Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 8/15 kur. 8-12
  • Ufuatiaji wa Uhuru Katika Senegali

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ufuatiaji wa Uhuru Katika Senegali
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • ‘Yehova Awataka Mpate Jengo Hili’
  • Shambani Pamoja na Wamisionari
  • Kawekwa Huru Ili Kufuatia Huduma ya Wakati Wote
  • Ndoa ya Wake Zaidi ya Mmoja Yapingana na Ndoa ya Mke Mmoja ya Kikristo
  • Ibada ya Vitu vya Kiuchawi Yapingana na Ibada ya Kweli
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 8/15 kur. 8-12

Ufuatiaji wa Uhuru Katika Senegali

KISIWA kidogo cha Gorée (Gore) kiko barani kutoka Dakar, jiji kuu la kisasa la Senegali. Kwenye kisiwa hicho kuna ukumbusho wenye ukatili wa sehemu ya historia yenye huzuni—nyumba ya watumwa iliyojengwa katika 1776.

Ni mojawapo ya nyumba nyingi kama hiyo ambamo watumwa 150 hadi 200 walifungwa katika hali mbaya kwa mpaka miezi mitatu kabla ya kupelekwa kwa meli kwenda mahali palipo mbali. Familia ziligawanywa, washiriki wasionane tena kamwe; baba angeweza kutumwa Louisiana katika Amerika Kaskazini, na mama Brazil au Cuba, na watoto Haiti, Guyana au Martinque. Ni utovu wa heshima ulioje kwa uhuru wa kibinadamu! Huo pia ni ukumbusho wenye nguvu kwamba uhuru ni pendeleo lenye thamani ambalo halijawa mali ya watu wote.

Mimi nilijifunza juu ya hayo kutoka broshua ya watalii niliyokuwa nikiisoma kwenye ndege iliyokuwa ikielekea Senegali, nchi iliyo sehemu ya magharibi kabisa kwenye bara kubwa linalotokeza la Afrika Magharibi. Mkoa wa savanna wa Senegali uko kati ya majangwa yaliyo kaskazini na mashariki na misitu minene iliyo kusini. Huko waweza kupata mbuyu mkubwa na wenye fahari wa tangu miaka mingi, pamoja na tunda lao la ajabu liitwalo mkate wa tumbili, ambalo kutoka hilo hamira soda yafanyizwa. Hiyo pia ni nchi ya tumbili na ndege wenye kupendeza na ya vijiji vya kizamani vyenye kupendeza vilivyo kati ya vichaka vya miembe.

Niliketi nikiwa nimestarehe nikafikiria ziara yangu ambayo nilikuwa nimengojea kwa muda mrefu kwenda kwenye mwingilio wa Afrika Magharibi. Leo Senegali, ikiwa na wenyeji milioni saba kutoka malezi tofauti-tofauti ya kitaifa, inaonea shangwe uhuru kamili. Lakini, je, mtu angeweza kuwa huru kimwili, na bado awe mtumwa wa mazoea na wa shirikina zinazomnyang’anya uhuru wa kweli? Nilitazamia kwa hamu sana kukutana na ndugu zangu wa kiroho nijue mimi mwenyewe, maendeleo ya kweli ifanyayo watu huru, katika sehemu hiyo ya ulimwengu.—Yohana 8:32.

‘Yehova Awataka Mpate Jengo Hili’

Jambo la kwanza katika ajenda (orodha ya mambo ya kufanywa) yangu lilikuwa ziara kwenye ofisi ya tawi ya Watch Tower na nyumba ya wamisionari katika Dakar. Tulipowasili kwenye jengo lenye sura la kisasa katika kiunga cha kimyakimya, niliona herufi J kubwa mbele. Swali langu la kwanza tulipokuwa tukizunguka ofisi ya tawi lilikuwa juu ya maana ya hiyo herufi J.

“Ni jambo la kupendeza,’ alieleza mwongozi wangu. “Katika 1985 tulipokuwa tukitafuta mahali pakubwa zaidi kwa ajili ya tawi, tulizuru jengo hili ambalo lilikuwa likijengwa. Laki-ni tuliona kwamba lilikuwa kubwa mno kwa mahitaji yetu. Mwenyewe aliposikia kwamba sisi tulikuwa Mashahidi wa Yehova, alitaka sana kutupangisha jengo hilo, kwa kuwa alijua sisi tu watu wa haki. ‘Mimi nina uhakika kwamba Mungu wenu, Yehova, awataka mpate jengo hili,’ akasema. ‘Kwani, tazameni! Kuna herufi J kubwa mbele! Nilipoagiza iwekwe hapo, nilifikiri ingesimamia jina langu John, lakini sasa nina uhakika yasimamia jina la Mungu, Jehovah (Yehova)!’ Tumekuwa wenye furaha kuwa katika jengo hili zuri kwa miaka mitano ambayo imepita.”

Halafu nilitaka kujua jinsi kazi ya kuhubiri ilivyoanza katika Senegali.

“Maji ya kweli yenye kuweka huru yaliletwa ndani ya Senegali katika miaka ya mapema ya 1950 na mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliyekuja kutoka Ufaransa kwa kazi ya mkataba. Katika 1965 ofisi ya tawi ilifunguliwa katika Dakar ili kusimamia kazi katika nchi za Senegali, Mali, na Mauritania, zenye kusema Kifaransa, na pia katika nchi ya Gambia yenye kusema Kiingereza. Tangu 1986 tumekuwa tukisimamia kazi katika Guinea-Bissau pia, ambapo Kireno kinasemwa.”

Kwa kujua kwamba zaidi ya asilimia 90 ya idadi ya watu huko ni wasio Wakristo, niliuliza ni maendeleo gani yamefanywa. “Ni kweli kwamba watu wengi katika nchi hizo hawaijui Biblia sana,” mwongozi wangu alisema, “lakini kazi inasonga taratibu. Katika Januari 1991 tulipendezwa kuona wahubiri wa Ufalme 596. Hiyo yaonyesha kwamba ndugu wa hapa na wamisionari wamekuwa wakifanya kazi kwa juhudi sana.”

“Nasikia kuna wamisionari wengi wanaotumikia huku,” nikasema.

“Naam, tuna karibu 60 ambao wamepewa mgawo kwenye maeneo mbalimbali tunayosimamia, nao walikuja kutoka nchi 13. Wanafanya kazi kwa juhudi nao wamechangia sana kufanya kazi iwe na msingi thabiti. Roho hiyo inaigwa na ndugu wa hapa katika upendo na bidii yao kwa ajili ya kweli. Kujapokuwa kukabili matatizo kama vile ukosefu wa kazi ya kuajiriwa na machumo madogo, ndugu wengi hutumia saa 15 na zaidi katika huduma ya shambani kila mwezi. Tunatumaini utakutana na wengine wa wafanyakazi hawa wenye bidii muda wa ziara yako.”

Nikatazamia kufanya hivyo.

Shambani Pamoja na Wamisionari

Margaret, aliyekuwa amekuwa katika utumishi wa misionari kwa zaidi ya miaka 20 kabla ya kifo chake cha juzi, alijitolea niende naye kwenye eneo lake katikati ya jiji. Tukapanda car rapide (gari lenye mbio sana) ili kupata mwonjo wa maisha ya huko. Kwa hakika, ilikuwa basi dogo lililosimama mara nyingi. Lilibeba abiria 25, na ikiwa wote wangekuwa wembamba, ningeweza kutambua jinsi safari hiyo ingeweza karibu sana kuwa yenye ustarehe. Akina mama wawili waliokuwa wakishiriki benchi yangu kwa wazi hawakuwa wembamba, lakini niliikubali hali hiyo kwa tabasamu.

“Katika eneo langu la mjini, waweza kuona mambo mengi yenye kupendeza,” akaeleza Margaret tulipofikia kituo chetu. “Waiona ndara hizo zenye rangi-rangi?” aliuliza, akielekeza kidole kwenye vibanda fulani karibu na kijia. “Zinafanyizwa kwa ngozi za kondoo na mbuzi zilizotiwa rangi.” Tukawakaribia watengenezaji ndara, na Margaret akaanza kuwahubiria katika lugha yao, Wolof (hutamkwa Jolof au Volof). Walisikiliza kwa makini na kuvutiwa na picha za Adamu na Hawa katika broshua yenye kupendeza.

Upesi tukakaribiwa na wachuuzi, wanaojulikana huko kuwa wanaume wa bana-bana, wanaotoa vifaa mbalimbali visivyo na mwisho. Baadhi yao walikuwa na fagio; wengine wakaonyesha nguo, kufuli, dawa, vibeti, machungwa, na hata ndege walio hai. Mmoja alitaka kuniuzia kora ala ya muziki yenye nyuzi iliyofanyizwa kwa nusu buyu, lenye kijiti cha shingo; hupigwa kwa mikono miwili. Nikaona kwamba kwenye upande wayo wa nyuma kulikuwa na taswira ndogo ya namna ya kifuniko cha uso kilichofanyizwa kwa ngozi, pembe ya mbuzi, na makombe madogo ya “bahati nzuri.” Tukaeleza kwamba hatungenunua kitu chochote kilichopambwa kwa ishara ambazo huenda zikahusiana na uchawi au desturi za kidini zisizo za Kikristo. Kwa mshangao wetu, mwanamume huyo wa bana-bana akakubali, akionyesha kwamba yeye mwenyewe alikuwa Mwislamu. Akaficha hiyo kora nyuma ya vazi au boubou (bubu) lake refu na legelege, akasikiliza kwa uangalifu Margaret alipotoa broshua, katika Kiarabu. Alichochewa sana sana hivi kwamba alichukua hiyo broshua akaanza kuisoma papo hapo. Baada ya kutushukuru sana, aliondoka na broshua na kora isiyonunuliwa. Tukawa na uhakika kwamba angejifunza broshua hiyo nyumbani.

Baadaye, nikaongea na John, ambaye alikuwa amekuwa misionari kwa zaidi ya miaka 20.

“Watu wa hapa ni wenye urafiki sana, nawe waweza kuongea na karibu kila mtu unaokuta,” John akaniambia. “Salamu yenye kutumiwa sana ‘assalam alaikum’ inamaanisha ‘amani iwe nawe,’ na watu walio wengi ni wenye amani. Hii ni nchi ya teranga, au ukaribishaji-wageni, nao unaonyeshwa kwa fadhili, uchangamfu wa kibinadamu, na furaha.” Ilikuwa inakuwa rahisi zaidi kwangu kuona kwa nini Mashahidi vijana wa kigeni wengi wangeweza kuacha familia na rafiki zao waje kutumikia katika shamba hili la umisionari.

Kawekwa Huru Ili Kufuatia Huduma ya Wakati Wote

Roho ya umisionari ina uvutano wenye kina kirefu kwa Mashahidi wa kule. Hilo laonekana hasa kwa sababu ukosefu wa kazi ya kuajiriwa ulioenea pote unafanya kujitia katika utumishi wa painia wa wakati wote kuwe jaribu kweli kweli. Marcel na Lucien, (Marseli na Lwisieni) waliowekwa huru na tabia nyingi zenye kudhuru kwa kujifunza kweli ya Biblia, walieleza hivi:

“Tulitaka kuonyesha kuthamini kwetu kwa kujitia katika utumishi wa painia. Lakini kazi isiyo ya wakati wote ilikuwa ngumu kupata. Tulijaribu utunzaji bustani, lakini haikuthibitika kuwa yenye kufaa. Kufua nguo kulitumia wakati wetu mwingi. Sasa tunafanya biashara ya uokaji, tukiwa na maduka yanayonunua bidhaa zetu kwa ukawaida, hiyo inafaulu vizuri.” Kwa wazi hiyo iliwahitaji wawe na imani na ufundi mwingi, pamoja na juhudi ya kweli, lakini hii yathibitisha kwamba inawezekana kuingia katika utumishi wa wakati wote hata wakati hali za kiuchumi ni ngumu.

Mashahidi wa Yehova walipoanza kujifunza Biblia na Michel (Mishel), wakati huo alikuwa akienda kwenye chuo kikuu katika Dakar. “Nilikuwa nimeshuka moyo kwa sababu ya roho ya ukosefu wa maadili ya wanafunzi walio wengi sana, na maswali ya kutatiza yalinirudia-rudia,” akasimulia. “Kwa nini mwanadamu alifanywa mtumwa wa mazoea na hali kama hizo zenye kudhuru? Biblia ilinipa majibu. Ilikuwa kana kwamba kitu kizito kilikuwa kimeondolewa kutoka mabega yangu. Ingawa wazazi wangu walisisitiza niendelee na mafunzo yangu, nilishiriki katika utumishi wa painia msaidizi kisha kutumikia nikiwa painia wa kawaida kwa wakati uliobaki ambao nilipaswa kuwa katika chuo kikuu. Naona kushiriki habari njema pamoja na wengine nikiwa painia, si kutafuta kazi-maisha katika mfumo ambao karibuni utamalizwa, kwaniletea shangwe iliyo kubwa zaidi.” Michel atumikia sasa akiwa painia wa pekee katika Mbour (Mbua).

Ndoa ya Wake Zaidi ya Mmoja Yapingana na Ndoa ya Mke Mmoja ya Kikristo

Desturi za huko hazipatani sikuzote na kanuni za Kikristo, na jambo hilo laweza kuleta majaribu mengi ya kipekee. Alioune (Aliune) mwangalizi msimamizi katika mojawapo ya makundi sita ya Mashahidi wa Yehova katika jiji la Dakar na maeneo yaliyo karibu, alisimulia hivi: “Niliposikia kwa mara ya kwanza kweli yenye kuweka huru, nilikuwa na wake wawili. Nikiwa Mwislamu mwenye kutenda, niliruhusiwa na dini yangu kuwa na wake hata zaidi. Baba yangu alikuwa na wanne, na karibu rafiki zangu wote walikuwa na wengi. Hiyo ni njia inayokubaliwa katika Afrika.” Lakini njia hiyo ya maisha ilikuwa na matokeo gani?

“Kuwa na wake zaidi ya mmoja kwaweza kusababisha matatizo mengi,” Alioune akaeleza, “hasa kuhusu watoto. Nina watoto kumi kwa mke wangu wa kwanza na wawili kwa yule wangu wa pili. Katika familia kama hizo, baba mara nyingi ni mgeni kwa watoto wake, kwa hiyo hawanufaiki kutokana na msaada wala nidhamu yake. Isitoshe, kuoa wake wengi hata hakukunilinda na uzini. Badala ya hiyo, ni kujidhibiti, tunda la roho ya Mungu, ambalo limefanya hivyo.” Kwa hiyo, Alioune alifanya nini?

“Nilimwambia mke wangu wa pili arudi nyumbani kwa wazazi wake,” akaendelea kusema, “na kwa busara nikaeleza kwamba haikuwa kwa sababu nilipata kwake jambo lolote lisilopendeza, lakini ni kwa sababu ya kutaka kutii matakwa ya Mungu. Nikafanya mipango ya pekee ili kuwatunza watoto wangu wote kimwili na kiroho, na mimi ninashukuru kwa vile leo nao pia wanamtumikia Yehova. Kati ya tisa ambao ni wahubiri, watano wamebatizwa, wawili hutumikia wakiwa mapainia wa pekee, na wale wengine watatu wakiwa mapainia wa kawaida na mapainia wasaidizi. Hakika kweli imeniweka huru na matatizo yaliyo mengi yanayohusika na kulea watoto.”

Ibada ya Vitu vya Kiuchawi Yapingana na Ibada ya Kweli

Jambo lililofuata kwenye ratiba yangu ya ziara lilikuwa kutembelea mkoa wa Casamance (Kasamansi) katika upande wa kusini. Nilivutiwa na jinsi kila kitu kilivyoonekana kuwa kibichikibichi. Eneo hilo likiwa limetiwa maji vizuri mwendo wa kilometa 300 kwa Mto mkubwa Casamance hutokeza mchele, mahindi, na njugu nyingi. Vibanda vya mviringo vyenye orofa mbili, vyenye kuezekwa majani katika namna ya mrija (mlizamu) ili kuchota maji kwa ajili ya majira ya ukavu, vimetawanyika kotekote katika sehemu ya mashambani. Mji mkuu, Ziguinchor (Ziganshori), umejengwa katika msitu wa miwese mingi. Nilifurahi kukutana na kundi lenye bidii la watu wa Yehova huko.

Dominic, mmisionari afanyaye kazi humo na kuzunguka Ziguinchor, aliniambia kwamba kazi ya kuhubiri katika eneo hilo inasonga mbele vizuri sana. “Miaka kumi tu iliyopita,” akasema, “kulikuwako wahubiri 18 katika kundi la Ziguinchor. Sasa kuna 80. Ili kusimamia ongezeko hilo kubwa, tumejenga Jumba la Ufalme mpya lenye kupendeza, kwa kutumia udongo mwekundu uliopatikana mahali penyewe pa kujengea. Mradi huo ulithibitika kuwa ushahidi mkubwa kwa jumuiya. Maneno yenye pongezi yalitolewa na wale walioona watu kutoka makabila mengi sana tofauti-tofauti wakifanya kazi pamoja kwa amani. Kwenye kusanyiko la mzunguko la karibuni, hudhurio la kilele lilikuwa 206, kukiwa na watu 4 wakibatizwa.”

Watu wengi katika sehemu hii ya Senegali bado hufuata imani za babu zao za kuabudu maumbile, wakiabudu vitu vya kiuchawi hata ingawa wanadai kuwa Wakristo au Waislamu. Nilisikiliza kwa makini hadithi iliyosimuliwa na Victor, mzee katika kundi la Ziguinchor.

“Nilizaliwa katika familia kubwa yenye kuabudu vitu vya kiuchawi Guinea. Wakati wa kuzaliwa kwangu, baba yangu aliniweka wakfu kwa roho fulani, au roho mwovu. Ili nipate upendeleo wa roho huyo, kwa kawaida, nilikuwa nikichukua sanduku jeusi kutoka chini ya kitanda changu, kusimamisha madhabahu ndogo, na kuitolea pembe, iliyowakilisha roho mwovu (shetani) mlinzi wangu, dhabihu za damu. Hata baada ya kuwa kwangu Mkatoliki, bado nilihisi kuwa mtumwa wa roho waovu. Nilipohama kwenda Senegali, Mashahidi wa Yehova walianza kujifunza Biblia pamoja nami. Mke wangu na mimi tulijifunza kwamba hatungeweza kuendelea ‘kuishiriki meza ya Yehova na meza ya mashetani.’ (1 Wakorintho 10:21) Lakini nilipoacha kutoa dhabihu, hao roho waovu wakaanza kutushambulia. Niliogopa kulitupa nje lile sanduku jeusi pamoja na vitu vyalo vyote vya kishetani kwa sababu nilijua yaliyompata mwanamume mmoja aliyekuwa amepata kichaa alipofanya hivyo.” Victor alikuwa katika hali mbaya kama nini!

“Mwishowe maneno ya Warumi 8:31, 38, 39 yakatupa nguvu tuliyohitaji ili kuondolea mbali kila kitu kilichohusika na ibada ya kiuchawi. Kwa kuwa tumeweka matumaini yetu katika Yehova, tumewekwa huru kweli kweli. Wote nyumbani mwangu wana lile tumaini zuri ajabu la uhai wa milele katika paradiso ya kidunia, ambamo ainabinadamu yote itakuwa huru na uvutano wa roho waovu.”

Hatimaye, ukawa wakati wangu kuondoka, nilipokuwa nikifunga mizigo yangu, nilifikiria ziara yangu ya Senegali, isiyoweza kusahauliwa. Ilikuwa yenye kuimarisha imani kama nini kwangu kukutana na kuongea na watu wengi sana ambao wamewekwa huru na utumwa wa matumizi mabaya ya dawa za kulevya, ukosefu wa maadili, na ushirikina na ambao sasa huonea shangwe uhuru wa kweli. Zijapokuwa hali ngumu za kiuchumi, wanapata shangwe na uradhi katika kumtumikia Yehova, aliyewaletea tumaini lenye uhakika la uhai wa milele katika dunia-paradiso. Sisi ni wenye shukrani kama nini kwake ambaye amefanya iwezekane kutangazisha habari njema hizo si katika Senegali tu bali pia ulimwenguni pote wakati wa “mwaka wa nia njema upande wa Yehova”! (Isaya 61:1, 2, NW)—Imechangwa.

[Ramani katika ukurasa wa 8]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

SENEGALI

St. Louis

Louga

Thiès

Dakar

Kaolack

GAMBIA

Banjul

[Picha katika ukurasa wa 9]

Maji ya kweli yenye kuweka huru hushirikiwa bila malipo katika vijiji

Nyumba ya Wamisionari na ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Dakar, Senegali

[Picha katika ukurasa wa 10]

Watu wa Senegali huusikia ujumbe wa Kikristo, kando kando ya pwani pia.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki