Hukumu Ya Mwisho
“Unapokufa nafsi yako itateswa yenyewe; hiyo itakuwa helo yake: lakini kwenye siku ya hukumu mwili wako utaungana na nafsi yako, kisha utakuwa na helo mbili, nafsi yako ikitokwa na jasho la damu, na mwili wako ukiwa umejaa maumivu makali.”
HIVYO ndivyo mhubiri C. H. Spurgeon (Spu̇jon) wa karne ya 19 alivyoeleza maoni ya makasisi juu ya siku ya hukumu na mateso ya waliolaaniwa. Michelangelo msanii Mwitaliano alikuwa na imani hiyo hiyo yenye kutia hofu, kama ionwavyo katika mchoro wake “Hukumu ya Mwisho,” (ambao sehemu yao umetolewa tena juu) kwenye ukuta wa kikanisa cha Sistine katika Roma. The New Encyclopœdia Britannica inasema juu ya mchoro huo hivi: “Kristo katika Hukumu ni mungu mwenye ngurumo badala ya kuwa mkombozi wa Kikristo, mwenye kuhusika zaidi katika kulaani jamii ya kibinadamu badala ya kuwakaribisha wabarikiwa mbinguni.”
Fundisho la Jumuiya ya Wakristo
Katika karne zilizopita, siku ya hukumu na moto wa helo zilikuwa habari za mahubiri zenye kupendwa sana. Kutoka kwa mimbara yao, wahubiri kama vile C. H. Spurgeon walisema kwa sauti kubwa yenye majivuno wakieleza waziwazi juu ya mateso mabaya sana yaliyokuwa yakiwangojea watenda dhambi. Siku hizi, kuhubiri huko kunasikika mara chache. Lakini moto wa helo na hukumu ya mwisho bado ni mafundisho rasmi ya makanisa yaliyo mengi.
Dini zilizo nyingi za Jumuiya ya Wakristo hukubaliana mara nyingi na fundisho la Katoliki Roma kwamba hukumu za Mungu hukuja katika hatua mbili. Kwanza, kuna ile “hukumu halisi.” Mtu anapokufa, nafsi yake inayodhaniwa kuwa haiwezi kufa inahukumiwa papo hapo na kupelekwa kwenye umilele ama katika helo ama mbinguni.a Kisha katika mwisho wa wakati, ile hukumu ya mwisho au ya ujumla yaja, wakati miili ya wafu inapofufuliwa na kuunganishwa tena pamoja na nafsi zao zisizoweza kufa.
Siku hiyo ya hukumu, nafsi zilizo mbinguni zabaki humo na kuungana pamoja na miili iliyofanywa isiweze kuharibika. Wale watesekao katika helo hubaki humo pia, na nafsi zao pia huungana na miili iliyofufuliwa isiyoweza kuharibika. Kulingana na wengine, kuungana huko katika helo husababisha mateso yao yawe makali zaidi. Wale walio hai duniani bado, hawafi. Wanahukumiwa wakiwa hai bado na kwenda, moja kwa moja mbinguni au helo, wakiwa “mwili na nafsi.”
Uwezekano wa kuvumilia mateso yasiyoelezeka katika moto wa helo umefanya habari yote ya hukumu ya mwisho mikononi mwa Yesu Kristo kuwa jambo la hofu kufikiria. Kwa sababu hiyo, je, ungestaajabu kujua kwamba, kwa hakika, hukumu za Mungu mara nyingi huwa sababu ya kushangilia na kwamba Siku ya Hukumu itakuwa mojawapo nyakati zenye furaha nyingi sana katika historia yote ya kibinadamu? Hiyo yaweza kuwaje?
[Maelezo ya Chini]
a Wakatoliki Roma huamini pia katika uwezekano wa tatu: adhabu ya muda katika Purgatori kabla ya kuingia mbinguni hatimaye.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
Random/Sipa Icono