Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 5/15 kur. 24-28
  • Tatizo la Kupanda Mbegu Ya Ufalme Katika Chile Kusini

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tatizo la Kupanda Mbegu Ya Ufalme Katika Chile Kusini
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Siku Moja Katika Kazi ya Kuhubiri
  • Ziara Kwenda Chiloé
  • Kurudi Kwenye Bara
  • Kuvuka Bío-Bío
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 5/15 kur. 24-28

Tatizo la Kupanda Mbegu Ya Ufalme Katika Chile Kusini

INAPENDEZA kama nini kutembea katika barabara iliyo kimya ya mashambani katika Chile kusini! Ng’ombe wanakula majani katika mashamba yenye mistari ya miti iliyo na mandhari-nyuma ya volkeno (zaha) tukufu zenye theluji juu ya vilele vyao. Waweza kusikia ndege wakitoa mlio mwembamba na majani yakicharakisha upeponi. Hata ikiwa mazingira hayo yaonekana kuwa mazuri sana, kuna majaribu hapa kwa wale wanaopanda mbegu ya kweli ya Ufalme.

Je! ungependa kukutana na baadhi ya mapainia wetu, au watangazaji wa wakati wote wa Ufalme? Vipi kupisha siku moja au mbili pamoja nao wakihubiri habari njema? Kwanza, tusikilize Jaime na Oscar wanapoeleza mapendezi na matatizo ya siku kama hiyo katika Chile kusini.

Siku Moja Katika Kazi ya Kuhubiri

“Tunaanza kusogea-sogea na kutambua baridi ambayo imeingia kikao chetu kidogo. Oscar akiwa amevaa soksi za sufi na akiwa na kofia bado kichwani mwake, aondoka kitandani. Awasha jiko la kuni, awasha chombo kidogo cha gesi kinachoongeza joto ili kuondoa baridi chumbani, kisha arudia joto la kitanda chake. Bado kuna giza nje, na tunaweza kusikia mvua ambayo imekuwa ikinyesha usiku kucha. Twatazama nje ya dirisha halafu twatazamana. Lo, jinsi ingekuwa rahisi kupumzika siku hiyo! Halafu twakumbuka mipango yetu ya siku hiyo na uhitaji wa kufanya kazi katika eneo lililo pekee ambalo halikufikiwa kabisa mwaka jana. Tunachochewa kuanza.

“Njiani kabla ya saa mbili asubuhi, tunatembea mwendo wa haraka na tunatumaini kwamba mtu atatubeba kwa gari au kwamba basi itakuja, ili kwamba tuweze kuharakisha safari yetu kwa barabara za nyuma-nyuma zinazoelekea kwenye nyumba na miji midogo iliyo pekee ya eneo letu. Tingatinga yaja ikiburuta gari lenye umbo wa jukwaa lililo na wafanya kazi juu yalo. Dereva asimama na kuturuhusu tupande juu yalo. Tunafurahi kwamba, kwa sababu ya mvua usiku wa jana, leo hatusafiri katika mavumbi kama kawaida. Tunapoenda tukiruka-ruka, tunashiriki habari njema na wafanya kazi wa ukulima. Wakati wa kushuka unapofika, tunawapa magazeti machache. Tunashukuru kama nini safari hiyo ya gari ambayo imetupunguzia kilometa 12 za kutembea!

“Itakuwa siku ndefu tunapovuka mashambani kwenda huku na huku katika kutafuta wanaostahili. Tulipoanza katika migawo yetu, hatukuweza kufahamu kwa nini watu wangekubaliana na yale tuliyokuwa tukiyasema lakini wakaonekana kutotaka kukubali vichapo vya Biblia. Tulijifunza kwamba mara nyingi hiyo ilikuwa kwa sababu hawakuweza kusoma. Kwa hiyo sisi huona kwamba inanufaisha kueleza kwamba vichapo vyetu ni zawadi ya ajabu sana kwa watoto na watu wa ukoo wao, ambao kisha waweza kushiriki nao yaliyomo ndani. Wengi wa wale tunaosema nao hawana mali nyingi za ulimwengu huu. Lakini kwa kuwa wana furaha ya kushiriki walicho nacho, wanapokuwa wamepokea vichapo vya Biblia, mara nyingi wametupa mayai, viazi, viazi vyekundu, vitunguu, maharagwe, dengu, na garbanzo.”

Jaime amejifunza kutoa madokezo mwenye nyumba anapotaka kuchanga vitu kwa ajili ya vichapo vya Biblia anavyopewa. Kwa nini? Wakati mmoja, mapainia walirudi wakiwa na kilo 15 za mboga, na mwenzi wake alipaswa kubeba kuku aliye hai katika mfuko wake wa vitabu ikiwa sehemu njema ya siku! Mara nyingi Jaime hudokeza merquén, kitoweo chenye ladha nzuri kinachotayarishwa kwa pilipili na vitu vingine vya kukolezea chakula. Usimulizi unaendelea hivi:

“Tunapovuka mashamba, tunapata ruca [nyumba] za wenyeji Wamapuche [inayomaanisha, “Watu wa bara hili”]. Ni vigumu kuongea na Wamapuche wazee, kwa kuwa wengi wao husema lugha yao ya kienyeji tu. Vijana wanapokuwa karibu, mara nyingi wao hutumika kuwa watafsiri. Tunaposogea ndani zaidi mashambani, tunakutana na watu ambao hawajaona kamwe Biblia au kuzuru mji mkubwa kama Temuco, mji mkuu wa eneo hilo. Hii hutokeza jaribu la kuwasaidia kufahamu jinsi hali za ulimwengu zinaharibika. Ni lazima tufanye hivyo hatua kwa hatua, tukiwaonyesha jinsi matatizo ya kwao yanavyoonyesha yale yanayotokea mahali penginepo.

“Siku inapoendelea, miguu yetu iliyochoka inahitaji pumziko. Hali ya hewa imebadilika kwa zamu kati ya jua lenye kung’aa na mvua kubwa sana ambayo hufanya mwavuli uwe wa bure. Mashamba yaliyolimwa karibuni kwa plau yameacha buti zetu zikiwa zimejaa matope. Tunaposikia maneno Pase no más (Karibuni), tunaingia jikoni kwa furaha na kuonea shangwe ujotojoto wa jiko la kuni, kikombe cha ‘kahawa’ chenye kutayarishwa kwa nafaka, jibini iliyotayarishwa nyumbani, na mkate mpya uliookwa nyumbani. Lo, hiyo harufu tamu sana ya mkate mpya!

“Nguvu zetu zikiwa zimefanywa upya, tunaendelea hadi mapema jioni, tukivuka mashamba ambayo mara chache tu hutenganishwa kwa nyua, ingawa utapata mashamba mengine ya ngano ambayo yamezingirwa na mti wa kichaka unaoitwa pica-pica, ambao ni mmea usiokauka wenye maua ya kimanjano. Kwa kuwa jua karibu litatoweka na ni lazima tufike barabara nyingine kuu ili kushika basi ya mwisho kurudi mjini, kutembea kwetu kilometa 20 kutaisha karibuni.

“Tunarudi salama salimini, tumechoka lakini wenye furaha, kwa kuwa tumekuwa na mazungumzo mengi yenye kupendeza pamoja na wenye mfano wa kondoo. Baada ya kula, tunapitia siku kisha tunaikokota kitandani miili yetu iliyochoka.”

Ziara Kwenda Chiloé

Akipelago ya Chiloé imefanyizwa na visiwa vidogo kadhaa. Kisiwa chayo kikuu kina urefu wa kilometa 180 nacho kina vilima vyenye majani mazuri vyenye kutenganishwa na maziwa madogo. Na ni mandhari ya pwani yenye kupendeza kama nini na vijiji vya uvuvi vyenye kupendeza vya mtindo wa zamani ambavyo vyaweza kuonwa popote uendapo!

Katika mji wa Achao, karibu tu na kisiwa kikuu, tunapata Rubén na Cecilia. Walipowasili katika Machi 1988, padre wa mahali hapo aliwaonya watu ‘wasisikilize hao wenzi wawili wanaotembea kote kote kisiwani wakiongea juu ya Biblia.’ Maelezo yake hasi yalifunga akili za wengine lakini yalichochea udadisi wa wengine. Wakati ulipopita Ruebén na Cecilia walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia 28. Mengi ya mafunzo hayo ni pamoja na walimu, ambao wanne wao hutumia vichapo vya Watch Tower “All Scripture Is Inspired of God and Beneficial” na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia kufundisha masomo ya dini katika shule zao.

Yehova hujali hao mapainia wenye bidii ya kufanya kazi, ambao hutembea hata kilometa 30 kila siku katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Siku moja, Rubén na Cecilia walikuwa wakitembea katika kijia kilichopakana na ufuko walipoona kwamba wakati wa maji kupwa, chorito (namna ya kome) wengi waliweza kupatikana kwa urahisi. Rubén alianza mavuno yake, lakini wangewapelekaje nyumbani? Cecila alitatua tatizo hilo. Soksi ndefu zake zikawa mifuko. Sasa mapainia hao walikuwa na uwezo wa kutengeneza chakula kitamu cha bahari!

Kaskazini tu mwa Achao, wahubiri wawili wa wakati wote wa Ufalme wanaojulikana kuwa mapainia wa pekee hushiriki na kundi dogo katika Linao. Kazi ya kuhubiri ilianza huko katika 1968, na Shahidi wa Yehova wa kwanza katika Linao alibatizwa katika 1970. Kwa miaka minne ndugu huyo alikuwa peke yake katika kazi ya kuhubiri na alihitaji kuvumilia mzaha kutoka kwa washiriki wa familia na watu aliowajua. Hatimaye, katika 1974, mke wake aliitikia kweli ya Biblia kwa kupendezwa na akabatizwa. Hiyo ilifuatwa na mabatizo ya ndugu wanne wa kimwili, dada wanne, wajomba wanne, wapwa sita, ndugu mkwe mmoja na mke wake. Kundi lililofanywa huko lilikuwa familia kubwa moja. Wakati ulipopita, watatu wa hao ndugu watano walianza kutumika wakiwa wazee na mmoja akiwa mtumishi wa huduma.

Luis na Juan ni wahubiri wa wakati wote ambao hukazia fikira juu ya kupanda mbegu ya Ufalme katika Quemchi, mji mdogo ulio kilometa 30 kutoka Linao. Kila siku, wao hupanda nyua, huvuka mashamba yenye kujaa mimea, na hupanda na kushuka vilima, wakiwa na upepo na mvua kama waandamizi wa daima. Ili kufikia visiwa vya karibu, wao hutumia mashua ndogo ambazo husafiri kwenda kisiwa Chiloé mara mbili au tatu kila juma. Wanabaki kisiwani kwa siku kadha wa kadha. Safari kati ya visiwa yaweza kumfanya mwenye kuzoea bara asikie kutapika kidogo, lakini ukaribishaji-wageni na fadhili za wakaa-visiwani zalipia jambo hilo zaidi ya kuwa sawa. Luis na Juan waliungwa na mhubiri wa Ufalme mwingine, na wao pamoja hujaribu kufikia wenyeji 11,500 katika eneo lao. Ingawa ongezeko lilikuwa la polepole, Luis na Juan walishangilia kuwa na 36 wakiwepo kwa mwadhimisho wa Ukumbusho wa 1989.

Kurudi Kwenye Bara

Tukiendelea kaskazini, tunavuka mlangobahari wa Chacoa na kufika bara. Katika sehemu hii, mapainia Ramón na Irene hufanya kazi kwenye eneo kubwa sana ambalo linatia pia vikundi vilivyo vya pekee katika Maullín, Carelmapu, na Pargua. Mashahidi katika kisiwa cha Chiloé hutembea kwa muda wa saa moja kisha hupanda transbordador (mashua ya kivukoni) kuvuka mlangobahari na kuhudhuria mikutano ya Kikristo katika Pargua. Ramón husafiri kwa muda wa saa moja na dakika 20 kwa basi kutoka Maullín ili kuongoza mikutano ambayo huhudhuriwa kwa ujumla na idadi ya watu mara mbili ya ile ya wahubiri. Kwa nini inachukua muda mrefu kama huo kwenda mwendo wa kilometa 38 tu? Kwa sababu basi husimama mahali popote barabarani ili kubeba abiria wenye kulemewa na mifuko ya matunda na mboga, magunia ya viazi na vitunguu, na nyakati nyingine hata na nguruwe na kuku walio hai. Kitu chochote ambacho hakiwezi kuwekwa juu ya basi huwekwa ndani. Hatimaye tokeo ni safari ndefu yenye minuko, miono na mivumo mingi.

Kwa kuwa walio wachache sana wa mapainia hao wana magari, kukosa basi inayosafiri kati ya miji kunahitaji kutembea mwendo mrefu, isipokuwa kama mtu fulani atoa msaada wa kupanda gari. Ramoń na mwanafunzi wa Biblia walipokuwa wakisafiri kwa gari pamoja na dereva mmoja, aliuliza hivi: “Watu wanaitikiaje kazi yenu?” Akiona mitazamo yao ya udadisi, alisema hivi: “Mimi ndiye padre katika pueblo hii, nanyi ni Mashahidi wa Yehova. Najua kazi yenu nami napenda magazeti yenu.” Kulikuwa na kipindi cha maswali na majibu kweli kweli kabla ya kuwashusha katika Pargua wakati wa mkutano. Padre huyo kwa hakika alijibiwa maswali mengine alipoendelea kusoma majarida yetu.

Si rahisi kwa Ramón na Irene kufikia nyumba ambapo wao huongoza mafunzo ya Biblia 20. Nyingine ziko ng’ambo ile nyingine ya Mto Maullín au katika vijiji vya uvuvi vilivyo pekee na vyapasa kufikiwa kwa mashua ndogo. Ingawa zile mvua nyingi zaweza kuvunja moyo, ilikuwa wazi kwamba uvumilivu ulioonyeshwa nao na wahubiri wa Ufalme wengine 18 waliotawanyika kote kote katika eneo hili la mashambani ulikuwa ukitokeza matunda wakati 77 walipokusanyika pamoja kwa ajili ya Ukumbusho.

Katika Los Muermos, Juan na Gladys watangazaji wa wakati wote wa Ufalme wameongoza mafunzo ya Biblia 23. Kutembea kurefu juu ya barabara zenye matope kunathawabishwa wakati mbegu ya Ufalme zinapopata mzizi katika mioyo ya watu mmoja mmoja wenye kufundishika. Katika eneo moja lililo pekee katika mfululizo wa milima ya pwani karibu na Estaquilla, Juan na Gladys walifanya kazi katika eneo ambalo halikuwa limezuriwa karibuni. Walimwomba mwanafunzi wa Biblia kama angewaazima farasi wake kwa siku hiyo. “Bila shaka,” akajibu. “Je! naweza kwenda pamoja nanyi?” Juan upesi akafahamu kwamba ni lazima huo uwe ulikuwa mwongozo wa Yehova. Ingekuwa rahisi kupotea katika ile miitu minene, lakini yule mtu mwenye kupendezwa alijua eneo hilo vizuri na kuwaongoza kwenye nyumba zisizoonekana kutoka kwa vijia vya mlima. Tukiwa tumeumia sana baada ya kutembea na kupanda farasi kwa muda wa saa tisa, painia wa pekee mmoja alimwuliza yule mwanafunzi wa Biblia jinsi alivyojisikia. Mtu huyo akaitikia hivi: “Jambo tu ambalo ninaomba ni kwamba mnichukue pamoja nanyi wakati ujao.” Mtu huyo mwenye kuthamini alizidi kufanya maendeleo ya kiroho na akabatizwa katika Januari 1988. Mke wake alibatizwa kwenye kusanyiko la mzunguko lililofuata.

Wakati wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko, wale wahubiri 11 katika Estaquilla walipendezwa kuwa na 110 wakihudhuria hotuba ya watu wote. Katika mji mdogo wa watu 1,000 ulio karibu zaidi na Los Muermos, 66 walikutana kwa ajili ya Ukumbusho. Kwa hiyo kuna zaidi ya kufanywa katika shamba hili kubwa.—Mathayo 9:37, 38.

Kaskazini zaidi, tunapata mapainia Alan na Fernando. Walipokuwa wakitembea katika barabara yenye vumbi siku moja, dereva aliwasaidia kusafiri nyuma ya lori yake. Waliposhuka, wakalazimika kucheka kwa sababu vumbi nene liliwafunika kabisa toka kichwani mpaka miguu. Kuwa na hali ya ucheshi na shangwe ya kuongoza mafunzo 20 ya Biblia nyumbani kunasaidia kushinda taabu kama hizo. Na ebu wazia shangwe yao wakati 65 walihudhuria Ukumbusho na watu wawili wa kwanza wa mahali pale wakajiunga nao katika kazi ya kuhubiri mwezi uliofuata!

Kuvuka Bío-Bío

Ili kufikia walio kama kondoo karibu zaidi na Milima ya Andes, ni lazima kuvuka korongo iliyo na maji yenye kuvuma ya Mto Bío-Bío yakiwa meta 50 chini. Hii inafanywa penye muundo wa mbao dhaifu ambao umening’inizwa kwenye nyuzi za chuma zilizonyoshwa upande mmoja hadi mwingine wa korongo. Ukiwa na wasiwasi, unapanda juu na kusogeza wenzo unaoachilia mbao zijongeze kwenye nyuzi za chuma. Unashikilia sana miti ya juu ya mbao unapojongea upesi kuelekea katikati ya korongo, ambapo unaning’inia kisha kusimama. Baada ya kupumua kidogo, unasogeza wenzo mwingine nyuma na mbele, ukiendelea kuvuka polepole nusu ile nyingine. Kwa wazi waoga hawawezi hiyo! Hata hivyo, dada mmoja hufanya hivyo kila juma ili kufikia mtu aliye kama kondoo katika kijiji cha mlimani cha mbali!

Mfano mzuri uliowekwa na mapainia na wahubiri wa Ufalme wengine unatia moyo wenye kupendezwa walio na mioyo yenye kuthamini kufanya bidii iyo hiyo ili kuhudhuria mikutano ya Kikristo. (Waebrania 10:24, 25) Familia hupanda farasi kusafiri kilometa 40 hadi Mto Bío-Bío kisha hutembea kilometa 12 nyingine kwenye Jumba la Ufalme.

Mapainia hukumbuka jambo gani wanapofikiria ya nyuma miaka iliyopita? Je! ni zile volkeno zenye theluji juu ya vilele vyazo, mashamba mazuri, na mito inayoenda kasi? Je! ni ile vumbi, mvua, na kule kutembea kurefu? Ndiyo, lakini wanakumbuka hasa watu wenye urafiki ambao waliitikia habari njema kwa kupendezwa. Hao walio kama kondoo kwa hakika hufanya bidii hiyo yote iwe yenye kufaa. Ni shangwe kama nini kupanda mbegu ya Ufalme katika Chile kusini!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki