Kutangaza Rasmi Habari Njema Katika “Mji wa Kipolinesia” wa New Zealand
“MJI wa Kipolinesia Ulio Mkubwa Zaidi Ulimwenguni.” Hivyo ndivyo wengine wameuita Auckland mji mkuu wa New Zealand. Kwa nini? Si kwamba tu huko ndiko kwa Wamaori, walio Wapolinesia wa New Zealand kwenyewe, bali pia kwa sababu Wapolinesia makumi ya maelfu wengine hukaa huko. Katika miaka ya karibuni, walihamia kutoka Samoa Magharibi, Visiwa vya Cook, Tonga, Niue, na Visiwa vingine vya Pasifiki. Sasa Wamaori wa Visiwa vya Cook walio katika New Zealand ni wengi kuliko wote walio katika kikundi chenyewe cha Visiwa vya Cook! Vivyo hivyo, wakaaji wa Niue katika Auckland ni wengi sana kuliko wale katika Niue.
Ingawa wakaa-visiwani hawa wa Pasifiki wamehamia Auckland hasa kwa ajili ya sababu za kiuchumi, wanayo pia mahitaji mengine. Moja lililo la maana kwa watu hawa wenye msingi wa kupenda Biblia ni uhitaji wao wa kiroho. (Mathayo 5:3) Wakitambua hilo, Mashahidi wa Yehova katika New Zealand wameweka jitihada sana ili watangaze rasmi “habari njema za Ufalme” miongoni mwa wakaa-visiwani hawa. (Mathayo 24:14, NW) Nini kimefanywa kuhusu hilo, na wakaa-visiwani wameitikiaje?
Wasamoa Wafanya Maendeleo
Elezo lililotolewa na misionari katika Samoa latuambia jambo fulani juu ya mtazamo wa mambo ya kiroho wa wakaa-visiwani. “Unapokutana na mtu mara ya kwanza katika New Zealand, ni desturi kumwuliza juu ya kazi yake ya kimwili,” yeye aeleza. “Katika Samoa swali la kwanza linaloulizwa kwa kawaida lahusu dini ambayo mtu hufuata.” Kwa hiyo, haishangazi kwamba yale makundi mawili yenye kusema Kisamoa ya Ma-shahidi wa Yehova katika Auckland yanakua kwa haraka kuliko kundi la kawaida katika New Zealand.
Kundi la kwanza la Kisamoa katika Auckland lilianzishwa katika 1977. Kwa sababu ya ukuzi wa kupewa na Mungu, la pili lilifanyizwa miaka saba baadaye. (Linganisha 1 Wakorintho 3:6.) Katika makundi mawili hayo, kuna jumla ya watangazaji wa Ufalme 154, kati ya hao 12 wakiwa wenye utendaji katika huduma ya wakati wote. Jumapili ya kawaida, watu zaidi ya 275 huhudhuria mikutano yenye msingi wa Biblia inayofanywa kwenye Jumba la Ufalme.
Ndugu na dada Wasamoa huchukua imani yao kwa uzito, kama vile inavyoonyeshwa na juhudi na azimio wanazoonyesha katika kazi za kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 28:19, 20) Hilo laweza kuonwa kutoka ono linalofuata la dada Msamoa:
Katika huduma ya nyumba kwa nyumba, dada huyo alikutana na mwanamke ambaye alilaumu dini zote kuwa za kiunafiki na akafunga mlango. Akiwa amefadhaishwa na kuvunjwa moyo, huyo dada hakujua la kufanya. ‘Siwezi kumwacha akidhani kwamba Mashahidi wa Yehova ni wanafiki,’ yeye aliwaza. Kwa hiyo aliamua kuacha barua fupi. “Nilieleza kwa kifupi msingi wa Kimaandiko wa kazi yangu na nikamwuliza kama angeweza kunipa wakati wa kumwelezea tumaini ambalo Biblia inatoa. Nilitia ndani pia namba ya simu yangu.”
Yule dada kisha akaendelea na huduma yake, akitembelea nyumba nyinginezo. Alipokuwa akifika nyumba ya nne njiani, alipewa ujumbe wa simu arudi amwone yule mwanamke ambaye alikuwa amefunga mlango kwa hasira mapema. “Huyo bibi aliomba msamaha kwa ajili ya itikio lake la kwanza,” dada aeleza, “na akatoa shukrani kwa ajili ya barua fupi niliyomwachia. Mazungumzo mazuri yenye matokeo mazuri yakafuata, na funzo la Biblia nyumbani likaanzishwa.”
Ilichangamsha moyo pia kuona roho ya umisionari yenye kujidhabihu ikionyeshwa na Mashahidi Wasamoa wengine. Ndugu mmoja na familia yake walihama kutoka Auckland kwenda Wellington katika 1981 ili kusaidia kikundi kidogo kinachofanya kazi miongoni mwa wenyeji Wasamoa huko. Kutoka chanzo cha wahubiri wa Ufalme 11 wakati huo, kundi la 47 limesitawi. “Zawadi zilipita dhabihu kwa wingi na kwa mbali,” asema yule ndugu. Karibuni, yeye na familia yake wameitikia ‘mwito wa Makedonia’ na wamehamia Samoa Magharibi tena. (Matendo 16:9, 10) Wengine pia wameparudia mahali pao pa kukaa pa kwanza na wamechukua upania wa pekee, umisionari, au utumishi wa Betheli.
Itikio la Waniue
Kazi ya kuhubiri inasonga mbele pia miongoni mwa Waniue katika Auckland. Mwangalizi asafiriye aripoti hivi: “Katika huduma ya nyumba kwa nyumba, huwa ni desturi kualikwa ndani ya nyumba. Kwa kawaida Biblia ya familia iko karibu, na inaonwa kuwa jambo la kawaida kuizungumza.”
Sasa kunalo kundi lenye kutenda sana la Kiniue katika Auckland. Pindi ya ziara ya mwangalizi asafiriye mwaka jana, wahubiri wa Ufalme 76 wanaoshiriki nalo waliweza kuwaalika watu 127 kwa hotuba ya Biblia ya watu wote siku ya Jumapili. Na kuna roho nzuri miongoni mwa akina ndugu na dada.
“Ziara inaonwa kuwa juma la pekee la kitia moyo kwa wote,” aonelea mwangalizi asafiriye. “Kila mlo ni shughuli ya kikundi. Na nyakati hizo ndizo za kuandalia vipendezi vya Waniue kama takihi (sahani ya mapapai, tarosi [mboga-mzizi ya kitropiki], na maji ya nazi zilizofungwa katika majani ya mgomba), pitako (mkate uliotengenezwa kwa viazi vya kienyeji, ndizi, na wanga wa muhogo), na punu povi (nyama ya ng’ombe yenye kukolea chumvi iliyo katika kopo), ambayo nyakati nyingine kwa kuchekesha inarejezewa kuwa kipande kikubwa cha nyama ya ng’ombe cha wakaa-visiwani.”
Vichapo vya Lugha ya Kipolinesia
Ili kuridhisha mahitaji ya kiroho ya wenyeji wa Kipolinesia katika Auckland na penginepo, Watch Tower Society imepanga kutoa vichapo kadhaa vya Biblia katika lugha za Kipolinesia. Kwa mfano, Mnara wa Mlinzi la Kirarotonga, au Kimaori cha Visiwa vya Cook linachapishwa mara mbili kwa mwezi. Mnara wa Mlinzi la Kiniue la mara moja kila mwezi linapokewa vizuri pia. Jumla ya hesabu ya chapa za Kirarotonga na Kiniue za Mnara wa Mlinzi kwa sasa ni nakala 1,000 hivi kwa kila moja, na nakala 900 hivi za chapa ya Kisamoa sasa zinazungushwa katika New Zealand.
Zaidi ya Mnara wa Mlinzi, vitabu na broshua kadhaa zinapatikana katika lugha mbalimbali za Kipolinesia. Kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, kilichochapishwa katika Kiniue katika 1989, ndicho kichapo cha kwanza katika lugha hiyo kinachoandaa ufahamu wa mafundisho ya msingi ya Biblia. Kitabu chenye matokeo zaidi katika eneo la Kimaori (Kirarotonga) cha Visiwa vya Cook ni Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani katika lugha hiyo. Karibu mafunzo yote ya Biblia nyumbani yanaongozwa kwa msaada wa kitabu hicho. “Ushuhuda kwamba hicho ndicho msaada wa kufundisha ulio na matokeo,” aonelea mzee mmoja, “ni ule wepesi wa wanafunzi wa kuanza kuhudhuria mikutano ya kundi.”
Zaidi ya ugawanyaji wao wa kawaida wa nyumba kwa nyumba wa vichapo hivyo, watu wa Yehova huangusha vichapo vingi katika ule unaoweza kuitwa ushahidi wa soko la nje. Kwa sababu ya ongezeko kubwa la idadi ya wenyeji wa Polinesia katika Auckland katika miaka ya hivi karibuni, masoko makubwa yaliyo na vibanda vya muda tu ya kuuzia hasa vyakula na vyombo vya ufundi vinavyotoka visiwa vya Pasifiki yametokea. Watu wengi kufikia hata 25,000 waweza kuja kwenye soko kama hilo asubuhi ya Jumamosi. Kwa kutumia kwa hekima nafasi hiyo, Mashahidi huenda kwenye masoko hayo na huongea na wenye vibanda na wanunuzi juu ya Ufalme wa Mungu.
Kupitia huduma yao, Mashahidi wa Yehova wameweza kupanda mbegu nyingi za Ufalme na kuangusha vichapo vya Biblia vingi kwa watu wa Polinesia. Ofisi ya tawi ya Watch Tower Society inaripoti kwamba pindi ya mwaka wa utumishi wa 1990, vichapo 23,928 mbalimbali vya lugha ya Kipolinesia vilipelekwa kwa meli kutoka kiwanda.
Kushangilia Kwenye Meza Moja ya Kiroho
Kwa kuwa na ufahamu wa uhitaji wao wa kiroho, Mashahidi Wapolinesia hutanguliza zaidi kuhudhuria mikutano ya Kikristo ya kila juma kwenye Majumba ya Ufalme, na pia kuhudhuria makusanyiko na mikusanyiko yao. (Waebrania 10:23-25) Katika “Haki ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya uliofanywa katika Auckland katika Desemba 1988, vikao mbalimbali vilifanywa katika Kisamoa, Kiniue, na Kimaori cha Visiwa vya Cook. Yenye kutokeza katika programu ya Kisamoa ilikuwa drama ya Biblia iliyozoezwa vizuri na yenye shauku. Mashahidi Waniue na wa Visiwa vya Cook wa Auckland walionyesha ukaribishaji-wageni wao wa Kikristo kwa kutumikia wakiwa wakaribishaji wenye hisani kwa wageni kutoka visiwa vya kwao. Mkusanyiko huo ulithibitika kuwa wakati wa kufurahisha na kushangilia kwenye meza ya Yehova ya kiroho. Kwenye mkusanyiko “Lugha Iliyo Safi” katika Auckland, kilele cha 503 walihudhuria vipindi vya Kisamoa.
Itikio chanya (zuri) kwa ujumbe wa Ufalme ni ushuhuda wa wazi kwamba watu kutoka visiwa vya Kipolinesia vya Pasifiki Kusini wamekuwa ‘wakingojea sheria ya Yehova.’ (Linganisha Isaya 42:4, 12.) Halafu, wao kwa shangwe hushiriki katika kutangaza rasmi habari njema katika “mji wa Kipolinesia” wa New Zealand.