Ripoti Yenye Kusisimua Kutoka Urusi
Upeo Wenye Shangwe kwa Miaka Mia Moja ya Kutoa Ushahidi
“KUSAJILI Hati ya Katiba ya Kitovu cha Uendeshaji wa matengenezo ya kidini ya ‘Mashahidi wa Yehova katika U.S.S.R.’”
Hiyo ndiyo tafsiri ya maneno ya kwanza ya hati katika lugha ya Kirusi iliyotolewa tena kwenye ukurasa huu. Kwa kweli, maneno hayo yanawakilisha jibu la sala nyingi. Hati hiyo ilitiwa sahihi na kupigwa muhuri katika Moscow na ofisa wa cheo cha juu wa Wizara ya Haki ya R.S.F.S.R. (Russian Soviet Federated Socialist Republic). Hiyo inamaanisha kwamba Mashahidi wa Yehova ni tengenezo la kidini linalotambulika kotekote katika Urusi. Hivyo, badiliko kuu limefikiwa katika historia yao ya miaka mia moja katika nchi hiyo kubwa.
Mwanzo Mdogo Sana
Eti miaka mia moja ya historia? Ndiyo. Katika nyakati za kisasa, mhubiri wa habari njema mwenye kujulikana wa mapema zaidi katika nchi hiyo alikuwa Charles Taze Russell, aliyeripoti ziara huko katika 1891. Katika toleo la Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence la September 1891, asimulia kwamba alisafiri kwenda Kishinev, Urusi, wakati wa safari ya kwenda Ulaya. Hapo alikutana na mtu fulani aliyeitwa Joseph Rabinowitch, aliyeamini katika Kristo naye alikuwa akijaribu kuhubiri familia za Kiyahudi katika eneo hilo. Russell anariporti kwa urefu juu ya ziara yake pamoja na Rabinowitch na juu ya mazungumzo yao ya kina kirefu, yenye kupendeza, juu ya Ufalme.
Habari Njema Yasikiwa Tena
Baada ya ziara ya Russell, mengi hayasikiwi juu ya kutoa ushahidi katika mahali ambapo sasa ni U.S.S.R., lakini hilo halimaanishi kwamba hakuna lolote lililotimizwa. Katika 1927 makundi matatu katika Urusi yalipelekea Sosaiti ripoti za mikutano yao ya Ukumbusho. Lakini maendeleo hayaonekani kuwa yalikuwa ya haraka mpaka vita ya ulimwengu ya pili. Vita hiyo ilitokeza kuhamishwa-hamishwa kwa watu wengi katika Ulaya. Tokeo moja lisilokusudiwa la kuhamishwa-hamishwa huko lilikuwa kuingia kwingi kwa wahubiri wa Ufalme ndani ya Urusi.
Kwa mfano, toleo la Mnara wa Mlinzi la Februari 1, 1946 (Kiingereza) laripoti hivi: “Zaidi ya wahubiri elfu moja waliohubiri katika lugha ya Ukrainia zamani katika sehemu ya mashariki ya Poland kwa sasa wamehamishwa sehemu za ndani ndani za Urusi. . . . Kisha pia, mamia ya ndugu walioishi katika Bessarabia, iliyokuwa sehemu ya Rumania zamani, kwa sasa ni wenyeji wa Urusi na wanaendelea na kazi yao ya kufanya wanafunzi miongoni mwa mataifa yote.”
Tena, wakati wa vita ya ulimwengu ya pili, raia wengi wa Urusi waliteseka katika kambi za mateso za Nazi. Kwa wengine ono hilo gumu lilitokeza mibaraka isiyotazamiwa. Ripoti moja yasema juu ya wanawake vijana Warusi 300 waliofungwa katika Ravensbrück. Hapo walikutana na Mashahidi wa Yehova, waliitikia kweli, wakafanya maendeleo hadi hatua ya kubatizwa. Mambo hayo hayo yalitukia katika kambi nyinginezo. Mashahidi hao waliobatizwa karibuni walipofunguliwa baada ya vita, walibeba habari njema ya Ufalme pamoja nao waliporudi Urusi. Kwa njia hiyo, vita ya ulimwengu ya pili ilitokeza ongezeko la haraka katika idadi ya wahubiri wa Ufalme katika eneo la Urusi. Katika 1946 ilikadiriwa kwamba wahubiri 1,600 walikuwa wenye kutenda huko.
Kuhubiri Gerezani
Magereza yaliendelea kuwa na sehemu kuu katika kueneza habari njema katika Urusi. Baada ya vita, mamlaka, kwa kukosea, ziliona Mashahidi kuwa tisho, na wengi wakafungwa gerezani. Lakini hilo halikusimamisha kuhubiri kwao. Lingeweza kufanyaje hivyo, wakati wao waliamini kweli kweli kwamba ujumbe juu ya Ufalme wa Mungu ni habari iliyo bora kabisa kwa ainabinadamu? Kwa hiyo kwa wengi wao, gereza lilikuwa eneo lao, na wanagereza wengi sana waliowasikia waliitikia. Ripoti kutoka 1957 lasema hivi: “Kati ya wote wajulikanao kuwa katika kweli leo katika Urusi imekatwa maneno kwamba asilimia arubaini wamepokea kweli gerezani na katika kambi.”
Je! Mashahidi walishuka moyo kwa sababu ya tisho hilo la daima la kufungwa gerezani? Hapana hata kidogo! Ripoti kutoka 1964 yasema hivi: “Kuna Mashahidi wa Yehova katika kambi hizo ambao wako huko kwa mara ya pili au ya tatu, kwa kuwa hawakuacha kuhubiri ujumbe baada ya wao kuachiliwa.” Wengine, inaendelea kusema, walikuwa wahalifu waliotiwa gerezani au katika kambi wakakutana na Mashahidi walipokuwa huko. Walikubali kweli na kufanya maendeleo hadi hatua ya kubatizwa kabla ya kuachiliwa kwao.
Kupunguka kwa Mbano
Katika miaka ya kati ya 1960, mamlaka zilichagua mtazamo usio kuwa mkali sana kuelekea Mashahidi. Yaonekana, walitambua kwamba watu wa Yehova hawakuwa tisho kwa sheria na utengemano wa umma. Kwa hiyo ingawa utendaji mbalimbali wa Wakristo hao wanyenyekevu bado haukuwa halali, hawakukamatwa-kamatwa sana wala nyumba zao hazikupekuliwa-pekuliwa sana, nao walishukuru sana kwa kupunguka huko kwa mbano. Tamaa yao kuu ilikuwa kuendelea na maisha yao ya Kikristo na kufanya kazi katika njia iliyo kimya, yenye upole, na yenye amani, kwa kadiri ambayo iliwategemea wao.—Warumi 12:17-19; 1 Timotheo 2:1, 2.
Katika 1966 wote ambao walikuwa wamepelekwa uhamishoni huko Siberia kwa muda mrefu waliwekwa huru na kukubaliwa kwenda mahali popote walipotaka nchini. Wengi walirudi nyumbani baada ya miaka mingi ya kutokuwapo, lakini wengine walichagua kubaki katika shamba hilo lenye kuzaa matunda mengi. Na si wote waliorudi ambao walichagua kubaki. Dada mmoja, aliyehamishwa akapelekwa Siberia pamoja na familia yake akiwa kisichana, alikuwa amerudi Urusi magharibi pamoja na wazazi wake. Lakini alikaa kwa muda mfupi tu. Aliwapenda watu wanyenyekevu, wenye ukaribishaji-wageni wa Siberia sana sana hivi kwamba aliacha familia yake na kurudi mashariki kuendelea kuhubiri kwa wale watu wenye usikivu.
Jambo lililoonwa lililokuwa la kawaida wakati huo, lilihusisha ndugu aliyehama kutoka jiji moja hadi jingine. Baada ya muda mfupi alipata Mashahidi wengine wawili. Hao watatu walisali ili kupata msaada na upesi wakakutana na mwanamke kijana wa malezi ya Kiorthodoksi ya Kigiriki. Alikubali kweli kwa haraka naye akawaongoza ndugu hao kwa wengine wawili waliopendezwa—mama yake na dada yake mchanga kuliko yeye. Ripoti hiyo yamalizia hivi: “Leo kuna watu arubaini wanaoshiriki na ndugu hao, thelathini kati ya hao waliojifunza kweli ndani ya miezi sita iliyopita.”
Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova walizuiwa katika utendaji wao mbalimbali kwa sababu ya kukosa utambuzi wa kisheria. Mikutano ilifanywa kwa hadhari. Kuhubiri kulifanywa kwa uangalifu. Kufungwa gerezani bado kulikuwa jambo lililoweza kutukia, na kutoa ushahidi nyumba kwa nyumba kwa uwazi hakukuwezekana. Hata hivyo, yajapokuwa hayo, Wakristo Warusi waaminifu hao waliendelea kumtumikia Mungu wao kwa uaminifu na kuwa raia wazuri wa nchi yao. (Luka 20:25) Akionyesha mtazamo wao, mmoja wao aliandika hivi: “Ni pendeleo tukufu kuvumilia majaribu yote na kubaki mwaminifu kwa Yehova Mungu, kumsifu Mungu milele maishani mwa mtu ili kupata uhai wa milele kutoka kwa Yehova kupitia Yesu Kristo.” Mashahidi Warusi hao wamekuwa mifano mizuri kama nini ya uvumilivu na uaminifu!
Kuhalalishwa Hatimaye!
Katika 1988 mambo yalianza kubadilika katika nchi zilizokuwa na ushirikiano pamoja na Urusi. Hali ya uhuru mkubwa zaidi ilianza kuenea, na nchi zilizokuwa zimezuia utendaji mbalimbali wa Mashahidi wa Yehova zilianza kutumia sera mpya mbalimbali. Poland, Hungary na Romania, na nchi nyinginezo ziliwapa hawa Wakristo wanyofu utambuzi wa kihalali, zikiwakubali kutenda waziwazi bila hofu ya kisasi. Hii miaka mitatu iliyopita imekuwa yenye furaha kama nini katika Ulaya Mashariki! Jinsi akina ndugu huko wametumia uhuru wao uliopatikana karibuni kwa faida yao ili kueneza ujumbe wenye amani wa Ufalme! Na Mashahidi wa Yehova katika ulimwengu uliosalia wameshangalia kama nini pamoja nao!
Mashahidi Warusi tayari wamenufaika na uhuru wao mbalimbali wenye kupanuka. Maelfu—wengine kutoka mbali hadi pwani ya Pasifiki ya Esia—walihudhuria mikusanyiko iliyoanza muhula mpya katika Poland katika 1989 na tena katika 1990, wakati Mashahidi 17,454 kutoka Urusi walipokuwapo katika Warsaw. Walienda kwao wakiwa na kumbukumba zilizoje! Wengi wao hawakuwa wameabudu kamwe pamoja na Wakristo wenzao zaidi ya wachache tu. Sasa walikuwa wamekuwa katika umati wa makumi ya maelfu!
Walirudia Urusi ambayo ilikuwa inakuwa yenye kuvumilia zaidi na zaidi. Mashahidi kuzunguka ulimwengu walitazama na kuuliza: Mashahidi wa Yehova katika Urusi watahalalishwa lini? Basi, ikawa hivyo katika 1991—miaka mia moja barabara baada ya ziara ya Charles Taze Russell huko! Siku ya Machi 27, 1991, “Kitovu cha Uendeshaji wa Matengenezo ya Kidini ya Mashahidi wa Yehova katika U.S.S.R.” kilisajiliwa katika hati iliyotiwa sahihi katika Moscow na Waziri wa Haki wa R.S.F.S.R. Mashahidi walipewa uhuru wa aina gani?
Katiba halali ya tengenezo hilo lililosajiliwa karibuni inatia ndani tangazo rasmi lifuatalo: “Kusudi la hili Tengenezo la Kidini ni kufuliza kazi ya kidini ya kujulisha jina la Yehova Mungu na maandalizi yake ya upendo kwa ainabinadamu kupitia Ufalme wake wa kimbingu kwa Yesu Kristo.”
Hilo lapaswa kufanywaje? Njia ambazo zimeorodheshwa zinatia ndani kuhubiri peupe na kuzuru nyumba za watu; kufunza kweli za Biblia kwa watu wenye nia ya kusikiza; kuongoza mafunzo ya Biblia pamoja nao bila malipo kwa msaada wa vichapo vya kujifunza Biblia; na kupanga kutafsiri, kuingiza nchini vitu kutoka nchi za kigeni, kutangaza, kuchapa, na kugawanywa kwa Biblia.
Hati hiyo pia inaeleza kwa ufupi tengenezo la Mashahidi chini ya Baraza Linaloongoza, kutia na makundi yenye mabaraza ya wazee, Halmashauri ya Usimamizi [ya Tawi] yenye washiriki saba kwa ajili ya nchi hiyo, na waangalizi wa mzunguko na wa wilaya.
Kwa wazi, Mashahidi wa Yehova waweza sasa kutenda kwa uhuru na kwa uwazi katika Urusi kwa kadiri wafanyavyo katika nchi nyingine nyingi. Ebu wazia shangwe ya washiriki watano kati ya wale saba wa Halmashauri ya Usimamizi na ya wale wazee watano wa tangu miaka mingi waliokuwa na pendeleo la kutia sahihi hati hiyo ya kihistoria na kuiona ikitiwa muhuri na Mkuu wa Idara ya Usajili ya Shirika za Umma na za Kidini! Kwa kufaa, Milton Henschel na Theodore Jaracz wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova walikuwapo pia kushuhudia tukio hilo lenye umaana. Kati ya vikundi vilivyoidhinishwa na R.S.F.S.R., Mashahidi wa Yehova walikuwa wa kwanza kupokea hati rasmi yao ya usajili. Ni thawabu iliyoje kwa ndugu Warusi waaminifu hao baada ya miaka mingi sana ya uvumilivu wenye subira!
Mashahidi wa Yehova kila mahali wanashukuru mamlaka za Urusi waliotoa uhalalisho huo. Wanashukuru hasa Yehova kwa moyo wao wote kwa uhuru huo mpya wa ndugu zao Warusi. Wanashangilia pamoja na Mashahidi wenzao katika U.S.S.R. na katika nchi nyingine za Ulaya Mashariki ambao sasa waweza kumtumikia Yehova Mungu kwa uwazi wa kadiri kubwa zaidi sana. Yehova na awabariki sana watumiapo uhuru huo kikamili katika kulisifu jina lake takatifu.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Ile Kremlin (Kitovu cha Serikali ya Urusi)
katika Moscow
[Picha katika ukurasa wa 10]
Wahudhuriaje Warusi kwenye Mkusanyiko
nje ya Urusi