Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 2/15 uku. 30
  • Ni kwa Njia Gani Adamu Alifanywa Katika Mfano wa Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni kwa Njia Gani Adamu Alifanywa Katika Mfano wa Mungu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Matokeo ya Dhambi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 2/15 uku. 30

Ni kwa Njia Gani Adamu Alifanywa Katika Mfano wa Mungu?

KWA kufanywa katika mfano wa Muumba wake Mtukufu, Adamu alikuwa na sifa za kimungu za upendo, hekima, haki, na uwezo; kwa hiyo alikuwa mwenye uwezo wa kutambua mema na mabaya uliohusika na dhamiri, jambo ambalo lilikuwa geni kabisa katika eneo la uhai wa kidunia. Akiwa katika mfano wa Mungu, Adamu angekuwa mtawala wa tufe lote na kutiisha viumbe wa baharini na barani na ndege wa angani.

Ili awe na sifa za kimungu, haikuhitajika kwamba Adamu awe kiumbe wa kiroho, kwa jumla au kwa sehemu. Yehova alimfanyiza mwanadamu kwa mavumbi ya nchi, akaweka ndani yake kani (nguvu) ya uhai hivyo akawa nafsi hai, na akampa uwezo wa kuonyesha mfano na sura ya Muumba wake. “Mtu wa kwanza atoka katika nchi, na ni wa udongo.” “Mtu wa kwanza, Adamu, akawa nafsi iliyo hai.” (Mwanzo 2:7; 1 Wakorintho 15:45, 47) Hiyo ilikuwa katika mwaka wa 4026 K. W. K. Yaelekea sana kwamba ilitokea wakati wa mwisho wa mwaka kwa kuwa kalenda nyingi za kale za ainabinadamu zilianza kuhesabu wakati kuanzia majira ya mwisho wa mwaka karibu na October 1 hivi, au wakati wa mwezi mwandamo wa kwanza wa mwaka-mwezi wa kijumuiya.

Makao ya Adamu yalikuwa paradiso ya pekee, bustani halisi ya kupendeza iliyoitwa Edeni, ambayo iliandaa vitu vyote vya kimwili vilivyohitajiwa kwa uhai, kwa maana hapo palikuwa na “kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa” kwa ajili ya riziki yake ya daima. (Mwanzo 2:9) Kila mahali Adamu alizungukwa na wanyama wa kila aina na namna. Lakini Adamu alikuwa peke yake. Hakukuwa na kiumbe mwingine wa ‘jinsi yake’ ambaye angeongea naye. Yehova alitambua kwamba “si vema huyo mtu awe peke yake.” Kwa hiyo kwa kutumia upasuaji wa kimungu, Yehova alitwaa ubavu kutoka kwa Adamu akaufanyiza kuwa mwanadamu wa kike awe mke wake na mama wa watoto wake, tukio la jinsi hilo ambalo ni la kwanza na la peke yake. Akishangilia mno kwa ajili ya msaidizi mrembo na mwenzi wa sikuzote kama huyo, Adamu alitokeza shairi la kwanza kurekodiwa, “huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu,” naye aliitwa mwanamke “kwa maana ametwaliwa katika mwanamume.” Baadaye Adamu alimwita mke wake Hawa. (Mwanzo 2:18-23; 3:20) Ukweli wa masimulizi haya unashuhudiwa na Yesu na mitume. —Mathayo 19:4-6; Marko 10:6-9; Waefeso 5:31; 1 Timotheo 2:13.

Zaidi ya hayo, Yehova alibariki hawa wenye kufunga ndoa hivi karibuni na kazi nyingi yenye kufurahisha. (Linganisha Mhubiri 3:13; 5:18.) Hawakulaaniwa na uzembe. Wangekuwa wenye kujishughulisha na wenye kutenda katika kazi ya kupamba na kutunza makao yao ya bustani, na walipoendelea kuongezeka na kuijaza dunia kwa mabilioni ya jinsi yao, wangepanua Paradiso hiyo kufikia mipaka ya dunia. Hilo lilikuwa agizo la kimungu.—Mwanzo 1:28.

“Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.” (Mwanzo 1:31) Kwa kweli, kutoka mwanzoni kabisa Adamu alikuwa mkamilifu katika kila jambo. Yeye aliandaliwa na uwezo wa usemi na msamiati wa hali ya juu sana. Aliweza kuwapa viumbe wenye uhai waliomzunguka majina yenye maana. Alikuwa na uwezo wa kuwa na maongezi pamoja na Mungu wake na pamoja na mke wake.

Kwa sababu hizi zote na mengine zaidi, Adamu alipaswa ampende, amwabudu, na amtii kikamili Muumba wake Mtukufu. Zaidi ya hayo, Mtoa-Amri wa Ulimwengu wote alimtajia amri ya utii isiyo na mambo mengi na alimjulisha kikamili juu ya adhabu iliyo haki na yenye kufaa kwa kutokutii. (Mwanzo 2:16, 17; 3:2, 3) Ijapokuwa alipewa amri hiyo ya wazi iliyofungamana na adhabu nzito kwa ajili ya kutokutii, alikosa kutii.

Matokeo ya Dhambi

Hawa alidanganywa kabisa na Shetani Ibilisi, lakini “Adamu hakudanganywa,” asema mtume Paulo. (1 Timotheo 2:14) Adamu akiwa na maarifa kamili alichagua kutotii kwa hiari na kwa kusudi na baada ya hapo alijaribu kujificha kama mhalifu. Alipokuwa akihukumiwa, Adamu alijaribu kujitetea na kuwapitishia wengine daraka, hata akimshtaki Yehova kwa ajili ya dhambi yake mwenyewe ya hiari, badala ya kuonyesha sikitiko au majuto au kuomba asamehewe. “Huyo mwanamke uliyenipa [ambaye wewe ulinipa, NW] awe pamoja nami ndiye aliyenipa matunda ya mti huo, nikala.” (Mwanzo 3:7-12) Kwa hiyo Adamu alitupwa nje ya Edeni katika dunia isiyotiishwa ambayo ililaaniwa itokeze miiba na michongoma, akapate riziki ya jasho, akivuna matunda machungu ya dhambi yake. Nje ya bustani, akingojea kifo, Adamu alikuwa baba wa wana na binti, ambao kwa hao majina ya watatu tu ndiyo yamehifadhiwa—Kaini, Habili, na Sethi. Adamu alipitisha dhambi na kifo chenye kurithiwa kwa watoto wake wote, kwa kuwa yeye mwenyewe alikuwa mwenye dhambi.—Mwanzo 3:23; 4:1, 2, 25.

Huo ndio uliokuwa mwanzo wenye huzuni ambao Adamu aliwatolea jamii ya binadamu. Paradiso, furaha, na uhai wa milele zilipotezwa, na dhambi, kuteseka, na kifo zikapatikana mahali pazo kupitia kutokutii. (Warumi 5:12, 14) Lakini Yehova katika upendo na hekima yake aliandaa “mtu wa pili,” “Adamu wa mwisho,” ambaye ni Bwana Yesu Kristo. Njia ilifunguliwa kupitia huyu “Mwana pekee wa Mungu” mwenye kutii ambapo wazao wa “Mtu wa kwanza, Adamu” aliyekosa kutii wangeweza kupata Paradiso na uhai wa milele tena, hata kanisa au kundi la Kristo lipate uhai wa kimbingu. “Kwa kuwa kama katika Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa.”—Yohana 3:16, 18; Warumi 6:23; 1 Wakorintho 15:22, 45, 47.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki