kuwa utatuzi pekee kwa matatizo ya ainabinadamu, na mara nyingi tulisali kwa Mungu wetu, Yehova. Jambo hili likajulikana kwa wote.

“Nyakati fulani mmimino wa risasi uliendelea kwa siku kadhaa, na hatukuweza kuhudhuria mikutano. Hivyo basi nikaja na gazeti Mnara wa Mlinzi na kujifunza hilo nikiwa nimekalia ngazi ya nyumba. Jambo hilo liliamsha upendezi wa majirani zetu. Wengine wao walikuwa wamekuwa hawaongei nasi kwa sababu sisi ni Mashahidi wa Yehova. Lakini nyumba yetu ilipopigwa na risau moja, walishangazwa sana na upendo ambao ndugu zetu walionyesha. Sasa walitaka kuongea nasi. Hiyo ilituwezesha kuwaangushia maandikisho fulani ya Amkeni!

“Maono haya yalinifanya niazimie kuendelea juu ya ukweli. Yehova anastahili ibada yetu yote na heshima yetu yote na utukufu wote.”

“Jina la Yehova Liliokoa Uhai Wangu”

Ndugu mmoja kutoka Kundi la Ras Beirut anasimulia hivi: “Mke wangu, wavulana wetu wadogo wawili, na mimi tulianza siku yetu katika huduma ya nyumba kwa nyumba katika sehemu ya magharibi ya Beirut. Saa za mchana, tulikuwa na mkutano wa lugha ya Kiingereza kwenye nyumba yangu. Kufika saa 12:30 jioni ilikuwa giza. Watu peke yao waliokuwa barabarani walikuwa wanaume wenye silaha. Makombora yalikuwa yakimiminika chini. Wakaaji walio wengi wa jengo letu wakawa wamekimbia. Hakukuwa na maji wala nguvu za umeme. Halafu tukasikia mlango ukigongwa.

“Kwa kufikiri ingeweza kuwa mmoja wa majirani zetu mwenye kuhitaji maji au mkate, mke wangu akafungua mlango. Wenye kusimama hapo walikuwa wanaume wanne wenye silaha. Walielekeza bunduki zao kwenye mke wangu na wakauliza niko wapi kwa kunitaja jina. Juma hilo wanaume tisa walikuwa wamechukuliwa kutoka nyumba zao kwa njia hii na kuuawa mara hiyo. Wanaume hao wenye silaha waliponiona, walielekeza bunduki zao otomatiki kwenye kichwa changu na kuniagiza niende pamoja nao. Mimi nikawaambia hivi: ‘Nitaenda pamoja nanyi. Lakini kwanza acheni nivae.’ Nilisali kwa Yehova kwa moyo wangu wote, nikiomba msaada wake. Nilipokuwa nikimaliza kusali, nilijiona nimestarehe sana na nikaanza kuwaona wanaume hawa wenye silaha na wenye kutisha kuwa watu wa kawaida tu. Ningeweza kuongea nao bila hofu.

“Nikawauliza hivi: ‘Mnataka nini kwangu? Acheni tuongee kidogo ndani ya nyumba kabla hatujaondoka.’ Tukiisha kuingia sebuleni, mkubwa wao akaniuliza hivi: ‘Wewe una haki gani kuingia nyumba za watu na kuwahubiri?’ Mimi nikajibu: ‘Wewe unabeba bunduki kutekeleza mapenzi yako, na hakuna mtu anayekupinga. Mimi nabeba habari njema za amani ambazo Yesu aliagiza zihubiriwe.’ Ndipo nikaeleza imani na kazi ya Mashahidi wa Yehova. Mara tu nilipotaja jina Yehova, wao wakasema: ‘Sisi tutatosheka kukuulizia maswali hapa. Hakuna uhitaji wa sisi kwenda pamoja nawe.’ Inaonekana kwamba mmoja miongoni mwao alijuana na ndugu fulani. Akasema hivi: ‘Huyu ni kama Jarjoura.’

“Tuliwatolea ushahidi washika-bunduki hao na kujibu maswali yao kwa muda wa saa moja na nusu. Halafu, badala ya kunichukua katika shimo la mizigo katika gari lao kama walivyokuwa wamefanyia wengine, waliomba msamaha, wakanibusu, wakajitolea kunipa msaada wakati wowote ikiwa ningeuhitaji, na kwenda zao. Muda wote huo, nilijiona nikiwa na ulinzi wa Yehova. Kushiriki katika kazi ya nyumba kwa nyumba asubuhi hiyo na kuhudhuria mkutano saa za mchana kulikuwa kumeniimarisha nisimame thabiti. Kwa kweli, jina la Yehova liliokoa uhai wangu.”—Mithali 18:10.

“Utunzaji wa Yehova Ulituzunguka”

Ndugu mwingine anaandika hivi kutoka Beirut: “Ilikuwa Jumatano, tarehe 31 ya Januari, 1990. Nikiwa ninafanya kazi pamoja na ndugu yangu kwenye nyumba ya dada mmoja, pigano lilianza tena. Makombora yakalipuka kila mahali. Kwa sababu ya pigano kali, hatungeweza kurudi nyumbani. Dada huyo alikuwa mkaribishaji sana hata ingawa alikuwa na vipande vichache tu vya mkate.

“Mimi nilikuwa na wasiwasi sana juu ya mke wangu kwa sababu yeye ni Mfilipino na hakuzoea jeuri ya vita. Hata hivyo, siku ya pili niliweza kuondoka niende nyumbani kwangu. Marundo ya vyombo vya nyumbani yalipingamiza barabara, lakini asante kwa Yehova, familia yangu ilikuwa salama. Baada ya utulivu mfupi, lile mimino la risasi likaanza tena. Tulijificha ndani ya nyumba ya ndugu iliyo karibu na yetu. Tulikuwa watano—mke wangu, mwana wangu wa miaka miwili, mimi, ndugu yangu, na mke wake. Makombora, risasi, na roketi zilianguka kila mahali kutuzunguka, lakini utunzaji wa Yehova ulituzunguka. Siku mbili za mmimino wa risasi zikapita, hali sisi tukiendelea kungoja tukiwa chini na huku moshi wa makombora ukiwa katika mianzi ya pua zetu.

“Tulipokuwa tukisikiliza milipuko ile, tulikumbuka maneno ya Daudi kwenye Zaburi 18:1-9, 16-22, 29, 30. Katika muda huo mgumu, na yajapokuwa yote yaliyokuwa yakitendeka, sisi tulifurahi na tukaweza bado kuwa na uso wenye furaha. Tulisali kwa Yehova kwamba ikiwa tungepaswa kufa, ingefaa tufe kwa urahisi, bila mteseko. Tumaini letu katika ufufuo lilikuwa imara.

“Siku iliyofuata haikuaminika. Karibu makombora 25 hivi yalianguka karibu na nyumba ambapo tulikuwa tukijificha, lakini hakuna mmoja wetu aliyeumia. Unaweza kuwazia maono yetu ya ndani tulipojisikia tukiwa na ulinzi wa Yehova? Asubuhi iliyofuata, tuliamua kukimbia mara hiyo. Gari langu pekee ndilo lililokuwa barabarani bila kuteketezwa. Niliendesha kati ya baruti zilizotegwa na makombora, na asante kwa Yehova, tuliweza kuponyoka kwenda eneo lililokuwa tulivu kuliko letu. Huko, kwa upendo ndugu zetu walitutolea mavazi, chakula, na pesa.

“Yajapokuwa magumu yote, tulijiona wenye furaha kwa sababu Yehova alikuwa pamoja nasi. Ilikuwa ni kana kwamba yeye alikuwa ametuma malaika zake kuepusha makombora yasitupate. (Zaburi 34:7) Ndiyo, shangwe yetu ilikuwa kubwa. Lakini shangwe yetu itakuwa kubwa zaidi baada ya kuokoka Har–Magedoni.”

Msaada Usiotazamiwa Katika Kitendo!

Maeneo fulani ya Beirut yalionekana kana kwamba tetemeko la dunia lilikuwa limepiga. Nyingi za nyumba za ndugu ziliharibiwa kidogo au zikaharibiwa kabisa. Hatari hii ya hivi majuzi ilipotokea, Halmashauri ya Tawi ilitengeneza halmashauri ya msaada usiotazamiwa ili kutunza mahitaji ya akina ndugu. Ilianza shughuli katika Februari 16, 1990, karibu tu na wakati ambapo sisi tungeweza hatimaye kuhamia maeneo yenye kukumbwa na shida. Kusudi la halmashauri hii lilikuwa na sehemu tatu: kuwapa akina ndugu kitia-moyo cha kiroho; kutunza mahitaji yao ya pesa, chakula, na maji; na kuwasaidia warekebishe au kujenga upya nyumba zao.

Hakukuwa na uhitaji wa kutoa mwito wa wenye kujitolea kwa hiari. Kila siku wengi walikuja mapema asubuhi kusaidia. Haya ni mengine ya maelezo ya wale waliosaidiwa:

Dada mmoja, wakati nyumba yake ilipokuwa ikisafishwa na kurudishwa, alisema hivi: “Mimi nilisikia juu ya msaada uliotolewa na akina ndugu wakati mabaya makubwa yanapotokea. Sasa mimi nauona na kujisikia nikisaidiwa hivyo.” Hata jirani yake, ambaye ni mwanamke Mwislamu, alimwambia hivi dada huyu: “Kwa kweli nyinyi mnapendana. Yenu ndiyo dini ya haki. Sasa mimi nitakimbilia kijiji chetu nikaambie kila mtu jambo mnalofanya hapa.” Jirani huyu aliwaletea chakula wafanya kazi wa kujitolea kwa moyo wa kupenda.

Dada mmoja mzee-mzee alieleza hivi: “Mimi nilitazamia kwamba mngekuja kunitembelea, lakini sikutazamia kwamba Sosaiti ingetuma mtu wa kuniletea maji.” Alikuwa akilia alipokuwa akimbusu ndugu aliyekuja kumsaidia.

Familia moja ya watatu—mume na mke waliokuwa wahubiri wasiobatizwa na kivulana wao—walitembelewa na kupewa sanduku kubwa la maziwa, mkate, maji ya kunywa, na pesa. Walipoambiwa kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wamefanya mpango huu, mume alisema hivi: “Mimi nilikuwa katika Kanisa Evanjeliko kwa miaka 11 na nilikuwa mtendaji sana. Lakini kwa miaka hii 15 ya vita katika Lebanoni, wao hawakufikiria kamwe kufanya jambo kama hili kwa ajili ya washiriki wao.” Akaendelea kusema: “Kwa kweli hili ndilo tengenezo la pekee la Mungu.” Mume huyo na mke wake walibatizwa kwenye kusanyiko moja katika Mei 1990.

Mzee mmoja alieleza hivi: “Maneno hayatoshi kutoa asante zetu kwa kazi za upendo ambazo nyinyi mlifanya kuelekea ndugu waliopatwa na shida. Mimi nilivutiwa sana mpaka nikatoa machozi nilipoona kikundi cha ndugu vijana, wenye kujitolea, wakijenga upya nyumba ya wazazi wangu. Hata majirani zetu wasio Mashahidi walionyesha uthamini wao. Sisi tunashukuru Yehova na tengenezo lake kikweli kwa ajili ya tegemezo lao lenye msaada ambalo limetolewa. Ni ya kweli kama nini maneno ya mtunga zaburi kwenye Zaburi 144:15: “Heri watu wenye BWANA [Yehova, NW] kuwa Mungu wao.’”

“Nyinyi Ni Watu wa Aina Gani?”

Dada mmoja mwenye familia aliandika hivi: “Ningependa kutoa shukrani zangu za ndani sana kwa upendo wa Yehova na tengenezo lake. Nyumba yangu iligongwa na risasi nyingi na kuchomwa. Wengi walituambia kwamba haingeweza kutengenezwa. Hata hivyo, ndiyo hii hapa ikiwa imerekebishwa kabisa kana kwamba hakuna jambo lililoipata, ikiwa imezungukwa na mamia ya nyumba katika barabara yetu ambayo yalichomwa na kuharibiwa.

“Hata majirani zetu, ambao si Mashahidi wa Yehova, wanauliza hivi: ‘Upendo huu unatoka wapi? Nyinyi ni watu wa aina gani? Ni nani watu hawa mmoja mmoja wanaofanya kazi kwa bidii ya jinsi hii na walio watulivu sana na wenye kujiendesha vema? Abarikiwe Mungu ambaye amewapa nyinyi upendo huu na roho ya kujinyima.’ Yanafaa kama nini maneno ya Zaburi 84:11, 12: ‘Kwa kuwa BWANA [Yehova, NW], Mungu, ni jua na ngao, BWANA [Yehova, NW] atatoa neema na utukufu. Hatawanyima kitu chema hao waendao kwa ukamilifu. Ee BWANA [Yehova, NW] wa majeshi, heri mwanadamu anayekutumaini Wewe.’”

Mwanamume mmoja ambaye mke na watoto wake ni Mashahidi wa Yehova aliandika hivi: “Ningependa kuwatolea nyinyi asante kwa msaada katika kutengeneza nyumba yetu. Kazi yenu ilionyesha upendo wa Kikristo wenye moyo mweupe ambao ni mchache sana siku hizi. Mungu na abariki jitihada zenu.”

Baada ya nyumba ya mzee mmoja kufanywa kama ilivyokuwa, alisema hivi: “Vinywa vyetu vinashindwa kueleza yaliyo katika mioyo yetu. Hatuwezi kupata maneno ya kuwaeleza juu ya uthamini wetu kwa Yehova na tengenezo lake. Tulijisikia tukiwa na ukaribu wa Yehova katika mabaya yaliyotupata. Upendo wenu umewatia moyo washiriki wote wa familia yangu kushiriki katika kusaidia wengine walio katika uhitaji.”

Katika Aprili, watu 194 katika Lebanoni waliionea shangwe kazi ya painia msaidizi. Usiku wa Ukumbusho ulikuwa mtulivu kuliko siku nyinginezo, na Ukumbusho ulifanywa ukiwa na hudhurio la jumla ya 5,034. Makusanyiko yote yaliyopangwa yalifanywa, na jumla ya hesabu ya watu waliobatizwa kwa mwaka huo ilikuwa , ikilinganishwa na 135 mwaka uliopita. Familia nyingi katika makundi ziliondoka nchini daima. Lakini wenye kupendezwa karibuni wanafanya maendeleo kuelekea ubatizo, na hesabu ya wahubiri wa Ufalme inaendelea kuongezeka. Wakati wa mwaka wa utumishi wa 1990, watu wote wa Yehova katika Lebanoni waliona uaminifu wa Yehova alipotutunza na kutuongoza kuzipitia nyakati zenye msukosuko.—Zaburi 33:4, 5; 34:1-5.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki